Tunza
Mheshimu Yehova Katika Maisha Yako—Sehemu ya 1—Katika Familia
1, 2. Vikumbusho vina umuhimu gani maishani mwetu?
1 “Kwa kupatana na Mtakatifu aliyewaita, ninyi wenyewe pia iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote, kwa sababu imeandikwa: ‘Muwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.’”—1 Pet. 1:15, 16.
2 Kwa miaka mingi, Yehova ametumia tengenezo lake kwa njia nyingi kutusaidia kufanya upya akili zetu katika mambo mengi. Leo, wengi wetu tunajua vizuri jinsi ya kutumia kanuni za Kimaandiko maishani. Hata hivyo, inafaa kurudia kanuni fulani kwa ajili ya wote, hasa wapya wengi ambao wamemjua Yehova hivi karibuni.—Rom. 12:2; 2 Pet. 1:12; 3:1.
Tunaionaje Ndoa?
3. Taja baadhi ya watumishi wa Yehova ambao walikuwa waseja.
3 Ingawa ndoa ilianzishwa na Mungu, je, hiyo ndiyo njia pekee ya kupata furaha? (Mhu. 12:13; Marko 12:30) Biblia ina mifano mingi ya watu waliomtumikia Yehova kwa furaha wakiwa waseja. Binti ya Yeftha alitimiza kiapo cha baba yake kwa kudumu akiwa mseja katika jamii iliyothamini sana ndoa na kuzaa watoto. (Amu. 11:34-40) Binti wanne wa Filipo ambao hawakuolewa ‘walitoa unabii,’ na bila shaka walipata uradhi mwingi katika utumishi wao uliomletea Yehova sifa. Yesu, aliye mfano wa “Mungu mwenye furaha,” hakufunga ndoa. (Mdo. 21:8, 9; 1 Tim. 1:11) Hivyo, haifai kuwadharau Wakristo wanaomtumikia Yehova wakiwa waseja.
4. Maoni ya kimapokeo kuhusu ndoa yana ubaya gani?
4 Ibada ya mababu imechangia maoni yasiyofaa kuhusu ndoa. Wazo la kwamba uhai wa mababu unapaswa “kuendelezwa,” linaweza kuwafanya wengi wakate kauli kwamba ni lazima wafunge ndoa na kuzaa watoto. Wengine wanaamini kwamba wasipofanya hivyo, mababu watakasirika. Lakini sisi Wakristo tunajua kwamba wafu “hawajui lolote kamwe.” Wamelala, na ufufuo ndilo tumaini lao la pekee. (Mhu. 9:5; Mdo. 24:15) Wakristo wote wanapaswa kujihadhari wasiathiriwe na mafundisho ya uwongo, na hakuna yeyote anayepaswa kuwadhihaki waseja eti kwa sababu hawajafunga ndoa.
5. (a) Biblia ina maoni gani kuhusu ndoa? (b) Watu fulani wametumiaje maisha yao ya useja kuendeleza kazi ya Ufalme?
5 Andiko la 1 Wakorintho 7:8, 9, 28, 32-34, na 38 lina maoni yaliyosawazika sana kuhusu ndoa. Wakristo hawajakatazwa kufunga ndoa. Ingefaa wale wasiofurahia kuwa waseja au wale wanaoweza kutumbukia kwa urahisi katika ukosefu wa maadili wafunge ndoa. Ndoa itatatua matatizo fulani, lakini itasababisha mengine. Mtume Paulo alisema kwamba waseja ‘watafanya vema’ kiroho iwapo hawatafunga ndoa. Ndugu na dada wengi wameamua kubaki waseja kwa muda fulani au kwa maisha yao yote. Ndugu na dada wengi waseja ni mapainia wa kawaida au wa pekee. Wengine ni watumishi wa kujitolea katika makao ya Betheli. Yehova hasahau uaminifu wao. (Ebr. 6:10) Wazazi, je, hamngefurahi ikiwa watoto wenu wangekuwa watumishi wa wakati wote kwa muda fulani kabla ya kufunga ndoa?
Mtu Unayeweza Kufunga Ndoa Naye
6, 7. (a) Kwa nini ni muhimu kufunga ndoa “katika Bwana”? (b) Mtu anapaswa kuchunguza mambo gani kumhusu mtu anayetarajia kufunga ndoa naye?
6 Maandiko yanatushauri tusifungwe nira isivyo sawa na wasioamini. (2 Kor. 6:14, 15) Mkristo anayepuuza shauri hilo hana hekima hata kidogo. Mtu asiyeamini ambaye anataka kufunga ndoa na Mkristo anaweza kuonekana kuwa mpole na asiyepinga kweli. Huenda hata akahudhuria mikutano ya Kikristo. Hata hivyo, anaweza kubadilika baada ya kufunga ndoa. Isitoshe, hatupaswi kufikiri kwamba Yehova atabariki ndoa ya watu ambao wanaamua kuvunja kimakusudi sheria zake kuhusu kufunga ndoa.—Ayu. 9:4b.
7 Utambuzi unahitajiwa hata mtu anapofunga ndoa “katika Bwana.” (1 Kor. 7:39) Mchunguze mtu kabla ya kukubali kufunga ndoa naye. Chunguza ikiwa anamtii Yehova, anathamini mambo ya kiroho, ana mazoea mazuri ya kujifunza, ni mnyenyekevu, mwenye fadhili, na kadhalika. Zungumza na Wakristo wakomavu wanaomjua vizuri. Vipi ikiwa bado una shaka? Kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia kinasema: “Shaka hizo zapaswa kufikiriwa kwa uangalifu. Hata iwe unahisi kimahaba jinsi gani au hata iwe una wasiwasi jinsi gani juu ya kufunga ndoa, usipuuze makosa mazito. (Mithali 22:3; Mhubiri 2:14) Ikiwa una uhusiano pamoja na mtu ambaye una shaka nzito juu yake, ni jambo la hekima kukatiza uhusiano huo na kuepuka uwajibikaji wenye kudumu pamoja na mtu huyo.” Kwa kuwa ndoa ni kifungo cha kudumu, ni muhimu uwe na uhakika kabisa kabla ya kufunga ndoa.—Mt. 19:5, 6.
Wajibu wa Mume
8. Eleza jinsi mwenendo wa mume akiwa kichwa unavyohusiana na ibada yake.
8 Mwanamume anapooa, yeye hupoteza kwa kadiri fulani uhuru wake, na hilo ni jambo gumu kwa wanaume fulani. Mume Mkristo anatambua kwamba ndoa ni takatifu. Asipomtunza mke wake ifaavyo, uhusiano wake na Yehova utaathiriwa. (1 Tim. 5:8) Badala ya kumtawala mke wake, yeye humwongoza kwa fadhili, akizingatia hali yake ya kimwili na kihisia. (1 Pet. 3:7) Atamsaidia kufanya kazi za nyumbani inapohitajika. Miaka kadhaa iliyopita, gazeti moja la Amkeni! lilisema: “Huenda waume wengi katika tamaduni fulani wasifurahie jambo hili, hata hivyo, ni muhimu kuwa na mpango mzuri wa kusaidiana kufanya kazi za nyumbani, hasa ikiwa mke pia ameajiriwa.” Mume atazingatia sana hali ya kiroho ya mke wake, naye atamwongoza katika funzo la familia, huduma ya shambani, na shughuli nyingine za Kikristo.
9. Mume anaweza kutimizaje mahitaji ya kimwili na ya kihisia ya mke wake?
9 Kwa kumwiga Yesu na kufuata mafundisho yake, mume Mkristo humpenda mke wake kama anavyojipenda mwenyewe. (Mt. 19:19; Efe. 5:28) Hilo linapaswa kuonekana kupitia jinsi anavyomtendea. Kwa mfano, hatakula chakula kizuri na kumpa makombo. Hatatumia nusu ya mshahara wake na kumwacha mke ataabike kulisha familia nzima kwa ile nusu nyingine. Mume atafanya mambo pamoja na mke wake: atatembea naye, ataketi naye, atamsikiliza, na atapanga kufanya mambo pamoja naye.
10. Mume Mkristo anapaswa kuwafafanulia watu wake wa ukoo jambo gani kuhusu ukichwa?
10 Katika maeneo fulani, mke huonwa kuwa mali ya jamaa wala haonwi kuwa msaidizi na kikamilisho cha mume wake. Huenda watu wa ukoo wa mume wakajaribu kumdhibiti kabisa mke wa mume Mkristo. Lakini Biblia inasema kwamba wake wanapaswa wajitiishe “kwa waume zao.” (Efe. 5:24) Mke atawaheshimu watu wa ukoo wa mume wake, lakini atamtii mume wake. Mume Mkristo atamwepusha mke wake na matatizo kwa kuwafafanulia watu wake wa ukoo kanuni ya ukichwa.
Wajibu wa Mke
11. Mke anapaswa kumwonaje mume wake, na Yehova anaonaje jambo hilo?
11 Sawa na mume wake, mke Mkristo hataendelea kuwa na uhuru aliokuwa nao alipokuwa mseja. Sasa yeye ni mwili mmoja na mume wake, ni “kikamilisho” chake. (Mwa. 2:18) Atasitawisha sifa kama vile “roho ya utulivu na ya upole, ambayo ni ya thamani kubwa machoni pa Mungu.” (1 Pet. 3:1-6) Mume akimtendea kwa fadhili, mke hatamwona kuwa dhaifu na kujaribu kunyakua ukichwa. Badala yake, atajitahidi kufuata mwongozo wa kiroho unaotolewa na mume wake. Akijitiisha, Yehova atafurahi.
12. Kulingana na Methali 31:10-31, ungemfafanuaje mwanamke Mkristo?
12 Wanawake Wakristo wanapaswa kupongezwa kwa kuwa na sifa nyingi nzuri. Inafaa kuchunguza masimulizi ya Methali 31:10-31 kumhusu mke mwenye uwezo. Mwanamke huyo hakufanya kazi za nyumbani tu, bali pia alinunua mashamba, akapanda shamba na kupata mazao, na kuendesha biashara ndogo. Katika hizi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” wake wengi wamelazimika kuajiriwa. (2 Tim. 3:1) Hata hivyo, bado mke aliyeajiriwa huangalia “shughuli za nyumba yake.” (Met. 31:27) Huo ni wajibu wake, wala si wajibu wa mtumishi wa nyumbani au wa mtu fulani wa ukoo. Familia ya Kikristo itanufaika mke akiweza kupunguza muda anaotumia kazini.
Haki ya Ndoa
13. Kwa nini mume anapaswa kumfikiria mke wake inapohusu ngono?
13 Maoni ya ulimwengu kuhusu ngono hayapatani na ya Yehova. Hata hivyo, mume Mkristo hufuata shauri la Yehova na kumtendea mke wake kwa upendo inapohusu ngono. Yeye hufikiria hali ya kimwili na ya kihisia ya mke wake, na hamlazimishi afanye jambo lolote analochukia. Kupatana na hilo, toleo la Mnara wa Mlinzi la Juni 1, 1989 linasema: “Katika Israeli, sheria ziliweka mipaka juu ya utendaji wa ngono hata ndani ya kifungo cha ndoa. Mume alipaswa kujiepusha kufanya ngono na mke wake wakati wa kipindi chake cha hedhi. (Law. 15:24; 18:19; 20:18) Jambo hilo lilitaka ufikirio wenye upendo na kujidhibiti kwa upande wa wanaume Waisraeli. Je! Wakristo wapungukiwe na ufikirio huo kuelekea wake zao? Mtume Petro anasema kwamba waume Wakristo wanapaswa kukaa pamoja na wake zao ‘kulingana na ujuzi,’ yaani, ujuzi kuhusu hali yao wakiwa ‘chombo dhaifu zaidi, yaani, mwanamke.’—1 Petro 3:7.”
14. Mume na mke wanaweza kuepukaje ‘kunyimana’ haki ya ndoa?
14 Kwa upande mwingine, Biblia inawashauri mume na mke hivi: “Msiwe mkinyimana [haki ya ngono].” (1 Kor. 7:3, 5) Mume au mke hapaswi kumnyima mwenzake haki ya ngono ili afanyiwe jambo fulani. Isitoshe, si hekima hata kidogo kwa mume na mke kutengana kwa muda mrefu kwa sababu ya kazi ya kimwili. Mara nyingi waume huacha familia zao mashambani na kwenda kufanya kazi mijini. Hatua hiyo isiyo ya hekima humpa Shetani nafasi ya kuwashawishi waume na wake watumbukie katika ukosefu wa maadili.
Kuzaa na Kulea Watoto
15. Ni baraka gani wanazopata wenzi wa ndoa wanaoamua kutopata watoto kwa muda fulani kwa ajili ya Ufalme?
15 Watoto ni thawabu kutoka kwa Yehova, nao huwaletea shangwe wazazi wao. (Zab. 36:9; 127:3) Baada ya kufikiria hali yao kwa makini, mume na mke wana daraka la kuamua kupata au kutopata watoto. Yehova amewabariki sana wenzi wa ndoa fulani ambao wameamua kutopata watoto kwa muda fulani ili wafanye kazi ya Ufalme. Wengi wao ni mapainia wa kawaida au wa pekee, waangalizi wanaosafiri, au watumishi wa kujitolea katika Betheli mbalimbali.a Lakini, ni jambo la kawaida kwa wenzi wengi wa ndoa kuamua kupata watoto. Vipi wakiamua kupata watoto?
16. (a) Kwa nini ni jambo la hekima kutopata watoto wengi? (b) Mume na mke wanapaswa kuzingatia nini wanapochagua njia ya kudhibiti uzazi?
16 Machoni pa Yehova, Wakristo wana wajibu wa kuwalea watoto wao ifaavyo. Lakini imekuwa vigumu kwa wazazi walio na watoto wengi kufanya hivyo. Kwa hiyo, ni muhimu wazazi wakubaliane watapata watoto wangapi. Je, Wakristo wanaweza kutumia njia za kuzuia kupata mimba ili wasipate watoto wengi? Mume na mke ndio wanaopaswa kufanya uamuzi huo. Hata hivyo, toleo la Amkeni! la Februari 22, 1993, linasema: “Njia ya kudhibiti uzazi ambayo mume na mke wanachagua yapaswa kuongozwa na staha yao kwa utakatifu wa uhai. Kwa kuwa Biblia huonyesha kwamba uhai wa mtu huanza wakati wa mtungo wa mimba, Wakristo wangeepuka vizuia-mimba ambavyo huharibu mimba, au kuangamiza uhai wa mtoto anayekua. . . . Madaktari na kliniki za kupanga uzazi zimetayarishwa ili kutoa shauri juu ya njia za kudhibiti uzazi na kuwasaidia waume na wake wachague ile inayotimiza vizuri zaidi mahitaji yao.”
17, 18. (a) Funzo la familia husaidiaje kuwazoeza watoto? (b) Toa mfano unaoonyesha jinsi wazazi wanavyoweza kuwasaidia watoto wao waelewe sababu za Kimaandiko za kutofanya jambo la fulani.
17 Kuna jambo fulani lililo muhimu zaidi kuliko kutimiza mahitaji ya kimwili ya familia. Biblia huwaagiza akina baba wawalee watoto wao “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Efe. 6:4). Hilo linatia ndani nini? Kuwazoeza ili wawe watumishi waaminifu wa Yehova. Ili ufanikiwe, unahitaji kuwafundisha watoto kwa kuwawekea mfano mzuri. (Yoh. 5:19) Rekebisha hali zako ili uweze kuwaongoza katika ibada ya Yehova. Kumbuka kwamba ili ufanikiwe kumzoeza kila mtoto, unahitaji kumpenda na kumjali sana, na pia kutumia wakati mwingi pamoja naye. Watoto ndio wanaoumia ikiwa wazazi hawapatikani nyumbani mara nyingi kwa sababu ya kuwatembelea rafiki zao badala ya kuwa pamoja na watoto wao.
18 Watoto wanapokuwa na umri wa kutosha, wasaidie waelewe sababu za kufanya au kutofanya mambo. Badala tu ya kuwaambia, “jambo hili ni baya,” “hatufanyi mambo kama haya,” au “jambo hili halikubaliwi,” wape sababu za Kimaandiko zinazoonyesha ubaya wa jambo fulani. Kwa mfano, unapozungumza nao kuhusu jinsi Yehova anavyoona uhai wa wanyama, unaweza kutumia andiko la Yona 4:11, linaloonyesha kwamba Yehova hakuwarehemu tu watu wa Ninawi, bali pia “wanyama wengi wa kufugwa.” Hali kadhalika, waonyeshe kwa nini inafaa kushukuru, kusema kweli, na kuwa safi. Kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu kimekusudiwa kukusaidia kuwafundisha watoto wako kanuni za Kikristo.
19. Wazazi wanapaswa kuzungumzia miradi gani ya kiroho pamoja na watoto wao?
19 Wawekee watoto wako miradi ya kiroho. Zungumzia pamoja nao faida za kuwa wahubiri wa wakati wote. Waalike mapainia nyumbani kwenu. Ikiwezekana, tembelea Betheli pamoja na watoto wako. Wanapofunga shule, watie moyo watoto ambao wamebatizwa wawe mapainia wasaidizi. Ni kweli kwamba mazoezi hayo yanaweza kupingana na maoni ya jamii kuwahusu watoto. Lakini ukiwapa mazoezi hayo utakuwa ukiweka msingi wa familia imara na yenye furaha.
20. Wazazi wanaweza kufuataje himizo la Kumbukumbu la Torati 6:6, 7?
20 Katika maeneo mengi ya Afrika, watoto huonwa kuwa bima ya uzeeni kwa wazazi wao. Wazazi walio na maoni hayo wana mwelekeo wa kuwapongeza watoto wao kwa kufanya vema shuleni wala si kwa kuwa wenye bidii kutanikoni. Wengine wako tayari kuwapeleka watoto wao kwenye shule za bweni zinazotoa elimu bora, lakini ambazo zinawapa watoto nafasi ndogo au zinawanyima kabisa uhuru wa kumtumikia Yehova. Watoto fulani wamedhoofika sana kiroho shuleni hivi kwamba wanapolazimishwa na walimu, wao hujihusisha na mambo ya dini za uwongo. Wazazi kama hao wameshindwa kabisa kutimiza mahitaji ya kiroho ya watoto wao!—Kum. 6:6, 7.
21. Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu elimu?
21 Tunahitaji kuwa na maoni yaliyosawazika kuhusu elimu. Huduma Yetu ya Ufalme ya Agosti 1999 inasema: “Kupata elimu nzuri ya msingi unapokuwa mchanga kwaweza kukupa stadi zinazohitajiwa ili uweze kusoma na kuandika vizuri . . . Wakati uo huo, unaweza kujifunza kufikiri waziwazi, kuchanganua mambo, kutatua matatizo, na kutoa mawazo yenye kusaidia.” Naam, inapowezekana ni muhimu watoto wote wapate elimu ya msingi. Hata hivyo, watoto wengi ambao wameenda kusoma au kupata elimu ya ziada mbali na nyumbani, wameiacha kweli. Wengine waliokuwa na mradi wa kuwa mapainia, wamefuatia mali baada ya kumaliza masomo chuoni. Mtu hupata hasara kubwa sana ya kiroho kwa sababu ya kufuatilia elimu kama hiyo! Elimu kuhusu kanuni za Biblia ndiyo elimu muhimu zaidi kwa mtoto. Anapaswa kujua jinsi ya kumsifu Yehova. Wazazi wanaompa Yehova watoto wao kwa ajili ya utumishi wa wakati wote, wanaweza kuwa na hakika kwamba hatawaacha watakapozeeka.—Zab. 37:25.
22. Familia itapata baraka gani wazazi wakiwasaidia watoto wao kumcha Mungu?
22 Jitihada na wakati zinahitajiwa ili kuwa na familia inayomcha Mungu. Wazazi watabarikiwa sana wakichukua wajibu wao kwa uzito. Wote katika familia watafurahi na “kuona mema kwa ajili ya kazi [yao] yote iliyo ngumu.”—Mhu. 2:24; 3:12, 13.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa mfano, ona Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 2000, ukurasa wa 20-23.