-
Jinsi ya Kuwa na Ndoa Yenye MafanikioAmkeni!—2008 | Julai
-
-
Kwa sababu sisi sote si wakamilifu, hatuwezi kuepuka kutoelewana na kutopatana. Hata hivyo mara nyingi, ndoa yenye mafanikio haitegemei kufaana kwa wenzi wa ndoa, bali inategemea jinsi wanavyokabiliana na mambo ambayo hawapatani. Hivyo, mbinu moja muhimu sana katika ndoa ni uwezo wa kusuluhisha mambo kwa upendo, kwa kuwa upendo “huunganisha kila kitu katika umoja ulio kamili.”—Wakolosai 3:14, Biblia Habari Njema.
▸ Zungumza kwa heshima. “Kuna mtu anayesema bila kufikiri kama kwa upanga unaochoma, lakini ulimi wa mwenye hekima huponya.” (Methali 12:18) Wachunguzi wamegundua kwamba mazungumzo mengi huisha vile yalivyoanza. Kwa hiyo, ikiwa mazungumzo yanaanza kwa heshima, kuna uwezekano mkubwa kwamba yatamalizika vivyo hivyo. Kwa upande mwingine, unajua jinsi unavyoumia mpendwa anapokuambia jambo bila kufikiri. Hivyo, sali na ujitahidi kuzungumza kwa staha, heshima, na upendo. (Waefeso 4:31) “Hata ingawa kila mmoja huona udhaifu wa mwenzake,” anaeleza Haruko,b mwanamke Mjapani ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka 44, “tunajitahidi kuheshimiana kwa maneno na mtazamo. Hilo limetusaidia kuwa na ndoa yenye mafanikio.”
▸ Sitawisha fadhili na huruma. “Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo.” (Waefeso 4:32) Kunapokuwa na ugomvi mkali, mara nyingi mwenzi mmoja akikasirika yule mwingine hukasirika pia. Huko Ujerumani, Annette, ambaye amekuwa katika ndoa yenye furaha kwa miaka 34 anakiri hivi: “Si rahisi kuwa mtulivu chini ya mfadhaiko—inaelekea utasema mambo yatakayomkasirisha mwenzi wako, na kufanya hali iwe mbaya hata zaidi.” Hata hivyo, kwa kujitahidi kuwa mwenye fadhili na huruma, unaweza kuchangia sana katika kunyoosha njia ya kupata ndoa yenye amani.
▸ Onyesha unyenyekevu. ‘Usifanye jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu wa akili ukiwaona wengine kuwa ni bora.’ (Wafilipi 2:3) Ugomvi mwingi hutokea kwa sababu badala ya kujinyenyekeza na kutafuta njia za kuboresha hali, kiburi huwafanya watu walaumu wenzi wao matatizo yanapotokea katika ndoa. Unyenyekevu wa akili unaweza kukusaidia usisisitize kwamba wewe ndiye uko sawa ugomvi unapotokea.
▸ Usiudhike haraka. “Usiwe na haraka kuudhika katika roho yako.” (Mhubiri 7:9) Jaribu kuepuka mwelekeo wa kupinga maoni ya mwenzi wako au kujitetea haraka mwenzi wako akikuuliza kuhusu jambo ulilosema au kufanya. Badala yake, sikiliza maoni ya mwenzi wako. Fikiria kwa uangalifu kabla ya kujibu. Watu wengi hujifunza wakiwa wamechelewa mno kwamba kuwa na uhusiano wenye upendo na wenzi wao ni muhimu kuliko kushinda mabishano.
▸ Jua wakati wa kukaa kimya. ‘Uwe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.’ (Yakobo 1:19) Bila shaka, mawasiliano mazuri ni mojawapo ya ishara muhimu sana katika barabara inayoelekeza kwenye ndoa yenye furaha. Kwa nini basi Biblia inasema kwamba kuna “wakati wa kukaa kimya”? (Mhubiri 3:7) Huenda huo ukawa wakati wa kusikiliza kwa makini ili uelewe anachosema mwenzi wako, na hiyo ni sehemu muhimu ya mawasiliano inayotia ndani kujua hisia za mwenzi wako wa ndoa na kwa nini anahisi hivyo.
▸ Onyesha hisia-mwenzi unaposikiliza. “Shangilieni pamoja na watu wanaoshangilia; lieni pamoja na watu wanaolia.” (Waroma 12:15) Hisia-mwenzi ni muhimu ili kuwasiliana inavyofaa kwa sababu inakuwezesha kuhisi hisia za ndani kabisa za mwenzi wako. Sifa hiyo inawezesha kuwe na hali ambayo maoni na hisia za kila mmoja zinaheshimiwa. Nella kutoka Brazili ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka 32 anasema hivi: “Tunapozungumzia matatizo yetu, mimi husikiliza kwa makini ili nielewe mawazo na hisia za Manuel.” Mwenzi wako anapozungumza, huo ni “wakati wa kukaa kimya” na kumsikiliza ukionyesha hisia-mwenzi.
-
-
Jinsi ya Kuwa na Ndoa Yenye MafanikioAmkeni!—2008 | Julai
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]
Mnapohitaji kuzungumzia tatizo fulani
◼ Pangeni kufanya hivyo wakati hamjachoka.
◼ Epukeni kuchambuana na muwe na mtazamo unaofaa.
◼ Epuka kumkatiza mwenzako anapoongea; kila mmoja awe na zamu ya kusikiliza na kuongea.
◼ Tambua hisia za mwenzi wako.
◼ Onyeshaneni hisia-mwenzi, hata msipokubaliana.
◼ Muwe na usawaziko na tayari kubadilikana.
◼ Omba msamaha kwa unyenyekevu unapokosea.
◼ Onyeshaneni uthamini na upendo.
-