-
“Fulizeni Kunitarajia”Mnara wa Mlinzi—1996 | Machi 1
-
-
Sababu za Hasira Kali ya Yehova
4. Ni katika maneno gani Yehova alitaja hasira yake dhidi ya Yuda na Yerusalemu?
4 Yehova alikuwa na sababu nzuri za kuhisi hasira dhidi ya viongozi na wakazi wa Yuda na jiji lalo kuu la Yerusalemu. Kupitia nabii wake Sefania, yeye alisema: “Nitaunyosha mkono wangu juu ya Yuda, na juu ya watu wote wakaao Yerusalemu; nami nitayakatilia mbali mabaki ya Baali, yasionekane mahali hapa, na hilo jina la Wakemari pamoja na makuhani; na wale walisujudiao jeshi la mbinguni juu ya dari za nyumba; na hao waabuduo, waapao kwa BWANA na kuapa pia kwa Malkamu.”—Sefania 1:4, 5.
5, 6. (a) Kulikuwa na hali gani ya kidini katika Yuda wakati wa Sefania? (b) Viongozi wa kijamii wa Yuda na wale waliotumikia chini yao walikuwa na hali gani?
5 Yuda lilichafuliwa na matendo yenye kupotoka ya ibada ya kiuzazi ya Baali, unajimu wa kishetani, na ibada ya mungu wa kipagani Malkamu. Ikiwa Malkamu ndiye Moleki, kama vile wengine wanavyodokeza, basi ibada bandia ya Yuda ilitia ndani tendo lenye kuchukiza mno la kuwadhabihu watoto. Mazoea hayo ya kidini yalimchukiza sana Yehova. (1 Wafalme 11:5, 7; 14:23, 24; 2 Wafalme 17:16, 17) Walimfanya akasirike hata zaidi kwa kuwa hawa waabudu sanamu bado waliapa kwa jina la Yehova. Hangevumilia tena ukosefu huo wa usafi wa kidini naye angewakatilia mbali wote makuhani wapagani na makuhani waasi-imani.
6 Isitoshe, viongozi wa kijamii wa Yuda walikuwa wafisadi. Wakuu walo walikuwa kama “simba wangurumao,” na waamuzi wao walilinganishwa na “mbwa-mwitu” wenye pupa. (Sefania 3:3) Wale waliotumikia chini yao walishutumiwa ‘kujaza nyumba ya bwana wao udhalimu na udanganyifu.’ (Sefania 1:9) Ufuatiaji wa vitu vya kimwili ulienea. Wengi walikuwa wakitumia fursa hiyo kurundika mali.—Sefania 1:13.
Shaka Kuhusu Siku ya Yehova
7. Sefania alitoa unabii muda gani kabla ya “siku ya BWANA iliyo kuu,” na Wayahudi wengi walikuwa na hali gani ya kiroho?
7 Kama tulivyokwisha kuona, hali mbaya sana ya kidini iliyoenea katika siku ya Sefania yaonyesha kwamba alifanya kazi yake akiwa shahidi na nabii kabla ya Mfalme Yosia kuanza kampeni yake dhidi ya ibada ya sanamu, karibu 648 K.W.K. (2 Mambo ya Nyakati 34:4, 5) Basi, yaelekea kwamba Sefania alitoa unabii angalau miaka 40 kabla ya “siku ya BWANA iliyo kuu” kuja juu ya ufalme wa Yuda. Katika kipindi hicho, Wayahudi wengi walikuwa na shaka ‘wakarudi nyuma’ wakiacha kumtumikia Yehova na kuwa wasiojali. Sefania asema juu ya wale “wasiomtafuta BWANA, wala kumwulizia.” (Sefania 1:6) Kwa wazi, watu mmoja-mmoja katika Yuda walikuwa na ubaridi, wasijihusishe na Mungu.
8, 9. (a) Kwa nini Yehova angekagua “watu walioganda juu ya sira zao”? (b) Ni katika njia zipi Yehova angewapa uangalifu wakazi wa Yuda na viongozi wao wa kijamii na kidini?
8 Yehova alijulisha kusudi lake la kukagua wale wanaodai kuwa watu wake. Miongoni mwa wale waliodai kuwa waabudu wake, angewatafuta wale waliokuwa na shaka katika mioyo yao juu ya uwezo wake au kusudi lake la kuingilia mambo ya wanadamu. Yeye alisema hivi: “Kisha itakuwa wakati ule, nitauchunguza Yerusalemu kwa taa; nami nitawaadhibu watu walioganda juu ya sira zao; wasemao katika mioyo yao, BWANA hatatenda mema, wala hatatenda mabaya.” (Sefania 1:12) Usemi “watu walioganda juu ya sira zao” (kwa kurejezea kutengeneza divai) warejezea wale ambao wametulia, kama sira chini ya pipa la divai, wasiotaka kusumbuliwa na tangazo lolote kwamba karibuni Mungu ataingilia mambo ya wanadamu.
9 Yehova angeelekeza fikira kwa wakazi wa Yuda na Yerusalemu na kwa makuhani wao waliokuwa wamechanganya ibada yake na upagani. Ikiwa walihisi salama, kana kwamba walifichwa na giza la usiku ndani ya kuta za Yerusalemu, yeye angewafichua kwa taa nyangavu ambazo zingepenya giza la kiroho ambamo walikuwa wamekimbilia. Angewaondoa kwenye ubaridi wao wa kidini, kwanza kwa jumbe zenye nguvu sana za hukumu, kisha kwa kutekeleza hukumu hizo.
“Siku ya BWANA Iliyo Kuu I Karibu”
10. Sefania alifafanuaje “siku ya BWANA iliyo kuu”?
10 Yehova alimpulizia Sefania kupiga mbiu: ‘Siku ya BWANA iliyo kuu i karibu; i karibu, nayo inafanya haraka sana; naam, sauti ya siku ya BWANA ni chungu.’ (Sefania 1:14) Kwa kweli siku zenye uchungu mno zilikuwa mbele ya kila mtu—makuhani, wakuu, na watu—aliyekataa kutii onyo na kurudia ibada safi. Ukifafanua siku hiyo ya kutekeleza hukumu, unabii huo waendelea kusema: “Siku ile ni siku ya ghadhabu, siku ya fadhaa na dhiki, siku ya uharibifu na ukiwa, siku ya giza na utusitusi, siku ya mawingu na giza kuu, siku ya tarumbeta na ya kamsa, juu ya miji yenye maboma, juu ya buruji zilizo ndefu sana.”—Sefania 1:15, 16.
11, 12. (a) Ni ujumbe gani wenye hukumu uliotangazwa dhidi ya Yerusalemu? (b) Je, ufanisi wa kimwili ungeokoa Wayahudi?
11 Katika miongo michache mifupi, majeshi ya Babiloni yangevamia Yuda. Yerusalemu halingeponyoka. Maeneo yalo ya makazi na ya biashara yangeharibiwa kabisa. “Katika siku ile, asema BWANA kutakuwako sauti ya kilio kutoka lango la samaki, na mlio mkuu katika mtaa wa pili, na mshindo mkuu kutoka milimani. Haya! lieni, ninyi mkaao katika Makteshi [eneo fulani la Yerusalemu], maana wafanya biashara wote wameangamia; hao wote waliokuwa na mizigo ya fedha wamekatiliwa mbali.”—Sefania 1:10, 11.
12 Wakikataa kuamini kwamba siku ya Yehova ilikuwa karibu, Wayahudi wengi walijihusisha sana na biashara zenye faida nyingi. Lakini kupitia Sefania, nabii wake mwaminifu, Yehova alitabiri kwamba utajiri wao “utakuwa mateka, na nyumba zao zitakuwa ukiwa.” Wao hawangekunywa divai waliyotengeneza, wala “fedha yao wala dhahabu yao havi[nge]weza kuwaokoa katika siku ile ya ghadhabu ya BWANA.”—Sefania 1:13, 18.
-
-
“Fulizeni Kunitarajia”Mnara wa Mlinzi—1996 | Machi 1
-
-
18. (a) Hukumu ya kimungu ilitekelezwaje juu ya Yerusalemu, na kwa nini? (b) Unabii wa Sefania kuhusu Moabu na Amoni ulitimizwaje?
18 Wayahudi wengi waliofuliza kumtarajia Yehova pia waliishi wakaona hukumu zake zikitekelezwa juu ya Yuda na Yerusalemu. Kuhusu Yerusalemu, Sefania alikuwa ametabiri: “Ole wake yeye aliyeasi na kutiwa unajisi, mji wa udhalimu! Hakuitii sauti; hakukubali kurudiwa; hakumwamini BWANA; hakumkaribia Mungu wake.” (Sefania 3:1, 2) Kwa sababu ya kukosa uaminifu, Yerusalemu lilizingirwa mara mbili na Wababiloni na hatimaye kutekwa na kuharibiwa katika 607 K.W.K. (2 Mambo ya Nyakati 36:5, 6, 11-21)
-