Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Maadili ya Biblia Ndiyo Bora Kabisa?
    Mnara wa Mlinzi—2000 | Novemba 1
    • Usimwache Mwenzi Wako

      Muumba wetu alimwumba Adamu kisha akamwumba Hawa kuwa mwenzi wake. Muungano wao ulikuwa ndoa ya kwanza katika historia na ulipasa kuwa uhusiano wa kudumu. Mungu alisema: “Mwanamume atamwacha mama yake na baba yake naye ataambatana na mkewe.” Miaka 4,000 hivi baadaye, Yesu Kristo alirudia kiwango hicho cha ndoa kwa wafuasi wake wote. Zaidi ya hayo, alishutumu uhusiano wa ngono nje ya ndoa.—Mwanzo 1:27, 28; 2:24; Mathayo 5:27-30; 19:5.

      Kulingana na Biblia, funguo mbili muhimu za ndoa yenye furaha ni upendo na staha kutoka kwa wenzi wote wawili. Mume, ambaye ni kichwa cha familia, apaswa kuonyesha upendo usio na ubinafsi kwa kuzingatia masilahi ya mkewe. Anapaswa kuishi naye “kulingana na ujuzi” na hapaswi “[kumkasirikia] kwa uchungu.” Mke apaswa kumpa mume wake “staha yenye kina kirefu.” Wenzi wa ndoa wakifuata kanuni hizo, wanaweza kuepuka au kutatua magumu mengi ya ndoa. Mume atataka kushikamana na mkewe, na mke vivyo hivyo.—1 Petro 3:1-7; Wakolosai 3:18, 19; Waefeso 5:22-33.

      Je, kiwango cha Biblia cha kushikamana kwa uaminifu na mwenzi wa ndoa hufanya ndoa iwe yenye furaha? Fikiria matokeo ya uchunguzi uliofanywa nchini Ujerumani. Watu waliulizwa ni mambo gani yaliyo muhimu kwa ndoa nzuri. Mojawapo ya mambo muhimu zaidi yaliyotajwa ni uaminifu wa wenzi wote wawili. Je, hukubali kwamba watu waliofunga ndoa huwa na furaha zaidi wanapojua kwamba wenzi wao ni waaminifu?

      Vipi Matatizo Yakitokea?

      Iweje mume na mke wanapokosa kuafikiana kabisa-kabisa? Vipi upendo wao ukipoa? Je, haingefaa kuvunja ndoa chini ya hali kama hizo? Au je, kiwango cha Biblia cha kushikamana kwa uaminifu na mwenzi wa ndoa bado ni chenye busara?

      Waandishi wa Biblia walitambua kwamba wenzi wote waliofunga ndoa watakuwa na matatizo kwa sababu ya kutokamilika kwa binadamu. (1 Wakorintho 7:28) Hata hivyo, wenzi wa ndoa wanaofuata viwango vya maadili vya Biblia hujaribu kusamehe na kutatua magumu yao pamoja. Bila shaka, kuna hali fulani—kama vile uzinzi au kutendwa vibaya kimwili—ambazo kwa kufaa huenda zikamfanya Mkristo afikirie kutengana au kutalikiana. (Mathayo 5:32; 19:9) Lakini kuvunja ndoa harakaharaka bila sababu nzito au ili kupata mwenzi mwingine kwaonyesha ubinafsi na kutowajali wengine. Bila shaka hakutokezi maisha yenye utulivu au yenye furaha. Acheni tuchukue mfano mmoja.

      Peter alihisi kwamba ndoa yake haikuwa na uchangamfu kama hapo mwanzoni.a Kwa hiyo, akaacha mke wake na kuanza kuishi na Monika aliyekuwa amemwacha mumewe. Mambo yakawaje? Baada ya miezi michache tu, Peter alikiri kwamba “haikuwa rahisi [kuishi na Monika] kama nilivyowazia.” Kwa nini? Mwenzi huyu mpya alikuwa na kasoro zilezile za kibinadamu alizokuwa nazo yule wa kwanza. Jambo lililokuwa baya zaidi ni kwamba uamuzi wake wa haraka na wa ubinafsi ulimletea matatizo makubwa sana ya kifedha. Isitoshe, watoto wa Monika waliathirika sana kihisia-moyo kwa sababu ya badiliko kubwa lililoikumba familia yao.

      Kama ionyeshwavyo na jambo hili, ndoa inapokumbwa na matatizo, utatuzi si kuivunja. Kwa upande mwingine, wakati wa matatizo, kuishi kwa kupatana na kanuni za maadili za Neno la Mungu, Biblia, mara nyingi kwaweza kuokoa ndoa. Ilikuwa hivyo kwa Thomas na Doris.

      Thomas na Doris walikuwa wameoana kwa zaidi ya miaka 30 wakati Thomas alipoanza kunywa vileo kupindukia. Doris alipatwa na mshuko-moyo, na wote wawili wakazungumza kuhusu kutalikiana. Doris alizungumza jambo hilo pamoja na mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Shahidi huyo alimwonyesha Doris yale ambayo Biblia husema kuhusu ndoa, na kumtia moyo asifanye haraka kutengana na mume wake lakini kwanza ajaribu kutatua matatizo yake pamoja naye. Doris akafanya hivyo. Baada ya miezi michache, hawakuzungumza tena kuhusu talaka. Thomas na Doris walikuwa wakitatua matatizo yao pamoja. Kufuata shauri la Biblia kuliimarisha ndoa yao na kukawapa wakati wa kutatua matatizo yao.

  • Je, Maadili ya Biblia Ndiyo Bora Kabisa?
    Mnara wa Mlinzi—2000 | Novemba 1
    • Zaidi ya hayo, wenzi wa ndoa waaminifu ndio msingi wa familia thabiti. Watu wengi watakubaliana na mwanasiasa mmoja wa Ulaya aliyesema hivi: “Kufikia sasa familia [ya kawaida] bado ndiyo huandaa mahali panapofaa sana kwa ajili ya usalama na maisha yenye maana ya wanadamu.” Amani katika familia huwapa watu wazima na watoto fursa bora kabisa ya kupata usalama wa kihisia-moyo. Kwa hiyo wale ambao ni waaminifu katika ndoa wanasaidia kujenga jamii thabiti.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki