Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Unapenda Neno la Mungu Kadiri Gani?
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Novemba 1
    • Unapenda Neno la Mungu Kadiri Gani?

      “Sheria yako naipenda mno ajabu, ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa.”—ZABURI 119:97.

      1. Watu wenye kumcha Mungu huonyesha kwa njia gani moja kwamba wanapenda Neno la Mungu?

      MAMIA ya milioni ya wanaume na wanawake wana Biblia. Lakini kuna tofauti kati ya kuwa na Biblia na kupenda Neno la Mungu. Je, kweli mtu anaweza kudai kwamba anapenda Neno la Mungu ikiwa yeye hulisoma mara chache tu? Bila shaka la! Tofauti na hivyo, wengine ambao zamani hawakuiheshimu Biblia sasa huisoma kila siku. Wao wamejifunza kupenda Neno la Mungu, na kama mtunga-zaburi, sasa wao hulitafakari Neno la Mungu “mchana kutwa.”—Zaburi 119:97.

      2. Imani ya mmoja wa Mashahidi wa Yehova ilitegemezwaje katika hali ngumu?

      2 Nasho Dori alijifunza kupenda Neno la Mungu. Akiwa pamoja na waamini wenzake, alivumilia kwa miongo mingi akitumikia Yehova katika nchi yao ya Albania. Kwa kipindi kirefu cha muda huo, Mashahidi wa Yehova walikuwa wamepigwa marufuku, na Wakristo hao waaminifu walikuwa wakipokea fasihi chache za Biblia. Lakini imani ya Ndugu Dori ilidumu ikiwa imara. Kwa njia gani? “Lengo langu,” akasema, lilikuwa “kusoma Biblia kwa angalau muda wa saa moja kila siku, na nilifanya hivyo kwa miaka ipatayo 60 kabla ya macho yangu kudhoofika.” Hadi hivi karibuni, Biblia nzima haikuwako katika Kialbania, lakini Ndugu Dori alijifunza Kigiriki akiwa mtoto mdogo, kwa hiyo alikuwa akisoma Biblia katika Kigiriki. Kusoma Biblia kwa ukawaida kulimtegemeza Ndugu Dori katika majaribu mengi, na kunaweza kututegemeza sisi vilevile.

      “Fanyizeni Hamu Sana” ya Neno la Mungu

      3. Wakristo wanapaswa kukuza mtazamo gani kuhusu Neno la Mungu?

      3 “Kama vitoto vichanga vilivyozaliwa karibuni,” akaandika mtume Petro, “fanyizeni hamu sana ya maziwa yasiyoghushiwa yaliyo ya neno.” (1 Petro 2:2) Kama vile mtoto hutamani sana maziwa ya mamake, Wakristo ambao wanaona uhitaji wao wa kiroho wanapaswa kufurahia sana kusoma Neno la Mungu. Je, ndivyo unavyohisi? Kama sivyo, usikate tumaini. Wewe pia unaweza kufanyiza hamu sana ya Neno la Mungu.

      4. Ni nini kinachohusika ili uwe na desturi ya kusoma Biblia kila siku?

      4 Ili ufanye hivyo, kwanza jitie nidhamu ili uwe na desturi ya kusoma Biblia kwa ukawaida, kila siku ikiwezekana. (Matendo 17:11) Huenda usiweze kutumia muda wa saa moja kila siku kusoma Biblia kama Nasho Dori, lakini yaelekea sana unaweza kutenga wakati fulani kila siku ili usome Neno la Mungu. Wakristo wengi huamka dakika chache mapema kidogo ili watafakari fungu fulani la Biblia. Je, kweli kuna njia nzuri kuliko hiyo ya kuanza siku? Wengine hupendelea kumaliza siku kwa kusoma Biblia kabla tu ya kulala. Wengine nao husoma Biblia wakati mwingine unaowafaa. Jambo muhimu ni kusoma Biblia kwa ukawaida. Kisha, tafakari kwa muda mfupi yale ambayo umesoma. Ebu tuone vielelezo vya watu ambao walinufaika kutokana na kusoma Neno la Mungu na kulitafakari.

      Mtunga-Zaburi Aliyependa Sheria ya Mungu

      5, 6. Ijapokuwa huenda tusijue jina la mwandikaji wa Zaburi ya 119, twaweza kujifunza nini juu yake kwa kusoma na kutafakari mambo aliyoyaandika?

      5 Kwa hakika mwandikaji wa Zaburi ya 119 alithamini sana Neno la Mungu. Ni nani aliyeandika zaburi hiyo? Mwandikaji huyo hatajwi katika Biblia. Lakini, tunajifunza mambo fulani juu yake kutokana na muktadha, na twajua kwamba alikuwa na matatizo maishani. Baadhi ya watu aliowajua ambao walipaswa kuwa waabudu wa Yehova hawakupenda kanuni za Biblia kama yeye. Lakini, huyo mtunga-zaburi hakuruhusu mtazamo wao umzuie asifanye yaliyo sawa. (Zaburi 119:23) Ikiwa unaishi au kufanya kazi na mtu ambaye haheshimu kanuni za Biblia, unaweza kuona jinsi hali yako inavyofanana na hali ya mtunga-zaburi.

      6 Japo mtunga-zaburi alikuwa mcha Mungu, hakujiona kamwe kuwa mwadilifu. Alikiri wazi kutokamilika kwake. (Zaburi 119:5, 6, 67) Lakini, hakuruhusu dhambi imtawale. “Jinsi gani kijana aisafishe njia yake?” akauliza. Akajibu: “Kwa kutii, akilifuata neno lako.” (Zaburi 119:9) Kisha, akikazia jinsi Neno la Mungu lilivyo na nguvu za kutokeza mema, mtunga-zaburi aliongezea: “Moyoni mwangu nimeliweka neno lako, nisije nikakutenda dhambi.” (Zaburi 119:11) Nguvu iwezayo kutusaidia kuepuka kutenda dhambi dhidi ya Mungu ina uwezo kwelikweli!

      7. Kwa nini vijana wanapaswa hasa kuona uhitaji wa kusoma Biblia kila siku?

      7 Inafaa vijana Wakristo wazingatie maneno ya mtunga-zaburi. Leo vijana Wakristo wanashambuliwa. Ibilisi angependa sana kufisidi kizazi hiki kichanga cha waabudu wa Yehova. Shetani analenga kuwashawishi vijana Wakristo washindwe na tamaa za kimwili na kuvunja sheria za Mungu. Mara nyingi sinema na programu za televisheni huonyesha fikira za Ibilisi. Watu wanaohusika katika programu hizo huonekana kuwa wenye kuvutia na wenye kupendeka; mahusiano yasiyo ya kiadili kati yao hayaonwi kuwa mabaya. Twapewa ujumbe gani? ‘Si vibaya kwa watu ambao hawajafunga ndoa kufanya ngono maadamu kwa kweli wanapendana.’ Kwa kusikitisha, kila mwaka vijana kadhaa Wakristo huona mambo kwa njia hiyo. Imani za wengine huvunjika. Kwa hiyo, mkazo upo! Lakini, je, mkazo huo ni mkali sana hivi kwamba nyinyi vijana hamwezi kuushinda? La hasha! Yehova ameandaa njia ambayo vijana Wakristo wanaweza kushinda tamaa zisizofaa. Wanaweza kukinza silaha yoyote ambayo Ibilisi anaweza kubuni ‘kwa kutii, na kulifuata Neno la Mungu, na kuliweka Neno la Mungu moyoni mwao.’ Je, wewe binafsi hutumia muda gani kusoma Biblia kwa ukawaida na kuitafakari?

      8. Vielelezo ambavyo vimetajwa katika fungu hili vinaweza kukusaidiaje uzidi kuthamini Sheria ya Kimusa?

      8 Mwandikaji wa Zaburi ya 119 alikazia: “Sheria yako naipenda mno ajabu.” (Zaburi 119:97) Alimaanisha sheria gani? Alimaanisha neno la Yehova lililofunuliwa, kutia ndani Sheria ya Kimusa. Kijuujuu wengine wanaweza kupuuza hiyo kanuni ya Sheria kuwa ya kikale na kujiuliza jinsi mtu awezavyo kuipenda. Lakini, tunapotafakari sehemu mbalimbali za Sheria ya Kimusa, kama alivyofanya mtunga-zaburi, tunaweza kuona hekima iliyotokezwa na Sheria hiyo. Mbali na mambo mengi ya kiunabii ya Sheria, kuna maagizo yahusuyo usafi na ulaji, ambayo yaliendeleza usafi na afya njema. (Mambo ya Walawi 7:23, 24, 26; 11:2-8) Sheria iliwatia moyo Waisraeli wafuatie haki katika biashara na kuwahimiza wawaonyeshe hisia-mwenzi waabudu wenzao waliokuwa na uhitaji. (Kutoka 22:26, 27; 23:6; Mambo ya Walawi 19:35, 36; Kumbukumbu la Torati 24:17-21) Maamuzi ya hukumu yalipasa kufanywa bila upendeleo. (Kumbukumbu la Torati 16:19; 19:15) Kwa kadiri mwandikaji wa Zaburi 119 alivyozidi kupata ujuzi maishani, inaelekea ndivyo alivyoona jinsi wale waliotumia Sheria ya Mungu walivyofaulu, na ndivyo alivyozidi kupenda Sheria hiyo. Leo vilevile, kadiri Wakristo wapatavyo mafanikio wanapotumia kanuni za Biblia, ndivyo wao huzidi kupenda Neno la Mungu na kulithamini.

      Mwana-Mfalme Aliyekuwa na Ujasiri wa Kuwa Tofauti

      9. Mfalme Hezekia alikuza mtazamo gani kuhusu Neno la Mungu?

      9 Yaliyomo katika Zaburi ya 119 yanapatana vizuri na mambo tunayojua kuhusu Hezekia alipokuwa angali mwana-mfalme kijana. Wasomi wengine wa Biblia hudokeza kwamba Hezekia ndiye aliyeandika zaburi hii. Ingawa jambo hilo si hakika, twajua kwamba Hezekia aliheshimu sana Neno la Mungu. Kupitia mwenendo wake maishani, alionyesha kwamba alikubaliana kabisa na maneno ya Zaburi 119:97. Biblia yasema hivi juu ya Hezekia: “Alishikamana na BWANA, hakuacha kumfuata, bali alizishika amri zake BWANA alizomwamuru Musa.”—2 Wafalme 18:6.

      10. Kielelezo cha Hezekia kinatiaje moyo Wakristo ambao hawakulelewa na wazazi wenye kumcha Mungu?

      10 Ripoti zaonyesha kwamba Hezekia hakulelewa katika nyumba inayomcha Mungu. Babake, Mfalme Ahazi, alikuwa mwabudu-sanamu asiye na imani ambaye alichoma motoni angalau mmojawapo wa wana wake—ndugu halisi wa Hezekia—akiwa hai awe dhabihu kwa mungu asiye wa kweli! (2 Wafalme 16:3) Japo mfano huo mbaya, Hezekia aliweza ‘kusafisha njia yake’ kutokana na uvutano wa kipagani kwa kulifahamu Neno la Mungu.—2 Mambo ya Nyakati 29:2.

      11. Mbele ya macho ya Hezekia, mambo yalikuwaje kwa babake asiye mwaminifu?

      11 Hezekia alipokuwa akikua, alijionea jinsi babake mwenye kuabudu sanamu alivyoshughulikia mambo ya Taifa. Yuda lilikuwa limezingirwa na maadui. Resini mfalme wa Siria alikuwa amejiunga na Mfalme Peka wa Israeli kuzingira Yerusalemu. (2 Wafalme 16:5, 6) Waedomu na Wafilisti pia walikuwa wameshambulia Yuda kwa mafanikio na hata wakateka baadhi ya majiji ya Yudea. (2 Mambo ya Nyakati 28:16-19) Ahazi alishughulikiaje matatizo hayo? Badala ya kumwomba Yehova amsaidie dhidi ya Siria, Ahazi alimwendea mfalme wa Ashuru, akimhonga kwa dhahabu na fedha, kutia ndani zile alizotoa kwenye hazina ya hekalu. Lakini jambo hilo halikuletea Yuda amani ya kudumu.—2 Wafalme 16:6, 8.

      12. Hezekia angeweza kuepuka kuyarudia makosa ya babake kwa kufanya nini?

      12 Hatimaye, Ahazi akafa na Hezekia akawa mfalme akiwa na umri wa miaka 25. (2 Mambo ya Nyakati 29:1) Japo alikuwa angali kijana kwa kadiri, hiyo haikumzuia asiwe mfalme mwenye mafanikio. Badala ya kuiga mwenendo wa babake asiye mwaminifu, yeye alishikamana na Sheria ya Yehova. Hiyo ilitia ndani amri ya kipekee kwa wafalme: “[Mfalme] aketipo juu ya kiti cha ufalme wake, ajiandikie nakala ya torati hii katika chuo, kufuata hicho kilicho mbele ya makuhani Walawi; na awe nayo, asome humo siku zote atakazoishi; ili apate kujifunza kumcha BWANA, Mungu wake, ayashike maneno yote ya torati hii.” (Kumbukumbu la Torati 17:18, 19) Kwa kusoma Neno la Mungu kila siku, Hezekia angejifunza kumcha Yehova na kuepuka kuyarudia makosa ya babake ambaye hakumcha Mungu.

      13. Mkristo anawezaje kuwa na hakika kwamba kwa njia ya kiroho, kila alitendalo litafanikiwa?

      13 Si wafalme wa Israeli tu waliotiwa moyo kufikiria Neno la Mungu daima, bali pia Waisraeli wote wenye kumcha Mungu walitakiwa wafanye hivyo. Zaburi ya kwanza yafafanua mtu mwenye furaha kwelikweli kuwa yule ambaye “sheria ya BWANA ndiyo impendezayo, na sheria yake huitafakari mchana na usiku.” (Zaburi 1:1, 2) Mtunga-zaburi asema hivi juu ya mtu kama huyo: “Kila alitendalo litafanikiwa.” (Zaburi 1:3) Kwa kutofautisha, Biblia yasema hivi kumhusu mtu ambaye hana imani katika Yehova Mungu: “Yeye ni mtu wa kusitasita kuamua, asiye imara katika njia zake zote.” (Yakobo 1:8) Sisi sote twataka kuwa wenye furaha na wenye mafanikio. Kusoma Biblia kwa ukawaida na kwa njia ya maana kwaweza kuchangia furaha yetu.

      Neno la Mungu Lilimtegemeza Yesu

      14. Yesu alionyeshaje kwamba anapenda Neno la Mungu?

      14 Katika pindi moja, wazazi wa Yesu walimpata akiwa ameketi kati ya walimu katika hekalu huko Yerusalemu. Wataalamu hao wa Sheria ya Mungu “walikuwa katika mshangao wa daima [kama nini] juu ya uelewevu wake na majibu yake”! (Luka 2:46, 47) Wakati huo Yesu alikuwa na umri wa miaka 12. Ndiyo, hata alipokuwa mchanga, kwa wazi Yesu alipenda Neno la Mungu. Baadaye, Yesu alitumia Maandiko kumkemea Ibilisi, akisema: “Binadamu lazima aishi, si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.” (Mathayo 4:3-10) Punde tu baadaye, Yesu aliwahubiria wakazi wa nyumbani kwao Nazareti, akitumia Maandiko.—Luka 4:16-21.

      15. Yesu aliwekaje kielelezo alipokuwa akiwahubiria wengine?

      15 Yesu alinukuu Neno la Mungu mara nyingi ili kutegemeza mafundisho yake. Wasikilizaji wake ‘walishangaa juu ya njia yake ya kufundisha.’ (Mathayo 7:28) Na si ajabu—mafundisho ya Yesu yalitoka kwa Yehova Mungu mwenyewe! Yesu alisema: “Kile nifundishacho si changu, bali ni chake yeye aliyenituma. Yeye ambaye husema kwa ubuni wake mwenyewe anatafuta sana utukufu wake mwenyewe; bali yeye atafutaye utukufu wake aliyemtuma, huyu ni wa kweli, na hakuna ukosefu wa uadilifu katika yeye.”—Yohana 7:16, 18.

      16. Yesu alionyesha upendo wake kwa Neno la Mungu kufikia hatua gani?

      16 Tofauti na mwandikaji wa Zaburi 119, ‘hakukuwa na ukosefu wa uadilifu’ katika Yesu. Alikuwa Mwana wa Mungu asiye na dhambi ambaye “alijinyenyekeza mwenyewe akawa mtiifu hadi kifo.” (Wafilipi 2:8; Waebrania 7:26) Lakini, japo alikuwa mkamilifu, Yesu alijifunza Sheria ya Mungu na kuitii. Hilo lilikuwa jambo kuu lililomwezesha kudumisha uaminifu wake wa maadili. Petro alipotumia upanga kujaribu kuzuia Bwana-Mkubwa wake asikamatwe, Yesu alimkemea mtume huyo na kuuliza: “Wafikiri kwamba siwezi kuomba Baba yangu anipe mimi katika dakika hii malejioni zaidi ya kumi na mawili ya malaika? Katika kisa hicho, Maandiko yangetimizwaje kwamba lazima itendeke kwa njia hii?” (Mathayo 26:53, 54) Naam, utimizo wa Maandiko ulikuwa muhimu zaidi kwa Yesu kuliko kuepuka kifo kikatili na chenye kufedhehesha sana. Huo ni wonyesho wenye kutokeza kama nini wa kupenda Neno la Mungu!

      Waigaji Wengine wa Kristo

      17. Neno la Mungu lilikuwa muhimu kadiri gani kwa mtume Paulo?

      17 Mtume Paulo aliwaandikia Wakristo wenzake hivi: “Iweni waigaji wangu, kama vile mimi nilivyo mwigaji wa Kristo.” (1 Wakorintho 11:1) Kama Bwana-Mkubwa wake, Paulo alikuza upendo kwa Maandiko. Alikiri hivi: “Ndani kabisa katika moyo wangu naifurahia sheria ya Mungu.” (Waroma 7:22, Biblia Habari Njema) Paulo alinukuu Neno la Mungu mara nyingi. (Matendo 13:32-41; 17:2, 3; 28:23) Paulo alipompa Timotheo, mhudumu mwenzake mpendwa, maagizo ya mwisho, alikazia fungu muhimu ambalo Neno la Mungu lapaswa kutimiza katika maisha ya kila siku ya kila “mtu wa Mungu.”—2 Timotheo 3:15-17.

      18. Taja kielelezo cha mtu ambaye alistahi Neno la Mungu katika nyakati hizi.

      18 Watumishi wengi waaminifu wa Yehova katika nyakati hizi vilevile wameiga jinsi Yesu alivyopenda Neno la Mungu. Mapema katika karne hii, kijana mmoja alipokea Biblia kutoka kwa rafikiye mmoja. Kijana huyo akaeleza matokeo ya zawadi hiyo aliyoithamini: “Nikaazimia maishani kusoma sehemu fulani ya Biblia kila siku.” Kijana huyo ni Frederick Franz, na upendo wake kwa Biblia ulifanya afurahie maisha marefu na yenye mafanikio katika utumishi wa Yehova. Yeye anakumbukwa kwa upendo kuwa mwenye uwezo wa kunukuu sura nzima-nzima za Biblia kutoka akilini.

      19. Wengine huweka ratiba gani ya kusoma Biblia kila juma kwa ajili ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi?

      19 Mashahidi wa Yehova hukazia sana kusoma Biblia kwa ukawaida. Kila juma, wanapotayarisha mojawapo ya mikutano yao ya Kikristo, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, wao husoma sura kadhaa za Biblia. Mambo makuu ya sehemu wanayosoma katika usomaji wa Biblia huzungumziwa kwenye mkutano huo. Mashahidi wengine hupendelea kugawanya usomaji wa Biblia wa juma katika sehemu saba ndogondogo na kusoma sehemu moja kila siku. Wasomapo, wao hutafakari habari hiyo. Inapowezekana, wao hufanya utafiti wa ziada wakitumia vichapo vinavyotegemea Biblia.

      20. Ni nini kinachohitajika ili kupata wakati wa kusoma Biblia kwa ukawaida?

      20 Huenda ukahitaji ‘kununua wakati’ kutoka kwenye utendaji mwingine ili usome Biblia kwa ukawaida. (Waefeso 5:16) Na utapata manufaa nyingi kushinda dhabihu zozote utakazofanya. Kadiri ukuzavyo tabia ya kusoma Biblia kila siku, ndivyo utakavyozidi kupenda Neno la Mungu. Muda usio mrefu, utasukumwa kusema kama mtunga-zaburi: “Sheria yako naipenda mno ajabu, ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa.” (Zaburi 119:97) Mtazamo kama huo unanufaisha sana sasa na katika wakati ujao, kama makala ifuatayo itakavyoonyesha.

  • Manufaa za Kupenda Neno la Mungu
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Novemba 1
    • Manufaa za Kupenda Neno la Mungu

      ‘Uipende hekima, nayo itakulinda. Itakupatia heshima, ukiikumbatia.’ —MITHALI 4:6, 8.

      1. Kupenda Neno la Mungu kwelikweli kwahusisha nini?

      NI MUHIMU kwa Mkristo kusoma Biblia. Lakini, kuisoma tu hakuonyeshi kwamba mtu anapenda Neno la Mungu. Namna gani kama mtu husoma Biblia lakini hutenda mambo ambayo Biblia inashutumu? Kwa wazi mtu huyo hapendi Neno la Mungu kama vile mwandikaji wa Zaburi 119 alivyolipenda. Kupenda Neno la Mungu kulimfanya aishi kupatana na matakwa yake.—Zaburi 119:97, 101, 105.

      2. Ni manufaa zipi zinazotokana na hekima inayotegemea Neno la Mungu?

      2 Kuishi kwa kupatana na Neno la Mungu kwahitaji urekebishe daima fikira zako na maisha yako. Kufanya hivyo kwaonyesha hekima ya kimungu, ambayo inamaanisha kutumia maishani ujuzi na ufahamu unaopatikana kwa kujifunza Biblia. ‘Uipende hekima, nayo itakulinda. Uitukuze, nayo itakukuza; itakupatia heshima, ukiikumbatia. Itakupa neema kuwa kilemba kichwani; na kukukirimia taji ya uzuri.’ (Mithali 4:6, 8, 9) Hicho ni kitia moyo kizuri kama nini cha kukuza upendo kwa Neno la Mungu na kuongozwa nalo! Ni nani asiyetaka kulindwa, kukuzwa, na kupewa heshima?

      Kulindwa Dhidi ya Madhara ya Kudumu

      3. Kwa nini Wakristo wanahitaji kulindwa wakati huu kuliko wakati mwingine wowote, na walindwe dhidi ya nani?

      3 Mtu hulindwaje na hekima inayopatikana kwa kujifunza Neno la Mungu na kulitumia? Kwanza, analindwa dhidi ya Shetani Ibilisi. Yesu alifundisha wafuasi wake wasali ili wakombolewe kutokana na yule mwovu, Shetani. (Mathayo 6:13) Ni muhimu sana leo kutaja ombi hili katika sala zetu. Shetani na roho wake waovu walitupwa kutoka mbinguni kufuatia mwaka wa 1914, na sasa Shetani ana “hasira kubwa, akijua ana kipindi kifupi cha wakati.” (Ufunuo 12:9, 10, 12) Katika wakati huu wa mwisho, ni lazima ana hasira kali sana anapojaribu bila mafanikio kupiga vita dhidi ya wale “washikao amri za Mungu na walio na kazi ya kutoa ushahidi kuhusu Yesu.”—Ufunuo 12:17.

      4. Wakristo hulindwaje dhidi ya misongo na mitego ya Shetani?

      4 Akiwa na hasira ya kisasi, Shetani anaendelea kuwasababishia matatizo wahudumu hawa Wakristo na kuchochea mnyanyaso mkali au kuwawekea vikwazo vingine katika utendaji wao. Pia anataka kuwashawishi watangazaji wa Ufalme wazingatie mambo kama umashuhuri wa kilimwengu, kupenda anasa, kupata mali, kufuatia maisha ya raha, badala ya kuzingatia kazi ya kuhubiri Ufalme. Ni nini ambacho hulinda watumishi waaminifu wa Mungu wasishindwe na mkazo wa Shetani au wasinaswe na mitego yake? Bila shaka, sala, uhusiano wa karibu na wa kibinafsi pamoja na Yehova, na imani ya kwamba ahadi zake ni za hakika ni mambo muhimu sana. Lakini hayo yote yanahusiana na ujuzi wa Neno la Mungu na azimio la kutii vikumbusha vyake. Vikumbusha hivyo hupatikana kwa kusoma Biblia na vichapo vinavyotusaidia kujifunza Biblia, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, kutii shauri la Kimaandiko linalotolewa na mwamini mwenzetu, au kutafakari tu kwa njia ya sala kanuni za Biblia ambazo roho ya Mungu hutukumbusha.—Isaya 30:21; Yohana 14:26; 1 Yohana 2:15-17.

      5. Hekima inayotegemea Neno la Mungu hutulinda kwa njia zipi?

      5 Wale wapendao Neno la Mungu hulindwa kwa njia nyinginezo. Kwa mfano, wao huepuka mkazo wa kihisia-moyo na maradhi ambayo husababishwa na mambo kama matumizi ya dawa za kulevya, matumizi ya tumbaku, na ukosefu wa adili kingono. (1 Wakorintho 5:11; 2 Wakorintho 7:1) Hawachochei mahusiano mabaya kwa kupiga porojo au kwa usemi usiofaa. (Waefeso 4:31) Wala hao si watu wenye kutilia shaka kwa kuchunguza sana falsafa zenye udanganyifu za hekima ya ulimwengu. (1 Wakorintho 3:19) Kwa kupenda Neno la Mungu, wao hulindwa dhidi ya mambo ambayo yangeweza kuharibu uhusiano wao na Mungu na tumaini la uhai udumuo milele. Wao wana shughuli za kuwasaidia majirani wao waweke imani katika ahadi nzuri ajabu zilizo katika Biblia, wakijua kwamba kwa kufanya hivyo ‘watajiokoa wao wenyewe na wale wawasikilizao pia.’—1 Timotheo 4:16.

      6. Hekima inayotegemea Neno la Mungu inaweza kutulindaje hata katika hali zilizo ngumu?

      6 Ni kweli kwamba kila mtu—hata wale wanaopenda Neno la Mungu—anaweza kupatwa na “wakati na tukio lisilotazamiwa.” (Mhubiri 9:11, linganisha NW.) Ni jambo lisiloepukika kwamba wengine miongoni mwetu watapatwa na misiba ya asili, magonjwa mabaya, aksidenti, au vifo vya mapema. Lakini bado tumelindwa. Hakuna msiba uwezao kusababisha madhara yenye kudumu kwa mtu ambaye kweli anapenda Neno la Mungu. Kwa hiyo, tusihangaikie kupita kiasi mambo yawezayo kutokea wakati ujao. Baada ya kuchukua tahadhari zote zinazofaa, ni afadhali kuacha mambo mikononi mwa Yehova bila kuruhusu ukosefu wa usalama maishani utuondolee amani. (Mathayo 6:33, 34; Wafilipi 4:6, 7) Kumbuka uhakika wa tumaini la ufufuo na wa maisha bora wakati Mungu ‘anapofanya vitu vyote kuwa vipya.’—Ufunuo 21:5; Yohana 11:25.

      Jithibitishe Kuwa “Udongo Mzuri”

      7. Yesu aliutolea kielezi gani umati uliokuja kumsikiliza?

      7 Umuhimu wa kuwa na maoni yanayofaa kuhusu Neno la Mungu ulikaziwa katika mmojawapo wa mifano ya Yesu. Yesu alipokuwa akitangaza habari njema kotekote katika Palestina, umati wa watu ulikuwa ukikusanyika kumsikiliza. (Luka 8:1, 4) Lakini si wote ambao kweli walilipenda Neno la Mungu. Yaelekea wengine walikuja kumsikiliza kwa sababu walitaka kuona miujiza au kwa sababu walifurahia njia yake nzuri ajabu ya kufundisha. Kwa hiyo, Yesu alitolea umati huo kielezi hiki: “Mpanzi alitoka kwenda kupanda mbegu yake. Basi, alipokuwa akipanda, baadhi ya hizo zikaanguka kando ya barabara zikakanyagwa-kanyagwa, na ndege wa mbinguni wakazila kabisa. Nyinginezo zikaanguka juu ya tungamo-mwamba, na, baada ya kuota, zikakauka kabisa kwa sababu ya kutokuwa na unyevunyevu. Nyinginezo zikaanguka katikati ya miiba, na miiba iliyokua pamoja nazo ikazisonga. Nyinginezo zikaanguka juu ya udongo mzuri, na, baada ya kuota, zikatokeza matunda mara mia.”—Luka 8:5-8.

      8. Katika kielezi cha Yesu, mbegu ni nini?

      8 Mfano wa Yesu ulionyesha kwamba watu wangeitikia kuhubiriwa kwa habari njema kwa njia tofauti-tofauti, ikitegemea hali ya moyo ya mwenye kusikiliza. Mbegu inayopandwa ni “neno la Mungu.” (Luka 8:11) Au, kama vile rekodi nyingine ya mfano huo isemavyo, mbegu ni “neno la ufalme.” (Mathayo 13:19) Yesu angeweza kutumia yoyote kati ya maneno hayo, kwa kuwa kichwa kikuu cha Neno la Mungu ni Ufalme wa kimbingu chini ya Yesu Kristo akiwa Mfalme, na kupitia huo Yehova atatetea enzi yake kuu na kulitakasa jina lake. (Mathayo 6:9, 10) Basi, mbegu ni ujumbe wa habari njema ulio katika Neno la Mungu, Biblia. Mashahidi wa Yehova hukazia ujumbe huu wa Ufalme wanapopanda mbegu kwa kumwiga Mpanzi wa awali, Yesu Kristo. Wanapata itikio gani?

      9. Ni nini kinachofananishwa na mbegu inayoanguka (a) kando ya barabara? (b) kwenye tungamo-mwamba? (c) kwenye udongo wenye miiba?

      9 Yesu alisema kwamba mbegu fulani inaanguka kando ya barabara na kukanyagwa-kanyagwa. Hiyo yarejezea watu ambao wana shughuli nyingi mno hivi kwamba mbegu ya Ufalme haiwezi kuota mizizi katika mioyo yao. Kabla hawajaweza kukuza upendo kwa Neno la Mungu, “Ibilisi huja na kuliondoa lile neno kutoka mioyoni mwao ili wasipate kuamini waokolewe.” (Luka 8:12) Mbegu nyingine inaanguka kwenye tungamo-mwamba. Hiyo yarejezea watu ambao wanavutiwa na ujumbe wa Biblia lakini hawaachi ujumbe huo uguse mioyo yao. Upinzani utokeapo au wanapopata ugumu wa kutumia shauri la Biblia, “wao huanguka” kwa sababu hawana mizizi. (Luka 8:13) Kisha kuna wale ambao husikia neno hilo lakini wanashindwa na “mahangaiko na mali na raha za maisha haya.” Hatimaye, kama mimea iliyoko katikati ya miiba, “wao husongwa kabisa.”—Luka 8:14.

      10, 11. (a) Ni nani wanaofananishwa na udongo mzuri? (b) Ni lazima tufanye nini ili ‘tulihifadhi’ Neno la Mungu mioyoni mwetu?

      10 Hatimaye, kuna mbegu inayoanguka kwenye udongo mzuri. Hiyo yaonyesha watu ambao wanapokea ujumbe kwa “moyo ulio bora na mwema.” Bila shaka kila mmoja wetu angependa kuwa katika kikundi hiki. Lakini, jambo muhimu hatimaye ni maoni ya Mungu. (Mithali 17:3; 1 Wakorintho 4:4, 5) Neno lake lasema kwamba twathibitisha kwamba tuna “moyo ulio bora na mwema” kwa matendo yetu tokea sasa hadi kifo chetu au hadi wakati Mungu atakapomaliza mfumo huu mwovu wa mambo. Ni jambo zuri ikiwa twaitikia ujumbe wa Ufalme ifaavyo kwa mara ya kwanza. Lakini, wale ambao wana moyo ulio bora na mwema hukubali Neno la Mungu na ‘kulihifadhi na kuzaa matunda kwa uvumilivu.’—Luka 8:15.

      11 Njia ya pekee iliyo hakika ya kudumisha Neno la Mungu moyoni mwetu ni kulisoma na kujifunza kwa faragha na vilevile kwa kushirikiana na waamini wenzetu. Hiyo yatia ndani kutumia vizuri chakula cha kiroho kinachoandaliwa kupitia njia iliyowekwa ya kushughulikia mahitaji ya kiroho ya wafuasi wa kweli wa Yesu. (Mathayo 24:45-47) Kwa njia hiyo, wale wanaohifadhi Neno la Mungu mioyoni mwao huchochewa na upendo “kuzaa matunda kwa uvumilivu.”

      12. Ni lazima tuzae matunda gani kwa uvumilivu?

      12 Udongo mzuri huzaa matunda gani? Kwa kawaida, mbegu huota na kuwa mimea ambayo huzaa matunda yenye mbegu kama ile ya awali, ambayo nayo inaweza kutawanywa ili kuzaa matunda mengine. Vivyo hivyo, mbegu ya neno hukua ndani ya wale ambao wana moyo ulio bora na mwema, ikifanya wafanye maendeleo ya kiroho kufikia hatua ambapo wao nao wanaweza kupanda mbegu katika mioyo ya wengine. (Mathayo 28:19, 20) Na wanafanya kazi yao ya kupanda mbegu kwa uvumilivu. Yesu alionyesha umuhimu wa uvumilivu katika kupanda aliposema: “Yeye ambaye amevumilia hadi mwisho ndiye atakayeokolewa. Na habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:13, 14.

      “Kuzaa Matunda Katika Kila Kazi Njema”

      13. Paulo alitoa sala gani ambayo ililinganisha matunda na ujuzi wa Neno la Mungu?

      13 Mtume Paulo pia alizungumzia uhitaji wa kuzaa matunda, na alihusianisha kuzaa matunda na Neno la Mungu. Alisali kwamba waamini wenzake ‘wapate kujazwa ujuzi sahihi wa mapenzi ya Mungu katika hekima yote na ufahamivu wa kiroho, kusudi watembee kwa kumstahili Yehova kwa madhumuni ya kumpendeza yeye kikamili wanapoendelea kuzaa matunda katika kila kazi njema.’—Wakolosai 1:9, 10; Wafilipi 1:9-11.

      14-16. Kwa kupatana na sala ya Paulo, ni matunda gani yanayotokezwa na wale ambao wanapenda Neno la Mungu?

      14 Basi Paulo aonyesha kwamba haitoshi tu kupata ujuzi wa Biblia. Badala yake, kupenda Neno la Mungu hutuchochea ‘tutembee kwa kumstahili Yehova’ kwa kuendelea “kuzaa matunda katika kila kazi njema.” Kazi gani njema? Kuhubiri habari njema ya Ufalme ni mgawo mkubwa sana kwa Wakristo katika hizi siku za mwisho. (Marko 13:10) Na zaidi, wale wanaopenda Neno la Mungu hufanya kadiri wawezavyo ili kutegemeza kifedha kazi hii kwa ukawaida. Wao hufurahia pendeleo hilo, wakijua kwamba “Mungu hupenda mpaji mchangamfu.” (2 Wakorintho 9:7) Michango yao hulipia gharama za kuendesha Betheli zaidi ya mia moja ambako utendaji wa kuhubiri Ufalme huongozwa, na baadhi ya Betheli hizo huchapisha Biblia na vichapo vya Biblia. Pia michango yao husaidia kulipia gharama za mikusanyiko mikubwa ya Kikristo na za kutuma waangalizi wasafirio, mishonari, na waeneza-evanjeli wengine wa wakati wote.

      15 Kazi nyinginezo njema pia zinahusisha kujenga na kutunza sehemu za ibada ya kweli. Kupenda Neno la Mungu huwachochea waabudu wake wahakikishe kwamba Majumba ya Kusanyiko na Majumba ya Ufalme hayapuuzwi. (Linganisha Nehemia 10:39.) Kwa kuwa jina la Mungu huonekana katika sehemu za mbele za majengo hayo, ni muhimu kwamba yadumishwe yakiwa safi na yenye kuvutia ndani na nje, na kwamba mwenendo wa wale wanaoabudu ndani ya majumba hayo usiwe wenye kushutumiwa. (2 Wakorintho 6:3) Wakristo wengine wanaweza kufanya mengi zaidi. Kupenda Neno la Mungu huwachochea kusafiri mbali ili kushiriki katika kujenga sehemu mpya za ibada katika maeneo ya ulimwengu ambayo yana uhitaji kwa sababu ya umaskini au ukosefu wa ustadi.—2 Wakorintho 8:14.

      16 “Kuzaa matunda katika kila kazi njema” pia kwahusisha kutimiza wajibu wa familia na kuwahangaikia Wakristo wenzetu. Kupenda Neno la Mungu hutuchochea kutambua haraka mahitaji ya wale ambao “katika imani ni jamaa zetu” na “kuzoea ujitoaji-kimungu kwa watu wa nyumbani [mwetu] wenyewe.” (Wagalatia 6:10; 1 Timotheo 5:4, 8) Basi, ni kazi njema kuzuru wagonjwa na kuwafariji wenye kuomboleza. Na ni kazi njema kama nini inayotimizwa na wazee wa kutaniko na Halmashauri za Uhusiano na Hospitali kwa kuwasaidia watu wanaokabili hali ngumu za kitiba! (Matendo 15:29) Misiba nayo inaongezeka—baadhi yake ni ya asili na mingine husababishwa na upumbavu wa mwanadamu. Kwa msaada wa roho ya Mungu, Mashahidi wa Yehova wana sifa nzuri katika sehemu nyingi za dunia kutokana na kuandaa msaada wa haraka kwa waamini wenzao na wengine wanaopatwa na misiba na aksidenti. Yote hayo ni matunda mema yanayodhihirishwa na wale wanaopenda Neno la Mungu.

      Manufaa Tukufu za Wakati Ujao

      17, 18. (a) Ni nini kinachotimizwa kwa kupanda mbegu ya Ufalme? (b) Ni matukio gani makubwa sana ambayo wapendao Neno la Mungu watashuhudia karibuni?

      17 Kupanda mbegu za Ufalme kwaendelea kuwanufaisha sana wanadamu. Katika miaka ya karibuni, zaidi ya watu 300,000 kila mwaka wameruhusu ujumbe wa Biblia kuota mizizi katika mioyo yao kwa kadiri ya kwamba wameweka wakfu maisha zao kwa Yehova na kuonyesha wakfu huo kwa ubatizo wa maji. Wanatarajia wakati ujao mtukufu kama nini!

      18 Wapendao Neno la Mungu wanajua kwamba karibuni Yehova Mungu atachukua hatua ya kutukuza jina lake. “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli, itaangamizwa. (Ufunuo 18:2, 8) Kisha, Mfalme Yesu Kristo atawaangamiza wale wanaokataa kuishi kwa kupatana na Neno la Mungu. (Zaburi 2:9-11; Danieli 2:44) Baadaye, Ufalme wa Mungu utaleta kitulizo cha kudumu kutokana na uhalifu, vita, na misiba mingine. Hakutakuwa tena na uhitaji wa kufariji watu kwa sababu ya maumivu, magonjwa, na kifo.—Ufunuo 21:3, 4.

      19, 20. Ni wakati gani ujao mtukufu unaotarajiwa na wale ambao kwa kweli wanapenda Neno la Mungu?

      19 Wale wapendao Neno la Mungu watatimiza kazi njema tukufu kama nini! Waokokaji wa Har–Magedoni wataanza kazi yenye kufurahisha ya kugeuza dunia hii iwe paradiso. Watakuwa na pendeleo lenye kusisimua la kufanya matayarisho kwa ajili ya mahitaji ya wanadamu waliokufa ambao sasa wanapumzika katika makaburi na ambao wako katika kumbukumbu ya Mungu kwa matazamio ya kufufuliwa katika ufufuo wa wafu. (Yohana 5:28, 29) Wakati huo, Mwenye Enzi Kuu, Yehova, atawapa wakazi wa dunia mwongozo mkamilifu kupitia Mwana wake aliyekwezwa, Yesu Kristo. ‘Hati-kunjo zitafunguliwa,’ zikionyesha maagizo ya Yehova kwa ajili ya maisha katika ulimwengu mpya.—Ufunuo 20:12.

      20 Katika wakati ufaao wa Yehova, Wakristo wote watiwa mafuta walio waaminifu watafufuliwa wapate zawadi yao ya kimbingu wakiwa “warithi-washirika pamoja na Kristo.” (Waroma 8:17) Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo, wanadamu wote walio duniani ambao wanapenda Neno la Mungu watainuliwa wawe wakamilifu kiakili na kimwili. Baada ya kujithibitisha kuwa waaminifu katika jaribu la mwisho, wanadamu hao watathawabishwa kwa uhai udumuo milele nao watafurahia “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Waroma 8:21; Ufunuo 20:1-3, 7-10) Huo utakuwa wakati mzuri kama nini! Kwa kweli, iwe Yehova ametupa tumaini la kimbingu au tumaini la kidunia, upendo wenye uvumilivu kwa Neno lake na azimio la kuishi kwa kupatana na hekima ya kimungu zitatulinda sasa. Na katika wakati ujao ‘zitatukuza kwa sababu tunazikumbatia.’—Mithali 4:6, 8.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki