-
Upweke Katika Ulimwengu Uliojaa MawasilianoAmkeni!—2010 | Septemba
-
-
Upweke Katika Ulimwengu Uliojaa Mawasiliano
SIMU za mkononi, ujumbe mfupi, barua-pepe, vituo vya mawasiliano, vituo vya maongezi—hakujawahi kuwa na pindi ambapo kuna njia nyingi za kuwasiliana kama leo. Hata hivyo, katika ulimwengu huu wenye njia nyingi za mawasiliano, watu wengi, vijana kwa wazee, ni wapweke sana. Kwa nini?
Katika kitabu chao Loneliness—Human Nature and the Need for Social Connection, watafiti John T. Cacioppo na William Patrick wanazungumzia kwa undani kuhusu upweke. Wanazungumzia uchunguzi mmoja uliosema kwamba “kutumia sana Intaneti badala ya kuzungumza na mtu moja kwa moja, kunaweza kufanya watu wajitenge na jamii na pia kuongeza kushuka moyo.”
Hekaheka za maisha ya kisasa zinafanya iwe vigumu kwa watu kuwasiliana kwa njia inayofaa. Kwa kawaida, huwezi kuona uso wenye tabasamu na upendo unapowasiliana na mtu kupitia simu au kwa kutuma ujumbe kupitia kompyuta.
Zaidi tu ya kutokea kazini, mambo yaliyotajwa hapa juu hutokea pia katika familia. Katika nyumba nyingi, watu wa familia huja na kuondoka bila kula pamoja au kuzungumza pamoja. Vijana wana kompyuta zao wenyewe nao hujitenga na watu wengine wa familia. Licha ya kwamba wana vifaa vingi vya mawasiliano, vijana wengi hujihisi wakiwa wapweke.
Siku hizi hata ndoa zinaweza kuhatarishwa kwa sababu ya wenzi kujihisi wakiwa wapweke. Wenzi wa ndoa wasipowasiliana, wanaweza kuwa katika nyumba moja lakini kila mtu anaishi maisha yake. Kuhisi upweke huku ukiwa unaishi na mwenzi wa ndoa ni upweke unaofadhaisha sana.
Wazazi wasio na mwenzi hasa wanaweza kupatwa na hisia za upweke. Mbali na vitu vingine vingi, kuwepo kwa vifaa vingi sana vya mawasiliano kunaweza kukatiza mawasiliano kati ya mzazi na watoto na hivyo kufanya hisia za upweke ziongezeke. Pia waseja wengi wanatamani kuwa na mwenzi, lakini mahitaji yao ya kihisia hayatoshelezwi.
Upweke umekuwa tatizo kubwa katika jamii ambalo linaweza kusababisha uraibu wa kileo, kula kupita kiasi, kutumia dawa za kulevya, kufanya ngono ovyoovyo, na hata kujiua. Kwa hiyo, ni muhimu kutambua visababishi vya upweke. Kuchukua hatua hiyo ya kwanza kutamsaidia mtu kukabiliana inavyofaa na tatizo hilo.
-
-
Upweke Unasababishwa na Nini?Amkeni!—2010 | Septemba
-
-
Upweke Unasababishwa na Nini?
KUNA tofauti kati ya upweke na kuwa peke yako. Upweke ni kuwa peke yako huku ukitamani kuwa na watu wa kushirikiana nao. Lakini mtu aliye peke yake ametengwa au kujitenga na watu wengine.
Ni vizuri kutaka kuwa peke yako nyakati nyingine. Mara nyingi watu hutafuta wakati wa kuwa peke yao ili wasali au kutafakari kama Yesu Kristo alivyofanya. (Mathayo 14:13; Luka 4:42; 5:16; 6:12) Kwa upande mwingine, upweke ni hisia inayoleta maumivu. Ni nini humfanya mtu ajihisi mpweke?
● Kujitenga Katika Majiji Yaliyojaa Watu
Katika majiji makubwa, maelfu au hata mamilioni ya watu huishi karibu-karibu. Hata hivyo, inashangaza kwamba msongamano huo wa watu huchangia upweke. Pilkapilka za maisha ya jijini hufanya watu wasiwafahamu vizuri majirani wao. Hilo huwafanya watu wanaoishi jijini wachangamane na watu wasiowajua. Hali ya watu kuwashuku watu wasiowajua na kutaka kulinda faragha yao, kumechangia pakubwa upweke katika majiji makubwa.
● Wafanyakazi Kutendewa Kinyama
Wasimamizi katika biashara na viwanda vikubwa wamefanya wafanyakazi wote wajihisi upweke na wasiofaa kitu. Mara nyingi, wafanyakazi hushinikizwa na kupata mkazo usiokoma.
Isitoshe, kuhamishwa-hamishwa kwa wafanyakazi katika makampuni makubwa huwafanya wahisi kwamba kazi yao iko hatarini, wametengwa, na ni wapweke. Likizungumzia idadi kubwa ya visa vya kujiua kati ya wafanyakazi wa makampuni fulani huko Ufaransa, gazeti International Herald Tribune lilisema kwamba “kwa sababu ya mabadiliko ya kiuchumi,” wafanyakazi wengi huko Ufaransa wanahisi kwamba “wanashinikizwa kupita uwezo wao.”
● Mawasiliano Yasiyo na Hisia
Nchini Japani, Profesa Tetsuro Saito alisema: “Simu za mkononi na vifaa vingine vinapunguza uwezo wetu wa kuwasiliana na wengine kwa hisia.” Huko Australia, gazeti The Sunday Telegraph liliripoti hivi: “Teknolojia . . . inawafanya watu wajitenge kihisia. Watu . . . hutumiana ujumbe mfupi au barua-pepe badala ya kuzungumza moja kwa moja.”
Akieleza ni kwa nini anajihisi mpweke, Rachel, mwenye umri wa miaka 21, anayeishi Ufaransa alilalamika hivi: “Watu hawajitahidi kukutembelea, kwa kuwa wanafikiri kwamba kukutumia ujumbe mfupi, barua-pepe, na kutumia vituo vya maongezi kunatosha. Lakini hilo hunifanya nijihisi mpweke hata zaidi.”
● Mazingira Mapya
Kuzorota kwa uchumi kumewalazimisha watu kuhamia maeneo mengine ili wadumishe kazi zao au watafute kazi. Kuhama hufanya watu waache majirani, marafiki, shule, na nyakati nyingine familia zao. Wale wanaohama ni kama mmea uliong’olewa na kupandwa mahali pengine lakini mizizi yake ikabaki mahali ulipong’olewa.
Francis, anakumbuka siku aliyowasili Ufaransa kutoka Ghana. Anaeleza, “Kwa kuwa sikuelewa lugha, sikuwa na marafiki, na kulikuwa na baridi sana, nilijihisi mpweke sana.”
Akikumbuka wakati alipowasili Uingereza akiwa mhamiaji, Behjat anasema: “Ilikuwa vigumu sana kuzoea desturi za huko. Niliwafahamu watu fulani lakini sikuwa na marafiki wa karibu au watu wa familia ambao ningeweza kuzungumza nao na kuwaeleza hisia zangu.”
● Kifo cha Mtu Unayempenda
Kifo cha mwenzi wa ndoa huacha pengo kubwa. Inakuwa hivyo hasa ikiwa mtu alimtunza mwenzi huyo kwa kipindi kirefu. Mtu huhisi maisha yake yakiwa matupu kabisa.
Fernande, mjane anayeishi Paris anaeleza, “Jambo linaloniumiza sana ni kwamba siwezi tena kumweleza rafiki yangu mkubwa, yaani, mume wangu mambo yaliyo moyoni.” Anny anasema kwamba anamkosa sana mume wake “hasa wakati nina maamuzi muhimu ya kufanya kuhusu afya au mambo mengine.”
● Talaka, Kutengana, Kuwa Mseja Bila Kutaka
Talaka au kutengana humfanya mtu ajihisi mpweke na hafai. Tofauti na ilivyodhaniwa na wataalamu, watoto ndio wanaoathiriwa zaidi. Wataalamu fulani wanasema kwamba kuna uwezekano wa watoto kuwa wapweke wanapokuwa watu wazima kwa sababu wazazi wao walitalikiana.
Wale ambao hawajafunga ndoa kwa sababu hawawezi kupata mwenzi wa ndoa anayefaa huhisi upweke pindi fulani. Hisia hizo zinaweza kuongezeka watu wanaposema maneno yenye kuumiza kama, “Ungekuwa na furaha zaidi ikiwa ungekuwa umefunga ndoa.”
Wazazi wasio na mwenzi pia huwa wapweke. Kazi ya kulea watoto ina shangwe na matatizo pia, na inabidi wazazi wasio na mwenzi watatue matatizo hayo wakiwa peke yao.
● Uzee na Vijana Wasio na Hekima
Huenda wazee wakahisi upweke hata ingawa wanatunzwa na watu wa familia. Huenda watu wa ukoo au marafiki wakawatembelea mara kwa mara, lakini namna gani pindi ambazo hakuna mtu anayewatembelea, labda kwa siku au majuma kadhaa?
Si wazee tu ambao huhisi upweke. Vijana wengi hujihisi wakiwa wapweke pia. Wengi wao wamekuwa waraibu wa burudani zisizohusisha watu wengine kama vile kutazama televisheni, kucheza michezo ya video, au kutumia kompyuta kwa saa nyingi.
Je, kuna suluhisho kwa tatizo hili linalozidi kuenea? Ni nini kinachoweza kumsaidia mtu kukabiliana na upweke?
[Blabu katika ukurasa wa 5]
“Kwa kuwa sikuelewa lugha, sikuwa na marafiki, na kulikuwa na baridi sana, nilijihisi mpweke sana”
-
-
Suluhisho la UpwekeAmkeni!—2010 | Septemba
-
-
Suluhisho la Upweke
IKIWA wewe ni mpweke, ingefaa ujiulize: ‘Je, kuna mambo ninayoweza kufanya ili kuboresha hali yangu? Je, huenda ninahitaji kufanya mabadiliko fulani maishani? Ikiwa ndivyo, nifanye mabadiliko gani?’ Maswali yafuatayo yanaweza kukusaidia kujichunguza na kupata suluhisho linalofaa.
Je, Ninahitaji Kubadili Mtazamo Wangu?
Mtu yeyote anaweza kuwa mpweke. Lakini hali hiyo inaleta matatizo inapoendelea kwa muda mrefu. Inapoendelea kwa muda mrefu, huenda hilo likaonyesha kwamba una mtazamo usiofaa. Huenda tatizo likawa jinsi unavyotenda unapokuwa na watu wengine. Huenda mtu akajiwekea ua wa seng’enge bila kutaka na kuwafanya wengine wasitake kuwa marafiki wake. Nyakati nyingine mtu anahitaji tu kubadili mtazamo wake.
Sabine, aliyehamia Uingereza anasema hivi: “Inachukua muda kwa marafiki wapya kuaminiana na kuzoeana. Mbona usiwaulize wengine kuhusu malezi yao? Niliambiwa hivi: ‘Huwezi kusema kwamba tamaduni fulani ndiyo bora. Jifaidi na mambo mazuri kutoka katika tamaduni zote.’” Kama Sabine alivyotiwa moyo kufanya, unaweza kutafuta sifa nzuri katika tamaduni za wengine ambazo zitakufaidi ukiziiga.
Je, Mimi Hupenda Kuwaepuka Wengine?
Huenda ukajiuliza: ‘Je, mimi hupenda kuwaepuka watu? Je, wanaweza kuwa wenye urafiki zaidi ikiwa nitakuwa mwenye urafiki zaidi?’ Ikiwa unahisi hilo ndilo tatizo, jitahidi kuwa mwenye urafiki zaidi. Roselise, mwenye umri wa miaka 30, kutoka Guadeloupe ambaye alihamia Uingereza alisema, “Watu wanaohisi upweke wana mwelekeo wa kujitenga na wengine.” Hivyo anashauri hivi: “Tafuta watu ambao pia wanaonekana kuwa wapweke. Chukua hatua ya kwanza ya kuzungumza nao. Nyakati nyingine, swali moja tu hutokeza urafiki wenye kudumu.”
Hata hivyo, wakati na jitihada zinahitajika ili kusitawisha urafiki wa karibu. Njia moja ya kufanya hivyo ni kuwa msikilizaji mzuri. Ukisikiliza kwa makini, utajua mambo yanayompendeza mwenzako. Kumbuka, kuwa na hisia-mwenzi huchangia urafiki!
Je, Nina Maoni Yasiyofaa?
Kujidharau kunaweza kumzuia mtu kuanzisha urafiki. Jiulize, ‘Je, nina mwelekeo wa kuwa na maoni yasiyofaa kujihusu?’ Abigaïl, mwenye umri wa miaka 15 anayeishi Ghana, anasema hivi: “Nyakati nyingine nilikuwa na maoni yasiyofaa ambayo yalinifanya niwe mpweke. Nilijihisi kuwa sifai na hakuna mtu anayenipenda.” Uwe na hakika kwamba ukichukua hatua ya kwanza kuwafikia na kuwasaidia wengine kwa njia fulani, hawatakudharau. Huenda hata wakataka kuwa rafiki zako. Kwa hiyo, mbona usichukue hatua hiyo ya kwanza?
Kuwa na maoni yanayofaa pia kutakusaidia kuanzisha urafiki na watu ambao si wa rika lako. Kuwa na marafiki ambao wamekuzidi umri au wale uliowazidi umri kunathawabisha. Abigaïl alishinda upweke hasa kwa kuwa na marafiki waliomzidi umri. Anaeleza, “Nilifaidika sana kutokana na uzoefu wao.”
Je, Mimi Hujitenga na Wengine?
Watu wengi walio wapweke hujituliza kwa kutazama televisheni au kucheza michezo ya video kwa vipindi virefu, au kutumia kompyuta zao. Lakini wanapozima vifaa hivyo, upweke hurudi. Elsa, mwenye umri wa miaka 21, anayeishi Paris anakubaliana na hilo, anasema, “Televisheni na michezo ya video inaweza kuwa kama dawa ya kulevya ambayo humwathiri mtu hadi afikie hatua ya kutotaka kuwa na marafiki.”
Madhara ya kutazama televisheni ni kwamba watu hawazungumzi, kubadilishana mawazo, au hawapati nafasi ya kusitawisha urafiki. Michezo ya video ina madhara hayohayo—inampeleka mtu kwenye ulimwengu wa kuwaziwa ambao hutoweka punde tu anapoacha kucheza. Kutembelea vituo mbalimbali vya Intaneti bila kusudi lolote kunaweza kumfanya mtu asahau matatizo yake, lakini pia vituo hivyo vinaweza kuonyesha mambo mapotovu kiadili na kufanya ukutane na watu wanaoficha utu wao. Intaneti si mahali pazuri pa kutafuta au kusitawisha urafiki wa kweli.
Je, Ninatafuta Mwenzi wa Ndoa?
Huenda waseja fulani wakataka kufunga ndoa ili tu waepuke kuwa wapweke. Ni kweli kwamba mwenzi mwenye fadhili na upendo anaweza kukufanya uwe na furaha sana maishani, lakini uwe mwangalifu usikimbilie ndoa.
Huenda ndoa isiwe suluhisho kwa tatizo la upweke. Inasemekana kwamba wenzi wa ndoa walio na tatizo la kuwasiliana ni “kati ya watu wapweke zaidi ulimwenguni.” Inasikitisha kwamba watu wengi sana wanakabili hali hiyo. Kwa hiyo, ikiwa ungependa kufunga ndoa siku moja, kwa nini usitatue tatizo hilo la upweke kwanza kabla ya kuanza uchumba? Ukibadili mtazamo wako na mazoea na kuchukua hatua ya kwanza ya kuwa na marafiki ukiwa bado mseja, huenda ukawa unajenga msingi imara wa ndoa yenye furaha.
Unaweza Kukabiliana na Upweke
Huenda tatizo lako la upweke lisitatuliwe mara moja. Lakini unaweza kukabiliana nalo kwa kufuata ile Kanuni Bora ambayo Yesu alitaja. Alisema: “Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Hivyo, ikiwa unataka wengine wawe wenye urafiki, basi wewe pia unapaswa kuwa mwenye urafiki. Ukitaka wengine wakufunulie yaliyo moyoni, lazima wewe uwafunulie yaliyo moyoni mwako. Huenda wengine wasiitikie mara moja, lakini baada ya muda, wataitikia. Hata wasipoitikia, utakuwa mwenye furaha kwa kuwa ulijitahidi.
Yesu alitaja kweli nyingine ambayo huenda ikakusaidia kukabiliana na upweke: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Ukitumia wakati wako kuwasaidia wengine, iwe ni kumsaidia mtoto kufanya kazi za shuleni au kumnunulia mzee vitu dukani au kumfanyia kazi za nyumbani au kumtunzia bustani, utakuwa na furaha zaidi na huenda ukapata rafiki wa kweli.
Jinsi ya Kupata Rafiki Bora
Kuna njia nyingine za kukabiliana na upweke. Usijifungie tu nyumbani. Ikiwezekana, tembea kwenye bustani au sehemu za mashambani. Ukiwa peke yako nyumbani tumia wakati huo kufanya mambo mbalimbali kama vile, kushona, kufanya kazi za nyumbani, kurekebisha vitu, au kusoma. Mtu mmoja aliandika, “Hakuna mfadhaiko ninaopata ambao hauwezi kutulizwa ninaposoma kwa saa moja.” Wengi wamepata kitulizo hasa kwa kusoma zaburi za Biblia.
Wataalamu wanasema kwamba kushirikiana na watu walio na imani moja ya kidini kunaweza kumsaidia mtu kushinda upweke na pia kuna manufaa ya afya. Unaweza kupata wapi watu wanaojitahidi kufuata ile Kanuni Bora? Katika kitabu kuhusu dini mbalimbali, mtazamaji mmoja asiyeunga mkono dini yeyote aliandika hivi: “Katika makutaniko yao, Mashahidi [wa Yehova] wanafanyiza jamii ya watu wenye kutumainiana na kuvumiliana kikweli.”
Yesu alionyesha jambo ambalo lingewatambulisha Wakristo wa kweli alipowaambia wanafunzi wake hivi: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Upendo huo—kwanza kumwelekea Mungu kisha kuwaelekea waabudu wenzao—ndio huwatambulisha wale wanaofuata dini ya kweli.—Mathayo 22:37-39.
Kusitawisha urafiki pamoja na Mungu ndio njia bora zaidi ya kukabiliana na upweke. Akiwa rafiki yako, huwezi kujihisi mpweke kamwe!—Waroma 8:38, 39; Waebrania 13:5, 6.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]
JINSI NINAVYOKABILIANA NA UPWEKE
Anny, mjane: “Mimi hujaribu kudhibiti mawazo yangu na kuwa na maoni yanayofaa kuhusu hali yangu.”
Carmen, mseja: “Nimejifunza kutokazia fikira mambo yaliyopita bali kusonga mbele na kuanzisha marafiki wapya.”
Fernande, mjane: “Ukijitahidi kuwasaidia wengine, unasahau matatizo yako.”
Jean-Pierre, mseja: “Kwa kawaida mimi hutembea kwa muda mrefu, na wakati huo ninamfungulia Mungu moyo wangu katika sala.”
Bernard, mjane: “Mimi huwasiliana kwa ukawaida na marafiki wangu kwa kuwapigia simu, si ili tukumbuke mambo yenye kuhuzunisha bali nifurahie kuwajulia hali.”
David, mseja: “Ingawa mimi hupenda faragha yangu, nimejitahidi sana kushirikiana na wengine.”
Lorenna, mseja: “Mimi huchukua hatua ya kwanza kuwafikia watu na kuanzisha urafiki.”
Abigaïl, miaka 15: “Mimi hutumia wakati mwingi pamoja na marafiki wanaonizidi umri na ninanufaika sana kutokana na uzoefu wao.”
Cherry, mseja: “Niligundua kwamba ukiwaambia watu kwamba wewe ni mpweke, wanajitahidi sana kuwa marafiki wako.”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]
NJIA ZA KUSHINDA UPWEKE
● Uwe na mtazamo unaofaa
● Punguza burudani zinazokutenga na wengine, kama vile kutazama televisheni
● Tafuta marafiki walio na viwango kama vyako kutia ndani wale ambao si wa rika lako
● Zaidi ya yote, sitawisha urafiki pamoja na Mungu
[Picha katika ukurasa wa 7]
Anzisha urafiki na watu ambao si wa rika lako
-