-
Samoa2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Mwingine aliyeshinda matatizo makubwa ya afya na kufanya maendeleo ya kiroho ni Saumalu Taua‘anae. Saumalu alikuwa na sura isiyo ya kawaida kwa sababu ya ukoma, naye alikuwa akiishi katika kijiji cha Aopo. Kwa sababu kijiji alichoishi kilikuwa mbali, mwanzoni alijifunza Biblia kupitia barua walizokuwa wakiandikiana na Ivan Thompson. Kisha Asa Coe, painia wa pekee, akahamia Savaii na kuendeleza funzo hilo. Saumalu alipohudhuria mkutano wake wa kwanza mwaka wa 1991, alisafiri kwa gari kwa saa mbili hadi Taga, kijiji kilichokuwa upande wa pili wa kisiwa hicho.
Saumalu hakuwa huru kuchangamana na watu kwa sababu ya sura yake. Hivyo, alipohudhuria kusanyiko la pekee, alisikiliza programu akiwa ndani ya gari lake. Hata hivyo, aliguswa moyo sana kwamba wakati wa mapumziko ya mchana, ndugu na dada walimjia kwa upendo na kumkaribisha kwa moyo mkunjufu. Alikubali mwaliko wao na kusikiliza programu iliyosalia akiwa ameketi pamoja na wasikilizaji wengine.
Punde si punde, Saumalu na mke wake, Torise, wakaanza kuhudhuria mikutano katika kijiji cha Faga, wakisafiri umbali wa zaidi ya saa moja. Saumalu alibatizwa mwaka wa 1993, na baada ya muda akastahili kutumikia akiwa mtumishi wa huduma. Baadaye, hata madaktari walipoukata mguu wake, bado alikuwa akiendesha gari lake kwenda kwenye mikutano. Kijiji chao kimepiga marufuku kazi ya kuhubiri inayofanywa na Mashahidi wa Yehova; kwa hiyo, Saumalu na Torise huwahubiria wengine kwa njia zisizo rasmi na kupitia simu.
Leo, wanaishi Apia, ambapo Saumalu hupata matibabu mbalimbali anayohitaji mara kwa mara. Badala ya kuwa na uchungu moyoni, anajulikana kuwa mtu mwenye matumaini na shangwe maishani. Yeye na mke wake wanaheshimiwa sana kwa sababu ya imani yao yenye nguvu.
-
-
Samoa2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 116]
Saumalu Taua‘anae
-