Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Watazame Wale Waaminifu-Washikamanifu!
    Mnara wa Mlinzi—1996 | Machi 15
    • Watazame Wale Waaminifu-Washikamanifu!

      “Ni nani ambaye kwa kweli hatakuhofu wewe, Yehova, na kulitukuza jina lako, kwa sababu wewe peke yako ni mwaminifu-mshikamanifu?”—UFUNUO 15:4, NW.

      1. Ni ushuhuda gani aliotoa J. F. Rutherford kuhusu uaminifu-mshikamanifu wa mtangulizi wake, C. T. Russell?

      JOSEPH F. RUTHERFORD, aliyemwandama C. T. Russell kuwa msimamizi wa Watch Tower Society katika 1917, alianza hotuba yake katika mkutano wa maziko ya Russell kwa kusema: “Charles Taze Russell alikuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa Mungu, mwaminifu-mshikamanifu kwa Kristo Yesu, mwaminifu-mshikamanifu kwa makusudi ya ufalme wa Mesiya. Alikuwa mwaminifu-mshikamanifu kabisa—ndiyo, mwaminifu-mshikamanifu hadi kifo.” Kwa kweli, hiyo ilikuwa sifa nzuri kwa mtumishi mwaminifu wa Yehova Mungu. Hakuna sifa nzuri tuwezayo kumpa mtu yeyote kuliko kusema kwamba alikabili mtihani wa uaminifu-mshikamanifu, kwamba alikuwa mwaminifu-mshikamanifu—mwaminifu-mshikamanifu kabisa.

      2, 3. (a) Kwa nini uaminifu-mshikamanifu hutokeza mtihani? (b) Ni nani pia wamejipanga dhidi ya Wakristo wa kweli katika jitihada zao za kuwa waaminifu-washikamanifu?

      2 Uaminifu-mshikamanifu ni mtihani mgumu. Kwa nini? Kwa sababu uaminifu-mshikamanifu hupingana na mapendezi ya kibinafsi. Wenye kutokeza sana miongoni mwa watu wasio waaminifu-washikamanifu kwa Mungu ni makasisi wa Jumuiya ya Wakristo. Pia, ukosefu wa uaminifu-mshikamanifu haujapata kamwe kuenea sana kama ulivyoenea katika ndoa leo. Uzinzi ni jambo la kawaida. Ukosefu wa uaminifu-mshikamanifu pia umeenea sana katika ulimwengu wa biashara. Kuhusu jambo hili, twaambiwa hivi: “Meneja na wastadi wengi wa kazi . . . huamini kwamba ni wajinga na mazuzu pekee walio waaminifu-washikamanifu leo.” Watu walio “waaminifu-washikamanifu kupita kiasi” hudharauliwa. “Uaminifu-mshikamanifu wako mkuu na wa pekee wapaswa uwe kwako mwenyewe” ndivyo msimamizi mmoja wa kampuni ya kutoa mashauri juu ya usimamizi wa kazi alivyosema. Hata hivyo, kusema kwamba uaminifu-mshikamanifu uwe kwako mwenyewe ni kupotosha maana ya neno hilo. Kwatukumbusha juu ya yale yaliyosemwa kwenye Mika 7:2 (NW): “Aliye mwaminifu-mshikamanifu ameangamia kutoka duniani.”

      3 Kwa kadiri kubwa zaidi, Shetani na roho wake waovu wamejipanga dhidi yetu, wakiwa wameazimia kuvunja uaminifu-mshikamanifu wetu kwa Mungu. Hiyo ndiyo sababu Wakristo wanaambiwa hivi kwenye Waefeso 6:12: “Kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.” Ndiyo, twahitaji kutii onyo hili: “Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze.”—1 Petro 5:8.

      4. Ni mielekeo gani hufanya uaminifu-mshikamanifu uwe mgumu sana?

      4 Jambo jingine linalofanya uaminifu-mshikamanifu uwe mgumu ni mielekeo ya ubinafsi ambayo tumerithi kutoka kwa wazazi wetu, kama inavyotajwa kwenye Mwanzo 8:21: “Mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya”—na yenye ubinafsi—“tangu ujana wake.” Sisi sote tuna tatizo ambalo mtume Paulo alikiri kuwa nalo: “Lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo.”—Warumi 7:19.

      Uaminifu-Mshikamanifu Ni Jambo la Kipekee

      5, 6. Ni nini laweza kusemwa kuhusu maana ya uaminifu-mshikamanifu, nao umefafanuliwaje?

      5 “Uaminifu-mshikamanifu” ni neno la kipekee sana. Hivyo, Insight on the Scriptures yasema: “Inaonekana hakuna maneno ya Kiingereza yalinganayo kabisa na maneno ya Kiebrania na Kigiriki, lakini neno ‘uaminifu-mshikamanifu,’ kutia ndani wazo la ujitoaji na uaminifu, kama linavyomaanisha, linapotumiwa kuhusiana na Mungu na utumishi wake, latumikia kutoa maana inayolikaribia.”a Kuhusu “uaminifu-mshikamanifu” pindi moja Mnara wa Mlinzi lilisema: “Uaminifu, wajibu, upendo, sharti, utii. Maneno haya yana ufanano gani? Hayo ni maana mbalimbali ya uaminifu-mshikamanifu.” Ndiyo kuna sifa nzuri nyingi ambazo ni maana tofauti-tofauti za uaminifu-mshikamanifu. Ni jambo la maana kuona ni mara ngapi uaminifu-mshikamanifu na uadilifu huhusianishwa katika Maandiko.

      6 Yenye msaada pia ni mafafanuzi yanayofuata: ‘Uaminifu-mshikamanifu waweza kuonyesha uaminifu na utii ulio thabiti na wenye kudumu, usiweze kukengeuka au kushawishika.’ ‘Uaminifu-mshikamanifu wadokeza uaminifu kwa ahadi ambazo mtu hutoa na utii wenye kuendelea kwa kanuni ambazo mtu huona ana wajibu wa kimaadili kutimiza; neno hilo halidokezi ushikamano tu bali ukinzani kwa madanganyo na vishawishi kutoka kwenye ushikamano huo.’ Hivyo, watu wanaoendelea kwa uaminifu wajapopata mitihani, upinzani, na mnyanyaso wastahili kuitwa “waaminifu-washikamanifu.”

      7. Ni tofauti gani inaweza kufanywa kati ya uaminifu-mshikamanifu na uaminifu?

      7 Hata hivyo, kwa habari ya uaminifu-mshikamanifu, ni vema kutoa kielezi cha tofauti iwezayo kufanywa kati ya uaminifu-mshikamanifu na uaminifu. Katika magharibi mwa Marekani, kuna chemchemi moto ambayo hububujisha maji karibu kila muda wa saa moja. Chemchemi hiyo hufanya hivyo kwa ukawaida sana hivi kwamba imeitwa Mkale Mwaminifu. Biblia husema juu ya vitu visivyo na uhai kama mwezi kuwa mwaminifu, kwa sababu unategemeka. Zaburi 89:37 husema juu ya mwezi kuwa “shahidi aliye mbinguni mwaminifu.” Maneno ya Mungu husemwa kuwa ya uaminifu. Ufunuo 21:5 lasema: “Yeye aketiye juu ya kile kiti cha enzi akasema, Tazama, nayafanya yote kuwa mapya. Akaniambia, Andika ya kwamba maneno hayo ni amini [“ya uaminifu,” NW] na kweli.” Vitu hivyo vyote ni vyenye uaminifu, vyenye kutegemeka, lakini havina uwezo wa kuwa na ushikamano wowote au wa kuwa na sifa za maadili, kama vile uaminifu-mshikamanifu.

      Yehova, Mwaminifu-Mshikamanifu Mkuu

      8. Ni ushuhuda gani wa Kimaandiko unaotambulisha kielelezo bora zaidi cha uaminifu-mshikamanifu?

      8 Bila shaka yoyote, Yehova Mungu ndiye kielelezo bora zaidi cha uaminifu-mshikamanifu. Yehova amekuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa jamii ya kibinadamu, hata kutoa Mwana wake ili wanadamu waweze kupata uhai udumuo milele. (Yohana 3:16) Kwenye Yeremia 3:12, twasoma: “Rudi, Ee Israeli mwenye kuasi, asema BWANA; sitakutazama kwa hasira; maana mimi ni mwenye rehema [“mwaminifu-mshikamanifu,” NW].” Yenye kutoa uthibitisho zaidi juu ya uaminifu-mshikamanifu wa Yehova ni maneno yaliyoandikwa kwenye Ufunuo 16:5: “Wewe u mwenye haki [“mwadilifu,” NW] uliyeko na uliyekuwako, Mtakatifu [“Mwaminifu-Mshikamanifu,” NW].” Na tena, kwenye Zaburi 145:17, tunaambiwa: “BWANA ni mwenye haki [“mwadilifu,” NW] katika njia zake zote, na mwenye fadhili [“uaminifu-mshikamanifu,” NW] juu ya kazi zake zote.” Kwa hakika, Yehova ni mwenye kutokeza sana katika uaminifu-mshikamanifu hivi kwamba Ufunuo 15:4 lasema: “Ni nani asiyekucha, Ee Bwana, na kulitukuza jina lako, kwa kuwa wewe peke yako u Mtakatifu [“mwaminifu-mshikamanifu,” NW]?” Yehova Mungu ni mwaminifu-mshikamanifu kwa kiwango cha juu sana.

      9, 10. Ni rekodi gani ya uaminifu-mshikamanifu aliyoweka Yehova katika shughuli zake pamoja na taifa la Israeli?

      9 Historia ya taifa la Israeli hasa ina ushuhuda mwingi sana wa uaminifu-mshikamanifu wa Yehova kwa watu wake. Katika siku za Waamuzi, Israeli liliacha ibada ya kweli kwa kurudia-rudia, lakini kwa kurudia-rudia Yehova alisikitika na kuwaokoa. (Waamuzi 2:15-22) Katika karne zote tano ambazo Israeli lilikuwa na wafalme, Yehova alionyesha uaminifu-mshikamanifu wake kwa taifa hilo.

      10 Uaminifu-mshikamanifu wa Yehova ulimfanya awe mwenye subira na watu wake, kama ionyeshwavyo kwenye 2 Mambo ya Nyakati 36:15, 16: “BWANA, Mungu wa baba zao, akatuma kwao kwa mikono ya wajumbe wake, akiondoka mapema, na kutuma; kwa sababu aliwahurumia watu wake, na makao yake; lakini waliwadhihaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake, na kuwacheka manabii wake, hata ilipozidi ghadhabu ya BWANA juu ya watu wake, hata kusiwe na kuponya.”

      11. Ni uhakikisho upi au faraja ipi ambayo uaminifu-mshikamanifu wa Yehova hutupa?

      11 Kwa sababu Yehova ni mwaminifu-mshikamanifu kabisa, mtume Paulo aliweza kuandika, kama ilivyorekodiwa kwenye Warumi 8:38, 39: “Nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.” Ndiyo, Yehova atuhakikishia: “Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa.” (Waebrania 13:5) Kwelikweli, inafariji kujua kwamba sikuzote Yehova Mungu ni mwaminifu-mshikamanifu!

      Yesu Kristo, Mwana Aliye Mwaminifu-Mshikamanifu

      12, 13. Tuna ushuhuda gani kuhusu uaminifu-mshikamanifu wa Mwana wa Mungu?

      12 Mwenye kumwiga Yehova kikamilifu katika kukabili mtihani wa uaminifu-mshikamanifu alikuwa na angali Yesu Kristo. Kwa kufaa, mtume Petro aliweza kunukuu Zaburi 16:10 na kulitumia kuhusu Yesu Kristo kwenye Matendo 2:27 (NW): “Hutaacha nafsi yangu katika Hadesi, wala hutaruhusu mwaminifu-mshikamanifu wako aone uharibifu.” Kwa kustahili Kristo Yesu anaitwa “mwaminifu-mshikamanifu.” Yeye ni mwaminifu-mshikamanifu kabisa, yeye ni mwaminifu-mshikamanifu kwa Baba yake na kwa Ufalme wa Mungu ulioahidiwa. Kwanza Shetani alijaribu kuvunja uaminifu-maadili wa Yesu kwa kutumia vishawishi, na kuvutia upendezi wake wa kibinafsi. Kwa kuwa Ibilisi alishindwa, aligeukia mnyanyaso, hatimaye akisababisha kifo cha Yesu kwenye mti wa kufisha. Yesu hakukengeuka kamwe kutoka kwenye uaminifu-mshikamanifu wake kwa Baba yake wa kimbingu, Yehova Mungu.—Mathayo 4:1-11.

      13 Yesu Kristo amekuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa wafuasi wake kwa kupatana na ahadi iliyoandikwa kwenye Mathayo 28:20: “Tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari.” Kwa utimizo wa ahadi hiyo, yeye amekuwa akitekeleza uongozi kwa uaminifu-mshikamanifu juu ya kutaniko lake tangu Pentekoste ya 33 W.K. hadi wakati huu.

      Wanadamu Wasiokamilika Waliokuwa Waaminifu-Washikamanifu

      14. Ni kielelezo gani cha uaminifu-mshikamanifu alichoweka Ayubu?

      14 Sasa, vipi juu ya wanadamu wasiokamilika? Je, wao waweza kuwa waaminifu-washikamanifu kwa Mungu? Tuna kisa chenye kutokeza cha Ayubu. Shetani alifanya suala hili liwe wazi kabisa. Je, Ayubu alikuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa Yehova Mungu, au alikuwa akimtumikia kwa sababu ya upendezi wake wa kibinafsi pekee? Shetani alijigamba kwamba yeye angeweza kumgeuza Ayubu kutoka kwa Yehova kwa kumletea Ayubu matatizo. Ayubu alipopoteza mali zake zote, watoto wake wote, na hata afya yake, mke wake alimhimiza hivi: “Umkufuru Mungu, ukafe.” Lakini Ayubu alikuwa mwaminifu-mshikamanifu, kwa kuwa alimwambia: “Wewe wanena kama mmoja wa hao wanawake wapumbavu anenavyo. Je! tupate mema mkononi mwa Mungu, nasi tusipate na mabaya? Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi kwa midomo yake.” (Ayubu 2:9, 10) Hata Ayubu aliwaambia wale ambao wangekuwa wafariji wake hivi: “Hata yeye [Mungu] aniue, bado nitamtumaini.” (Ayubu 13:15, New International Version) Si ajabu kwamba Ayubu alipokea kibali cha Yehova! Hivyo, Yehova alimwambia Elifazi Mtemani: “Hasira zangu zinawaka juu yako, na juu ya hao rafiki zako wawili; kwa kuwa ninyi hamkunena yaliyo sawa katika habari zangu, kama alivyonena mtumishi wangu Ayubu.”—Ayubu 42:7, 10-16; Yakobo 5:11.

      15. Tuna ushuhuda gani wa Kimaandiko kuhusu uaminifu-mshikamanifu wa watumishi wengi wa Yehova Mungu?

      15 Wanaume na wanawake wote wenye imani wanaofafanuliwa katika Waebrania sura ya 11 waweza kutajwa kuwa waaminifu-washikamanifu. Wao hawakuwa waaminifu tu bali walikuwa pia waaminifu-washikamanifu walipokabili mikazo. Hivyo, twasoma juu ya wale “ambao kwa imani . . . walifunga vinywa vya simba, walizima nguvu za moto, waliokoka na makali ya upanga . . . Wengine walijaribiwa kwa dhihaka na mapigo, naam, kwa mafungo, na kwa kutiwa gerezani; walipigwa kwa mawe, walikatwa kwa misumeno, walijaribiwa, waliuawa kwa upanga; walizunguka-zunguka wakivaa ngozi za kondoo na ngozi za mbuzi; walikuwa wahitaji, wakiteswa, wakitendwa mabaya.”—Waebrania 11:33-37.

      16. Mtume Paulo aliweka kielelezo gani cha uaminifu-mshikamanifu?

      16 Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo pia huandaa kielelezo chenye kutokeza cha mtume Paulo. Kwa kufaa aliweza kuwaambia Wakristo wa Thesalonike kuhusu huduma yake: “Ninyi ni mashahidi, na Mungu pia, jinsi tulivyokaa kwenu ninyi mnaoamini, kwa utakatifu [“uaminifu-mshikamanifu,” NW] na kwa haki [“uadilifu,” NW] bila kulaumiwa.” (1 Wathesalonike 2:10) Tuna uthibitisho zaidi wa uaminifu-mshikamanifu wa Paulo katika maneno yake yaliyoandikwa kwenye 2 Wakorintho 6:4, 5, ambapo twasoma hivi: “Katika kila neno tujipatie sifa njema, kama watumishi wa Mungu; katika saburi nyingi, katika dhiki, katika misiba, katika shida; katika mapigo, katika vifungo, katika fitina, katika taabu, katika kukesha, katika kufunga.” Haya yote yatoa ushuhuda juu ya kujistahi kwa mtume Paulo kwa sababu alikuwa mwaminifu-mshikamanifu.

      Waaminifu-Washikamanifu Katika Nyakati za Kisasa

      17. Ni maneno yapi ya J. F. Rutherford yaliyoonyesha azimio lake la kuwa mwaminifu-mshikamanifu?

      17 Kuhusu nyakati za kisasa, tuna kielelezo kizuri ambacho tayari tumeona katika utangulizi wetu. Ona yale yaliyosemwa katika kitabu Usalama Ulimwenguni Pote Chini ya “Mwana-Mfalme wa Amani,” kwenye ukurasa 146 chini ya kichwa-kidogo “Ushikamanifu [Uaminifu-Mshikamanifu] Wakati wa Kufungwa Gerezani.” Hapo palisema hivi: “Akionyesha ushikamanifu [uaminifu-mshikamanifu] kwa tengenezo la Yehova wakati wa kifungo chake gerezani, msimamizi wa [Watch Tower Society], Joseph F. Rutherford, Desemba 25, 1918, aliandika yafuatayo: ‘Kwa sababu mimi nilikataa kukubaliana na Babuloni, lakini kwa uaminifu nikajaribu kumtumikia Bwana yangu, nimo gerezani, na kwa ajili ya hilo nashukuru. . . . Mimi ningependelea zaidi kibali Chake na tabasamu na kuwa gerezani, kuliko kukubaliana au kukubali kushindwa na yule Mnyama na kuwa huru na kusifiwa na ulimwengu wote.’”b

      18, 19. Tuna vielelezo gani vizuri sana vya uaminifu-mshikamanifu katika nyakati za kisasa?

      18 Tuna vielelezo bora vya uaminifu-mshikamanifu vya Wakristo wengine ambao wamevumilia mnyanyaso. Miongoni mwa watu waaminifu-washikamanifu hivyo mna Mashahidi wa Yehova Wajerumani wakati wa utawala wa Nazi, kama ionyeshwavyo katika vidio Purple Triangles, iliyoenezwa sana katika lugha ya Kiingereza. Wenye kutokeza pia ni Mashahidi wengi wa Yehova Waafrika wenye uaminifu-mshikamanifu, kama wale walio Malawi. Huko, mlinzi mmoja wa gereza alitoa ushuhuda juu ya uaminifu-mshikamanifu wa Mashahidi, akisema: “Wao hawataridhiana kamwe. Wanaongezeka tu.”

      19 Mtu hawezi kukosa kusoma Vitabu-Mwaka vya Mashahidi wa Yehova vya majuzi bila kuvutiwa na uaminifu-mshikamanifu ulioonyeshwa na Wakristo wa kweli, kama vile wale walio katika Ugiriki, Msumbiji, na Poland. Wengi wao walivumilia mateso yenye uchungu mno; wengine waliuawa kimakusudi. Ukurasa 177 wa Kitabu-Mwaka cha 1994 unaonyesha picha za wanaume tisa Wakristo katika Ethiopia waliokabili mtihani wa uaminifu-mshikamanifu kufikia hatua ya kuuawa kimakusudi. Tukiwa Mashahidi wa Yehova, je, hatufurahi kuwa na vielelezo vingi vya kutuchochea kukabili mtihani wa uaminifu-mshikamanifu?

      20. Ni nini kitakachofuata tukibaki waaminifu-washikamanifu?

      20 Kwa kukinza kwa uaminifu-mshikamanifu vishawishi na mikazo, sisi hujistahi. Basi, tunataka kuwa upande wa nani katika suala la uaminifu-mshikamanifu? Kwa kukabili mtihani wa uaminifu-mshikamanifu, sisi huchukua upande wa Yehova Mungu wa suala hilo na kumthibitisha Shetani Ibilisi kuwa mwovu mwenye uwongo mtupu! Kwa kufanya hivyo twapata kibali cha Mfanyi wetu, Yehova Mungu, na thawabu ya uhai udumuo milele katika furaha. (Zaburi 37:29; 144:15b) Jambo linalohitajiwa kukabili mtihani wa uaminifu-mshikamanifu litafuata kuzungumziwa.

  • Kukabili Mtihani wa Uaminifu-Mshikamanifu
    Mnara wa Mlinzi—1996 | Machi 15
    • Kukabili Mtihani wa Uaminifu-Mshikamanifu

      “Mvae utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.”—WAEFESO 4:24, NW.

      1. Kwa nini tuna wajibu wa kuwa waaminifu-washikamanifu kwa Yehova Mungu?

      KUKABILI mtihani wa uaminifu-mshikamanifu kuna pande nyingi. Muhimu zaidi ya yote ni kukabili mtihani wa uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova Mungu. Kwelikweli, kwa kufikiria Yehova ni nani na yale ambayo ametufanyia, na kwa sababu ya wakfu wetu kwake, tuna wajibu wa kuwa waaminifu-washikamanifu kwake. Twaonyeshaje uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova Mungu? Njia kuu ni kwa kuwa waaminifu-washikamanifu kwa kanuni zenye uadilifu za Yehova.

      2, 3. Kuna uhusiano gani kati ya uaminifu-mshikamanifu na uadilifu?

      2 Ili kukabili mtihani huo, ni lazima tutii maneno yapatikanayo kwenye 1 Petro 1:15, 16 (NW): “Kwa kupatana na Mtakatifu aliyewaita, nyinyi wenyewe pia iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote, kwa sababu imeandikwa: ‘Lazima mwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.’” Uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova Mungu utatufanya tumtii sikuzote, tukifanya mawazo, maneno, na matendo yetu yapatane na mapenzi yake matakatifu. Wamaanisha kuhifadhi dhamiri njema, kama tunavyoamriwa kwenye 1 Timotheo 1:3-5: “Mwisho wa agizo hilo [la kutofundisha fundisho tofauti au kusikiliza hadithi bandia] ni upendo utokao katika moyo safi na dhamiri njema, na imani isiyo na unafiki.” Ni kweli kwamba hakuna mmoja wetu aliyekamilika, lakini twapaswa tuwe tukijaribu kadiri tuwezavyo, sivyo?

      3 Uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova utatuzuia tusiridhiane kwa ubinafsi kanuni zenye uadilifu. Kwa kweli, uaminifu-mshikamanifu utatuzuia tusiwe wanafiki. Mtunga-zaburi alikuwa akifikiria uaminifu-mshikamanifu alipoimba hivi: “Ee BWANA, unifundishe njia yako; nitakwenda katika kweli yako; moyo wangu na ufurahi kulicha jina lako.” (Zaburi 86:11) Uaminifu-mshikamanifu wataka kile ambacho kwa kufaa kimefafanuliwa kuwa “utii kwa mambo yasiyoweza kutekelezwa.”

      4, 5. Uaminifu-mshikamanifu utatufanya tuwe waangalifu tusifanye nini?

      4 Uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova Mungu pia utatuzuia tusifanye jambo lolote liwezalo kuletea jina lake na Ufalme wake suto. Kwa kielelezo, pindi moja Wakristo wawili walitatizana sana hivi kwamba wakachukua hatua isiyofaa ya kupelekana katika mahakama ya kilimwengu. Hakimu aliuliza, ‘Je, nyote wawili ni Mashahidi wa Yehova?’ Kwa wazi hakuelewa ni kwa nini walienda mahakamani. Hilo lilikuwa suto kama nini! Uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova Mungu ungewafanya ndugu hao watii shauri hili la Paulo: “Basi imekuwa upungufu kwenu kabisa kwamba mnashitakiana ninyi kwa ninyi. Maana si afadhali kudhulumiwa? Maana si afadhali kunyang’anywa mali zenu?” (1 Wakorintho 6:7) Hakika, mwendo wa uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova Mungu ni mtu mwenyewe kupata hasara badala ya kuletea Yehova na tengenezo lake suto.

      5 Uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova Mungu pia huhusisha kutoshindwa na hali ya kuhofu mwanadamu. “Kuwaogopa wanadamu huleta mtego; bali amtumainiye BWANA atakuwa salama.” (Mithali 29:25) Hivyo, haturidhiani tunapokabiliwa na mnyanyaso, lakini twafuata kielelezo kilichowekwa na Mashahidi wa Yehova katika ule uliokuwa Muungano wa Sovieti, katika Malawi, katika Ethiopia, na katika nchi nyinginezo nyingi.

      6. Uaminifu-mshikamanifu utatuzuia tusishirikiane na nani?

      6 Tukiwa waaminifu-washikamanifu kwa Yehova Mungu, tutaepuka kufanya urafiki na wale wote ambao ni adui zake. Hiyo ndiyo sababu mwanafunzi Yakobo aliandika: “Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.” (Yakobo 4:4) Tunataka kuwa na uaminifu-mshikamanifu ambao Mfalme Daudi alionyesha aliposema hivi: “Je! BWANA nisiwachukie wanaokuchukia? Nisikirihike nao wakuasio? Nawachukia kwa ukomo wa chuki, wamekuwa adui kwangu.” (Zaburi 139:21, 22) Hatutaki kuchangamana na watu wowote watendao dhambi kimakusudi, kwa kuwa hakuna jambo la kutushirikisha nao. Je, uaminifu-mshikamanifu kwa Mungu hautatuzuia kuchangamana na maadui wowote wa Yehova kama hao, wawe ni watu au iwe ni televisheni?

      Kumtetea Yehova

      7. Uaminifu-mshikamanifu utatusaidia tufanye nini kwa habari ya Yehova, naye Elihu alifanyaje hivyo?

      7 Uaminifu-mshikamanifu utatusukuma tumtetee Yehova Mungu. Tuna kielelezo kizuri kama nini cha Elihu! Ayubu 32:2, 3 (NW), latuambia: “Hasira ya Elihu . . . ikawaka. Dhidi ya Ayubu hasira yake iliwaka kwa sababu alitangaza nafsi yake mwenyewe kuwa yenye uadilifu kuliko Mungu. Pia, hasira yake iliwaka dhidi ya waandamani wake watatu juu ya jambo la kwamba hawakupata jibu lakini waliendelea kumtangaza Mungu kuwa mwovu.” Katika Ayubu sura 32 hadi 37, Elihu amtetea Yehova. Kwa kielelezo, yeye alisema hivi: “Ningojee kidogo nami nitakueleza; kwa kuwa nikali na maneno kwa ajili ya Mungu. . . . Nitampa haki Muumba wangu. . . . Yeye hawaondolei macho yake wenye haki.”—Ayubu 36:2-7.

      8. Kwa nini tunahitaji kumtetea Yehova?

      8 Kwa nini kuna uhitaji wa kumtetea Yehova? Leo, Mungu wetu Yehova anakufuriwa katika njia nyingi sana. Yadaiwa kwamba hayupo, kwamba yeye ni sehemu ya Utatu, kwamba yeye hutesa watu milele katika helo yenye kuwaka moto, kwamba anajaribu kihafifu kubadili ulimwengu, kwamba hajali wanadamu, na kadhalika. Sisi huonyesha uaminifu-mshikamanifu kwake kwa kumtetea na kuthibitisha kwamba kwa kweli Yehova yupo; kwamba yeye ni mwenye hekima, haki, mwenye uweza, na Mungu mwenye upendo; kwamba ameweka wakati wa kila kitu; na kwamba wakati wake uwadiapo, yeye atakomesha uovu wote na kufanya dunia yote iwe paradiso. (Mhubiri 3:1) Hilo lamaanisha kwamba tutumie kila fursa kutoa ushahidi kwa jina la Yehova na Ufalme wake.

      Uaminifu-Mshikamanifu kwa Tengenezo la Yehova

      9. Ni juu ya masuala gani wengine walionyesha ukosefu wa uaminifu-mshikamanifu?

      9 Sasa twafikia jambo la kuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa tengenezo linaloonekana la Yehova. Hakika, tuna wajibu wa kuwa waaminifu-washikamanifu kwalo, kutia ndani “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” ambaye kupitia kwake, kutaniko la Kikristo linalishwa kiroho. (Mathayo 24:45-47) Tuseme jambo fulani latokea katika vichapo vya Watch Tower ambalo hatulielewi au kukubaliana nalo kwa wakati huu. Tutafanya nini? Tuudhike na kuacha tengenezo? Hivyo ndivyo wengine walivyofanya miaka mingi iliyopita wakati The Watch Tower lilipotaja kwamba lile agano jipya lilitumika wakati wa Mileani. Wengine waliudhika na jambo ambalo wakati mmoja Mnara wa Mlinzi lilisema juu ya suala la kutokuwamo. Wale waliokwazwa na mambo hayo wangalikuwa waaminifu-washikamanifu kwa tengenezo na kwa ndugu zao, wangalimngoja Yehova kuelewesha wazi mambo hayo, na ndivyo alivyofanya kwa wakati wake. Hivyo, uaminifu-mshikamanifu hutia ndani kungoja kwa subira mpaka uelewevu zaidi utangazwe na mtumwa mwaminifu mwenye akili.

      10. Uaminifu-mshikamanifu utatusaidia tusiwe wadadisi kuhusu nini?

      10 Uaminifu-mshikamanifu kwa tengenezo lionekanalo la Yehova pia wamaanisha kukataa katakata waasi-imani. Wakristo waaminifu-washikamanifu hawapaswi kudadisi yale ambayo watu hawa wanasema. Ni kweli kwamba wale ambao Yehova Mungu anawatumia kuelekeza kazi yake duniani si wakamilifu. Lakini Neno la Mungu latuambia tufanye nini? Tuache tengenezo la Mungu? La. Shauku ya kidugu inapaswa kutufanya tuwe waaminifu-washikamanifu kwalo, nasi twapaswa kuendelea “kupendana kwa moyo.”—1 Petro 1:22.

      Uaminifu-Mshikamanifu kwa Wazee Waaminifu-Washikamanifu

      11. Uaminifu-mshikamanifu utatulinda dhidi ya fikira gani hasi?

      11 Jambo fulani lisemwapo au kufanywa kutanikoni ambalo hatuelewi vizuri, uaminifu-mshikamanifu utatuzuia tusihukumu-hukumu mambo nao utatusaidia kuona kwamba labda hilo ni jambo la uamuzi. Je, si afadhali sana kufikiria sifa nzuri za wazee waliowekwa rasmi kutanikoni na waamini wenzetu wengine badala ya kufikiria mapungufu yao? Ndiyo twataka kulinda dhidi ya fikira hasi kama hizo, kwa kuwa zinahusiana na kukosa uaminifu-mshikamanifu! Uaminifu-mshikamanifu pia utatusaidia kutii mwelekezo wa Paulo wa ‘kutosema kwa ubaya juu ya yeyote.’—Tito 3:1, 2, NW.

      12, 13. Ni mitihani gani hasa wazee hulazimika kukabili?

      12 Uaminifu-mshikamanifu hutokeza mtihani hususa kwa wazee. Mojawapo mitihani hiyo ni suala la kuweka siri. Mshiriki wa kutaniko aweza kusema na mzee mambo yake ya siri. Uaminifu-mshikamanifu kwa huyo utamzuia huyo mzee asivunje kanuni ya kuweka siri. Yeye atatii shauri lipatikanalo kwenye Mithali 25:9: “Usiifunue siri ya mtu mwingine.” Hilo lamaanisha kutofunua jambo hilo hata kwa mke wake!

      13 Wazee pia wanakabili mitihani mingine ya uaminifu-mshikamanifu. Je, wao watakuwa wapendeza-watu, au wao watasaidia kwa moyo mkuu na kwa upole wale wanaohitaji kusahihishwa, hata kama hawa ni watu wa ukoo au marafiki wa karibu? Uaminifu-mshikamanifu kwa tengenezo la Yehova utasaidia wale miongoni mwetu ambao ni wazee kujaribu kusaidia yeyote anayehitaji msaada wa kiroho. (Wagalatia 6:1, 2) Ingawa tutakuwa wenye fadhili, uaminifu-mshikamanifu utatufanya tuwe wanyoofu kwa wazee wenzetu, kama vile Paulo alivyosema na mtume Petro kwa unyoofu. (Wagalatia 2:11-14) Kwa upande mwingine, waangalizi wanataka kuwa waangalifu, isije ikawa kwamba kwa kutenda bila hekima au kwa kubagua au wakitumia vibaya mamlaka yao kwa njia fulani, wanafanya iwe vigumu kwa wale walio chini yao kuwa waaminifu-washikamanifu kwa tengenezo la Mungu.—Wafilipi 4:5.

      14, 15. Ni mambo gani yawezayo kutahini uaminifu-mshikamanifu wa washiriki wa kutaniko?

      14 Kuna pande nyinginezo za suala la kukabili mtihani wa uaminifu-mshikamanifu kwa kutaniko na wazee walo. Iwapo kwa njia fulani kuna matatizo katika kutaniko, hilo hutupa fursa ya kuonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova na kwa wale wanaomwakilisha. (Ona Mnara wa Mlinzi, Juni 15, 1987, kurasa 15-17.) Ikiwa mtu ametengwa na ushirika, uaminifu-mshikamanifu wataka kwamba tuunge mkono wazee, si kujaribu kufikiria kama kulikuwa na sababu za kutosha zilizofanya hatua hiyo ichukuliwe.

      15 Uaminifu-mshikamanifu kwa kutaniko pia wataka tuunge mkono mikutano yote mitano ya kila juma kwa kadiri hali na uwezo wetu uruhusuvyo. Uaminifu-mshikamanifu wataka kwamba tusihudhurie tu mikutano hiyo kwa ukawaida bali pia kujitayarisha na kutoa maelezo yenye kujenga kadiri hali iruhusuvyo.—Waebrania 10:24, 25.

      Uaminifu-Mshikamanifu wa Ndoa

      16, 17. Ni mitihani gani ya uaminifu-mshikamanifu Wakristo waliofunga ndoa hulazimika kukabili?

      16 Ni kwa nani pia tuna wajibu wa kuwa waaminifu-washikamanifu? Ikiwa tumefunga ndoa, kwa kupatana na nadhiri zetu za ndoa, ni lazima tukabili mtihani wa kuwa waaminifu-washikamanifu kwa mwenzi wetu wa ndoa. Uaminifu-mshikamanifu kwa mwenzi wetu wa ndoa utatuzuia tusifanye kosa la kuwa wema zaidi kwa wanawake au wanaume wengine kuliko tulivyo kwa mke au mume wetu mwenyewe. Uaminifu-mshikamanifu kwa wenzi wetu pia wataka tusifunulie wengine udhaifu na mapungufu ya mwenzi wetu wa ndoa. Ni rahisi zaidi kulalamika kuliko kujitahidi kudumisha hali nzuri ya mawasiliano na mwenzi wetu wa ndoa, ambako tunapaswa kufanya kwa kupatana na Kanuni Bora. (Mathayo 7:12) Hakika, ndoa hutokeza mtihani mgumu kwa uaminifu-mshikamanifu wetu wa Kikristo.

      17 Ili kukabili mtihani huu wa uaminifu-mshikamanifu, ni lazima tuepuke kuwa na hatia ya mwenendo mbaya sana na vilevile ni lazima tulinde dhidi ya mawazo na hisia zetu wenyewe. (Zaburi 19:14) Kwa mfano, mioyo yetu yenye hila ikiwa na pupa ya raha na msisimuko, ni rahisi sana kwetu kwa ubinafsi kuacha kupenda kitu na kuanza kukitamani. Akihimiza uaminifu katika ndoa kwa njia ya kitamathali, Mfalme Sulemani ashauri waume ‘wanywe maji ya birika lao wenyewe.’ (Mithali 5:15) Na Yesu alisema: “Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake.” (Mathayo 5:28) Waume wanaojiingiza katika vitu vya kiponografia hujihatarisha kushawishika kufanya uzinzi, hivyo wakitendea wake zao kwa udanganyifu na kukosa uaminifu-mshikamanifu kwao. Kwa hali iyo hiyo, mke anayefuatia sana vipindi vya kuendelezwa vyenye kuhusika na hali za uzinzi anaweza kushawishika kukosa uaminifu-mshikamanifu kwa mume wake. Hata hivyo, kwa kuwa waaminifu-washikamanifu kwelikweli kwa mwenzi wetu wa ndoa, twaimarisha vifungo vya ndoa, na kusaidiana katika jitihada zetu za kumpendeza Yehova Mungu.

      Misaada ya Kudumisha Uaminifu-Mshikamanifu

      18. Kujua nini kutatusaidia kuwa waaminifu-washikamanifu?

      18 Ni nini kitakachotusaidia kukabili mtihani wa kuwa waaminifu-washikamanifu katika sehemu hizo nne: uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova, kwa tengenezo lake, kwa kutaniko, na kwa mwenzi wetu wa ndoa? Msaada mmoja ni kujua kwamba kukabili mtihani wa uaminifu-mshikamanifu kunahusiana kwa ukaribu na kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova. Ndiyo, kwa kubaki tukiwa waaminifu-washikamanifu twaonyesha kwamba twamwona Yehova kuwa Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote Mzima. Hivyo twaweza pia kujistahi na kuwa na tumaini la uhai udumuo milele katika ulimwengu mpya wa Yehova. Twaweza kujisaidia tubaki tukiwa waaminifu-washikamanifu kwa kufikiria vielelezo vizuri vya uaminifu-mshikamanifu, tokea Yehova hadi wale wanaotajwa katika Biblia na katika vichapo vyetu vya Watch Tower, kutia ndani masimulizi ya Yearbook.

      19. Imani hutimiza fungu gani katika kuwa kwetu waaminifu-washikamanifu?

      19 Imani yenye nguvu kwa Yehova Mungu na hofu ya kutompendeza itatusaidia kukabili mtihani wa uaminifu-mshikamanifu. Tunaimarisha imani yetu katika Yehova na katika kumhofu kwa kujifunza Neno la Mungu kwa bidii na kwa kushiriki katika huduma ya Kikristo. Hilo litatusaidia kutenda kwa kupatana na shauri la Paulo lililorekodiwa kwenye Waefeso 4:23, 24 (NW): “Mfanywe upya katika kani inayotendesha akili yenu, na mvae utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.”

      20. Zaidi ya yote, ni sifa gani itatusaidia kuwa waaminifu-washikamanifu kwa Yehova na kwa wengine wote ambao tuna wajibu wa kuwaonyesha uaminifu-mshikamanifu?

      20 Uthamini wa sifa za Yehova hutusaidia kuwa waaminifu-washikamanifu. Zaidi ya yote, upendo usio na ubinafsi kwa Baba yetu wa kimbingu na shukrani kwa yale yote ambayo ametufanyia, kumpenda kwa moyo wetu wote na nafsi yetu yote na akili yetu yote kutatusaidia kuwa waaminifu-washikamanifu kwake. Isitoshe, kuwa na upendo ambao Yesu alisema ungetambulisha wafuasi wake utatusaidia kuwa waaminifu-washikamanifu kwa Wakristo wote katika kutaniko na katika familia yetu. Kwa maneno mengine, ni jambo la kuwa ama mwenye ubinafsi ama kutokuwa na ubinafsi. Ukosefu wa uaminifu-mshikamanifu wamaanisha kuwa mwenye ubinafsi. Uaminifu-mshikamanifu wamaanisha kutokuwa na ubinafsi.—Marko 12:30, 31; Yohana 13:34, 35.

      21. Jambo la kukabili mtihani wa uaminifu-mshikamanifu laweza kusemwaje kwa ufupi?

      21 Kwa ufupi: Uaminifu-mshikamanifu ni sifa nzuri sana ionyeshwayo na Yehova Mungu, na Yesu Kristo, na watumishi wote wa kweli wa Yehova. Ili kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova Mungu, ni lazima tukabili mtihani wa uaminifu-mshikamanifu kwake kwa kuishi kupatana na matakwa yake yenye uadilifu, kwa kukataa katakata kushirikiana na adui zake, na kwa kumtetea Yehova katika kutoa ushahidi kirasmi na kivivi-hivi. Ni lazima pia tukabili mtihani wa kuwa waaminifu-washikamanifu kwa tengenezo lionekanalo la Yehova. Ni lazima tuwe waaminifu-washikamanifu kwa makutaniko yetu na kuwa waaminifu-washikamanifu kwa wenzi wetu wa ndoa. Kwa kukabili mtihani wa uaminifu-mshikamanifu kwa mafanikio, tunashiriki katika kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova, nasi tunachukua upande wake katika hilo suala. Kwa kufanya hivyo atatupendelea nasi tutapokea thawabu ya uhai udumuo milele. Yale aliyosema mtume Paulo kuhusu ujitoaji kimungu yaweza kusemwa pia kuhusu kukabili kwetu mtihani wa uaminifu-mshikamanifu. Wafaa kwa maisha ya sasa na yale yajayo.—Zaburi 18:25; 1 Timotheo 4:8.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki