-
Upweke Katika Ulimwengu Uliojaa MawasilianoAmkeni!—2010 | Septemba
-
-
Katika kitabu chao Loneliness—Human Nature and the Need for Social Connection, watafiti John T. Cacioppo na William Patrick wanazungumzia kwa undani kuhusu upweke. Wanazungumzia uchunguzi mmoja uliosema kwamba “kutumia sana Intaneti badala ya kuzungumza na mtu moja kwa moja, kunaweza kufanya watu wajitenge na jamii na pia kuongeza kushuka moyo.”
Hekaheka za maisha ya kisasa zinafanya iwe vigumu kwa watu kuwasiliana kwa njia inayofaa. Kwa kawaida, huwezi kuona uso wenye tabasamu na upendo unapowasiliana na mtu kupitia simu au kwa kutuma ujumbe kupitia kompyuta.
Zaidi tu ya kutokea kazini, mambo yaliyotajwa hapa juu hutokea pia katika familia. Katika nyumba nyingi, watu wa familia huja na kuondoka bila kula pamoja au kuzungumza pamoja. Vijana wana kompyuta zao wenyewe nao hujitenga na watu wengine wa familia. Licha ya kwamba wana vifaa vingi vya mawasiliano, vijana wengi hujihisi wakiwa wapweke.
Siku hizi hata ndoa zinaweza kuhatarishwa kwa sababu ya wenzi kujihisi wakiwa wapweke. Wenzi wa ndoa wasipowasiliana, wanaweza kuwa katika nyumba moja lakini kila mtu anaishi maisha yake. Kuhisi upweke huku ukiwa unaishi na mwenzi wa ndoa ni upweke unaofadhaisha sana.
Wazazi wasio na mwenzi hasa wanaweza kupatwa na hisia za upweke. Mbali na vitu vingine vingi, kuwepo kwa vifaa vingi sana vya mawasiliano kunaweza kukatiza mawasiliano kati ya mzazi na watoto na hivyo kufanya hisia za upweke ziongezeke. Pia waseja wengi wanatamani kuwa na mwenzi, lakini mahitaji yao ya kihisia hayatoshelezwi.
-
-
Upweke Unasababishwa na Nini?Amkeni!—2010 | Septemba
-
-
Ni nini humfanya mtu ajihisi mpweke?
● Kujitenga Katika Majiji Yaliyojaa Watu
Katika majiji makubwa, maelfu au hata mamilioni ya watu huishi karibu-karibu. Hata hivyo, inashangaza kwamba msongamano huo wa watu huchangia upweke. Pilkapilka za maisha ya jijini hufanya watu wasiwafahamu vizuri majirani wao. Hilo huwafanya watu wanaoishi jijini wachangamane na watu wasiowajua. Hali ya watu kuwashuku watu wasiowajua na kutaka kulinda faragha yao, kumechangia pakubwa upweke katika majiji makubwa.
● Wafanyakazi Kutendewa Kinyama
Wasimamizi katika biashara na viwanda vikubwa wamefanya wafanyakazi wote wajihisi upweke na wasiofaa kitu. Mara nyingi, wafanyakazi hushinikizwa na kupata mkazo usiokoma.
Isitoshe, kuhamishwa-hamishwa kwa wafanyakazi katika makampuni makubwa huwafanya wahisi kwamba kazi yao iko hatarini, wametengwa, na ni wapweke. Likizungumzia idadi kubwa ya visa vya kujiua kati ya wafanyakazi wa makampuni fulani huko Ufaransa, gazeti International Herald Tribune lilisema kwamba “kwa sababu ya mabadiliko ya kiuchumi,” wafanyakazi wengi huko Ufaransa wanahisi kwamba “wanashinikizwa kupita uwezo wao.”
● Mawasiliano Yasiyo na Hisia
Nchini Japani, Profesa Tetsuro Saito alisema: “Simu za mkononi na vifaa vingine vinapunguza uwezo wetu wa kuwasiliana na wengine kwa hisia.” Huko Australia, gazeti The Sunday Telegraph liliripoti hivi: “Teknolojia . . . inawafanya watu wajitenge kihisia. Watu . . . hutumiana ujumbe mfupi au barua-pepe badala ya kuzungumza moja kwa moja.”
Akieleza ni kwa nini anajihisi mpweke, Rachel, mwenye umri wa miaka 21, anayeishi Ufaransa alilalamika hivi: “Watu hawajitahidi kukutembelea, kwa kuwa wanafikiri kwamba kukutumia ujumbe mfupi, barua-pepe, na kutumia vituo vya maongezi kunatosha. Lakini hilo hunifanya nijihisi mpweke hata zaidi.”
● Mazingira Mapya
Kuzorota kwa uchumi kumewalazimisha watu kuhamia maeneo mengine ili wadumishe kazi zao au watafute kazi. Kuhama hufanya watu waache majirani, marafiki, shule, na nyakati nyingine familia zao. Wale wanaohama ni kama mmea uliong’olewa na kupandwa mahali pengine lakini mizizi yake ikabaki mahali ulipong’olewa.
Francis, anakumbuka siku aliyowasili Ufaransa kutoka Ghana. Anaeleza, “Kwa kuwa sikuelewa lugha, sikuwa na marafiki, na kulikuwa na baridi sana, nilijihisi mpweke sana.”
Akikumbuka wakati alipowasili Uingereza akiwa mhamiaji, Behjat anasema: “Ilikuwa vigumu sana kuzoea desturi za huko. Niliwafahamu watu fulani lakini sikuwa na marafiki wa karibu au watu wa familia ambao ningeweza kuzungumza nao na kuwaeleza hisia zangu.”
● Kifo cha Mtu Unayempenda
Kifo cha mwenzi wa ndoa huacha pengo kubwa. Inakuwa hivyo hasa ikiwa mtu alimtunza mwenzi huyo kwa kipindi kirefu. Mtu huhisi maisha yake yakiwa matupu kabisa.
Fernande, mjane anayeishi Paris anaeleza, “Jambo linaloniumiza sana ni kwamba siwezi tena kumweleza rafiki yangu mkubwa, yaani, mume wangu mambo yaliyo moyoni.” Anny anasema kwamba anamkosa sana mume wake “hasa wakati nina maamuzi muhimu ya kufanya kuhusu afya au mambo mengine.”
● Talaka, Kutengana, Kuwa Mseja Bila Kutaka
Talaka au kutengana humfanya mtu ajihisi mpweke na hafai. Tofauti na ilivyodhaniwa na wataalamu, watoto ndio wanaoathiriwa zaidi. Wataalamu fulani wanasema kwamba kuna uwezekano wa watoto kuwa wapweke wanapokuwa watu wazima kwa sababu wazazi wao walitalikiana.
Wale ambao hawajafunga ndoa kwa sababu hawawezi kupata mwenzi wa ndoa anayefaa huhisi upweke pindi fulani. Hisia hizo zinaweza kuongezeka watu wanaposema maneno yenye kuumiza kama, “Ungekuwa na furaha zaidi ikiwa ungekuwa umefunga ndoa.”
Wazazi wasio na mwenzi pia huwa wapweke. Kazi ya kulea watoto ina shangwe na matatizo pia, na inabidi wazazi wasio na mwenzi watatue matatizo hayo wakiwa peke yao.
● Uzee na Vijana Wasio na Hekima
Huenda wazee wakahisi upweke hata ingawa wanatunzwa na watu wa familia. Huenda watu wa ukoo au marafiki wakawatembelea mara kwa mara, lakini namna gani pindi ambazo hakuna mtu anayewatembelea, labda kwa siku au majuma kadhaa?
Si wazee tu ambao huhisi upweke. Vijana wengi hujihisi wakiwa wapweke pia. Wengi wao wamekuwa waraibu wa burudani zisizohusisha watu wengine kama vile kutazama televisheni, kucheza michezo ya video, au kutumia kompyuta kwa saa nyingi.
-