-
Ni Matatizo Gani Yanayoweza Kutokea?Amkeni!—2008 | Julai
-
-
Tatizo la Kuwasiliana
Ni makosa gani ya kuwasiliana yanayoweza kuepukwa ili kuwa na uhusiano wa ndoa wenye nguvu? Wenzi fulani wa ndoa huwa na zoea la kusikia bila kusikiliza kwa makini na kuzungumza bila kuwasiliana. Badala ya mazungumzo machangamfu na yenye upendo, wanazungumzia tu mambo ya lazima. Huenda ugomvi usiokoma kuhusu kitu chochote ukachukua mahali pa mazungumzo ya waziwazi kutoka moyoni. Ugomvi hutokea kwa sababu ya kumwelewa yule mwingine vibaya na mwenzi mmoja anaposhambuliwa kwa maneno anaamua kunyamaza.
Kwa kusikitisha, watu wengi hawaoni tabia nzuri za mwenzi wao wa ndoa au wakiziona hawawaambii wenzi wao kwamba wanazithamini. Isitoshe, kwa kuwa siku hizi huenda wenzi wote wakafanya kazi ya kuajiriwa, wanawake wengi walioolewa hukasirika kwa sababu wanaachiwa kazi zote za nyumbani. Pia, wake wengi huhisi kwamba mahitaji yao ya kihisia yanapuuzwa.
-
-
Jinsi ya Kuwa na Ndoa Yenye MafanikioAmkeni!—2008 | Julai
-
-
▸ Zungumza kwa heshima. “Kuna mtu anayesema bila kufikiri kama kwa upanga unaochoma, lakini ulimi wa mwenye hekima huponya.” (Methali 12:18) Wachunguzi wamegundua kwamba mazungumzo mengi huisha vile yalivyoanza. Kwa hiyo, ikiwa mazungumzo yanaanza kwa heshima, kuna uwezekano mkubwa kwamba yatamalizika vivyo hivyo. Kwa upande mwingine, unajua jinsi unavyoumia mpendwa anapokuambia jambo bila kufikiri. Hivyo, sali na ujitahidi kuzungumza kwa staha, heshima, na upendo. (Waefeso 4:31) “Hata ingawa kila mmoja huona udhaifu wa mwenzake,” anaeleza Haruko,b mwanamke Mjapani ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka 44, “tunajitahidi kuheshimiana kwa maneno na mtazamo. Hilo limetusaidia kuwa na ndoa yenye mafanikio.”
▸ Sitawisha fadhili na huruma. “Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo.” (Waefeso 4:32) Kunapokuwa na ugomvi mkali, mara nyingi mwenzi mmoja akikasirika yule mwingine hukasirika pia. Huko Ujerumani, Annette, ambaye amekuwa katika ndoa yenye furaha kwa miaka 34 anakiri hivi: “Si rahisi kuwa mtulivu chini ya mfadhaiko—inaelekea utasema mambo yatakayomkasirisha mwenzi wako, na kufanya hali iwe mbaya hata zaidi.” Hata hivyo, kwa kujitahidi kuwa mwenye fadhili na huruma, unaweza kuchangia sana katika kunyoosha njia ya kupata ndoa yenye amani.
▸ Onyesha unyenyekevu. ‘Usifanye jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu wa akili ukiwaona wengine kuwa ni bora.’ (Wafilipi 2:3) Ugomvi mwingi hutokea kwa sababu badala ya kujinyenyekeza na kutafuta njia za kuboresha hali, kiburi huwafanya watu walaumu wenzi wao matatizo yanapotokea katika ndoa. Unyenyekevu wa akili unaweza kukusaidia usisisitize kwamba wewe ndiye uko sawa ugomvi unapotokea.
▸ Usiudhike haraka. “Usiwe na haraka kuudhika katika roho yako.” (Mhubiri 7:9) Jaribu kuepuka mwelekeo wa kupinga maoni ya mwenzi wako au kujitetea haraka mwenzi wako akikuuliza kuhusu jambo ulilosema au kufanya. Badala yake, sikiliza maoni ya mwenzi wako. Fikiria kwa uangalifu kabla ya kujibu. Watu wengi hujifunza wakiwa wamechelewa mno kwamba kuwa na uhusiano wenye upendo na wenzi wao ni muhimu kuliko kushinda mabishano.
▸ Jua wakati wa kukaa kimya. ‘Uwe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.’ (Yakobo 1:19) Bila shaka, mawasiliano mazuri ni mojawapo ya ishara muhimu sana katika barabara inayoelekeza kwenye ndoa yenye furaha. Kwa nini basi Biblia inasema kwamba kuna “wakati wa kukaa kimya”? (Mhubiri 3:7) Huenda huo ukawa wakati wa kusikiliza kwa makini ili uelewe anachosema mwenzi wako, na hiyo ni sehemu muhimu ya mawasiliano inayotia ndani kujua hisia za mwenzi wako wa ndoa na kwa nini anahisi hivyo.
▸ Onyesha hisia-mwenzi unaposikiliza. “Shangilieni pamoja na watu wanaoshangilia; lieni pamoja na watu wanaolia.” (Waroma 12:15) Hisia-mwenzi ni muhimu ili kuwasiliana inavyofaa kwa sababu inakuwezesha kuhisi hisia za ndani kabisa za mwenzi wako. Sifa hiyo inawezesha kuwe na hali ambayo maoni na hisia za kila mmoja zinaheshimiwa. Nella kutoka Brazili ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka 32 anasema hivi: “Tunapozungumzia matatizo yetu, mimi husikiliza kwa makini ili nielewe mawazo na hisia za Manuel.” Mwenzi wako anapozungumza, huo ni “wakati wa kukaa kimya” na kumsikiliza ukionyesha hisia-mwenzi.
▸ Uwe na zoea la kuonyesha uthamini. “Mjionyeshe kuwa wenye shukrani.” (Wakolosai 3:15) Waume na wake katika ndoa imara huhakikisha kwamba wenzi wao wanajua jinsi wanavyowathamini. Hata hivyo, kwa sababu ya pilka-pilka za kila siku katika ndoa, watu fulani wamepuuza sehemu hiyo muhimu ya mawasiliano na kudhani kwamba wenzi wao wanajua wanathaminiwa. “Wenzi wengi,” anasema Dakt. Ellen Wachtel, “wangeweza kuonyeshana uthamini ikiwa wangekumbuka kufanya hivyo.”
Wake hasa wanahitaji kuhakikishiwa kwa upendo na kuonyeshwa na waume wao kwamba wanathaminiwa. Waume, mnaweza kufanya mengi kuboresha ndoa yenu na hali njema ya wake wenu na yenu wenyewe kwa kuwa na zoea la kuwapongeza wake wenu kwa sababu ya matendo mazuri na sifa zao.
Ni muhimu kumhakikishia hivyo kwa maneno na kwa matendo. Mume, unapombusu mke wako, kumgusa kwa wororo, na kutabasamu kwa uchangamfu, mambo hayo yanatimiza mengi zaidi ya kumwambia “nakupenda.” Kufanya hivyo kunamhakikishia kwamba yeye ni mwenye thamani kwako na unamhitaji. Mpigie simu au umwandikie ujumbe mfupi kwa simu ukimwambia, “ninakukosa” au ukimwuliza “Siku yako inaendeleaje?” Ikiwa umeacha mazoea hayo ambayo ulikuwa nayo mlipokuwa mkichumbiana, ingefaa uanze tena. Endelea kutafuta ni nini kinachomgusa moyo.
Maneno haya ya mama ya Mfalme Lemueli wa Israeli la kale yanafaa: “Mumewe huimba sifa zake. Husema, ‘Wanawake wengi wametenda mambo ya ajabu, lakini wewe umewashinda wote.’” (Methali 31:1, 28, 29, BHN) Wewe ulimsifu mke wako lini mara ya mwisho? Au ikiwa wewe ni mke, ulimsifu mume wako lini?
-