Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kuushinda Upweke
    Amkeni!—2004 | Juni 8
    • Kuushinda Upweke

      KUKABILI upweke si jambo rahisi. Hisia za upweke zina nguvu. Mtu anaweza kukabilianaje na upweke? Watu fulani wamefanya nini ili kushinda hisia za upweke?

      Kukabili Upweke

      Helena anapenda kuwa peke yake anapofanya maamuzi fulani, lakini anahisi kwamba upweke unaweza kuwa hatari. Alipokuwa mtoto, hakuwa akiwasiliana na wazazi wake. Kwa kuwa hakujua jinsi ya kuwasiliana nao, alikuwa akijifungia chumbani mwake. Anaeleza hivi: “Nilianza kuwa na matatizo ya kula. Nilishuka moyo sana. Nilikuwa nikijiambia, ‘Kwa nini nijihangaishe na matatizo ya wazazi wangu na wao hawahangaikii matatizo yangu?’ Kisha nikafikiri kwamba ndoa ingeniondolea upweke. Niliona ndoa kuwa kimbilio. Lakini punde si punde nikajiuliza: ‘Kwa nini nimharibie mtu mwingine maisha? Kwanza, ni lazima nijirekebishe!’ Nilimwomba Yehova msaada na kumjulisha hangaiko langu.

      “Nilipata maneno yenye kufariji sana katika Biblia. Kwa mfano, andiko la Isaya 41:10 linasema hivi: ‘Usiogope, kwa maana mimi nipo pamoja nawe. Usitazame huku na huku, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu. Nitakusaidia kwelikweli. Nitakushika kwelikweli kwa mkono wangu wa kuume wa uadilifu.’ Maneno hayo yalinisaidia sana kwa sababu nilijiona kama yatima. Leo mimi husoma Biblia kwa ukawaida na kusali kwa Baba yangu wa mbinguni. Nimejifunza kushinda upweke.”

      Mtu anapofiwa na mtu anayempenda anakuwa na huzuni inayoweza kumfanya ahisi upweke. Luisa, mwenye umri wa miaka 16, anaeleza huzuni yake hivi: “Baba yangu aliuawa nilipokuwa na umri wa miaka mitano. Nilitazamia kufarijiwa na nyanya yangu. Lakini sikuhisi kwamba ananipenda. Nilipokuwa mchanga, sikuonyeshwa upendo niliohitaji sana. Nilipokuwa na umri wa kati ya miaka nane na tisa, nilijaribu kujiua mara tatu. Nilidhani kwamba kufanya hivyo kungefaidi familia yetu kwa sababu mama yangu alikuwa na kazi ngumu ya kunilisha mimi na dada zangu watatu. Kisha tukaanza kushirikiana na Mashahidi wa Yehova. Wenzi wawili wa ndoa walipendezwa nami kikweli. Walikuwa wakiniambia: ‘Tunakuthamini na tunakuhitaji.’ Maneno ‘tunakuhitaji,’ yaliniimarisha sana. Nyakati nyingine siwezi kumweleza mtu ninavyohisi, lakini ninaposoma makala zinazochapishwa katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! mimi humshukuru Yehova kwa maana vichapo hivyo vimeniwezesha kujua kwamba ananipenda. Nimefanya mabadiliko mengi. Leo ninaweza kutabasamu na ninaweza pia kumweleza mama yangu ninapokuwa na huzuni au shangwe. Nyakati nyingine mimi hukumbuka mambo yaliyopita lakini sihisi kama zamani, wakati ambapo nilitaka kujiua na hata kuacha kuongea na wapendwa wangu. Sikuzote mimi hukumbuka alivyosema mtunga-zaburi Daudi: ‘Kwa ajili ya ndugu zangu na wenzangu nitasema sasa: “Amani na iwe ndani yako.”’”—Zaburi 122:8.

      Martha aliyetalikiwa miaka 22 iliyopita na ambaye amemlea mtoto katika kipindi hicho anasema hivi, “Mimi huanza kuhisi upweke na kwamba sifai kitu ninapofikiri kwamba nimekosa kufanya jambo fulani.” Yeye hukabilianaje na hisia hizo? Anaeleza hivi: “Nimeona kwamba njia bora zaidi ya kushughulika na hisia hizo ni kuongea na Yehova Mungu bila kukawia. Ninaposali, ninajua kwamba siko peke yangu. Yehova ananielewa vizuri zaidi kuliko ninavyojielewa. Pia, mimi hujaribu kupendezwa na watu wengine. Huduma yangu ya wakati wote hunisaidia sana kushinda hisia hizo mbaya. Unapoongea na watu wengine kuhusu baraka za Ufalme wa Mungu na kutambua kwamba wasikilizaji wako hawana tumaini lolote na kwamba wanaona matatizo yao kuwa ya kudumu, unatambua kwamba maisha yana kusudi na unapata nguvu za kukabiliana na hisia hizo.”

      Elba, mwenye umri wa miaka 93 na ambaye mtoto wake wa pekee ni mishonari katika nchi nyingine, anasema hivi kuhusu anavyokabiliana na upweke: “Binti yangu na mume wake walipoalikwa kuhudhuria Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower, niliona nyuso zao ziking’aa kwa shangwe, nami nikashangilia pamoja nao. Baadaye, walipopokea mgawo wa kutumikia katika nchi ya kigeni, nilianza kuwa na ubinafsi kidogo. Nilijua kwamba sitakuwa karibu nao tena, nikahuzunika kwa kiasi fulani. Hali hiyo ilionekana kama ile ya Yeftha na binti yake wa pekee inayosimuliwa kwenye Waamuzi sura ya 11. Nilimwomba Yehova nikilia, na kumwomba anisamehe. Watoto wangu huwasiliana nami sikuzote. Ninajua kwamba wana shughuli nyingi sana, lakini popote wanapotumikia, wao hutafuta wakati wa kuwasiliana nami, wakinieleza mambo ambayo wamejionea katika huduma ya shambani. Mimi husoma barua zao tena na tena. Ni kana kwamba wanazungumza nami kila juma, nami ninathamini sana jambo hilo. Pia, wazee Wakristo katika kutaniko letu hutuhangaikia sisi tulio wazee na dhaifu kimwili, wakihakikisha kwamba tuna namna ya kufika kwenye mikutano ya kutaniko na kutuandalia mahitaji yetu mengine. Mimi huwaona ndugu na dada zangu wa kiroho kuwa baraka kutoka kwa Yehova.”

      Wewe Pia Unaweza Kukabiliana na Upweke

      Uwe mchanga au mzee, mseja au umefunga ndoa, mtoto mwenye wazazi au yatima, na uwe umefiwa na wapendwa au unahisi upweke kwa sababu ya hali nyingine, kuna njia za kukabiliana na hisia zako. Jocabed, msichana mwenye umri wa miaka 18, ambaye baba yake aliiacha familia ya watu sita na kuhamia nchi nyingine, anasema hivi: “Sema waziwazi! Ni muhimu kueleza hisia zetu. Tusipofanya hivyo, hakuna mtu atakayetuelewa.” Anapendekeza hivi: “Usijifikirie sana. Tafuta msaada kutoka kwa watu wakomavu badala ya vijana ambao huenda hali zao zikawa mbaya zaidi kuliko zako.” Luisa, aliyetajwa awali, anasema hivi, “Kusali kwa Yehova kutoka moyoni hutusaidia kukabiliana na upweke.” Jorge, aliyefiwa na mkewe, anaeleza jinsi anavyokabiliana na upweke: “Ustahimilivu unahitajiwa. Kupendezwa na watu wengine hunisaidia sana. ‘Kuonyesha hisia-mwenzi’ tunapozungumza na wengine kunaweza kufanya mazungumzo yetu yawe na maana na kunaweza kutusaidia kutambua sifa nzuri za watu wengine.”—1 Petro 3:8.

      Tunaweza kufanya mengi ili kushinda upweke. Lakini, je, kuna wakati ambapo upweke hautakuwapo? Ikiwa ndivyo, itawezekanaje? Makala inayofuata itajibu maswali hayo.

      [Maelezo ya Chini]

      a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

      [Blabu katika ukurasa wa 8]

      “Kusali kwa Yehova kutoka moyoni hutusaidia kukabiliana na upweke.”—Luisa

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

      Jinsi Unavyoweza Kukabiliana na Upweke

      ◼ Kumbuka kwamba hali yako inaweza kubadilika, si hali ya kudumu na kwamba watu wengi wako katika hali hiyo.

      ◼ Usitazamie mengi kupita kiasi.

      ◼ Ridhika na hali yako kwa ujumla.

      ◼ Sitawisha mazoea mazuri ya kula, kufanya mazoezi ya mwili, na kupata usingizi wa kutosha.

      ◼ Unapokuwa peke yako, tumia wakati huo kufanya mambo mapya na kujifunza stadi mpya.

      ◼ Jihadhari usiwahukumu watu unaokutana nao kulingana na mambo yaliyokupata wakati uliopita.

      ◼ Wathamini rafiki zako na sifa zao za pekee. Jitahidi kupata rafiki wazuri. Omba maoni ya watu wenye umri mkubwa zaidi na wenye uzoefu.

      ◼ Fanyia wengine mambo kama vile kutabasamu, kusema jambo la fadhili, na kuwatajia jambo fulani kutoka katika Biblia. Kuhisi kwamba wengine wanakuhitaji kunaweza kukusaidia kushinda upweke.

      ◼ Epuka kuwazia-wazia uwezekano wa kuwa na uhusiano na watu maarufu kwenye sinema, televisheni, Intaneti, au kwenye vitabu.

      ◼ Ikiwa umefunga ndoa, usimtazamie mwenzi wako akutimizie mahitaji yako yote ya kihisia. Jifunzeni kushirikiana na kupatana, kusaidiana na kutegemezana.

      ◼ Jifunze kuongea na wengine, na kusitawisha uwezo wako wa kuzungumza kwa njia yenye kuvutia. Zingatia watu wengine na mapendezi yao. Uwe na hisia-mwenzi.

      ◼ Kubali kwamba unahisi upweke, na uzungumze na rafiki mzuri mkomavu, unayemwamini. Usijinyamazie.

      ◼ Epuka kunywa pombe kupita kiasi, au hata usinywe kamwe. Pombe haiondoi matatizo yako, muda si muda, matatizo hayo huzuka tena.

      ◼ Epuka kuwa na kiburi. Wasamehe wale wanaokuumiza, na kufanya mapatano nao. Usiwe mwenye kushuku watu kupita kiasi.

  • Wakati Ambapo Hakuna Mtu Atakayehisi Upweke Tena
    Amkeni!—2004 | Juni 8
    • Rafiki bora zaidi tunayeweza kumpata ni Yehova Mungu. Mtume Paulo anakiri kwamba Yehova ni “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote.” (2 Wakorintho 1:3, 4) Yehova mwenyewe huhuzunishwa anapoona yeyote kati ya watumishi wake akiteseka. Yeye ni Mungu mwenye hisia-mwenzi. “Kwa maana yeye mwenyewe analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.” (Zaburi 103:14) Je, huvutiwi na Yehova Mungu na kuthamini uangalifu wake wenye upendo, fadhili, na jinsi anavyotujali?

      Yehova Huwategemeza Wapweke

      Watumishi wa zamani wa Mungu walikabili hali zilizowafanya wahisi upweke. Yehova aliwategemeza na kuwafariji. Kwa mfano, mfikirie Yeremia, aliyepata utume wa kuwa nabii akiwa kijana. Kati ya watu 40 walioandika Biblia, yaelekea Yeremia ndiye aliyeeleza mengi zaidi kuhusu hisia zake. Aliogopa na kuhisi kwamba hakustahili kupokea mgawo wake wa kwanza kutoka kwa Mungu. (Yeremia 1:6) Ili kutimiza mgawo wake, alihitaji kumtegemea Yehova kabisa. Kwa kweli, alimwona Yehova kuwa “mwenye nguvu anayetisha.”—Yeremia 1:18, 19; 20:11.

      Miaka 300 hivi kabla ya wakati wa Yeremia, Malkia Yezebeli aliapa kumwua Eliya aliposikia kuhusu kuuawa kwa manabii wake wa Baali. Eliya alikimbia kilometa zipatazo 450 hadi Horebu katika Rasi ya Sinai. Kisha akaingia pangoni ili kukaa humo usiku, naye Yehova Mungu akamwuliza hivi: “Una kazi gani hapa, Eliya?” Eliya akaeleza kwamba anahisi kuwa yeye peke yake ndiye mwabudu wa Yehova katika Israeli yote, nabii pekee aliyekuwa na bidii kwa ajili ya utumishi wa Mungu. Yehova alimhakikishia kwamba hakuwa peke yake. Yehova alikuwa pamoja naye. Waisraeli wenzake 7,000 walikuwa pamoja naye pia, ingawa Eliya hakujua. Yehova alimfariji, akamtuliza Eliya na kuimarisha imani yake. Alimchochea Eliya, na kumtia moyo asiuache mgawo wake. (1 Wafalme 19:4, 9-12, 15-18) Tukihisi upweke au kuhisi kwamba hatufai, kama alivyohisi Eliya, sisi pia tunaweza kumwomba Yehova atuimarishe. Pia, kwa kutumia utambuzi, wazee Wakristo wanaweza kuwafariji wale walio waaminifu, wakiwasaidia kuona sehemu wanayotimiza katika kusudi la Mungu.—1 Wathesalonike 5:14.

      Kutokana na mfano huo na mingine mingi, tunaweza kuona kwamba Yehova yuko tayari kuwategemeza na kuwafariji kwa upendo wale wanaohisi upweke. Naam, “Yehova atakuwa kilele salama kwa ajili ya mtu yeyote aliyekandamizwa, kilele salama wakati wa taabu.”—Zaburi 9:9; 46:1; Nahumu 1:7.

      Mtu Aliyekuwa na Hisia Nyingi na Huruma

      Yesu Kristo alimwiga Yehova kwa kudhibiti hisia zake kikamili. Luka anaeleza jinsi Yesu alivyofanya alipoukaribia umati uliokuwa ukienda kumzika mfu katika jiji la Naini: “Kulikuwa na mfu akiwa anapelekwa nje, mwana mzaliwa-pekee wa mama yake. . . . Bwana alipomwona akamsikitikia, akamwambia: ‘Acha kulia.’ Ndipo akakaribia na kuligusa sanduku, na wachukuzi wakasimama tuli, naye akasema: ‘Kijana, ninakuambia, Inuka!’ Na huyo mfu akaketi na kuanza kusema, naye akamkabidhi kwa mama yake.” (Luka 7:12-15) Hisia za Yesu zilichochewa sana. Alikuwa mwenye huruma. Hebu wazia shangwe ya mjane huyo mpweke Yesu alipomfufua mwana wake! Upweke wake uliisha.

      Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yesu anaweza “kuusikitikia udhaifu wetu.” Yeye huwasikitikia watu wenye upweke ambao ni wanyofu. Ama kweli, kupitia yeye tunaweza “[kupokea] rehema na kupata fadhili zisizostahiliwa kuwa msaada kwa wakati unaofaa.” (Waebrania 4:15, 16) Kwa kumwiga Yesu, tunaweza kuwasikitikia walio na huzuni, wanaoteseka, na wapweke. Tukiwasaidia wengine, hatutahisi upweke. Lakini, bado kuna njia nyingine inayoweza kutusaidia kushinda hisia mbaya za upweke.

      Neno la Yehova Linaweza Kutusaidia Kushinda Upweke

      Wengi wameona kwamba “kupitia faraja kutokana na Maandiko [tuna] tumaini.” Neno la Mungu lina mashauri mengi yanayoweza kutusaidia kushinda upweke. (Waroma 15:4; Zaburi 32:8) Kwa mfano, Neno la Mungu hutuhimiza ‘tusijifikirie wenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.’ (Waroma 12:3) Ili tutumie shauri hilo, huenda tukahitaji kubadili maoni yetu. Kuwa na unyenyekevu na kiasi, yaani kutambua uwezo wetu, kutatusaidia kuwa na usawaziko na kutotazamia mambo yanayopita uwezo wetu. Neno la Mungu hutushauri pia tupendezwe kikweli na wengine. (Wafilipi 2:4) Unapojitahidi kupendezwa na kuwahangaikia wengine, wao pia watapendezwa na kukuhangaikia. Ushirika huo mzuri huondoa upweke na hufanya maisha yetu yawe na kusudi.

      Biblia hututia moyo sisi Wakristo ‘tusiache kukusanyika pamoja sisi wenyewe.’ (Waebrania 10:24, 25) Kwa hiyo, shiriki katika utendaji wenye manufaa, kama vile kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova kwa ukawaida. Bila shaka, mikutano ya Kikristo inaweza kuchangia afya yetu ya kiroho, kihisia, na kimwili. Kuzungumza na wengine kuhusu habari njema za Ufalme wa Mungu kunaweza kufanya maisha yetu yawe na furaha. Kufanya hivyo hutufanya tukazie fikira zetu mambo yanayofaa, huimarisha imani yetu, na kulinda tumaini letu.—Waefeso 6:14-17.

      Mkaribie Yehova katika sala. Daudi alisihi hivi: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza.” (Zaburi 55:22) Ukijifunza Neno la Mungu, utakuwa na furaha. (Zaburi 1:1-3) Ukilemewa na hisia za upweke, tafakari upendo wa Yehova unaofunuliwa katika Neno lake. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Nafsi yangu imekuwa ikishikamana na mavumbi. Nihifadhi hai kulingana na neno lako.”—Zaburi 119:25.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki