-
Tamaa ya KupendwaAmkeni!—2006 | Machi
-
-
Tamaa ya Kupendwa
Hapo zamani za kale katika jiji ambalo leo ni sehemu fulani ya nchi ya Uturuki kulikuwa na msichana aliyeitwa Lea. Lea hakuwa mrembo, lakini dada yake mdogo Raheli alikuwa mrembo.
RAHELI alikutana na mwanamume aliyempenda sana hivi kwamba alikubali kumfanyia baba yake kazi kwa miaka saba ili amwoe. Hata hivyo, usiku wa harusi, baba ya wasichana hao alimwoza Lea badala ya dada yake. Hatujui Lea alihisije kuhusu njama ya baba yake, lakini lazima awe alijua kwamba hiyo haikuwa njia nzuri ya kuanza maisha ya ndoa.
Alipogundua kilichotokea, bwana harusi aliteta. Baba alimweleza kwamba ilikuwa desturi yao kumwoza kwanza msichana mkubwa. Baadaye mwanamume huyo alimwoa pia yule msichana mdogo. Hivyo, Lea alijikuta ameolewa kwa hila na mwanamume ambaye alimpenda dada yake mdogo. Lazima Lea awe alihuzunika sana kuona dada yake akipendwa zaidi! Lea hakuwa na uchumba wenye upendo naye alikuwa na kumbukumbu chache tu zenye kufurahisha kuhusu siku ya harusi yake. Lazima awe alitamani kupendwa kama Raheli! Kwa hiyo, kwa sababu ya hali ambazo hangeweza kuzuia, huenda mara nyingi Lea alijihisi kuwa hapendwi wala hatakikani.a
Kwa kiasi fulani, watu wengi leo wanaweza kuelewa hali ya Lea. Sote tunahitaji kupenda na kupendwa. Labda tunatamani kupata mwenzi atakayetupenda. Tunataka pia kupendwa na wazazi wetu, watoto wetu, ndugu na dada zetu, na marafiki. Kama vile Lea, huenda tukaona wengine wakipendwa hali sisi hatupendwi.
Tangu utotoni sisi husikia hadithi za mahaba kuhusu watu wenye kuvutia ambao hupendana na kuishi raha mustarehe. Waimbaji huimba kwa hisia nyingi kuhusu upendo; washairi husifu upendo. Hata hivyo, mtafiti mmoja aliandika hivi kuhusu upendo: “Hakuna shughuli au utendaji wowote ambao huanzishwa mtu akiwa na matumaini na matarajio makubwa kama upendo. Hata hivyo, mara nyingi sana upendo hushindwa kufaulu.” Kwa kweli, mara nyingi mahusiano yetu ya karibu ndiyo hufanya mioyo yetu ishuke na kutuhuzunisha badala ya kutuletea shangwe ya kudumu. Katika nchi kadhaa, asilimia 40 hivi ya watu wote waliofunga ndoa hutalikiana, na wenzi wengi wa ndoa ambao hawajatalikiana hawana furaha.
Katika nchi nyingi, idadi ya familia zenye matatizo na zile zenye mzazi mmoja ambapo watoto pia wameathiriwa imeongezeka. Hata hivyo, watoto hasa wanahitaji kuwa katika familia yenye kujali na yenye upendo. Hivyo basi, kwa nini watu hawapendani? Tunaweza kupata wapi habari kuhusu sifa hiyo yenye thamani? Makala zinazofuata zitajibu maswali hayo.
[Maelezo ya Chini]
a Simulizi hili linapatikana katika sura ya 29 na ya 30 ya kitabu cha Biblia cha Mwanzo.
-
-
Kwa Nini Ni Vigumu Kupata Upendo wa Kweli?Amkeni!—2006 | Machi
-
-
Kwa Nini Ni Vigumu Kupata Upendo wa Kweli?
Kuna mashauri chungu nzima kuhusu upendo wa kimahaba. Madaktari na washauri hutoa mwongozo. Mara nyingi kunakuwa na mijadala kuhusu habari hiyo kwenye televisheni au redio.
VITUO vingi vya Intaneti hudai kwamba vinatoa maagizo kuhusu jinsi ya kupata upendo. Huenda ukaambiwa kwamba utagundua “siri zenye kustaajabisha” na utajifunza kutoka kwa “wataalamu wa kutafutia watu wachumba,” “wataalamu wa mahusiano,” “madaktari wa upendo,” na vilevile kutoka kwa wataalamu wa akili, wanasaikolojia, na wanajimu.
Watu hununua sana vitabu na magazeti ambayo huzungumzia upendo, na baadhi yake hutoa ahadi zilizotiwa chumvi. Kwa mfano, kitabu kimoja kinadai kuwa kinaweza kukuonyesha “jinsi ya kumfanya mtu yeyote akupende.” Kitabu kingine husema kinaweza kukuonyesha jinsi ya kupata “mwenzi bora zaidi katika mwezi mmoja tu.” Kwa wale wanaohisi kuwa mwezi mmoja ni muda mrefu sana, kuna kitabu kinachofunua jinsi ambavyo katika muda “usiozidi dakika 90,” unaweza kumfanya mtu akupende milele.
Mashauri mengi hugharimu. Nao watu wengi hulipa katika njia mbili. Wao hutoa pesa kupata mashauri. Kisha, mwongozo huo unapokuwa na kasoro, na mara nyingi huwa nayo, watu hao huumia kihisia.
Hata hivyo, kuna chanzo kimoja cha mashauri ambacho mashauri yake hufaulu yanapofuatwa. Isitoshe, kinazungumzia habari hiyo kwa unyoofu bila kutoa madai yenye kusisimua yasiyo na msingi na ahadi zisizoweza kutimizwa. Ingawa kiliandikwa zamani sana, mashauri yake hayajapitwa na wakati. Mtungaji wake ana hekima na upendo usio na kifani. Huenda tayari una zawadi hii ya pekee, yaani, Biblia Takatifu. Haidhuru hali au malezi yetu, Biblia hutufundisha yale tunayohitaji kujua kuhusu upendo. Na mashauri yake hayatozwi.
Je, Biblia inaweza kutusaidia tuwe na uhusiano mzuri na kila mtu? La. Watu fulani hawawezi kuwa rafiki zetu hata tujitahidi kadiri gani. Nao upendo wa kweli hauwezi kulazimishwa. (Wimbo wa Sulemani 8:4) Hata hivyo, tukifuata mwongozo wa Biblia, itakuwa rahisi zaidi kusitawisha mahusiano yenye upendo, ingawa huenda hilo likahitaji wakati na jitihada nyingi. Jambo hilo litazungumziwa katika makala inayofuata. Lakini kwanza fikiria sababu inayofanya iwe vigumu zaidi kupata upendo wa kweli siku hizi.
Upendo “Utapoa”
Katika unabii wake wenye mambo mengi kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu alitabiri kwa usahihi kuhusu hali na maelekeo ya watu katika siku zetu. Alisema kwamba kungekuwa na uasi-sheria na vita, mambo yaliyo kinyume cha upendo! Alisema pia kwamba ‘watu wengi . . . watasalitiana na kuchukiana’ na kwamba “upendo wa walio wengi zaidi utapoa.” (Mathayo 24:3-12) Je, hukubali kwamba upendo wa wengi umepoa, na kwamba upendo wa kweli unakosekana hata katika familia?
Kuongezea maneno ya Yesu, mtume Paulo alifafanua kwa njia ya wazi zaidi tabia za watu katika “siku za mwisho.” Aliandika kwamba watu wangekuwa “wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.” (2 Timotheo 3:1-4) Katika nchi nyingi tabia hizo zimekuwa za kawaida.
Fikiria maswali haya: Je, wewe huvutiwa na watu wenye kiburi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, ambao wanaweza kukuchongea au kukusaliti? Je, wewe huvutiwa na watu wanaojipenda wenyewe, wanaopenda pesa, au wanaopenda raha? Kwa kuwa watu wenye ubinafsi huruhusu pupa na mapendezi yao wenyewe yaongoze mahusiano yao, huenda wakapendezwa na watu wengine kwa sababu za kibinafsi. Kwa hekima, Maandiko hushauri hivi: “Geukia mbali kutoka kwa hao.”—2 Timotheo 3:5.
Pia ona kwamba Paulo anasema kuwa katika siku za mwisho watu watakuwa “wasio na upendo wa asili,” au kama tafsiri nyingine inavyosema, “hawatakuwa na upendo wa kawaida kwa familia zao.” Kwa kuhuzunisha, watoto wengi wanakua katika familia kama hizo. Mara nyingi, watoto hao hujifunza kuhusu upendo kutoka kwenye vyombo vya habari. Lakini je, vyombo vya habari huwafundisha mambo sahihi kuhusu upendo ambao utawasaidia kuwa na mahusiano mazuri zaidi?
Je, Ni Upendo wa Kuwaziwa au Ni Upendo Halisi?
Kwa kiwango fulani, sisi sote tunaathiriwa na vyombo vya habari. Mtafiti mmoja aliandika hivi: “Tangu utotoni, sisi hupata habari chungu nzima kuhusu hadithi za kuwaziwa na maoni yaliyokita mizizi kuhusu ngono, upendo, na mahusiano ya kimahaba katika sinema na televisheni, vitabu na magazeti, redio na muziki, matangazo ya kibiashara, na hata kwenye habari.” Pia alieleza hivi: “Mambo ambayo vyombo vingi vya habari huonyesha kuhusu ngono, upendo, na mahusiano ya kimahaba hufanya tuwe na matarajio yasiyoweza kutimia ambayo huwa vigumu kuyaondoa akilini kabisa. Mambo hayo hufanya tusitosheke na wenzi wetu wala tusiridhike na jinsi tulivyo.”
Mara nyingi vitabu, sinema, na nyimbo hazielezi upendo kwa usahihi kwani lengo la vyombo vya habari si kuelimisha bali ni kutumbuiza. Kwa hiyo, waandikaji hutunga hali za kuwaziwa na hadithi za mahaba ambazo zitawaletea pesa nyingi. Hata hivyo, kwa kusikitisha, si rahisi kutofautisha kati ya mambo halisi na yale ya kuwaziwa. Kwa hiyo, mara nyingi watu hutamauka mahusiano yao yasipokuwa kama yale ya watu wanaosimuliwa katika hadithi za kuwaziwa. Hivyo, tunawezaje kutofautisha kati ya hadithi za kuwaziwa na mambo halisi, kati ya upendo wa kimahaba unaoonyeshwa katika vyombo vya habari na upendo wa kweli? Fikiria tofauti zifuatazo.
Tofauti Kati ya Upendo wa Kuwaziwa na Upendo wa Kweli
Iwe ni katika vitabu, sinema, au michezo ya kuigiza, hadithi za mahaba zinaweza kutofautiana, lakini mambo ya msingi hayatofautiani. Gazeti Writer linasema hivi: “Hadithi nyingi za mahaba hazitofautiani. Na kuna sababu nzuri. Hadithi ifuatayo hupendwa sana na watu: Mvulana fulani akutana na msichana, kisha mvulana anampoteza msichana huyo halafu mvulana anampata tena msichana huyo. Hadithi hiyo huwavutia watu haidhuru imesimuliwa lini, wapi na mara ngapi.” Na tuchunguze kwa uangalifu hadithi hiyo inayopendwa sana.
Mvulana fulani akutana na msichana: Mwana wa mfalme mwenye kuvutia anakutana na mwanamke mrembo, nao wanapendana. Mwandishi mmoja mwenye mafanikio anawashauri hivi wale wanaotaka kuwa waandishi wa riwaya za mahaba: “Lazima msomaji wako aone kwamba watu hao wawili walipendana mara tu walipokutana kwa mara ya kwanza.”
Wazo la kwamba watu wanaweza kupendana wanapokutana tu mara ya kwanza huwafanya watu wafikiri kwamba upendo wa kweli ni hisia tu, hisia yenye nguvu sana ambayo hukulemea unapokutana na mtu wa pekee, na kwamba upendo wa aina hiyo hutukia ghafula pasipo jitihada yoyote na hata huhitaji kumjua sana yule mtu mwingine. Hata hivyo, upendo wa kweli si hisia tu. Ni kweli kwamba hisia zinahusika, lakini upendo ni kifungo chenye nguvu kinachotia ndani kanuni fulani. Upendo huendelea kuimarika unapokuzwa na kudumishwa.—Wakolosai 3:14.
Isitoshe, unahitaji muda kumjua mtu mwingine. Kufikiri kwamba umempata mwenzi anayekufaa mnapokutana tu kwa mara ya kwanza ni kama hadithi ya kuwaziwa na mara nyingi hukatisha tamaa. Kwa kuongezea, ukikata kauli haraka kwamba umepata mtu unayempenda kikweli, huenda ukapuuza mambo yanayoonyesha kwamba huo si upendo wa kweli. Kuchagua mwenzi anayekufaa kunahitaji mengi zaidi kuliko kuwa na hisia zenye nguvu zinazochochewa na kupumbazwa ghafula na upendo bandia. Kwa hiyo, usiwe na haraka. Uchunguzi mbalimbali umeonyesha kwamba kuchagua mwenzi asiyekufaa kunaweza kuathiri kazi yako, afya yako ya akili na mwili, na hata kufupisha maisha yako.
Mvulana anampoteza msichana: Mwanamume fulani mwenye cheo anamteka nyara mwanamke huyo mrembo kutoka kwenye kasri. Mwana wa mfalme anafunga safari hatari ili kumtafuta mrembo huyo. Msemaji wa Shirika la Waandishi wa Riwaya za Mahaba la Marekani anasema hivi: “Hadithi hiyo inapaswa kuzungumzia watu wawili wanaopendana na wanaofanya juu chini ili uhusiano wao ufanikiwe.” Katika riwaya nyingi, wasomaji hujua kwamba uhusiano huo utafaulu. Vikwazo vyovyote vile hushindwa.
Katika mahusiano halisi, matatizo husababishwa ama na watu walio katika uhusiano huo au na watu wengine. Huenda yakasababishwa na pesa, kazi, watu wa ukoo, na marafiki. Matatizo hutokea pia wakati mmoja wao hatimizi matarajio ya mwingine. Katika hadithi za kuwaziwa, kasoro za wahusika huwa ndogo tu, lakini sivyo ilivyo katika mahusiano halisi. Isitoshe, kwa kuwa watu wanapendana kikweli hiyo haimaanishi kwamba mambo yatakuwa shwari licha ya majaribu au licha ya kwamba watu hao wana maoni, malezi, tamaa, na nyutu tofauti. Upendo unahusisha ushirikiano, unyenyekevu, upole, subira, na ustahimilivu. Hizo ni sifa ambazo lazima mtu akuze.—1 Wakorintho 13:4-7.
Mvulana anampata msichana tena. Mwana wa mfalme anamwokoa mwanamke mrembo na kumfukuza yule mwanamume mwenye cheo. Wenzi hao wanaoana na kuishi raha mustarehe. Mhariri mmoja wa riwaya za mahaba aliwashauri hivi wanaotaka kuwa waandishi: “Umalizio wako unapaswa kuonyesha kwamba wenzi hao waliishi raha mustarehe. . . . Msomaji anapaswa kuridhika kwamba wenzi hao wanaishi pamoja na wana furaha.” Mara chache sana riwaya za mahaba huzungumza kuhusu maisha ya wenzi hao miaka kadhaa baada ya ndoa. Katika kipindi hicho huenda kutoelewana, magumu na matatizo mengine yakawa yamejaribu uhusiano wao. Kama takwimu za talaka zinavyoonyesha, baada ya muda ndoa nyingi hushindwa kustahimili majaribu na hivyo huvunjika.
Naam, upendo wa riwaya hauhitaji jitihada; upendo halisi si mchezo. Kuelewa tofauti kati ya aina hizo mbili za upendo kutakulinda dhidi ya kutarajia mambo yasiyowezekana. Pia kutakusaidia usitoe ahadi harakaharaka ambazo utajutia baadaye. Makala inayofuata itazungumzia jinsi unavyoweza kusitawisha upendo wa kweli usio na ubinafsi na jinsi unavyoweza kuwa mtu anayependeka kwa urahisi.
[Blabu katika ukurasa wa 5]
Watu ambao hawawapendi wengine sana hawapendwi sana
[Blabu katika ukurasa wa 7]
Upendo wa riwaya hauhitaji jitihada; upendo halisi si mchezo
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]
Mashujaa wa Mahaba—wa Kiume na wa Kike
Nchini Marekani, waandishi wa riwaya za mahaba hupata mabilioni ya dola kila mwaka. Karibu riwaya zote zinazouzwa nchini humo ni za mahaba. Kulingana na takwimu zilizochapishwa na Shirika la Waandishi wa Riwaya za Mahaba la Marekani, mambo matatu ambayo wasomaji, ambao asilimia 90 kati yao ni wanawake hutafuta katika mashujaa wa kiume ni misuli, sura yenye kuvutia, na akili. Mambo matatu yanayopendwa katika mashujaa wa kike ni akili, utu wenye nguvu, na urembo.
[Picha katika ukurasa wa 6, 7]
Ni mara chache sana vyombo vya habari hufundisha mambo sahihi kuhusu upendo
-
-
Jinsi Unavyoweza Kupata Upendo wa KweliAmkeni!—2006 | Machi
-
-
Jinsi Unavyoweza Kupata Upendo wa Kweli
Unaweza kufanya nini ili upate upendo na upendwe zaidi, na si kwa njia ya kimahaba tu? Je, unahitaji kuwa tajiri? Au unahitaji kuboresha sura yako?
WANAUME na wanawake hufikiri hilo ndilo suluhisho kwa kuwa wameathiriwa na matangazo ya biashara na vyombo vya habari. Bila shaka, ni jambo la kawaida na linalofaa kujali sura yetu, lakini urembo haudumu, na huo au utajiri hauwezi kuweka msingi wa kuwa na kifungo cha kudumu. Lakini kuwa na upendo usio na ubinafsi kunaweza kusaidia watu wapate upendo wa kweli. Yesu alifundisha hivi: “Muwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi.” (Luka 6:38) Kwa ufupi, ukitaka kupendwa, waonyeshe wengine upendo.
Tunaweza kuonyeshaje upendo? Akiandika chini ya mwongozo wa roho takatifu ya Mungu, mtume Paulo alijibu swali hilo. Alifunua kwamba upendo una nguvu, nao huonyeshwa si kwa hisia, bali kupitia yale ambayo mtu huwatendea wengine na yale anayojizuia kutenda. Ona maneno haya ya Paulo: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo hauna wivu, haujigambi, haujivuni, haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. Haushangilii juu ya ukosefu wa uadilifu, bali hushangilia pamoja na kweli. Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote.”—1 Wakorintho 13:4-7.
Wewe huhisije mtu anapokuonyesha fadhili au anapokuvumilia licha ya kwamba wewe husema au kufanya mambo madogomadogo yanayoudhi? Je, huvutiwi na mtu anayekujali kikweli, hakasiriki upesi, husamehe na husema kweli hata ingawa si rahisi kusamehe au kuwa mnyoofu?
Basi watendee wengine vivyo hivyo. Yesu alisema: “Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Si rahisi sikuzote kuonyesha upendo, lakini kuna manufaa ya kujitahidi kufanya hivyo. Kwanza, utapendwa na familia yako, marafiki, mwenzi wako wa ndoa, au yule atakayekuwa mwenzi wako wa ndoa. Pia, utakuwa na furaha kwa kuwa unafanya jambo lililo sawa na unajitoa kwa ajili ya wengine. Naam, “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.
Jifunze Upendo Kutoka kwa Mwenye Mamlaka Kuu Zaidi
Yehova ni Mungu wa upendo, naye ndiye mtaalamu bora zaidi wa upendo. (1 Yohana 4:8) Upendo wake humchochea kuwafundisha wote wanaotaka kujifunza sifa hiyo. Fikiria kanuni kadhaa za Biblia ambazo zinaweza kutusaidia kupendwa na kuwaonyesha wengine upendo.
‘Iweni wepesi kuhusu kusikia, si wepesi wa kusema.’ (Yakobo 1:19) Uchunguzi uliofanyiwa wenzi wa ndoa zaidi ya 20,000 ulionyesha kwamba watu waliokuwa na furaha zaidi ni wale ambao wenzi wao waliwasikiliza kwa makini. Mawasiliano mazuri ni muhimu katika uhusiano. Profesa mmoja wa masuala ya kijamii aliandika hivi: “Utajihisi mpweke ikiwa mwenzi wako hajui mambo unayokabiliana nayo. Au hali yako inaweza kuwa mbaya hata zaidi ikiwa mwenzi wako anajua yale unayokabili lakini haelewi sababu inayofanya mambo hayo yakuhangaishe sana.” Profesa huyo anaongeza kusema kwamba hata kama watu wawili wanatofautiana sana, “ikiwa mwenzi mmoja anajali maoni ya mwenzake na yale yanayompata maishani, basi tofauti hizo si kitu.”
“Mmesongwa mkakosa nafasi katika upendo wenu mwororo. . . . Panukeni.” (2 Wakorintho 6:12, 13) Sisi hunufaika tunapopanua upendo wetu kwa wengine. Kichapo kimoja cha Chuo cha Kitiba cha Harvard kinasema: “Uchunguzi mwingi umeonyesha kwamba watu walio na utegemezo wa jamii, yaani, watu walio na uhusiano mzuri na familia, marafiki, na jamii, huwa na furaha zaidi, huwa na matatizo machache zaidi ya afya, nao huishi muda mrefu zaidi.”
“Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri.” (Waebrania 10:24, 25) Sisi huathiriwa na marafiki wetu. Unaposhirikiana na wale wanaoonyesha upendo wa kweli wa Kikristo, utaonyeshwa sifa hiyo nawe utajifunza jinsi ya kuwaonyesha wengine sifa hiyo. Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuonyeshana upendo huo, wakijua kwamba sifa hiyo huwatambulisha kuwa wanafunzi wa kweli wa Yesu. (Yohana 13:35) Unakaribishwa uhudhurie mikutano yao ya Kikristo.
Ukihisi kwamba hupendwi, usivunjike moyo wala usijilaumu sana. Kumbuka kwamba Yehova anaona hali yako. Je, unamkumbuka Lea aliyetajwa katika makala ya kwanza ya mfululizo huu? Yehova aliona hali yake, naye akapata wana sita na binti mmoja, na hiyo ilikuwa baraka kwelikweli katika kizazi ambacho kilithamini sana watoto! Isitoshe, baadaye wana wote wa Lea walikuwa babu wa makabila ya Israeli. (Mwanzo 29:30-35; 30:16-21) Lazima Lea awe alifarijika sana kuona jinsi ambavyo Mungu alimjali kwa upendo.
Katika ulimwengu mpya unaoahidiwa katika Biblia, hakuna mtu atakayehisi kuwa hapendwi. Badala yake, wanadamu wote wataonyeshana upendo wa kweli. (Isaya 11:9; 1 Yohana 4:7-12) Basi na tuonyeshe sasa kwamba tunataka kuishi katika ulimwengu huo kwa kusitawisha upendo unaofundishwa katika Biblia na ambao umeonyeshwa na Mtungaji wake. Naam, shangwe ya kweli haitokani tu na kupendwa, bali inatokana na kuwaonyesha wengine upendo usio na ubinafsi.—Mathayo 5:46-48; 1 Petro 1:22.
[Blabu katika ukurasa wa 8]
“Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35
[Picha katika ukurasa wa 8]
Ukitaka kuonyeshwa upendo, waonyeshe wengine upendo
-