Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • “MWISHO WA DINI YA UWONGO UNAKARIBIA!”

      Mnamo Oktoba (Mwezi wa 10) na Novemba (Mwezi wa 11) 2006, Mashahidi wa Yehova waliongeza utendaji wao wa kuhubiri ulimwenguni pote kwa kugawa trakti Habari za Ufalme Na. 37, yenye kichwa, “Mwisho wa Dini ya Uwongo Unakaribia!” Ujumbe huo wenye kuchochea umekuwa na matokeo gani?

      “Ujumbe wake ni sahihi kabisa!” akasema mwanamume fulani nchini Sweden ambaye amehangaishwa na unafiki katika dini ya uwongo. Kama mwanamume huyo, watu wengi walianza kujifunza Biblia kwa sababu ya trakti Habari za Ufalme.

      Nepal

      Huko Kathmandu, Dil alimpa mwanamume fulani ambaye alienda kanisani kwa ukawaida trakti Habari za Ufalme lakini mke wa mwanamume huyo alikuwa amemwacha miezi miwili hivi iliyotangulia kwa sababu ya ulevi. Dil alirudi na mume wake, Buddha, ili wazungumzie trakti Habari za Ufalme. Mwanamume huyo aliwaambia kwamba hapendi mwenendo wa washiriki fulani wa kanisa na kwamba mambo aliyosikia kutoka kwa Mashahidi wa Yehova yalikuwa tofauti na yale aliyosikia kanisani. Walimwonyesha Ufunuo 18:2-4 na kukazia umuhimu wa kutoka katika “Babiloni Mkubwa.” Kwenye ziara ya tatu, walianza kujifunza somo la 13 katika broshua Anataka. Kwenye ziara ya tano, walimkuta mke wake, ambaye alikuwa amerudi nyumbani. Aliwajua Mashahidi wa Yehova na alipenda ujumbe wetu. Kwenye ziara ya saba, mume huyo na mke wake walijifunza broshua hiyo pamoja. Mke wake alisema, “Sasa mume wangu hanywi kileo.”

      Brazili

      Dereva wa teksi ya pikipiki ambaye alipokea trakti Habari za Ufalme aliibandika nyuma ya koti lake kwa siku kadhaa na hivyo watu wengi wakaiona. Abiria walilazimika kusoma ukurasa wa kwanza walipokuwa wakisafirishwa.

      Dada wawili nchini Brazili walipokaribia nyumba fulani walishtuka kuona kibandiko kilichosema, “Unaweza kuingia, lakini hutatoka ukiwa hai.” Wakiwa na woga waliwauliza ndugu wawili wafanye nini. Ndugu hao waliamua kwenda kwenye nyumba hiyo. Baada ya kusali wapate mwongozo wa Yehova, ndugu hao walipiga makofi ili mwenye nyumba awasikie. Mwenye nyumba, ambaye alikuwa polisi, alikubali trakti Habari za Ufalme. Alieleza kwamba alikuwa akikarabati nyumba yake na alikuwa na vifaa vingi vya ujenzi upande wa nyuma wa nyumba. Kwa hiyo aliweka kibandiko hicho ili kuwaogopesha wezi. Wahubiri hao waliporudi kumtembelea, alikubali kujifunza Biblia.

      Mongolia

      Tsetsegmaa alijaribu kumhubiria dada yake mkubwa mara nyingi. Ingawa dada yake alihudhuria mikutano michache na akahudhuria Ukumbusho mara mbili, hakupendezwa sana na alikataa kujifunza Biblia. Lakini alipoona trakti Habari za Ufalme Na. 37 katika nyumba ya Tsetsegmaa, upendezi wake uliamshwa. Katika mazungumzo yaliyoendelea kwa saa mbili, aliuliza maswali mengi ambayo Tsetsegmaa aliyajibu kwa kutumia Biblia. Dada yake mkubwa alishangazwa na yale aliyojifunza, akataka kujifunza mengi zaidi, na sasa anafurahia kujifunza Biblia kwa ukawaida.

      Georgia

      Mashahidi walimpa mwanamke fulani trakti Habari za Ufalme naye aliuliza ikiwa ni ya kidini. Alipoambiwa kuwa ni ya kidini, aliichukua na akaahidi kuisoma. Mashahidi hao waliporudi, mwanamke huyo aliuliza ikiwa alikuwa amedanganywa na Kanisa Othodoksi. Alihangaishwa na hali za ulimwengu na kuzorota kwa viwango vya maadili kati ya vijana. Alisema kwamba haikuwa rahisi kupata mambo ya kuzungumzia na watoto wake. Mashahidi hao walimsomea 2 Timotheo 3:1-5, na akakubali kitabu Biblia Inafundisha. Mashahidi hao walipokuwa wakiondoka, aliwaambia hivi: “Ninasadiki kwamba dini yenu ndiyo ya kweli. Sina budi kuwapongeza vijana wenu kwa kuvalia kwa njia nzuri na kwa unyoofu wao na viwango vyao vya juu vya maadili.” Mwanamke huyo anafurahia kusoma magazeti yetu kwa ukawaida.

      Bangladesh

      Richel mwenye umri wa miaka 19 aligawa trakti Habari za Ufalme Na. 37 katika eneo ambalo halijawahi kuhubiriwa. Ingawa eneo hilo lilikuwa mbali na mahali ambapo Richel aliishi, bado alihisi kwamba anapaswa kwenda kwa sababu ilikuwa kampeni ya pekee. Kwenye nyumba ya pili aliyohubiri, aliwakuta wasichana wawili waliodai kuwa Wakristo ambao baba yao alikuwa amekufa miezi miwili iliyotangulia. Walimwuliza hivi: “Kwa nini Mungu aliruhusu jambo hilo litupate?” Richel aliwajibu kwa kutumia Biblia, na wasichana hao wakakubali trakti Habari za Ufalme, kisha wakamwambia, “Mungu amekutuma nyumbani kwetu.” Akitambua uhitaji wa kiroho wa wasichana hao, Richel aliwauliza ikiwa wangependa ajifunze Biblia pamoja nao. Wasichana hao walikubali mara moja. Wao ni wanafunzi wenye bidii na wana maswali mengi. Richel anahitaji kufanya utafiti mwingi, lakini anafurahia uradhi unaotokana na kuwafunza kweli watu wenye njaa ya kiroho.

      Armenia

      Painia wa kawaida anayeitwa Eliza alipigiwa simu na Lilit ambaye hapo awali alikuwa akijifunza naye Biblia. Alimwambia hivi: “Lazima uache mambo yote uliyopangia kesho ili uje tuanze kujifunza tena.” Kwani nini kilikuwa kimetukia? Lilit alipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, mume wake alimwambia: “Chagua utamwacha nani, mimi au Yehova.” Kwa hiyo akaacha kujifunza. Sasa, miaka miwili baadaye, alipokea trakti Habari za Ufalme Na. 37 alipokuwa akiwatembeza watoto wake bustanini. Trakti hiyo ilimfanya apendezwe sana hivi kwamba akamwambia hivi mume wake kwa ujasiri, “Huenda ukatosheka kuishi miaka 50 ukiwa na afya njema kisha ufe, lakini mimi ninataka mengi zaidi.” Kisha akamwahidi mume wake kwamba kujifunza Biblia kutamsaidia abadili utu wake usiofaa, kwa hiyo akaacha kumpinga. Sasa anafurahia kujifunza bila kupingwa na mume wake ambaye huwatunza watoto Lilit anapojifunza.

      Kambodia

      Wakati wa kampeni ya pekee, mmishonari anayeitwa Hugues alimtembelea mwanamume Mwislamu. Aliposoma trakti Habari za Ufalme, mwanamume huyo alikubali kuwa dini hazipaswi kujihusisha katika vita. Alisema anasikitishwa sana na dini yake kwa sababu watu wanaoshikilia sana dini waliiletea jina mbaya. Hugues alimsomea Zaburi 46:9 na kumwonyesha ahadi ya Mungu ya ulimwengu usiokuwa na vita. Juma lililofuata Hugues alimwonyesha kitabu Biblia Inafundisha. Sasa mwanamume huyo anathamini sana Biblia na anajifunza Biblia kwa kawaida.

      Urusi

      “Ninajua kwamba ninyi mnafundisha kweli,” akasema kasisi wa Kanisa Othodoksi ambaye alipokea nakala ya trakti Habari za Ufalme kutoka kwa dada wawili, “na kwamba Mungu wenu, Yehova, ataharibu dini zote za uwongo na kuacha yenu.” Kisha akawaambia mambo aliyojua kuhusu tumaini la kimbingu na paradiso duniani. Dada hao walimwuliza kwa nini hakuiacha dini yake ikiwa alijua kwamba itaharibiwa. Akajibu, “Ni kwa sababu ya kazi yangu. Nina nyumba tatu na magari manne. Siwezi kuacha vitu hivyo vyote.”

  • Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

      Kweli Ilikuwa Kampeni ya Ulimwenguni Pote

      Watu kadhaa katika sehemu mbalimbali walijiuliza ikiwa kweli trakti Habari za Ufalme ilikuwa ikisambazwa ulimwenguni pote. Kwa mfano, mwenye nyumba fulani huko Brazili ambaye alikuwa na shaka alimwambia mhubiri angoje ampigie simu rafiki yake huko Marekani ili ajue ikiwa alikuwa ameipata. Rafiki yake akamjibu, “Ndiyo, nimepata nakala moja dakika kumi zilizopita.” Akiwa ameshangaa, mwenye nyumba huyo alikubali trakti Habari za Ufalme na akaahidi kuisoma kwa makini.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki