-
Kufaidika na Fadhili-upendo za YehovaMnara wa Mlinzi—2002 | Mei 15
-
-
Kufaidika na Fadhili-upendo za Yehova
‘Ni nani mwenye hekima? Atakaza fikira zake kuelekea matendo ya Yehova ya fadhili-upendo.’—ZABURI 107:43, NW.
1. Usemi “fadhili-upendo” ulitumiwa kwa mara ya kwanza katika Biblia wakati gani, nasi tutachunguza maswali gani kuhusu sifa hiyo?
MIAKA 4,000 hivi iliyopita, Loti, mwana wa ndugu ya Abrahamu alisema hivi kumhusu Yehova: “Umezidisha rehema [“fadhili-upendo,” NW] zako.” (Mwanzo 19:19) Hii ndiyo mara ya kwanza usemi “fadhili-upendo” umetumiwa katika Biblia. Yakobo, Naomi, Daudi, na watumishi wengine wa Mungu pia walitaja sifa hiyo ya Yehova. (Mwanzo 32:10; Ruthu 1:8; 2 Samweli 2:6) Kwa kweli, usemi “fadhili-upendo,” ukiwa katika umoja na katika wingi, unapatikana mara 250 hivi katika Biblia ya New World Translation of the Holy Scriptures. Lakini fadhili-upendo za Yehova ni nini? Ni nani walioonyeshwa sifa hiyo zamani? Nasi hufaidikaje na sifa hiyo leo?
2. Kwa nini ni vigumu sana kueleza maana ya neno la Kiebrania tunalozungumzia, nalo linaweza kutafsiriwaje?
2 Katika Maandiko, neno la Kiebrania linalotafsiriwa “fadhili-upendo” lina maana pana sana hivi kwamba lugha nyingi haziwezi kutumia neno moja kueleza maana kamili ya neno hilo. Hivyo, tafsiri kama “upendo,” “rehema,” na “uaminifu” hazitoi maana sahihi na kamili ya neno hilo. Hata hivyo, kitabu Theological Wordbook of the Old Testament kinasema kwamba usemi “fadhili-upendo” ‘unakaribiana sana na maana kamili ya neno hilo la Kiebrania.’ Kwa kufaa, tafsiri ya New World Translation of the Holy Scriptures—With References inaonyesha kwamba usemi “upendo mwaminifu-mshikamanifu” unaweza kutumiwa kutafsiri neno hilo la Kiebrania badala ya usemi “fadhili-upendo.”—Kutoka 15:13; Zaburi 5:7; kielezi-chini.
Fadhili-Upendo Ni Tofauti na Upendo na Uaminifu-Mshikamanifu
3. Sifa ya fadhili-upendo inatofautianaje na upendo?
3 Sifa ya fadhili-upendo, au upendo mwaminifu-mshikamanifu, inakaribiana sana na sifa ya upendo na ya uaminifu-mshikamanifu. Hata hivyo, sifa ya fadhili-upendo ni tofauti na sifa hizo nyingine katika njia mbalimbali muhimu. Fikiria jinsi fadhili-upendo na upendo zinavyotofautiana. Tunaweza kupenda vitu na pia maoni fulani. Biblia inasema juu ya ‘kupenda mvinyo’ na ‘kupenda hekima.’ (Mithali 21:17; 29:3) Lakini fadhili-upendo hutumiwa kuhusu watu wala si kuhusu maoni au vitu visivyo na uhai. Kwa mfano, andiko la Kutoka 20:6, NW linazungumza juu ya watu linaposema kwamba Yehova ‘huonyesha fadhili-upendo kwa kizazi cha elfu.’
4. Sifa ya fadhili-upendo inatofautianaje na uaminifu-mshikamanifu?
4 Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “fadhili-upendo” pia lina maana pana zaidi kuliko usemi “uaminifu-mshikamanifu.” Katika lugha fulani, usemi “uaminifu-mshikamanifu” hutumiwa mara nyingi kuonyesha jinsi mfanyakazi anavyopaswa kutenda kuelekea mkubwa wake. Lakini mtafiti mmoja anasema kwamba ‘mara nyingi Biblia hutumia usemi fadhili-upendo kuonyesha uhusiano ulio tofauti na wa mfanyakazi na mkubwa wake: yaani, mkubwa anakuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa aliye mnyonge na mwenye uhitaji.’ Hivyo mfalme Daudi angeweza kumwomba Yehova hivi: “Umwangaze mtumishi wako kwa nuru ya uso wako. Uniokoe kwa ajili ya fadhili [“fadhili-upendo,” NW] zako.” (Zaburi 31:16) Yehova, ambaye ndiye mwenye uwezo, anaombwa aonyeshe fadhili-upendo, au upendo mwaminifu-mshikamanifu kwa Daudi mwenye uhitaji. Kwa kuwa wenye uhitaji hawana mamlaka juu ya wenye uwezo, sifa ya fadhili-upendo katika uhusiano kama huo inaonyeshwa kwa nia ya kupenda wala si kwa kulazimishwa.
5. (a) Ni mambo gani yanayohusiana na fadhili-upendo za Mungu yanayokaziwa katika Neno lake? (b) Tutachunguza mambo gani yanayoonyesha fadhili-upendo za Yehova?
5 “Ni nani mwenye hekima?” akauliza mtunga-zaburi. ‘Atakaza fikira zake kuelekea matendo ya Yehova ya fadhili-upendo.’ (Zaburi 107:43, NW) Tunaweza kukombolewa na kuhifadhiwa kwa sababu ya fadhili-upendo za Yehova. (Zaburi 6:4; 119:88, 159) Sifa hiyo ni ulinzi na huleta kitulizo kutokana na matatizo. (Zaburi 31:16, 21; 40:11; 143:12) Kwa sababu ya sifa hiyo, watu wanaweza kukombolewa kutoka katika dhambi. (Zaburi 25:7) Kwa kuchunguza masimulizi na mistari fulani ya Biblia, tutaona kwamba fadhili-upendo za Yehova huonyeshwa (1) kwa matendo fulani hususa na (2) kwa watumishi wake waaminifu.
Ukombozi—Tendo la Fadhili-Upendo
6, 7. (a) Yehova alizidisha fadhili-upendo zake kwa Loti jinsi gani? (b) Loti alitaja fadhili-upendo za Yehova wakati gani?
6 Labda njia iliyo bora zaidi ya kujua ni kwa kadiri gani Yehova huonyesha sifa ya fadhili-upendo ni kuchunguza masimulizi ya Maandiko yanayohusu sifa hiyo. Katika andiko la Mwanzo 14:1-16, tunaona kwamba Loti, mwana wa ndugu ya Abrahamu, alichukuliwa mateka na majeshi ya adui. Lakini Abrahamu akamwokoa. Uhai wa Loti ulikuwa hatarini tena Yehova alipoamua kuharibu jiji lenye uovu la Sodoma, walikoishi Loti na familia yake.—Mwanzo 18:20-22; 19:12, 13.
7 Muda mfupi kabla ya kuharibiwa kwa Sodoma, malaika wa Yehova walimsindikiza Loti na familia yake kutoka katika jiji hilo. Wakati huo, Loti alisema: “Mtumwa wako ameona kibali machoni pako, nawe umezidisha rehema [“fadhili-upendo,” NW] zako ulizonifanyia kwa kuponya nafsi yangu.” (Mwanzo 19:16, 19) Kwa maneno hayo Loti alikubali kwamba Yehova alimwonyesha fadhili-upendo za pekee kwa kumwokoa. Katika kisa hicho, Mungu alionyesha fadhili-upendo zake kwa kumkomboa na kumhifadhi Loti.—2 Petro 2:7.
Fadhili-Upendo za Yehova na Mwongozo Wake
8, 9. (a) Mtumishi wa Abrahamu alipewa mgawo gani? (b) Kwa nini mtumishi huyo alisali kwa Mungu amwonyeshe fadhili-upendo, na kulitokea nini alipokuwa akisali?
8 Katika kitabu cha Mwanzo sura ya 24, tunasoma kuhusu tendo lingine linaloonyesha fadhili-upendo au upendo mwaminifu-mshikamanifu wa Mungu. Masimulizi hayo yanaonyesha kwamba Abrahamu alimtuma mtumishi wake asafiri kwenda nchi ya watu wa jamaa ya Abrahamu ili kumtafutia mwanawe Isaka mke. (Mstari wa 2-4) Huo ulikuwa mgawo mgumu, lakini mtumishi huyo alihakikishiwa kwamba malaika wa Yehova angemwongoza. (Mstari wa 7) Mwishowe, mtumishi huyo alifika kwenye kisima kimoja nje ya “mji wa Nahori” (ama Harani au mji mwingine uliokuwa karibu) wakati wanawake walipokuwa wakija kuchota maji. (Mstari wa 10, 11) Alipoona wanawake hao wakikaribia, alijua kwamba huo ulikuwa wakati muhimu zaidi kuhusiana na mgawo wake. Lakini angechaguaje mwanamke atakayefaa?
9 Kwa kuwa alijua kwamba alihitaji msaada wa Mungu, mtumishi wa Abrahamu alisali: “Ee BWANA, Mungu wa bwana wangu [Abrahamu] nakuomba mambo yangu uyajalie yawe heri leo, ukamfadhili [“ukamwonyeshe fadhili-upendo,” NW] bwana wangu [Abrahamu].” (Mstari wa 12) Yehova angeonyeshaje fadhili-upendo zake? Mtumishi huyo aliomba apewe ishara hususa ya kumtambua mwanamke ambaye Mungu amechagua. (Mstari wa 13, 14) Mwanamke mmoja alitenda sawasawa na vile mtumishi huyo alivyomwomba Yehova. Alitenda kana kwamba alikuwa amesikia sala yake! (Mstari 15-20) Hivyo, mtumishi huyo ‘akamkazia macho kwa mshangao.’ Lakini kuna mambo fulani muhimu aliyohitaji kujua. Je, mwanamke huyo mrembo alikuwa wa jamaa ya Abrahamu? Na je, alikuwa bado hajaolewa? Kwa hiyo mtumishi huyo “akanyamaza, ili ajue kwamba BWANA ameifanikisha safari yake ama sivyo.”—Mstari wa 16, 21.
10. Kwa nini mtumishi wa Abrahamu alisema kwamba Yehova alimwonyesha bwana wake fadhili-upendo?
10 Muda mfupi baadaye, mwanamke huyo kijana alijitambulisha kuwa “binti wa Bethueli mwana wa Milka, aliyemzalia Nahori [ndugu ya Abrahamu].” (Mwanzo 11:26; 24:24) Papo hapo mtumishi huyo akatambua kwamba Yehova alikuwa amejibu sala yake. Kwa furaha, aliinama chini na kusema: “Na atukuzwe BWANA, Mungu wa bwana wangu [Abrahamu], ambaye hakuacha rehema [“fadhili-upendo,” NW] zake na kweli yake kwa bwana wangu. BWANA akaniongoza mimi nami njiani hata nyumba ya nduguze bwana wangu.” (Mstari wa 27) Kwa kutoa mwongozo, Mungu alionyesha fadhili-upendo kwa Abrahamu, bwana wa mtumishi huyo.
Fadhili-Upendo za Mungu Huleta Kitulizo na Ulinzi
11, 12. (a) Yehova alimwonyesha Yosefu fadhili-upendo wakati wa majaribu gani? (b) Mungu alimwonyeshaje Yosefu fadhili-upendo?
11 Sasa, na tuchunguze kitabu cha Mwanzo sura ya 39. Sura hiyo inazungumza juu ya Yosefu, kitukuu wa Abrahamu, ambaye aliuzwa utumwani Misri. Hata hivyo, “BWANA akawa pamoja na [Yosefu].” (Mstari wa 1, 2) Kwa kweli, hata Potifa, Mmisri ambaye alikuwa bwana-mkubwa wa Yosefu, aliona kwamba Yehova alikuwa pamoja na Yosefu. (Mstari wa 3) Hata hivyo, Yosefu alipatwa na jaribu kali sana. Alishtakiwa isivyo kweli kwamba alitaka kumbaka mke wa Potifa na akafungwa gerezani. (Mstari wa 7-20) Akiwa “gerezani,” “walimwumiza miguu yake kwa pingu, akatiwa katika minyororo ya chuma.”—Mwanzo 40:15; Zaburi 105:18.
12 Ni nini kilichotokea wakati wa jaribu hilo kali sana? “BWANA akawa pamoja na [Yosefu], akamfadhili [“akamwonyesha fadhili-upendo,” NW].” (Mstari wa 21a) Tendo moja hususa la fadhili-upendo lilisababisha mfululizo wa matukio ambayo baadaye yalimletea Yosefu kitulizo kutokana na matatizo yake. Yehova alimwezesha Yosefu kupata “kibali machoni pa mkuu wa gereza.” (Mstari wa 21b) Kwa hiyo, mkuu huyo akampa Yosefu madaraka makubwa. (Mstari wa 22) Halafu, Yosefu akakutana na mtu aliyefanya ajulikane kwa Farao, mtawala wa Misri. (Mwanzo 40:1-4, 9-15; 41:9-14) Baadaye, mfalme alimpandisha Yosefu cheo akawa mtawala wa pili wa Misri. Cheo hicho kilimwezesha kuokoa uhai wakati nchi ya Misri ilipopatwa na njaa kali. (Mwanzo 41:37-55) Mateso ya Yosefu yalianza alipokuwa na umri wa miaka 17 na kuendelea kwa miaka zaidi ya 12! (Mwanzo 37:2, 4; 41:46) Lakini katika miaka hiyo yote ambayo Yosefu aliteseka na kutaabika, Yehova Mungu alimwonyesha fadhili-upendo kwa kumlinda asipatwe na madhara makubwa na kwa kumhifadhi ili kutimiza daraka la pekee katika kusudi la Mungu.
Fadhili-Upendo za Mungu Hazishindwi
13. (a) Ni maneno gani yanayohusu fadhili-upendo za Yehova yanayopatikana kwenye Zaburi ya 136? (b) Fadhili-upendo ni nini hasa?
13 Yehova aliwaonyesha Waisraeli fadhili-upendo mara nyingi sana. Zaburi ya 136 inasema kwamba kwa sababu ya fadhili-upendo zake aliwakomboa (Mstari wa 10-15, NW), akawaongoza (Mstari wa 16, NW), na kuwalinda. (Mstari wa 17-20, NW) Mungu pia amewaonyesha watu mmoja-mmoja fadhili-upendo zake. Mtu anayewaonyesha wanadamu wenzake fadhili-upendo hufanya hivyo kwa kujitolea kufanya mambo fulani ili kutimiza uhitaji fulani muhimu. Kuhusu fadhili-upendo, kitabu kimoja kinachozungumza juu ya Biblia kinasema: ‘Ni sifa ambayo hufanya maisha yawe bora zaidi. Inasaidia wale waliopatwa na mabaya au taabu.’ Msomi mmoja anaeleza fadhili-upendo kuwa “upendo unaoonyeshwa kwa matendo.”
14, 15. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Loti alikuwa mtumishi wa Mungu aliyekubaliwa?
14 Masimulizi ya kitabu cha Mwanzo ambayo tumechunguza yanatuonyesha kwamba Yehova hashindwi kuwaonyesha fadhili-upendo wale wanaompenda. Loti, Abrahamu, na Yosefu waliishi katika hali tofauti na walipatwa na majaribu yaliyotofautiana kabisa. Walikuwa wanadamu wasio wakamilifu, lakini walikuwa watumishi waliokubalika machoni pa Yehova, nao walihitaji msaada wake. Tunapata faraja kujua kwamba Baba yetu wa mbinguni huwaonyesha watu kama hao fadhili-upendo.
15 Loti alifanya maamuzi fulani yasiyo ya hekima yaliyomletea matatizo. (Mwanzo 13:12, 13; 14:11, 12) Lakini alionyesha sifa fulani nzuri. Wakati malaika wawili wa Mungu walipofika Sodoma, Loti aliwakaribisha vizuri. (Mwanzo 19:1-3) Kwa imani aliwaonya wakwe zake wa kiume kuhusu uharibifu wa Sodoma uliokuwa unakaribia. (Mwanzo 19:14) Maoni ya Mungu kuhusu Loti yanapatikana katika 2 Petro 2:7-9, ambapo tunasoma: “[Yehova] alimkomboa Loti mwadilifu, aliyetaabishwa sana na kujitia mno kwa watu wanaokaidi sheria katika mwenendo mlegevu—kwa maana mtu huyo mwadilifu kwa yale ambayo aliona na kusikia alipokuwa akikaa miongoni mwao kutoka siku hadi siku alikuwa akitesa-tesa nafsi yake yenye uadilifu kwa sababu ya vitendo vyao vya kuasi sheria—Yehova ajua jinsi ya kukomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu.” Naam, Loti alikuwa mtu mwadilifu, na andiko hilo linaonyesha kwamba alikuwa mtu mwenye ujitoaji-kimungu. Kama yeye, sisi hufurahia fadhili-upendo za Mungu tunapofanya “matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu.”—2 Petro 3:11, 12.
16. Biblia inatumia maneno gani ya sifa inapozungumza juu ya Abrahamu na Yosefu?
16 Masimulizi ya kitabu cha Mwanzo sura ya 24 yanaeleza wazi uhusiano wa karibu kati ya Abrahamu na Yehova. Mstari wa kwanza unasema kwamba ‘BWANA alimbariki Abrahamu katika vitu vyote.’ Mtumishi wa Abrahamu alimwita Yehova ‘Mungu wa bwana wangu Abrahamu.’ (Mstari wa 12, 27) Naye mwanafunzi Yakobo anasema kwamba Abrahamu ‘alitangazwa kuwa mwadilifu’ na “akaja kuitwa ‘rafiki ya Yehova.’” (Yakobo 2:21-23) Yosefu pia alikuwa na uhusiano wa karibu na Yehova ambao unakaziwa katika sura yote ya Mwanzo 39. (Mstari wa 2, 3, 21, 23) Zaidi ya hayo, mwanafunzi Stefano alisema hivi kumhusu Yosefu: “Mungu alikuwa pamoja naye.”—Matendo 7:9.
17. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mifano ya Loti, Abrahamu, na Yosefu?
17 Watu waliopokea fadhili-upendo za Mungu ambazo tumetoka tu kuzungumzia walikuwa na uhusiano mzuri na Yehova Mungu nao walitimiza kusudi lake katika njia mbalimbali. Walikabili vizuizi ambavyo hawangeweza kuvishinda kwa nguvu zao. Mambo haya yalikuwa hatarini: Maisha ya Loti, kuendelezwa kwa ukoo wa Abrahamu, na daraka ambalo Yosefu angetimiza. Yehova tu ndiye angeweza kutimiza mahitaji ya wanaume hao wenye kumwogopa, naye alifanya hivyo kwa matendo ya fadhili-upendo. Ili Yehova atuonyeshe fadhili-upendo milele, ni lazima tudumishe uhusiano wa karibu pamoja naye na kuendelea kufanya mapenzi yake.—Ezra 7:28; Zaburi 18:50.
Watumishi wa Mungu Wana Kibali
18. Maandiko mbalimbali ya Biblia huonyesha nini kuhusu fadhili-upendo za Yehova?
18 Fadhili-upendo za Yehova ‘zimejaa duniani,’ nasi tunathamini kama nini sifa hiyo ya Mungu! (Zaburi 119:64) Tunaitikia kwa moyo wote maneno haya yenye kurudiwa-rudiwa ya mtunga-zaburi: “Na wamshukuru BWANA, kwa fadhili [“fadhili-upendo,” NW] zake, na maajabu yake kwa wanadamu.” (Zaburi 107:8, 15, 21, 31) Tunafurahi kwamba Yehova huwaonyesha fadhili-upendo watumishi wake wanaokubalika machoni pake—wawe watu mmoja-mmoja au kikundi. Danieli alimtaja Yehova katika sala kuwa “[Mungu wa kweli], Mungu mkuu, mwenye kutisha, ashikaye maagano na rehema kwao wampendao, na kuzishika amri zake.” (Danieli 9:4) Mfalme Daudi alisali: “Uwadumishie wakujuao fadhili [“fadhili-upendo,” NW].” (Zaburi 36:10) Tunashukuru kama nini kwamba Yehova huwaonyesha watumishi wake fadhili-upendo!—1 Wafalme 8:23; 1 Mambo ya Nyakati 17:13.
19. Tutachunguza maswali gani katika makala inayofuata?
19 Kwa kweli Yehova anatukubali sisi watu wake! Tunafaidika na upendo ambao Mungu anaonyesha wanadamu kwa ujumla na pia kufurahia baraka za pekee zinazotokana na fadhili-upendo au upendo mwaminifu-mshikamanifu wa Baba yetu wa mbinguni. (Yohana 3:16) Tunanufaika zaidi na sifa hiyo nzuri ya Yehova, hasa tunapokuwa na uhitaji. (Zaburi 36:7) Lakini tunaweza kuigaje fadhili-upendo za Yehova Mungu? Je, sisi mmoja-mmoja tunaonyesha sifa hiyo ya pekee? Maswali hayo na mengine yanayohusiana nayo yatazungumziwa katika makala ifuatayo.
-
-
Waonyeshe Fadhili-upendo Wenye UhitajiMnara wa Mlinzi—2002 | Mei 15
-
-
Waonyeshe Fadhili-upendo Wenye Uhitaji
‘Tendeaneni kwa fadhili-upendo.’—ZEKARIA 7:9, NW.
1, 2. (a) Kwa nini tunapaswa kuonyesha fadhili-upendo? (b) Tutazungumzia maswali gani?
NENO la Yehova Mungu hututia moyo kupenda “rehema [“fadhili-upendo,” NW].” (Mika 6:8) Na pia hutupatia sababu za kufanya hivyo. Hiyo ni kwa sababu “mwenye rehema [“fadhili-upendo,” NW] huitendea mema nafsi yake.” (Mithali 11:17) Maneno hayo ni ya kweli kabisa! Tunapoonyesha fadhili-upendo, tunasitawisha urafiki wa karibu na wenye kudumu pamoja na wengine. Hivyo, tutakuwa na marafiki waaminifu-washikamanifu—ambao ni zawadi yenye thamani kubwa!—Mithali 18:24.
2 Zaidi ya hayo, Maandiko yanatuambia: “Aandamaye haki na fadhili [“fadhili-upendo,” NW] ataona uhai.” (Mithali 21:21) Naam, tukifuata fadhili-upendo tutapendwa na Mungu na tutakuwa na taraja la kufurahia baraka za wakati ujao zinazotia ndani uhai udumuo milele. Lakini tunaweza kuonyeshaje fadhili-upendo? Tuonyeshe nani fadhili-upendo? Na je, fadhili-upendo ni tofauti na fadhili ambazo kwa kawaida wanadamu huonyesha?
Fadhili Ambazo Wanadamu Huonyesha na Fadhili-Upendo
3. Sifa ya fadhili-upendo inatofautianaje na fadhili ambazo wanadamu huonyesha?
3 Sifa ya fadhili-upendo inatofautiana kwa njia mbalimbali na fadhili ambazo kwa kawaida wanadamu huonyesha. Kwa mfano, mara nyingi mtu anayeonyesha fadhili hufanya hivyo bila kujihusisha kibinafsi, au kuwa na uhusiano na watu anaowaonyesha fadhili. Hata hivyo, tunapoonyesha mtu fadhili-upendo tunashikamana naye kwa upendo. Katika Biblia, matendo ya fadhili-upendo kati ya wanadamu huenda yakategemea uhusiano uliopo tayari. (Mwanzo 20:13; 2 Samweli 3:8; 16:17) Au huenda yakategemea uhusiano unaotokana na matendo ya fadhili-upendo ambayo mtu alikuwa ametendewa hapo awali. (Yoshua 2:1, 12-14; 1 Samweli 15:6; 2 Samweli 10:1, 2) Ili kuonyesha tofauti hiyo, na tulinganishe mifano miwili ya Biblia inayoonyesha fadhili-upendo na fadhili ambazo wanadamu huonyesha.
4, 5. Mifano miwili inayotajwa katika Biblia inaonyeshaje tofauti kati ya fadhili ambazo wanadamu huonyesha na fadhili-upendo?
4 Mfano mmoja wa fadhili ambazo wanadamu huonyesha unahusu watu fulani walioharibikiwa na meli. Mtume Paulo alikuwa mmoja wao. Watu hao walipelekwa na maji hadi ufuo wa kisiwa cha Malta. (Matendo 27:37–28:1) Watu wa Malta hawakuwa na uhusiano na wasafiri hao waliokuwa taabani. Na zaidi, wasafiri hao hawakuwa wamewatendea watu wa Malta jambo lolote ambalo lingewafanya wahisi wakiwa na daraka la kuwasaidia. Hata hivyo, wakazi hao wa visiwani waliwakaribisha wageni hao vizuri na kuwaonyesha “fadhili ya kibinadamu isiyo ya kawaida.” (Matendo 28:2, 7) Ukaribishaji huo ulikuwa tendo la fadhili kwa wageni ambalo halikutazamiwa. Kwa hiyo ukaribishaji wao ulikuwa fadhili ambazo wanadamu huonyesha.
5 Kwa kulinganisha, fikiria jinsi Mfalme Daudi alivyomkaribisha Mefiboshethi, mwana wa Yonathani rafiki yake. Daudi alimwambia hivi Mefiboshethi: “Utakula chakula mezani pangu daima.” Akimweleza sababu ya kufanya hivyo, Daudi alimwambia: “Nitakutendea mema; kwa ajili ya Yonathani, baba yako.” (2 Samweli 9:6, 7, 13) Kwa kufaa, ukaribishaji huo wa Daudi unatajwa kuwa fadhili-upendo, si fadhili tu, kwa kuwa alionyesha uaminifu-mshikamanifu kwa uhusiano uliokuwa tayari umeanzishwa. (1 Samweli 18:3; 20:15, 42) Vivyo hivyo leo, watumishi wa Mungu huwaonyesha fadhili wanadamu kwa ujumla. Lakini wanaonyesha fadhili-upendo zenye kudumu, au upendo mwaminifu-mshikamanifu kwa wenzao ambao wana uhusiano wenye kukubalika kwa Mungu.—Mathayo 5:45; Wagalatia 6:10.
6. Ni mambo gani yanayohusiana na fadhili-upendo zinazoonyeshwa kati ya wanadamu ambayo yamekaziwa katika Neno la Mungu?
6 Ili kufahamu mambo mengine yanayohusiana na fadhili-upendo, tutachunguza kwa ufupi masimulizi matatu ya Biblia yanayokazia sifa hiyo. Kutokana na masimulizi hayo tutaona kwamba wanadamu huonyesha fadhili-upendo kwa (1) matendo hususa, (2) kwa nia ya kupenda, na (3) hasa kwa wale walio na uhitaji. Zaidi ya hayo, masimulizi hayo yanaonyesha jinsi tunavyoweza kuonyesha fadhili-upendo leo.
Baba Aonyesha Fadhili-Upendo
7. Mtumishi wa Abrahamu alimwambia nini Bethueli na Labani, na mtumishi huyo alizusha suala gani?
7 Andiko la Mwanzo 24:28-67 linamalizia masimulizi kuhusu mtumishi wa Abrahamu, aliyetajwa katika makala iliyotangulia. Baada ya kukutana na Rebeka, mtumishi huyo alialikwa nyumbani kwa Bethueli, babake Rebeka. (Mstari wa 28-32) Huko mtumishi huyo alisimulia kwa undani mgawo wake wa kumtafutia mwana wa Abrahamu mke. (Mstari wa 33-47) Alikazia kwamba aliona kufanikiwa kwake kufikia wakati huo kuwa ishara kutoka kwa Yehova, “aliyeniongoza njiani, nimtwalie mwana wa bwana wangu binti wa ndugu yake.” (Mstari wa 48) Yaelekea mtumishi huyo alitumaini kwamba maelezo yake ya kutoka moyoni kuhusu tukio hilo yangemhakikishia Bethueli na mwanawe Labani kwamba Yehova alibariki mgawo huo. Mwishowe mtumishi huyo alisema: “Kama mnataka kumfanyia rehema [“fadhili-upendo,” NW] na kweli bwana wangu, niambieni kama sivyo, niambieni; ili nigeuke upande wa kuume au wa kushoto.”—Mstari wa 49.
8. Bethueli aliitikiaje katika kisa hiki kinachomhusu Rebeka?
8 Tayari Yehova alikuwa amemwonyesha Abrahamu fadhili-upendo. (Mwanzo 24:12, 14, 27) Je, Bethueli angekuwa tayari kufanya vivyo hivyo kwa kumruhusu Rebeka aende na mtumishi wa Abrahamu? Je, yeye pia angeonyesha fadhili-upendo kama zile zilizoonyeshwa na Mungu? Au safari ndefu ya mtumishi huyo ingekuwa ya bure? Ni lazima mtumishi huyo wa Abrahamu awe alifarijika sana kusikia Labani na Bethueli wakisema: “Neno hili limetoka kwa BWANA.” (Mstari wa 50) Walitambua kwamba Yehova alikuwa anahusika katika jambo hilo na wakakubali uamuzi wake bila kusita. Kisha, Bethueli akaonyesha fadhili-upendo zake kwa kuendelea kusema: “Rebeka huyu hapa; mchukue uende. Na awe mke wa mwana wa bwana wako kama Mwenyezi-Mungu alivyosema.” (Mstari wa 51, BHN) Rebeka alikubali kwenda na mtumishi wa Abrahamu na muda si muda akawa mke mpendwa wa Isaka.—Mstari wa 49, 52-58, 67.
Mwana Aonyesha Fadhili-Upendo
9, 10. (a) Yakobo alimwomba mwanawe Yosefu amfanyie nini? (b) Yosefu alimwonyeshaje babake fadhili-upendo?
9 Yakobo, mjukuu wa Abrahamu pia alionyeshwa fadhili-upendo. Kama Mwanzo sura ya 47 inavyoeleza, Yakobo alikuwa akiishi Misri wakati huo na ‘siku za kufa kwake zikakaribia.’ (Mstari wa 27-29) Alikuwa na wasiwasi kwa kuwa angekufa nje ya nchi ambayo Mungu alimwahidi Abrahamu. (Mwanzo 15:18; 35:10, 12; 49:29-32) Hata hivyo, Yakobo hakutaka kuzikwa Misri, hivyo akapanga mwili wake upelekwe katika nchi ya Kanaani. Hakuna mtu mwingine ambaye angeweza kuhakikisha kwamba tamaa yake imetimizwa isipokuwa tu mwanawe Yosefu aliyekuwa na uwezo.
10 Masimulizi hayo yanasema: “Yakobo akamwita mwanawe [Yosefu], akamwambia, Kama nimeona kibali machoni pako, . . . ukanifanyie rehema [“fadhili-upendo,” NW] na kweli; nakusihi usinizike katika Misri. Lakini nitakapolala pamoja na baba zangu, unichukue toka Misri, unizike katika kaburi lao.” (Mwanzo 47:29, 30) Yosefu aliahidi kutimiza ombi hilo, na muda mfupi baadaye Yakobo akafa. Yosefu na wana wengine wa Yakobo walibeba mwili wake ‘mpaka nchi ya Kanaani, nao wakamzika katika pango ya shamba la Makpela, aliyoinunua Abrahamu.’ (Mwanzo 50:5-8, 12-14) Hivyo, Yosefu akamwonyesha babake fadhili-upendo.
Binti-Mkwe Aonyesha Fadhili-Upendo
11, 12. (a) Ruthu alimwonyeshaje Naomi fadhili-upendo? (b) Ni katika njia gani Ruthu alionyesha fadhili-upendo nyingi zaidi wakati wa “mwisho” kuliko “mwanzo”?
11 Kitabu cha Ruthu kinasimulia jinsi Naomi alivyoonyeshwa fadhili-upendo na Ruthu, binti-mkwe wake aliyekuwa Mmoabu. Wote wawili walikuwa wajane. Naomi alipoamua kurudi Bethlehemu huko Yuda, Ruthu alionyesha fadhili-upendo na nia thabiti aliposema: “Wewe uendako nitakwenda, na wewe ukaapo nitakaa. Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu.” (Ruthu 1:16) Baadaye Ruthu alionyesha fadhili-upendo alipokubali kuolewa na Boazi, aliyekuwa mzee kutoka ukoo wa Naomi.a (Kumbukumbu la Torati 25:5, 6; Ruthu 3:6-9) Boazi alimwambia Ruthu hivi: “Umezidi kuonyesha fadhili [“fadhili-upendo,” NW] zako mwisho kuliko mwanzo, kwa vile usivyowafuata vijana, kama ni maskini kama ni matajiri.”—Ruthu 3:10.
12 Ruthu alionyesha fadhili-upendo zake “mwanzo” alipowaacha watu wao na kuandamana na Naomi. (Ruthu 1:14; 2:11) Tendo la “mwisho” la fadhili-upendo lilikuwa bora kuliko la “mwanzo” kwa kuwa Ruthu alikubali kuolewa na Boazi. Kwa kuwa Naomi alikuwa amepita umri wa kuzaa, sasa Ruthu angeweza kumzalia mrithi. Boazi na Ruthu walioana, na baadaye Ruthu alipopata mtoto, wanawake wa Bethlehemu wakapaaza sauti: “Naomi amezaliwa mwana.” (Ruthu 4:14, 17) Kwa kweli Ruthu alikuwa “mwanamke mwema,” aliyethawabishwa na Yehova kwa kupewa pendeleo zuri la kuwa nyanya ya Yesu Kristo.—Ruthu 2:12; 3:11; 4:18-22; Mathayo 1:1, 5, 6.
Zaonyeshwa kwa Matendo
13. Bethueli, Yosefu, na Ruthu walionyeshaje fadhili-upendo?
13 Je, umeona jinsi Bethueli, Yosefu, na Ruthu walivyoonyesha fadhili-upendo? Walifanya hivyo kwa maneno yenye fadhili na kwa matendo hususa. Bethueli hakusema tu, “Rebeka huyu hapa” bali ‘alimwacha Rebeka aende.’ (Mwanzo 24:51, 59, BHN) Yosefu hakusema tu, “Nitafanya kama ulivyosema” bali yeye na ndugu zake walimfanyia Yakobo “kama alivyowaagiza.” (Mwanzo 47:30; 50:12, 13) Naye Ruthu hakusema tu, “Wewe uendako nitakwenda,” lakini aliwaacha watu wao na kuandamana na Naomi, “wakaendelea wote wawili hata walipofika Bethlehemu.” (Ruthu 1:16, 19) Huko Yuda, Ruthu pia ‘alifanya yote kama vile mkwewe alivyomwagiza.’ (Ruthu 3:6) Naam, fadhili-upendo za Ruthu, kama za wale wengine, zilionyeshwa kwa matendo.
14. (a) Watumishi wa Yehova wa siku hizi wanaonyeshaje fadhili-upendo kwa matendo? (b) Ni matendo gani ya fadhili-upendo yanayofanywa na Wakristo katika eneo lako?
14 Inachangamsha moyo kuona jinsi watumishi wa Mungu leo wanavyoendelea kuonyesha fadhili-upendo kwa matendo. Kwa mfano, fikiria wale wanaoendelea kuwategemeza kihisia-moyo waamini wenzao walio wagonjwa, walioshuka moyo, au wenye huzuni. (Mithali 12:25) Au fikiria Mashahidi wengi wa Yehova ambao kwa uaminifu hutumia magari yao kuwapeleka wazee-wazee kwenye Jumba la Ufalme ili kuhudhuria mikutano ya kila juma ya kutaniko. Wengi wana maoni kama haya ya Anna mwenye umri wa miaka 82 ambaye ana ugonjwa wa yabisi kavu: “Kupelekwa kwa gari kwenye mikutano yote ni baraka kutoka kwa Yehova. Ninamshukuru kutoka moyoni kwa kunipatia ndugu na dada kama hao wenye upendo.” Je, unafanya vivyo hivyo katika kutaniko lako? (1 Yohana 3:17, 18) Ikiwa unafanya hivyo, uwe na uhakika kwamba fadhili-upendo zako zinathaminiwa sana.
Zaonyeshwa kwa Nia ya Kupenda
15. Ni sifa gani inayohusiana na fadhili-upendo ambayo pia inakaziwa na masimulizi matatu ya Biblia ambayo tumechunguza?
15 Masimulizi ya Biblia ambayo tumechunguza yanaonyesha pia kwamba fadhili-upendo zinaonyeshwa kwa nia ya kupenda, pasipo kulazimishwa. Bethueli na Rebeka walishirikiana na mtumishi wa Abrahamu kwa nia ya kupenda. (Mwanzo 24:51, 58) Yosefu alionyesha fadhili-upendo bila kusukumwa na yeyote. (Mwanzo 50:4, 5) Ruthu “alikaza nia yake kufuatana na [Naomi].” (Ruthu 1:18) Naomi alipomshauri Ruthu azungumze na Boazi, Mmoabi huyo alichochewa na fadhili-upendo kusema: “Hayo yote unenayo mimi nitayafanya.”—Ruthu 3:1-5.
16, 17. Ni nini kinachofanya fadhili-upendo za Bethueli, Yosefu, na Ruthu ziwe na umuhimu wa kipekee, nao walichochewa na nini kuonyesha sifa hiyo?
16 Fadhili-upendo zilizoonyeshwa na Bethueli, Yosefu, na Ruthu zina umuhimu wa kipekee kwa sababu Abrahamu, Yakobo, na Naomi hawangeweza kuwalazimisha kutenda jinsi walivyotenda. Kwani, hakuna sheria ambayo ingemlazimisha Bethueli aache binti yake aende. Ingekuwa rahisi kwake kumwambia mtumishi wa Abrahamu hivi: ‘La, sitaki binti yangu anayefanya kazi kwa bidii awe mbali nami.’ (Mwanzo 24:18-20) Vivyo hivyo, Yosefu alikuwa huru kuamua kama atatimiza au hatatimiza ombi la babake, kwa kuwa Yakobo angekuwa amekufa na hangeweza kumlazimisha alitimize. Naomi mwenyewe alisema kwamba Ruthu alikuwa huru kukaa Moabu. (Ruthu 1:8) Ruthu pia alikuwa huru kuolewa na mmoja wa “vijana” badala ya kuolewa na Boazi aliyekuwa mzee.
17 Bethueli, Yosefu, na Ruthu walionyesha fadhili-upendo kwa nia ya kupenda; walichochewa kufanya hivyo kutoka moyoni. Walihisi wana daraka la kuwaonyesha fadhili-upendo watu waliokuwa na uhusiano nao, kama vile baadaye Mfalme Daudi alivyohisi ana wajibu wa kuonyesha sifa hiyo kwa Mefiboshethi.
18. (a) Wazee Wakristo ‘huchunga kundi’ wakiwa na mtazamo gani? (b) Mzee mmoja alisema anahisije kuhusu kuwasaidia waamini wenzake?
18 Sifa ya fadhili-upendo inatambulisha watu wa Mungu kutia ndani wale wanaochunga kundi lake. (Zaburi 110:3; 1 Wathesalonike 5:12) Wazee hao, au waangalizi, wanahisi wana daraka la kutimiza mambo wanayotazamiwa kutimiza wanapowekwa kuwa wazee. (Matendo 20:28) Hata hivyo, wao hufanya uchungaji na matendo mengine ya fadhili-upendo kwa ajili ya kutaniko, “si kwa kushurutishwa, bali kwa nia ya kupenda.” (1 Petro 5:2) Wazee huchunga kundi kwa sababu wana daraka hilo na wanatamani kufanya hivyo. Wanawaonyesha kondoo wa Kristo fadhili-upendo kwa sababu wanapaswa kufanya hivyo nao pia wanataka kufanya hivyo. (Yohana 21:15-17) “Ninapenda kutembelea akina ndugu nyumbani au kuwapigia simu ili kuwaonyesha tu nilikuwa ninawafikiria,” anasema mzee mmoja Mkristo. “Kuwasaidia akina ndugu huniletea furaha na uradhi mwingi!” Wazee wote wanaojali wanakubaliana na maneno hayo kabisa.
Waonyeshe Fadhili-Upendo Wenye Uhitaji
19. Masimulizi ya Biblia yaliyozungumziwa katika makala hii yanakazia nini kuhusu fadhili-upendo?
19 Masimulizi ya Biblia tuliyozungumzia pia yanakazia kwamba fadhili-upendo zinapaswa kuonyeshwa wale ambao hawawezi kujitimizia mahitaji yao. Abrahamu alihitaji msaada wa Bethueli ili kuendeleza ukoo wake. Naye Yakobo alihitaji msaada wa Yosefu ili mwili wake upelekwe Kanaani. Naomi pia alihitaji msaada wa Ruthu ili kupata mrithi. Abrahamu, Yakobo, na Naomi hawangeweza kutimiza mahitaji yao bila kusaidiwa. Vivyo hivyo leo, fadhili-upendo zinapaswa hasa kuonyeshwa wale wenye uhitaji. (Mithali 19:17) Tunapaswa kumwiga mzee wa ukoo Yobu, ambaye alijali ‘maskini aliyelilia msaada, yatima asiyekuwa na wa kumsaidia’ na pia wale “waliokuwa karibu kuangamia.” Yobu pia ‘aliwafanya wajane waone tena furaha moyoni’ na akawa ‘macho kwa kipofu na miguu kwa viwete.’—Ayubu 29:12-15, BHN.
20, 21. Ni nani tunaohitaji kuwaonyesha fadhili-upendo, na sote tunapaswa kuazimia kufanya nini?
20 Kwa kweli, kuna ‘maskini wanaolilia msaada’ katika kila kutaniko la Kikristo. Huenda kilio chao kikasababishwa na upweke, kuvunjika moyo, kuhisi hawafai, kukatishwa tamaa na wengine, ugonjwa mbaya sana, au kifo cha mpendwa. Hata sababu iwe nini, Wakristo hao wapendwa wana mahitaji ambayo yanaweza na yanapaswa kutimizwa kwa matendo yetu ya fadhili-upendo tunayofanya kwa nia ya kupenda na kwa kuendelea.—1 Wathesalonike 5:14.
21 Hivyo basi, na tuendelee kumwiga Yehova Mungu, ambaye ni “mwingi wa rehema [“fadhili-upendo,” NW].” (Kutoka 34:6; Waefeso 5:1) Tunaweza kufanya hivyo kwa kuwatendea jambo fulani hususa hasa wale wenye uhitaji. Na bila shaka tutamtukuza Yehova na kupata furaha nyingi ‘tunapotendeana kwa fadhili-upendo.’—Zekaria 7:9, NW.
[Maelezo ya Chini]
a Ili upate kujua zaidi kuhusu aina ya ndoa kati ya Boazi na Ruthu, ona ukurasa wa 370 katika Buku la Kwanza la Insight on the Scriptures, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-