-
Familia, Sifuni Mungu Mkiwa Sehemu ya Kutaniko LakeMnara wa Mlinzi—1999 | Julai 1
-
-
2. (a) Kwa nini kujitayarisha ni muhimu katika kusaidia wachanga wafurahie mikutano? (b) Ni kielelezo cha nani ambacho ni muhimu?
2 Ni kweli kwamba huenda ikawa vigumu kuwasaidia wachanga wazoee kawaida yenye kujenga ya utendaji wa kutaniko. Huenda tatizo likawa nini ikiwa watoto fulani wanaohudhuria mikutano pamoja na wazazi wao hawaonekani kufurahia mikutano? Bila shaka, watoto wengi hukaza fikira zao kwa kipindi kifupi nao huchoshwa haraka. Kujitayarisha kwaweza kusaidia kutatua tatizo hilo. Bila kujitayarisha, watoto hawawezi kushiriki kwenye mikutano kwa njia yenye maana. (Mithali 15:23) Bila kujitayarisha, itakuwa vigumu kwao kufanya maendeleo ya kiroho yanayoridhisha. (1 Timotheo 4:12, 15) Ni nini kiwezacho kufanywa? Kwanza, wazazi wahitaji kujiuliza kama wao wenyewe hujitayarisha kwa ajili ya mikutano. Kielelezo chao ni uvutano wenye nguvu. (Luka 6:40) Kupanga kwa uangalifu kwa ajili ya funzo la familia kwaweza pia kuwa jambo muhimu.
-
-
Familia, Sifuni Mungu Mkiwa Sehemu ya Kutaniko LakeMnara wa Mlinzi—1999 | Julai 1
-
-
Kujitayarisha kwa Ajili ya Mikutano ya Kutaniko
8. (a) Ni nini kiwezacho kutusaidia tutie ndani ya funzo letu la familia mambo yote yanayohitaji uangalifu? (b) Funzo hili ni muhimu jinsi gani?
8 Kuna mambo mengi yanayohitaji uangalifu wakati wa funzo la familia. Unaweza kuyashughulikiaje yote? Haiwezekani kufanya mambo yote wakati uleule. Lakini huenda ukaona kwamba kuandika orodha kunasaidia. (Mithali 21:5) Mara kwa mara, pitia orodha hiyo na uchunguze kile kinachohitaji uangalifu wa pekee. Pendezwa kipekee na maendeleo ya kila mshiriki wa familia. Mpango huo wa funzo la familia ni sehemu muhimu ya elimu ya Kikristo, inayotuandaa kwa maisha ya sasa na kututayarisha kwa uhai udumuo milele utakaokuja.—1 Timotheo 4:8.
9. Ni miradi gani kuhusiana na kujitayarisha kwa ajili ya mikutano ambayo huenda tukashughulikia hatua kwa hatua wakati wa mafunzo yetu ya familia?
9 Je, funzo la familia yako latia ndani kujitayarisha kwa ajili ya mikutano ya kutaniko? Kuna mambo kadhaa mnayoweza kushughulikia hatua kwa hatua mnapojifunza pamoja. Baadhi ya mambo hayo yaweza kuchukua muda wa majuma kadhaa, miezi kadhaa, au hata miaka kadhaa ili kuyatimiza. Fikiria miradi hii: (1) kila mmoja katika familia kuwa tayari kutoa maelezo kwenye mikutano ya kutaniko; (2) kila mmoja kujitahidi kutoa maelezo katika maneno yake mwenyewe; (3) kutia ndani maandiko katika maelezo; na (4) kuchanganua habari kwa lengo la kuitumia kibinafsi. Mambo hayo yote yanaweza kusaidia mtu aitumie kweli katika maisha yake mwenyewe.—Zaburi 25:4, 5.
10. (a) Twaweza kutoaje uangalifu kwa kila mkutano wa kutaniko? (b) Kwa nini hilo lafaa?
10 Hata ikiwa funzo lenu la familia kwa kawaida hutegemea somo la Mnara wa Mlinzi la kila juma, usipuuze umuhimu wa kujitayarisha kibinafsi au mkiwa familia kwa ajili ya Funzo la Kitabu la Kutaniko, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na Mkutano wa Utumishi. Hizo pia ni sehemu muhimu za programu ya kutufundisha kutembea katika njia ya Yehova. Huenda mara kwa mara mkaweza kujitayarisha kwa ajili ya mikutano yote mkiwa kikundi cha familia. Kwa kujifunza pamoja, ustadi wenu wa kujifunza utaboreka. Tokeo likiwa kwamba manufaa nyingi zaidi zitapatikana kutokana na mikutano yenyewe. Kati ya mambo mengine, zungumzieni manufaa za kujitayarisha kwa ukawaida kwa ajili ya mikutano hiyo na umuhimu wa kuwa na wakati hususa uliotengwa kwa ajili ya kufanya hivyo.—Waefeso 5:15-17.
11, 12. Kutayarisha kwa ajili ya kuimba katika mikutano kwaweza kutunufaishaje, na jambo hilo laweza kufanywaje?
11 Kwenye Mikusanyiko ya “Njia ya Mungu ya Maisha,” tulitiwa moyo tujitayarishe kwa ajili ya sehemu nyingine ya mikutano—kuimba. Je, umefanya hivyo? Kufanya hivyo kwaweza kukazia kweli za Biblia katika akili na mioyo yetu na wakati huohuo kufanya tufurahie zaidi mikutano ya kutaniko.
12 Kujitayarisha ambako hutia ndani kusoma na kuzungumzia maana ya maneno katika nyimbo zilizoratibiwa kwaweza kutusaidia kuimba kutoka moyoni. Katika Israeli la kale, ala za muziki zilitumiwa sana katika ibada. (1 Mambo ya Nyakati 25:1; Zaburi 28:7) Je, kuna mmoja katika familia yenu ambaye hupiga ala fulani ya muziki? Kwa nini msitumie ala hiyo kujizoeza wimbo mmoja kati ya nyimbo zitakazoimbwa juma hilo, kisha mwimbe mkiwa familia. Mnaweza pia kutumia kaseti za nyimbo hizo. Katika nchi fulani ndugu zetu huimba vizuri bila ala za muziki. Wanapotembea barabarani au wanapohubiri shambani, mara nyingi hufurahia kuimba nyimbo ambazo zimeratibiwa kuimbwa kwenye mikutano ya kutaniko juma hilo.—Waefeso 5:19.
-