-
Je, Ndoa Inaweza Kustahimili Msukosuko?Amkeni!—2006 | Julai
-
-
Je, Ndoa Inaweza Kustahimili Msukosuko?
“Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”—MATHAYO 19:6.
NYUMBA zilizoonekana kuwa imara zilibomolewa kabisa. Hivi karibuni dhoruba kali zilipokumba maeneo makubwa ulimwenguni, ubora na udumifu wa majengo mengi ulijaribiwa.
Leo, ndoa zinaweza kulinganishwa na nyumba ambayo msingi wake unapigwa na dhoruba. Stephanie Coontz, mwanahistoria wa masuala ya ndoa, anasema kwamba “watu na jamii hawaiheshimu tena ndoa.”
Je, unaona madhara yanayoletwa na mtazamo huo? Je, unahisi kwamba jamii haiheshimu tena ndoa? Ikiwa ndivyo, kwa nini? Na mtu anaweza kuwa na tumaini gani la kuwa na ndoa yenye furaha au kuidumisha ikiwa hivyo? Hata hivyo, kwanza kabisa ni nini kinachohatarisha ndoa?
Ndoa Yashambuliwa
Ndoa imekuwa ikishambuliwa tangu mwanzo wa historia ya wanadamu. Sifa na mitazamo iliyokuzwa na wazazi wetu wa kwanza imetokeza msukosuko tunaoona leo katika ndoa. Adamu na Hawa walifanya dhambi walipojiruhusu washindwe na tamaa za kibinafsi na hivyo ‘dhambi ikaingia katika ulimwengu.’ (Waroma 5:12) Rekodi ya historia ya Biblia inasema kwamba punde baada ya hapo, “kila mwelekeo wa fikira za moyo [wa mwanadamu] ulikuwa mbaya tu wakati wote.”—Mwanzo 6:5.
Hali haijabadilika sana tangu wakati huo. Kati ya maelekeo yenye kudhuru ambayo yanakabili ndoa ni kujaribu kujitosheleza bila kujizuia. Huenda mpango wa ndoa ukaonekana kuwa umepitwa na wakati na kwamba haufai katika ulimwengu wa kisasa unaoongozwa na maadili mapya. Na kulegezwa kwa sheria ambazo huzuia kuvunjika kwa ndoa kumeondoa aibu ambayo hapo awali ilihusianishwa na talaka.
Watu wasio na subira ambao hutaka kujitosheleza mara moja, hawafikirii sana au hawafikirii hata kidogo kuhusu madhara ya talaka. Wakidhani kwamba watapata uhuru, wanaamini kuwa talaka italeta furaha.
Watu fulani wanapokabili matatizo magumu katika ndoa, wao hutafuta msaada wa washauri wa ndoa au vitabu vilivyoandikwa na watu hao. Kwa kusikitisha, baadhi ya “wataalamu” wa ndoa wa kisasa wamekuwa wakichochea talaka badala ya kutetea ndoa. Kitabu The Case for Marriage kinasema kwamba “labda kwa mara ya kwanza katika historia ya wanadamu, ndoa, mpango ambao umeheshimiwa kwa muda mrefu, inazidi kushambuliwa kwa mafanikio. Nyakati nyingine ndoa hushambuliwa moja kwa moja na ‘wataalamu’ wanaoamini kwamba ni jambo lenye kukandamiza au lisilopatana na akili kuweka nadhiri ya kuishi pamoja muda wote wa maisha.”
Maoni ya Watu Yamebadilika
Pia maoni ya watu kuhusu ndoa na kusudi la ndoa yamebadilika. Labda umeona kwamba watu hawaoni umuhimu wa wenzi wa ndoa kuwa waaminifu na kutegemezana. Jambo kuu kwao ni kujitosheleza hata ikiwa mara nyingi kufanya hivyo kutamuumiza mwenzi yule mwingine. Jarida Journal of Marriage and Family linasema kwamba badiliko hilo la maoni ya ubinafsi kuhusu ndoa “lilianza katika miaka ya 1960 na kuongezeka haraka katika miaka ya 1970.” Sababu za msingi ambazo ziliwafanya watu wafunge ndoa, kama vile kutamani kupendwa, kuwa na uhusiano wa karibu, uaminifu, watoto, na kutoshelezana, hazionwi kuwa muhimu sana.
Matukio mengine ya hivi karibuni yamechangia sana kubadilika kwa ndoa katika nchi nyingi. Kwanza, katika nchi nyingi, majukumu ya mwanamume ya kutafuta riziki na ya mwanamke ya kutunza nyumba yamebadilika. Kwa kuwa wanawake wameanza kufanya kazi za kuajiriwa, kumekuwa na ongezeko la familia ambazo waume na wake hufanya kazi. Pili, kupata watoto nje ya ndoa ni jambo linalozidi kukubaliwa, hivyo kuongeza idadi ya familia zenye mzazi mmoja. Tatu, watu wengi zaidi wanaishi pamoja bila kufunga ndoa. (Ona sanduku “Si Thabiti Kama Ndoa.”) Nne, ndoa kati ya watu wa jinsia moja na harakati zinazotetea kuhalalishwa kwa ndoa hizo zimeungwa mkono na watu wengi. Je, matukio hayo ya kisasa yameathiri maoni yako kuhusu ndoa?
Ongezeko la Talaka
Na tuchunguze nchi kadhaa ili tuone jinsi ambavyo kuongezeka kwa talaka kumeathiri ndoa sana. Ripoti moja ya hivi karibuni inasema kwamba nchini Marekani, “idadi ya wenzi waliotalikiana iliongezeka mara nne kati ya mwaka wa 1970 na 1996.” Inakadiriwa kwamba ndoa 1 kati ya 5 zimeishia katika talaka. Ni ndoa zipi ambazo huvunjika kwa urahisi? Takwimu zinaonyesha kwamba asilimia 60 hivi ya talaka hutukia katika miaka kumi ya kwanza ya ndoa.
Pia, katika nchi nyingine idadi ya talaka imeongezeka. Mnamo 2004, jumla ya talaka nchini Uingereza na Wales ilifikia 153,490. Nchini Australia, inatazamiwa kwamba karibu asilimia 40 ya ndoa zitaishia kwenye talaka. Katika Jamhuri ya Korea, kulikuwa na ongezeko la talaka 21,800 katika mwaka mmoja tu, kuanzia 2002 hadi 2003. Katika kipindi hicho, jumla ya wenzi wa ndoa 167,100 walitalikiana. Idadi ya talaka nchini Japani, ambako ndoa 1 kati ya 4 huishia katika talaka, sasa inakaribia ile ya Ulaya. “Hapo zamani ndoa mbaya kabisa ndizo ziliishia kwenye talaka,” akasema mtaalamu wa masuala ya familia katika Chuo Kikuu cha Red Cross nchini Japani. “Sasa talaka zimekuwa mtindo wa maisha.”
Katika nchi nyingi dini na desturi za kijamii zilichangia kuimarishwa kwa kifungo cha ndoa. Hata hivyo, haziwezi kuzuia mwelekeo wa jamii wa kukubali talaka. Kwa mfano, fikiria Kanisa Katoliki, ambalo huiona ndoa kuwa takatifu. Mnamo 1983 kanisa hilo lililegeza sheria zake kuhusu ndoa na kufanya iwe rahisi zaidi kwa Wakatoliki kuvunja ndoa. Kwa hiyo, ndoa nyingi zimevunjwa tangu wakati huo.
Ni wazi kwamba, kanuni ambazo hushikilia ndoa zinazorota. Lakini si visababishi vyote vinavyoonekana wazi. Kwa kweli, mbali na kuzorota kwa jamii, kuna kisababishi kingine kikubwa cha kuongezeka kwa kuvunjika kwa ndoa ambacho hakionekani waziwazi na wanadamu wengi.
Kisababishi Kisicho Wazi cha Msukosuko Uliopo
Biblia inatuambia kwamba Shetani Ibilisi, ambaye ndiye chanzo cha ubinafsi, ametokeza uvutano mbaya usioonekana ulimwenguni. Kwa nini? Kwa sababu ametupwa kutoka mbinguni hadi kwenye ujirani wa dunia naye ana hasira kali. Kwa kweli, amekusudia kusababisha “ole,” au taabu nyingi iwezekanavyo, na mpango wa Mungu wa ndoa ni moja tu kati ya shabaha za hasira kali ya Shetani.—Ufunuo 12:9, 12.
Akizungumza kuhusu jinsi ambavyo hali ingekuwa baada ya Shetani kufukuzwa kutoka mbinguni, Yesu alisema hivi: “Kwa sababu ya kuongezeka kwa uasi-sheria upendo wa walio wengi zaidi utapoa.” (Mathayo 24:12) Vivyo hivyo, mtume Paulo aliandika: “Watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili [au wa kifamilia], wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.” (2 Timotheo 3:2-4) Sikuzote watu wamedhihirisha tabia hizo mbaya kwa kadiri fulani, lakini zimeongezeka katika nyakati za karibuni kama watu wengi wanavyoweza kukubali.
Kwa kufikiria msukosuko unaokumba ndoa, tunawezaje kujikinga na kuwa na ndoa yenye furaha kwelikweli na yenye kudumu? Swali hilo litajibiwa katika makala inayofuata.
[Blabu katika ukurasa wa 5]
“Katika jamii ambayo imezoea kutupa vitu, huenda watu wakawa na mtazamo huohuo kuhusu mahusiano.”—SANDRA DAVIS, MTAALAMU WA SHERIA YA FAMILIA
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 4]
“Si Thabiti Kama Ndoa”
Wenzi wengi wa jinsia tofauti huishi pamoja bila kufunga ndoa. Hata hivyo, maisha hayo “si thabiti kama ndoa,” inasema ripoti moja ya Vituo vya Marekani vya Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa. Baadhi ya wenzi hao huishi pamoja ili kuona kama watafaana kabla ya kuoana. Lakini je, kuishi pamoja kabla ya kufunga ndoa huwafanya watu wafaane kabisa na kuboresha ndoa zao? Kulingana na jarida Journal of Marriage and Family, uthibitisho unaonyesha kwamba sivyo ilivyo. “Kati ya watu waliooana, wale walioishi pamoja kabla ya ndoa walikosa uradhi katika ndoa . . . , walikuwa na matatizo mengi zaidi ya ndoa, na . . . uwezekano mkubwa wa kuvunjika kwa ndoa,” lasema jarida hilo.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]
Maisha Marefu na Ndoa
Leo watu huishi muda mrefu zaidi. Ingawa jambo hilo linapendeza, limeongeza mkazo katika ndoa. Zamani ndoa nyingi zilikoma mwenzi wa ndoa alipokufa, lakini leo zinavunjwa kwa talaka. Fikiria hali isiyo ya kawaida ambayo inaathiri wanawake ambao wameolewa kwa muda mrefu nchini Japani. Kulingana na gazeti The Washington Post, wataalamu wanasema hali hiyo inaitwa “tatizo la wanaume waliostaafu.” Akikumbuka wakati mume wake alipostaafu, mwanamke mmoja ambaye ameolewa kwa miaka 40 alisema kwamba wakati huo alifikiri: “Sasa itanibidi kumtaliki. Alipokuwa akirudi nyumbani kutoka kazini nilikuwa nikimfanyia kila jambo, nami sikufurahia hilo. Lakini siwezi kuvumilia kuwa pamoja naye nyumbani wakati wote.”
-
-
Jinsi ya Kuwa na Ndoa Yenye FurahaAmkeni!—2006 | Julai
-
-
Jinsi ya Kuwa na Ndoa Yenye Furaha
“Mwanamume . . . atashikamana na mke wake nao watakuwa mwili mmoja.”—MWANZO 2:24.
MUUMBA wetu, Yehova Mungu, alianzisha ndoa ikiwa kifungo cha kudumu kati ya mwanamume na mwanamke. Andiko la Mwanzo 2:18, 22-24 linasema hivi: “Yehova Mungu akaendelea kusema: ‘Si vema huyo mwanamume aendelee kuwa peke yake. Nitamfanyia msaidizi, awe kikamilisho chake.’ Na Yehova Mungu akaufanya ubavu ambao alikuwa ameuchukua kutoka kwa mwanamume kuwa mwanamke na kumleta kwa huyo mwanamume. Ndipo huyo mwanamume akasema: ‘Mwishowe huyu ni mfupa wa mifupa yangu na nyama ya nyama yangu. Huyu ataitwa Mwanamke, kwa sababu huyu alitolewa katika mwanamume.’ Hiyo ndiyo sababu mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake nao watakuwa mwili mmoja.”
Ni kweli kwamba si rahisi kuwa na ndoa yenye furaha na yenye kudumu, lakini inawezekana. Wenzi wengi wa ndoa wameishi pamoja kwa furaha kwa miaka 50, 60, au zaidi. Ni nini kimewasaidia kufanikiwa? Wao hujitahidi kufanikisha ndoa yao sikuzote na bila ubinafsi kwa kujitahidi “kupata kibali” cha mwenzi wao. (1 Wakorintho 7:33, 34) Jambo hilo hutaka jitihada. Ikiwa uko tayari kutumia wakati na kujitahidi, wewe pia unaweza kuwa na ndoa yenye furaha, ambayo itadumu kwa muda mrefu.
Fuata Maagizo kwa Makini
Mjenzi yeyote mwenye kutegemeka hawezi kuanza kujenga kabla ya kuchunguza ramani kwanza. Vivyo hivyo, hatuwezi kufaulu kuwa na ndoa yenye furaha bila kuchunguza kwa makini maagizo ya Mungu ya kufanya hivyo. Maagizo hayo yanapatikana katika Neno la Mungu. “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida . . . kwa kunyoosha mambo,” aliandika mtume Paulo.—2 Timotheo 3:16.
Waume na wake wanaweza kujifunza mengi kuhusu ndoa kwa kufikiria jinsi Yesu alivyoshughulika na wanafunzi wake. Jinsi gani? Katika Biblia, uhusiano kati ya Yesu na wale watakaotawala pamoja naye mbinguni unalinganishwa na uhusiano kati ya mwanamume na mke wake. (2 Wakorintho 11:2) Yesu aliendelea kuwa mshikamanifu kwa wanafunzi wake, hata katika nyakati za taabu. ‘Aliwapenda mpaka mwisho.’ (Yohana 13:1) Akiwa kiongozi mwenye huruma, sikuzote Yesu alifikiria kupungukiwa na udhaifu wa wafuasi wake. Hakudai kamwe wafanye mambo yaliyozidi uwezo wao.—Yohana 16:12.
Hata rafiki zake wa karibu waliposhindwa kufanya yale aliyotarajia, Yesu aliendelea kuwa mpole. Hakuwakemea, lakini badala yake alijaribu kuwarekebisha kwa unyenyekevu na fadhili za kimungu. (Mathayo 11:28-30; Marko 14:34-38; Yohana 13:5-17) Hivyo, ukichunguza kwa makini jinsi Yesu alivyoshughulika kwa wororo na wafuasi wake na jinsi walivyomtendea, utajifunza mambo mazuri unayoweza kufanya ili kuwa na ndoa yenye furaha.—1 Petro 2:21.
Jenga Juu ya Msingi Imara
Bila shaka, majaribu yaliyo kama dhoruba yatashambulia msingi wa ndoa yako. Hilo litaathiri msingi wa uhusiano wako na mwenzi wako. Hata hivyo, msingi imara zaidi wa kuwa na ndoa yenye furaha ni kuwajibika kwa upendo. Yesu alikazia umuhimu wa kuwajibika aliposema: “Basi aliyewaunganisha Mungu, mutu asiwatenganishe.” (Mathayo 19:6, Zaire Swahili Bible) Neno “mutu” linatia ndani mume na mke wake, ambao wameweka nadhiri ya kuwa waaminifu kwa mmoja na mwenzake.
Huenda wengine wakaona kuwajibika kuwa mzigo, na kwamba kunadai wakati, mali, na jitihada nyingi. Leo, watu wengi huchagua kufanya mambo ambayo hayatawalazimu kujidhabihu kwa watu wanaowajibika kwao.
Ni nini kinachoweza kuwasaidia watu wawajibike kwa ndoa? Mtume Paulo aliandika: “Waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.” (Waefeso 5:28, 29) Basi, kwa kiasi fulani, ‘kuunganishwa’ kunamaanisha kwamba unafikiria hali ya mwenzako kana kwamba ni yako. Watu waliooana wanapaswa kubadili kufikiri kwao. Neno “changu” linapaswa kuwa “chetu” na “mimi” kuwa “sisi.”
Kukabiliana kwa mafanikio na msukosuko katika ndoa yenu kutawafanya mwe na hekima. Hekima hiyo inaweza kutokeza furaha. Methali 3:13 inasema: “Mwenye furaha ni mtu ambaye amepata hekima.”
Tumia Vifaa Visivyoteketea kwa Moto
Ili nyumba idumu na iwe salama, lazima ijengwe vizuri. Kwa hiyo, azimia kufanya ndoa yako iwe yenye kudumu. Tumia vifaa vyenye kudumu, ambavyo vinaweza kuhimili majaribu makali ya ushikamanifu wako. Thamini sana sifa nzuri kama vile hekima ya kimungu, ukarimu, utambuzi, kumwogopa Mungu, uchangamfu, kuonyesha uthamini wenye upendo kwa ajili ya sheria za Mungu, na imani ya kweli.
Furaha na uradhi katika ndoa haipatikani kupitia vitu vya kimwili au vyeo vya kilimwengu. Inapatikana tu moyoni na akilini, na sifa hizo huimarishwa na kweli kutoka katika Neno la Mungu. Himizo la kwamba “kila mmoja na aendelee kuangalia jinsi anavyojenga” linaweza kutumiwa kuhusu ndoa.—1 Wakorintho 3:10.
Matatizo Yanapotokea
Ili jengo lidumu kwa muda mrefu, lazima kuwe na ratiba nzuri ya kulidumisha. Mume na mke wanaposaidiana kwa ukawaida ili kutimiza miradi yao na wanapoheshimiana, ndoa yao itakuwa thabiti. Hawawi na ubinafsi, na hudhibiti hasira.
Mambo yanayosababisha hasira na kuudhika yasipotatuliwa yanaweza kufanya ndoa isiwe na upendo. Mtume Paulo aliwashauri hivi wanaume: “Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu nanyi msiwakasirikie kwa uchungu.” (Wakolosai 3:19) Kanuni hiyohiyo inawahusu wake. Wenzi wa ndoa wanapojitahidi kuwa wenye ufikirio, fadhili, na wenye kuelewa hali, hilo hufanya wapate furaha na uradhi. Kuepuka hasira na uchokozi husaidia kuzuia ugomvi matatizo yanapotokea. Paulo alituhimiza “iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari.”—Waefeso 4:32.
Vipi ukiudhika kwa sababu ya kuhisi kuwa hoi, umechokozeka, au huthaminiwi? Kwa utulivu, mweleze mwenzi wako waziwazi mambo yanayokuhangaisha. Hata hivyo, huenda ikafaa kufunika mambo madogo-madogo kwa upendo.—1 Petro 4:8.
Mume mmoja ambaye ndoa yake ya miaka 35 imepatwa na majaribu mbalimbali, anasema kwamba hata mwenzi wako akukasirishe kadiri gani, hupaswi kamwe “kuacha kuzungumza naye.” Anaendelea kusema hivi kwa hekima, “Msiache kupendana kamwe.”
Unaweza Kuwa na Ndoa Yenye Furaha!
Ni kweli kwamba si rahisi kuwa na ndoa yenye furaha. Hata hivyo, wenzi wa ndoa wanapojitahidi sana kumtia Mungu katika ndoa yao, watakuwa na furaha na usalama. Kwa hiyo, chunguza kwa makini hali ya kiroho ya familia yako; wajibika kabisa katika ndoa yako. Na kumbuka kwamba kama vile Yesu alivyosema, ndoa inapokuwa yenye furaha si mume wala mke anayesifiwa bali ni Mwanzilishi wa ndoa, Yehova Mungu. “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”—Mathayo 19:6.
USOMAJI WA ZIADA
Kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, kina madokezo mazuri ya kuwa na ndoa yenye furaha na mafanikio. Mamia ya maelfu ya watu waliooana ulimwenguni pote wameona kwamba shauri lake linalofaa na ambalo linategemea Biblia limewasaidia kuboresha ndoa zao.—Ona ukurasa wa 32 wa gazeti hili.
[Sanduku katika ukurasa wa 9]
Unachoweza Kufanya Ili Ndoa Yako Iwe Yenye Furaha
◼ Jifunzeni Neno la Mungu pamoja kwa ukawaida, na kusali kwa Mungu ili mpate msaada na mwongozo wa kutatua matatizo.—Methali 3:5, 6; Wafilipi 4:6, 7; 2 Timotheo 3:16, 17.
◼ Vutiwa kingono na mwenzi wako tu.—Methali 5:15-21; Waebrania 13:4.
◼ Zungumzeni waziwazi, kwa unyoofu, na kwa upendo kuhusu matatizo yenu na hali ya kutoelewana.—Methali 15:22; 20:5; 25:11.
◼ Zungumza na mwenzi wako kwa fadhili na ufikirio; epuka milipuko ya hasira, chokochoko, na maneno makali ya kuchambua.—Methali 15:1; 20:3; 21:9; 31:26, 28; Waefeso 4:31, 32.
◼ Fuata kwa unyenyekevu shauri la Biblia hata unapohisi kwamba mwenzi wako hafanyi yote anayopaswa.—Waroma 14:12; 1 Petro 3:1, 2.
◼ Jitahidi kusitawisha sifa za kiroho zinazotajwa katika Biblia.—Wagalatia 5:22, 23; Wakolosai 3:12-14; 1 Petro 3:3-6.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Fuata maagizo ya Mungu kuhusu ndoa yanayopatikana katika Biblia
[Picha katika ukurasa wa 7]
Fanya ushikamanifu na upendo usio na ubinafsi uwe msingi imara wa ndoa yako
[Picha katika ukurasa wa 8]
Sitawisha sifa za kiroho zinazoweza kuhimili majaribu makali
[Picha katika ukurasa wa 8]
Dumisha furaha katika ndoa yako
-