-
“Zawadi Zikiwa Wanadamu” Ili Kutunza Kondoo za YehovaMnara wa Mlinzi—1999 | Juni 1
-
-
“Zawadi Zikiwa Wanadamu” Ili Kutunza Kondoo za Yehova
“Alipopaa juu alichukua mateka; alitoa zawadi zikiwa wanadamu.”—WAEFESO 4:8.
1. Dada mmoja Mkristo alisema nini kuhusu wazee katika kutaniko lao?
“ASANTENI kwa kutujali sana. Tabasamu zenu, wema wenu, na hangaiko lenu ni nyofu kabisa. Sikuzote mko tayari kutusikiliza na kutuambia maneno ya Biblia yanayotutia moyo. Naomba kwamba nisiwapuuze kamwe.” Hivyo ndivyo dada mmoja Mkristo alivyowaandikia wazee katika kutaniko lake. Kwa wazi, upendo ulioonyeshwa na wachungaji Wakristo wenye kujali uligusa moyo wake.—1 Petro 5:2, 3.
2, 3. (a) Kulingana na Isaya 32:1, 2, wazee wenye huruma hutunzaje kondoo za Yehova? (b) Mzee anaweza kuonwa kuwa zawadi anapofanya nini?
2 Wazee ni uandalizi wa Yehova wa kuchunga kondoo zake. (Luka 12:32; Yohana 10:16) Yehova anawapenda sana kondoo zake hivi kwamba aliwanunua kwa damu ya Yesu yenye thamani kubwa. Basi, haishangazi kwamba Yehova hufurahi wazee walitunzapo kundi lake kwa wororo. (Matendo 20:28, 29) Ona ufafanuzi wa kiunabii kuhusu hawa wazee, au “viongozi”: “Kila mmoja atakuwa kama mahali pa kujikinga na upepo, kama mahali pa kujificha wakati wa tufani. Watakuwa kama vijito vya maji katika nchi kame, kama kivuli cha mwamba mkubwa jangwani.” (Isaya 32:1, 2, Biblia Habari Njema) Naam, wanapaswa kuwalinda, kuwaburudisha, na kuwafariji kondoo zake. Kwa hiyo, wazee wanaolichunga kundi kwa huruma wanajitahidi kutimiza yale ambayo Mungu huwatazamia wafanye.
3 Wazee kama hao hurejezewa katika Biblia kuwa “zawadi zikiwa wanadamu.” (Waefeso 4:8) Unapofikiria zawadi, unafikiria kitu ambacho mtu hupewa ili kutimiza uhitaji fulani au kumfurahisha mwenye kukipokea. Mzee anaweza kuonwa kuwa zawadi anapotumia uwezo wake mbalimbali ili kutoa msaada unaohitajiwa na kuchangia furaha ya kundi. Yeye anaweza kufanyaje hivyo? Jibu, ambalo limo katika maneno ya Paulo kwenye Waefeso 4:7-16, hutukuza hangaiko lenye upendo la Yehova kwa kondoo zake.
“Zawadi Zikiwa Wanadamu”—Kutoka Wapi?
4. Yehova ‘alipaaje juu’ kwa kutimiza Zaburi 68:18, na “zawadi zikiwa wanadamu” walikuwa nani?
4 Paulo alipotumia usemi “zawadi zikiwa wanadamu,” alikuwa akimnukuu Mfalme Daudi, aliyesema hivi kumhusu Yehova: “Umepaa juu; umechukua mateka; umechukua zawadi zikiwa wanadamu.” (Zaburi 68:18, NW) Baada ya Waisraeli kukaa katika Bara Lililoahidiwa kwa miaka fulani, Yehova ‘alipaa’ Mlima Zayoni kitamathali na kulifanya Yerusalemu kuwa makao makuu ya ufalme wa Israeli, Daudi akiwa mfalme wake. Lakini “zawadi zikiwa wanadamu” walikuwa nani? Walikuwa watu waliochukuliwa mateka wakati wa kutiishwa kwa bara. Baadaye, Walawi walipewa baadhi ya mateka hao ili wasaidie kufanya kazi katika tabenakulo.—Ezra 8:20.
5. (a) Paulo anaonyeshaje kwamba Zaburi 68:18 ina utimizo fulani katika kutaniko la Kikristo? (b) Yesu ‘alipaa juu’ kwa njia gani?
5 Katika barua yake kwa Waefeso, Paulo anaonyesha kuwa maneno ya mtunga-zaburi yana utimizo mkubwa zaidi katika kutaniko la Kikristo. Akijumlisha maneno ya Zaburi 68:18, Paulo aandika hivi: “Basi kila mmoja wetu alipewa fadhili isiyostahiliwa kulingana na jinsi Kristo alivyopima hiyo zawadi ya bure. Kwa sababu hii yeye asema: ‘Alipopaa juu alichukua mateka; alitoa zawadi zikiwa wanadamu.’” (Waefeso 4:7, 8) Hapo Paulo anaitumia zaburi hiyo imhusu Yesu akiwa mwakilishi wa Mungu. Yesu ‘aliushinda ulimwengu’ kwa mwendo wake mwaminifu. (Yohana 16:33) Yeye pia alikishinda kifo na kumshinda Shetani kwa kuwa Mungu alimfufua kutoka kwa wafu. (Matendo 2:24; Waebrania 2:14) Mwaka wa 33 W.K., Yesu aliyefufuliwa alipaa “juu zaidi sana kuliko mbingu zote”—juu zaidi kuliko viumbe wengine wote wa kimbingu. (Waefeso 4:9, 10; Wafilipi 2:9-11) Akiwa mshindi, Yesu alichukua “mateka” kutoka kwa adui. Jinsi gani?
6. Kuanzia Pentekoste 33 W.K., Yesu aliyepaa alianza kuiporaje nyumba ya Shetani, naye aliwafanyia nini “mateka” hao?
6 Yesu alipokuwa duniani, alionyesha kuwa ana nguvu kuliko Shetani kwa kuwakomboa wale waliokuwa mateka wa roho waovu. Ilikuwa kana kwamba Yesu aliivamia nyumba ya Shetani, akamfunga, na kutwaa mali zake. (Mathayo 12:22-29) Ebu wazia, baada ya kufufuliwa na kukabidhiwa ‘mamlaka yote mbinguni na duniani,’ sasa Yesu angeweza kumpora kama nini! (Mathayo 28:18) Kuanzia siku ya Pentekoste 33 W.K., Yesu aliyepaa, akiwa mwakilishi wa Mungu, alianza kupora nyumba ya Shetani kwa ‘kuwachukua mateka’—wanadamu ambao kwa muda mrefu walikuwa katika utumwa wa dhambi na kifo na chini ya utawala wa Shetani. Kwa hiari “mateka” hao wakawa “watumwa wa Kristo, [wa]kifanya mapenzi ya Mungu kwa nafsi yote.” (Waefeso 6:6) Kwa kweli, Yesu aliwanyakua kutoka mkononi mwa Shetani, na kwa niaba ya Yehova, akawakabidhi kwa kutaniko kama “zawadi zikiwa wanadamu.” Ebu wazia hasira kali ya Shetani wakati walipokuwa wakinyakuliwa kutoka mkononi mwake, huku asiweze kufanya lolote!
7. (a) “Zawadi zikiwa wanadamu” wanatumikia wakiwa na nyadhifa gani makutanikoni? (b) Yehova amempa fursa gani kila mwanamume anayetumikia akiwa mzee?
7 Je, tuna “zawadi zikiwa wanadamu” kutanikoni leo? Ndiyo! Wao wanatumikia wakiwa wazee, wakifanya kazi kwa bidii wakiwa ‘waeneza-evanjeli, wachungaji, na walimu’ katika makutaniko yanayozidi 87,000 ya watu wa Mungu ulimwenguni pote. (Waefeso 4:11) Shetani angelifurahi sana ikiwa wao wangelitenda kundi vibaya. Lakini Mungu kupitia Yesu hakuwakabidhi kwa kutaniko ili walitende vibaya. Badala yake, Yehova ameandaa hawa wanaume kwa ajili ya hali njema ya kutaniko, nao wanawajibika kwake kuhusiana na kondoo waliokabidhiwa. (Waebrania 13:17) Ikiwa wewe unatumikia ukiwa mzee, Yehova amekupa fursa nzuri ajabu ya kujithibitisha mwenyewe kuwa zawadi, au baraka, kwa ndugu zako. Unaweza kufanya hivyo kwa kutimiza madaraka manne muhimu.
Uhitaji wa ‘Kurekebisha Upya’ Unapozuka
8. Nyakati nyingine sisi sote huhitaji kurekebishwa upya katika njia zipi?
8 Kwanza, “zawadi zikiwa wanadamu” huandaliwa “kwa kusudi la kuwarekebisha upya watakatifu,” Paulo asema. (Waefeso 4:12) Nomino ya Kigiriki inayotafsiriwa ‘kurekebisha upya’ hurejezea “kunyosha” kitu. Tukiwa wanadamu wasiokamilika, sote tunahitaji kurekebishwa upya mara kwa mara—ili kufikiri kwetu, mitazamo yetu, au mwenendo wetu “zinyoshwe” kwa kupatana na kufikiri kwa Mungu na mapenzi yake. Yehova ametuandalia kwa upendo “zawadi zikiwa wanadamu” ili watusaidie kufanya marekebisho yanayohitajika. Wao hufanyaje hivyo?
9. Mzee anaweza kusaidiaje kumrekebisha upya kondoo aliyekosea?
9 Nyakati fulani, huenda mzee akahitaji kumsaidia kondoo aliyekosea, ambaye labda ‘amechukua hatua fulani isiyo ya kweli kabla ya kuijua.’ Mzee anaweza kusaidiaje? Andiko la Wagalatia 6:1 lasema kwamba “jaribuni kumrekebisha upya mtu wa namna hiyo katika roho ya upole.” Kwa hiyo mzee atoapo shauri, hamkemei mkosaji kwa maneno makali. Shauri lapasa kumtia moyo, wala si ‘kumwogofya,’ yule anayelipokea. (2 Wakorintho 10:9; linganisha Ayubu 33:7.) Huenda mtu huyo tayari ameaibika, kwa hiyo mchungaji mwenye upendo huepuka kuiponda roho yake. Wakati shauri, hata karipio zito, linapotolewa kwa upendo, yaelekea litanyosha kufikiri au mwenendo wa mkosaji, na kwa njia hiyo limrekebishe.—2 Timotheo 4:2.
10. Kuwarekebisha upya wengine kunatia ndani nini?
10 Yehova alipoandaa “zawadi zikiwa wanadamu” ili kuturekebisha upya, alitazamia wazee wawe wenye kuburudisha kiroho na wenye kustahili kuigwa na watu wake. (1 Wakorintho 16:17, 18; Wafilipi 3:17) Kurekebisha upya wengine kunatia ndani kuwasaidia waaminifu wadumu kufuata mwendo unaofaa, na kuwasahihisha wale wanaofuatilia mwendo wenye makosa.a Leo, kwa kuwa kuna matatizo mengi sana yanayoelekea kuvunja moyo, wengi wanahitaji kitia-moyo ili waendelee. Huenda wengine wakahitaji msaada unaotolewa kwa wororo ili kufikiri kwao kunyoshwe kupatana na kufikiri kwa Mungu. Kwa mfano, baadhi ya Wakristo waaminifu hupambana na hisia za ndani zinazowafanya wahisi kwamba hawastahili wala hawafai. “Nafsi zilizoshuka moyo” kama hao huenda wakaona kuwa Yehova hawezi kamwe kuwapenda na kwamba Mungu hawezi hata kuzikubali jitihada zao bora za kumtumikia. (1 Wathesalonike 5:14) Lakini kufikiri hivyo hakupatani na jinsi Mungu awaonavyo waabudu wake kikweli.
11. Wazee wanaweza kufanya nini ili kuwasaidia wale wanaopambana na hisia za kuona kuwa hawafai?
11 Enyi wazee, mnaweza kufanya nini ili kuwasaidia watu kama hao? Waonyesheni kwa fadhili uthibitisho wa Kimaandiko unaoonyesha kuwa Yehova humjali kila mmoja wa watumishi wake, nanyi wahakikishieni kuwa maandiko hayo ya Biblia huwahusu wao kibinafsi. (Luka 12:6, 7, 24) Wasaidieni waelewe kuwa Yehova ‘amewavuta’ ili wamtumikie, na basi ni lazima awe anawathamini. (Yohana 6:44) Wahakikishieni kuwa si wao pekee—watumishi wengi waaminifu wa Yehova wamekuwa na hisia kama hizo. Wakati mmoja nabii Eliya alishuka moyo sana hivi kwamba akatamani kufa. (1 Wafalme 19:1-4) Baadhi ya Wakristo watiwa-mafuta katika karne ya kwanza walihisi kuwa mioyo yao ‘inawalaumu.’ (1 Yohana 3:20) Tunafarijika kujua kwamba watu waaminifu katika nyakati za Biblia walikuwa na “hisia kama zetu.” (Yakobo 5:17) Mnaweza pia kupitia makala zenye kutia moyo zilizo katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! mkiwa pamoja na watu waliovunjika moyo. Mungu ambaye amewakabidhi nyinyi mkiwa “zawadi zikiwa wanadamu” hatakosa kuona jitihada zenu zenye upendo za kumfanya awe na matumaini tena.—Waebrania 6:10.
‘Kulijenga’ Kundi
12. Ni nini kionyeshwacho na usemi “kuujenga mwili wa Kristo,” na ufunguo wa kulijenga kundi ni nini?
12 Pili, “zawadi zikiwa wanadamu” wamekabidhiwa kwa kusudi la “kuujenga mwili wa Kristo.” (Waefeso 4:12) Hapo Paulo anatumia usemi wa mfano. ‘Kujenga’ hutukumbusha ujenzi, na “mwili wa Kristo” hurejezea watu—washiriki wa kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta. (1 Wakorintho 12:27; Waefeso 5:23, 29, 30) Wazee wanahitaji kuwasaidia ndugu zao waimarike kiroho. Kusudi lao ni ‘kulijenga na si kulibomoa’ kundi. (2 Wakorintho 10:8) Ufunguo wa kulijenga kundi ni upendo, kwa sababu “upendo hujenga.”—1 Wakorintho 8:1.
13. Inamaanisha nini kuwa mwenye hisia-mwenzi, na kwa nini ni muhimu wazee waonyeshe hisia-mwenzi?
13 Sehemu moja ya upendo inayowasaidia wazee kulijenga kundi ni hisia-mwenzi. Kuwa na hisia-mwenzi kwamaanisha kuwahurumia wengine—kujiweka katika hali ya fikira zao na hisia zao, mkikumbuka mapungukio yao. (1 Petro 3:8) Kwa nini ni muhimu kwa wazee kuwa na hisia-mwenzi? Sababu muhimu zaidi ni kwamba Yehova—yeye ambaye huandaa “zawadi zikiwa wanadamu”—ni Mungu mwenye hisia-mwenzi. Watumishi wake wanapoteseka au wakiwa katika maumivu, yeye huwahurumia. (Kutoka 3:7; Isaya 63:9) Yeye hufikiria udhaifu wao. (Zaburi 103:14) Basi, wazee wanaweza kuonyeshaje hisia-mwenzi?
14. Wazee wanaweza kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi kwa njia zipi?
14 Mtu ambaye amevunjika moyo anapowajia, wao husikiliza, wakitambua hisia zake. Wao hujaribu kuelewa malezi, utu, na hali mbalimbali za ndugu zao. Kisha wazee wanapotoa msaada wa Kimaandiko wenye kujenga, itakuwa rahisi kwa kondoo kuukubali kwa sababu unatoka kwa wachungaji wanaowaelewa na kuwajali kikweli. (Mithali 16:23) Hisia-mwenzi pia husababisha wazee kufikiria mapungukio ya wengine na hisia ambazo zinaweza kutokezwa na mapungukio hayo. Kwa mfano, huenda Wakristo fulani waaminifu wakahisi wana hatia kwa sababu hawawezi kufanya zaidi katika kumtumikia Mungu, labda kwa sababu ya uzee au ugonjwa. Kwa upande mwingine, huenda wengine wakahitaji kitia-moyo ili kuiboresha huduma yao. (Waebrania 5:12; 6:1) Hisia-mwenzi itawafanya wazee watafute “maneno yapendezayo” yanayowajenga wengine. (Mhubiri 12:10) Kondoo za Yehova wanapojengwa na kuchochewa, upendo wao kwa Mungu utawasukuma kufanya yote wawezayo katika kumtumikia!
Wanaume Wanaoendeleza Umoja
15. Usemi “umoja katika imani” humaanisha nini?
15 Tatu, “zawadi zikiwa wanadamu” wameandaliwa ili “sisi sote tuufikie umoja katika imani na katika ujuzi sahihi wa Mwana wa Mungu.” (Waefeso 4:13) Usemi “umoja katika imani” haumaanishi umoja wa itikadi pekee bali pia umoja wa waamini. Hiyo basi ni sababu nyingine ambayo imefanya Mungu atupe “zawadi zikiwa wanadamu”—ili kuendeleza umoja miongoni mwa watu wake. Wao hufanyaje hivyo?
16. Kwa nini ni muhimu kwa wazee kudumisha umoja miongoni mwao?
16 Kwanza kabisa, ni lazima wadumishe umoja miongoni mwao wenyewe. Ikiwa wachungaji wamegawanyika, huenda kondoo wakapuuzwa. Wakati wenye thamani ambao ungetumiwa katika kulichunga kundi huenda ukatumiwa isivyofaa katika mikutano mirefu na mijadala juu ya masuala yasiyo ya lazima. (1 Timotheo 2:8) Huenda wazee wasikubaliane tu juu ya kila suala wanalozungumzia, kwa sababu wao ni watu walio na nyutu ambazo huenda zikawa tofauti-tofauti sana. Umoja haumaanishi kwamba wasiwe na maoni yanayotofautiana au hata kwamba wasiyatoe kwa njia yenye usawaziko wakati wanapozungumzia mambo kwa wazi. Wazee hudumisha umoja wao kwa kusikiliza kila mmoja kwa heshima pasipo kuhukumu mapema. Na maadamu hakuna kanuni ya Biblia inayokiukwa, kila mmoja anapaswa kuwa tayari kukubali na kuunga mkono uamuzi wa mwisho wa baraza la wazee. Roho ya kunyenyekea huonyesha kuwa wao wanaongozwa na “hekima ya kutoka juu,” ambayo ni “yenye kufanya amani, yenye kukubali sababu.”—Yakobo 3:17, 18.
17. Wazee wanaweza kusaidiaje kudumisha umoja kutanikoni?
17 Wazee pia wako macho kudumisha umoja kutanikoni. Uvutano wenye kusababisha migawanyiko—kama vile porojo yenye kudhuru, mwelekeo wa kushuku wengine, au roho yenye ugomvi—unapotisha kuvuruga amani, wao hutoa shauri lenye kusaidia mara moja. (Wafilipi 2:2, 3) Kwa mfano, huenda wazee wanawafahamu watu fulani walio wachambuzi kupita kiasi au walio na mwelekeo wa kuingilia mambo ya wengine, na hivyo kuwa wadukizi. (1 Timotheo 5:13; 1 Petro 4:15) Wazee watajaribu kuwasaidia watu kama hao watambue kuwa mwendo wa aina hiyo ni kinyume cha mambo ambayo tumefundishwa na Mungu na kwamba kila mmoja ni lazima “[achukue] mzigo wake mwenyewe.” (Wagalatia 6:5, 7; 1 Wathesalonike 4:9-12) Kwa kutumia Maandiko, wataeleza kuwa Yehova humwachia kila mmoja wetu aamue mambo mengi akitumia dhamiri yake mwenyewe, na basi yeyote miongoni mwetu asiwahukumu wengine kwa masuala kama hayo. (Mathayo 7:1, 2; Yakobo 4:10-12) Ili tutumikie pamoja kwa umoja, ni lazima kuwe na hali ya kutumainiana na staha kutanikoni. “Zawadi zikiwa wanadamu” hutusaidia kuhifadhi amani na umoja wetu kwa kutoa shauri la Kimaandiko inapohitajika.—Waroma 14:19.
Kulilinda Kundi
18, 19. (a) “Zawadi zikiwa wanadamu” hutulinda kutokana na watu gani? (b) Kondoo wanahitaji kulindwa kutokana na hatari gani nyingine, na wazee hutendaje ili kuwalinda kondoo?
18 Nne, Yehova huandaa “zawadi zikiwa wanadamu” ili kutulinda tusiathiriwe na “kila upepo wa fundisho kwa njia ya mbinu ya hadaa ya watu, kwa njia ya ujanja katika kutunga kosa.” (Waefeso 4:14) Neno la awali lililotafsiriwa “hadaa” linasemekana kuwa lamaanisha “kudanganya kwenye mchezo wa dadu [mchezo wa kamari]” au “mbinu ya kutumia dadu kwa udanganyifu.” Je, hilo halitukumbushi namna waasi-imani wajanja wanavyotenda? Wakitumia hoja zenye ujanja, wao hutumia Maandiko vibaya wakijaribu kuwahadaa Wakristo wa kweli waiache imani yao. Lazima wazee wawe macho kutambua hao “mbwa-mwitu wenye kuonea”!—Matendo 20:29, 30.
19 Kondoo za Yehova wanahitaji kulindwa kutokana na hatari nyingine vilevile. Daudi, mchungaji wa kale, alilinda kwa ujasiri kondoo za baba yake kutokana na wanyama-wawindaji. (1 Samweli 17:34-36) Leo vilevile, huenda kukawa nyakati ambapo wachungaji Wakristo wenye kujali wanapaswa kuonyesha ujasiri ili waweze kulilinda kundi kutokana na yeyote ambaye huenda akawatenda vibaya au kuwaonea kondoo za Yehova, hasa wale walio dhaifu. Wazee watafanya haraka kuwaondoa kutanikoni watenda-dhambi wenye kukusudia ambao hutumia ujanja, udanganyifu, na hila kimakusudi ili kuendeleza uovu.b—1 Wakorintho 5:9-13; linganisha Zaburi 101:7.
20. Kwa nini tunaweza kuhisi usalama tukiwa katika utunzaji wa “zawadi zikiwa wanadamu”?
20 Twashukuru kama nini kwa sababu ya “zawadi zikiwa wanadamu”! Tunaweza kuhisi usalama tukiwa katika utunzaji wao wenye upendo, kwa kuwa wao huturekebisha upya kwa wororo, hutujenga kwa upendo, wanahifadhi umoja wetu kwa utayari, nao hutulinda kwa ujasiri. Lakini “zawadi zikiwa wanadamu” wanapaswa kulionaje daraka lao kutanikoni? Nasi tunaweza kuonyeshaje kwamba tunawathamini? Maswali hayo yatazungumziwa katika makala inayofuata.
-
-
Kuthamini “Zawadi Zikiwa Wanadamu”Mnara wa Mlinzi—1999 | Juni 1
-
-
Kuthamini “Zawadi Zikiwa Wanadamu”
“Mwe na staha kwa wale wanaofanya kazi kwa bidii miongoni mwenu na . . . mwape ufikirio ambao ni zaidi kuliko ule wa kawaida katika upendo kwa sababu ya kazi yao.”—1 WATHESALONIKE 5:12, 13.
1. Kulingana na Matendo 20:35, kutoa kuna uwezo gani? Toa kielezi.
“KUNA furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Je, unaweza kukumbuka wakati ulipoona ukweli wa maneno hayo ya Yesu? Labda ilikuwa zawadi uliyompa mtu umpendaye sana. Uliichagua kwa makini, kwa sababu ulitaka iwe kitu ambacho mpendwa wako angekithamini sana. Uso wenye furaha wa mpendwa wako ulikuchangamsha moyo kama nini! Kutoa, kunapofanywa kwa nia nzuri, ni wonyesho wa upendo, na kuonyesha upendo kunaweza kutuletea furaha.
2, 3. (a) Kwa nini yaweza kusemwa kuwa hakuna mtu aliye na furaha kuliko Yehova, na uandalizi wa “zawadi zikiwa wanadamu” unaweza kufanyaje moyo wake ufurahi? (b) Hatungependa kuitendeaje zawadi kutoka kwa Mungu?
2 Ni nani, basi, awezaye kuwa na furaha kuliko Yehova, aliye Mpaji wa “kila zawadi njema”? (Yakobo 1:17; 1 Timotheo 1:11) Yeye hutoa kila zawadi kwa upendo. (1 Yohana 4:8) Jambo hilo ni kweli pia kuhusiana na zawadi ambayo Mungu kupitia Kristo amelikabidhi kutaniko—wale “zawadi zikiwa wanadamu.” (Waefeso 4:8) Uandalizi wa Yehova wa wazee wa kulichunga kundi ni wonyesho wa upendo mkubwa wa Mungu kwa watu wake. Wanaume hawa huchaguliwa kwa makini—ni lazima watimize sifa za Kimaandiko. (1 Timotheo 3:1-7; Tito 1:5-9) Wao wanajua kuwa ni lazima ‘walitendee kundi kwa wororo,’ ndipo kondoo watakapokuwa na sababu ya kuonyesha shukrani kwa ajili ya wachungaji hawa wenye upendo. (Matendo 20:29; Zaburi 100:3) Yehova aonapo kuwa kondoo zake wana mioyo iliyojaa shukrani kama hiyo, kwa hakika lazima moyo wake pia unafurahi!—Mithali 27:11.
3 Kwa hakika, hatungependa kupuuza thamani ya zawadi kutoka kwa Mungu; wala hatungependa kuzidharau zawadi zake. Hivyo, maswali mawili yanazuka: Wazee wanapaswa kulionaje daraka lao kutanikoni? Na washiriki wengine wa kundi wanaweza kuonyeshaje kuwa wanathamini “zawadi zikiwa wanadamu”?
‘Sisi Ni Wafanyakazi Wenzenu’
4, 5. (a) Paulo analifananisha kutaniko na nini, na kwa nini kielezi hicho chafaa? (b) Kielezi cha Paulo kinaonyesha nini kuhusiana na jinsi tunavyopaswa kuwaona na kuwatendea wenzetu?
4 Yehova amewakabidhi “zawadi zikiwa wanadamu” kiasi fulani cha mamlaka kutanikoni. Bila shaka, wazee hawangependa kutumia vibaya mamlaka yao, ingawa wao wanajua kuwa ni rahisi sana kwa wanadamu wasiokamilika kufanya hivyo. Basi, wao wanapaswa kujionaje kuhusiana na washiriki wengine wa kundi? Fikiria kielezi ambacho mtume Paulo alitumia. Akiisha kuzungumzia sababu ya kuandaliwa kwa “zawadi zikiwa wanadamu,” Paulo aliandika hivi: “Na tukue kwa upendo katika mambo yote katika yeye aliye kichwa, Kristo. Kutoka katika yeye mwili wote, kwa kuunganishwa pamoja kwa upatano na kufanywa ushirikiane kupitia kila kiungo ambacho hupa kile kihitajiwacho, kulingana na utendaji wa kila kiungo kimoja-kimoja katika kipimo kipasacho, hutokeza ukuzi wa mwili ili kujijenga huo wenyewe katika upendo.” (Waefeso 4:15, 16) Hivyo Paulo alilifananisha kutaniko, pamoja na wazee na washiriki wengine, na mwili wa binadamu. Kwa nini kielezi hicho chafaa?
5 Mwili wa binadamu una viungo vingi mbalimbali lakini una kichwa kimoja pekee. Hata hivyo, hakuna chochote mwilini—kiwe ni msuli, neva, au mshipa wa damu—ambacho hakifai. Kila kiungo ni muhimu, nacho huchangia jambo fulani kwa afya na uzuri wa mwili wote. Vivyo hivyo, kutaniko limefanyizwa na washiriki mbalimbali, lakini kila mmoja—wachanga kwa wazee, wenye nguvu au wenye udhaifu—anaweza kuchangia jambo fulani kwa afya ya kiroho na uzuri wa kutaniko kwa ujumla. (1 Wakorintho 12:14-26) Yeyote asione kuwa hafai chochote. Kwa upande mwingine wenye kupita kiasi, yeyote asijione kuwa bora, kwa kuwa sisi sote—wachungaji na kondoo vilevile—ni sehemu ya mwili, na kuna kichwa kimoja tu, Kristo. Hivyo Paulo atoa mfano mzuri wa upendo, kujali, na staha tunazopaswa kuonyeshana. Kutambua jambo hilo kunawasaidia wazee kuwa na maoni ya unyenyekevu na yenye usawaziko juu ya daraka lao kutanikoni.
6. Ingawa Paulo alikuwa na mamlaka ya kimitume, yeye alionyeshaje roho ya unyenyekevu?
6 Hao “zawadi zikiwa wanadamu” hawatafuti kudhibiti maisha au imani ya waabudu wenzao. Ingawa Paulo alikuwa na mamlaka ya kimitume, kwa unyenyekevu aliwaambia Wakorintho hivi: “Si kwamba sisi ndio mabwana-wakubwa juu ya imani yenu, bali sisi ni wafanyakazi wenzi kwa shangwe yenu, kwa maana ni kwa imani yenu kwamba nyinyi mnasimama.” (2 Wakorintho 1:24) Paulo hakutaka kudhibiti imani na njia ya maisha ya ndugu zake. Kwa hakika hakuona uhitaji wa kufanya hivyo, kwa kuwa alionyesha uhakika kwamba tayari walikuwa wanaume na wanawake waaminifu waliokuwa katika tengenezo la Yehova kwa sababu walitaka kufanya yaliyo mema. Kwa hiyo, akisema kujihusu mwenyewe na kumhusu mwandamani wake Timotheo, kwa kweli Paulo alikuwa akimaanisha hivi: ‘Ni wajibu wetu kuwasaidia nyinyi mmtumikie Mungu kwa shangwe.’ (2 Wakorintho 1:1) Hiyo ilikuwa roho ya unyenyekevu kama nini!
7. Wazee wanyenyekevu hutambua nini kuhusu daraka lao kutanikoni, nao wana uhakika upi na wafanyakazi wenzao?
7 Leo, “zawadi zikiwa wanadamu” wana wajibu huohuo. Wao ni ‘wafanyakazi wenzi kwa shangwe yetu.’ Wazee wanyenyekevu hutambua kwamba si juu yao kuamua kiasi ambacho wengine wanaweza kufanya katika utumishi kwa Mungu. Wanajua kuwa ingawa huenda wakawatia wengine moyo wapanue au kuboresha huduma yao, utumishi kwa Mungu unapasa kutoka ndani ya moyo wenye kupenda. (Linganisha 2 Wakorintho 9:7.) Wao wana uhakika kuwa ikiwa wafanyakazi wenzao wana shangwe, watafanya kadiri wawezavyo. Kwa njia hiyo wao wana tamaa kubwa ya kuwasaidia ndugu zao ‘wamtumikie BWANA kwa furaha.’—Zaburi 100:2.
Kuwasaidia Wote Watumikie kwa Shangwe
8. Wazee wanaweza kuwasaidia ndugu zao kwa njia zipi ili wamtumikie Mungu kwa shangwe?
8 Enyi wazee, mnaweza kuwasaidiaje ndugu zenu watumikie kwa shangwe? Mnaweza kutia moyo kwa kuweka kielelezo. (1 Petro 5:3) Acheni bidii na shangwe yenu katika huduma ionekane, na huenda wengine watatiwa moyo kuiga kielelezo chenu. Wapongezeni wengine kwa jitihada zao za nafsi yote. (Waefeso 4:29) Pongezi changamfu na ya kweli huwasaidia wengine kuona kuwa wanafaa na wanahitajiwa. Hiyo huwatia moyo kondoo watake kufanya yaliyo bora zaidi wakimtumikia Mungu. Epukeni kufanya ulinganishi isivyofaa. (Wagalatia 6:4) Ulinganishi wa aina hiyo huelekea kuvunja moyo badala ya kuwatia wengine moyo ili waboreshe hali yao. Mbali na hayo, kondoo za Yehova ni watu binafsi—walio na hali mbalimbali na uwezo mbalimbali. Kama Paulo, onyesheni kwamba mna uhakika na ndugu zenu. Upendo “huamini mambo yote,” hivyo tunafanya vema kuamini kuwa ndugu zetu wanampenda Mungu nao wanataka kumpendeza. (1 Wakorintho 13:7) ‘Mnapowaonyesha wengine heshima,’ mnafanya wafanye yote wawezayo. (Waroma 12:10) Mwe na hakika kwamba kondoo wanapotiwa moyo na kuburudishwa, wengi wao watafanya yote wawezayo katika kumtumikia Mungu, nao watapata shangwe katika utumishi huo.—Mathayo 11:28-30.
9. Ni maoni gani kuhusu wazee wengine yatakayomsaidia kila mzee kutumikia kwa shangwe?
9 Kuwa na maoni yenye unyenyekevu kwamba wewe ni ‘mfanyakazi mwenzi’ kutakusaidia wewe kutumikia kwa shangwe na kuzithamini zawadi za pekee za wazee wenzako. Kila mzee ana vipaji na uwezo wake mwenyewe anavyoweza kutumia kwa faida ya kutaniko. (1 Petro 4:10) Huenda mzee mmoja ana zawadi ya kufundisha. Huenda mwingine akawa ana uwezo wa kuratibu mambo. Na bado huenda mwingine akawa mwenye kufikiwa kwa urahisi zaidi kwa sababu ya uchangamfu wake na huruma zake. Ukweli ni kwamba hakuna mzee aliye na kila zawadi kwa kiwango kilekile. Je, kuwa na zawadi fulani hususa—kwa mfano, zawadi ya kufundisha—humfanya mzee mmoja kuwa bora kuliko mwingine? La, hasha! (1 Wakorintho 4:7) Kwa upande mwingine, hakuna haja kuhusudu zawadi ambayo mwingine anayo au kuona kuwa hufai wakati mzee mwingine anapopongezwa na wengine kwa sababu ya uwezo wake. Kumbuka kuwa wewe mwenyewe una zawadi ambazo Yehova huziona ndani yako. Naye anaweza kukusaidia kuzisitawisha zawadi hizo na kuzitumia kwa faida ya ndugu zako.—Wafilipi 4:13.
‘Iweni Watiifu na Wenye Kunyenyekea’
10. Kwa nini inafaa tuthamini “zawadi zikiwa wanadamu”?
10 Tunapopokea zawadi, inafaa tushukuru. “Jionyesheni wenyewe kuwa wenye shukrani,” lasema andiko la Wakolosai 3:15. Vipi, basi, kuhusu “zawadi zikiwa wanadamu,” zawadi yenye thamani ambayo Yehova ametupa? Bila shaka, sisi tunamshukuru Yehova hasa, Mpaji-Zawadi mkarimu. Lakini namna gani kuhusu “zawadi zikiwa wanadamu” wenyewe? Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunawathamini?
11. (a) Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunawathamini “zawadi zikiwa wanadamu”? (b) Ni nini maana ya semi “iweni watiifu” na “wenye kunyenyekea”?
11 Tunaweza kuonyesha uthamini wetu kwa “zawadi zikiwa wanadamu” kwa kutii mara moja mashauri na maamuzi yao yanayotegemea Biblia. Biblia inatushauri hivi: “Iweni watiifu kwa wale ambao wanaongoza miongoni mwenu na kuwa wenye kunyenyekea, kwa maana wao wanafuliza kulinda juu ya nafsi zenu kama wale watakaotoa hesabu; ili wapate kufanya hili kwa shangwe na si kwa kutweta, kwa maana hili lingekuwa lenye hasara kwenu.” (Waebrania 13:17) Ona kuwa ni lazima tuwe “watiifu” na pia wenye “kunyenyekea” kwa wale wanaoongoza. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “wenye kunyenyekea” lamaanisha kihalisi “kubali.” Akielezea juu ya semi “iweni watiifu” na “wenye kunyenyekea,” msomi wa Biblia R. C. H. Lenski asema hivi: “Mtu hutii anapokubaliana na jambo analoambiwa afanye, anaposadiki usahihi wa jambo hilo na faida yake; mtu hukubali . . . anapokuwa na maoni tofauti.” Tunapoelewa na kukubaliana na mwelekezo wa wale wanaoongoza, huenda tukatii kwa urahisi. Lakini vipi ikiwa hatuelewi sababu ya kufanywa kwa uamuzi fulani?
12. Kwa nini tunyenyekee, au tukubali, hata ikiwa hatuelewi kikamili sababu ya kufanywa kwa uamuzi fulani?
12 Basi hapo ndipo tunapohitaji kunyenyekea, au kukubali. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba tunahitaji kutumaini kuwa wanaume hawa wanaostahili kiroho wanatujali. Kwani, wanajua vema kuwa ni lazima watoe hesabu kwa Yehova kwa ajili ya kondoo waliokabidhiwa kutunza. (Yakobo 3:1) Kwa kuongezea, ni vema tukumbuke kuwa huenda tusijue mambo yote ya siri yaliyowaongoza kufanya uamuzi uliotegemea mambo wanayofahamu.—Mithali 18:13.
13. Ni nini kinachoweza kutusaidia kunyenyekea kuhusiana na maamuzi ya hukumu ya wazee?
13 Vipi juu ya kunyenyekea inapohusu maamuzi ya hukumu? Ni kweli, huenda jambo hilo lisiwe rahisi, hasa ikiwa uamuzi unafanywa wa kumtenga na ushirika mtu tumpendaye—mtu wa ukoo au rafiki mkubwa. Hapa tena, ni bora kunyenyekea uamuzi wa “zawadi zikiwa wanadamu.” Wao wako katika hali ya kutopendelea kuliko vile sisi tuwezavyo kuwa, nao huenda wakajua mambo mengi kuliko sisi. Mara nyingi ndugu hawa huumia sana moyoni juu ya maamuzi hayo; ni daraka zito ‘kumfanyia BWANA hukumu.’ (2 Mambo ya Nyakati 19:6) Wao hufanya kila jitihada ya kuonyesha rehema, kwa kuwa wanatambua kwamba Mungu yuko “tayari kusamehe.” (Zaburi 86:5) Lakini ni lazima wao pia watunze usafi wa kutaniko, na Biblia huonyesha kwamba wawatenge na ushirika wakosaji wasiotubu. (1 Wakorintho 5:11-13) Katika visa vingi mkosaji mwenyewe hukubali uamuzi huo. Huenda hasa anahitaji nidhamu ya aina hiyo ili arudiwe na fahamu. Ikiwa sisi, wapendwa wake, tunanyenyekea kuhusu uamuzi huo, huenda kwa njia hiyo tunamsaidia kufaidika kutokana na nidhamu hiyo.—Waebrania 12:11.
“Mwape Ufikirio Ambao Ni Zaidi Kuliko Ule wa Kawaida”
14, 15. (a) Kulingana na 1 Wathesalonike 5:12, 13, ni kwa nini wazee hustahili ufikirio wetu? (b) Kwa nini inaweza kusemwa kwamba wazee ‘wanafanya kazi kwa bidii miongoni mwetu’?
14 Pia, tunaweza kuwathamini “zawadi zikiwa wanadamu” kwa kuwapa ufikirio. Akiliandikia kutaniko huko Thesalonike, Paulo aliwashauri washiriki wake hivi: “Mwe na staha kwa wale wanaofanya kazi kwa bidii miongoni mwenu na kuwasimamia nyinyi katika Bwana na kuwaonya nyinyi kwa upole; na mwape ufikirio ambao ni zaidi kuliko ule wa kawaida katika upendo kwa sababu ya kazi yao.” (1 Wathesalonike 5:12, 13) ‘Kufanya kazi kwa bidii’—je, hilo halifafanui wazee ambao hujitolea wenyewe bila ubinafsi kwa niaba yetu? Fikiria kidogo ule mzigo mzito ambao ndugu hawa wapendwa huubeba.
15 Wengi wao ni wanaume wenye familia wanaolazimika kufanya kazi ili kuandalia familia zao riziki. (1 Timotheo 5:8) Ikiwa mzee ana watoto, wachanga hao huhitaji kupewa wakati na uangalifu wa baba yao. Huenda akahitaji kuwasaidia na masomo yao ya shule nyumbani, na vilevile kuwapangia wakati fulani ili waweze kutumia nguvu zao za ujana katika tafrija inayofaa. (Mhubiri 3:1, 4) Jambo muhimu zaidi ni kwamba yeye hutunza mahitaji ya kiroho ya familia yake, huongoza funzo la Biblia la familia kwa ukawaida, huhubiri pamoja nao kwenye huduma ya shambani, na kuwapeleka kwenye mikutano ya Kikristo. (Kumbukumbu la Torati 6:4-7; Waefeso 6:4) Na tusisahau kuwa mbali na madaraka hayo ambayo wengi wetu tunayo, wazee wana wajibu zaidi: kutayarisha sehemu za mikutano, kufanya ziara za uchungaji, kutunza hali njema ya kiroho ya kutaniko na ikihitajika, kushughulikia kesi za hukumu. Wengine huwa na madaraka zaidi katika makusanyiko ya mzunguko, mikusanyiko ya wilaya, ujenzi wa Majumba ya Ufalme, na katika Halmashauri za Uhusiano na Hospitali. Kwa kweli, ndugu hawa ‘wanafanya kazi kwa bidii’!
16. Eleza jinsi tuwezavyo kuwapa wazee ufikirio.
16 Tunaweza kuwaonyeshaje ufikirio? Mithali ya Biblia yasema hivi: “Neno linenwalo wakati wa kufaa ni jema kama nini!” (Mithali 15:23; 25:11) Hivyo, maneno yenye uthamini wa kweli na yenye kutia moyo yaweza kuwaonyesha kuwa hatuipuuzi kazi yao ya bidii. Pia, tunapaswa kusawazika kuhusiana na yale tunayowatazamia watimize. Kwa upande mwingine, tunapaswa kujisikia huru kuwaendea ili kupata msaada. Huenda kukawa nyakati ambapo ‘moyo wetu unaumia ndani yetu’ nasi tunahitaji kitia-moyo, mwongozo, au mashauri ya Kimaandiko ya wale ambao wana “sifa ya kustahili kufundisha” Neno la Mungu. (Zaburi 55:4; 1 Timotheo 3:2) Wakati huohuo, tunahitaji kukumbuka kwamba mzee hawezi kutupa wakati mwingi mno, kwa kuwa hawezi kupuuza mahitaji ya familia yake mwenyewe au ya wengine kutanikoni. Tukiwa na “hisia-mwenzi” kwa hawa ndugu wanaofanya kazi kwa bidii, hatungependa kudai mengi mno kutoka kwao. (1 Petro 3:8) Badala yake, acheni tuthamini wakati na uangalifu wowote ule ambao kwa kufaa wanaweza kutupa.—Wafilipi 4:5.
17, 18. Wake wengi ambao waume zao ni wazee hujidhabihu kwa njia zipi, nasi tunaweza kuonyeshaje kuwa hatuwapuuzi dada hawa waaminifu?
17 Vipi kuhusu wake wa wazee? Je, wao pia hawastahili ufikirio wetu? Kwani, hawa wanashiriki waume zao na kutaniko. Mara nyingi hali hiyo huhitaji wajidhabihu. Mara kwa mara, wazee hulazimika kutumia saa za jioni wakitunza mambo ya kutaniko ilhali wangekuwa wakitumia wakati huo pamoja na familia zao. Katika makutaniko mengi, wanawake Wakristo waaminifu wanajidhabihu kwa hiari ili waume zao waweze kutunza kondoo za Yehova.—Linganisha 2 Wakorintho 12:15.
18 Tunaweza kuonyeshaje kwamba hatuwapuuzi hawa dada Wakristo waaminifu? Kwa hakika tunaweza kufanya hivyo kwa kutodai mengi mno kutoka kwa waume zao. Na vilevile tusisahau pia uwezo wa maneno sahili ya shukrani. Mithali 16:24 yasema hivi: “Maneno yapendezayo ni kama sega la asali; ni tamu nafsini, na afya mifupani.” Fikiria jambo hili lililoonwa. Baada ya mkutano wa Kikristo, wenzi wawili wa ndoa walimwendea mzee na kumwomba waongee naye kuhusu mwana wao tineja. Mzee huyo alipokuwa akiongea na wenzi hao, mke wake alingojea kwa subira. Baadaye, mama huyo akamwendea mke wa mzee na kusema: “Ningependa kukushukuru kwa ajili ya wakati ambao mume wako alitumia ili kusaidia familia yangu.” Maneno hayo ya shukrani, yaliyo sahili na matamu kwa kweli yaliugusa moyo wa mke huyo wa mzee.
19. (a) Wakiwa kikundi, wazee wanatimiza kwa uaminifu mambo gani? (b) Sote tunapaswa kuazimia kufanya nini?
19 Uandalizi wa wazee wa kuwachunga kondoo ni mojawapo ya “zawadi njema” za Yehova. (Yakobo 1:17) Na wanaume hawa si wakamilifu; wao hufanya makosa kama sisi sote. (1 Wafalme 8:46) Ingawa hivyo, wakiwa kikundi wazee katika makutaniko ulimwenguni pote wanatimiza kwa uaminifu mambo ambayo Yehova alinuia watimize—yaani, kulirekebisha upya, kulijenga, kuliunganisha, na kulilinda kundi. Kila mzee na aazimie kuendelea kutunza kondoo za Yehova kwa wororo, hivyo akijithibitisha mwenyewe kuwa zawadi, au baraka, kwa ndugu zake. Nasi sote na tuazimie kuonyesha kwamba tunawathamini hao “zawadi zikiwa wanadamu” kwa kuwa watiifu na kujinyenyekeza kwao na kwa kuwaonyesha ufikirio kwa ajili ya kazi yao ya bidii. Tunashukuru kama nini kwa sababu Yehova ameandaa kwa upendo wanaume ambao, kwa kweli, huambia kondoo zake hivi: ‘Ni wajibu wetu kuwasaidia nyinyi mmtumikie Mungu kwa shangwe’!
-