Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Msiba Mkubwa Sana
    Amkeni!—2003 | Februari 22
    • Msiba Mkubwa Sana

      Erika ana umri wa miezi sita. Lakini uzito na kimo chake ni kama cha mtoto mwenye umri wa mwezi mmoja au miwili. Amekonda sana lakini miguu, tumbo na uso wake umevimba. Ngozi yake imekuwa nyeusi, nywele zake zimechakaa na zinakatika kwa urahisi, na ana vidonda mwilini. Anaonekana mwenye kukasirika haraka. Ni lazima daktari awe mwangalifu anapoyachunguza macho ya Erik kwa sababu ngozi ya macho inaweza kubambuka kwa urahisi sana. Inaelekea ukuzi wake wa kiakili umeathiriwa. Inahuzunisha kwamba watoto wengi wanaugua ugonjwa huo.

      “ZAIDI ya nusu ya watoto wanaokufa ulimwenguni pote hufa kutokana na ugonjwa huo. Tangu ile tauni kubwa iliyotukia katika karne ya 14, hakuna ugonjwa mwingine wa kuambukiza ambao umewaangamiza watu wengi kama ugonjwa huu. Lakini ugonjwa huu hauwezi kuambukizwa. Unawalemaza mamilioni ya watu na kudhoofisha mfumo wao wa kinga na uwezo wao wa kiakili. Unahatarisha uhai wa wanawake, familia, na jamii nzima.”—The State of the World’s Children, Shirika la Hazina ya Watoto la Umoja wa Mataifa.

      Ni ugonjwa gani huo? Ni utapiamlo—ukosefu wa chakula bora hasa chakula kinachojenga mwili. Ugonjwa huo umetajwa na Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) kuwa hatari iliyofichika. Ugonjwa huo umeenea kadiri gani? Shirika la WHO linasema kwamba “unaua angalau nusu ya watoto milioni 10.4 wanaokufa kila mwaka.”

      Utapiamlo unahusisha magonjwa mengine mengi, kutia ndani magonjwa ya kukosa kirutubisho kimoja au kadhaa mwilini—kama vile vitamini au madini—na kunenepa kupita kiasi na magonjwa mengine sugu yanayohusiana na vyakula. Hata hivyo, shirika la WHO linasema kwamba “ukosefu wa protini mwilini ndio ugonjwa hatari zaidi kati ya aina zote za utapiamlo.” Ugonjwa huo huwapata hasa watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano.

      Hebu tua kidogo na umfikirie Erik, aliyetajwa mwanzoni, na mamilioni ya watoto walio na ugonjwa huo. Hawakujiletea ugonjwa huo, wala hawawezi kujinasua. Mtaalamu wa magonjwa ya watoto yanayosababishwa na ukosefu wa lishe Georgina Toussaint alimwambia hivi mwandishi wa Amkeni!: “Wale wanaoteseka na kuumia hawana hatia wala uwezo wa kujikinga.”

      Huenda wengine wakadhani kwamba tatizo hilo haliwezi kuepukwa—eti hakuna chakula cha kuwatosha watu wote. Jambo hilo linashangaza kwa sababu kulingana na shirika la WHO “kuna chakula tele ulimwenguni leo.” Kuna chakula cha kuwatosha wanadamu wote duniani—na cha ziada. Isitoshe, hakuna ugonjwa unaoweza kuzuiwa kwa urahisi na kutibiwa kwa gharama ndogo kama utapiamlo. Je, husumbuliwi na habari hizo?

      Ni Nani Wanaopatwa na Ugonjwa Huo?

      Utapiamlo hauwapati watoto peke yao. Ripoti ya shirika la WHO ya mwezi wa Julai 2001 inasema kwamba “utapiamlo unasambaa sana, unawaathiri watu wapatao milioni 800—asilimia 20 ya watu wanaoishi katika nchi zinazoendelea.” Hiyo yamaanisha kwamba mtu 1 kati ya kila watu 8 ulimwenguni ana utapiamlo.

      Ingawa idadi kubwa ya watu wasiopata chakula cha kutosha wako Asia—hasa kwenye maeneo ya kusini na ya kati—bara la Afrika lina idadi kubwa zaidi ya watu wasiopata chakula cha kutosha ukilinganisha na idadi ya watu wanaoishi humo. Kisha inafuatwa na nchi kadhaa zinazoendelea za Amerika ya Latini na Karibea.

      Je, nchi zilizoendelea zinakumbwa na ugonjwa huo? Ndiyo. Kichapo The State of Food Insecurity in the World 2001 kinasema kwamba watu milioni 11 wanaoishi katika nchi zilizoendelea wana utapiamlo. Na watu wengine milioni 27 walio na utapiamlo wanaishi katika nchi zinazoendelea kusitawi kiviwanda, hasa nchi zilizo Mashariki mwa Ulaya na jamhuri za ule uliokuwa Muungano wa Sovieti.

      Kwa nini utapiamlo umekuwa tatizo kubwa sana? Je, kuna jambo lolote linaloweza kuboresha hali ya watu wasiopata chakula cha kutosha hivi sasa? Je, tatizo hilo litawahi kutoweka duniani? Makala zifuatazo zitajibu maswali hayo.

      [Maelezo ya Chini]

      a Si jina lake halisi.

      [Chati/Ramani katika ukurasa wa 4]

      (Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

      NCHI ZINAZOKABILI UHABA WA CHAKULA BORA

      UHABA MKUBWA

      UHABA WA WASTANI

      UHABA MDOGO

      HAKUNA UHABA AU TAKWIMU KAMILI HAZIPATIKANI

      [Picha katika ukurasa wa 3]

      Wasubiri misaada ya chakula nchini Sudan

      [Hisani]

      UN/DPI Photo by Eskinder Debebe

  • Visababishi Vilivyotia Mizizi, Athari Mbaya za Utapiamlo
    Amkeni!—2003 | Februari 22
    • Visababishi Vilivyotia Mizizi, Athari Mbaya za Utapiamlo

      “Nilipohisi njaa, mlianzisha tume ya kuchunguza chanzo cha tatizo langu. Nilipokosa makao, mlitangaza magazetini. Nilipokuwa mgonjwa, mlifanya mkutano wa kujadili watu wa hali ya chini katika jamii. Mlichunguza matatizo yangu yote kinaganaga lakini ningali mgonjwa, nina njaa na sina makao.”—Mwandishi hajulikani.

      MASHIRIKA ya ulimwengu yameshindwa kabisa kukomesha utapiamlo licha ya jitihada nyingi ambazo zimefanywa. Kwa mfano, mnamo mwaka wa 1996, Mkutano wa Chakula Ulimwenguni uliopangwa na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) uliazimia kupunguza idadi ya watu wenye utapiamlo kwa asilimia 50—karibu watu milioni 400—kufikia mwaka wa 2015.a

      Maendeleo fulani yamefanywa. Lakini kwa kusikitisha, ripoti ya hivi karibuni ya shirika la FAO, The State of Food Insecurity in the World 2001, inakiri hivi: “Ni wazi kwamba jitihada ya kupunguza idadi ya watu wasiopata chakula cha kutosha ulimwenguni imepungua.” Kwa hiyo inaonekana kwamba azimio la mkutano huo bado haliwezi kutimizwa. Zaidi ya hayo, ripoti hiyo inakiri kwamba “idadi ya watu wasio na chakula cha kutosha imeongezeka sana katika nchi nyingi zinazoendelea.”

      Kwa nini ni vigumu sana kushinda tatizo hilo? Ili kupata jibu, ni vyema kuujua kwanza ugonjwa wa utapiamlo, na kuchunguza athari na visababishi vilivyotia mizizi vya ugonjwa huo.

      Utapiamlo Husababishwa na Nini?

      Utapiamlo husababishwa na ukosefu wa vitamini na madini ya kutosha katika chembe za mwili, na kwa kawaida husababishwa na mambo mawili: (1) ukosefu wa protini, nishati, vitamini, na madini na (2) maambukizo ya mara kwa mara.

      Magonjwa kama vile kuharisha, surua, malaria, na magonjwa ya kupumua hudhoofisha mwili sana na kupunguza vitamini na madini. Magonjwa hayo humfanya mgonjwa apoteze hamu ya kula naye hula chakula kidogo sana, na hivyo anapata utapiamlo. Kwa upande mwingine, mtoto asiyepata chakula cha kutosha anaweza kuambukizwa magonjwa kwa urahisi. Jambo hilo huongeza idadi ya watoto wanaokufa kwa sababu ya kukosa vyakula vinavyojenga mwili.

      Kwa nini utapiamlo unawashambulia hasa watoto? Watoto wanakua haraka na hivyo wanahitaji nishati na protini nyingi zaidi. Vivyo hivyo, akina mama wajawazito na wanaonyonyesha wanaweza kupata utapiamlo.

      Mara nyingi, mtoto mchanga huanza kuathiriwa akiwa tumboni. Ikiwa mama hapati chakula cha kutosha au hali chakula bora kabla na wakati wa mimba, basi atajifungua mtoto mwenye uzito kidogo. Mtoto huyo akiachishwa kunyonya mapema, asipolishwa vizuri, au usafi usipozingatiwa, anaweza kuugua utapiamlo.

      Mtoto hawezi kukua au kusitawi vizuri asipopata vitamini na madini muhimu. Yeye hulia bila sababu yoyote na kuwa mgonjwa-mgonjwa. Kadiri hali yake inavyozorota ndivyo anavyozidi kukonda, macho na utosi wa kichwa hubonyea, ngozi na tishu za mwili hukauka, na uwezo wa kudhibiti joto la mwili hupungua.

      Utapiamlo humwathiri mtoto kwa njia nyingine ambazo pia zinaweza kuathiri ukuzi wake. Kwa mfano, kutopata madini ya kutosha—hasa chuma, iodini, na zinki—na vitamini—hasa vitamini A—kunaweza kusababisha madhara hayo. Shirika la Hazina ya Watoto ya Umoja wa Mataifa (UNICEF) linasema kwamba ukosefu wa vitamini A huathiri watoto wachanga milioni 100 hivi ulimwenguni na husababisha upofu. Vilevile unadhoofisha mfumo wa kinga, na hivyo kupunguza uwezo wa mtoto wa kukinza maambukizo.

      Madhara Mabaya Zaidi

      Utapiamlo hudhuru kabisa mwili, hasa mwili wa mtoto. Unaweza kudhuru viungo na mifumo yote mwilini kutia ndani moyo, mafigo, tumbo, matumbo, mapafu, na ubongo.

      Uchunguzi mbalimbali umeonyesha kwamba ukuzi wa polepole wa mtoto hudhoofisha maendeleo yake ya kiakili na uwezo wa kufikiri na kufanya vyema shuleni. Ripoti moja ya Umoja wa Mataifa inasema hizo ndizo athari mbaya zaidi na za kudumu za utapiamlo.

      Mtoto anaweza kuendelea kuathiriwa na matokeo ya utapiamlo hata anapokuwa mtu mzima. Ndiyo sababu shirika la UNICEF lililalamika hivi: “Kudhoofisha uwezo wa akili wa binadamu kwa kadiri kubwa hivyo—kwa sababu ambazo zinaweza kuzuiwa—ni kosa kubwa sana la kimaadili na hasara kubwa.” Kwa hiyo matokeo ya kudumu ya utapiamlo ni mabaya sana. Uchunguzi wa hivi majuzi unaonyesha kwamba kutokula chakula cha kutosha wakati wa utotoni kunaweza kusababisha magonjwa hatari kama vile ugonjwa wa moyo, kisukari, na shinikizo la juu la damu mtu anapokuwa mtu mzima.

      Hata hivyo, watu wengi hawaugui utapiamlo hatari, kama shirika la UNICEF linavyokiri: “Zaidi ya robo tatu ya watu wanaokufa kutokana na magonjwa yanayohusiana na ukosefu wa chakula, hufa kwa sababu ya utapiamlo mdogo au wa wastani.” (Italiki ni zetu.) Watoto wanaopatwa na utapiamlo mdogo au wa wastani wanaweza kupata matatizo ya kudumu ya afya. Kwa hiyo ni muhimu kugundua watoto wenye dalili za utapiamlo ili waweze kupata matibabu yanayofaa.—Ona sanduku kwenye ukurasa wa 7.

      Visababishi Vilivyotia Mizizi

      Kama ilivyotajwa awali, utapiamlo husababishwa na ukosefu wa chakula. Lakini, unasababishwa pia na mambo mengine mazito zaidi ya kijamii, kiuchumi, kitamaduni, na ya kimazingira. Kisababishi kikuu ni umaskini, ambao huathiri mamilioni ya watu, hasa katika nchi zinazoendelea. Hata hivyo, mbali na kuwa kisababishi, umaskini pia husababishwa na utapiamlo. Ukosefu wa chakula cha kutosha hupunguza uwezo wa kufanya kazi, na hilo huzidisha umaskini.

      Kuna mambo mengine yanayochangia utapiamlo. Watu huwa na mazoea mabaya ya kula kwa sababu ya kukosa elimu. Kama tulivyoona, maambukizo huchangia pia. Vilevile kuna sababu za kijamii na za kitamaduni, kama vile ugawaji usiofaa wa chakula na kuwabagua wanawake. Mara nyingi wanawake hula chakula kichache kilichosalia baada ya wanaume kula. Wanawake hunyimwa pia fursa za kupata elimu ambayo ingewasaidia kuwatunza watoto wao vyema.

      Zaidi ya hayo, hali za kimazingira kama vile misiba ya kiasili na vita hupunguza uzalishaji wa chakula. Ripoti ya The State of Food Insecurity in the World 2001, ilisema kwamba kati ya Oktoba 1999 na Juni 2001, nchi 22 ziliathiriwa na ukame, nchi 17 na vimbunga au mafuriko, nchi 14 na vita vya wenyewe kwa wenyewe au migogoro, nchi 3 na baridi kali kupita kiasi, na nchi 2 na matetemeko ya ardhi.

      Kutibu na Kuzuia

      Mtoto mwenye utapiamlo anaweza kutibiwaje? Ikiwa mtoto huyo amedhoofika kabisa huenda ikafaa alazwe hospitalini kwanza. Kichapo kimoja cha madaktari kilichochapishwa na Shirika la Afya Ulimwenguni kinasema kwamba madaktari wanapaswa kumchunguza mtoto huyo na kutibu maambukizo yoyote au upungufu wa maji mwilini. Anaweza kuanza kulishwa hatua kwa hatua, labda kupitia mrija kwa muda wa juma moja hivi.

      Katika hatua ya pili, mtoto hunyonyeshwa na kusaidiwa ale chakula kingi iwezekanavyo. Ni muhimu kuboresha tena hali yake ya kihisia na ya kimwili wakati huo. Mtoto huyo anaweza kukua vyema akitunzwa kwa uangalifu na kuonyeshwa upendo. Wakati huo huenda ikafaa kumfundisha mama kumtunza mtoto wake kwa kumlisha chakula kinachofaa na kutunza afya yake ili asipate tena utapiamlo. Kisha mtoto hurudishwa nyumbani. Ni muhimu mtoto apelekwe hospitalini au kwenye kliniki ili maendeleo yake yachunguzwe.

      Hata hivyo, kuuzuia utapiamlo ndilo jambo la maana zaidi. Ndiyo sababu serikali na mashirika yasiyo ya kiserikali katika nchi nyingi yameanzisha miradi ya kuboresha chakula kinacholiwa na umma. Jamii pia hujitahidi kuzuia utapiamlo kwa njia nyingi, kama vile kuanzisha mipango ya kuwaelimisha watu kuhusu chakula, kuwa na maji safi ya kunywa, kujenga vyoo, kudumisha usafi wa mazingira, kutoa michango kwa ajili ya kampeni za chanjo, na kusimamia ukuzi na maendeleo ya watoto.

      Lakini mtu mmoja-mmoja anaweza kufanya nini ili kuzuia utapiamlo? Sanduku lililo kwenye ukurasa wa 8 lina madokezo kadhaa yenye faida. Pamoja na hayo, mtaalamu wa magonjwa ya watoto yanayosababishwa na lishe, Georgina Toussaint anapendekeza kwamba, mama anapaswa kumwona tena daktari wa watoto au kurudi hospitalini siku saba baada ya kujifungua, mtoto anapokuwa na umri wa mwezi mmoja, na kila mwezi baada ya hapo. Mama anapaswa pia kumwona daktari mtoto anapokuwa na dalili za kupungukiwa na maji mwilini, anaharisha sana, au akiwa na dalili za homa.

      Ijapokuwa mapendekezo hayo yanasaidia kuboresha chakula cha watoto, hatuna budi kukubali kwamba utapiamlo ni tatizo kubwa sana lisiloweza kutatuliwa na wanadamu. Kitabu Encyclopædia Britannica kinakiri: “Kuwapa watu wote chakula cha kutosha na kuwaelimisha kuhusu lishe bora bado ni tatizo kubwa sana.” Basi je, kuna tumaini kwamba hatari hiyo iliyofichika itakoma?

      [Maelezo ya Chini]

      a Kwa habari zaidi kuhusu Mkutano huo wa Chakula Ulimwenguni, soma gazeti la Amkeni! la Agosti 8, 1997, ukurasa wa 12-14.

      [Sanduku katika ukurasa wa 7]

      JE, MTOTO WAKO ANA UTAPIAMLO?

      Wataalamu wa afya wanawezaje kujua kama mtoto ana utapiamlo? Huenda wakachunguza dalili fulani-fulani, wakauliza maswali kuhusu mazoea yake ya kula, na kuomba apimwe kwenye maabara. Hata hivyo, mara nyingi wao humpima mtoto moja kwa moja. Wao hupima mwili wa mtoto na kulinganisha vipimo hivyo na vipimo vya kawaida. Na hivyo wanajua mtoto anakosa chakula gani na athari za ugonjwa huo.

      Vitu muhimu sana wanavyopima ni uzito, kimo, na unene wa mkono. Wanaweza kujua athari za utapiamlo kwa kulinganisha uzito wa mwili na umri wake; mtoto aliyeathiriwa sana huwa amedhoofika na kukonda. Mtoto huonwa kuwa ameathiriwa sana na utapiamlo iwapo uzito wake umepungua kwa asilimia 40, na ameathiriwa kwa kadiri ikiwa uzito wake umepungua kwa asilimia 25 hadi 40, na ameathiriwa kidogo iwapo uzito wake umepungua kwa asilimia 10 hadi 25. Ikiwa mtoto ana uzito mdogo sana na umri wake ni mkubwa, hiyo ni ishara ya kwamba ni mgonjwa sana—na hakui kamwe.

      Ugonjwa wa marasmus, ugonjwa wa kwashiorkor, na mchanganyiko wa magonjwa hayo mawili husababishwa na aina ya utapiamlo ulio hatari sana wa kukosa vyakula vinavyojenga mwili. Ugonjwa wa marasmus huwapata watoto wanaonyonya wenye umri wa kati ya miezi 6 na miezi 18. Huanza polepole kwa upungufu mkubwa wa nishati, vitamini na madini na husababishwa na kutonyonya vya kutosha au kula vyakula vya badala visivyo na virutubisho vya kutosha. Mtoto mwenye ugonjwa huo hukonda sana, misuli yake hunyauka kiasi cha kubaki mifupa na ngozi, naye hakui. Uso wake huwa kama wa mtu aliyezeeka, anakasirika haraka na kulia sana.

      Neno la Kiafrika kwashiorkor linamaanisha “mtoto aliyeachishwa.” Linawahusu hasa watoto ambao wanaachishwa kunyonya ili ndugu au dada zao wachanga zaidi wanyonye. Ugonjwa huo huanza baada ya mtoto kuachishwa kunyonya. Unasababishwa na ukosefu mkubwa sana wa protini na upungufu wa kalori mwilini. Maji hurundamana mwilini na kumfanya mtoto avimbe tumbo, mikono na miguu. Nyakati nyingine uso wake huvimba na kuwa na umbo la mwezi mpevu. Vidonda hutokea kwenye ngozi na nywele hubadilika rangi na kukauka. Watoto wenye ugonjwa huu huvimba ini, hukosa uchangamfu na furaha. Ndivyo alivyokuwa Erik, aliyetajwa awali, ambaye alinyonyeshwa na mamaye kwa mwezi mmoja tu; kisha akaanza kunyweshwa maziwa ya ng’ombe yaliyotiwa maji. Alianza kunyweshwa mchuzi wa mboga na maji yenye sukari akiwa na umri wa miezi mitatu na kuachiwa jirani amtunze.

      Aina ya tatu ya utapiamlo huwa ni mchanganyiko wa ugonjwa wa marasmus na kwashiorkor. Magonjwa hayo yanaweza kuua yasipotibiwa haraka.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]

      MLINDE MTOTO WAKO ASIPATE UTAPIAMLO!

      ◼ Ni muhimu mama ale chakula bora. Akina mama wajawazito na wanaonyonyesha wanahitaji nishati na protini zaidi. Protini hasa humsaidia mama kuongeza maziwa. Kwa hiyo kunapokuwa na uhaba wa chakula, walisheni kwanza akina mama wenye umri wa kupata watoto na watoto wachanga.

      ◼ Mara nyingi, chakula bora zaidi kwa mtoto mchanga ni maziwa ya mama. Wanahitaji kunyonya hasa siku za kwanza-kwanza baada ya kuzaliwa kwa sababu maziwa ya mama yana kingamwili zinazomlinda mtoto asiambukizwe magonjwa. Katika miezi minne hivi ya kwanza, maziwa ya mama huwa na madini na vitamini zote ambazo mtoto anahitaji ili kukua ifaavyo.

      ◼ Ijapokuwa mtoto hutegemea sana maziwa ya mama, anaweza kulishwa vyakula vingine kati ya mwezi wa nne na wa sita. Mlishe hatua kwa hatua matunda na mboga zilizopondwa-pondwa. Kila mara mlishe mtoto chakula kipya. Siku mbili au tatu baadaye, akisha zoea chakula hicho, mlishe kingine tofauti. Bila shaka, unahitaji kuwa na subira na kumzoeza mara nyingi ili mtoto akubali chakula kipya. Unapotayarisha chakula hicho, kumbuka kwamba kila kitu chapaswa kuwa safi kabisa. Osha vyakula na vyombo vizuri!

      ◼ Kati ya mwezi wa tano na wa tisa, kwa kawaida watoto huhitaji nishati na protini zaidi kuliko zinazopatikana kwenye maziwa. Endelea kuwalisha vyakula vingine vipya bila kuacha. Anza kwa kuwalisha nafaka na vyakula vyenye mboga zinazoweza kuliwa na watoto, kisha uwalishe nyama na vyakula vilivyotengenezwa kutokana na maziwa. Ingawa mwanzoni vyakula vinavyoliwa na watoto huchujwa sana, baadaye vinaweza kukatwa-katwa vipande vidogo kuanzia mwezi wa sita na kuendelea. Hakuna haja wala haipendekezwi uongeze chumvi au sukari kwenye vyakula hivyo.

      ◼ Baada ya miezi minane, mtoto hategemei sana maziwa ya mama, bali hayo ni nyongeza tu. Yeye huanza kula vyakula vinavyoliwa na wengine katika familia. Vyakula vinapasa kuwa safi kabisa, na vinapasa kukatwa-katwa vipande vidogo ili mtoto avitafune kwa urahisi. Mlo unaofaa unatia ndani matunda na mboga, nafaka na kunde, nyama na vyakula vilivyotengenezwa kutokana na maziwa.b Watoto wanahitaji hasa vyakula vyenye vitamini A. Kwa mfano, maziwa ya mama, mboga za kijani, matunda na mboga zenye rangi ya machungwa kama vile maembe, mapapai, na karoti. Watoto wenye umri wa chini ya miaka mitatu wanahitaji kula mara tano au sita kwa siku.

      ◼ Vyakula mbalimbali vilivyochanganywa kwa njia mbalimbali huwa na vitamini na madini yanayomlinda mtoto wako. Mama anapaswa kujitahidi kumlisha mtoto chakula bora, bila kumlazimisha ale wakati ameshiba wala kumnyima anapotaka kula zaidi.

      [Maelezo ya Chini]

      b Utapata habari zaidi katika makala “Vyakula Bora Unavyoweza Kupata,” katika Amkeni! ya Mei 8, 2002.

  • Utapiamlo Utakoma Karibuni!
    Amkeni!—2003 | Februari 22
    • Utapiamlo Utakoma Karibuni!

      ‘LEO kuna chakula tele ulimwenguni kuliko miaka michache iliyopita. . . . Kuna chakula kinachoweza kuwatosha watu wote na cha ziada.’ Ndivyo unavyosema uchunguzi mmoja wa Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO). Kama kuna chakula tele, mbona kuna utapiamlo?

      Shirika la WHO linasema “tatizo ni kwamba chakula hakizalishwi wala kugawanywa kwa usawa. Mara nyingi wakazi maskini, wenye njaa wanaoishi katika maeneo yenye rutuba katika nchi zinazoendelea hujionea mazao mengi mno yakiuzwa nchi za nje ili kuleta pesa. Watu wachache hupata faida kubwa ya kifedha kwa muda mfupi huku wengi wakiumia kwa muda mrefu.” Uchunguzi uliofanywa hivi majuzi na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) unaonyesha kwamba ‘asilimia 20 ya watu matajiri ulimwenguni hula asilimia 45 ya nyama na samaki huku asilimia 20 ya watu maskini wakila asilimia 5 tu.’

      Kwa upande mwingine, “utapiamlo husababishwa pia na kutokuwa na elimu nzuri na habari sahihi,” lasema Shirika la Hazina ya Watoto ya Umoja wa Mataifa, kisha laongezea hivi: “Bila mipango thabiti ya kuwafundisha na kuwaelimisha watu wote, hawatakuwa na ujuzi, ustadi na mazoea yanayohitajiwa ili kukabiliana na utapiamlo.” Utapiamlo hudhoofisha afya ya mtu na uwezo wake wa kupata elimu bora zaidi—na hilo huendeleza ugonjwa huo.

      Haki na Kuwapenda Wengine Bila Ubinafsi

      Licha ya vizuizi hivyo vyenye kuvunja moyo, baadhi ya wataalamu wanaoshughulikia tatizo hilo bado wana matumaini. Kwa mfano, mkurugenzi mkuu wa shirika la FAO, Jacques Diouf, alieleza mambo anayotumaini kuona: “Ninatumaini kuona ulimwengu ambamo kila mwanamume, mwanamke na mtoto atakuwa na chakula salama cha kutosha kila siku. Ninatumaini kwamba pengo lenye kushtua kati ya matajiri na maskini litapungua. Ninatarajia wakati ambapo watu watavumiliana badala ya kubaguana; kutakuwa na amani badala ya vita; rasilimali zitatumiwa bila mazingira kuharibiwa; watu wote watakuwa na ufanisi wala hawatavunjika moyo.”

      Hata hivyo, kama tulivyoona matumaini hayo hayategemei kuwa tu na chakula cha kutosha na kukigawanya vizuri. Ni lazima tuwatendee wote kwa haki na kuwapenda bila ubinafsi. Lakini sifa hizo bora sana hazipatikani katika ulimwengu wa kisasa wa kibiashara.

      Je, vizuizi vikubwa sana kama pupa, umaskini, vita, na ubinafsi vinaweza kukomeshwa ili kusiwe na utapiamlo ulimwenguni? Au hiyo ni ndoto tu?

      Suluhisho Pekee la Kweli

      Biblia yaonyesha kwamba hatupaswi kushangazwa na mambo yanayosababisha utapiamlo. Neno la Mungu linasema: “Katika siku za mwisho nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha, . . . wasio na shauku ya kiasili, wasiotaka upatano wowote, . . . wasio na upendo wa wema, . . . wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakithibitika kuwa si kweli kwa nguvu ya hiyo.”—2 Timotheo 3:1-5.

      Je, wanadamu wanaweza kukomesha tabia hizo zilizokita mizizi bila msaada wa Mungu? Yaonekana hawawezi, sivyo? Labda umegundua kwamba watu fulani wenye mamlaka huwa na nia nzuri ya kukomesha matatizo ya kijamii yanayokumba wanadamu, lakini ubinafsi, kupenda pesa, na kutokamilika kwa wengine huvuruga na hata kuharibu jitihada hizo nzuri.—Yeremia 10:23.

      Hata hivyo, tatizo hilo litasuluhishwa kikweli. Biblia inaahidi kwamba Ufalme wa Mungu utakomesha tatizo la ukosefu wa haki na matatizo mengine yanayowakumba wanadamu leo.

      Andiko la Isaya 9:6-7 hutupatia tumaini hili zuri ajabu: “Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, tumepewa mtoto mwanamume; na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; naye ataitwa jina lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme wa amani. Maongeo ya enzi yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe, katika kiti cha enzi cha Daudi na ufalme wake; kuuthibitisha na kuutegemeza kwa hukumu na kwa haki, tangu sasa na hata milele. Wivu wa BWANA wa majeshi ndio utakaotenda hayo.”

      Ni Ufalme huohuo ambao watu husali juu yake wanapokariri ile Sala ya Bwana na kumwambia Mungu hivi: “Acha ufalme wako uje.” (Mathayo 6:9, 10) Ona kwamba Isaya anasema kwamba “wivu wa BWANA wa majeshi ndio utakaotenda hayo.” Naam, Yehova Mungu hutaka daima kutimiza mahitaji ya wanadamu. Ameiumba dunia hii ili izae chakula cha kuwatosha watu wote.

      Zaburi 65:9-13 yasema hivi kumhusu: “Umeijilia nchi na kuisitawisha, umeitajirisha sana. Mto wa Mungu umejaa maji; wawaruzuku watu nafaka maana ndiwe uitengenezaye ardhi. Matuta yake wayajaza maji; wapasawazisha palipoinuka, wailainisha nchi kwa manyunyu; waibariki mimea yake. . . . Na malisho yamevikwa kondoo, na mabonde yamepambwa nafaka.”

      Naam, Yehova Muumba, ndiye mtimizaji bora wa mahitaji ya wanadamu. Ndiye ‘anayekipa kila chenye mwili chakula chake; kwa maana fadhili zake ni za milele.’—Zaburi 136:25.

      Tunaweza kuwa na hakika kwamba Ufalme wa Mungu chini ya Kristo utawatunza watu wote. Biblia yasema kwamba ‘kutakuwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.’ Pia watu wote watapata chakula cha kutosha, kwa kuwa “[Yesu Kristo] atamkomboa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. . . . Nafsi za wahitaji ataziokoa.” (Zaburi 72:12, 13, 16) Kwa hiyo jipe moyo! Hatari hiyo iliyofichika itakomeshwa kabisa hivi karibuni.

  • Utapiamlo Utakoma Karibuni!
    Amkeni!—2003 | Februari 22
    • [Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 10]

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki