Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Kweli Uhai Udumuo Milele Wawezekana?
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Aprili 15
    • Je, Kweli Uhai Udumuo Milele Wawezekana?

      “Mwalimu, ni lazima nifanye wema gani kusudi nipate uhai udumuo milele?”—MATHAYO 19:16.

      1. Ni nini liwezalo kusemwa kuhusu urefu wa maisha yetu ya kibinadamu?

      MFALME Mwajemi Shasta wa Kwanza, aitwaye Ahasuero katika Biblia, alikuwa akilikagua jeshi lake kabla ya pigano mwaka wa 480 K.W.K. (Esta 1:1, 2) Kulingana na mwanahistoria Mgiriki Herodoto, mfalme alitokwa machozi alipowatazama wanaume wake. Kwa sababu gani? “Yanihuzunisha,” Shasta akasema, “nifikiriapo juu ya ufupi wa maisha ya mwanadamu. Kwa kuwa watu hawa wote, hakuna hata mmoja atakayekuwa hai miaka mia moja kutoka sasa.” Huenda wewe pia umeona kwamba maisha ni mafupi vya kusikitisha na kwamba hakuna yeyote anayetaka kuzeeka, kuwa mgonjwa, na kufa. Ah, laiti tungeweza kufurahia maisha katika hali na furaha ya ujana!—Ayubu 14:1, 2.

      2. Watu wengi huwaza juu ya tumaini gani, na kwa nini?

      2 Ni jambo la maana kwamba The New York Times Magazine la Septemba 28, 1997, lilikuwa na makala “Wao Wataka Kuishi.” Lilimnukuu mtafiti aliyesema haya: “Kwa kweli naamini kwamba huenda tukawa kizazi cha kwanza ambacho kitaishi milele”! Huenda wewe pia unaamini kwamba uhai udumuo milele wawezekana. Huenda ukafikiri hivyo kwa sababu Biblia yaahidi kwamba twaweza kuishi milele hapa duniani. (Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3, 4) Ingawa hivyo, watu fulani huamini kwamba uhai udumuo milele wawezekana ikitegemea sababu nyingine mbali na zile zipatikanazo katika Biblia. Kuchunguza sababu mbili kati ya hizo kutatusaidia tutambue kwamba kweli uhai udumuo milele wawezekana.

      Tumebuniwa Tuishi Milele

      3, 4. (a) Kwa nini watu wengine huamini kwamba twapaswa kuishi milele? (b) Daudi alisema nini kuhusu jinsi alivyoumbwa?

      3 Sababu moja inayowafanya watu wengi waamini kwamba wanadamu wapaswa kuishi milele yahusiana na jinsi ambavyo tumeumbwa kwa namna ya ajabu. Kwa mfano, ni jambo la kimwujiza kweli jinsi tulivyoumbwa ndani ya tumbo la uzazi la mama yetu. Mtu mmoja mwenye ujuzi juu ya hali ya kuzeeka aliandika hivi: “Baada ya kufanya miujiza inayotupata kutoka kutungwa mimba hadi kuzaliwa kisha hadi upevuko wa kingono na utu uzima, hali-asili ilichagua kutounda kile kionekanacho kuwa mfumo wa utendaji ulio sahili zaidi ambao ungedumisha miujiza hiyo milele.” Ndiyo, tufikiriapo jinsi tulivyoumbwa kimwujiza, swali hili labaki, Kwa nini inakuwa lazima tufe?

      4 Maelfu ya miaka iliyopita, Daudi, mwandishi wa Biblia, alifikiria kwa makini miujiza hiyo, ingawa hangeweza kuona kihalisi ndani ya tumbo la uzazi kama wanasayansi wawezavyo kuona leo. Daudi alitafakari juu ya jinsi alivyoumbwa alipoandika kwamba alikuwa ‘amefichwa tumboni mwa mama yake.’ Alisema ‘figo zake zilifanyizwa’ wakati huo. Pia, yeye alisema kuhusu kuumbwa kwa “mifupa” yake wakati, kama alivyosema, “Nilipoumbwa kwa siri.” Kisha Daudi akasema juu ya “kiinitete changu” na kutaarifu kuhusu kiinitete hicho katika tumbo la uzazi la mama yake hivi: “Chuoni mwako ziliandikwa zote.”—Zaburi 139:13-16, NW.

      5. Ni miujiza gani huhusika katika kufanyizwa kwetu ndani ya tumbo la uzazi?

      5 Kwa wazi, hakukuwa ramani halisi iliyoandikwa kwa mkono kwa ajili ya kufanyizwa kwa Daudi ndani ya tumbo la uzazi la mama yake. Lakini katika kutafakari kwa Daudi juu ya kufanyizwa kwa “figo” zake, “mifupa” yake, na sehemu nyingine za mwili wake, kwake ilionekana kana kwamba ukuzi wa vitu hivi uliendelea kwa mpango—kwamba kila kitu kilikuwa, kusema kitamathali, ‘kimeandikwa chuoni.’ Ilikuwa kana kwamba chembe iliyotungishwa mimba ndani ya mama yake ilikuwa na chumba kikubwa kilichojaa vitabu vikiwa na maagizo mengi mno kuhusu namna ya kufanyiza mtoto wa kibinadamu na maagizo hayo tata yakapitishwa hadi kwa kila chembe iliyokuwa ikifanyizwa. Hivyo, gazeti Science World latumia mfano wa ‘kila chembe katika kiinitete kinachokua kuwa ina kabati iliyojaa ramani.’

      6. Kuna uthibitisho gani kwamba sisi, kama alivyoandika Daudi, ‘tumeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha’?

      6 Je, umewahi kufikiria jinsi mwili wetu unavyofanya kazi kimwujiza? Mwanabiolojia Jared Diamond alitaarifu hivi: “Sisi hubadilisha chembe zilizo ukutani mwa matumbo yetu mara moja baada ya siku chache, zile zilizo ukutani mwa kibofu cha mkojo mara moja baada ya miezi miwili, na chembe zetu nyekundu za damu mara moja kwa miezi minne.” Alimalizia kusema hivi: “Nguvu za asili zatutawanya vipande-vipande na kutuunganisha tena kila siku.” Hilo lamaanisha nini hasa? Lamaanisha kwamba haidhuru huenda tukaishi miaka mingapi—iwe 8, 80, au hata 800—mwili wetu wabaki ukiwa mchanga sana. Wakati mmoja, mwanasayansi fulani alikadiria hivi: “Kwa mwaka mmoja atomi ambazo sisi hupata kupitia hewa, chakula, na maji tunayotumia, zitachukua mahali pa zile atomi zipatazo asilimia 98 tulizo nazo sasa.” Kwa kweli, kama Daudi alivyosifu, tumeumbwa kwa “jinsi ya ajabu ya kutisha.”—Zaburi 139:14.

      7. Kwa kutegemea jinsi ambavyo miili yetu imebuniwa, watu fulani wamefikia mkataa gani?

      7 Ikitegemea muundo wa maumbile ya miili yetu, mamlaka yenye kuheshimika juu ya hali ya kuzeeka ilisema hivi: “Haiko wazi kwa nini kuzeeka kwapaswa kutokea.” Kwa kweli yaonekana kwamba twapaswa kuishi milele. Na hiyo ndiyo sababu watu wanajaribu kufikia lengo hilo kupitia tekinolojia zao. Muda mfupi uliopita, Dakt. Alvin Silverstein aliandika akiwa na uhakika katika kitabu chake Conquest of Death: “Tutavumbua mambo yanayotatanisha juu ya uhai. Tutafahamu . . . jinsi mtu anavyozeeka.” Kukiwa na matokeo gani? Alitabiri hivi: “Hakutakuwa tena na watu ‘wazee’ kwa kuwa ujuzi utakaoruhusu kushindwa kwa kifo utaleta pia ujana usio na mwisho.” Kwa kufikiria uchunguzi wa kisasa wa kisayansi kuhusu maumbile ya mwanadamu, je, wazo la uhai udumuo milele lasikika kuwa lisiloaminika? Kuna sababu nyingine yenye nguvu hata zaidi ya kuamini kwamba uhai udumuo milele wawezekana.

      Tamaa ya Kuishi Milele

      8, 9. Ni tamaa gani ya asili ambayo watu wamewaza juu yake katika historia yote?

      8 Je, umewahi kutambua kwamba kuishi milele ni tamaa ya asili ya mwanadamu? Daktari mmoja aliandika hivi katika jarida la Ujerumani: “Ile tamaa kubwa ya uhai udumuo milele labda ni ya zamani kama mwanadamu mwenyewe.” Kikieleza itikadi fulani za Wanaulaya wa kale, kichapo The New Encyclopædia Britannica hutaarifu hivi: “Watu wanaostahili wataishi milele katika jumba lenye kung’aa lililoezekwa kwa dhahabu.” Na, lo! jinsi ambavyo watu wamejitahidi sana kutosheleza tamaa hiyo ya msingi ya uhai udumuo milele!

      9 Kichapo The Encyclopedia Americana chasema kwamba zaidi ya miaka 2,000 iliyopita huko China, “wamaliki na watu wengine wa [kawaida] pia, chini ya uongozi wa makuhani wa Kitao, walipuuza kazi ngumu ili kutafuta madawa ya kurefusha maisha”—yanayoitwa eti chemchemi ya ujana. Kwa kweli, katika historia yote, watu wameamini kwamba kwa kutumia michanganyo mbalimbali au hata kunywa maji fulani, wangeweza kubaki wakiwa vijana.

      10. Ni jaribio gani la kisasa ambalo limefanywa ili kufikia uhai uliorefushwa?

      10 Jitihada za kisasa za kujaribu kutosheleza tamaa ya asili ya kuishi milele ni zenye kutokeza vilevile. Mfano unaojulikana na wengi ni zoea la kugandisha mtu aliyekufa kutokana na ugonjwa. Hilo limefanywa kwa matumaini ya kumrudishia mtu huyo uhai wakati fulani ujao, wakati tiba ya ugonjwa huo itakapokuwa imepatikana. Mtetezi wa zoea hili linaloitwa cryonics, aliandika hivi: “Ikiwa matumaini yetu chanya yatathibitika, na kujifunza jinsi ya kutibu na kurekebisha madhara yote—kutia ndani udhaifu wa umri wa uzee—ndipo wale ‘wafao’ leo watakapopata maisha yaliyoendelezwa kwa kipindi kisichojulikana kwa wakati ujao.”

      11. Kwa nini watu hutamani kuishi milele?

      11 Huenda ukauliza, kwa nini hii tamaa ya uhai udumuo milele imekazwa sana ndani ya akili zetu? Je, ni kwa sababu “[Mungu] ameweka milele akilini mwa mwanadamu”? (Mhubiri 3:11, Revised Standard Version) Hilo ni jambo linalohitaji kufikiriwa kwa uzito! Hebu fikiria: Kwa nini tutamani kuishi milele ikiwa lisingalikuwa kusudi la Muumba wetu kwamba tamaa hiyo itoshelezwe? Na, je, lingekuwa jambo la upendo kwa Mungu kutuumba tukiwa na tamaa ya uhai udumuo milele kisha atukatishe tamaa kwa kutuzuia tusitimize kamwe tamaa hiyo?—Zaburi 145:16.

      Tumtumaini Nani?

      12. Watu fulani wana uhakika upi, lakini, je, wewe unaamini kwamba uhakika huo una msingi mzuri?

      12 Lakini tumaini letu la kupata uhai udumuo milele lapasa kuwekwa wapi, au katika kitu gani? Katika tekinolojia ya kibinadamu ya karne ya 20 au ya 21? Makala ya gazeti The New York Times Magazine yenye kichwa “Wao Wataka Kuishi” ilizungumzia juu ya “mungu: tekinolojia” na ile “shauku juu ya uwezo wa tekinolojia.” Hata ilisemekana kwamba mtaalamu mmoja ana “uhakika kwa furaha . . . kwamba mbinu za utokezaji jeni zitapatikana mapema vya kutosha ku[tu]okoa kwa kukomesha kuzeeka, hata pengine kutokeza ujana.” Hata hivyo, kwa kweli jitihada za wanadamu za kukomesha uzee au kushinda kifo zimeshindwa kabisa.

      13. Muundo wa ubongo wetu huonyeshaje kwamba tulikusudiwa tuishi milele?

      13 Je, hilo lamaanisha kwamba hakuna njia ya kupata uhai udumuo milele? Sivyo kabisa! Njia ipo! Muundo wa ubongo wetu, ukiwa na uwezo usio na kikomo wa kujifunza mambo, wapaswa utusadikishe juu ya hilo. Mwanabiolojia wa molekuli James Watson aliuita ubongo wetu “kitu tata zaidi ambacho tumepata kugundua katika ulimwengu wetu.” Naye mtaalamu wa elimu ya mfumo wa neva Richard Restak alisema hivi: “Hakuna chochote katika ulimwengu ujulikanao kinachofanana nao hata kidogo.” Sababu gani tuwe na ubongo wenye uwezo wa kuhifadhi na kukusanya habari isiyoelekea kuwa na kikomo na mwili uliobuniwa kuishi milele ikiwa hatukukusudiwa kuishi milele?

      14. (a) Waandikaji wa Biblia wanaelekeza kwenye mkataa gani unaohusu uhai wa mwanadamu? (b) Kwa nini yatupasa tuweke tumaini letu katika Mungu wala si katika mwanadamu?

      14 Basi, twaweza kufikia mkataa gani wa pekee, wenye kupatana na akili, na wenye kutegemea mambo ya hakika? Je, si kwamba tulibuniwa na kuumbwa na Mfanyi mwenye nguvu zote na mwenye akili ili tupate kuishi milele? (Ayubu 10:8; Zaburi 36:9; 100:3; Malaki 2:10; Matendo 17:24, 25) Kwa hiyo, je, hatupaswi kutii kwa hekima agizo lililopuliziwa la mtunga-zaburi wa Biblia: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake”? Kwa nini tusimtumainie mwanadamu? Kwa sababu, kama mtunga-zaburi alivyoandika, “pumzi yake hutoka, huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.” Kwa kweli, licha ya uwezekano wa kuishi milele, wanadamu hawana uwezo kabisa wanapokabili kifo. Mtunga-zaburi afikia mkataa huu: “Heri ambaye . . . tumaini lake ni kwa BWANA, Mungu wake.”—Zaburi 146:3-5.

      Je, Kweli Ni Kusudi la Mungu?

      15. Ni nini kionyeshacho kwamba ni kusudi la Mungu tuishi milele?

      15 Lakini, huenda ukauliza, Je, kweli ni kusudi la Yehova kwamba tufurahie uhai udumuo milele? Ndiyo, bila shaka! Neno lake laahidi uhai udumuo milele mara nyingi. “Zawadi ambayo Mungu hutoa ni uhai udumuo milele,” Biblia yatuhakikishia. Yohana mtumishi wa Mungu aliandika hivi: “Hili ndilo jambo lililoahidiwa ambalo [Mungu] mwenyewe alituahidi, uhai udumuo milele.” Haishangazi kwamba mwanamume kijana alimwuliza Yesu hivi: “Mwalimu, ni lazima nifanye wema gani kusudi nipate uhai udumuo milele?” (Waroma 6:23; 1 Yohana 2:25; Mathayo 19:16) Kwa hakika, mtume Paulo aliandika juu ya “tumaini la uhai udumuo milele ambao Mungu, asiyeweza kusema uwongo, aliahidi kabla ya nyakati zinazodumu muda mrefu.”—Tito 1:2.

      16. Huenda Mungu aliuahidi uhai udumuo milele “kabla ya nyakati zinazodumu muda mrefu” katika maana gani?

      16 Yamaanisha nini kwamba Mungu aliuahidi uhai udumuo milele “kabla ya nyakati zinazodumu muda mrefu”? Wengine hufikiria kwamba mtume Paulo alimaanisha kwamba kabla ya kuumbwa kwa wenzi wa kwanza, Adamu na Hawa, Mungu alikusudia kwamba wanadamu wapaswa kuishi milele. Hata hivyo, ikiwa Paulo alikuwa akirejezea wakati fulani baada ya wanadamu kuumbwa na wakati Yehova alipotaarifu kusudi lake, bado ni wazi kwamba mapenzi ya Mungu yatia ndani uhai udumuo milele kwa wanadamu.

      17. Kwa nini Adamu na Hawa waliondolewa katika bustani ya Edeni, na kwa nini makerubi waliwekwa langoni?

      17 Biblia yasema kwamba katika bustani ya Edeni, “BWANA Mungu akachipusha katika ardhi . . . mti wa uzima.” Sababu iliyotolewa ya kumwondoa Adamu nje ya bustani ni ili “asije akanyosha mkono wake akatwaa matunda ya mti wa uzima, akala, akaishi”—naam, milele! Baada ya kuwafukuza Adamu na Hawa kutoka bustani ya Edeni, Yehova akaweka “Makerubi . . . na upanga wa moto uliogeuka huko na huko, kuilinda njia ya mti wa uzima.”—Mwanzo 2:9; 3:22-24.

      18. (a) Kula kutoka kwa mti wa uzima kungemaanisha nini kwa Adamu na Hawa? (b) Kula kutoka kwa mti huo kuliwakilisha nini?

      18 Iwapo Adamu na Hawa wangeruhusiwa kula kutokana na mti wa uhai, hilo lingemaanisha nini kwao? Naam, pendeleo la kuishi milele katika Paradiso! Msomi mmoja wa Biblia alikisia hivi: “Mti wa uzima ni lazima uwe ulikuwa na uwezo fulani ambao kupitia huo, mwanadamu hangedhoofishwa na umri, wala kuoza kunakomalizikia katika kifo.” Hata alidai kwamba “kulikuwa na mitishamba katika paradiso, yenye uwezo wa kukabiliana na athari” za kuzeeka. Hata hivyo, Biblia haisemi kwamba mti wa uzima wenyewe ulikuwa na ubora wenye kutoa uhai. Badala yake, mti huo uliwakilisha uhakikisho kamili wa Mungu wa uhai udumuo milele kwa yeyote yule ambaye angeruhusiwa kula matunda yake.—Ufunuo 2:7.

      Kusudi la Mungu Halikubadilika

      19. Kwa nini Adamu alikufa, na kwa nini sisi, uzao wake, tunakufa pia?

      19 Adamu alipokosea, alipoteza haki ya uhai udumuo milele kwa ajili yake na wazao wake wote ambao hawakuwa wamezaliwa. (Mwanzo 2:17) Alipopata kuwa mtenda-dhambi kwa sababu ya kutotii kwake, akawa mwenye kasoro, asiye mkamilifu. Tokea wakati huo na kuendelea, kwa kweli mwili wa Adamu ukapangiwa kufa. Kama isemavyo Biblia, “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” (Waroma 6:23) Isitoshe, uzao usio mkamilifu wa Adamu nao pia ukapangiwa kufa, wala si kuishi milele. Biblia yaeleza hivi: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikasambaa kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”—Waroma 5:12.

      20. Ni nini kionyeshacho kwamba wanadamu walikusudiwa waishi milele duniani?

      20 Lakini vipi kama Adamu hangefanya dhambi? Vipi kama asingalikosa kumtii Mungu na awe ameruhusiwa kula kutokana na mti wa uzima? Angefurahia zawadi ya Mungu ya uhai udumuo milele akiwa wapi? Mbinguni? La! Mungu hakusema lolote kuhusu kupelekwa kwa Adamu mbinguni. Yeye alipewa kazi ya kufanya duniani. Biblia yaeleza kwamba “BWANA Mungu akachipusha katika ardhi kila mti unaotamanika kwa macho na kufaa kwa kuliwa,” nayo yasema: “BWANA Mungu akamtwaa huyo mtu, akamweka katika bustani ya Edeni, ailime na kuitunza.” (Mwanzo 2:9, 15) Baada ya Hawa kuumbwa awe mwenzi wa Adamu, wote wawili walipewa mgawo wa ziada wa kazi hapa duniani. Mungu aliwaambia hivi: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.”—Mwanzo 1:28.

      21. Ni matazamio gani ya ajabu yaliyofurahiwa na wanadamu wa kwanza?

      21 Wazia mataraja ya ajabu ya kidunia ambayo maagizo hayo kutoka kwa Mungu yalifungulia Adamu na Hawa! Walipaswa kulea wana na binti wenye afya kamili katika Paradiso ya kidunia. Kadiri watoto wao wapendwa walivyokua, wangeshiriki pamoja nao katika kuzaa na kufanya kazi ya kufurahisha kwenye bustani, ili kuidumisha Paradiso. Na wanyama wote wakijitiisha chini yao, maisha yao yangekuwa yenye kuridhisha sana. Fikiria ile shangwe ya kupanua mipaka ya bustani ya Edeni hivi kwamba dunia yote hatimaye ingekuwa paradiso! Je, ungefurahia maisha pamoja na watoto katika makao mazuri kama hayo bila kuhangaikia uzee na kifo? Acha moyo wako ujibu swali hilo.

      22. Kwa nini twaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu hakubadili kusudi lake kwa dunia?

      22 Kwa hiyo, basi, Adamu na Hawa walipokosa kutii na kufukuzwa kutoka katika bustani ya Edeni, je, Mungu alibadili kusudi lake la wanadamu kuishi milele katika Paradiso duniani? La hasha! Ikiwa Mungu angefanya hivyo ingemaanisha kukubali kushindwa kwa uwezo wake wa kutimiza kusudi lake la awali. Twaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu hufanya yale anayoahidi, kama atangazavyo mwenyewe hivi: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”—Isaya 55:11.

      23. (a) Ni nini huthibitisha kwa mara nyingine kwamba ni kusudi la Mungu kwa wenye mwelekeo wa uadilifu kuishi milele duniani? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

      23 Biblia yaonyesha waziwazi kwamba kusudi la Mungu kwa dunia halijabadilika, ambapo Mungu aahidi hivi: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” Hata Yesu Kristo alisema katika Mahubiri ya Mlimani kwamba wenye tabia-pole watairithi dunia. (Zaburi 37:29; Mathayo 5:5) Hata hivyo, twaweza kupataje uhai udumuo milele, nasi twapaswa kufanya nini ili tuufurahie uhai huo? Hilo litazungumziwa katika makala inayofuata.

  • Njia Pekee Iendayo Kwenye Uhai Udumuo Milele
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Aprili 15
    • Njia Pekee Iendayo Kwenye Uhai Udumuo Milele

      “Mimi ndiyo njia na kweli na uhai.”—YOHANA 14:6.

      1, 2. Yesu aliilinganisha njia iendayo kwenye uhai udumuo milele na nini, na ni nini maana ya kielezi chake?

      KATIKA Mahubiri ya Mlimani yanayojulikana sana, Yesu ailinganisha njia iendayo kwenye uhai udumuo milele na barabara ambayo mtu huingia kupitia lango kuu. Tambua kuwa Yesu anakazia kwamba njia inayokwenda kwenye uhai si rahisi, akisema hivi: “Ingieni kupitia lango jembamba; kwa sababu ni pana na yenye nafasi barabara inayoongoza kuingia katika uharibifu, na wengi ndio wanaoingia kupitia hiyo; lakini lango ni jembamba na barabara ni yenye kufinyana inayoongoza kuingia katika uhai [udumuo milele], na wachache ndio wanaoipata.”—Mathayo 7:13, 14.

      2 Je, waelewa maana ya kielezi hiki? Je, hakionyeshi kuna barabara moja au njia moja tu iongozayo kwenye uhai na kwamba itahitaji uangalifu mkubwa kwa upande wetu ili kuepuka kupotea kutoka njia hiyo iendayo kwenye uhai? Basi, njia pekee inayoenda kwenye uhai udumuo milele ni ipi?

      Fungu la Yesu Kristo

      3, 4. (a) Biblia huonyeshaje fungu muhimu la Yesu katika wokovu wetu? (b) Ni lini Mungu alipofunua kwa mara ya kwanza kwamba mwanadamu angeweza kupata uhai udumuo milele?

      3 Kwa wazi, Yesu ana fungu muhimu la kutimiza kwa habari ya njia hiyo, kama vile Petro, mtume wake, alivyotangaza: “Hakuna wokovu katika mwingine yeyote, kwa maana hakuna jina jingine [isipokuwa lile la Yesu] chini ya mbingu ambalo limepewa miongoni mwa watu ambalo kwalo lazima sisi tupate kuokolewa.” (Matendo 4:12) Vivyo hivyo, mtume Paulo alitangaza hivi: “Zawadi ambayo Mungu hutoa ni uhai udumuo milele kwa njia ya Kristo Yesu Bwana wetu.” (Waroma 6:23) Yesu mwenyewe alifunua kwamba njia pekee iendayo kwenye uhai udumuo milele ni kupitia yeye, kwa kuwa alitangaza hivi: “Mimi ndiyo njia na kweli na uhai.”—Yohana 14:6.

      4 Hivyo, ni jambo la maana kwamba tukubali fungu analotimiza Yesu katika kufanya uhai udumuo milele uwezekane. Basi, acheni tuchunguze fungu lake kwa ukaribu zaidi. Je, wajua ni lini Yehova Mungu alipojulisha kwamba mwanadamu angefurahia uhai udumuo milele baada ya Adamu kufanya dhambi? Ilikuwa mara tu baada ya Adamu kufanya dhambi. Acheni sasa tuchunguze jinsi ambavyo uandalizi wa Yesu Kristo akiwa Mwokozi wa wanadamu ulivyotabiriwa kwa mara ya kwanza.

      Mbegu Iliyoahidiwa

      5. Twaweza kumtambuaje nyoka aliyemtongoza Hawa?

      5 Yehova Mungu alimtambulisha Mwokozi aliyeahidiwa kwa kutumia lugha ya kitamathali. Alifanya hivyo alipotangaza hukumu juu ya “nyoka” ambaye alikuwa ameongea na Hawa na kumshawishi asimtii Mungu kwa kula tunda lililokatazwa. (Mwanzo 3:1-5) Bila shaka, huyo hakuwa nyoka halisi. Alikuwa kiumbe wa roho mwenye nguvu ambaye hutambulishwa katika Biblia kuwa “nyoka wa awali, yeye aitwaye Ibilisi na Shetani.” (Ufunuo 12:9) Shetani alimtumia mnyama huyu wa hali ya chini kuwa msemaji wake katika kumtongoza Hawa. Hivyo, akimhukumu Shetani, Mungu alimwambia hivi: “Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo [yaani, mbegu ya mwanamke] utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.”—Mwanzo 3:15.

      6, 7. (a) Mwanamke anayezaa “mbegu” ni nani? (b) Mbegu aliyeahidiwa ni nani, naye anatimiza nini?

      6 “Mwanamke” huyu ni nani ambaye Shetani ana uadui au chuki naye? Sawa tu na vile yule “nyoka wa awali” atambulishwavyo katika Ufunuo sura ya 12, ndivyo na mwanamke huyu ambaye Shetani amchukia. Ona katika mstari wa 1 kwamba yeye asemwa kuwa “a[m]epambwa jua, na mwezi ulikuwa chini ya miguu yake, na juu ya kichwa chake kulikuwa na taji la nyota kumi na mbili.” Mwanamke huyu huwakilisha tengenezo la Mungu la kimbingu la malaika waaminifu, naye ‘mwana wa kiume’ ambaye yeye huzaa huwakilisha Ufalme wa Mungu, Yesu Kristo akitawala akiwa Mfalme.—Ufunuo 12:1-5.

      7 Ni nani basi, “mbegu” hii, au uzao, wa mwanamke, anayerejezewa kwenye Mwanzo 3:15, atakayemponda Shetani “kichwa,” hivyo akimpiga pigo la kifo? Ni yule ambaye Mungu alimtuma kutoka mbinguni azaliwe kimwujiza na bikira, naam, mwanadamu Yesu. (Mathayo 1:18-23; Yohana 6:38) Sura ya 12 ya Ufunuo hufunua kwamba akiwa mtawala aliyefufuliwa wa kimbingu, Mbegu hii, Yesu Kristo, angeongoza katika kumshinda Shetani na kusimamisha, kama Ufunuo 12:10 usemavyo, “ufalme wa Mungu wetu na mamlaka ya Kristo wake.”

      8. (a) Ni jambo gani jipya ambalo Mungu aliandaa kuhusiana na kusudi lake la awali? (b) Ni nani hufanyiza serikali mpya ya Mungu?

      8 Ufalme huo ukiwa mikononi mwa Yesu Kristo ni jambo moja jipya aliloandaa Mungu kuhusiana na kusudi la awali la wanadamu kufurahia uhai udumuo milele duniani. Baada ya uasi wa Shetani, Yehova alitenda mara moja ili kuondoa matokeo yote mabaya ya uovu kupitia kwa serikali hiyo mpya ya Ufalme. Yesu alipokuwa duniani, alifunua kwamba asingelikuwa peke yake katika serikali hiyo. (Luka 22:28-30) Wengine wangechaguliwa kutoka kwa wanadamu, nao wangejiunga naye mbinguni ili kushiriki katika kutawala, na hivyo wangefanyiza sehemu ya pili ya mbegu ya mwanamke. (Wagalatia 3:16, 29) Katika Biblia, idadi ya hao watawala wenzi pamoja na Yesu—wote wakiwa wametwaliwa kutoka kwa wanadamu wenye dhambi duniani—ni 144,000.—Ufunuo 14:1-3.

      9. (a) Kwa nini Yesu alihitaji kuja duniani akiwa mwanadamu? (b) Yesu alizitanguaje kazi za Ibilisi?

      9 Hata hivyo, kabla ya Ufalme kuanza kutawala ilikuwa muhimu kwamba sehemu ya msingi ya mbegu, Yesu Kristo, itokee duniani. Kwa nini? Kwa sababu alikuwa amechaguliwa na Yehova Mungu akiwa Yule ‘atakayevunja-vunja [au, kutangua] kazi za Ibilisi.’ (1 Yohana 3:8) Baadhi ya kazi za Shetani ni kule kumchochea Adamu afanye dhambi, kulikowaletea wazao wote wa Adamu laana ya dhambi na kifo. (Waroma 5:12) Yesu aliitangua kazi hii ya Ibilisi kwa kutoa uhai Wake ukiwa fidia. Hivyo aliandaa msingi wa kuachiliwa kwa aina ya binadamu kutokana na dhambi na kifo na kufungua njia ya uhai udumuo milele.—Mathayo 20:28; Waroma 3:24; Waefeso 1:7.

      Kile Ambacho Fidia Hutimiza

      10. Yesu na Adamu walifanana katika njia zipi?

      10 Kwa kuwa uhai wa Yesu ulihamishwa kutoka mbinguni hadi kwenye tumbo la uzazi la mwanamke, alizaliwa akiwa mwanadamu mkamilifu, asiyetiwa doa na dhambi iliyotokana na Adamu. Angaliweza kuishi milele duniani. Hali moja na hiyo, Adamu aliumbwa akiwa mwanadamu mkamilifu akiwa na mataraja ya kuishi milele duniani. Mtume Paulo alikuwa na ulinganifu baina ya hao wanaume wawili akilini alipoandika hivi: “‘Mtu wa kwanza Adamu akawa nafsi hai.’ Adamu wa mwisho [Yesu Kristo] akawa roho ipayo uhai. Mtu wa kwanza ni wa kutoka duniani na amefanywa kwa mavumbi; mtu wa pili ni wa kutoka mbinguni.”—1 Wakorintho 15:45, 47.

      11. (a) Adamu na Yesu waliathirije jamii ya kibinadamu? (b) Twapaswa tuoneje dhabihu ya Yesu?

      11 Ulinganifu baina ya watu hao wawili—watu wawili pekee wakamilifu waliopata kuwapo duniani—umekaziwa na tangazo la Biblia kwamba Yesu “[alijitoa] mwenyewe kuwa fidia inayolingana kwa ajili ya wote.” (1 Timotheo 2:6) Yesu alilingana na nani? Naam, na Adamu alipokuwa angali mtu mkamilifu! Dhambi ya Adamu wa kwanza ilitokeza kuhukumiwa kifo kwa jamii yote ya kibinadamu. Dhabihu ya “Adamu wa mwisho” huandaa msingi wa kuokolewa kutoka kwenye dhambi na kifo, ili tuweze kuishi milele. Jinsi dhabihu ya Yesu ilivyo yenye thamani kubwa! Mtume Petro alisema hivi: “Haikuwa kwa vitu vyenye kuharibika, kwa fedha au dhahabu, kwamba mlikombolewa.” Bali, Petro alieleza: “Ilikuwa kwa damu yenye bei, kama ile ya mwana-kondoo asiye na waa na asiye na doa, naam, ya Kristo.”—1 Petro 1:18, 19.

      12. Biblia hufafanuaje kutanguliwa kwa hukumu ya kifo juu yetu?

      12 Biblia hueleza kwa kupendeza namna hukumu ya kifo juu ya jamii ya kibinadamu itakavyotanguliwa, ikisema hivi: “Kupitia kosa moja [la Adamu] tokeo kwa watu wa namna zote lilikuwa ni hatia, hivyohivyo pia kupitia tendo moja la kutetewa kuwa haki [kifo cha Yesu] tokeo kwa watu wa namna zote ni kutangazwa kwao kuwa waadilifu kwa ajili ya uhai. Kwa maana kama vile kupitia kutotii kwa mtu mmoja [Adamu] wengi walifanywa watenda-dhambi, vivyo hivyo pia kupitia utii wa mtu mmoja [Yesu] wengi watafanywa waadilifu.”—Waroma 5:18, 19.

      Tazamio Tukufu

      13. Kwa nini watu wengi huhisi jinsi wahisivyo kuhusu kuishi milele?

      13 Uandalizi huu wa Mungu wapaswa utufurahishe sana! Je, husisimuki kwa sababu Mwokozi amekwisha andaliwa? Walipoulizwa, “Je, taraja hili la kuishi milele lakupendeza?” katika uchunguzi uliofanywa wakati mmoja na gazeti la mji mmoja mkuu wa Marekani, idadi ya kushangaza ya asilimia 67.4 ya waliohojiwa walijibu, “La.” Kwa sababu gani walisema hawakutaka kuishi milele? Kwa wazi ni kwa sababu maisha duniani sasa huhusianishwa na matatizo mengi sana. Mtu mmoja alisema hivi: “Sifurahii wazo la kuonekana mwenye umri wa miaka 200.”

      14. Kwa nini kuishi milele kutakuwa ni raha kamili?

      14 Hata hivyo, Biblia haizungumzi juu ya kuishi milele katika ulimwengu ambamo watu hupatwa na magonjwa, uzee, na majanga mengine. La, kwani, akiwa Mtawala wa Ufalme wa Mungu, Yesu atatangua matatizo yote yanayosababishwa na Shetani. Kulingana na Biblia, Ufalme wa Mungu ‘utavunja vipande vipande na kuziharibu’ serikali zote zenye kuonea za ulimwengu huu. (Danieli 2:44) Wakati huo, sala ambayo Yesu aliwafundisha wafuasi wake itajibiwa, “mapenzi” ya Mungu “[yatatimizwa], hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10, UV) Katika ulimwengu mpya wa Mungu, baada ya ubaya wote kuondolewa duniani, manufaa za fidia ya Yesu zitatumika kwa ukamili. Naam, wote watakaostahili watarudishwa kwenye afya kamili!

      15, 16. Ni hali gani zitakazokuwa katika ulimwengu mpya wa Mungu?

      15 Kwa watu wanaoishi katika ulimwengu mpya wa Mungu, fungu hili la Biblia litatumika: “Nyama ya mwili wake itakuwa laini kuliko ya mtoto; huzirudia siku za ujana wake.” (Ayubu 33:25) Ahadi nyingine ya Biblia pia itapata utimizo: “Macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”—Isaya 35:5, 6.

      16 Hebu wazia: Haidhuru umri wetu wakati huo, iwe tuna miaka 80, 800, au hata umri mkubwa zaidi, miili yetu itabaki ikiwa na afya nzuri sana. Itakuwa kama Biblia inavyoahidi: “Hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.” Wakati huo ahadi hii pia itatimizwa: “[Mungu] atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Isaya 33:24; Ufunuo 21:3, 4.

      17. Twaweza kutazamia matimizo gani kutoka kwa watu katika ulimwengu mpya wa Mungu?

      17 Katika ulimwengu huo mpya, tutaweza kutumia ubongo wetu wa kustaajabisha katika njia ambayo Muumba wetu alikusudia, alipoubuni ukiwa na uwezo wa kujifunza mambo bila kikomo. Hebu wazia mambo ya ajabu tuwezayo kutimiza! Hata wanadamu wasio wakamilifu wametokeza kutoka maghala ya elementi za dunia kila kitu tukionacho kutuzunguka—simu, maikrofoni, saa, pagers, kompyuta, ndege, naam, na vingine vingi. Hakuna kimoja chavyo kilichofanyizwa kwa vifaa vilivyoletwa kutoka mbali ulimwenguni. Tukiwa na uhai usiokwisha mbele yetu katika Paradiso inayokuja, uwezo wa mafanikio katika kubuni utakuwa bila kikomo!—Isaya 65:21-25.

      18. Kwa nini maisha hayatakuwa yenye kuchosha kamwe katika ulimwengu mpya wa Mungu?

      18 Na uhai hautakuwa wenye kuchosha. Hata sasa, sisi hutazamia kwa hamu mlo unaofuata, hata ingawa huenda tumekula makumi ya maelfu ya milo. Katika ukamilifu wa kibinadamu, tutafurahia hata zaidi mazao yaliyo matamu sana ya dunia Paradiso. (Isaya 25:6) Nasi tutakuwa na shangwe ya milele ya kutunza wanyama wengi walio hai duniani, na kufurahia machweo ya jua yenye kutazamisha, milima, mito, na mabonde. Kwa kweli, maisha hayatakuwa yenye kuchosha kamwe katika ulimwengu mpya wa Mungu!—Zaburi 145:16.

      Kutimiza Matakwa ya Mungu

      19. Kwa nini ni jambo lenye kupatana na akili kuamini kwamba kuna matakwa ya kupokea zawadi ya Mungu ya uhai?

      19 Je, ungetazamia kupokea zawadi kubwa ya uhai udumuo milele kutoka kwa Mungu katika Paradiso bila kufanya lolote kuipata? Je, si jambo lenye kupatana na akili kwamba Mungu angetaka tufanye kitu fulani? Kwa hakika ndiyo. Kwa kweli, Mungu hatutupii tu zawadi hiyo. Yeye hututolea, lakini ni sharti tujitahidi kuifikia na kuitwaa. Jitihada zahusika. Huenda ukauliza swali lile lile ambalo yule mtawala kijana tajiri alimwuliza Yesu: “Nifanye nini ili kurithi uhai udumuo milele?” Au huenda ukauliza swali hilo kama vile yule mlinzi wa jela Mfilipi alivyomwuliza mtume Paulo: “Ni nini ambalo lazima nifanye ili nipate kuokolewa?”—Mathayo 19:16; Matendo 16:30.

      20. Ni takwa jipi la lazima ili kupata uhai udumuo milele?

      20 Usiku uliotangulia kifo chake, Yesu alionyesha takwa moja la msingi aliposema kupitia sala kwa Baba yake wa kimbingu hivi: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’ (Yohana 17:3) Je, si takwa lenye kupatana na akili kwamba tutwae ujuzi juu ya Yehova, aliyefanya uhai udumuo milele uwezekane, na ujuzi juu ya yule aliyetufia, Yesu Kristo? Na bado, mengi yahitajiwa kuliko tu kutwaa ujuzi huo.

      21. Twaonyeshaje kwamba tunatimiza takwa la kudhihirisha imani?

      21 Biblia pia yasema hivi: “Yeye ambaye hudhihirisha imani katika Mwana ana uhai udumuo milele.” Kisha yaongezea hivi: “Yeye ambaye hukosa kutii Mwana hataona uhai, bali hasira ya kisasi ya Mungu hukaa juu yake.” (Yohana 3:36) Unaweza kuonyesha kwamba unadhihirisha imani katika Mwana kwa kufanya mabadiliko maishani mwako na kuyapatanisha na mapenzi ya Mungu. Lazima uukatae mwendo wowote mbaya ambao huenda umekuwa ukiufuatia na kuchukua hatua kufanya yanayompendeza Mungu. Unahitaji kufanya yale ambayo mtume Petro aliamuru: “Kwa hiyo, tubuni na mgeuke kabisa ili mpate kufutiwa dhambi zenu, ili majira ya kuburudisha yapate kuja kutoka kwa utu wa Yehova.”—Matendo 3:19.

      22. Ni matendo gani yanayohusika katika kufuata hatua za Yesu?

      22 Acheni tusisahau kamwe kwamba ni kwa kudhihirisha imani katika Yesu tu ndipo twaweza kufurahia uhai udumuo milele. (Yohana 6:40; 14:6) Twaonyesha kwamba twadhihirisha imani katika Yesu kwa ‘kufuata hatua zake kwa ukaribu.’ (1 Petro 2:21) Ni nini linalotiwa ndani katika kufanya hivyo? Yesu alipokuwa akisali kwa Mungu, alipaaza sauti hivi: “Tazama! Nimekuja . . . ili kufanya mapenzi yako, Ee Mungu.” (Waebrania 10:7) Ni muhimu kumwiga Yesu kwa kukubali kufanya mapenzi ya Mungu na kuweka maisha yako wakfu kwa Yehova. Baadaye wahitaji kuonyesha wakfu huo kupitia ubatizo wa maji; Yesu pia alijitoa ili abatizwe. (Luka 3:21, 22) Kuchukua hatua hizo ni jambo lenye kupatana na akili kabisa. Mtume Paulo alitaarifu kwamba “upendo alio nao Kristo hutushurutisha.” (2 Wakorintho 5:14, 15) Kwa njia gani? Naam, upendo ulimsukuma Yesu kutoa uhai wake kwa ajili yetu. Je, huo haupaswi kutushurutisha kuitikia kwa kudhihirisha imani katika yeye? Ndiyo, wapaswa kutushurutisha tufuate kielelezo chake cha upendo katika kujitoa mwenyewe kuwasaidia wengine. Kristo aliishi kwa kufanya mapenzi ya Mungu; nasi twapaswa kufanya vivyo hivyo, tusiendelee tena kuishi kwa ajili yetu wenyewe.

      23. (a) Ni lazima wale wanaopokea uhai waongezwe juu ya nini? (b) Ni nini linalotakwa kutoka kwa wale walio katika kutaniko la Kikristo?

      23 Huo sio mwisho wa mambo. Biblia yasema kwamba watu 3,000 walipobatizwa siku ya Pentekoste 33 W.K., ‘waliongezwa.’ Waliongezwa juu ya nini? “Wakaendelea kujitoa wenyewe kwa fundisho la mitume na kushirikiana,” Luka aeleza. (Matendo 2:41, 42) Naam, walikutana pamoja wajifunze Biblia na kushirikiana na hivyo waliongezwa kwa, au wakawa sehemu ya, kutaniko la Kikristo. Wakristo wa mapema walihudhuria mikutano kwa ukawaida ili kupata agizo la kiroho. (Waebrania 10:25) Leo, Mashahidi wa Yehova hufanya hivyo, nao wangependa kukutia moyo uhudhurie mikutano hiyo pamoja nao.

      24. “Uhai ulio halisi” ni nini, nao utapatikana jinsi gani na lini?

      24 Mamilioni ya watu sasa wanatembea kwenye barabara iliyosonga iongozayo kwenye uhai. Kudumu katika barabara hii iliyosonga hutaka jitihada! (Mathayo 7:13, 14) Paulo alionyesha jambo hilo katika ombi lake lenye moyo mchangamfu: “Pigana pigano bora la imani, pata mshiko imara juu ya uhai udumuo milele ambao uliitiwa.” Kuendeleza pigano hilo kwahitajika ili “kuwa na mshiko imara juu ya uhai ulio halisi.” (1 Timotheo 6:12, 19) Uhai huo si uhai wa wakati huu wenye maumivu na kuteseka tulikoletewa kupitia dhambi ya Adamu. Bali, ni uhai katika ulimwengu mpya wa Mungu, utakaokuja karibuni wakati dhabihu ya fidia ya Kristo itakapotumiwa kwa niaba ya wote wanaompenda Yehova Mungu na Mwana wake baada ya mfumo huu wa mambo kuondolewa. Acheni sisi sote tuchague uhai—“uhai ulio halisi”—uhai udumuo milele katika ulimwengu mpya mtukufu wa Mungu.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki