-
Rebeka—Mwanamke Mwenye Bidii Aliyemwogopa MunguMnara wa Mlinzi—2004 | Aprili 15
-
-
Je, Rebeka Ana Sifa Zinazohitajiwa?
Rebeka ni mjukuu wa ndugu ya Abrahamu. Yeye haogopi kuongea na mtu asiyemjua, wala si mwenye urafiki kupita kiasi. Anakubali kumpatia Eliezeri maji anapomwomba. Ingetazamiwa afanye hivyo kwa kuwa hilo ni tendo la heshima. Namna gani sehemu ya pili ya jaribu hilo?
Rebeka anasema: “Kunywa, bwana wangu.” Lakini si hayo tu, bali anaongeza hivi: “Nitateka maji pia kwa ajili ya ngamia zako mpaka wamalize kunywa.” Anajitolea kufanya mengi zaidi ya yale ambayo kwa kawaida angetazamiwa kufanya. Kwa haraka, ‘anamimina upesi maji ya mtungi wake ndani ya chombo cha kunyweshea wanyama na kukimbia tena na tena kisimani ili kuteka maji, naye anaendelea kuteka kwa ajili ya ngamia zake wote.’ Anafanya kazi hiyo kwa bidii sana. Masimulizi hayo yanasema, ‘Wakati huo wote yule mwanamume anamkazia macho kwa kustaajabu.’—Mwanzo 24:19-21.
Anapotambua kwamba mwanamke huyo kijana ni wa jamaa ya Abrahamu, Eliezeri anasujudu kwa kumshukuru Yehova. Anamuuliza Rebeka kama yeye na watu anaoandamana nao wanaweza kupata nafasi ya kulala usiku nyumbani kwa baba yake. Rebeka anamwambia kuna nafasi kisha anakimbia nyumbani kuwapasha habari kuhusu wageni hao.—Mwanzo 24:22-28.
Baada ya kumsikiliza Eliezeri, Labani, ndugu ya Rebeka, na baba yake, Bethueli, wanatambua kwamba Mungu ndiye anayeongoza mambo. Hakika Rebeka amechaguliwa awe mke wa Isaka. Wanasema, “Mchukue uende, na awe mke wa mwana wa bwana wako, kama vile ambavyo Yehova amesema.” Rebeka anahisije? Anapoulizwa kama ataondoka mara moja, yeye anajibu kwa neno moja tu la Kiebrania linalomaanisha: “Mimi niko tayari kwenda.” Yeye halazimishwi kukubali aolewe na Isaka. Abrahamu alikuwa amemwambia Eliezeri waziwazi kwamba angekuwa amewekwa huru kutoka kwenye kiapo chake ‘ikiwa huyo mwanamke hatataka’ kuondoka. Lakini Rebeka pia anatambua kwamba Mungu ndiye anayeongoza mambo. Hivyo, anaacha familia yake mara moja na kwenda kuolewa na mwanamume ambaye hamjui. Uamuzi huo wa ujasiri ni wonyesho wa kipekee wa imani. Bila shaka, yeye ndiye anayefaa kuwa mke wa Isaka!—Mwanzo 24:29-59.
Anapokutana na Isaka, Rebeka anajifunika uso kama ishara ya ujitiisho. Isaka anamchukua awe mke wake, na bila shaka anaanza kumpenda kwa sababu ya sifa zake bora.—Mwanzo 24:62-67.
-
-
Rebeka—Mwanamke Mwenye Bidii Aliyemwogopa MunguMnara wa Mlinzi—2004 | Aprili 15
-
-
Mambo tunayojua kumhusu Rebeka hufanya tuvutiwe naye. Alikuwa mrembo sana, lakini urembo wake halisi ulihusiana na ujitoaji wake kimungu. Hiyo ndiyo sifa ambayo Abrahamu alitaka binti-mkwe wake awe nayo. Yaelekea alikuwa na sifa nyingine nyingi tena nzuri kuliko vile Abrahamu alivyotazamia. Imani na ujasiri wake katika kufuata mwongozo wa Mungu, pamoja na bidii, kiasi, na ukarimu wake, ni sifa ambazo wanawake wote Wakristo wanapaswa kuiga. Hizo ndizo sifa ambazo Yehova mwenyewe hutafuta katika mwanamke ambaye kwa kweli ni kielelezo kizuri.
-