Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Kutafuta Pesa Kuna Madhara?
    Amkeni!—2007 | Juni
    • Je, Kutafuta Pesa Kuna Madhara?

      IKIWA ungetajirika ghafula, ungefanya nini? Je, ungetulia na kufurahia maisha? Je, ungeacha kufanya kazi na kutumia wakati mwingi zaidi pamoja na familia yako na marafiki? Au ungetafuta kazi nyingine unayofurahia zaidi? Inashangaza kwamba watu wengi wanaotajirika hawafanyi hivyo. Badala yake, wao huendelea kutafuta pesa zaidi ili kulipa madeni yao mapya au kujitajirisha zaidi.

      Hata hivyo, wengine ambao wamefanya hivyo wametambua kwamba tamaa ya mali inaathiri afya yao, maisha ya familia, na tabia za watoto wao. Hivi karibuni, vitabu, makala mbalimbali, vipindi vya televisheni, na video zimewaonya watu kuhusu kuponda raha kupita kiasi, na badala yake zimependekeza watu waishi maisha yenye usawaziko. Habari mbalimbali zimeonyesha kwamba kutafuta mali sana kunaweza kumdhuru mtu kiakili, kihisia, na hata kimwili.

  • Jinsi Unavyoweza Kuathiriwa na Azimio la Kuwa Tajiri
    Amkeni!—2007 | Juni
    • Jinsi Unavyoweza Kuathiriwa na Azimio la Kuwa Tajiri

      KATIKA ulimwengu ambamo zaidi ya watu milioni 850 hawana chakula cha kutosha, inaweza kuwa vigumu kukubali kwamba kuwa na mali nyingi kupita kiasi kunaweza kusababisha matatizo. Lakini je, uliona kwamba andiko lililonukuliwa katika makala iliyotangulia lilionya dhidi ya kupenda pesa na kuazimia kuwa tajiri bali si dhidi ya pesa wala mali? Inakuwaje watu wanapofanya kusudi lao kuu maishani liwe kutafuta mali na vitu ambavyo vinaweza kununuliwa? Hebu kwanza fikiria jinsi watoto wao wanavyoathiriwa.

      Jinsi Watoto Wanavyoathiriwa

      Inakadiriwa kwamba katika mwaka mmoja tu, mtoto mmoja nchini Marekani hutazama matangazo ya biashara 40,000 kwenye televisheni. Zaidi ya hilo, kuna michezo ya video, mashine za hali ya juu za kuchezea muziki, programu za kompyuta, na nguo za kisasa ambazo watoto huona madukani na katika nyumba za marafiki wao. Kwa kweli, wazazi hupata maombi mengi sana kutoka kwa watoto wao. Wazazi fulani wameamua kuwapa watoto wao chochote wanachoomba. Kwa nini?

      Kwa kuwa wazazi fulani walinyimwa anasa za maisha walipokuwa watoto, wao hawataki kamwe kuwafanya watoto wao wahisi kuwa wananyimwa chochote. Wazazi wengine wanafikiri kwamba wasipowapa watoto wao vitu wanavyotaka, basi wataacha kuwapenda. Mwanzilishi-mshirika wa chama kimoja cha wazazi huko Boulder, Colorado, Marekani, alisema: “Wanataka kuwa marafiki wa karibu sana wa watoto wao na kuhakikisha kwamba wanafurahi.” Wazazi wengine wanafikiri kwamba kuwapa watoto zawadi nyingi kutalipia ule wakati mwingi ambao wanatumia kazini wakiwa mbali nao. Pia, baada ya kuchoshwa na kazi juma zima, wazazi hawangependa kuanzisha ugomvi kwa kuwaambia watoto wao, “Hapana, sitakununulia kitu hicho.”

      Lakini je, wazazi wanaowapa watoto wao kila kitu wanachotaka wanawasaidia au wanawadhuru? Kwa kushangaza, imeonekana kwamba badala ya kuwapenda wazazi wao zaidi, watoto wanaopewa chochote wanachotaka hawana shukrani. Hata hawathamini zawadi ambazo wanazililia. Msimamizi wa shule fulani ya msingi alisema: “Nimeona kwamba wakati watoto wanapopewa haraka vitu wanavyoomba, mara nyingi wao huacha kuvitumia baada ya majuma mawili tu.”

      Watoto wanaopewa chochote wanachotaka huwaje wanapokua watu wazima? Kulingana na gazeti la Newsweek, uchunguzi unaonyesha kwamba wanapokuwa watu wazima “wanashindwa kushughulikia matatizo maishani.” Kwa kuwa hawakujifunza kufanyia kazi vitu wanavyotaka, wengi wao hawafanikiwi shuleni, kazini, na katika ndoa, na mwishowe inawabidi wawategemee wazazi wao kifedha. Pia, wanaweza kushuka moyo na kuwa na mahangaiko mara nyingi.

      Kwa hiyo, watoto wanaopewa chochote wanachotaka huwa wananyimwa mambo fulani ya maana. Hawafundishwi faida za kufanya kazi, kujiheshimu, na kuwa na tabia nzuri. Daktari mmoja anayeitwa Jessie O’Neill anaonya hivi: “Ukiwafundisha watoto kwamba wanaweza kupata chochote wanachotaka wakati wowote ule, unawawekea msingi mbaya maishani.”

      Watu Wazima Wanaathiriwaje?

      Jarida la Psychology Today linasema kwamba ikiwa umefunga ndoa “hata iwe ni kwa muda gani au mna pesa nyingi kadiri gani, labda mtagombana hasa kuhusu pesa.” Pia gazeti hilo linasema kwamba “jinsi ambavyo wenzi wa ndoa wanashughulikia hali za kutoelewana au matatizo yanayosababishwa na pesa kunaweza kuonyesha ikiwa uhusiano wao utadumu au kuvunjika.” Wenzi wa ndoa wanaoona pesa na mali kuwa za maana sana wanahatarisha ndoa yao. Hata imekadiriwa kwamba asilimia 90 ya visa vya talaka husababishwa hasa na ugomvi kuhusu pesa.

      Lakini, hata wenzi wa ndoa wanapokaa pamoja, ndoa yao inaweza kuathiriwa ikiwa kusudi lao kuu maishani ni kutafuta pesa na anasa. Kwa mfano, wenzi wa ndoa walio na deni wanaweza kukasirika ovyoovyo, huku kila mmoja akimlaumu yule mwingine kwa matatizo yao ya pesa. Katika visa vingine, kila mwenzi anaweza kujishughulisha sana na mali zake mwenyewe hivi kwamba anakosa wakati wa kufanya mambo pamoja na mwenzi wake. Inakuwaje mwenzi mmoja anaponunua kitu cha bei ghali na kumficha mwenzake? Mwenzi anapofanya hivyo anakuwa msiri, anasababisha hali ya kutoaminiana, na kuhisi hatia. Yote hayo huvunja ndoa hatua kwa hatua.

      Watu wazima fulani, iwe wamefunga ndoa au la, wamejitoa mhanga kutafuta mali. Wengine huko Afrika Kusini wamejaribu kujiua kwa sababu wamefadhaika kwa kujitahidi kuwaiga watu wa Ulaya walio na mali nyingi. Nchini Marekani, mtu mmoja alimuua mke wake, mwana wake mwenye umri wa miaka 12, halafu akajiua, labda kwa sababu ya matatizo ya pesa.

      Ni kweli kwamba watu wengi hawafi kwa sababu ya kutafuta mali. Hata hivyo, wanaweza kukosa uradhi maishani. Pia, maisha yao yanaweza kuathiriwa wakati mkazo unaosababishwa na kazi au matatizo ya pesa unapowafanya wawe na tatizo la kushtuka-shtuka, wakose usingizi, waumwe na kichwa, au kuwa na vidonda vya tumbo—hali ambazo zinaweza kusababisha kifo cha mapema. Hata mtu akigundua kwamba anahitaji kubadili maoni yake kuhusu mambo ambayo anapaswa kutanguliza maishani, huenda ikawa tayari amepatwa na madhara ya kudumu. Labda mwenzi wake hamwamini tena, huenda tayari watoto wake wameathiriwa kihisia, na huenda ikawa afya yake imedhoofika kabisa. Huenda madhara fulani yanaweza kurekebishwa, lakini jitihada nyingi zinahitajika. Watu kama hao tayari “wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.”—1 Timotheo 6:10.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki