-
Jerome—Mtangulizi Mwenye Kubishaniwa Katika Utafsiri wa BibliaMnara wa Mlinzi—1999 | Januari 1
-
-
Jerome—Mtangulizi Mwenye Kubishaniwa Katika Utafsiri wa Biblia
APRILI 8, 1546, Baraza la Trent lilitoa agizo kwamba Vulgate ya Kilatini “imeidhinishwa na Kanisa [Katoliki] . . . na kwamba yeyote asithubutu kuikataa kwa kisingizio chochote kile.” Ingawa Vulgate ilikamilishwa miaka elfu moja mapema, tafsiri hiyo na vilevile mtafsiri wake, Jerome, alikuwa kitovu cha ubishi kwa muda mrefu. Jerome alikuwa nani? Kwa nini yeye na tafsiri yake ya Biblia vilisababisha ubishi? Maandishi yake yanaathirije kazi ya kutafsiri Biblia leo?
-
-
Jerome—Mtangulizi Mwenye Kubishaniwa Katika Utafsiri wa BibliaMnara wa Mlinzi—1999 | Januari 1
-
-
Hata hivyo, licha ya wale waliomkashifu, Jerome alipokea utegemezo kamili wa Papa Damasus. Papa huyo alikuwa na sababu nzuri za kumtia moyo Jerome aendelee na uchunguzi wa Biblia. Wakati huo, kulikuwa na tafsiri nyingi za Biblia katika Kilatini zilizokuwa zikitumiwa. Nyingi ya hizo zilikuwa zimetafsiriwa bila uangalifu, nazo zilikuwa na makosa yenye kuonekana wazi. Hangaiko jingine alilokuwa nalo Damasus ni kwamba lugha ilikuwa ikiitenganisha milki ya Mashariki na ya Magharibi ya kanisa. Ni wachache waliokijua Kilatini upande wa Mashariki; na wachache hata zaidi upande wa Magharibi walikijua Kigiriki.
Hivyo basi, Papa Damasus alihangaikia sana kuwa na tafsiri ya Kilatini iliyosahihishwa ya Gospeli. Damasus alitaka tafsiri ambayo ingedhihirisha Kigiriki cha asili kwa usahihi, na bado iwe yenye ufasaha na kueleweka vizuri katika Kilatini. Jerome alikuwa mmoja wa wasomi wachache ambao wangetokeza tafsiri kama hiyo. Kwa vile alikuwa na ufasaha wa Kigiriki, Kilatini, na Kisiria na pia ujuzi wa kadiri wa Kiebrania, Jerome alistahili sana kupewa kazi hiyo. Basi Damasus alipompa utume, Jerome akaanza mradi ambao ungechukua zaidi ya miaka 20 iliyofuata ya maisha yake.
Ubishi Waongezeka
Ijapokuwa alizitafsiri Gospeli kwa haraka mno, Jerome alionyesha ustadi wa kisomi ulio wazi. Kwa kuzilinganisha hati zote za Kigiriki zilizopatikana wakati huo, alifanya masahihisho ya kimtindo na kimaana pia katika maandishi ya Kilatini, ili kuyafanya yapatane kwa ukaribu zaidi na maandishi ya Kigiriki.
Tafsiri ya Jerome ya zile Gospeli nne ilipokewa vyema kwa ujumla, kama zilivyopokelewa Zaburi alizofanyia marekebisho kwa Kilatini, marekebisho ambayo yalitegemea maandishi ya Kigiriki ya Septuagint. Hata hivyo, bado kulikuweko waliomchambua. “Viumbe fulani wa kudharauliwa,” akaandika Jerome, “walinishambulia kimakusudi kwa kudai kwamba nilijitahidi kusahihisha mafungu katika gospeli, kinyume cha amri ya wahenga na maoni ya ulimwengu wote.” Shutuma za hadharani kama hizo ziliongezeka baada ya kifo cha Papa Damasus katika mwaka wa 384 W.K. Kwa sababu uhusiano kati ya Jerome na papa mpya haukuwa mzuri, aliamua kuondoka Roma. Kwa mara nyingine tena, Jerome akaelekea mashariki.
Asitawi Kuwa Msomi wa Kiebrania
Katika mwaka wa 386 W.K., Jerome alikaa Bethlehemu, ambako aliishi muda wote uliobaki wa maisha yake. Aliandamana na kikundi kidogo cha wafuasi waaminifu-washikamanifu kwake, miongoni mwao akiwa Paula, mwanamke tajiri wa uzawa wa kiungwana kutoka Roma. Paula alikuwa ameikubali njia ya maisha ya kujinyima raha likiwa tokeo la mahubiri ya Jerome. Kwa kutumia pesa ambazo Paula alitoa, kao la watawa likajengwa chini ya mwelekezo wa Jerome. Hapo Jerome akafuatilia kazi yake ya kisomi, akamaliza kazi iliyo kubwa zaidi katika maisha yake.
Kuishi Palestina kulimpa Jerome fursa ya kuboresha uelewevu wa lugha ya Kiebrania. Aliwalipa wafunzi kadhaa Wayahudi ili wamsaidie kuyaelewa mambo magumu zaidi ya lugha hiyo. Hata hivyo, haikuwa rahisi ajapokuwa na mfunzi. Kuhusu mwalimu mmoja, Baraninas wa Tiberio, Jerome alisema: “Ilinitaabisha na kunigharimu sana kumshawishi Baraninas anifundishe usiku.” Ni kwa nini walijifunza usiku? Kwa sababu Baraninas aliyaogopa maoni ya jamii ya Wayahudi juu ya ushirikiano wake na “Mkristo”!
Katika siku ya Jerome, mara nyingi Wayahudi waliwadhihaki Wasio Wayahudi ambao walisema Kiebrania kwa sababu ya kushindwa kwao kutamka sauti za kooni vizuri. Na bado baada ya juhudi nyingi, Jerome akawa stadi wa sauti hizo. Pia, Jerome alitohoa maneno mengi sana ya Kiebrania kwa Kilatini. Hatua hii ilimsaidia kuyakumbuka maneno hayo na pia ilihifadhi matamshi ya Kiebrania cha wakati huo.
Ubishi Mkubwa Zaidi wa Jerome
Haijulikani Papa Damasus alitaka Jerome atafsiri kiasi gani cha Biblia. Lakini hakuna shaka juu ya jinsi Jerome alivyoliona jambo hilo. Jerome alimakinika sana na kujitolea. Tamaa yake kubwa ilikuwa kutokeza kifaa ambacho kingekuwa “msaada kwa Kanisa, kinachofaa vizazi vya baadaye.” Hivyo akaazimia kutokeza tafsiri iliyosahihishwa ya Biblia nzima ya Kilatini.
Ili kutafsiri Maandiko ya Kiebrania, Jerome alinuia kuitumia Septuagint ikiwa msingi wa tafsiri yake. Wengi waliiona tafsiri hiyo ya Kigiriki ya Maandiko ya Kiebrania, ambayo ilitafsiriwa mara ya kwanza katika karne ya tatu K.W.K., kuwa ilipuliziwa moja kwa moja na Mungu. Kwa hiyo, Septuagint ilienezwa sana miongoni mwa Wakristo waliosema Kigiriki wakati huo.
Hata hivyo, Jerome alipoendelea na kazi yake, alipata mambo yasiyopatana kati ya hati za Kigiriki, ambayo ni sawa na yale aliyopata katika hati za Kilatini. Jerome akavunjika moyo zaidi. Hatimaye, akakata kauli kwamba ili kutokeza tafsiri inayoweza kutumainiwa, lazima apuuze hati za Kigiriki, Septuagint ikiwa miongoni mwao, na aende moja kwa moja kwa maandishi-awali ya Kiebrania.
Uamuzi huo ulisababisha upinzani mkali. Baadhi ya watu wakamwita Jerome mpotoshaji wa maandiko, mwenye kumkufuru Mungu na mwenye kuacha mapokeo ya kanisa kwa kupendelea Wayahudi. Hata Augustine—mwanatheolojia mkuu wa kanisa wakati huo—alimsihi sana Jerome ayarudie maandishi ya Septuagint, akisema: “Ikiwa tafsiri yako itaanza kusomwa na wote katika makanisa mengi, hilo litakuwa jambo la kuhuzunisha sana kwa sababu, wakati wa kusoma Andiko, lazima tofauti zitatokea baina ya Makanisa ya Kilatini na Makanisa ya Kigiriki.”
Naam, hofu ya Augustine ilikuwa kwamba huenda kanisa lingegawanyika ikiwa makanisa ya Magharibi yangetumia maandishi ya Kilatini ya Jerome—yanayotegemea maandishi ya Kiebrania—huku makanisa ya Kigiriki ya Mashariki yakiwa yangali yanatumia tafsiri ya Septuagint.b Kwa kuongezea, Augustine alitoa maoni yenye mashaka juu ya kuiacha Septuagint kwa kupendelea tafsiri ambayo ni Jerome pekee angeweza kuitetea.
Jerome aliwajibuje wapinzani wote hao? Kama ilivyo kawaida yake, Jerome aliwapuuza wachambuzi wake. Aliendelea kutafsiri moja kwa moja kutoka kwa Kiebrania, na kufikia mwaka wa 405 W.K., akawa ameimaliza Biblia yake ya Kilatini. Miaka mingi baadaye tafsiri yake ikapewa jina Vulgate, linalorejezea tafsiri iliyopokewa na wengi (hilo neno la Kilatini vulgatus likimaanisha “kawaida, kinachopendwa na wengi”).
Matimizo ya Kudumu
Tafsiri ya Maandiko ya Kiebrania ya Jerome ilikuwa zaidi ya kuyarekebisha tu maandishi yaliyokuwepo. Hiyo ilibadili mtindo wa kujifunza na kutafsiri Biblia wa vizazi vya baadaye. “Hiyo Vulgate,” akasema mwanahistoria Will Durant, “bado ndiyo utimizo mkuu na wenye kuvutia zaidi wa kifasihi wa karne ya nne.”
Ingawa Jerome alikuwa mtu mwenye kejeli na mgomvi, alifaulu akiwa peke yake kuurudisha tena uchunguzi wa Biblia hadi kwenye maandishi yaliyopuliziwa ya Kiebrania. Alichunguza kwa makini na kulinganisha hati za kale za Biblia za Kiebrania na Kigiriki ambazo hatuwezi kuzipata leo. Pia, maandishi yake yalitangulia yale ya Wamasora Wayahudi. Hivyo, Vulgate ni marejeo yenye mafaa sana ya kulinganishia tafsiri nyingine za maandishi ya Biblia.
Bila kupuuza tabia ya Jerome yenye kupita kiasi au maoni yake ya kidini, wapendao Neno la Mungu waweza kuthamini juhudi zenye bidii za huyu mtangulizi mwenye kubishaniwa katika utafsiri wa Biblia. Na ni kweli, Jerome alifikia mradi wake—alitokeza kitu “kinachofaa vizazi vya baadaye.”
-
-
Jerome—Mtangulizi Mwenye Kubishaniwa Katika Utafsiri wa BibliaMnara wa Mlinzi—1999 | Januari 1
-
-
b Kama ilivyotokea baadaye, tafsiri ya Jerome ikawa Biblia ya msingi kwa Jumuiya ya Wakristo ya Magharibi, ilhali Septuagint yaendelea kutumiwa katika Jumuiya ya Wakristo ya Mashariki hadi leo.
-