-
Ndoa Ziko TaabaniAmkeni!—2008 | Julai
-
-
Ndoa Ziko Taabani
“Siwezi kuvumilia tena!” Je, umewahi kusikia watu wakisema hivyo kuhusu ndoa yao? Ikiwa umefunga ndoa, je, umewahi kuhisi hivyo?
MAELFU ya watu huanza maisha ya ndoa baada ya kusitawisha uhusiano wenye upendo wakati wa uchumba, ilhali wengine huoana haraka kwa sababu ya mahaba. Katika visa vyote viwili, wao hutarajia kuwa na furaha. Mshauri mmoja anasema hivi: “Lakini wanapokuja kuniona, wengi wao wanaamini kwamba hawatapata furaha tena. Tayari wametamaushwa na wenzi wao, ndoa, upendo, na nyakati nyingine hata maisha yenyewe.” Wengi wao wako pamoja tu kwa sababu wana cheti cha ndoa na wanaishi katika nyumba moja.
Ndoa nyingine huvunjika kwa sababu ya kuongezeka kwa mfadhaiko na mahangaiko. Kazi zenye kuchosha, kazi zinazofanywa kwa zamu, na kazi zinazofanywa kwa saa nyingi huwaacha hata watu wanaopendana sana wakiwa wamechoka kihisia. Upendo na heshima zinaweza kudhoofishwa polepole na matatizo ya kiuchumi, matatizo ya kulea watoto, kuhamia nyumba nyingine, kubadilisha kazi, na matatizo ya kiafya. Kwa ufupi, mabadiliko yanayotukia kadiri wakati unavyopita yanaweza kuleta mfadhaiko unaoweza kuwatenganisha wenzi wa ndoa.
Akina mama wengi hufanya kazi mbili—kazi ya kuajiriwa na kazi za nyumbani. Hilo linaweza kuwanyima wakati wa kufanya mambo mengine isipokuwa kazi yao ya kuajiriwa na kutunza watoto. Kwa sababu ya mfadhaiko na uchovu, wenzi wengi hawana wakati wa kuwa pamoja. Hivyo, wengi huhisi kana kwamba hawawezi kudhibiti maisha yao na hilo huwafanya wakate tamaa na kujitenga.
-
-
Ni Matatizo Gani Yanayoweza Kutokea?Amkeni!—2008 | Julai
-
-
Ni Matatizo Gani Yanayoweza Kutokea?
SI JAMBO linalopatana na akili kutarajia kwamba ndoa haitakuwa na matatizo. Hata wenzi wanaofaana kabisa hawatapatana katika kila jambo. Kwa hiyo, matatizo fulani hayaepukiki. Kama vile tu kutu iliyo chini ya rangi inavyoweza kuharibu chuma kilichopakwa rangi, mambo kadhaa yanaweza kuharibu ndoa. Ili tujue mambo tunayoweza kufanya ili kuboresha ndoa, acheni kwanza tuchunguze baadhi ya matatizo yanayoweza kutokea.
Nyakati Zenye Kufadhaisha Sana
Biblia ilitabiri kwamba watu wengi wanaoishi nyakati zetu wangekuwa “wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, . . . wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi.” (2 Timotheo 3:2-4) Tabia hizo zinaweza kuongeza kutoelewana, kutowasiliana, na kusema bila kufikiri, jambo ambalo hufanyika kwa urahisi kwa sababu ya kutokuwa wakamilifu.
“Kwa waliofunga ndoa hiki si kipindi rahisi,” anasema mchunguzi mmoja. “Kwa upande mmoja . . . , tuna habari nyingi sana ambazo zinaweza kuimarisha ndoa zetu . . . Kwa upande mwingine, tunakabili uvutano mwingi wa kijamii na kiuchumi ambao unafanya iwe vigumu kuwa na ndoa nzuri.”
Matarajio Yasiyo Halisi
“Matarajio yasiyo halisi,” anasema mtaalamu mmoja wa ndoa, “ni moja kati ya visababishi vikubwa vya kutoridhika katika ndoa.” Watu wengi waliofunga ndoa hutamauka wanapogundua kwamba maisha ya ndoa si kama walivyoyatarajia na mwenzi wao ni tofauti na walivyofikiri atakuwa. Wanatamaushwa sana na kasoro za mwenzi wao ambazo hawakuwa wameziona au udhaifu ambao ni mkubwa kuliko walivyotarajia.
Hata hivyo, Biblia inasema waziwazi kwamba ndoa inaweza kusababisha “uchungu na huzuni.” (1 Wakorintho 7:28, The New English Bible) Kwa nini? Sababu moja ni kwamba muda si muda uhusiano kati ya watu wawili wasio wakamilifu utafunua kasoro zao.
Kwa kuongezea, watu wengi huwa na matarajio yasiyo halisi kwamba ndoa yao itakuwa na furaha bila kufanya jitihada zozote. Kwa kuwa wamepofushwa na wazo la kwamba watakuwa na ndoa yenye furaha mara moja, wanapuuza madaraka na bidii inayohitajiwa kusitawisha ndoa yenye furaha. Wanapogundua kwamba ndoa si kama walivyokuwa wamedhania, huenda wakachanganyikiwa na kukata tamaa. Kwa kawaida, kadiri wanavyokuwa na matarajio mengi yasiyo halisi ndivyo wanavyokatishwa tamaa hata zaidi.
Tatizo la Kuwasiliana
Ni makosa gani ya kuwasiliana yanayoweza kuepukwa ili kuwa na uhusiano wa ndoa wenye nguvu? Wenzi fulani wa ndoa huwa na zoea la kusikia bila kusikiliza kwa makini na kuzungumza bila kuwasiliana. Badala ya mazungumzo machangamfu na yenye upendo, wanazungumzia tu mambo ya lazima. Huenda ugomvi usiokoma kuhusu kitu chochote ukachukua mahali pa mazungumzo ya waziwazi kutoka moyoni. Ugomvi hutokea kwa sababu ya kumwelewa yule mwingine vibaya na mwenzi mmoja anaposhambuliwa kwa maneno anaamua kunyamaza.
Kwa kusikitisha, watu wengi hawaoni tabia nzuri za mwenzi wao wa ndoa au wakiziona hawawaambii wenzi wao kwamba wanazithamini. Isitoshe, kwa kuwa siku hizi huenda wenzi wote wakafanya kazi ya kuajiriwa, wanawake wengi walioolewa hukasirika kwa sababu wanaachiwa kazi zote za nyumbani. Pia, wake wengi huhisi kwamba mahitaji yao ya kihisia yanapuuzwa.
-