Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Watu Wanaweza Kuishi Muda Mrefu Kadiri Gani?
    Mnara wa Mlinzi—2004 | Novemba 15
    • Watu Wanaweza Kuishi Muda Mrefu Kadiri Gani?

      MACHI 3, 1513, mvumbuzi Mhispania Juan Ponce de León alifunga safari muhimu. Alisafiri kwa meli kutoka Puerto Riko akitumaini kufika kisiwa cha Bimini. Kulingana na hekaya, alikuwa akitafuta chemchemi ya kimuujiza—Chemchemi ya Ujana. Lakini safari yake ilimfikisha jimbo ambalo sasa ni Florida, Marekani. Bila shaka, hakuipata ile chemchemi ya ujana kwa kuwa hakuna chemchemi kama hiyo.

      Leo, wanadamu kwa ujumla hawaishi zaidi ya miaka 70 au 80. Ingawa Biblia hutaja watu walioishi miaka mingi, kitabu 2002 Guinness Book of World Records husema kwamba mwanadamu aliyepata kuishi muda mrefu zaidi aliishi miaka 122 na siku 164. (Mwanzo 5:3-32) Hata hivyo, John Harris, mtaalamu wa elimu-maadili ya kibiolojia alisema hivi: “Utafiti mpya unaonyesha kwamba huenda ikawezekana kuwa na jamii ambayo haitazeeka au hata kufa.” Wataalamu wengi wa karne ya 21 huzungumza juu ya “hali ya kutoweza kufa kabisa,” “uhai usio na kikomo kufikia mwaka wa 2099,” “uwezekano wa chembe za mwili kuendelea kuongezeka bila kukoma,” na mambo kama hayo.

      Katika kitabu chake The Dream of Eternal Life, Mark Benecke anasema hivi: “Karibu chembe zote za mwili hufanyizwa upya mara kadhaa maishani. . . . Baada ya miaka saba hivi, sisi huwa na mwili mpya kihalisi.” Hata hivyo, jambo hilo haliendelei milele kwa sababu chembe huacha kuongezeka baada ya kujigawanya mara ambazo zimeratibiwa. Benecke anasema kwamba kama chembe hazingeacha kujigawanya, “mwili wa binadamu ungeendelea kujifanyiza upya kwa muda mrefu sana—hata milele.”

      Fikiria pia uwezo mkubwa ajabu wa ubongo wa mwanadamu. Sisi hutumia sehemu ndogo sana ya ubongo wetu wakati wa maisha yetu mafupi. Kulingana na kitabu Encyclopædia Britannica, ubongo wa mwanadamu “una uwezo mkubwa sana hivi kwamba mwanadamu hawezi kuutumia wote wakati wa maisha yake.” (Chapa ya 1976, Buku la 12, ukurasa wa 998) Kitabu How the Brain Learns, kilichoandikwa na David A. Sousa chasema hivi: “Kwa kweli, ubongo una uwezo usio na kikomo wa kuhifadhi habari.”—Ukurasa wa 78, Chapa ya Pili, haki ya kunakili 2001.

      Kwa nini watafiti wameshindwa kupata sababu za kiasili zinazosababisha kifo? Na kwa nini ubongo wa mwanadamu una uwezo mkubwa hivyo? Je, inawezekana kwamba tuliumbwa ili tuendelee kujifunza milele? Kwa nini tunaweza kuwazia kuishi milele?

      Biblia inasema: “Tena wakati usio na kipimo [Mungu] ameuweka ndani ya moyo wao, ili mwanadamu asiweze kugundua kazi ambazo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho.” (Mhubiri 3:11) Maneno hayo yanaonyesha kwamba Mungu aliweka ndani yetu wazo la kuishi milele ili daima tuweze kujifunza mambo fulani kumhusu yeye na kazi zake. Ikiwa tungeishi kwa mabilioni ya miaka—naam, milele—tungeweza kujifunza daima mambo mengi sana kuhusu maajabu ya kazi za Mungu za uumbaji.

      Maneno ya Yesu Kristo pia yanaonyesha kwamba wanadamu wanaweza kuishi milele. Alisema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Namna gani wewe? Je, unataka kuishi milele?

      [Picha katika ukurasa wa 3]

      Juan Ponce de León alitafuta chemchemi ya ujana

      [Hisani]

      Ponce de León: Harper’s Encyclopædia of United States History

  • Je, Unataka Kuishi Milele?
    Mnara wa Mlinzi—2004 | Novemba 15
    • Je, Unataka Kuishi Milele?

      “MIMI siogopi kufa,” akasema mwanamke mmoja mzee huko Japani. “Lakini jambo linalonihuzunisha ni kwamba nitayaacha maua haya.” Mhudumu Mkristo aliyemtembelea nyumbani kwake alielewa alichomaanisha kwa kuwa mwanamke huyo alikuwa na bustani maridadi. Wengi wanaosema kwamba hawaogopi kufa kwa kweli hufurahia maajabu ya uumbaji na hata huenda wakatamani kuishi milele.

      Kuishi milele? Wengi wangepuuza wazo hilo. Huenda hata wengine wakasema kwamba hawatamani kuishi milele. Kwa nini huenda wakahisi hivyo?

      Je, Uzima wa Milele Utachosha?

      Wengine hufikiri kwamba kuishi milele kutachosha. Huenda wakataja maisha yenye kuchosha ya watu wengi waliostaafu ambao huketi tu kitako na kutazama televisheni. Ikiwa una maoni hayo, hebu fikiria jibu la mtaalamu wa anga Robert Jastrow alipoulizwa ikiwa kuishi milele kungekuwa baraka au laana. Jastrow alijibu hivi: “Ni baraka kwa watu wenye akili ya kudadisi mambo na walio na hamu isiyoisha ya kujifunza. Wao wangefarijika sana kuwazia kwamba watajifunza milele. Lakini kwa wale ambao hawapendi kujifunza mambo mapya na wenye akili finyu, kuishi milele ni laana mbaya sana. Hawatakuwa na jambo la kufanya.”

      Mtazamo wako utaamua ikiwa kuishi milele kutachosha au la. Ikiwa una ‘akili ya kudadisi mambo na hamu isiyoisha ya kujifunza,’ fikiria yale unayoweza kutimiza katika mambo ya sanaa, muziki, usanifu wa majengo, utunzaji wa bustani, au kazi nyingine yoyote unayopenda. Kuishi milele hapa duniani kutakupatia nafasi zuri ya kutumia kikamili uwezo wako wa kufanya mambo mbalimbali.

      Maisha yatakuwa yenye kuridhisha kwelikweli kwa kuwa tutaweza kuonyesha na kuonyeshwa upendo milele. Tumeumbwa tukiwa na uwezo wa kuonyesha upendo, nasi husitawi tunapoonyeshwa upendo. Kuonyeshana upendo wa kweli huridhisha sana na upendo huo haupungui kadiri wakati unavyopita. Kuishi milele kutatupatia nafasi nyingi za kusitawisha upendo kwa wanadamu wenzetu na hasa kwa Mungu. Mtume Paulo alisema kwamba “ikiwa yeyote anampenda Mungu, huyo anajulikana naye.” (1 Wakorintho 8:3) Kumjua na kujulikana na Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote ni tarajio zuri kama nini! Isitoshe, hakuna kikomo cha kujifunza kumhusu Muumba wetu mwenye upendo. Hivyo basi, kuishi milele hakutachosha wala hakutakosa kuridhisha.

      Maisha Ni Mafupi na Yenye Thamani

      Wengine hufikiri kwamba maisha ni yenye thamani kwa sababu ni mafupi. Huenda wakalinganisha uhai na dhahabu, ambayo haipatikani kwa urahisi. Wao husema kwamba ikiwa dhahabu ingeweza kupatikana kila mahali, basi thamani yake ingepungua. Lakini bado dhahabu ingekuwa kitu chenye kupendeza. Ndivyo ilivyo na uhai.

      Tunaweza kulinganisha kuishi milele na kuwa na hewa nyingi. Mgodi unapoporomoka, wachimbaji waliofukiwa hutamani sana hewa. Baada ya kuokolewa, je, unafikiri wataanza kulalamika bila shukrani kwamba kuna hewa nyingi sana? Sivyo.

      Kama wachimbaji-migodi hao, tunaweza kuokolewa na kuwa na tarajio kubwa la kupata uzima wa milele. “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo,” akaandika mtume Paulo, “lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.” (Waroma 6:23) Kupitia dhabihu ya fidia ya Yesu, Mungu ataondoa kutokamilika kwa kibinadamu na kifo na kuwapa wanadamu watiifu zawadi ya uzima wa milele. Tunapaswa kushukuru kama nini kwa mpango huo wenye upendo!

      Namna Gani Wapendwa Wako?

      Huenda watu fulani wakauliza: ‘Namna gani wapendwa wangu? Uzima wa milele hapa duniani hautakuwa na faida yoyote kwangu ikiwa hawatakuwa pamoja nami.’ Pengine umejifunza Biblia na kupata kujua kwamba kuna uwezekano wa kufurahia uzima wa milele katika paradiso duniani. (Luka 23:43; Yohana 3:16; 17:3) Bila shaka, ungependa washiriki wa familia yako ya karibu, wapendwa wako wengine, na rafiki wapendwa wawe katika paradiso hiyo, nyote mkifurahia baraka ambazo wewe unatumaini kupata katika ulimwengu mpya wenye uadilifu ambao Mungu ameahidi.—2 Petro 3:13.

      Lakini namna gani ikiwa rafiki zako na wapendwa wako hawataki kuishi milele katika dunia paradiso? Usivunjike moyo. Endelea kutwaa ujuzi sahihi wa Maandiko na kuishi kupatana nao. Mtume Paulo aliandika hivi: “Wewe mama Mkristo, unawezaje kuwa na hakika kwamba hutaweza kumwokoa mume wako? Au wewe mume Mkristo, unawezaje kuwa na hakika kwamba hutaweza kumwokoa mkeo?” (1 Wakorintho 7:16, Biblia Habari Njema) Watu wanaweza kubadilika. Kwa mfano, mwanamume fulani ambaye wakati mmoja alipinga Ukristo, alibadilika na baadaye akawa mzee katika kutaniko la Kikristo. Anasema hivi: “Nashukuru sana kwamba familia yangu ninayoipenda ilishikilia kanuni za Biblia kwa uaminifu licha ya upinzani wangu.”

      Mungu anajali sana uhai wako na uhai wa wapendwa wako. Kwa kweli, “Yehova . . . hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:9) Yehova Mungu anataka wewe na wapendwa wako mwishi milele. Upendo wake ni mkubwa sana kuliko upendo wa wanadamu wasio wakamilifu. (Isaya 49:15) Hivyo basi, sitawisha uhusiano mzuri pamoja na Mungu. Ukifanya hivyo, huenda ukawasaidia wapendwa wako wasitawishe uhusiano naye. Hata kama hawana tumaini la kuishi milele kwa sasa, mtazamo wao unaweza kubadilika wanapokuona ukiishi kupatana na ujuzi sahihi wa Biblia.

      Namna gani wapendwa wako ambao huenda wamekufa? Biblia inatoa tumaini zuri kwamba mamilioni ambao wamekufa, watafufuliwa, yaani, wataamshwa kutoka katika kifo ili waishi milele kwenye paradiso duniani. Yesu Kristo aliahidi hivi: ‘Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watatoka.’ (Yohana 5:28, 29) Hata wale waliokufa kabla ya kumjua Mungu watafufuliwa, kwa kuwa Biblia inasema: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Itakuwa furaha iliyoje kuwakaribisha watu hao kutoka kwa wafu!

      Uzima wa Milele —Tarajio Lenye Kufurahisha

      Ikiwa unaweza kuwa na furaha na uradhi sasa licha ya matatizo yote yaliyomo duniani, basi bila shaka utaweza kufurahia kuishi milele katika paradiso duniani. Mmoja wa Mashahidi wa Yehova alipomweleza mwanamke fulani kuhusu baraka za uzima wa milele, mwanamke huyo alijibu hivi: “Mimi sitaki kuishi milele. Maisha haya ya miaka 70 au 80 yamenitosha.” Mkristo mmoja anayetumikia akiwa mzee ambaye alikuwepo alimuuliza hivi: “Je, umewahi kufikiria jinsi watoto wako watakavyohisi ukifa?” Mwanamke huyo alitiririkwa na machozi alipofikiria huzuni ambayo wangepata kwa kumpoteza mama yao. Alikiri hivi: “Kwa mara ya kwanza nilitambua kwamba nilikuwa na ubinafsi. Sasa ninatambua kwamba kuishi milele si tumaini lenye ubinafsi, linahusisha wengine pia.”

      Wengine hufikiri kwamba hakuna anayejali ikiwa wataishi au kufa. Hata hivyo, Yule aliyetupa uhai anajali, naye anasema: “Kama ninavyoishi, . . . ninapendezwa, si na kifo cha mwovu, bali kwamba mtu mwovu ageuke na kuiacha njia yake na kwa kweli aendelee kuishi.” (Ezekieli 33:11) Kwa kuwa Mungu anajali sana hata uhai wa waovu, bila shaka yeye huwajali sana wale wanaompenda.

      Mfalme Daudi wa Israeli la kale alikuwa na uhakika kwamba Yehova anampenda na kumjali. Pindi fulani Daudi alisema hivi: “Hata ikiwa baba yangu na mama yangu wangeniacha, Yehova mwenyewe angenichukua.” (Zaburi 27:10) Huenda Daudi alikuwa na uhakika kwamba wazazi wake walimpenda. Lakini hata kama wazazi wake—watu wa ukoo wa karibu sana—wangemwacha, alijua kwamba Mungu hangemwacha. Kwa kuwa Yehova anatupenda na kutujali, yeye hututolea nafasi ya kupata uzima wa milele na kuwa na urafiki usio na kikomo pamoja naye. (Yakobo 2:23) Je, hatupaswi kukubali zawadi hizo nzuri kwa shukrani?

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Upendo kwa Mungu na jirani utafanya kuishi milele kuwe jambo la maana

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki