-
Estonia2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
KUSANYIKO LENYE SHANGWE NCHINI URUSI
Tukio lingine muhimu katika historia ya kitheokrasi ni kusanyiko la kimataifa lililofanyika huko St. Petersburg, nchini Urusi, mnamo Juni 1992. Kwa wengi kati ya wajumbe 1,000 waliohudhuria kutoka Estonia, hiyo ilikuwa pindi nzuri ya kukutana tena na wafungwa wenzao na Mashahidi wengine waliokutana nao walipokuwa uhamishoni huko Siberia.
“Kusanyiko hilo lilipangwa kufanyika wakati unaofaa kabisa,” mjumbe mmoja anasema. “Tulikodi gari-moshi maalum kwa gharama ya chini kwa kutumia rubo za Urusi. Kisha, juma moja kabla ya kusanyiko, Estonia ikaanza kutumia krooni ya Estonia badala ya rubo. Kama tungekuwa nje ya Estonia juma hilo la kubadilisha pesa, hatungeweza kubadilisha pesa zetu. Hata hivyo, ingawa tulikuwa Estonia tuliruhusiwa kubadilisha kiasi kidogo tu cha pesa. Tungefanya nini na rubo ambazo hatukuweza kubadilisha? Kwa sababu rubo bado zilikuwa zinatumiwa nchini Urusi, akina ndugu walibeba rubo hizo kwenye kusanyiko na kuzitumbukiza katika masanduku ya michango. Zaidi ya hilo, kama kusanyiko lingefanywa juma moja baadaye, wakati sheria mpya za mipaka zilipotekelezwa, tungehitaji kupata viza kwa gharama ya juu ili kuvuka mpaka. Kusanyiko hilo lilifanywa wakati unaofaa kabisa kwa akina ndugu!”
Mmoja kati ya watu wengi walioguswa sana na kusanyiko hilo la kihistoria ni mwanamke fulani mwenye kupendezwa ambaye alipanga kusafiri pamoja na Mashahidi wa Estonia. “Sikuelewa vizuri muda wa kuondoka,” anasema. “Nilipofika kwenye kituo, gari-moshi lilikuwa tayari limeondoka. Lakini nilikuwa tayari nimelipa nauli. Ningefanya nini sasa? Nilisali kwa Yehova, nikimwomba anisaidie na kumwahidi kwamba nitafanya chochote niwezacho ili niweze kufika kusanyikoni.”
“Msimamizi wa kituo cha gari-moshi aliniambia kwamba ninapaswa kununua tiketi nyingine, lakini sikuwa na pesa za kutosha! Ghafla, nikaona kikundi cha watu wakiwasili. Wote walikuwa na shangwe na walivalia vizuri! Walikuwa Mashahidi kutoka kisiwa cha Sarema. Gari-moshi lao lilikuwa bado halijawasili, na hivyo ningeweza kutumia tiketi yangu kusafiri pamoja nao. Nilifarijika sana!
“Tulipokuwa tukisafiri Mashahidi waliimba nyimbo za Ufalme, ambazo zilinigusa sana. Nilijihisi kana kwamba nimekubalika kuwa mshiriki wa familia yao ya kiroho. Nilikaa nao muda wote wa kusanyiko na kuona kuwa walikuwa wanyofu na wenye upendo. Hilo liliondoa shaka zangu zote. Sasa ilikuwa wazi kwangu kwamba nilikuwa nimepata tengenezo la kidunia la Mungu.” Mwanamke huyo sasa anatumika akiwa painia wa kawaida pamoja na mume wake.
-
-
Estonia2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 238]
Kusanyiko la kimataifa jijini St. Petersburg, Urusi, mwaka wa 1992
-