-
Maarifa Ni Mengi Lakini Mabadiliko Ni MachacheAmkeni!—2002 | Agosti 8
-
-
Maarifa Ni Mengi Lakini Mabadiliko Ni Machache
“Ijapokuwa kumekuwa na maendeleo mengi ya kisayansi, wanadamu hawajafanya mabadiliko makubwa katika kipindi cha miaka elfu mbili iliyopita; kwa hiyo, tungali twahitaji kujitahidi kujifunza kutokana na yaliyopita.” —Kenneth Clark, Civilisation—A Personal View.
BILA shaka, kumekuwa na maendeleo makubwa ya kisayansi katika karne zilizopita. Gazeti la Time linasema kwamba maendeleo hayo “yamewawezesha mamilioni ya watu kuishi maisha ya hali ya juu kuliko katika kipindi kingine chochote.” Maendeleo ya kitiba ni kati ya maendeleo makubwa ambayo yamefanywa. Mwanahistoria Zoé Oldenbourg anasema kwamba katika zama za kati ‘watu walitibiwa bila ustadi na bila huruma. Daktari angeweza kuponya ama kusababisha kifo.’
Nyakati Nyingine Watu Wamekataa Kujifunza
Nyakati nyingine watu wamekataa kujifunza. Kwa mfano, mwishoni mwa miaka ya 1800, madaktari wengi walipuuza uthibitisho wa kutosha kwamba walikuwa wakiwaambukiza wagonjwa wao magonjwa kwa njia fulani. Kwa hiyo waliendelea na mazoea yao hatari na wakakataa kunawa mikono kabla ya kumhudumia mgonjwa mwingine.
Hata hivyo, kulikuwa na maendeleo ya kisayansi na ya kitekinolojia. Basi ni jambo la akili kusema kwamba wanadamu walipaswa kujifunza kutokana na mambo yaliyopita jinsi ambavyo wangeweza kuleta furaha na usalama ulimwenguni. Lakini hawakufanya hivyo.
Hebu fikiria yaliyotukia huko Ulaya katika miaka ya 1600. Kipindi hicho kiliitwa kipindi cha maarifa na akili. Lakini, kama vile Kenneth Clark anavyosema, ‘licha ya maendeleo mengi katika sanaa na sayansi, bado watu waliwanyanyasa wengine bila sababu na watu walipigana kwa ukatili kuliko wakati mwingine wowote.’
Katika nyakati zetu, bado watu hawataki kujifunza kutokana na yaliyopita ili kuepuka kurudia makosa yaleyale yaliyofanywa zamani. Ndiyo sababu inaonekana kwamba uhai wa wanadamu unahatarishwa. Mwandishi Joseph Needham alikata kauli kuwa hali imekuwa hatari sana hivi kwamba ‘twaweza tu kuomba na kutumaini kwamba watu wenye kichaa hawatatumia silaha zinazoweza kuangamiza wanadamu wote na viumbe wote duniani.’
Ni kwa nini kuna jeuri na ukatili mwingi ulimwenguni ijapokuwa wanadamu wana akili nyingi na maarifa mengi? Je, hali hiyo itabadilika? Makala mbili zinazofuata zitazungumzia maswali hayo.
-
-
Bado Mataifa Hayajajifunza SomoAmkeni!—2002 | Agosti 8
-
-
Bado Mataifa Hayajajifunza Somo
‘Iwapo sisi wanadamu tungeweza kujifunza kutokana na yaliyopita—tungejifunza masomo muhimu sana! Lakini hisia kali na migawanyiko hutupofusha, na masomo tunayopata kutokana na mambo tuliyojionea ni kama taa iliyowekwa kwenye sehemu ya nyuma ya mashua ambayo inaangazia tu mawimbi yaliyo nyuma yetu!’—Samuel Taylor Coleridge.
JE, UNAKUBALIANA na maneno hayo ya mshairi Mwingereza, Samuel Coleridge? Je, hisia zetu kwa ajili ya harakati fulani zaweza kutupofusha sana hivi kwamba turudie kufanya makosa makubwa ambayo yalifanywa na vizazi vya kale?
Vita ya Dini
Kwa mfano, hebu fikiria mambo fulani ambayo watu walifanya wakati wa zile Vita za Dini. Mnamo mwaka wa 1095 W.K., Papa Urban wa Pili aliwachochea “Wakristo” kuwanyang’anya Waislamu ile Nchi Takatifu. Wafalme, watu wenye vyeo, mashujaa, na watu wa kawaida katika mataifa yote yaliyosimamiwa na Urban wa Pili walikubali mwito wake. Mwanahistoria mmoja wa zama za kati alisema kwamba “karibu mataifa yote yaliyoishi kulingana na sheria ya Kristo” yaliitikia mwito huo haraka.
Mwanahistoria Zoé Oldenbourg anasema kwamba wapiganaji wengi wa zile Vita za Dini “walisadiki kabisa kwamba [walikuwa] wakimtumikia Mungu Mwenyewe walipopigana vita hizo.” Anasema kwamba walijiona kuwa “malaika waangamizi wanaowashambulia watoto wa ibilisi.” Pia, kama vile mwandishi Brian Moynahan anavyosema, waliamini kwamba wapiganaji “wote ambao walikufa wangepata tuzo huko mbinguni ya wale wanaofia imani.”
Huenda ikawa wapiganaji wa zile Vita za Dini hawakufahamu kwamba adui zao waliamini vivyo hivyo. Katika kitabu chake Shorter History of the World, mwanahistoria J. M. Roberts anasema kwamba wanajeshi Waislamu walienda vitani pia wakisadiki kwamba walikuwa wakimpigania Mungu na “kwamba baada ya kuuawa na kafiri vitani wangeingia katika paradiso” huko mbinguni.
Wapiganaji wa pande zote mbili walifundishwa kwamba walikuwa wakipigana vita ya uadilifu—iliyokubaliwa na kubarikiwa na Mungu. Viongozi wa kidini na wa kisiasa waliendeleza maoni hayo na kuchochea hisia za raia zao. Na pande zote mbili zilitenda mambo mengi ya ukatili yenye kuogopesha.
Ni Watu wa Aina Gani Waliohusika?
Ni watu wa aina gani waliotenda maovu hayo? Wengi wao walikuwa watu wa kawaida—ambao hawakuwa tofauti na watu wanaoishi leo. Ni wazi kwamba wengi wao walichochewa na maoni mazuri na tamaa ya kutaka kurekebisha hali mbaya zilizokuwapo ulimwenguni wakati huo. Kwa sababu walikuwa na hisia kali sana, hawakutambua kwamba harakati zao za kupigania “haki,” zilisababisha ukosefu wa haki, maumivu, na kuteseka kwa mamia ya maelfu ya wanaume, wanawake, na watoto wasio na hatia ambao hawangeweza kutoroka maeneo ya vita.
Je, si kweli kwamba mambo hayo yametukia tena na tena katika historia yote? Je, si kweli kwamba viongozi wenye uvutano wamewachochea mamilioni ya watu tena na tena kupigana vita za unyama na za ukatili dhidi ya maadui wao wa kidini na wa kisiasa hata ingawa watu hao katika hali ya kawaida hawangefikiria kamwe kufanya hivyo? Kule kujihusisha kwa pande zote mbili katika pambano hilo na yale madai kwamba Mungu aliunga mkono kila upande, yalihalalisha ukandamizaji wa maadui wa kisiasa na wa kidini. Mbinu hiyo imerudiwa tena na tena na imewafaidi watawala wa kimabavu kwa karne nyingi. Moynahan anasema kwamba mbinu hiyo ndiyo “iliyotumiwa na watu waliochochea yale Maangamizi Makubwa ya Nazi na yale mauaji ya jamii nzima-nzima katika nyakati zetu kama vile ilivyotumiwa katika vita ya kwanza ya dini.”
Lakini huenda ukasema hivi, ‘Watu wenye akili leo hawawezi kukubali kudanganywa jinsi hiyo. ‘Sisi tumestaarabika zaidi.’ Hivyo ndivyo mambo yanavyopasa kuwa. Lakini je, kweli watu wamejifunza kutokana na yaliyopita? Ni nani awezaye kusema kwamba hilo ni kweli anapozingatia mambo yaliyotukia katika muda wa miaka mia moja iliyopita?
Vita ya Kwanza ya Ulimwengu
Kwa mfano, mambo yaliyotukia wakati wa zile Vita za Dini yalirudiwa wakati wa vita ya kwanza ya ulimwengu. Roberts anasema kwamba ‘mojawapo ya mambo ya ajabu kuhusu mwaka wa 1914 ni kwamba katika nchi zote yaonekana watu wengi sana wa vikundi vyote, dini zote, na jamii zote, walienda vitani kwa utayari na kwa furaha.’
Mbona watu wengi sana wa kawaida walienda “vitani kwa utayari na kwa furaha”? Ni kwa sababu imani na maadili yao yaliathiriwa na falsafa za wakati huo sawa na wale wapiganaji wa zamani ambao walienda vitani kwa utayari. Ijapokuwa huenda ikawa wengine walitaka kupigania uhuru na haki, ni wazi kwamba wengi walichochewa na maoni ya kiburi kwamba nchi yao ilikuwa bora kuliko nchi nyingine na hivyo ilistahili kutawala.
Watu hao walishawishiwa kuamini kwamba vita ni jambo lisiloepukika—jambo la “asili na la lazima.” Mwandishi Phil Williams anasema kwamba nadharia moja ilifanya watu waamini kwamba vita ni njia halali ya “kuangamiza viumbe ambao hawakustahili kuishi.”
Kwa wazi, kila mtu alifikiri kwamba alikuwa akifanya jambo zuri. Na tokeo likawa nini? Mwandishi Martin Gilbert, ambaye pia ni mwanahistoria, anasema kwamba wakati wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, “serikali zilichochea na kuunga mkono ukabila, uzalendo na uwezo wa kijeshi”—na watu wakaziunga mkono bila kufikiri. John Kenneth Galbraith, mtaalamu wa uchumi, alilelewa katika sehemu ya mashambani ya Kanada wakati wa vita hiyo. Alisema kwamba kotekote watu walizungumza kuhusu “upumbavu wa pambano hilo huko Ulaya.” Walisema kwamba “watu wenye akili . . . hawakuunga mkono upumbavu huo.” Lakini kwa mara nyingine tena walihusika. Na matokeo yakawa nini? Wanajeshi Wakanada wapatao 60,000 walikuwa kati ya wale wanajeshi zaidi ya milioni tisa ambao walikufa katika pande zote mbili za pambano hilo lenye kuchukiza ambalo baadaye liliitwa vita ya kwanza ya ulimwengu.
Somo Halijazingatiwa
Katika miaka 20 iliyofuata, kwa mara nyingine tena mtazamo uliokuwapo awali ulianza kuonekana wazi wakati utawala wa Ufashisti na wa Nazi ulipoanza. Hugh Purcell anaandika kwamba Wafashisti walianza kutumia “mbinu za kawaida za propaganda kama vile ishara na hekaya mbalimbali ili kuchochea hisia za watu.” Mbinu moja waliyotumia ambayo ilikuwa na uvutano mkubwa sana ni kuchanganya dini na siasa, kwa kumwomba Mungu awabariki wanajeshi wao.
Adolf Hitler ni mtu mmoja alikuwa “stadi kwa kushawishi umati wa watu na vilevile msemaji hodari.” Katika kitabu cha Hitler and Nazism, Dick Geary anasema kwamba Hitler aliamini kwamba ‘watu waliongozwa na hisia zao wala si akili zao,’ kama vile viongozi wengi wa kale wenye ustadi wa kushawishi walivyoamini pia. Hitler alitumia udhaifu huo wa wanadamu kwa ujanja kuwafanya watu wamchukie adui mmoja—kama wakati ‘alipowaongoza Wajerumani kuwachukia Wayahudi,’ asema Purcell. Aliwakashifu Wayahudi, akisema, ‘Myahudi ndiye anayeharibu taifa la Ujerumani.’
Jambo la kuogopesha kuhusu kipindi hicho chote ni kwamba mamilioni ya watu wenye akili timamu walichochewa kwa urahisi kuwaua watu wengi. Geary anauliza hivi: “Watu wa nchi iliyosemekana kuwa imestaarabika waliwezaje kukubali na hata kujihusisha katika matendo ya ukatili ya serikali ya Nazi?” Zaidi ya hayo, mbali na kuwa nchi ambayo “imestaarabika,” ilikuwa pia nchi iliyosemekana kuwa ya Kikristo! Walishawishiwa kwa sababu walipenda falsafa na hila za wanadamu badala ya mafundisho ya Yesu Kristo. Na tangu wakati huo wanaume na wanawake wengi wenye nia nzuri wameongozwa kufanya matendo ya ukatili!
Georg Hegel, mwanafalsafa Mjerumani, anasema hivi: “Mambo tuliyojionea na mambo yaliyopita yanatufundisha kwamba mataifa na serikali mbalimbali hazijajifunza somo lolote kutokana na yaliyotukia wala hazijatenda kulingana na masomo yoyote ambayo zingeweza kujifunza.” Wengi wanaweza kukataa falsafa za Hegel kuhusu maisha, lakini ni wachache tu wanaoweza kupinga taarifa hiyo. Kwa kusikitisha, inaonekana ni vigumu sana kwa watu kujifunza kutokana na mambo yaliyopita. Lakini je, yapaswa kuwa hivyo kwa upande wako?
Kwa wazi, somo moja la wazi tunalojifunza ni hili: Ili tuweze kuepuka misiba iliyokumba vizazi vilivyopita, tunahitaji kitu chenye kutegemeka zaidi kuliko falsafa za wanadamu zenye kasoro. Basi, ni nini kinachoweza kuongoza kufikiri kwetu ikiwa falsafa za wanadamu haziwezi? Zaidi ya miaka elfu moja kabla ya zile Vita za Dini kuanza, wanafunzi wa Yesu Kristo walionyesha njia ya kweli ya Ukristo ambayo inafaa kufuatwa. Hebu tuchunguze kile walichofanya ili kuepuka kujihusisha katika mapambano ya umwagaji-damu ya wakati huo. Lakini je, yawezekana kwamba mataifa yaliyopo leo yatajifunza jinsi ya kufanya hivyo na kuepuka mapambano? Na bila kujali yale ambayo mataifa yatafanya, Mungu atafanya nini ili kukomesha taabu zinazowapata wanadamu?
[Picha katika ukurasa wa 6]
Mapambano ya wanadamu yamesababisha matendo ya ukatili na kuteseka
[Picha katika ukurasa wa 7]
Juu: Wakimbizi katika eneo lenye vita
Watu waliosemekana kuwa wamestaarabika waliwezaje kujihusisha katika matendo hayo ya ujeuri mwingi?
[Hisani]
Wakimbizi wa Rwanda: UN PHOTO 186788/J. Isaac; kuporomoka kwa jengo la World Trade Center: AP Photo/Amy Sancetta
-
-
Kujifunza Kutokana na Wakristo wa Karne ya KwanzaAmkeni!—2002 | Agosti 8
-
-
Kujifunza Kutokana na Wakristo wa Karne ya Kwanza
“Jihadharini: labda huenda kukawa na mtu fulani ambaye atawachukua nyinyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyo mtupu kulingana na mapokeo ya wanadamu, kulingana na mambo ya msingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo.”—Wakolosai 2:8.
HIVYO ndivyo mtume Paulo alivyowaonya Wakristo wa karne ya kwanza kuhusu hatari za kufuata falsafa za wanadamu bila kufikiri. Wangeweza kushikamana na mwongozo wenye kutegemeka ambao Yesu na mitume wake waliwapa, mafundisho ambayo tayari yalikuwa yamewaletea faida nyingi, au wangedanganywa na maoni ya wanadamu yenye kubadilika-badilika, ambayo yalikuwa yamewaletea mamilioni ya watu fadhaa na taabu.—1 Wakorintho 1:19-21; 3:18-20.
Kuishi “Kulingana na Kristo”
Wapiganaji waliohusika katika zile Vita za Dini miaka ipatayo elfu moja iliyopita hawakutambua kwamba kuishi “kulingana na Kristo” kunahusisha mengi zaidi ya kudai kumwamini Yesu Kristo. (Mathayo 7:21-23) Kunahusisha kufuata kabisa mafundisho ya Yesu yanayopatikana katika Neno la Mungu, Biblia. (Mathayo 7:15-20; Yohana 17:17) Yesu Kristo alisema hivi: “Ikiwa nyinyi mwakaa katika neno langu, nyinyi kwa kweli ni wanafunzi wangu.” (Yohana 8:31) Alisema kwamba “wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.”—Yohana 13:35.
Kwa kweli, wapiganaji wa zile Vita za Dini walipotoshwa na “udanganyo mtupu kulingana na mapokeo ya wanadamu.” Na haishangazi kwamba watu wa kawaida walidanganywa wakati viongozi wao wa kidini, naam, maaskofu wao, “walipojulikana wazi kuwa wanajeshi.” Kitabu Cyclopedia of Biblical, Theological, and Ecclesiastical Literature, cha McClintock na Strong, kinasema kwamba “roho ya vita ilikuwepo sana miongoni mwa makasisi hivi kwamba wakati wowote ambapo faida yoyote ingeweza kupatikana [kupitia vita], walikuwa tayari kupigana.”
Ni nini kilichosababisha hali hiyo ya kuhuzunisha? Baada ya kifo cha mitume Wakristo wa karne ya kwanza, viongozi wa kidini waasi-imani walizidi kupotosha mafundisho ya Kristo, kama vile Neno la Mungu lilivyokuwa limetabiri. (Matendo 20:29, 30) Dini iliyopotoka ikazidi kujihusisha na serikali hatua kwa hatua. Katika karne ya nne, yasemekana kwamba Maliki Mroma Konstantino alibadili dini na kuwa Mkristo alipokuwa karibu kufa. Halafu, kitabu Cyclopedia kinasema kwamba, “kubadili zile bendera zenye sanamu kuwa bendera yenye Msalaba kuliwawajibisha Wakristo wote kuwa wanajeshi.”
Ni wazi kwamba Wakristo hawakuwa kamwe na wajibu huo. Lakini “hoja zenye kushawishi” za falsafa za wanadamu ziliwakengeusha wasifuate kabisa mfano wa Kristo. (Wakolosai 2:4) Hoja fulani zenye udanganyifu mwingi zimetumiwa kwa muda mrefu ili kuthibitisha uhalali wa vita na mapambano ya wanadamu. Hata hivyo, kama vile kitabu Cyclopedia kinavyosema, mtu mwenye huruma au mtu wa Mungu anayejihusisha na ‘matendo ya ukatili ya vita, kama ilivyokuwa katika nyakati za kale au katika nyakati zetu, hawezi hata kidogo kusemwa kuwa anafuata kanuni za Ukristo.’
Mbali na dini zinazodai kuwa za Kikristo, dini nyingine pia zimejihusisha katika vita katika karne zote zilizopita. Sawa na makanisa yanayodai kuwa ya Kikristo, watu wa dini hizo pia wamewachinja watu wa dini zao na wa dini nyingine kwa sababu ya tofauti za kitaifa, kisiasa, na za kidini. Dini hizo zimetumia ujeuri au vitisho ili kubadili imani ya watu. Baadhi ya dini hizo zimeshiriki katika mauaji makubwa ili kujaribu kutimiza malengo yake. Dini hizo hazitofautiani hata kidogo na dini zinazodai kuwa za Kikristo.
Kujitenga na Ulimwengu
Wakristo wa karne ya kwanza waliwezaje kujitenga na vita vyenye ukatili na siasa za wakati wao? Kanuni mbili kuu ziliwasaidia. Jambo la kwanza lilikuwa lile agizo ambalo Yesu alimpa mtume Petro wakati Petro alipotumia upanga kujikinga: “Rudisha upanga wako mahali pao, kwa maana wale wote wauchukuao upanga wataangamia kwa upanga.” (Mathayo 26:52) Na la pili lilikuwa yale maneno ya Yesu kwa Pilato wakati alipomwuliza Yesu kuhusu ufalme wake: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, mahadimu wangu wangalipigana ili nisikabidhiwe kwa Wayahudi. Lakini, kama ilivyo, ufalme wangu si kutoka chanzo hiki.”—Yohana 18:36.
Wakristo wa karne ya kwanza walitumiaje kanuni hizo? Walijitenga kabisa na ulimwengu, wakidumisha msimamo wa kutounga mkono upande wowote wa kisiasa na wa kijeshi. (Yohana 15:17-19; 17:14-16; Yakobo 4:4) Walikataa kutumia silaha dhidi ya wanadamu wenzao. Historia inaonyesha wazi kwamba Wakristo wa karne ya kwanza hawakujiunga na harakati za Kiyahudi za uzalendo wala majeshi ya milki ya Roma. Zaidi ya hayo, hawakujaribu kuwaambia viongozi wa kisiasa mambo waliyopaswa kufanya, kwani hilo lilikuwa daraka la viongozi hao wa serikali.—Wagalatia 6:5.
Katika karne ya pili W.K., Justin Martyr aliandika kwamba Wakristo walikuwa ‘wamefua panga zao ziwe majembe.’ (Mika 4:3) Akiwajibu wale waliopinga msimamo wa Wakristo, Tertullian aliuliza hivi: “Je, inapaswa kuonwa kuwa halali kuwa mwanajeshi, ilhali Bwana anatangaza kwamba yule anayetumia upanga ataangamia kwa upanga?”
‘Mtii Mungu Kuwa Mtawala Kuliko Wanadamu’
Wakristo wa mapema walikabili magumu walipokataa kwenda vitani. Jambo hilo halikupatana na maoni yaliyokubaliwa na watu wa wakati huo. Celsus, adui mmoja wa Ukristo, alidhihaki msimamo wao. Alionelea kwamba watu wote walipaswa kwenda vitani walipoamriwa na wenye mamlaka. Licha ya ukatili mwingi, Wakristo wa mapema walikataa kufuata falsafa zozote za wanadamu ambazo zilipinga mafundisho ya Kristo. Walisema hivi: “Lazima sisi tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 4:19; 5:29.
Mashahidi wa Yehova katika nyakati za kisasa wamefuata mfano wao. Kwa mfano, katika Ujerumani ya Nazi walikataa katakata kujihusisha katika vita za Hitler zenye mauaji mengi. Walikuwa tayari kuvumilia mnyanyaso mkali, hata kufa ikiwa lazima, badala ya kubadili msimamo wao wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote. Inaripotiwa kwamba “nusu ya idadi yao walifungwa gerezani na robo moja ya idadi yao waliuawa” na Wanazi kwa sababu ya kutii kanuni za Biblia. (Kitabu Of Gods and Men) Hivyo, kati ya makumi ya mamilioni ya watu waliokufa katika Vita ya Pili ya Ulimwengu, hakuna hata mmoja aliyeuawa na Shahidi wa Yehova. Badala ya kuwaua wengine, Mashahidi walikuwa tayari kufa, na wengi wao waliuawa kwa sababu hiyo.
Somo Tunaloweza Kujifunza
Ni masomo gani tunayoweza kujifunza kutokana na mambo yaliyopita? Hapana shaka, somo moja tunalojifunza ni hili: Falsafa za wanadamu zimeendelea kusababisha chuki na mauaji kati ya mataifa na makabila. Andiko la Mhubiri 8:9 linasema hivi kwa kufaa: “Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.” (Chapa ya 1989) Na sababu ya jambo hilo inaonyeshwa kwenye Yeremia 10:23, ambapo Neno la Mungu linasema hivi: “Njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” Naam, Mungu hakuwaumba wanadamu wasimamie shughuli zao wenyewe kwa mafanikio, bila kumtegemea. Hawakupewa uwezo huo. Historia yote imethibitisha hilo.
Kwa hiyo, tukiwa watu mmoja-mmoja hatuwezi kubadili mambo ambayo viongozi wa mataifa hufanya wanaposababisha tena misiba ya zamani, wala hatujaruhusiwa kujaribu kuwashawishi kufanya mambo kwa njia fulani. Lakini si lazima tushawishiwe kuhusika na kushiriki katika mapambano yao. Yesu alisema hivi kuhusu wanafunzi wake: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:14) Ili kuepuka kushiriki katika mapambano ya ulimwengu huu, ni sharti tukubali Neno la Mungu, Biblia, liongoze maisha yetu wala si falsafa za wanadamu zenye kubadilika-badilika.—Mathayo 7:24-27; 2 Timotheo 3:16, 17.
Wakati Ujao Mzuri Ajabu
Neno la Mungu lenye kutegemeka halitufahamishi tu kuhusu mambo yaliyopita na yanayotukia sasa. Linatupa mwongozo hakika kuhusu wakati ujao. (Zaburi 119:105; Isaya 46:9-11) Pia, linatuonyesha waziwazi kusudi la Mungu kwa ajili ya sayari hii. Hatawaruhusu wanadamu kuharibu dunia kwa kutumia vibaya uwezo mwingi sana ambao wamepata kutokana na sayansi na tekinolojia. Atahakikisha kwamba dunia itakuwa Paradiso kama alivyokusudia awali.—Luka 23:43.
Kwa habari hiyo, Neno la Mungu linasema hivi: “Maana wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.” (Mithali 2:21, 22) Hilo litatukia hivi punde kwa kuwa hizi siku zenye msukosuko zinaonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu mwovu wa mambo. (2 Timotheo 3:1-5, 13) Na kwa hakika, hizi siku za mwisho zimehesabiwa; zinakaribia kwisha. Unabii wa Biblia hutufundisha hivi: “Ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.”—1 Yohana 2:17; Danieli 2:44.
Karibuni Mungu ‘atawaleta kwenye uangamizi wale wanaoiangamiza dunia’ na ataondoa ulimwengu huu wa sasa wenye jeuri na kuleta ulimwengu mpya ambamo “uadilifu utakaa.” (Ufunuo 11:18; 2 Petro 3:10-13) Kisha, kwa habari ya wale watakaobaki, “atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe.” (Ufunuo 21:1-4) Vita na jeuri hazitakuwapo tena kamwe, kwani unabii ulio kwenye Isaya 2:4 utatimizwa kikamili: “Watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” Wewe pia unaweza kufurahia wakati ujao mzuri ajabu wa milele ukijifunza kutokana na yaliyopita.—Yohana 17:3.
-