-
Je, Wewe Umedanganywa?Mnara wa Mlinzi—2011 | Oktoba 1
-
-
Je, Wewe Umedanganywa?
NI MAMBO machache yanayoumiza zaidi kuliko kujua kwamba mtu fulani unayemwamini amekudanganya. Unaweza kukasirika, kuhisi umedharauliwa au hata kusalitiwa. Udanganyifu unavunja urafiki na ndoa; na unafanya watu wapoteze mamilioni ya pesa.
Basi, wazia jinsi ambavyo ungehisi kama ungejua kwamba umedanganywa kumhusu Mungu. Ikiwa unamwogopa Mungu, matokeo yanaweza kuwa mabaya kama ilivyokuwa kwa watu wafuatao ambao walikuwa wafuasi wa dini:
● “Nilihisi kwamba nimesalitiwa na kanisa.”—DEANNE.
● “Nilikasirika. Nilihisi kuwa nimedanganywa, yaani, nilihisi kuwa matumaini na malengo yangu hayana maana yoyote.”—LUIS.
Huenda hata usiwazie kwamba inawezekana kuwa umedanganywa kumhusu Mungu. Yaelekea mambo unayojua kumhusu uliyasikia kutoka kwa mtu unayemwamini na ambaye hawezi kamwe kukuumiza kimakusudi, kama vile mzazi wako, kasisi, pasta, au rafiki wa karibu. Huenda umeamini fundisho fulani katika maisha yako yote. Lakini je, hukubali kwamba fundisho fulani linaweza kuwa la uwongo ingawa watu wengi wanaliamini? Aliyekuwa rais wa Marekani, Franklin D. Roosevelt alitambua jambo hilo, kwa kuwa alisema: “Kurudia-rudia uwongo hakuufanyi kuwa ukweli.”
Unaweza kujua jinsi gani kwamba umedanganywa? Wakati mmoja Yesu alisali hivi kwa Mungu: “Neno lako ni kweli.” (Yohana 17:17) Ndiyo, Neno la Mungu, Biblia, linatusaidia kutofautisha ukweli na uwongo.
Acha tuone mafundisho matano ya uwongo kumhusu Mungu ambayo Biblia inafunua. Utaona jinsi ukweli unavyoweza kubadili maisha yako yawe bora.
-
-
1 Mungu Ni Fumbo—Je, Ni Kweli?Mnara wa Mlinzi—2011 | Oktoba 1
-
-
1 Mungu Ni Fumbo—Je, Ni Kweli?
Jambo ambalo huenda umesikia: “Mungu hufanya kazi kwa njia za mafumbo, au zisizoeleweka.”
“Baba haeleweki, Mwana haeleweki, na Roho Mtakatifu Haeleweki.”—Fundisho la Athanasia linalofafanua Utatu ambao unafundishwa na dini nyingi zinazodai kuwa za Kikristo.
Biblia inafundisha nini?: Yesu alisema kwamba wale ‘wanaopata ujuzi juu ya Mungu wa pekee wa kweli,’ watapata baraka. (Yohana 17:3) Lakini tunaweza kupata ujuzi juu ya Mungu jinsi gani ikiwa yeye ni fumbo, au haeleweki? Badala ya kuficha ukweli kujihusu, Mungu anataka kila mtu amjue.—Yeremia 31:34.
Ni kweli kwamba hatuwezi kujua kila kitu kumhusu Mungu. Hiyo ni kwa sababu mawazo na njia zake ziko juu kuliko zetu.—Mhubiri 3:11; Isaya 55:8, 9.
Jinsi kujua ukweli kunavyokusaidia: Ikiwa Mungu ni fumbo, basi kuna sababu gani ya kujaribu kumjua? Mungu anatuwezesha kumjua na pia kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. Alimrejelea Abrahamu, mwanamume mwaminifu, kuwa ‘rafiki yake,’ naye Mfalme Daudi wa Israeli akaandika: “Urafiki wa karibu pamoja na Yehova ni wa wale wanaomwogopa.”—Isaya 41:8; Zaburi 25:14.
Je, kuwa na urafiki wa karibu pamoja na Mungu ni jambo lisilowezekana? Labda inaonekana hivyo, lakini ona andiko la Matendo 17:27 linavyosema: “[Mungu] hayuko mbali na kila mmoja wetu.” Kwa njia gani? Kupitia Biblia, Mungu anaandaa habari tunazohitaji ili tumjue vizuri.a
Anatuambia jina lake ni Yehova. (Isaya 42:8) Anatueleza katika Biblia jinsi ambavyo ameshughulika na wanadamu ili tuweze kujua yeye ni Mungu wa aina gani. Zaidi ya hayo, Mungu anatufunulia hisia zake. Yeye ni “mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo na kweli.” (Kutoka 34:6) Matendo yetu yanaweza kumfurahisha au kumhuzunisha. Kwa mfano, Waisraeli wa kale ‘walimhuzunisha’ walipomwasi, lakini wale ambao kwa hekima wanamtii, wanafanya ashangilie.—Zaburi 78:40; Methali 27:11.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari zaidi kuhusu yale ambayo Biblia inasema kumhusu Mungu, ona sura ya 1 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
[Blabu katika ukurasa wa 4]
Kama Mungu angekuwa Utatu usioeleweka, tungemjua jinsi gani?
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 4]
The Trinity c.1500, Flemish School, (16th century)/H. Shickman Gallery, New York, USA/The Bridgeman Art Library International
-
-
2 Mungu Hajali—Je, Ni Kweli?Mnara wa Mlinzi—2011 | Oktoba 1
-
-
2 Mungu Hajali—Je, Ni Kweli?
Jambo ambalo huenda umesikia: “Ikiwa kwa kweli Mungu anawajali wanadamu, basi anapaswa kuondoa uovu na mateso ulimwenguni. Na hata kama anawajali wanadamu kwa ujumla, hanijali mimi binafsi.”
Biblia inafundisha nini?: Yehova Mungu hasababishi uovu wala kuteseka. (Yakobo 1:13) Ingawa anaweza kuondoa mambo hayo wakati wowote, anaruhusu watu wapotovu waendelee kuishi ili asuluhishe masuala ambayo yalizushwa mwanzoni mwa historia ya mwanadamu kuhusu uaminifu na utawala. Mwishowe, atachukua hatua ili kuwasaidia wanadamu na kuondoa matatizo yote yanayosababishwa na wale wanaokataa utawala wake.—Mwanzo 3:1-6; Isaya 65:17.a
Ingawa Mungu anawajali wanadamu kwa ujumla, anampenda sana kila mmoja wetu. Andiko la Mathayo 10:29-31 linaonyesha kwamba anaona mambo mengi madogo-madogo kutuhusu ambayo hata sisi wenyewe hatuyajui: “Je, shomoro wawili hawauzwi kwa sarafu ya thamani ndogo? Na bado hakuna hata mmoja wao atakayeanguka chini bila Baba yenu kujua. Lakini nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote. Kwa hiyo msiogope: Ninyi ni bora kuliko shomoro wengi.”
Jinsi kujua ukweli kunavyokusaidia: Kwa kawaida sisi huwaepuka watu ambao ni wakali au wasiojali. Si ajabu kwamba uwongo kuwa Mungu hajali huwafanya watu wengi wasitake kumjua hata kidogo au wasali kwake tu wakati wanaposhindwa kutatua matatizo yao. Ukijua kwamba Yehova Mungu anakujali kikweli, utataka kujifunza mengi zaidi kumhusu na kusitawisha urafiki pamoja naye.
Kwa mfano, huenda ulisali kwa Mungu lakini ukawa na shaka kama anakusikiliza au kama atakujibu. Biblia inatuhakikishia kwamba nyakati zote “msikiaji wa sala” huwasikiliza wote wanaozungumza naye kwa unyofu.—Zaburi 65:2.
Mungu anataka ‘umtupie mahangaiko yako yote, kwa sababu yeye anakujali.’ (1 Petro 5:7) Tunaweza kumtegemea nyakati za taabu kubwa kwa sababu Neno lake linasema: “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.”—Zaburi 34:18.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari zaidi kuhusu sababu zinazofanya Mungu aruhusu wanadamu wateseke, ona sura ya 11 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?
[Blabu katika ukurasa wa 5]
Ikiwa Mungu hajali, kwa nini anatuambia tusali kwake?
-
-
3 Mungu Analipiza Kisasi—Je, Ni Kweli?Mnara wa Mlinzi—2011 | Oktoba 1
-
-
3 Mungu Analipiza Kisasi—Je, Ni Kweli?
Mambo ambayo huenda umesikia: “Mungu anaweka rekodi ya dhambi zote ambazo wanadamu wanafanya, naye hulipiza kisasi kwa kuwaadhibu milele katika moto wa mateso.”
“Mungu anatumia misiba ya asili kuwaadhibu watenda dhambi.”
Biblia inafundisha nini?: Andiko la 2 Petro 3:9 linasema kwamba Yehova “hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” Badala ya kukazia fikira makosa yetu, yeye anakazia fikira sifa zetu nzuri. “Macho [ya Mungu] yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.”—2 Mambo ya Nyakati 16:9.
Moto wa mateso si fundisho la Biblia. Hata wazo la kuwatesa waovu milele katika moto linamchukiza Mungu. Adhabu yake kuu kwa waovu ni kifo. (Yeremia 7:31; Waroma 6:7) Mungu hasababishi misiba ya asili ambayo huharibu bila kuchagua. Misiba hiyo ni matukio yasiyotazamiwa yanayoweza kumpata mtu yeyote.—Mhubiri 9:11.
Jinsi kujua ukweli kunavyokusaidia: Tunaweza kumkaribia Mungu zaidi tunapotambua kwamba yuko “tayari kusamehe” na si mwepesi wa kuhukumu. (Zaburi 86:5) Hatupaswi kumtumikia Mungu kwa sababu tunajihisi tuna hatia au tunaogopa sana kuadhibiwa. Badala yake, tunaweza kusitawisha imani yetu tukiwa na nia inayofaa kabisa—kumpenda Yehova. Upendo huo unakuwa kama nguvu inayotuchochea kufanya yote tuwezayo ili kumfurahisha.—Mathayo 22:36-38; 1 Yohana 5:3.
Ingawa Mungu anataka kila mtu abadilike na kufanya mema, anajua kwamba wengi hawatafanya hivyo. Kama hangechukua hatua dhidi ya wale ambao wameamua kufanya mambo mabaya, basi hangekuwa tofauti na mtawala anayetoa sheria bila kuhakikisha kwamba zinafuatwa, na hivyo kuruhusu ukosefu wa haki na kuteseka kuongezeke bila kufanya lolote. (Mhubiri 8:11) Kujua kwamba Mungu hataendelea kuvumilia uovu milele kunafanya tuwe na tumaini lenye nguvu kuhusu wakati ujao. Mungu ameahidi kuondoa wale wanaoendelea kufanya mambo maovu, ili “wapole” wafurahie uzima wa milele duniani kama alivyokusudia mwanzoni.—Zaburi 37:10, 11, 29.a
[Maelezo ya Chini]
a Ili kujifunza mengi zaidi kuhusu jinsi Mungu atakavyofanya dunia kuwa paradiso, ona sura ya 3 na ya 8 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?
[Blabu katika ukurasa wa 6]
Je, Mungu angetaka tumwabudu kwa sababu tunaogopa kuadhibiwa?
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 6]
Engravings by Doré
-
-
4 Mungu Hatendi kwa Haki—Je, Ni Kweli?Mnara wa Mlinzi—2011 | Oktoba 1
-
-
4 Mungu Hatendi kwa Haki—Je, Ni Kweli?
Jambo ambalo huenda umesikia: “Mungu ndiye anayeutawala ulimwengu huu, na kila kitu kinatendeka kwa mapenzi yake. Kwa hiyo, kwa kuwa ulimwengu umejaa ukosefu wa haki, ukandamizaji, na ubaguzi yeye ndiye anayepaswa kulaumiwa.”
Biblia inafundisha nini?: Mungu hasababishi ukosefu wa haki ulimwenguni. Biblia inasema hivi kumhusu Yehova: “Kazi zake ni kamilifu, kwa maana njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, ambaye hana ukosefu wowote wa haki.”—Kumbukumbu la Torati 32:4.
Mungu ni mkarimu kwa wote, hata kwa wale wanaoonekana kama hawastahili. Kwa mfano, “yeye hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” (Mathayo 5:45) Anawatendea kwa haki watu wa jamii na tamaduni zote, kama andiko la Matendo 10:34, 35 linavyoonyesha: “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”
Hivyo basi, chanzo cha ukosefu wa haki ni nini? Watu wengi huchagua kutenda isivyo haki, wakikataa kumwiga Mungu ambaye anafuata haki. (Kumbukumbu la Torati 32:5) Pia, Biblia inaonyesha kwamba Mungu amemruhusu adui yake Ibilisi autawale ulimwengu.a (1 Yohana 5:19) Hata hivyo, hivi karibuni Mungu ataukomesha utawala wa Ibilisi ambao haufuati haki. Tayari ameandaa njia yake ya ‘kuzivunja kazi za Ibilisi.’—1 Yohana 3:8.
Jinsi kujua ukweli kunavyokusaidia: Unaweza kushangazwa na ripoti nyingi zinazotolewa kuhusu ufisadi, ukandamizaji, na ukosefu wa haki. Kujua chanzo cha matatizo hayo kutakusaidia uelewe kwa nini hali ni mbaya sana na kwa nini jitihada za mwanadamu za kuwa na ulimwengu bora hushindwa nyakati zote. (Zaburi 146:3) Badala ya kutumia wakati na nguvu kufanya mabadiliko ambayo ni ya muda tu, unaweza kuwa na tumaini hakika kuhusu wakati ujao linalotegemea imani yako katika ahadi za Mungu.—Ufunuo 21:3, 4.
Kuelewa chanzo halisi cha ukosefu wa haki kutatusaidia hasa tunapopatwa na matatizo. Tunapotendewa isivyo haki, huenda tukasema kama mtumishi wa Mungu Habakuki: “Sheria hufa ganzi, na haki haitendeki kamwe.” (Habakuki 1:4) Mungu hakumkemea Habakuki kwa kusema hivyo. Badala yake, alimhakikishia Habakuki kwamba ameweka wakati wa kurekebisha mambo na akamsaidia kupata furaha wakati huo wa taabu. (Habakuki 2:2-4; 3:17, 18) Vivyo hivyo, kuamini ahadi ya Mungu kwamba ataondoa ukosefu wa haki kunaweza kukusaidia kupata utulivu na amani ya akili katika ulimwengu huu usiofuata haki.
[Maelezo ya Chini]
a Ili kujua Ibilisi alitoka wapi, ona sura ya 3 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?
[Blabu katika ukurasa wa 7]
Je, kweli Mungu ndiye anayesababisha mateso na ukosefu wa haki?
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 7]
© Sven Torfinn/Panos Pictures
-
-
5 Mungu Anakubali Ibada Yoyote Ile Ikiwa Tu Inatoka Moyoni—Je, Ni Kweli?Mnara wa Mlinzi—2011 | Oktoba 1
-
-
5 Mungu Anakubali Ibada Yoyote Ile Ikiwa Tu Inatoka Moyoni—Je, Ni Kweli?
Jambo ambalo huenda umesikia: “Kama vile tu kulivyo na njia na barabara nyingi za kwenda mahali fulani, ndivyo pia kulivyo na njia nyingi za kumfikia Mungu. Kila mtu anapaswa kutafuta njia yake mwenyewe ya kumfikia Mungu.”
Biblia inafundisha nini?: Ni lazima tumwabudu Mungu kwa unyofu wa moyo, bila unafiki. Yesu aliwaambia viongozi wa kidini wa siku zake sababu iliyofanya Mungu awakatae: “Isaya kwa kufaa alitoa unabii juu yenu wanafiki, kama ilivyoandikwa, ‘Watu hawa huniheshimu mimi kwa midomo yao, bali mioyo yao iko mbali nami.’” (Marko 7:6) Hata hivyo, unyofu wa moyo peke yake si uhakikisho wa kwamba Mungu atakubali ibada yetu.
Yesu alionyesha jambo hilo waziwazi kwa kufunua kasoro kubwa katika ibada iliyotolewa na viongozi hao wa kidini na wafuasi wao. Alitumia maneno haya ya Mungu kuwahusu: “Wao huniabudu bure, kwa sababu wao hufundisha amri za wanadamu kuwa mafundisho.” (Marko 7:7) Ibada yao ilikuwa ya “bure,” au isiyo na maana yoyote, kwa sababu badala ya kutanguliza matakwa ya Mungu walitanguliza mapokeo yao ya kidini.
Biblia haiungi mkono wazo la kwamba kuna njia nyingi zinazokubalika za kumfikia Mungu, badala yake, inafundisha kwamba kuna njia moja tu. Andiko la Mathayo 7:13, 14 linasema: “Ingieni kupitia lango jembamba; kwa sababu barabara inayoongoza kwenye uharibifu ni pana na kubwa, na wengi ndio wanaoipitia; lakini lango ni jembamba na barabara inayoongoza kwenye uzima ina nafasi ndogo, na wachache ndio wanaoipata.”
Jinsi kujua ukweli kunavyokusaidia: Wazia jinsi ambavyo ungehisi kama ungefanya mazoezi kwa miezi kadhaa, kisha ushiriki katika mbio za masafa marefu na kushinda, lakini kwa sababu ya kuvunja sheria fulani bila kujua, unapokonywa taji lako. Ungehisi kwamba jitihada zako zote zilikuwa za bure. Je, inaweza kuwa hivyo kuhusiana na ibada yetu kwa Mungu?
Akilinganisha ibada yetu na mashindano ya mbio, mtume Paulo aliandika: “Kama yeyote akishindana hata katika michezo, havikwi taji isipokuwa awe ameshindana kulingana na sheria.” (2 Timotheo 2:5) Tunapata kibali cha Mungu kwa kumwabudu “kulingana na sheria,” yaani, katika njia ambayo yeye anakubali. Hatuwezi kujichagulia njia yetu wenyewe ya kumfikia Mungu kama vile tu mkimbiaji asivyoweza kukimbia jinsi anavyotaka na atazamie kutangazwa mshindi.
Ili kumfurahisha Mungu, ni lazima tuepuke kuchanganya ibada yetu na mafundisho ya uwongo kumhusu. Yesu alisema: “Waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa roho na kweli.” (Yohana 4:23) Tunajifunza kuhusu njia ya kweli ya kumfikia Mungu katika Neno lake Biblia.—Yohana 17:17.a
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari zaidi kuhusu ibada ambayo Mungu anakubali, ona sura ya 15 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?
[Blabu katika ukurasa wa 8]
Je, dini zote zinawafundisha watu wamwabudu Mungu kwa njia ambayo yeye anakubali?
-
-
Ukweli Unaweza Kubadili Maisha YakoMnara wa Mlinzi—2011 | Oktoba 1
-
-
Ukweli Unaweza Kubadili Maisha Yako
HUENDA umesikia au umefundishwa mojawapo ya mafundisho ya uwongo kumhusu Mungu ambayo yamefunuliwa katika makala zilizotangulia. Hata hivyo, huenda ukasitasita kubadili imani yako kuhusu fundisho hilo, hasa ikiwa umeliamini kwa muda mrefu.
Hali hiyo ya kusitasita inaeleweka. Dini fulani hazipendi kulinganisha mafundisho yao na yale ambayo Biblia inasema. Nyingine hujaribu kutetea mafundisho yao ya uwongo kwa kusema kwamba si rahisi kuilewa Biblia, hivyo haikusudiwi kueleweka na kila mtu. Hata hivyo, wengi wa wanafunzi wa Yesu walikuwa watu wa kawaida tu, wasio na elimu ya juu, na walielewa kwa urahisi mambo aliyofundisha.—Matendo 4:13.
Huenda ukasitasita kuchunguza kama mafundisho unayoamini ni ya kweli ukiogopa kwamba kufanya hivyo kutaonyesha ukosefu wa imani. Lakini je, unafikiri ni jambo linalopatana na akili kwamba Mungu hatapendezwa nawe eti kwa sababu umeamua kuchunguza Biblia, ujumbe wake kwa wanadamu, ili kuelewa anachotaka ufanye? Kinyume cha hilo, Neno lake linakutia moyo uyachunguze Maandiko kibinafsi, linaposema: ‘Jihakikishieni wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.’—Waroma 12:2.
Kujifunza ukweli kumhusu Mungu kunamaanisha mengi zaidi ya kupata tu ujuzi—kunaweza kuboresha maisha yako. (Yohana 8:32) Sasa Deanne, aliyetajwa katika makala ya kwanza, amesitawisha imani inayotegemea Neno la Mungu. Anasema: “Sikujua kamwe kwamba kuelewa Maandiko si jambo gumu hadi nilipoanza kujifunza Biblia. Sasa ninamjua Yehova kama Baba yangu wa mbinguni mwenye upendo, bali si kama Mungu tu nisiyeweza kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. Sasa nimepata kusudi halisi maishani.”
Labda umewahi kujifunza Biblia lakini hukuona kama unafaidika. Ikiwa ndivyo, usikate tamaa. Kujaribu kuilewa Biblia ukiwa umefundishwa mambo ya uwongo kumhusu Mungu ni kama kufunga safari ya kwenda mahali ambako hujui ukitumia ramani ambayo si sahihi. Huenda ukaanza safari yako vizuri, lakini ukakata tamaa baada ya kukosea njia mara kadhaa. Hivyo, ikiwa unataka kufika mahali hapo, anza safari kwa kufuata barabara inayofaa ukiwa na ramani yenye maelezo sahihi kuhusu mahali unakoenda.
-