-
Ulimwengu Wenye Maoni Yaliyopotoka Kuhusu UaminifuMnara wa Mlinzi—2002 | Agosti 15
-
-
Ulimwengu Wenye Maoni Yaliyopotoka Kuhusu Uaminifu
IJUMAA moja jioni, kijana mmoja alijiunga na vijana waliokuwa wakisubiri kuingia katika klabu moja ya usiku huko Tel Aviv, Israel. Muda mfupi baadaye, kulitokea mlipuko mkubwa sana katikati ya umati huo.
Mlipuaji mwingine aliyejitolea kufa alijiua na kuwaua vijana wengine 19 kikatili. “Viungo vya miili ya vijana hao vilitapakaa kila mahali. Wote walikuwa wachanga sana. Sijapata kushuhudia tukio lenye kutisha kama hilo,” daktari mmoja akawaambia waandishi wa habari baadaye.
Mwandishi Thurstan Brewin aliandika hivi katika kichapo The Lancet: ‘Sifa kama vile uaminifu, ambayo huvutia kila mtu, inaweza kusababisha vita na kufanya iwe vigumu kukomesha vita.’ Naam, kuanzia Krusedi za Jumuiya ya Wakristo hadi mauaji ya halaiki yaliyopangwa na kutekelezwa na Ujerumani ya Nazi, watu wengi sana wameuawa na watu ambao walitaka tu kuthibitisha uaminifu wao kwa dini zao au vyama vyao vya kisiasa.
Watu Wanazidi Kuathiriwa na Ukosefu wa Uaminifu
Ni kweli kwamba uaminifu unaoonyeshwa pasipo kufikiri ni hatari. Hata hivyo, kutokuwa waaminifu kunaweza kuangamiza jamii. Kuwa mwaminifu kunamaanisha kuwa mtiifu kwa mtu au harakati fulani na hudokeza hali ya kushikamana kabisa na mtu huyo hata unaposhawishiwa kumwacha au kumsaliti. Ingawa watu wengi husema kwamba wanavutiwa na uaminifu wa aina hiyo, jamii inateseka sana kwa sababu ya ukosefu wa uaminifu katika familia. Talaka zimeongezeka sana kwa sababu ya watu kutaka kujitosheleza, mikazo na misongo ya maisha, na matokeo ya kukosa uaminifu katika ngono. Kama wale vijana waliokufa baada ya kulipuliwa na bomu huko Tel Aviv, mara nyingi vijana wasio na hatia ndio huumia.
Ripoti moja inasema kwamba “mara nyingi elimu ya mtoto huathiriwa na mvurugo katika familia ambao husababishwa na talaka, mtengano, au kulelewa na mzazi mmoja.” Wavulana katika familia ambazo mama ndiye mzazi pekee hukabili hatari ya kukosa elimu, kujiua, na kuhusika katika uhalifu wakiwa wadogo. Kila mwaka, watoto milioni moja nchini Marekani huathiriwa na talaka ya wazazi wao. Kwa mwaka wowote ule, yaelekea nusu ya watoto waliozaliwa na wazazi waliofunga ndoa katika nchi hiyo wataathiriwa na talaka ya wazazi wao wanapofikisha umri wa miaka 18. Takwimu zinaonyesha kwamba vijana wengi katika sehemu nyingi za ulimwengu wanakabili hali hizohizo zenye kuhuzunisha.
Je, Ni Vigumu Sana Kudumisha Uaminifu?
Kwa sababu ya ukosefu wa uaminifu uliopo, maneno ya Mfalme Daudi yanafaa sana sasa kuliko wakati mwingine wowote: “BWANA, uokoe, maana mcha Mungu amekoma, maana waaminifu wametoweka katika wanadamu.” (Zaburi 12:1) Kwa nini ukosefu wa uaminifu umeenea sana? Roger Rosenblatt, alisema hivi katika gazeti Time: ‘Ingawa uaminifu ni sifa nzuri, tunashindwa kuidumisha kwa sababu ya udhaifu wetu na pia sifa zetu za asili kama vile hofu, kutojiamini, kutaka kujinufaisha, na tamaa ya makuu.’ Biblia husema hivi waziwazi inapofafanua kipindi tunachoishi: “Watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, . . . wasio waaminifu-washikamanifu, wasio na shauku ya kiasili.”—2 Timotheo 3:1-5.
Tunapofikiria jinsi ambavyo uaminifu—au ukosefu wa uaminifu—huathiri fikira na matendo ya watu, huenda tukauliza, ‘Inafaa tuwe waaminifu kwa nani?’ Ona jibu la swali hilo katika makala inayofuata.
-
-
Unapaswa Kuwa Mwaminifu kwa Nani?Mnara wa Mlinzi—2002 | Agosti 15
-
-
Unapaswa Kuwa Mwaminifu kwa Nani?
“Nchi yetu: . . . Iwe imekosea au la; bado ni nchi yetu.”—Stephen Decatur, ofisa wa jeshi la wanamaji wa Marekani, 1779-1820.
WENGI huona kwamba daraka lao kubwa ni kuwa waaminifu kabisa kwa nchi yao. Huenda wengine wakabadili maneno ya Stephen Decatur, na kusema ‘Dini yangu, iwe imekosea au la; bado ni dini yangu.’
Ni kweli kwamba mara nyingi sisi huwa waaminifu kwa nchi au dini fulani ikitegemea mahali tulipozaliwa, lakini uamuzi kuhusu ni nani tunayepaswa kuwa waaminifu kwake ni wa maana sana hivi kwamba hatuwezi kuufanya bila uhakika. Hata hivyo, kuchunguza upya ujitoaji ambao tumekuwa nao tangu tulipokuwa wadogo hutaka tuwe jasiri na pia hutokeza magumu.
Uaminifu Wajaribiwa
Mwanamke mmoja aliyekulia nchini Zambia asema: “Nilipendezwa na dini tangu nilipokuwa mchanga. Tulisali kila siku tukiwa familia kwenye chumba kitakatifu, tukaadhimisha sikukuu za kidini, na kuhudhuria ibada kwa ukawaida kwenye hekalu. Dini na ibada yangu ilihusiana sana na utamaduni, jumuiya, na familia yangu.”
Hata hivyo, alipokuwa tineja, alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova na muda mfupi baadaye akaamua kubadili dini yake. Je, huo ulikuwa ukosefu wa uaminifu?
Zlatko alilelewa Bosnia, na kwa muda fulani alishiriki vita iliyopiganwa nchini mwao. Yeye pia alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Sasa amekataa kujihusisha na vita. Je, amekosa uaminifu?
Utajibu maswali hayo kupatana na maoni yako. Mwanamke aliyetangulia kutajwa anasema: “Katika jumuiya yetu, kubadili dini huonwa kuwa jambo lenye kuaibisha; ni kukosa uaminifu, kusaliti familia na jamii.” Vivyo hivyo, marafiki wa awali wa Zlatko ambao ni wanajeshi waliona mtu yeyote aliyekataa kujiunga nao vitani kuwa msaliti. Hata hivyo, mwanamke huyo na Zlatko wanahisi kwamba uaminifu wa kiwango cha juu—uaminifu kwa Mungu—ndio huwachochea kutenda. Jambo la maana zaidi ni, Mungu huonaje wale wanaotaka kuwa waaminifu kwake?
Uaminifu wa Kweli Ni Udhihirisho wa Upendo
Mfalme Daudi alimwambia Yehova Mungu hivi: “Wewe ni mwaminifu kwa walio waaminifu.” (2 Samweli 22:26) Neno la Kiebrania ambalo limetafsiriwa “uaminifu” hapa linatoa wazo la fadhili ambayo hushikamana kwa upendo na kitu fulani hadi kusudi la kitu hicho litimie. Kama vile mama mwenye mtoto anyonyaye, Yehova hushikamana kwa upendo na wale walio waaminifu kwake. Yehova alisema hivi kuhusu watumishi wake waaminifu katika Israeli la kale: “Je! mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata asimhurumie mwana wa tumbo lake? Naam, hawa waweza kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe.” (Isaya 49:15) Mungu anawahakikishia wale walio tayari kutanguliza uaminifu wao kwake kwamba atawatunza kwa upendo.
Uaminifu kwa Yehova unategemea upendo. Sifa hiyo huchochea mtu apende mambo ambayo Yehova hupenda na kuchukia mambo maovu ambayo Yehova huchukia. (Zaburi 97:10) Kwa kuwa upendo ndiyo sifa kuu ya Yehova, uaminifu kwa Mungu humzuia mtu asiwatendee wengine kwa njia isiyo ya upendo. (1 Yohana 4:8) Kwa hiyo iwapo mtu anabadili imani yake ya kidini ili kuonyesha uaminifu kwa Mungu, hiyo haimaanishi kwamba hapendi familia yake.
Uaminifu kwa Mungu Hunufaisha
Mwanamke aliyetangulia kutajwa asema hivi kuhusu hatua alizochukua: “Kwa kujifunza Biblia, nilipata kumjua Yehova kuwa Mungu wa kweli, na kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja naye. Yehova si kama miungu niliyoabudu hapo awali; yeye husawazisha upendo, haki, hekima, na nguvu zake. Kwa kuwa Yehova hutaka ujitoaji usiohusisha wengine, nililazimika kuacha kuabudu miungu mingine.
“Mara kwa mara wazazi wangu waliniambia kwamba nimewakasirisha sana na kwamba ninawakatisha tamaa. Jambo hilo lilikuwa gumu sana kwangu kwa kuwa ninatamani sana kupata kibali cha wazazi. Lakini nilipozidi kuongeza ujuzi wa kweli ya Biblia hatua kwa hatua, nilijua uamuzi ambao ningefanya. Singeweza kumkataa Yehova.
“Kuamua kuwa mwaminifu kwa Yehova badala ya kuwa mwaminifu kwa mapokeo ya kidini hakumaanishi kwamba mimi si mwaminifu kwa familia yangu. Mimi hujitahidi kuwaonyesha kwa maneno na matendo kwamba ninaelewa jinsi wanavyohisi. Lakini nisipokuwa mwaminifu kwa Yehova, basi huenda nikazuia familia yetu wasipate kumjua, na kufanya hivyo kungekuwa kukosa uaminifu kabisa.”
Vivyo hivyo, mtu hawi msaliti anapokataa kujihusisha na siasa na vita kwa sababu ya uaminifu wake kwa Mungu. Zlatko asema hivi kuhusu hatua alizochukua: “Ingawa nililelewa nikiwa Mkristo wa jina tu, nilioa mtu ambaye si Mkristo. Vita ilipoanza nilipaswa kuwa mwaminifu kwa pande zote mbili. Nililazimika kuamua nitapigania upande upi. Nilipigana kwa muda wa miaka mitatu na nusu. Hatimaye mimi na mke wangu tukatorokea Kroatia ambapo tulikutana na Mashahidi wa Yehova.
“Baada ya kujifunza Biblia, tuling’amua kwamba tunapaswa kuwa waaminifu kwa Yehova kwanza ambaye hutaka tupende jirani yetu hata awe ni wa jamii au dini gani. Sasa mimi na mke wangu tumeungana katika ibada ya Yehova, nami nimejifunza kwamba siwezi kuwa mwaminifu kwa Mungu na wakati huo huo nipigane na jirani yangu.”
Uaminifu Unaoongozwa na Ujuzi Sahihi
Kwa kuwa Yehova ndiye Muumba wetu, tunapaswa kutanguliza uaminifu wetu kwake kuliko kwa watu wengine. (Ufunuo 4:11) Hata hivyo, ili uaminifu wetu kwa Mungu usibadilike na kutokeza madhara, unapaswa kuongozwa na ujuzi sahihi. Biblia hutuhimiza: ‘Mfanywe upya katika kani inayotendesha akili yenu, na mvae utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uaminifu-mshikamanifu wa kweli.’ (Waefeso 4:23, 24) Mtu huyo mashuhuri aliyeandika maneno hayo yaliyoongozwa na Mungu alikuwa na ujasiri wa kuchunguza upya uaminifu alioonyesha tangu alipokuwa mdogo. Baada ya kufanya uchunguzi, alibadilika na kupata manufaa.
Naam, Sauli alikabili jaribu la kuonyesha uaminifu linalowakabili watu wengi wanaoishi wakati huu. Sauli alilelewa katika familia iliyoshikilia sana mapokeo, naye akawa mwaminifu sana kwa dini ya wazazi wake. Kwa sababu ya kuwa mwaminifu kwa dini yake, aliwadhulumu wale waliopinga maoni yake. Sauli alijulikana kwa kuvamia nyumba za Wakristo na kuwaburuta waadhibiwe na hata kuuawa.—Matendo 22:3-5; Wafilipi 3:4-6.
Hata hivyo, baada ya Sauli kupata ujuzi sahihi wa Biblia, alichukua hatua ambayo wengi wa marafiki wake waliiona kuwa ya kipuuzi. Alibadili dini yake. Sauli, ambaye baadaye alikuja kuitwa mtume Paulo, alichagua kuwa mwaminifu kwa Mungu badala ya kuwa mwaminifu kwa mapokeo. Uaminifu kwa Mungu ambao ulitegemea ujuzi sahihi ulimchochea Sauli kuwa mvumilivu, mwenye upendo, na mwenye kujenga, tofauti na alivyokuwa hapo awali, muumini shupavu na mwenye kuleta madhara.
Kwa Nini Uwe Mwaminifu?
Bila shaka inanufaisha wakati uaminifu wetu unapoongozwa na viwango vya Mungu. Kwa mfano, ripoti moja ya mwaka wa 1999 kutoka Taasisi ya Australia ya Uchunguzi wa Familia ilisema kwamba kati ya mambo ya msingi yanayofanya ndoa zidumu na ziwe zenye kuridhisha ni “imani na uaminifu . . . [na] kutambua uhitaji wa kiroho.” Uchunguzi huohuo ulionyesha kwamba “ndoa thabiti na zenye kuridhisha” hufanya wanaume na wanawake wawe wenye furaha zaidi, wenye afya zaidi, na waishi maisha marefu, na kwamba ndoa thabiti huwapa watoto fursa ya kuishi maisha yenye furaha.
Katika ulimwengu wa sasa wenye misukosuko, uaminifu ni kama kamba ya kuokolea ambayo humwunganisha mwogeleaji na meli ya kuokolea. Ikiwa “mwogeleaji” si mwaminifu, atatupwa huku na huku na mawimbi na upepo. Lakini iwapo uaminifu wake umeelekezwa mahali pasipofaa, ni kana kwamba kamba yake ya kuokolea imefungwa kwenye meli inayozama. Kama Sauli, anaweza kujikuta amechukua hatua inayoongoza kwenye uharibifu. Hata hivyo, uaminifu kwa Yehova ambao unategemea ujuzi sahihi ni kamba ya kuokolea ambayo hutuimarisha na kutuongoza kwenye wokovu.—Waefeso 4:13-15.
Yehova anatoa ahadi hii kwa wale walio waaminifu kwake: “Kwa kuwa BWANA hupenda haki, wala hawaachi watauwa [“washikamanifu,” NW] wake. Wao hulindwa milele.” (Zaburi 37:28) Hivi karibuni, wote walio waaminifu kwa Yehova wataruhusiwa kuingia katika paradiso duniani, ambapo watafurahia maisha yasiyo na majonzi na maumivu na kufurahia uhusiano wa kudumu usio na migawanyiko ya kidini na kisiasa.—Ufunuo 7:9, 14; 21:3, 4.
Hata sasa, mamilioni ya watu ulimwenguni pote wametambua kwamba furaha ya kweli hutokana na kuwa waaminifu kwa Yehova. Kwa nini usiwaruhusu Mashahidi wa Yehova wakusaidie kuchunguza maoni yako kuhusu uaminifu kwa kutumia kweli ya Biblia? Biblia hutuambia: “Fulizeni kujijaribu kama nyinyi mumo katika imani, fulizeni kujithibitisha wenyewe nyinyi ni nini.”—2 Wakorintho 13:5.
Tunahitaji ujasiri ili kuchunguza upya imani yetu na kwa nini tunashikamana na imani hiyo, lakini kwa kufanya hivyo tunaweza kupokea thawabu kubwa zaidi ya kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova Mungu. Mwanamke aliyetangulia kutajwa adhihirisha maoni ya wengi anaposema: “Nimejifunza kwamba kuwa waaminifu kwa Yehova na kwa viwango vyake hutusaidia kuwa na usawaziko tunaposhughulika na familia zetu na kuwa raia bora katika jamii. Hata majaribu yawe magumu kadiri gani, tukiwa waaminifu kwa Yehova, atakuwa mwaminifu kwetu sikuzote.”
[Picha katika ukurasa wa 6]
Sauli alichochewa na ujuzi sahihi kubadili dini yake
[Picha katika ukurasa wa 7]
Kwa nini usichunguze upya uaminifu wako kwa kutumia kweli ya Biblia?
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 4]
Churchill, juu kushoto: U.S. National Archives photo; Joseph Göbbels, mbali kulia: Library of Congress
-