Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Yehova Hatawaacha Washikamanifu Wake
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Agosti 15
    • Yehova Hatawaacha Washikamanifu Wake

      “[Yehova] hatawaacha washikamanifu wake. Hakika watalindwa mpaka wakati usio na kipimo.”—ZAB. 37:28.

      1, 2. (a) Ni mambo gani yaliyojaribu ushikamanifu wa watumishi wa Mungu katika karne ya kumi K.W.K.? (b) Yehova aliwalinda washikamanifu wake katika hali gani tatu?

      NI KARNE ya kumi K.W.K. na ni wakati wa kufanya uamuzi. Vita vya wenyewe kwa wenyewe vimeepukwa chupuchupu wakati makabila ya kaskazini ya Israeli yenye msukosuko yanapopewa uhuru wa kadiri fulani. Yeroboamu, mfalme wao aliyewekwa rasmi hivi karibuni tu, anaimarisha haraka mamlaka yake kwa kuanzisha dini mpya ya taifa. Anataka raia wake wamtii kikamili. Watumishi waaminifu wa Yehova watafanya nini? Je, watabaki washikamanifu kwa Mungu wanayemwabudu? Maelfu wanafanya hivyo, na Yehova anawalinda wanapodumisha utimilifu wao.—1 Fal. 12:1-33; 2 Nya. 11:13, 14.

      2 Leo pia ushikamanifu wa watumishi wa Mungu unajaribiwa. Biblia inaonya hivi: “Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda. Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” Je, tunaweza kufanikiwa ‘kuchukua msimamo kumpinga yeye, tukiwa imara katika imani’? (1 Pet. 5:8, 9) Acheni tuchunguze mambo fulani yaliyotukia Mfalme Yeroboamu alipowekwa rasmi mwaka wa 997 K.W.K. na kuona yale tunayoweza kujifunza. Katika nyakati hizo ngumu, watumishi waaminifu wa Yehova walikuwa wakikandamizwa. Walikabiliana pia na uvutano mbalimbali wa uasi-imani walipokuwa wakitimiza migawo migumu. Katika kila moja ya hali hizo, Yehova hakuwaacha washikamanifu wake, naye hatawaacha leo.—Zab. 37:28.

      Wanapokandamizwa

      3. Kwa nini utawala wa Mfalme Daudi haukuwakandamiza watu?

      3 Acheni kwanza tuchunguze ni katika hali gani Yeroboamu alikuja kuwa mfalme. Andiko la Methali 29:2 linasema hivi: “Mtu yeyote mwovu anapotawala, watu huugua.” Chini ya utawala wa Mfalme Daudi wa Israeli la kale, watu hawakuugua. Daudi hakuwa mkamilifu, lakini alikuwa mshikamanifu kwa Mungu na alimtegemea. Utawala wa Daudi haukuwakandamiza watu. Yehova alifanya agano pamoja na Daudi, na kumwambia: “Nyumba yako na ufalme wako hakika zitakuwa imara mpaka wakati usio na kipimo mbele yako; nacho kiti chako cha ufalme kitafanywa imara mpaka wakati usio na kipimo.”—2 Sam. 7:16.

      4. Baraka ambazo watu walifurahia wakati wa utawala wa Sulemani zilitegemea nini?

      4 Mwanzoni, utawala wa Sulemani, mwana wa Daudi, ulikuwa wenye amani na ufanisi sana hivi kwamba ulifananisha vizuri Utawala ujao wa Miaka Elfu wa Kristo Yesu. (Zab. 72:1, 17) Wakati huo, hakuna hata kabila moja kati ya makabila 12 ya Israeli ambalo lilikuwa na sababu ya kuasi. Hata hivyo, baraka ambazo Sulemani na raia wake walifurahia zilikuwa na masharti. Yehova alimwambia Sulemani hivi: “Ukitembea katika sheria zangu na kutenda maamuzi yangu ya hukumu na kushika amri zangu zote kwa kutembea ndani yake, mimi pia hakika nitakutimizia neno nililomwambia Daudi baba yako; nami hakika nitakaa katikati ya wana wa Israeli, wala sitawaacha watu wangu Israeli.”—1 Fal. 6:11-13.

      5, 6. Kulikuwa na matokeo gani Sulemani alipoacha kuwa mshikamanifu kwa Mungu?

      5 Alipozeeka, Sulemani aliacha kuwa mwaminifu kwa Yehova naye akaanza kushiriki katika ibada ya uwongo. (1 Fal. 11:4-6) Hatua kwa hatua, Sulemani aliacha kutii sheria za Yehova na akawakandamiza sana watu. Aliwakandamiza watu sana hivi kwamba baada ya kifo chake, watu waliendelea kulalamika kumhusu kwa mwana na mrithi wake, Rehoboamu, na kumwomba awapunguzie nira nzito. (1 Fal. 12:4) Yehova alihisi jinsi gani Sulemani alipoacha kuwa mwaminifu?

      6 Biblia inatuambia hivi: “Yehova akamkasirikia Sulemani, kwa sababu moyo wake ulikuwa umegeuka ukamwacha . . . Mungu wa Israeli, yeye aliyemtokea mara mbili.” Yehova akamwambia Sulemani: “Kwa sababu . . . hukushika agano langu na sheria zangu nilizokuamuru, hakika nitaurarua ufalme kutoka kwako, nami nitampa mtumishi wako.”—1 Fal. 11:9-11.

      7. Ingawa Sulemani alikataliwa, Yehova aliwajali jinsi gani washikamanifu Wake?

      7 Kisha, Yehova akamtuma nabii Ahiya amtie mafuta mkombozi. Mkombozi huyo alikuwa Yeroboamu, mwanamume mwenye uwezo aliyefanya kazi katika serikali ya Sulemani. Ingawa Yehova alibaki mshikamanifu kwa agano la Ufalme alilofanya na Daudi, Alikubali serikali ya makabila 12 igawanyike. Yeroboamu angepewa makabila kumi; na mawili yangebaki katika familia ya ukoo wa Daudi, ambayo sasa iliwakilishwa na Mfalme Rehoboamu. (1 Fal. 11:29-37; 12:16, 17, 21) Yehova alimwambia Yeroboamu hivi: “Itatukia kwamba, ukitii yote ambayo nitakuamuru, nawe utembee katika njia zangu na kwa kweli ufanye yaliyo sawa machoni pangu kwa kushika sheria zangu na amri zangu, kama Daudi mtumishi wangu alivyofanya, mimi pia nitakuwa pamoja nawe, nami nitakujengea nyumba yenye kudumu, kama nilivyomjengea Daudi, nami nitakupa Israeli.” (1 Fal. 11:38) Yehova alichukua hatua ili kuwasaidia watu wake naye akatayarisha njia ili kuwatoa katika ukandamizaji huo.

      8. Ni majaribu gani yanayowapata watu wa Mungu leo?

      8 Leo ukandamizaji na ukosefu wa haki umeenea. Andiko la Mhubiri 8:9 linasema hivi: “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.” Huenda biashara zenye pupa na utawala wenye ufisadi ukafanya hali za kiuchumi ziwe ngumu. Mara nyingi viongozi katika serikali, biashara, na dini ni mifano mibaya kiadili. Kwa hiyo, kama Loti aliyekuwa mwadilifu, washikamanifu wa Mungu leo ‘wanataabishwa sana na kule kujitia mno katika mwenendo mpotovu kwa watu wanaokaidi sheria.’ (2 Pet. 2:7) Zaidi ya hayo, ingawa tunajitahidi sana kuishi kulingana na viwango vya Mungu bila kuwasumbua watu wengine, mara nyingi tunakuwa shabaha ya mateso kutoka kwa watawala wenye kiburi.—2 Tim. 3:1-5, 12.

      9. (a) Tayari Yehova amefanya nini ili kuwakomboa watu wake? (b) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba sikuzote Yesu atakuwa mshikamanifu kwa Mungu?

      9 Hata hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kuhusu ukweli huu wa msingi: Yehova hatawaacha washikamanifu wake! Hebu fikiria hatua ambazo tayari amechukua ili kuwaondoa watawala wa ulimwengu waliopotoka. Ufalme wa Kimasihi wa Mungu ulio mikononi mwa Kristo Yesu tayari umesimamishwa. Yesu Kristo amekuwa akitawala mbinguni kwa karibu miaka mia moja sasa. Hivi karibuni atawaletea kitulizo kamili wale wanaoliogopa jina la Mungu. (Soma Ufunuo 11:15-18.) Tayari Yesu amejithibitisha mwenyewe kuwa mshikamanifu kwa Mungu mpaka kifo. Hatawakatisha tamaa raia wake, kama Sulemani alivyofanya.—Ebr. 7:26; 1 Pet. 2:6.

      10. (a) Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunathamini Ufalme wa Mungu? (b) Tunapokabili majaribu, tunaweza kuwa na uhakika gani?

      10 Ufalme wa Mungu ni serikali halisi ambayo itakomesha ukandamizaji wote. Tunamtii Yehova Mungu na Ufalme wake. Tukiwa na uhakika kabisa katika Ufalme, tunauchukia kabisa ulimwengu usiomwogopa Mungu na tunafuatilia kwa bidii kazi njema. (Tito 2:12-14) Tunajitahidi kubaki bila doa kutokana na ulimwengu huu. (2 Pet. 3:14) Hata tukikabili majaribu gani sasa, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatulinda tusipatwe na madhara ya kiroho. (Soma Zaburi 97:10.) Zaidi ya hayo, Zaburi 116:15 inatuhakikishia hivi: “Ni chenye thamani machoni pa Yehova kifo cha washikamanifu wake.” Watumishi wa Yehova ni wenye thamani sana machoni pake hivi kwamba hataruhusu kamwe waangamie wakiwa kikundi.

      Wanapokabili Uvutano Mbalimbali wa Uasi-Imani

      11. Yeroboamu aliacha jinsi gani kuwa mshikamanifu?

      11 Utawala wa Mfalme Yeroboamu ungewaletea watu wa Mungu kitulizo fulani. Badala yake, matendo yake yalijaribu hata zaidi ushikamanifu wao kwa Mungu. Kwa kuwa hakuridhika na heshima na pendeleo alilokuwa tayari amepewa, Yeroboamu alianza kutafuta njia za kuimarisha cheo chake. Alifikiri hivi: “Watu hawa wakiendelea kwenda kutoa dhabihu katika nyumba ya Yehova huko Yerusalemu, moyo wa watu hawa pia utarudi kwa bwana wao, Rehoboamu mfalme wa Yuda; nao hakika wataniua na kurudi kwa Rehoboamu mfalme wa Yuda.” Hivyo, Yeroboamu akaanzisha dini mpya iliyotegemea ndama wawili wa dhahabu. “Kisha akaweka mmoja kule Betheli, na mwingine akamweka kule Dani. Na jambo hilo likaja kusababisha dhambi, na watu wakaanza kwenda mpaka kule Dani mbele ya yule aliyekuwa huko. Naye akaanza kujenga nyumba ya mahali pa juu na kuweka makuhani kutoka kwa watu wa kawaida, ambao hawakuwa wa wana wa Lawi.” Yeroboamu hata akaanzisha siku yake mwenyewe ya “sherehe kwa ajili ya wana wa Israeli,” naye akaanza “kutoa matoleo juu ya madhabahu ili kufukiza moshi wa dhabihu.”—1 Fal. 12:26-33.

      12. Washikamanifu wa Mungu katika ufalme wa kaskazini walifanya nini Yeroboamu alipoanzisha ibada ya ndama huko Israeli?

      12 Sasa washikamanifu wa Mungu katika ufalme wa kaskazini wangefanya nini? Walawi waliokuwa wakiishi katika majiji waliyopewa katika eneo la ufalme wa kaskazini walichukua hatua mara moja kama walivyofanya mababu wao waaminifu. (Kut. 32:26-28; Hes. 35:6-8; Kum. 33:8, 9) Waliacha urithi wao wote, wakahamishia familia zao kusini huko Yuda, ambako wangeendelea kumwabudu Yehova bila vipingamizi. (2 Nya. 11:13, 14) Waisraeli wengine ambao walikuwa wakiishi kwa muda huko Yuda waliamua kubaki Yuda badala ya kurudi nyumbani. (2 Nya. 10:17) Yehova alihakikisha kwamba njia ya kurudia ibada ya kweli iliachwa wazi ili katika vizazi vya baadaye wengine kutoka katika ufalme wa kaskazini waweze kuacha ibada ya ndama na kurudi Yuda.—2 Nya. 15:9-15.

      13. Katika nyakati za kisasa, watu wa Mungu wamejaribiwa jinsi gani na uvutano wa waasi-imani?

      13 Waasi-imani na uvutano wao ni hatari kwa watu wa Mungu leo. Watawala fulani wamejaribu kuanzisha dini yao ya taifa na kuwasukuma raia wao waikubali. Makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo na watu wengine wenye kimbelembele wamejaribu kujinyakulia ukuhani wa kiroho. Hata hivyo, Wakristo wa kweli tu ndio walio na watiwa-mafuta wa kweli, wanaofanyiza “ukuhani wa kifalme.”—1 Pet. 2:9; Ufu. 14:1-5.

      14. Tunapaswa kuchukua hatua gani kuelekea mawazo ya waasi-imani?

      14 Kama Walawi waaminifu wa karne ya kumi K.W.K., washikamanifu wa Mungu leo hawadanganywi na mawazo ya waasi-imani. Watiwa-mafuta na washiriki wenzao Wakristo wanaepuka na kukataa kabisa mawazo ya waasi-imani. (Soma Waroma 16:17.) Ingawa tunajitiisha kwa kupenda kwa mamlaka za serikali katika mambo ya kimwili na hatuungi mkono upande wowote katika mizozo ya ulimwengu, tunashikamana na Ufalme wa Mungu. (Yoh. 18:36; Rom. 13:1-8) Tunakataa madai ya uwongo ya wale wanaodai kumtumikia Mungu lakini wanamvunjia heshima kwa mwenendo wao.—Tito 1:16.

      15. Kwa nini “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anastahili ushikamanifu wetu?

      15 Fikiria pia ukweli wa kwamba Yehova amefungua njia ili watu wenye mioyo minyoofu watoke, kwa njia ya mfano, katika ulimwengu mwovu, na kuingia katika paradiso ya kiroho ambayo ametokeza. (2 Kor. 12:1-4) Tukiwa na mioyo iliyojaa shukrani, tunabaki karibu na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimweka rasmi juu ya watumishi wake wa nyumbani, awape chakula chao kwa wakati unaofaa.” Kristo amemweka rasmi mtumwa huyo “juu ya mali zake zote.” (Mt. 24:45-47) Kwa hiyo, hata ikiwa sisi binafsi hatuelewi kikamili msimamo fulani wa jamii ya mtumwa, hiyo si sababu ya kukataa jamii hiyo au kurudi tena katika ulimwengu wa Shetani. Badala yake, ushikamanifu utatuchochea kutenda kwa unyenyekevu na kumngojea Yehova afunue mambo waziwazi.

      Wanapotimiza Migawo Ambayo Wamepewa na Mungu

      16. Nabii fulani kutoka Yuda alipewa mgawo gani?

      16 Yehova alimhukumu Yeroboamu kwa sababu ya uasi-imani. Yehova alimtuma nabii fulani kutoka Yuda aende kaskazini mpaka Betheli ili amwone Yeroboamu alipokuwa akifukiza moshi wa dhabihu kwenye madhabahu. Nabii huyo alipaswa kumpa Yeroboamu ujumbe wa hukumu wenye kushtua. Bila shaka, huo ulikuwa mgawo mgumu.—1 Fal. 13:1-3.

      17. Yehova alimlinda mjumbe wake jinsi gani?

      17 Yeroboamu alikasirika sana aliposikia hukumu ya Yehova. Akamnyooshea mkono mwakilishi wa Mungu na kuwapaazia sauti wanaume waliokuwa karibu, akisema: “Mkamateni!” Lakini papo hapo, kabla mtu yeyote hajatenda, ‘mkono aliomnyooshea ukapooza, naye hakuweza kuurudisha nyuma kwake. Na ile madhabahu ikapasuka hivi kwamba majivu yenye mafuta yakamwagika kutoka katika madhabahu.’ Yeroboamu alilazimika kumwomba nabii huyo autulize uso wa Yehova na kusali ili mkono huo uliopooza uponywe. Nabii huyo alifanya hivyo, na mkono ukapona. Hivyo, Yehova alimlinda mjumbe wake asipatwe na madhara.—1 Fal. 13:4-6.

      18. Yehova anatulinda jinsi gani tunapomtolea utumishi mtakatifu bila woga?

      18 Tunaposhiriki kwa ushikamanifu katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi, nyakati nyingine tunakutana na watu wenye ubaridi, au hata wakali. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Lakini hatupaswi kamwe kuruhusu woga wa kupingwa na watu upunguze bidii yetu katika huduma. Kama yule nabii asiyetajwa jina katika siku za Yeroboamu, tuna “pendeleo la kumtolea [Yehova] utumishi mtakatifu bila woga kwa ushikamanifu.”a (Luka 1:74, 75) Ingawa leo hatutazamii tulindwe kimuujiza, bado Yehova anatulinda na kututegemeza tukiwa Mashahidi wake kupitia roho yake takatifu na malaika. (Soma Yohana 14:15-17; Ufunuo 14:6.) Mungu hatawaacha kamwe wale wanaoendelea kusema neno lake bila woga.—Flp. 1:14, 28.

      Yehova Atawalinda Washikamanifu Wake

      19, 20. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova hatatuacha kamwe? (b) Ni maswali gani yatakayozungumziwa katika habari inayofuata?

      19 Yehova ni Mungu wetu mshikamanifu. (Ufu. 15:4; 16:5) Yeye ni “mshikamanifu katika kazi zake zote.” (Zab. 145:17) Na Biblia inatuhakikishia hivi: “Atailinda njia ya washikamanifu wake.” (Met. 2:8) Washikamanifu wa Mungu wanapokabili majaribu au mawazo ya uasi-imani au wanapotimiza mgawo mgumu, wanaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atawaongoza na kuwategemeza.

      20 Jambo ambalo kila mmoja wetu anapaswa kufikiria sasa ni hili: Ni nini kitakachonisaidia kuendelea kuwa mshikamanifu kwa Yehova hata ninapopatwa na majaribu au vishawishi vya aina yoyote? Yaani, ninaweza kuuimarisha jinsi gani ushikamanifu wangu kwa Mungu?

      [Maelezo ya Chini]

      a Makala inayofuata itaonyesha ikiwa nabii huyo aliendelea kumtii Yehova na yale yaliyompata baadaye.

  • Dumisha Ushikamanifu Ukiwa na Moyo Kamili
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Agosti 15
    • Dumisha Ushikamanifu Ukiwa na Moyo Kamili

      “Nitatembea katika kweli yako. Unganisha moyo wangu ili kuliogopa jina lako.”—ZAB. 86:11.

      1, 2. (a) Kulingana na Zaburi 86:2, 11, ni nini kitakachotusaidia kubaki waaminifu kwa Yehova tunapopatwa na majaribu au vishawishi? (b) Tunapaswa kusitawisha ushikamanifu kwa moyo wote wakati gani?

      KWA nini Wakristo fulani ambao wamebaki waaminifu kwa miaka mingi ingawa wamefungwa gerezani au kuteswa, baadaye wanaanza kupenda vitu vya kimwili? Jibu kwa swali hilo linahusiana na moyo wetu wa mfano, yaani, jinsi moyo wetu ulivyo kikweli. Zaburi ya 86 inahusianisha ushikamanifu na moyo uliounganika, yaani, moyo kamili, moyo ambao haujagawanyika. Mtunga-zaburi Daudi alisali hivi: “Uilinde nafsi yangu, kwa maana mimi ni mshikamanifu. Umwokoe mtumishi wako—wewe ni Mungu wangu—anayekutegemea.” Daudi alisali hivi pia: “Unifundishe, Ee Yehova, juu ya njia yako. Nitatembea katika kweli yako. Unganisha moyo wangu ili kuliogopa jina lako.”—Zab. 86:2, 11.

      2 Tusipomtegemea Yehova kwa moyo wetu wote, mahusiano na mahangaiko mengine yatadhoofisha ushikamanifu wetu kwa Mungu wa kweli. Tamaa za kibinafsi ni kama mabomu ya ardhini yaliyotegwa chini ya barabara tunayotembelea. Hata ingawa huenda tumebaki waaminifu kwa Yehova chini ya hali ngumu, tunaweza kunaswa na mitego ya Ibilisi. Ni jambo la maana kama nini kwamba tusitawishe kwa moyo wote ushikamanifu kwa Yehova sasa, kabla hatujapatwa na majaribu au vishawishi! Biblia inasema hivi: “Linda moyo wako kuliko vitu vingine vyote vinavyopaswa kulindwa.” (Met. 4:23) Tunaweza kujifunza masomo ya maana kutokana na yale yaliyompata nabii fulani kutoka Yuda aliyetumwa na Yehova kwa Mfalme Yeroboamu wa Israeli.

      “Nikupe Zawadi”

      3. Yeroboamu alitenda jinsi gani aliposikia ujumbe wa hukumu uliotolewa na nabii wa Mungu?

      3 Fikiria tamasha hii. Mtu wa Mungu ametoka tu kutoa ujumbe mzito kwa Mfalme Yeroboamu, ambaye alianzisha ibada ya ndama katika ufalme wa kaskazini wa Israeli wa makabila kumi. Mfalme anakasirika. Anaamuru wanaume wake wamkamate mjumbe huyo. Lakini Yehova yuko pamoja na mtumishi wake. Papo hapo, mkono ambao mfalme amenyoosha kwa hasira unapooza kimuujiza, na madhabahu inayotumiwa kwa ajili ya ibada ya uwongo inapasuka katika sehemu mbili. Kwa ghafula, mtazamo wa Yeroboamu unabadilika. Anamsihi hivi mtu wa Mungu: “Tafadhali, utulize uso wa Yehova Mungu wako, na kusali kwa ajili yangu ili nirudishiwe mkono wangu.” Nabii huyo anasali, na mkono wa mfalme unapona.—1 Fal. 13:1-6.

      4. (a) Kwa nini mwaliko wa mfalme ulijaribu ushikamanifu wa nabii huyo? (b) Nabii huyo alijibu nini?

      4 Kisha Yeroboamu anamwambia hivi huyo mtu wa Mungu wa kweli: “Njoo pamoja nami twende nyumbani ule chakula, nami nikupe zawadi.” (1 Fal. 13:7) Sasa nabii huyo atafanya nini? Je, akubali ukarimu wa mfalme baada ya kumtangazia ujumbe wa hukumu? (Zab. 119:113) Au akatae mwaliko wa mfalme, hata ingawa mfalme anaonekana ametubu? Bila shaka, Yeroboamu ni tajiri na anaweza kuwapa marafiki wake zawadi za bei ghali. Ikiwa nabii huyo wa Mungu ana tamaa yoyote moyoni mwake kuelekea vitu vya kimwili, inaelekea mwaliko huo wa mfalme utakuwa kishawishi kikubwa kwake. Hata hivyo, Yehova amemwamuru nabii huyo hivi: “Usile mkate wala usinywe maji, nawe usirudi kwa njia ile uliyoiendea.” Kwa hiyo, nabii huyo anajibu hivi kwa uthabiti: “Hata ukinipa nusu ya nyumba yako, siwezi kwenda pamoja nawe na kula mkate au kunywa maji mahali hapa.” Kisha nabii huyo anatoka Betheli kupitia njia nyingine. (1 Fal. 13:8-10) Uamuzi wa nabii huyo unatufundisha somo gani kuhusu ushikamanifu unaotoka moyoni?—Rom. 15:4.

      ‘Uwe Mwenye Kuridhika’

      5. Kupenda vitu vya kimwili kunajaribu ushikamanifu wetu jinsi gani?

      5 Huenda kupenda vitu vya kimwili kusionekane kuwa jambo linalojaribu ushikamanifu wetu, lakini ni jaribu la ushikamanifu. Je, tunaamini ahadi ya Yehova ya kutuandalia mambo ambayo kwa kweli tunahitaji? (Mt. 6:33; Ebr. 13:5) Badala ya kutumia njia yoyote ile ili kupata vitu fulani vya kimwili vyenye kustarehesha ambavyo hatuna uwezo wa kuvipata kwa sasa, je, inawezekana tuishi bila vitu hivyo? (Soma Wafilipi 4:11-13.) Je, tunashawishiwa kuacha mapendeleo ya kitheokrasi ili tupate vitu tunavyotaka sasa? Je, tunatanguliza utumishi mshikamanifu kwa Yehova katika maisha yetu? Majibu yetu yatategemea sana ikiwa tunamtumikia Mungu kwa moyo wetu wote au hapana. Mtume Paulo aliandika hivi: “Ni njia ya kupata faida kubwa, huu ujitoaji-kimungu pamoja na ujitoshelevu. Kwa maana hatukuleta chochote katika ulimwengu, wala hatuwezi kuchukua chochote nje. Kwa hiyo, tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutaridhika na vitu hivyo.”—1 Tim. 6:6-8.

      6. Tunaweza kuahidiwa “zawadi” gani, na ni jambo gani litakalotusaidia kuamua ikiwa tutazikubali?

      6 Kwa mfano, huenda mwajiri wetu wa kazi anataka kutupandisha cheo kazini, kutuongezea mshahara, na kutupa faida nyingine. Au labda tunaona kwamba tunaweza kupata pesa nyingi zaidi ikiwa tutahamia nchi nyingine au eneo lingine ili kupata kazi. Mwanzoni, nafasi hizo zinaweza kuonekana kuwa baraka kutoka kwa Yehova. Lakini kabla ya kufanya uamuzi, tunapaswa kuchunguza nia yetu. Swali kuu tunalopaswa kujiuliza ni: “Uamuzi wangu utakuwa na matokeo gani kuelekea uhusiano wangu pamoja na Yehova?”

      7. Kwa nini ni jambo la maana kung’oa kabisa katika mioyo yetu tamaa ya kupenda vitu vya kimwili?

      7 Mfumo wa Shetani unawatia watu moyo sana kupenda vitu vya kimwili. (Soma 1 Yohana 2:15, 16.) Kusudi la Ibilisi ni kuharibu mioyo yetu. Hivyo, tunahitaji kuwa macho ili kutambua na kung’oa kabisa katika mioyo yetu tamaa ya kupenda vitu vya kimwili. (Ufu. 3:15-17) Yesu alikataa kwa uthabiti falme zote za ulimwengu ambazo Shetani alitaka kumpa. (Mt. 4:8-10) Alionya hivi: “Endeleeni kufungua macho yenu na mjilinde na kila namna ya tamaa, kwa sababu hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.” (Luka 12:15) Ushikamanifu utatusaidia kumtegemea Yehova badala ya kujitegemea wenyewe.

      Nabii Fulani Mzee “Alimdanganya”

      8. Ushikamanifu wa nabii wa Mungu ulijaribiwa jinsi gani?

      8 Mambo yangemwendea vizuri nabii wa Mungu ikiwa angeendelea na safari yake ya kurudi nyumbani. Hata hivyo, punde tu baadaye, alikabili jaribu lingine. Biblia inasema hivi: “Nabii fulani mzee alikuwa akikaa Betheli, na wanawe wakaja na kumsimulia” mambo yote yaliyotendeka mapema siku hiyo. Anaposikia habari hiyo, mwanamume huyo mzee anawaomba wanawe wamtandikie punda ili amfuate nabii wa Mungu. Punde si punde, anamkuta nabii huyo akipumzika chini ya mti mkubwa na kumwambia: “Njoo pamoja nami nyumbani, ule mkate.” Mtu wa Mungu wa kweli anapokataa mwaliko huo, mwanamume huyo mzee anasema: “Mimi pia ni nabii kama wewe, na malaika alisema nami kwa neno la Yehova hivi, ‘Mrudishe pamoja nawe nyumbani kwako ili ale mkate na anywe maji.’” Lakini Maandiko yanasema: “Alimdanganya.”—1 Fal. 13:11-18.

      9. Maandiko yanasema nini kuhusu wadanganyifu, nao wanawadhuru nani?

      9 Hata ingawa hatujui nia ya nabii huyo mzee, ukweli ni kwamba alidanganya. Labda wakati fulani mwanamume huyo mzee alikuwa nabii mwaminifu wa Yehova. Hata hivyo, wakati huu, alikuwa akidanganya. Maandiko yanashutumu vikali mwenendo kama huo. (Soma Methali 3:32.) Wadanganyifu wanaharibu hali yao wenyewe ya kiroho na mara nyingi wanawadhuru wengine kiroho.

      “Akarudi Pamoja” na Yule Mwanamume Mzee

      10. Nabii wa Mungu alitenda jinsi gani alipoalikwa na mwanamume mzee, na matokeo yalikuwa nini?

      10 Nabii huyo kutoka Yuda alipaswa kutambua ujanja wa nabii huyo mzee. Alipaswa kujiuliza, ‘Kwa nini Yehova anamtuma malaika kwa mtu mwingine akiwa na maagizo tofauti kwa ajili yangu?’ Nabii huyo angemwomba Yehova afafanue mwongozo huo waziwazi, lakini Maandiko hayaonyeshi kwamba alifanya hivyo. Badala yake, ‘alirudi pamoja na yule mwanamume mzee ili ale mkate nyumbani kwake na kunywa maji.’ Yehova hakufurahi. Mwishowe, nabii aliyedanganywa alipokuwa njiani akirudi Yuda, alikutana na simba na simba huyo akamuua. Huo ulikuwa mwisho wenye kusikitisha kama nini kwa kazi yake akiwa nabii!—1 Fal. 13:19-25.a

      11. Ahiya aliweka mfano gani mzuri?

      11 Kwa upande mwingine, nabii Ahiya, aliyetumwa kumtia mafuta Yeroboamu ili awe mfalme, alibaki mwaminifu hata alipokuwa mzee. Ahiya alipozeeka na kuwa kipofu, Yeroboamu alimtuma mke wake amuulize Ahiya kuhusu hali ya mwana wao aliyekuwa mgonjwa. Kwa ujasiri, Ahiya alitabiri kwamba mwana wa Yeroboamu angekufa. (1 Fal. 14:1-18) Ahiya alipata baraka nyingi kutia ndani pendeleo la kuchangia habari iliyotumiwa kuandika Neno la Mungu lililoongozwa na roho. Jinsi gani? Baadaye, kuhani Ezra alitumia maandishi ya Ahiya kuwa chanzo cha habari yake.—2 Nya. 9:29.

      12-14. (a) Tunaweza kujifunza somo gani kutokana na yale yaliyompata yule nabii kijana? (b) Toa mifano inayoonyesha uhitaji wa kusali na kufikiria kwa uzito mashauri yanayotegemea Biblia ambayo yanatolewa na wazee.

      12 Biblia haisemi kwa nini nabii huyo kijana hakumuuliza Yehova kabla ya kurudi kula na kunywa pamoja na nabii yule mzee. Je, inawezekana kwamba yule mwanamume mzee alimweleza nabii huyo mambo ambayo alitaka kusikia? Tunapata somo gani hapa? Tunapaswa kusadiki kabisa kwamba matakwa ya Yehova ni ya uadilifu. Na tunapaswa kuazimia kuyafuata kwa vyovyote vile.

      13 Wengine wanataka kusikia tu mashauri ambayo yanawapendeza. Kwa mfano, huenda mhubiri akapewa kazi itakayochukua wakati ambao anaweza kutumia pamoja na familia yake na katika utendaji wa kitheokrasi. Huenda akamwomba mzee wa kutaniko mashauri. Pengine mzee huyo anaweza kuanza kwa kumweleza kwamba si daraka lake kumwambia ndugu huyo jinsi anavyopaswa kuitunza familia yake. Kisha huenda mzee huyo akazungumza na ndugu huyo kuhusu hatari za kiroho zinazohusika katika kukubali kazi ambayo amepewa. Je, ndugu huyo atakumbuka tu maelezo ya kwanza yaliyotolewa na mzee huyo, au atafikiria kwa uzito maelezo ya pili? Ni wazi kwamba ndugu huyo anahitaji kuamua jambo litakalomfaidi zaidi kiroho.

      14 Fikiria mfano mwingine. Huenda dada fulani akamuuliza mzee wa kutaniko ikiwa anapaswa kutengana na mume wake asiyeamini. Bila shaka, mzee atamweleza kwamba ni juu yake kuamua ikiwa atatengana na mume wake. Kisha mzee huyo anaweza kumwonyesha mashauri ya Biblia kuhusu habari hiyo. (1 Kor. 7:10-16) Je, dada huyo atafikiria kwa uzito yale ambayo mzee huyo anasema? Au tayari ameamua kutengana na mume wake? Dada huyo anapofanya uamuzi, itakuwa vizuri kwake kusali na kufikiria mashauri yanayotegemea Biblia.

      Uwe Mwenye Kiasi

      15. Tunajifunza nini kutokana na kosa la nabii wa Mungu?

      15 Tunaweza kujifunza jambo gani lingine kutokana na kosa lililofanywa na yule nabii kutoka Yuda? Andiko la Methali 3:5 linasema hivi: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe.” Badala ya kuendelea kumtegemea Yehova kama alivyofanya wakati uliopita, mara hii nabii huyo kutoka Yuda alitegemea akili zake mwenyewe. Kwa sababu ya kosa hilo, alipoteza uhai wake na uhusiano wake mzuri pamoja na Mungu. Mambo yaliyompata yanakazia vizuri sana umuhimu wa kuwa wenye kiasi na washikamanifu tunapomtumikia Yehova!

      16, 17. Ni nini kitakachotusaidia kubaki washikamanifu kwa Yehova?

      16 Mioyo yetu ina mwelekeo wa kichoyo unaoweza kutupotosha. “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.” (Yer. 17:9) Ili tubaki washikamanifu kwa Yehova, tunapaswa kuendelea kufanya bidii kuvua kabisa utu wa zamani pamoja na mielekeo yake, yaani, kimbelembele na kujitegemea. Na ni lazima tuvae utu mpya, “ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.”—Soma Waefeso 4:22-24.

      17 Andiko la Methali 11:2 linasema kwamba “wenye kiasi wana hekima.” Kuwa wenye kiasi kwa kumtegemea Yehova kunatusaidia kuepuka kutenda makosa yanayoweza kutuletea hasara kubwa sana. Kwa mfano, kuvunjika moyo kunaweza kutuzuia tusifanye maamuzi mazuri. (Met. 24:10) Tunaweza kuchoshwa na sehemu fulani za utumishi mtakatifu na kuanza kuhisi kwamba tumetumikia vya kutosha kwa miaka mingi, na kufikiri kwamba tunapaswa kuwaachia wengine majukumu hayo. Au tunaweza kutamani kuwa na maisha ya “kawaida.” Hata hivyo, ‘tukijitahidi sana’ na tukiwa ‘sikuzote na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana’ tutailinda mioyo yetu.—Luka 13:24; 1 Kor. 15:58.

      18. Tunaweza kufanya nini ikiwa hatujui uamuzi wa kufanya?

      18 Nyakati nyingine, huenda tukahitaji kufanya maamuzi mazito, na huenda tusijue njia nzuri ya kufuata. Basi je, tutashawishiwa kufuata njia yetu wenyewe? Tunapojikuta katika hali kama hizo, ni jambo la hekima kumwomba Yehova atusaidie. Andiko la Yakobo 1:5 linasema hivi: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu.” Baba yetu wa mbinguni atatupa roho takatifu tunayohitaji ili tuweze kufanya maamuzi mazuri.—Soma Luka 11:9, 13.

      Azimia Kubaki Mshikamanifu

      19, 20. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

      19 Katika miaka iliyofuata ya misukosuko, baada ya Sulemani kuacha ibada ya kweli, ushikamanifu wa watumishi wa Mungu ulijaribiwa vikali. Ni kweli kwamba wengi walilegeza msimamo wao kwa njia moja au nyingine. Hata hivyo, wengine walibaki washikamanifu kwa Yehova.

      20 Kila siku, tunakabili maamuzi ambayo yanajaribu ushikamanifu wetu. Sisi pia tunaweza kujithibitisha kuwa waaminifu. Acheni sikuzote tubaki washikamanifu kwa Yehova tunapoendelea kuunganisha moyo wetu, tukiwa na hakika kabisa kwamba ataendelea kuwabariki washikamanifu wake.—2 Sam. 22:26.

      [Maelezo ya Chini]

      a Biblia haisemi ikiwa Yehova alimuua nabii huyo mzee.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki