-
Je, Unazungumza Ile “Lugha Safi” kwa Ufasaha?Mnara wa Mlinzi—2008 | Agosti 15
-
-
Acheni tuchunguze hatua fulani za msingi ambazo watu wanatumia wanapojifunza lugha nyingine na tuone jinsi hatua hizo zinavyoweza kutusaidia kujifunza lugha hiyo mpya ya mfano.
Kuzungumza Ile Lugha Safi kwa Ufasaha
8, 9. Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunataka kujifunza ile lugha safi, na kwa nini hilo ni jambo la maana sana?
8 Sikiliza kwa uangalifu. Mwanzoni, lugha mpya inaweza kusikika kuwa ngeni kabisa kwa mtu ambaye hajapata kuisikia. (Isa. 33:19) Lakini anapoendelea kujifunza kukazia fikira mambo anayosikia, ataanza kuelewa maneno fulani-fulani na njia za kuzungumza. Vivyo hivyo, tunahimizwa hivi: “Ni lazima kwetu kuyakazia uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida mambo tuliyosikia, ili tusipeperushwe kamwe.” (Ebr. 2:1) Yesu aliwahimiza tena na tena wafuasi wake hivi: “Yule aliye na masikio na asikilize.” (Mt. 11:15; 13:43; Marko 4:23; Luka 14:35) Ndiyo, tunahitaji ‘kusikiliza na kuelewa maana’ ya mambo tunayosikia ili tufanye maendeleo katika kuielewa lugha safi.—Mt. 15:10; Marko 7:14.
9 Ili kusikiliza, tunahitaji kukaza fikira, na kuna faida za kufanya hivyo. (Luka 8:18) Tunapokuwa kwenye mikutano ya Kikristo, je, tunakazia fikira mambo yanayosemwa, au fikira zetu zinatangatanga? Ni jambo la maana tufanye yote tunayoweza kukazia fikira mambo yanayozungumziwa. Tusipofanya hivyo, tunaweza kuwa wazito katika kusikia.—Ebr. 5:11.
10, 11. (a) Zaidi ya kusikiliza kwa uangalifu, tunapaswa kufanya nini? (b) Ni jambo gani lingine linalohusika katika kuzungumza ile lugha safi?
10 Iga wasemaji wenye ufasaha. Zaidi ya kusikiliza kwa uangalifu, watu wanaojifunza lugha mpya wanatiwa moyo pia wajaribu kuiga matamshi ya wasemaji wenye ufasaha na njia yao ya kuzungumza. Hilo linawasaidia watu hao kuepuka matamshi yasiyofaa ambayo huenda baadaye yakawazuia wasizungumze kwa njia inayoeleweka. Vivyo hivyo, tunapaswa kujifunza kutoka kwa wale walio na “ufundi wa kufundisha” lugha hiyo mpya. (2 Tim. 4:2) Omba msaada. Uwe tayari kukubali kurekebishwa unapokosea.—Soma Waebrania 12:5, 6, 11.
11 Kuzungumza ile lugha safi hakuhusishi tu kuamini kweli na kuwafundisha wengine kweli hiyo bali pia kujiendesha kupatana na sheria na kanuni za Mungu. Kuwaiga wengine kutatusaidia kufanya hivyo. Hilo linatia ndani kuiga imani na bidii yao. Pia inatia ndani kuiga jinsi Yesu alivyojiendesha katika maisha yake yote. (1 Kor. 11:1; Ebr. 12:2; 13:7) Tukiendelea kufanya hivyo, tutachangia umoja kati ya watu wa Mungu, na ni kana kwamba tutakuwa tukitamka maneno kwa njia ileile.—1 Kor. 4:16, 17.
12. Kukumbuka mambo kunahusika jinsi gani katika kujifunza lugha mpya?
12 Jitahidi kukumbuka mambo. Watu wanaojifunza lugha nyingine wanahitaji kukumbuka mambo mengi mapya. Hiyo inatia ndani kukumbuka maneno na misemo mipya. Kwa Wakristo, kujitahidi kukumbuka mambo kunaweza kuwa msaada mkubwa katika kuijua vizuri ile lugha safi. Bila shaka, tunapaswa kujitahidi kukumbuka majina ya vitabu vya Biblia kama vinavyofuatana. Wengine wamejiwekea mradi wa kukumbuka maneno ya maandiko fulani ya Biblia au mahali ambapo maandiko fulani yanapatikana. Wengine wameona faida za kujitahidi kukumbuka maneno ya nyimbo za Ufalme, majina ya makabila ya Israeli na ya wale mitume 12, na sifa ambazo ni sehemu ya matunda ya roho. Katika nyakati za zamani, Waisraeli wengi walizijua zaburi neno kwa neno. Katika nyakati za sasa, mvulana mmoja alijifunza mistari zaidi ya 80 ya Biblia neno kwa neno kufikia wakati ambapo alikuwa na umri wa miaka sita tu. Mbona tusitumie vizuri uwezo huo wenye thamani wa kukumbuka mambo?
13. Kwa nini ni jambo la maana sana kurudia-rudia mambo?
13 Kurudia-rudia kunasaidia kumbukumbu, na vikumbusho vinavyotolewa tena na tena ni vya maana katika elimu yetu ya Kikristo. Mtume Petro alisema hivi: “Sikuzote nitakuwa na mwelekeo wa kuwakumbusha ninyi kuhusu mambo haya, ijapokuwa mnayajua hayo na mmewekwa imara katika kweli iliyo ndani yenu.” (2 Pet. 1:12) Kwa nini tunahitaji vikumbusho? Kwa sababu vinatusaidia kuelewa mambo kwa undani zaidi, kupanua maoni yetu, na kuimarisha azimio letu la kubaki tukiwa imara kiroho. (Zab. 119:129) Kurudia-rudia viwango na kanuni za Mungu kunatusaidia kujichunguza na kutuzuia tusiwe ‘wasikiaji wasahaulifu.’ (Yak. 1:22-25) Tusipoendelea kujikumbusha ile kweli, mambo mengine yatapotosha mioyo yetu na huenda tukashindwa kuzungumza ile lugha safi kwa ufasaha.
14. Ni nini kitakachotusaidia tunapojifunza ile lugha safi?
14 Soma kwa sauti. (Ufu. 1:3) Wanafunzi fulani wanajaribu kujifunza lugha mpya kimyakimya wakiwa peke yao. Lakini hawapati matokeo mazuri. Tunapojifunza ile lugha safi, huenda nyakati nyingine tukahitaji kusoma “kwa sauti ya chini” ili tuweze kukaza fikira. (Soma Zaburi 1:1, 2.) Kufanya hivyo kunakazia kikiki akilini mwetu habari ambazo tunasoma. Katika Kiebrania, maneno ‘kusoma kwa sauti ya chini’ yanahusiana sana na kutafakari. Kama vile chakula kinavyohitaji kusagwa ili kitufaidi kabisa, tunahitaji kutafakari ili tuelewe waziwazi mambo tunayosoma. Je, tunatenga wakati wa kutosha ili kutafakari mambo tunayojifunza? Baada ya kusoma Biblia, tunapaswa kufikiria kwa uzito mambo ambayo tumesoma.
15. Ni kwa njia gani tunaweza kujifunza “kanuni” za ile lugha safi?
15 Chunguza kanuni za lugha. Baada ya muda inafaa kujifunza kanuni za lugha hiyo mpya na njia ya kupanga maneno, yaani, sarufi. Hilo linatuwezesha kuelewa muundo wa lugha hiyo, na kutuwezesha kuizungumza vizuri. Kama vile lugha ilivyo na kielelezo cha maneno au njia ya kupanga maneno, ile lugha safi ya kweli ya Biblia ina “kielelezo cha maneno yenye afya.” (2 Tim. 1:13) Tunapaswa kuiga “kielelezo” hicho.
16. Ni mwelekeo gani ambao tunahitaji kuushinda, nasi tunaweza kuushinda namna gani?
16 Endelea kufanya maendeleo. Huenda mtu akajifunza lugha kiasi cha kuweza kuitumia katika mazungumzo ya kawaida, lakini anaweza kuacha kufanya maendeleo. Wale wanaozungumza ile lugha safi wanaweza pia kuwa na tatizo kama hilo. (Soma Waebrania 5:11-14.) Ni nini kinachoweza kutusaidia kuushinda mwelekeo huo? Uwe tayari kuendelea kujifunza maneno zaidi ya lugha hiyo. “Kwa kuwa sasa tumeliacha fundisho la msingi juu ya Kristo, na tusonge mbele kuelekea ukomavu, tusiweke msingi tena, yaani, kutubu matendo yaliyokufa, na imani kwa Mungu, fundisho juu ya mabatizo na kuwekewa mikono, kufufuliwa kwa wafu na hukumu ya milele.”—Ebr. 6:1, 2.
17. Kwa nini ni jambo la maana kujifunza kwa ukawaida? Toa mfano.
17 Uwe na wakati hususa wa kujifunza. Kujifunza kwa ukawaida kwa muda mfupi ni afadhali kuliko kujifunza mara kwa mara kwa muda mrefu. Jifunze wakati ambapo uko chonjo na wakati ambapo akili yako haitangitangi kwa urahisi. Kujifunza lugha mpya ni kama kupasua njia katika msitu. Kadiri njia hiyo inavyotumiwa, ndivyo safari inavyokuwa rahisi zaidi. Njia hiyo isipotumiwa, muda si muda itafunikwa na majani. Kwa hiyo, kuendelea kujifunza kwa ukawaida ni jambo la maana sana! (Dan. 6:16, 20) Kwa msaada wa sala, ‘endelea kukaa macho daima’ unapozungumza ile lugha safi ya kweli ya Biblia.—Efe. 6:18.
18. Kwa nini tuzungumze ile lugha safi katika kila nafasi tunayopata?
18 Zungumza! Zungumza! Zungumza! Huenda watu fulani wanaojifunza lugha mpya wakasita kuizungumza kwa sababu wanaona aibu au wanaogopa kwamba watakosea. Hilo litawazuia wasifanye maendeleo. Mwanafunzi anapojifunza lugha mpya ni jambo la maana sana kufanya mazoezi. Kadiri mwanafunzi huyo anavyozungumza lugha hiyo mpya, ndivyo atakavyoizoea na kuitumia kwa urahisi zaidi.
-
-
Je, Unazungumza Ile “Lugha Safi” kwa Ufasaha?Mnara wa Mlinzi—2008 | Agosti 15
-
-
[Sanduku katika ukurasa wa 23]
Unaweza Kuzungumza Lugha Safi kwa Ufasaha Zaidi kwa
◆ kusikiliza kwa uangalifu.
◆ kuiga wasemaji wenye ufasaha.
◆ kujitahidi kukumbuka mambo na kuyarudia-rudia.
◆ kusoma kwa sauti.
◆ kuchunguza “kanuni za lugha.”
◆ kuendelea kufanya maendeleo.
◆ kuwa na wakati hususa wa kujifunza.
◆ kuizungumza.
-