-
Kwa Nini Tupo Hapa?Amkeni!—2008 | Desemba
-
-
Kwa Nini Tupo Hapa?
Ni nini kusudi la uhai?
MARA nyingi watu wamejiuliza maswali yaliyo hapo juu. Pia wao hujiuliza: Je, kuna kusudi lingine isipokuwa kuishi kwa miaka 70 au 80 kisha tufe?—Zaburi 90:9, 10.
Huenda tukajiuliza maswali kama hayo hasa tunapotambua kwamba maisha yetu ni mafupi sana. Bila shaka, si lazima tuwe tunakabili hatari maishani ili kujiuliza kwa nini tupo hapa. Kukata tamaa pia kunaweza kutufanya tujiulize swali hilo. Na watu wengine hujiuliza swali hilo wanapotafakari juu ya maisha yao.
Dave alikuwa na kazi yenye mshahara mnono, nyumba nzuri, na alifurahia kuwa pamoja na marafiki wake. Anasema hivi: “Usiku mmoja nilikuwa nikirudi nyumbani kutoka kwenye sherehe nilipojiuliza swali hili, ‘Je, hili ndilo kusudi la uhai?—Je, nitaishi kwa muda mfupi tu kisha nife? Au je, kuna kusudi lingine?’ Jambo lililonisumbua ni kugundua sikuwa na kusudi maishani wakati huo.”
Katika kitabu chake Man’s Search for Meaning, Viktor Frankl alisema kwamba baada ya kuachiliwa kutoka katika kambi za mateso, baadhi ya waokokaji wenzake wa yale Maangamizi Makubwa waliuliza swali kama hilo. Waliporudi nyumbani, baadhi yao walikuta kwamba wapendwa wao walikuwa wameangamia. Frankl aliandika hivi: “Ole wake yule ambaye siku ya kuachiliwa, alikuta maisha yakiwa tofauti sana kuliko alivyotarajia!”
Watu Wanaouliza Swali Hilo
Swali kuhusiana na kusudi la uhai limeulizwa na watu katika vizazi vyote. Biblia inatuambia kuhusu watu waliotaka kujua maisha yana kusudi gani. Ayubu aliuliza hivi baada ya kupoteza mali na watoto wake na alipougua ugonjwa mbaya: “Kwa nini sikufa tokea tumbo la uzazi? Kwa nini sikutoka tumboni kisha nikate pumzi?”—Ayubu 3:11.
Nabii Eliya alihisi vivyo hivyo. Huku akihisi kwamba yeye ndiye mwabudu pekee wa Mungu, alilalamika hivi: “Inatosha! Sasa, Ee Yehova, iondoe nafsi yangu.” (1 Wafalme 19:4) Watu wengi sana wamehisi hivyo. Kwa kweli, Biblia inamfafanua Eliya kuwa “mtu mwenye hisia kama zetu.”—Yakobo 5:17.
Safari Yenye Mafanikio Maishani
Maisha hulinganishwa na safari. Kama vile unavyoweza kuanza safari bila kufikiria utafika wapi, unaweza kuishi bila kutambua kusudi halisi la maisha. Ukifanya hivyo, utakuwa kama watu ambao mwandishi anayejulikana Stephen R. Covey anasema wanatafuta kusudi kwa kufanya maisha yawe yenye shughuli nyingi sana. Aliandika kuhusu wale ambao “wanapata mafanikio yasiyo na maana, mafanikio ambayo wamepata kwa kupoteza vitu ambavyo ghafula wanatambua vilikuwa vya muhimu zaidi kwao.”
Je, hukubali kwamba kuongeza mwendo katika safari ni bure ikiwa hatuelekei upande unaofaa? Vivyo hivyo, kutafuta kusudi maishani kwa kuwa na shughuli nyingi hakutaleta uradhi wa kweli.
Tamaa ya kujua kwa nini tupo hapa ni kawaida kwa watu wa utamaduni na umri mbalimbali. Inatokana na uhitaji muhimu ambao sote tunao, uhitaji wa kiroho ambao hauwezi kutoshelezwa hata baada ya mahitaji yetu ya kimwili kutimizwa. Hebu ona jinsi wengine wamejaribu kutosheleza uhitaji huo wanapotafuta kusudi la maisha.
[Blabu katika ukurasa wa 4]
Kutafuta kusudi maishani kwa kuwa na shughuli nyingi hakutaleta uradhi wa kweli
[Picha katika ukurasa wa 3]
Ayubu aliuliza kwa nini alizaliwa
[Picha katika ukurasa wa 4]
Eliya alikuwa na “hisia kama zetu”
-
-
Unaweza Kupata Wapi Majibu?Amkeni!—2008 | Desemba
-
-
Unaweza Kupata Wapi Majibu?
LENGO moja la dini ni kufundisha kuhusu kusudi la uhai. Hata hivyo, watu wengi wametambua kwamba mahitaji yao ya kiroho hayajatoshelezwa na mafundisho ya dini zao. Denise aliyelelewa na wazazi Wakatoliki, anakumbuka: “Katekisimu ya Baltimore inatia ndani swali hili, ‘Kwa nini Mungu alituumba?’ na inajibu hivi, ‘Mungu alituumba ili kuonyesha wema Wake na kushiriki nasi furaha Yake ya milele mbinguni.’
“Hilo halikunieleza ni kwa nini nipo hapa,” Denise anaendelea. “Ikiwa ninangojea tu kwenda mbinguni, ninapaswa kuwa nikifanya nini sasa?” Watu wengi wana mawazo kama ya Denise. Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba asilimia 66 hivi ya wale waliohojiwa wanaamini kwamba kanisa na masinagogi mengi hayawasaidii watu kupata kusudi maishani.
Kwa sababu hiyo, wanatafuta majibu kwingineko, iwe ni kupitia sayansi au falsafa za aina mbalimbali. Kwa nini watu wanaendelea kutafuta majibu, ingawa ni wachache tu wanaoonekana kupata uradhi?
Tuna Uhitaji wa Kiroho
Dakt. Kevin S. Seybold anasema kwamba kuna “mwelekeo wa wanadamu ulimwenguni pote wa kuabudu kitu fulani.” Katika miaka ya karibuni wanasayansi kadhaa wamefikia mkataa wa kwamba wanadamu wamezaliwa na mwelekeo wa kutafuta kusudi halisi maishani. Watu fulani wanaamini kwamba chembe za urithi na utendaji wa wanadamu unaonyesha kwamba wanadamu wana uhitaji wa asili wa kuwa na uhusiano na nguvu zisizo za kawaida.
Ingawa wasomi wanatilia shaka wazo la kwamba wanadamu wana uhitaji wa kiroho, watu wengi hawahitaji uchunguzi wa kisayansi ili waamini jambo hilo. Ni uhitaji huo wa kiroho ambao hufanya tujiulize yale ambayo watu fulani wameyaita maswali muhimu zaidi: Kwa nini tupo hapa? Tunapaswa kufanya nini na maisha yetu? Je, tunawajibika kwa Muumba Mweza-Yote?
Ukitenga wakati kuchunguza ulimwengu wa asili, utapata baadhi ya majibu ya maswali hayo. Kwa mfano, fikiria vitu vya asili vyenye kutatanisha, kuanzia viumbe vyenye chembe moja hadi makundi ya nyota yaliyo mbali sana angani. Je, havituonyeshi kwamba kuna Mbuni, au Muumba mwenye akili? Biblia inasema hivi: “Kwa maana sifa [za Mungu] ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu, hivi kwamba hawana sababu ya kujitetea.”—Waroma 1:20.
Tosheleza Uhitaji Wako wa Kiroho
Biblia inasema hivi kuhusiana na jinsi Mungu alivyowaumba wanadamu: “Ameweka milele vilevile ndani ya mioyo yao.” (Mhubiri 3:11, Zaire Swahili Bible) Tumezaliwa na tamaa ya kuishi, si kufa. Tuna tamaa ya kupata kusudi la maisha, kujua majibu ya maswali.
Kwa hiyo, ni kawaida kwa wanadamu kuuliza maswali. Baada ya kutaja kuhusu maendeleo ya kisayansi na kitekinolojia, mhariri wa jarida The Wall Street Journal aliandika: “Bado tunajiuliza sisi ni nani na kwa nini tupo hapa na tunaelekea wapi.” Kwa hekima, tutatafuta majibu kutoka chanzo bora zaidi. Biblia inasema hivi kuhusu Chanzo hicho: “[Mungu] ndiye aliyetufanya, wala si sisi wenyewe.”—Zaburi 100:3.
Je, haipatani na akili kumtazamia Yule aliyefanya miujiza kama ile ya uumbaji atosheleze uhitaji wetu wa kiroho? Yesu Kristo alipendekeza kwamba tufanye hivyo. Alitambua kwamba Muumba wetu ambaye ndiye Chanzo pekee cha uhai, anaweza kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho.—Zaburi 36:5, 9; Mathayo 5:3, 6.
Kwa kweli, kupata jibu linalotegemeka la swali hili, Kwa nini tupo hapa? ni muhimu ili kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho. Tafadhali fikiria maoni yenye kupendeza ya Muumba wetu kuhusu jambo hilo.
-