Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Uzima wa Milele Duniani—Tumaini Ambalo Tumepewa na Mungu
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Agosti 15
    • Uzima wa Milele Duniani—Tumaini Ambalo Tumepewa na Mungu

      “Uumbaji ulitiishwa chini ya ubatili . . . juu ya msingi wa tumaini.”—ROM. 8:20.

      1, 2. (a) Kwa nini tumaini la uzima wa milele duniani ni la maana sana kwetu? (b) Kwa nini watu wengi wana shaka kuhusu uzima wa milele duniani?

      LABDA unakumbuka shangwe ambayo ulihisi ulipojifunza kwa mara ya kwanza kwamba hivi karibuni watu hawatazeeka na kufa tena, bali wataishi milele duniani. (Yoh. 17:3; Ufu. 21:3, 4) Huenda umefurahia kuwaambia wengine kuhusu tumaini hilo linalotegemea Maandiko. Kwa kweli, tumaini la uzima wa milele ni sehemu ya maana sana ya habari njema tunayohubiri. Tumaini hilo linatusaidia kuwa na mtazamo unaofaa maishani.

      2 Kwa kiwango kikubwa, dini zinazodai kuwa za Kikristo zimepuuza tumaini la kuishi milele duniani. Ingawa Biblia inafundisha kwamba nafsi inakufa, makanisa mengi yanafundisha fundisho lisilopatana na Maandiko la kwamba mwanadamu ana nafsi isiyoweza kufa ambayo inaendelea kuishi katika makao ya roho baada ya mtu kufa. (Eze. 18:20) Hivyo, watu wengi wana shaka kuhusu uzima wa milele duniani. Basi, tunaweza kujiuliza hivi: Je, kweli Biblia inaunga mkono tumaini hilo? Ikiwa ndivyo, Mungu aliwafunulia wanadamu tumaini hilo kwa mara ya kwanza wakati gani?

      “Ulitiishwa Chini ya Ubatili . . . Juu ya Msingi wa Tumaini”

      3. Tangu mwanzoni mwa historia ya wanadamu, kusudi la Mungu kwa ajili ya wanadamu lilionyeshwa wazi jinsi gani?

      3 Kusudi la Yehova kwa ajili ya wanadamu lilionyeshwa wazi tangu mwanzoni mwa historia ya wanadamu. Mungu alionyesha wazi kwamba Adamu angeishi milele ikiwa angetii. (Mwa. 2:9, 17; 3:22) Bila shaka, wazao wa mapema wa Adamu walijua jinsi wanadamu walivyopoteza ukamilifu, na waliona wazi matokeo ya kutokamilika. Njia ya kuingia kwenye bustani ya Edeni ilifungwa, na watu wakaanza kuzeeka na kufa. (Mwa. 3:23, 24) Kadiri muda ulivyopita, ndivyo urefu wa maisha ya wanadamu ulivyopungua. Adamu aliishi miaka 930. Shemu aliyeokoka Gharika aliishi miaka 600 tu na mwana wake Arpakshadi aliishi miaka 438. Tera, baba ya Abrahamu, aliishi miaka 205. Abrahamu aliishi miaka 175, mwana wake Isaka aliishi miaka 180, naye Yakobo aliishi miaka 147. (Mwa. 5:5; 11:10-13, 32; 25:7; 35:28; 47:28) Inaonekana watu wengi walitambua kwamba kupungua kwa miaka ya maisha ya wanadamu kulimaanisha kuwa tumaini la uzima wa milele lilipotea! Je, walikuwa na sababu ya kutumaini kwamba uzima wa milele ungerudishwa tena?

      4. Wanaume waaminifu wa zamani walikuwa na msingi gani wa kuamini kwamba Mungu angerudisha baraka ambazo Adamu alipoteza?

      4 Neno la Mungu linasema: “Uumbaji [wanadamu] ulitiishwa chini ya ubatili . . . juu ya msingi wa tumaini.” (Rom. 8:20) Tumaini gani? Unabii wa kwanza kabisa wa Biblia ulizungumza kuhusu “uzao” ambao ‘ungemponda nyoka kichwa.’ (Soma Mwanzo 3:1-5, 15.) Ahadi ya Uzao huo iliwapa wanadamu waaminifu msingi wa kutumaini kwamba Mungu hangetupilia mbali kusudi lake kwa ajili ya wanadamu. Ahadi hiyo iliwapa wanaume kama vile Abeli na Noa sababu ya kuamini kwamba Mungu angerudisha baraka ambazo Adamu alipoteza. Huenda wanaume hao walitambua kwamba damu ingemwagika wakati ambapo ‘uzao huo ungetiwa jeraha kwenye kisigino.’—Mwa. 4:4; 8:20; Ebr. 11:4.

      5. Ni nini kinachoonyesha kwamba Abrahamu aliamini ufufuo?

      5 Mfikirie Abrahamu. Abrahamu alipokuwa akijaribiwa, “ni kana kwamba alimtoa Isaka, . . . mwana wake mzaliwa-pekee.” (Ebr. 11:17) Kwa nini alikuwa tayari kufanya hivyo? (Soma Waebrania 11:19.) Aliamini ufufuo! Abrahamu alikuwa na msingi wa kuamini ufufuo. Yehova alikuwa amemrudishia Abrahamu uwezo wake wa kuzaa na alimwezesha yeye na mke wake, Sara, kuzaa mwana wakiwa wamezeeka. (Mwa. 18:10-14; 21:1-3; Rom. 4:19-21) Pia, Abrahamu alikuwa na neno la Yehova. Mungu alikuwa amemwambia hivi: “Ule utakaoitwa uzao wako utakuwa kupitia Isaka.” (Mwa. 21:12) Kwa hiyo, Abrahamu alikuwa na sababu nzuri za kutazamia kwamba Mungu angemfufua Isaka.

      6, 7. (a) Ni agano gani ambalo Yehova alifanya na Abrahamu? (b) Ahadi ambayo Yehova alimpa Abrahamu iliwaletea wanadamu tumaini jinsi gani?

      6 Kwa sababu ya imani yenye nguvu sana ya Abrahamu, Yehova alifanya agano pamoja naye kuhusu mzao au “uzao” wake. (Soma Mwanzo 22:18.) Yesu Kristo alithibitika kuwa sehemu ya msingi ya “uzao” huo. (Gal. 3:16) Yehova alikuwa amemwambia Abrahamu kwamba “uzao” wake ungeongezeka na kuwa “kama nyota za mbinguni na kama chembe za mchanga zilizo kando ya bahari”—idadi ambayo Abrahamu hakujua. (Mwa. 22:17) Hata hivyo, baadaye idadi hiyo ilifunuliwa. Yesu Kristo na wale 144,000, ambao watatawala pamoja naye katika Ufalme wake, wanafanyiza “uzao” huo. (Gal. 3:29; Ufu. 7:4; 14:1) Kupitia kwa Ufalme wa Kimasihi “mataifa yote ya dunia . . . yatajibariki.”

      7 Inawezekana kwamba Abrahamu hakuelewa kikamili umuhimu wa agano ambalo Yehova alifanya pamoja naye. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba “alikuwa akingojea jiji lililo na misingi ya kweli.” (Ebr. 11:10) Jiji hilo ni Ufalme wa Mungu. Ni lazima Abrahamu awe hai tena ili apokee baraka chini ya Ufalme huo. Abrahamu ataweza kuishi milele duniani kupitia ufufuo. Na wale watakaookoka Har–Magedoni au wale watakaofufuliwa wataishi milele.—Ufu. 7:9, 14; 20:12-14.

      “Roho Imeleta Mkazo Juu Yangu”

      8, 9. Kwa nini kitabu cha Ayubu si simulizi tu la majaribu ya mwanamume mmoja?

      8 Ayubu aliishi baada ya Yosefu, mwana wa mjukuu wa Abrahamu na kabla ya nabii Musa. Kitabu cha Biblia cha Ayubu, ambacho inaelekea kiliandikwa na Musa, kinaeleza kwa nini Yehova aliruhusu Ayubu ateseke na mafanikio aliyopata baadaye. Hata hivyo, kitabu cha Ayubu hakisimulii tu majaribu ya mwanamume mmoja; kinakazia masuala ya maana sana yanayohusu ulimwengu wote. Kitabu hicho kinatusaidia kuelewa kwa undani jinsi Yehova anavyotawala kwa uadilifu, na kinafunua kwamba utimilifu na matarajio ya kupata uzima ya watumishi wote wa Mungu duniani yanahusiana na suala lililotokezwa katika Edeni. Ingawa Ayubu hakuelewa suala hilo, hakuwaruhusu marafiki wake watatu wamfanye afikiri kwamba hakuwa mtimilifu. (Ayu. 27:5) Hilo linapaswa kuitia nguvu imani yetu na kutusaidia kutambua kwamba tunaweza kudumisha utimilifu wetu na kuunga mkono enzi kuu ya Yehova.

      9 Baada ya wafariji watatu wa uwongo wa Ayubu kumaliza kuzungumza, “Elihu mwana wa Barakeli, Mbuzi, akajibu.” Ni nini kilichomchochea kuzungumza? Alisema hivi: “Nimejaa maneno. Roho imeleta mkazo juu yangu ndani ya tumbo langu.” (Ayu. 32:5, 6, 18) Ingawa mambo ambayo Elihu alisema chini ya mwongozo wa roho ya Mungu yalitimia wakati majaribu ya Ayubu yalipokoma, bado maneno yake yana maana kwa wengine pia. Yanawapa tumaini wote wanaodumisha utimilifu.

      10. Ni nini kinachoonyesha kwamba nyakati nyingine Yehova alimpa mtu mmoja ujumbe ambao unawahusu wanadamu wote?

      10 Nyakati nyingine, Yehova alimpa mtu mmoja ujumbe ambao unawahusu wanadamu wote. Hilo linathibitishwa na unabii wa Danieli kuhusu ndoto ya Mfalme Nebukadneza wa Babiloni iliyohusu mti mkubwa uliokatwa. (Dan. 4:10-27) Ingawa ndoto hiyo ilitimia kuhusiana na Nebukadneza, ilionyesha jambo fulani ambalo ni kubwa zaidi. Ilionyesha kwamba utawala wa Mungu juu ya dunia ambao uliwakilishwa na ufalme wa ukoo wa Mfalme Daudi ungerudishwa baada ya kipindi cha miaka 2,520, kuanzia mwaka wa 607 K.W.K.a Utawala wa Mungu juu ya dunia yetu ulianza upya wakati Yesu Kristo alipowekwa rasmi kuwa Mfalme wa kimbingu katika mwaka wa 1914. Hebu wazia jinsi utawala wa Ufalme utakavyotimiza matumaini ya wanadamu watiifu hivi karibuni!

      “Mwachilie Ili Asishuke Chini Kuingia Shimoni!”

      11. Maneno ya Elihu yalionyesha nini kumhusu Mungu?

      11 Anapomjibu Ayubu, Elihu anasema kuhusu “mjumbe, . . . msemaji, mmoja kati ya elfu, ili kumwambia mwanadamu unyoofu wake.” Namna gani ikiwa mjumbe huyo ‘anamsihi Mungu ili amfurahie’? Elihu anasema: “Ndipo [Mungu] anapompa kibali na kusema, ‘Mwachilie ili asishuke chini kuingia shimoni! Nimepata fidia! Nyama yake na iwe laini kuliko wakati wa ujana; na arudi kwenye siku za nguvu za ujana wake.’” (Ayu. 33:23-26) Maneno hayo yalionyesha kwamba Mungu alikuwa tayari kukubali “fidia,” au “kifuniko,” kwa faida ya wanadamu wenye kutubu.—Ayu. 33:24.

      12. Maneno ya Elihu yanawapa wanadamu kwa ujumla tumaini gani?

      12 Huenda Elihu hakuelewa kikamili maana ya fidia au dhabihu ya ukombozi, kama vile tu manabii hawakuelewa kikamili kila jambo ambalo waliandika. (Dan. 12:8; 1 Pet. 1:10-12) Hata hivyo, maneno ya Elihu yanaonyesha tumaini la kwamba siku moja Mungu angekubali fidia na hivyo kuwaweka wanadamu huru kutokana na kifo na pia kutokana na matokeo mabaya ya kuzeeka. Maneno ya Elihu yalitoa tumaini zuri ajabu la uzima wa milele. Kitabu cha Ayubu kinaonyesha pia kwamba kutakuwa na ufufuo.—Ayu. 14:14, 15.

      13. Maneno ya Elihu yanamaanisha nini kwa Wakristo?

      13 Leo, maneno ya Elihu yanaendelea kuwa na maana kwa mamilioni ya Wakristo ambao wanatumaini kuokoka uharibifu wa mfumo huu wa mambo. Waliozeeka kati ya waokokaji hao watarudishiwa tena nguvu zao za ujana. (Ufu. 7:9, 10, 14-17) Tumaini la kuwaona wale watakaofufuliwa wakirudishiwa tena nguvu zao za ujana linaendelea kuwafurahisha watu waaminifu. Bila shaka, ili Wakristo watiwa-mafuta wapate uhai usioweza kufa mbinguni, na “kondoo wengine” wa Yesu wapate uzima wa milele duniani, ni lazima wawe na imani katika dhabihu ya ukombozi ya Kristo.—Yoh. 10:16; Rom. 6:23.

      Kifo Kitamezwa Kutoka Duniani

      14. Ni nini kinachoonyesha kwamba Waisraeli walihitaji kitu kingine zaidi ya Sheria ya Musa ili wawe na tumaini la kuishi milele?

      14 Wazao wa Abrahamu walikuja kuwa taifa huru walipofanya agano pamoja na Mungu. Yehova aliwaambia hivi alipokuwa akiwapa Sheria hiyo: “Mtazishika sheria zangu na maamuzi yangu ya hukumu, ambazo ikiwa mtu atazifanya, yeye pia ataishi kwa hizo.” (Law. 18:5) Hata hivyo, kwa kuwa hawangeweza kuishi kulingana na viwango vikamilifu vya Sheria, Waisraeli walihukumiwa na Sheria na walihitaji kuwekwa huru kutokana na hukumu hiyo.—Gal. 3:13.

      15. Daudi aliongozwa na roho ya Mungu kuandika kuhusu baraka gani za wakati ujao?

      15 Baada ya Musa, Yehova aliwaongoza kwa roho yake waandikaji wengine wa Biblia ili waandike kuhusu tumaini la uzima wa milele. (Zab. 21:4; 37:29) Kwa mfano, mtunga-zaburi Daudi alimalizia hivi zaburi moja iliyohusu umoja wa waabudu wa kweli huko Sayuni: “Huko Yehova aliamuru baraka iwepo, naam, uzima mpaka wakati usio na kipimo.”—Zab. 133:3.

      16. Kupitia Isaya, Yehova aliahidi nini kuhusu wakati ujao wa “dunia yote”?

      16 Yehova alimwongoza Isaya atabiri kuhusu uzima wa milele duniani. (Soma Isaya 25:7, 8.) Kama vile “kifuniko” au blanketi inavyomfunika mtu, dhambi na kifo vimewafunika na kuwalemea kabisa wanadamu. Yehova anawahakikishia watu wake kwamba dhambi na kifo vitamezwa, au vitaondolewa “katika dunia yote.”

      17. Masihi anatimiza daraka gani la kinabii ambalo linawapa watu nafasi ya kupata uzima wa milele?

      17 Fikiria pia utaratibu ulioonyeshwa katika Sheria ya Musa kuhusu mbuzi wa Azazeli. Mara moja kwa mwaka, katika Siku ya Upatanisho, kuhani mkuu ‘aliweka mikono yake miwili juu ya kichwa cha mbuzi aliye hai na aliungama juu yake makosa yote ya wana wa Israeli, na aliyaweka juu ya kichwa cha yule mbuzi na mbuzi huyo alichukua juu yake mwenyewe makosa yao yote mpaka katika nchi ya jangwa.’ (Law. 16:7-10, 21, 22) Isaya alitabiri kuja kwa Masihi, ambaye angetimiza daraka kama hilo na kubeba “magonjwa,” “maumivu,” na “dhambi ya watu wengi,” na hivyo kuwapa nafasi ya kupata uzima wa milele.—Soma Isaya 53:4-6, 12.

      18, 19. Ni tumaini gani linalokaziwa kwenye Isaya 26:19 na Danieli 12:13?

      18 Kupitia Isaya, Yehova aliwaambia watu wake Waisraeli hivi: “Wafu wako wataishi. Maiti wangu—wataamka. Amkeni, pigeni vigelegele kwa shangwe, enyi mnaokaa mavumbini! Kwa maana umande wako ni kama umande wa miholi, na dunia itawaacha hata wale wasiojiweza katika kifo waanguke katika kuzaliwa.” (Isa. 26:19) Maandiko ya Kiebrania yanaonyesha waziwazi kwamba kuna tumaini la watu kufufuliwa na kuishi duniani. Kwa mfano, Danieli alipokuwa na umri wa karibu miaka 100, Yehova alimhakikishia hivi: “Utapumzika, lakini utasimama kwa ajili ya fungu lako mwishoni mwa zile siku.”—Dan. 12:13.

      19 Kwa sababu ya tumaini la ufufuo, Martha alimwambia Yesu hivi kuhusu ndugu yake aliyekufa: “Ninajua atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.” (Yoh. 11:24) Je, mafundisho ya Yesu na maandishi ya wanafunzi wake yaliyoongozwa na roho ya Mungu yalibadili tumaini hilo? Je, bado uzima wa milele duniani ni tumaini ambalo Yehova amewaahidi wanadamu? Tutazungumzia majibu ya maswali hayo katika habari inayofuata.

      [Maelezo ya chini]

      a Ona sura ya 6 ya kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli!

  • Uzima wa Milele Duniani—Je, Ni Tumaini la Kikristo?
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Agosti 15
    • Uzima wa Milele Duniani—Je, Ni Tumaini la Kikristo?

      “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena.”—UFU. 21:4.

      1, 2. Tunajua jinsi gani kwamba Wayahudi wengi wa karne ya kwanza walitumaini kupata uzima milele duniani?

      KIJANA mmoja tajiri na mashuhuri alimkimbilia Yesu, akapiga magoti mbele yake na kumuuliza hivi: “Mwalimu Mwema, nifanye nini ili niurithi uzima wa milele?” (Marko 10:17) Kijana huyo alikuwa akiuliza kuhusu kurithi uzima wa milele, lakini wapi? Kama tulivyozungumzia katika habari iliyotangulia, karne nyingi mapema Mungu aliwapa Wayahudi tumaini la ufufuo na la uzima wa milele duniani. Wayahudi wengi wa karne ya kwanza bado walikuwa na tumaini hilo.

      2 Inaelekea Martha, rafiki ya Yesu, alikuwa akifikiria tumaini la watu kufufuliwa duniani aliposema hivi kuhusu ndugu yake aliyekufa: “Ninajua atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.” (Yoh. 11:24) Kwa kweli, wakati huo Masadukayo hawakuamini ufufuo. (Marko 12:18) Hata hivyo, katika kitabu chake (Judaism in the First Centuries of the Christian Era), George Foot Moore anasema hivi: “Maandishi . . . ya karne ya pili au ya kwanza kabla ya wakati wetu yanathibitisha imani ya kwamba katika wakati uliotarajiwa wa mabadiliko katika historia ya ulimwengu wale waliokufa katika vizazi vya zamani watafufuliwa na kuishi tena duniani.” Yule mwanamume tajiri aliyemwendea Yesu alitaka kupata uzima wa milele duniani.

      3. Tutazungumzia maswali gani katika habari hii?

      3 Leo, dini nyingi na wasomi wengi wa Biblia wanapinga kwamba tumaini la kuishi milele duniani ni fundisho la Kikristo. Watu wengi wanatumaini kuishi mbinguni baada ya kufa. Hivyo, wasomaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo wanapoona maneno “uzima wa milele,” wengi wanafikiri kwamba sikuzote yanamaanisha kuishi mbinguni. Je, ni kweli? Yesu alimaanisha nini aliposema kuhusu uzima wa milele? Wanafunzi wake waliamini nini? Je, Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanafundisha kuhusu tumaini la kuishi milele duniani?

      Uzima wa Milele “Katika Uumbaji-Mpya”

      4. Ni mambo gani yatakayotukia “katika uumbaji-mpya”?

      4 Biblia inafundisha kwamba Wakristo watiwa-mafuta watafufuliwa ili watawale juu ya dunia wakiwa mbinguni. (Luka 12:32; Ufu. 5:9, 10; 14:1-3) Hata hivyo, Yesu alipozungumza kuhusu uzima wa milele, sikuzote hakuwa tu akifikiria kikundi hicho. Fikiria yale aliyowaambia wanafunzi wake baada ya yule kijana tajiri kukataa kwa huzuni mwaliko wa kuacha mali yake yote na kuwa mfuasi wa Kristo. (Soma Mathayo 19:28, 29.) Yesu aliwaambia mitume wake kwamba watakuwa kati ya wale ambao watatawala wakiwa wafalme na kuyahukumu “makabila kumi na mawili ya Israeli,” yaani, ulimwengu wa wanadamu bila kutia ndani wale watakaotawala wakiwa mbinguni. (1 Kor. 6:2) Pia, alisema kwamba “kila mtu” ambaye atamfuata atapata thawabu. Watu hao pia ‘watarithi uzima wa milele.’ Mambo hayo yote yatatukia “katika uumbaji-mpya.”

      5. “Uumbaji-mpya” ni nini?

      5 Yesu alimaanisha nini aliposema “uumbaji-mpya”? Maneno hayo yanatafsiriwa kuwa “ulimwengu mpya” katika Biblia Habari Njema. Katika Biblia ya The Jerusalem Bible yanatafsiriwa kuwa “mambo yote yatakapofanywa mapya,” na katika Biblia ya The Holy Bible—New International Version yanatafsiriwa kuwa “kufanywa upya kwa mambo yote.” Kwa kuwa Yesu alitumia maneno hayo bila kuyafafanua, ni wazi kwamba alikuwa akizungumza kuhusu tumaini ambalo Wayahudi walikuwa nalo kwa karne nyingi. Kungekuwa na uumbaji-mpya wa hali za dunia, hivi kwamba mambo yangekuwa kama yalivyokuwa katika bustani ya Edeni kabla ya Adamu na Hawa kutenda dhambi. Uumbaji-mpya utatimiza ahadi ya Mungu ya ‘kuumba mbingu mpya na dunia mpya.’—Isa. 65:17.

      6. Mfano wa kondoo na mbuzi unatufundisha nini kuhusu tumaini la uzima wa milele?

      6 Yesu alitaja pia uzima wa milele katika hotuba yake kuhusu umalizio wa mfumo wa mambo. (Mt. 24:1-3) Alisema hivi: “Wakati Mwana wa binadamu atakapofika katika utukufu wake, na malaika wote pamoja naye, ndipo atakapoketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu. Na mataifa yote yatakusanyika mbele yake, naye atawatenganisha watu, mmoja kutoka kwa mwenzake, kama vile mchungaji anavyotenganisha kondoo na mbuzi.” Wale watakaohukumiwa adhabu “watakatiliwa mbali milele, lakini waadilifu wataingia katika uzima wa milele.” “Waadilifu” ambao watapokea uzima wa milele ni wale ambao wanawaunga mkono kwa ushikamanifu “ndugu” za Kristo waliotiwa-mafuta kwa roho. (Mt. 25:31-34, 40, 41, 45, 46) Kwa kuwa watiwa-mafuta wanachaguliwa ili wawe watawala katika Ufalme wa mbinguni, “waadilifu” hao ni lazima wawe raia wa kidunia wa Ufalme huo. Biblia ilitabiri hivi: “[Mfalme wa Yehova] atakuwa na raia kutoka bahari mpaka bahari na kutoka ule Mto mpaka miisho ya dunia.” (Zab. 72:8) Raia hao watafurahia uzima wa milele duniani.

      Injili ya Yohana Inaonyesha Nini?

      7, 8. Yesu alizungumza na Nikodemo kuhusu matumaini gani mawili tofauti?

      7 Kama ilivyoandikwa katika Injili ya Mathayo, Marko, na Luka, Yesu alitumia maneno “uzima wa milele” katika pindi zilizotajwa hapo juu. Injili ya Yohana inanukuu mara 17 maneno ya Yesu kuhusu kuishi milele. Acheni tuchunguze baadhi ya manukuu hayo ili tuone yale ambayo Yesu alisema kuhusu tumaini la kuishi milele duniani.

      8 Kulingana na Yohana, mtu wa kwanza ambaye Yesu alizungumza naye kuhusu uzima wa milele alikuwa Farisayo aliyeitwa Nikodemo. Alimwambia Nikodemo hivi: “Mtu asipozaliwa kwa maji na roho, hawezi kuingia katika ufalme wa Mungu.” Ni lazima wale wanaoingia katika Ufalme wa mbinguni ‘wazaliwe tena.’ (Yoh. 3:3-5) Yesu hakusema hayo tu. Pia, alisema kuhusu tumaini ambalo watu wote ulimwenguni wanaweza kupata. (Soma Yohana 3:16.) Yesu alikuwa akizungumza kuhusu tumaini la uzima wa milele huko mbinguni kwa ajili ya wafuasi wake watiwa-mafuta na kwa wengine duniani.

      9. Yesu alizungumza na mwanamke Msamaria kuhusu tumaini gani?

      9 Baada ya kuzungumza na Nikodemo huko Yerusalemu, Yesu alisafiri upande wa kaskazini kuelekea Galilaya. Njiani, alikutana na mwanamke mmoja kwenye chemchemi ya Yakobo karibu na jiji la Sikari huko Samaria. Alimwambia hivi: “Yule atakayekunywa maji ambayo nitampa hatapatwa na kiu hata kidogo, lakini maji ambayo nitampa yatakuwa chemchemi ya maji ndani yake, inayobubujika ili kutokeza uzima wa milele.” (Yoh. 4:5, 6, 14) Maji hayo yanawakilisha maandalizi ya Mungu ya kuwarudishia wanadamu wote uzima wa milele, kutia ndani wale ambao wataishi duniani. Katika kitabu cha Ufunuo, Mungu mwenyewe anasema hivi: “Kwa yeyote aliye na kiu mimi nitampa maji bure kutoka kwenye chemchemi ya maji ya uzima.” (Ufu. 21:5, 6; 22:17) Kwa hiyo, Yesu alizungumza na yule mwanamke Msamaria kuhusu uzima wa milele si tu kwa ajili ya warithi wa Ufalme watiwa-mafuta bali pia kwa ajili ya wanadamu waaminifu ambao wana tumaini la kuishi duniani.

      10. Baada ya kumponya mtu fulani mgonjwa karibu na dimbwi la Bethzatha, Yesu aliwaambia nini wapinzani wa kidini kuhusu uzima wa milele?

      10 Mwaka uliofuata, Yesu alirudi tena Yerusalemu. Akiwa huko, alimponya mtu fulani mgonjwa karibu na dimbwi la Bethzatha. Yesu aliwaambia hivi Wayahudi ambao walishutumu jambo alilofanya: “Mwana hawezi kufanya hata jambo moja kwa uamuzi wake mwenyewe, ila tu lile analomwona Baba akifanya.” Baada ya kuwaambia kwamba Baba “amemkabidhi Mwana kazi yote ya kuhukumu,” Yesu alisema: “Yule ambaye husikia neno langu na kumwamini yule aliyenituma ana uzima wa milele.” Pia, Yesu alisema hivi: “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [ya Mwana wa binadamu] na kutoka, wale waliotenda mambo mema kwenye ufufuo wa uzima, wale waliokuwa na zoea la kutenda mambo maovu kwenye ufufuo wa hukumu.” (Yoh. 5:1-9, 19, 22, 24-29) Yesu alikuwa akiwaambia Wayahudi waliokuwa wakimtesa kwamba yeye ndiye aliyewekwa rasmi na Mungu kutimiza tumaini la Wayahudi la kupata uzima wa milele duniani na kwamba angefanya hivyo kwa kuwafufua wafu.

      11. Tunajua jinsi gani kwamba maneno ambayo Yesu alisema kwenye Yohana 6:48-51 yanahusu pia tumaini la kuishi milele duniani?

      11 Akiwa Galilaya, maelfu ya watu waliotaka mikate ambayo Yesu aliandaa kimuujiza walianza kumfuata. Yesu akawaambia kuhusu mkate wa aina nyingine—“mkate wa uzima.” (Soma Yohana 6:40, 48-51.) Alisema hivi: “Mkate ambao nitatoa ni mwili wangu.” Yesu alitoa uhai wake si kwa ajili tu ya wale ambao atatawala nao katika Ufalme wake wa kimbingu, bali pia “kwa ajili ya uzima wa ulimwengu” wa wanadamu wanaoweza kukombolewa. “Yeyote akila mkate huu,” yaani, akionyesha imani katika uwezo wa kukomboa wa dhabihu ya Yesu, atakuwa na tumaini la kupata uzima wa milele. Kwa kweli, maneno ‘kuishi milele’ yalitia ndani tumaini ambalo Wayahudi walikuwa nalo kwa muda mrefu la kuishi milele duniani chini ya utawala wa Masihi.

      12. Yesu alikuwa akizungumza kuhusu tumaini gani alipowaambia wapinzani wake kwamba ‘atawapa kondoo wake uzima wa milele’?

      12 Baadaye, kwenye Sherehe ya Wakfu huko Yerusalemu, Yesu aliwaambia hivi wapinzani wake: “Hamwamini, kwa sababu ninyi hamko kati ya kondoo wangu. Kondoo wangu huisikiliza sauti yangu, nami ninawajua, nao wananifuata. Nami ninawapa hao uzima wa milele.” (Yoh. 10:26-28) Je, Yesu alikuwa akizungumza tu kuhusu uzima wa milele mbinguni, au alikuwa pia akizungumzia uzima wa milele katika paradiso duniani? Muda mfupi kabla ya hapo, Yesu alikuwa amewafariji wafuasi wake kwa maneno haya: “Msiogope, kundi dogo, kwa sababu Baba yenu amekubali kuwapa ninyi ufalme.” (Luka 12:32) Hata hivyo, wakati wa Sherehe hiyo ya Wakfu, Yesu alisema: “Nina kondoo wengine, ambao si wa zizi hili; hao pia nitawaleta.” (Yoh. 10:16) Kwa hiyo, Yesu alipozungumza na wapinzani hao, alimaanisha tumaini la kuishi mbinguni kwa ajili ya “kundi dogo” na tumaini la kuishi milele duniani kwa ajili ya mamilioni ya “kondoo wengine.”

      Tumaini Ambalo Halikuhitaji Kufafanuliwa

      13. Yesu alimaanisha nini aliposema: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso”?

      13 Yesu alipokuwa akiteseka kwenye mti wa mateso, alitoa uthibitisho usioweza kupingwa wa tumaini la wanadamu. Mtenda-maovu mmoja aliyetundikwa kando yake alimwambia hivi: “Yesu, unikumbuke utakapoingia katika ufalme wako.” Yesu alimwahidi hivi: “Kwa kweli mimi nakuambia leo, Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” (Luka 23:42, 43) Kwa kuwa ni wazi kwamba mtu huyo alikuwa Myahudi, hakuhitaji kufafanuliwa kuhusu Paradiso. Alijua kuhusu tumaini la uzima wa milele duniani wakati ujao.

      14. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba ilikuwa vigumu kwa mitume kuelewa maelezo kuhusu tumaini la kwenda mbinguni? (b) Ni wakati gani wafuasi wa Yesu walipoelewa vizuri kabisa tumaini la kwenda mbinguni?

      14 Hata hivyo, yaliyohitaji kufafanuliwa ni maelezo ya Yesu kuhusu tumaini la kwenda mbinguni. Alipowaambia wanafunzi wake kwamba anaenda mbinguni ili kuwatayarishia mahali, hawakuelewa kile alichomaanisha. (Soma Yohana 14:2-5.) Baadaye aliwaambia hivi: “Bado nina mambo mengi ya kuwaambia, lakini hamwezi kuyastahimili kwa sasa. Hata hivyo, huyo atakapofika, roho ya ile kweli, atawaongoza ninyi ndani ya kweli yote.” (Yoh. 16:12, 13) Ni baada tu ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. walipotiwa mafuta kwa roho ya Mungu ili kuwa wafalme wakati ujao ndipo wafuasi wa Yesu walipoelewa kwamba viti vyao vya ufalme vitakuwa mbinguni. (1 Kor. 15:49; Kol. 1:5; 1 Pet. 1:3, 4) Tumaini la urithi wa kimbingu lilikuwa jambo jipya, na lilikaziwa zaidi katika barua zilizoongozwa na roho ya Mungu ambazo ni sehemu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Je, barua hizo zinathibitisha tumaini la wanadamu la kuishi milele duniani?

      Barua Zilizoongozwa na Roho ya Mungu Zinasema Nini?

      15, 16. Barua kwa Waebrania iliyoongozwa na roho ya Mungu na maneno ya Petro yanaonyesha jinsi gani tumaini la kuishi milele duniani?

      15 Katika barua yake kwa Waebrania, mtume Paulo aliwaita waamini wenzake “ndugu watakatifu, washiriki wa mwito wa mbinguni.” Hata hivyo, alisema pia kwamba Mungu ameitiisha chini ya Yesu “dunia yenye kukaliwa inayokuja.” (Ebr. 2:3, 5; 3:1) Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno la awali linalotafsiriwa “dunia yenye kukaliwa” sikuzote linamaanisha dunia inayokaliwa na wanadamu. Kwa hiyo, “dunia yenye kukaliwa inayokuja” ni mfumo wa mambo wa wakati ujao duniani chini ya utawala wa Yesu Kristo. Wakati huo, Yesu atatimiza ahadi hii ya Mungu: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zab. 37:29.

      16 Mtume Petro pia aliongozwa na roho ya Mungu kuandika kuhusu wakati ujao wa wanadamu. Aliandika hivi: “Mbingu na dunia za sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto nazo zinahifadhiwa mpaka ile siku ya hukumu na ya kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.” (2 Pet. 3:7) Ni nini kitakachochukua mahali pa mbingu za kiserikali na jamii ya sasa ya wanadamu waovu? (Soma 2 Petro 3:13.) Zitaondolewa na mahali pake kuchukuliwa na “mbingu mpya,” yaani, Ufalme wa Kimasihi wa Mungu, na “dunia mpya,” yaani, jamii ya wanadamu waadilifu ambao ni waabudu wa kweli.

      17. Tumaini la wanadamu linaelezwa jinsi gani kwenye Ufunuo 21:1-4?

      17 Mioyo yetu inachochewa na maono ya kitabu cha mwisho cha Biblia yanayohusu kurudishwa kwa wanadamu kwenye hali ya ukamilifu. (Soma Ufunuo 21:1-4.) Wanadamu waaminifu wamekuwa na tumaini hilo tangu ukamilifu wa wanadamu ulipopotezwa katika bustani ya Edeni. Watu waadilifu wataishi milele katika Paradiso duniani bila kuzeeka. Tumaini hilo linategemea kabisa Maandiko ya Kiebrania na pia Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, na linaendelea kuwatia nguvu watumishi waaminifu wa Yehova mpaka leo.—Ufu. 22:1, 2.

  • Uzima wa Milele Duniani—Tumaini Lililofunuliwa Tena
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Agosti 15
    • Uzima wa Milele Duniani—Tumaini Lililofunuliwa Tena

      “Ee Danieli, yafanye siri maneno hayo . . . mpaka wakati wa mwisho. Wengi watakwenda huku na huku, na ujuzi wa kweli utakuwa mwingi.”—DAN. 12:4.

      1, 2. Tutachunguza maswali gani katika habari hii?

      MAMILIONI ya watu leo wanaelewa wazi msingi wa Kimaandiko wa tumaini la kuishi milele katika paradiso duniani. (Ufu. 7:9, 17) Mwanzoni mwa historia ya wanadamu, Mungu alifunua kwamba mwanadamu hakuumbwa ili aishi miaka michache tu kisha afe, bali aliumbwa aishi milele.—Mwa. 1:26-28.

      2 Waisraeli walitumaini kwamba wanadamu watarudishiwa hali ya ukamilifu ambayo Adamu alipoteza. Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanaeleza jinsi ambavyo Mungu atawawezesha wanadamu kuishi milele katika Paradiso duniani. Hivyo basi, kwa nini tumaini la wanadamu lilihitaji kufunuliwa tena? Lilifunuliwa jinsi gani na kutangazwa kwa mamilioni ya watu?

      Tumaini Ambalo Lilikuwa Limefichwa

      3. Kwa nini haishangazi kwamba tumaini la wanadamu la kuishi milele duniani lilifichwa?

      3 Yesu alitabiri kwamba manabii wa uwongo wangepotosha mafundisho yake na kwamba watu wengi wangepotoshwa. (Mt. 24:11) Mtume Petro aliwaonya Wakristo hivi: ‘Pia kutakuwa na walimu wa uwongo katikati yenu.’ (2 Pet. 2:1) Mtume Paulo alisema kuhusu ‘kipindi cha wakati ambapo watu hawangevumilia fundisho lenye afya, bali, kwa kupatana na tamaa zao wenyewe, wangejikusanyia walimu kwa ajili yao wenyewe ili masikio yao yafurahishwe.’ (2 Tim. 4:3, 4) Shetani anahusika katika kuwapotosha watu na ametumia Wakristo waasi-imani kuficha kweli zenye kuchangamsha moyo kuhusu kusudi la Mungu kwa ajili ya wanadamu na dunia.—Soma 2 Wakorintho 4:3, 4.

      4. Viongozi wa kidini waasi-imani wamekataa tumaini gani la wanadamu?

      4 Maandiko yanaeleza kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali iliyo mbinguni ambayo itaziponda na kuzikomesha serikali zote za wanadamu. (Dan. 2:44) Wakati wa utawala wa miaka elfu wa Kristo, Shetani atafungiwa ndani ya abiso, wafu watafufuliwa, na wanadamu watainuliwa na kuwa wakamilifu hapa duniani. (Ufu. 20:1-3, 6, 12; 21:1-4) Hata hivyo, viongozi waasi-imani wa dini zinazodai kuwa za Kikristo wamekubali mawazo mengine. Kwa mfano, Origen wa Aleksandria, Baba wa Kanisa katika karne ya tatu aliwashutumu watu walioamini kwamba Utawala wa Miaka Elfu utaleta baraka duniani. Mwanatheolojia Mkatoliki Augustine wa Hippo (354-430 W.K.) “aliamini kwamba hakutakuwa na utawala wa miaka elfu,” kinasema kitabu kimoja (The Catholic Encyclopedia).a

      5, 6. Kwa nini Origen na Augustine walipinga fundisho la utawala wa miaka elfu?

      5 Kwa nini Origen na Augustine walipinga fundisho la utawala wa miaka elfu? Origen alikuwa mwanafunzi wa Clement wa Aleksandria, ambaye alikubali wazo la kutokufa kwa nafsi ambalo lilitegemea mapokeo ya Wagiriki. Origen alifuata sana mawazo ya Plato kuhusu nafsi hivi kwamba “akaingiza katika mafundisho ya Kikristo mawazo ya Plato kuhusu nafsi na mahali inapoenda,” anasema mwanatheolojia Werner Jaeger. Kwa hiyo, Origen alifundisha kwamba baraka zozote za Utawala wa Miaka Elfu hazingekuwa duniani bali zingekuwa katika makao ya roho.

      6 Kabla ya kuwa “Mkristo” akiwa na umri wa miaka 33, Augustine alikuwa mfuasi wa falsafa mpya za Plato ambazo zilianzishwa na Plotinus katika karne ya tatu. Baada ya Augustine kuwa Mkristo, aliendelea kufuata falsafa hizo mpya za Plato. Kitabu kimoja (The New Encyclopædia Britannica) kinasema hivi kumhusu Augustine: “Alitimiza fungu kubwa sana katika kuchanganya kabisa mafundisho ya Agano Jipya na mafundisho ya Plato ya falsafa za Kigiriki.” Kitabu kingine (The Catholic Encyclopedia) kinasema kuwa Augustine alieleza kwamba Utawala wa Miaka Elfu unaotajwa katika kitabu cha Ufunuo sura ya 20 ulikuwa wa “mfano” tu. Kinaongezea hivi: “Maelezo hayo . . . yalikubaliwa na wanatheolojia wa nchi za Magharibi walioishi baadaye, na fundisho la mwanzoni la utawala wa miaka elfu halikuungwa mkono tena.”

      7. Ni imani gani ya uwongo iliyoficha tumaini la wanadamu la kuishi milele duniani, na ililificha jinsi gani?

      7 Tumaini la wanadamu la kuishi milele duniani lilifichwa na wazo ambalo lilifundishwa katika Babiloni la kale na kuenea ulimwenguni pote, wazo la kwamba mwanadamu ana nafsi isiyoweza kufa au roho inayokaa tu katika mwili wa mwanadamu. Dini zinazodai kuwa za Kikristo zilipokubali wazo hilo, wanatheolojia walipotosha Maandiko ili kufanya mistari inayozungumzia tumaini la mbinguni ionekane kwamba inafundisha kuwa watu wote wazuri wanaenda mbinguni. Kulingana na maoni hayo, maisha ya mtu duniani yamekusudiwa kuwa mafupi tu, yaani, anajaribiwa ili kuona ikiwa anastahili kuishi mbinguni. Jambo fulani kama hilo lilitukia kuhusiana na tumaini la mwanzoni la Wayahudi la kuishi milele duniani. Wayahudi walipokubali hatua kwa hatua wazo la Wagiriki la kwamba nafsi haiwezi kufa, tumaini lao la hapo mwanzoni la kuishi duniani lilitoweka. Wazo hilo ni tofauti kabisa na fundisho la Biblia kuhusu mwanadamu! Mwanadamu ni kiumbe aliye na mwili wa nyama, wala si kiumbe wa roho. Yehova alimwambia mwanadamu wa kwanza hivi: “Wewe ni mavumbi.” (Mwa. 3:19) Dunia ndiyo makao ya milele ya mwanadamu, bali si mbingu.—Soma Zaburi 104:5; 115:16.

      Kweli Inaangaza Gizani

      8. Wasomi fulani katika miaka ya 1600 walisema nini kuhusu tumaini la wanadamu?

      8 Ingawa dini nyingi zinazodai kuwa za Kikristo zinakataa tumaini la kuishi milele duniani, sikuzote Shetani hakufaulu kuficha ukweli. Tangu zamani, wasomaji wachache waangalifu wa Biblia waliona nuru ya kweli ikiangaza walipoendelea kuelewa mambo fulani yanayoonyesha jinsi Mungu atakavyowarudisha wanadamu kwenye ukamilifu. (Zab. 97:11; Mt. 7:13, 14; 13:37-39) Kufikia miaka ya 1600, kazi ya kutafsiri na kuchapisha Biblia iliwawezesha watu wengi kupata Maandiko Matakatifu. Mwaka wa 1651, msomi mmoja aliandika kwamba kwa kuwa kupitia Adamu watu “wamepoteza Paradiso, na Uzima wa Milele Duniani,” hivyo katika Kristo, “watu wote watawezeshwa kuishi Duniani; ikiwa sivyo, ulinganifu huo haufai.” (Soma 1 Wakorintho 15:21, 22.) Mmoja wa watungaji maarufu wa mashairi katika nchi zinazozungumza Kiingereza ulimwenguni, John Milton (1608-1674), aliandika shairi lenye kichwa Paradiso Iliyopotea na la pili Paradiso Iliyopatikana. Katika mashairi hayo, Milton alitaja thawabu ambayo waaminifu watapata katika paradiso duniani. Ingawa Milton alitumia wakati mwingi wa maisha yake kujifunza Biblia, alitambua kwamba kweli ya Kimaandiko haingeeleweka kikamili mpaka wakati wa kuwapo kwa Kristo.

      9, 10. Isaac Newton aliandika nini kuhusu tumaini la wanadamu? (b) Kwa nini Newton aliona kwamba wakati wa kuwapo kwa Kristo ulikuwa mbali sana?

      9 Pia, mtaalamu mashuhuri wa hesabu Sir Isaac Newton (1642-1727) alipendezwa sana na Biblia. Alielewa kwamba watakatifu watafufuliwa na kuishi mbinguni nao watatawala bila kuonekana pamoja na Kristo. (Ufu. 5:9, 10) Aliandika hivi kuhusu raia wa Ufalme huo: “Dunia itaendelea kukaliwa na wanadamu wanaoweza kufa baada ya siku ya hukumu na si kwa miaka 1000 tu bali hata kwa umilele wote.”

      10 Newton alikuwa na maoni ya kwamba kuwapo kwa Kristo kungetukia karne nyingi baadaye. Mwanahistoria Stephen Snobelen alisema hivi: “Sababu moja iliyomfanya Newton aseme kwamba Ufalme wa Mungu ungekuja baada ya muda mrefu ni kwamba alitilia shaka sana fundisho la uasi-imani la Utatu ambalo lilikuwa limeenea sana.” Habari njema ilikuwa bado imefichwa. Na Newton hakuona kikundi chochote cha Kikristo ambacho kingeweza kuhubiri habari hiyo njema. Aliandika hivi: “Unabii huu wa Danieli na wa Yohana [ambao unapatikana katika kitabu cha Ufunuo] hautaeleweka mpaka wakati wa mwisho.” Newton alieleza hivi: “‘Kisha,’ Danieli akasema, ‘wengi watakimbia huku na huku, na ujuzi utaongezeka.’ Ni lazima Injili ihubiriwe katika mataifa yote kabla ya ile dhiki kuu na mwisho wa ulimwengu. Umati mkubwa unaobeba matawi ya mitende mikononi, ambao unatoka katika hiyo dhiki kuu, hauwezi kuwa na watu wengi wasiohesabika kutoka katika mataifa yote, isipokuwa Injili ihubiriwe kabla ya dhiki hiyo kufika.”—Dan. 12:4; Mt. 24:14; Ufu. 7:9, 10.

      11. Kwa nini tumaini la wanadamu liliendelea kufichwa kwa watu wengi katika siku za Milton na Newton?

      11 Katika siku za Milton na Newton, ilikuwa hatari kupinga mafundisho rasmi ya kanisa. Kwa hiyo, maandishi mengi kuhusu utafiti wao wa Biblia hayakuchapishwa mpaka baada ya kifo chao. Marekebisho ya Kidini ya karne ya 16 yalishindwa kurekebisha fundisho la kwamba nafsi haiwezi kufa, na makanisa makubwa ya Kiprotestanti yaliendelea kufundisha wazo la Augustine la kwamba Utawala wa Miaka Elfu ulikuwa umepita, na haungekuja wakati ujao. Je, ujuzi umeongezeka wakati huu wa mwisho?

      “Ujuzi wa Kweli Utakuwa Mwingi”

      12. Ujuzi wa kweli ungekuwa mwingi wakati gani?

      12 Danieli alitabiri kwamba jambo zuri sana lingetukia katika “wakati wa mwisho.” (Soma Danieli 12:3, 4, 9, 10.) Yesu alisema: “Wakati huo waadilifu watang’aa kwa uangavu kama jua.” (Mt. 13:43) Ujuzi wa kweli ulikuwa mwingi jinsi gani katika wakati wa mwisho? Chunguza matukio fulani ya kihistoria katika makumi ya miaka kabla ya mwaka wa 1914, mwaka ambao wakati wa mwisho ulianza.

      13. Charles Taze Russell aliandika nini baada ya kuchunguza kuhusu kurudishwa kwa wanadamu kwenye ukamilifu?

      13 Katika miaka ya mwisho ya 1800, watu wachache wanyoofu walikuwa wakijitahidi kuelewa “kielelezo cha maneno yenye afya.” (2 Tim. 1:13) Mmoja wa watu hao alikuwa Charles Taze Russell. Katika mwaka wa 1870, yeye na watu wengine wachache waliokuwa wakitafuta kweli walianzisha kikundi cha kujifunza Biblia. Katika mwaka wa 1872, walichunguza kuhusu kurudishwa kwa wanadamu kwenye ukamilifu. Baadaye, Russell aliandika: “Kufikia wakati huo, hatukuwa tumeona wazi tofauti kubwa kati ya thawabu ya kanisa ambalo linajaribiwa sasa na thawabu ya wanadamu wote waaminifu.” Wanadamu waaminifu “watarudishwa katika hali ya ukamilifu ambayo pindi moja babu yao na kichwa, Adamu, alifurahia katika Edeni.” Russell alikiri kwamba watu wengine walimsaidia kujifunza Biblia. Ni nani hao?

      14. (a) Henry Dunn alielewa jinsi gani andiko la Matendo 3:21? (b) Dunn alisema ni nani watakaoishi milele duniani?

      14 Mmoja wao alikuwa Henry Dunn. Alikuwa ameandika kuhusu “kurudishwa kwa mambo yote ambayo Mungu alisema kupitia kinywa cha manabii wake watakatifu wa nyakati za kale.” (Mdo. 3:21) Dunn alijua kwamba kurudishwa huko kulitia ndani kuinuliwa kwa wanadamu kwenye ukamilifu duniani wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. Pia, Dunn alichunguza swali ambalo liliwatatanisha wengi, Ni nani watakaoishi milele duniani? Alieleza kwamba mamilioni ya watu watafufuliwa, wafundishwe kweli, kisha wapewe nafasi ya kuonyesha imani katika Kristo.

      15. George Storrs alielewa nini kuhusu ufufuo?

      15 Mwaka wa 1870, George Storrs alikata kauli pia kwamba watu wasio waadilifu watafufuliwa na kupewa nafasi ya kuishi milele. Pia, alielewa kutokana na Maandiko kwamba mtu atakayefufuliwa ambaye hatatumia vizuri nafasi hiyo “atakufa, hata ingawa ‘mtenda-dhambi huyo atakuwa na umri wa miaka mia moja.’” (Isa. 65:20) Storrs aliishi Brooklyn, New York, na alikuwa mhariri wa gazeti lililoitwa Bible Examiner.

      16. Ni nini kilichowatofautisha Wanafunzi wa Biblia na dini zinazodai kuwa za Kikristo?

      16 Russell alitambua kutokana na Biblia kwamba wakati ulikuwa umefika wa kutangaza habari njema ulimwenguni pote. Hivyo, katika mwaka wa 1879, alianza kuchapisha gazeti Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence, sasa linaitwa Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova. Kabla ya hapo, ni watu wachache sana walioelewa ukweli kuhusu tumaini la wanadamu, lakini sasa vikundi vya Wanafunzi wa Biblia katika nchi nyingi vilikuwa vikipokea na kujifunza gazeti la Mnara wa Mlinzi. Imani ya kwamba ni watu wachache tu ndio wanaoenda mbinguni, huku mamilioni ya watu wakipewa uhai mkamilifu wa kibinadamu duniani, iliwafanya Wanafunzi wa Biblia wawe tofauti kabisa na dini nyingi zinazodai kuwa za Kikristo.

      17. Ujuzi wa kweli uliongezeka sana jinsi gani?

      17 “Wakati wa mwisho” uliotabiriwa ulianza mwaka wa 1914. Je, ujuzi wa kweli kuhusu tumaini la wanadamu uliongezeka sana? (Dan. 12:4) Kufikia mwaka wa 1913, hotuba za Russell zilichapishwa katika magazeti 2,000 yaliyosomwa na jumla ya wasomaji milioni 15. Kufikia mwisho wa mwaka wa 1914, watu zaidi ya milioni 9 katika mabara matatu walikuwa wameona sinema ya picha na slaidi ya “Photo-Drama of Creation” (Photo-Drame de la Création) ambayo ilieleza kuhusu Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. Kuanzia mwaka wa 1918 mpaka 1925, hotuba yenye kichwa “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe,” ambayo ilieleza kuhusu tumaini la uzima wa milele duniani, ilitolewa na watumishi wa Yehova katika lugha zaidi ya 30 ulimwenguni pote. Kufikia mwaka wa 1934, Mashahidi wa Yehova walitambua kwamba wale wanaotumaini kuishi milele duniani walipaswa kubatizwa. Uelewaji huo uliwachochea kuwa na bidii zaidi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme. Leo, mamilioni ya watu wanamshukuru sana Yehova kutoka moyoni kwa sababu ya tumaini la kuishi milele duniani.

      “Uhuru Wenye Utukufu” Uko Mbele!

      18, 19. Ni maisha ya aina gani yanayotabiriwa kwenye Isaya 65:21-25?

      18 Nabii Isaya aliongozwa na roho ya Mungu kuandika kuhusu maisha ambayo watu wa Mungu watafurahia duniani. (Soma Isaya 65:21-25.) Kwa kweli, miti fulani ambayo ilikuwepo miaka 2,700 hivi iliyopita Isaya alipoandika maneno hayo bado ipo leo. Je, unaweza kujiwazia ukiishi kwa muda mrefu hivyo ukiwa na nguvu na afya nzuri?

      19 Badala ya wanadamu kuishi kwa muda mfupi na kisha kufa, watakuwa na nafasi nyingi za kujenga, kupanda, na kujifunza. Fikiria nafasi utakazokuwa nazo za kupata marafiki wengi. Mahusiano hayo yenye upendo yatadumu milele. “Watoto wa Mungu” watafurahia “uhuru wenye utukufu” kama nini duniani!—Rom. 8:21.

      [Maelezo ya chini]

      a Augustine alidai kwamba Utawala wa Miaka Elfu wa Ufalme wa Mungu haukuwa wa wakati ujao bali ulianza wakati kanisa lilipoanzishwa.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki