-
‘Baba Yenu Ni Mwenye Rehema’Mnara wa Mlinzi—2007 | Septemba 15
-
-
‘Baba Yenu Ni Mwenye Rehema’
“Endeleeni kuwa wenye rehema, kama vile Baba yenu alivyo mwenye rehema.”—LUKA 6:36.
1, 2. Maneno ya Yesu kwa waandishi na Mafarisayo na kwa wafuasi wake yanaonyesha jinsi gani kwamba rehema ni sifa yenye kupendeza?
SHERIA iliyotolewa kupitia Musa ilikuwa na matakwa na masharti 600 hivi. Ingawa lilikuwa jambo la maana kutimiza matakwa ya Sheria ya Musa, lilikuwa pia jambo la maana kuonyesha rehema. Fikiria yale ambayo Yesu aliwaambia Mafarisayo ambao hawakuwaonyesha wengine rehema. Mara mbili, aliwakemea akisema kwamba Mungu alikuwa ametangaza hivi: “Ninataka rehema, wala si dhabihu.” (Mathayo 9:10-13; 12:1-7; Hosea 6:6) Mwishoni mwa huduma yake, Yesu alisema: “Ole wenu ninyi, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! kwa sababu ninyi huitoa sehemu ya kumi ya mnanaa na dili na bizari, lakini mmepuuza mambo mazito zaidi ya Sheria, yaani, haki na rehema na uaminifu.”—Mathayo 23:23.
2 Ni wazi kwamba Yesu aliona rehema kuwa sifa ya maana sana. Aliwaambia wafuasi wake hivi: “Endeleeni kuwa wenye rehema, kama vile Baba yenu alivyo mwenye rehema.” (Luka 6:36) Hata hivyo, ili tuwe “waigaji wa Mungu,” tunahitaji kujua rehema ya kweli ni nini. (Waefeso 5:1) Zaidi ya hayo, kuelewa faida za rehema kutatuchochea kuonyesha sifa hiyo kwa ukamili zaidi katika maisha yetu.
Kuwaonyesha Rehema Wenye Uhitaji
3. Kwa nini tunapaswa kumwendea Yehova ili tujifunze maana ya rehema ya kweli?
3 Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Yehova ni mwenye neema na mwenye rehema, si mwepesi wa hasira naye ni mkuu katika fadhili zenye upendo. Yehova ni mwema kwa wote, na rehema zake ziko juu ya kazi zake zote.” (Zaburi 145:8, 9) Yehova ni “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote.” (2 Wakorintho 1:3) Tunaonyesha rehema kwa kumtendea mtu mwingine kwa huruma. Hiyo ni sehemu muhimu sana ya utu wa Mungu. Tunaweza kujifunza maana ya rehema ya kweli kupitia kielelezo cha Mungu na maagizo anayotupa.
4. Andiko la Isaya 49:15 linatufundisha nini kuhusu rehema?
4 Kama inavyoonyeshwa kwenye Isaya 49:15, Yehova anasema: “Je, mke anaweza kumsahau mtoto wake anayenyonya hivi kwamba asimhurumie mwana wa tumbo lake?” Maneno mbalimbali ya Kiebrania yanayohusiana sana na neno linalotafsiriwa hapa kuwa ‘kuhurumia’ yanatumiwa kuhusiana na rehema katika andiko la Zaburi 145:8, 9, linalonukuliwa hapo juu. Hisia zinazomchochea Yehova kuwa mwenye rehema zinalinganishwa na hisia ambazo kwa kawaida mama mwenye kunyonyesha anazo kuelekea mtoto wake. Pengine mtoto ana njaa au ana uhitaji mwingine. Hisia hizo zinamchochea mama kuwa na huruma, na hivyo anatosheleza mahitaji ya mtoto wake. Yehova ana hisia nyororo kama hizo kuelekea wale ambao anawaonyesha rehema.
5. Yehova alionyesha namna gani kwamba alikuwa “tajiri katika rehema” kuwaelekea Waisraeli?
5 Ni jambo zuri kuwahurumia wengine, lakini ni jambo bora hata zaidi kusukumwa na huruma kuchukua hatua ili kuwasaidia wenye uhitaji. Fikiria jinsi Yehova alivyoitikia waabudu wake walipokuwa utumwani huko Misri miaka 3,500 iliyopita. Alimwambia Musa hivi: “Pasipo shaka nimeyaona mateso ya watu wangu walio Misri, nami nimesikia kilio chao kwa sababu ya wale wanaowalazimisha kufanya kazi; kwa sababu nayajua vizuri maumivu waliyo nayo. Nami ninashuka ili kuwakomboa kutoka katika mkono wa Wamisri na kuwatoa katika nchi hiyo mpaka kwenye nchi nzuri na kubwa, nchi inayotiririka maziwa na asali.” (Kutoka 3:7, 8) Miaka 500 hivi baada ya Waisraeli kukombolewa kutoka Misri, Yehova aliwakumbusha: “Mimi ndiye niliyewatoa Israeli kutoka Misri nami nikawakomboa ninyi kutoka mkono wa Misri na kutoka mkono wa falme zote zilizokuwa zikiwakandamiza ninyi.” (1 Samweli 10:18) Kwa sababu ya kuacha viwango vya uadilifu vya Mungu, mara kwa mara Waisraeli walikuwa katika hali ngumu. Hata hivyo, Yehova aliwahurumia na aliwaokoa tena na tena. (Waamuzi 2:11-16; 2 Mambo ya Nyakati 36:15) Hilo linaonyesha jinsi Mungu huyo mwenye upendo anavyowatendea wale walio katika uhitaji, hatari, au hali ngumu. Yehova ni “tajiri katika rehema.”—Waefeso 2:4.
6. Yesu Kristo alimwiga Baba yake jinsi gani katika kuonyesha rehema?
6 Alipokuwa duniani, Yesu Kristo alimwiga Baba yake kikamilifu katika kuonyesha rehema. Yesu alitenda namna gani wanaume wawili vipofu walipomsihi hivi: “Bwana, uturehemu, Mwana wa Daudi”? Walikuwa wakimsihi Yesu awarudishie kimuujiza uwezo wa kuona. Yesu alifanya hivyo, lakini hakufanya muujiza bila hisia. ‘Akiwasikitikia,’ inasema Biblia, “[Yesu] akayagusa macho yao, na mara moja wakapata kuona.” (Mathayo 20:30-34) Sikitiko lilimchochea Yesu kufanya miujiza mingi ambayo iliwaletea kitulizo vipofu, watu waliokuwa na roho waovu, wenye ukoma, na wazazi wenye watoto waliokuwa wakiteseka.—Mathayo 9:27; 15:22; 17:15; Marko 5:18, 19; Luka 17:12, 13.
7. Mfano wa Yehova Mungu na Mwana wake unatufundisha nini kuhusu rehema?
7 Mfano wa Yehova Mungu na Yesu Kristo unaonyesha kwamba rehema inahusisha mambo mawili—hisia za huruma, au sikitiko kuelekea wenye uhitaji na matendo yanayoleta kitulizo kwa wale walio katika uhitaji. Ili kuwa mwenye rehema ni lazima mtu awe na hisia na atende. Katika Maandiko, mara nyingi rehema inarejelea tendo la fadhili kuelekea wale walio katika uhitaji. Hata hivyo, rehema inaonyeshwa jinsi gani katika hukumu? Je, rehema inahusu pia kutofanya jambo fulani kama vile kujizuia kutoa adhabu?
Kuwaonyesha Rehema Wakosaji
8, 9. Rehema ambayo Daudi alionyeshwa baada ya dhambi yake pamoja na Bath-sheba ilitia ndani nini?
8 Fikiria yale yaliyotukia baada ya nabii Nathani kuzungumza na Mfalme Daudi wa Israeli la kale kuhusu uzinzi wa Daudi pamoja na Bath-sheba. Daudi aliyetubu alisali hivi: “Ee Mungu, unionyeshe kibali kulingana na fadhili zako zenye upendo. Ufutilie mbali makosa yangu kulingana na wingi wa rehema zako. Unioshe kabisa kutokana na kosa langu, na kunitakasa kutokana na dhambi yangu. Kwa maana mimi mwenyewe nayajua makosa yangu, na dhambi yangu iko mbele yangu daima. Dhidi yako wewe, wewe peke yako, nimetenda dhambi, nami nimefanya lililo baya machoni pako.”—Zaburi 51:1-4.
9 Daudi alisikitika sana. Yehova alimsamehe dhambi yake na alijizuia kuwahukumu vikali Daudi na Bath-sheba. Kulingana na Sheria ya Musa, Daudi na Bath-sheba walipaswa kuuawa. (Kumbukumbu la Torati 22:22) Ingawa hawakuuawa, hawakuepuka matokeo mabaya ya dhambi yao. (2 Samweli 12:13) Rehema ya Mungu inatia ndani kusamehe makosa. Hata hivyo, hajizuii kutoa adhabu inayostahili.
10. Ingawa Yehova ni mwenye rehema anapotekeleza hukumu, kwa nini hatupaswi kuchezea rehema zake?
10 Kwa kuwa “kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu,” na “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo,” wanadamu wote wanastahili kifo. (Waroma 5:12; 6:23) Tunashukuru kama nini kwamba Yehova anaonyesha rehema anapotekeleza hukumu! Hata hivyo, tunapaswa kuwa waangalifu ili tusichezee rehema za Mungu. ‘Njia zote za Yehova ni haki,’ linasema andiko la Kumbukumbu la Torati 32:4. Anapoamua kuonyesha rehema, Mungu hapuuzi viwango vyake vikamilifu vya haki.
11. Yehova alionyesha jinsi gani kwamba hakupuuza haki aliposhughulikia dhambi ya Daudi pamoja na Bath-sheba?
11 Daudi na Bath-sheba walipaswa kwanza kusamehewa kabla ya hukumu ya kifo kupunguzwa. Waamuzi wa Israeli hawakuruhusiwa kusamehe dhambi. Ikiwa wangeruhusiwa kushughulikia kisa hicho, wangelazimika tu kutoa hukumu ya kifo. Sheria ilitaka watoe hukumu hiyo. Hata hivyo, kwa sababu ya agano lake pamoja na Daudi, Yehova alitaka kuona ikiwa kulikuwa na msingi wa kusamehe dhambi ya Daudi. (2 Samweli 7:12-16) Hivyo, Yehova Mungu, yule “Mwamuzi wa dunia yote,” ambaye ni “mchunguzaji wa moyo,” aliamua kushughulikia kisa hicho yeye mwenyewe. (Mwanzo 18:25; 1 Mambo ya Nyakati 29:17) Mungu aliweza kusoma kwa usahihi moyo wa Daudi, akaona kwamba alikuwa ametubu kikweli, na hivyo akamsamehe.
12. Wanadamu wenye dhambi wanaweza kufaidika jinsi gani na rehema ya Mungu?
12 Rehema ambayo Yehova anatuonyesha kwa kutuwezesha kuwekwa huru kutokana na adhabu ya kifo kwa sababu ya dhambi tuliyorithi inapatana na haki yake. Ili asamehe dhambi bila kuvunja haki yake, Yehova ameandaa dhabihu ya fidia ya Mwana wake, Yesu Kristo, ambalo ndilo tendo kubwa zaidi la rehema. (Mathayo 20:28; Waroma 6:22, 23) Ili tufaidike kutokana na rehema ya Mungu, ambayo inaweza kutuokoa tusipatwe na adhabu ya kifo kwa sababu ya dhambi tuliyorithi, tunapaswa ‘kumwamini Mwana.’—Yohana 3:16, 36.
Mungu wa Rehema na Haki
13, 14. Je, rehema ya Mungu inapunguza uzito wa haki yake? Eleza.
13 Ingawa rehema ya Yehova haivunji kiwango chake cha haki, je, kwa kadiri fulani rehema inabadili haki yake? Je, rehema inapunguza uzito wa haki ya Mungu? Hapana.
14 Kupitia nabii Hosea, Yehova aliwaambia Waisraeli hivi: “Nitakuchumbia mpaka wakati usio na kipimo, nitakuchumbia uwe wangu katika uadilifu na katika haki na katika fadhili zenye upendo na katika rehema.” (Hosea 2:19) Maneno hayo yanaonyesha wazi kwamba rehema ya Yehova sikuzote inapatana na sifa zake nyingine, kutia ndani haki. Yehova ni “Mungu mwenye rehema na neema, . . . anayesamehe kosa na ubaya na dhambi, lakini kwa vyovyote hatakosa kuadhibu.” (Kutoka 34:6, 7) Yehova ni Mungu wa rehema na haki. Biblia inasema hivi kumhusu: “Yeye Mwamba, kazi zake ni kamilifu, kwa maana njia zake zote ni haki.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Haki ya Mungu ni kamilifu, kama ilivyo rehema yake. Hakuna iliyo kubwa kuliko nyingine, wala hakuna ile inayohitaji kupunguza uzito wa nyingine. Badala yake, sifa hizo mbili zinafanya kazi pamoja kwa upatano.
15, 16. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba haki ya Mungu si yenye ukatili? (b) Waabudu wa Yehova wanaweza kuwa na uhakika gani wakati Yehova atakapotekeleza hukumu yake juu ya mfumo huu mbovu wa mambo?
15 Haki ya Yehova si yenye ukatili. Sikuzote haki inahusiana na sheria, na kwa kawaida hukumu inatolewa kwa wakosaji ambao wanastahili adhabu. Hata hivyo, haki ya Mungu inaweza pia kutia ndani wokovu kwa ajili ya wale wanaostahili. Kwa mfano, watu waovu katika majiji ya Sodoma na Gomora walipoharibiwa, mzee wa ukoo Loti na mabinti wake wawili waliokolewa.—Mwanzo 19:12-26.
16 Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakapotekeleza hukumu juu ya mfumo huu mbovu wa mambo, ule “umati mkubwa” wa waabudu wa kweli, ambao “wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo,” utaokolewa. Kwa hiyo, waabudu hao ‘watatoka katika ile dhiki kuu.’—Ufunuo 7:9-14.
Kwa Nini Tuwe Wenye Rehema?
17. Ni nini sababu ya msingi ya kuwa wenye rehema?
17 Kwa kweli, mfano wa Yehova na wa Yesu Kristo unatufundisha maana ya rehema ya kweli. Likitupa sababu ya msingi ya kuwa wenye rehema, andiko la Methali 19:17 linasema hivi: “Anayemwonyesha kibali mtu wa hali ya chini anamkopesha Yehova, na Yeye atamlipa matendo yake.” Yehova anafurahi tunapomwiga yeye na Mwana wake kwa kuwa wenye rehema tunaposhughulika na wenzetu. (1 Wakorintho 11:1) Wengine pia wanatiwa moyo kuwa wenye rehema, kwa kuwa tunapowaonyesha wengine rehema wao pia wanatuonyesha rehema.—Luka 6:38.
18. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kuwa wenye rehema?
18 Rehema ni mchanganyiko wa sifa nyingi nzuri. Inatia ndani neema, upendo, fadhili, na wema. Hisia nyororo za huruma ndizo zinazotuchochea kutenda kwa rehema. Ingawa rehema ya Mungu haipunguzi uzito wa haki yake, Yehova si mwepesi wa hasira na kwa subira anawapa wakosaji wakati wa kutosha ili watubu. (2 Petro 3:9, 10) Kwa hiyo, rehema inahusiana na subira na ustahimilivu. Kwa kuwa rehema ni mchanganyiko wa sifa nyingi nzuri, kutia ndani sifa mbalimbali za matunda ya roho ya Mungu, rehema inaweza kutusaidia kusitawisha sifa hizo. (Wagalatia 5:22, 23) Ni jambo la maana kama nini tujitahidi kuwa wenye rehema!
“Wenye Furaha ni Wale Walio na Rehema”
19, 20. Ni katika maana gani rehema inafurahi juu ya hukumu?
19 Mwanafunzi Yakobo anatuambia kwa nini rehema inapaswa kuwa sifa muhimu katika maisha yetu. Aliandika hivi: “Rehema hufurahi kwa njia ya ushindi juu ya hukumu.” (Yakobo 2:13b) Yakobo alikuwa akisema kuhusu rehema ambayo mwabudu wa Yehova anawaonyesha wengine. Rehema inafurahi kwa njia ya ushindi juu ya hukumu katika maana ya kwamba wakati unapofika wa mtu ‘kutoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe,’ Yehova anafikiria matendo ya rehema ya mtu huyo naye anamsamehe kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Mwana Wake. (Waroma 14:12) Bila shaka, sababu moja iliyofanya Daudi aonyeshwe rehema kuhusiana na dhambi yake pamoja na Bath-sheba ni kwamba Daudi mwenyewe alikuwa mtu mwenye rehema. (1 Samweli 24:4-7) Kwa upande mwingine, “yeye asiye na mazoea ya kuonyesha rehema atapata hukumu yake bila rehema.” (Yakobo 2:13a) Haishangazi kwamba wale “wasio na rehema” wanaorodheshwa kati ya watu ambao Mungu anaona kuwa “wanastahili kifo”!—Waroma 1:31, 32.
20 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale walio na rehema, kwa kuwa wataonyeshwa rehema.” (Mathayo 5:7) Maneno hayo yanaonyesha kwa mkazo kama nini kwamba wale wanaotafuta rehema ya Mungu wanapaswa wao wenyewe kuwa wenye rehema! Habari inayofuata itazungumzia jinsi tunavyoweza kuonyesha rehema katika maisha yetu ya kila siku.
-
-
Tunaweza Jinsi Gani Kutenda Kwa Rehema?Mnara wa Mlinzi—2007 | Septemba 15
-
-
Tunaweza Jinsi Gani Kutenda Kwa Rehema?
“Tuwatendee wote mema, na hasa wale ambao katika imani ni jamaa zetu.”—WAGALATIA 6:10.
1, 2. Mfano wa Msamaria mwema unatufundisha nini kuhusu rehema?
ALIPOKUWA akizungumza na Yesu, mtu mmoja mwenye ujuzi mwingi wa Sheria alimuuliza hivi: “Ni nani kwa kweli aliye jirani yangu?” Yesu alimjibu kwa kusimulia mfano unaofuata: “Mtu fulani alikuwa akishuka kutoka Yerusalemu kwenda Yeriko akaanguka katikati ya wanyang’anyi, ambao walimvua nguo na pia kumpiga, kisha wakaenda zao, wakamwacha karibu kufa. Sasa, ikatukia kwamba, kuhani fulani alikuwa akishuka katika barabara hiyo, lakini, alipomwona, akapita upande ule mwingine. Vivyo hivyo, Mlawi pia, alipofika chini katika mahali hapo na kumwona, akapita kando upande wa pili. Lakini Msamaria fulani aliyekuwa akisafiri katika barabara ile alikuja, akamkuta na, alipomwona, akamsikitikia. Kwa hiyo akamkaribia akayafunga majeraha yake, na kumwaga mafuta na divai juu yake. Kisha akampandisha juu ya mnyama wake mwenyewe akamleta kwenye nyumba ya wageni na kumtunza. Na siku iliyofuata akatoa dinari mbili, akampa hizo mtu aliyekuwa akitunza nyumba hiyo ya wageni, na kusema, ‘Mtunze, na chochote utakachotumia mbali na hiki, mimi nitakulipa nitakaporudi hapa.’” Kisha, Yesu akamuuliza hivi msikilizaji wake: “Ni nani kati ya watu hao watatu anayeonekana kwako kuwa alijifanya kuwa jirani kwa mtu aliyeanguka katikati ya wanyang’anyi?” Mtu huyo akajibu: “Ni yule aliyemtendea kwa rehema.”—Luka 10:25, 29-37a.
2 Tendo la Msamaria huyo la kumtunza mtu aliyeumizwa linaonyesha waziwazi maana ya rehema ya kweli. Akichochewa na sikitiko, au huruma, Msamaria huyo alitenda kwa njia ambayo ilimtuliza mtu huyo aliyeumizwa. Zaidi ya hayo, Msamaria huyo hakumjua mtu huyo aliyekuwa na uhitaji. Rehema haizuiwi na mipaka ya kitaifa, kidini, au kitamaduni. Baada ya kutoa mfano huo wa Msamaria mwema, Yesu alimshauri msikilizaji wake hivi: “Nenda, na uwe ukifanya vivyo hivyo.” (Luka 10:37b) Tunaweza kutii himizo hilo na kujitahidi kuwa wenye rehema kwa wengine. Lakini jinsi gani? Tunaweza kutenda kwa rehema katika maisha yetu ya kila siku katika njia gani?
“Ikiwa Ndugu . . . Yuko Uchi”
3, 4. Kwa nini tuhangaikie kutenda kwa rehema hasa katika kutaniko la Kikristo?
3 Mtume Paulo alisema hivi: “Tukiwa na wakati unaofaa kwa ajili ya hilo, tuwatendee wote mema, na hasa wale ambao katika imani ni jamaa zetu.” (Wagalatia 6:10) Basi, acheni kwanza tuchunguze jinsi tunavyoweza kuwatendea kwa rehema nyingi wale ambao katika imani ni jamaa zetu.
4 Akiwahimiza Wakristo wa kweli wawe wenye rehema kuelekea mmoja na mwenzake, mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Yeye asiye na mazoea ya kuonyesha rehema atapata hukumu yake bila rehema.” (Yakobo 2:13) Mistari inayozunguka maneno hayo yaliyoongozwa na roho inatuonyesha njia fulani tunazoweza kutenda kwa rehema. Kwa mfano, tunasoma hivi kwenye Yakobo 1:27: “Namna ya ibada iliyo safi na isiyotiwa unajisi kwa maoni ya Mungu wetu na Baba ni hii: kuwatunza mayatima na wajane katika dhiki yao, na kuendelea kujitunza bila doa kutokana na ulimwengu.” Andiko la Yakobo 2:15, 16 linasema hivi: “Ikiwa ndugu au dada yuko uchi naye hana chakula cha kutosha kwa ajili ya siku, na mmoja wenu amwambie: ‘Nenda kwa amani, jipashe moto na kula vizuri,’ lakini ninyi mkose kumpa mahitaji ya mwili wake, ina faida gani?”
5, 6. Tunaweza jinsi gani kutenda matendo mengi ya rehema tunaposhirikiana na kutaniko la kwetu?
5 Kuwajali wengine na kuwasaidia wale walio katika uhitaji ni jambo linaloitambulisha dini ya kweli. Ibada yetu haituruhusu kuwahangaikia wengine kwa maneno matupu tu ya kuwatakia mema. Badala yake, hisia nyororo za huruma zinatuchochea kuwasaidia wale walio na uhitaji mkubwa. (1 Yohana 3:17, 18) Ndiyo, kumpikia mgonjwa, kumsaidia kazi za nyumbani mtu aliyezeeka, kumpeleka kwenye mikutano ya Kikristo inapohitajika, na kutokuwa mchoyo kuelekea wale wanaostahili msaada ni kati ya matendo mengi ya rehema ambayo tunapaswa kutenda.—Kumbukumbu la Torati 15:7-10.
6 Ingawa ni jambo la maana kuwasaidia kimwili washiriki wa kutaniko la Kikristo linalopanuka, ni jambo la maana hata zaidi kuwasaidia kiroho. Tunahimizwa ‘tuseme kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika, na kutegemeza walio dhaifu.’ (1 Wathesalonike 5:14) “Wanawake wenye umri mkubwa” wanatiwa moyo kuwa “walimu wa yaliyo mema.” (Tito 2:3) Kuhusu waangalizi Wakristo, Biblia inasema hivi: “Kila mmoja atakuwa kama mahali pa kujificha kutokana na upepo na mahali pa kujificha kutokana na dhoruba ya mvua.”—Isaya 32:2.
7. Tunajifunza nini kuhusu kuonyesha rehema kutokana na wanafunzi huko Siria ya Antiokia?
7 Zaidi ya kuwajali wajane, mayatima, na wale waliohitaji kusaidiwa na kutiwa moyo katika maeneo ya kwao, nyakati nyingine makutaniko ya karne ya kwanza yalituma misaada kwa waamini wenzao wa maeneo mengine. Kwa mfano, nabii Agabo alipotabiri kwamba “njaa kali ilikuwa karibu kuja juu ya dunia nzima inayokaliwa,” wanafunzi huko Siria ya Antiokia ‘waliamua, kila mmoja kwa kadiri ambayo yeyote angeweza kutoa, wafanye huduma ya kupeleka misaada kwa akina ndugu waliokuwa wakikaa Yudea.’ Misaada hiyo ilitumwa kwa wazee wa huko “kwa mkono wa Barnaba na Sauli.” (Matendo 11:28-30) Namna gani leo? “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” amepanga kuwe na halmashauri za kutoa misaada ili ziwatunze ndugu zetu ambao huenda wamepatwa na misiba ya asili, kama vile vimbunga, matetemeko ya nchi, au mawimbi ya tsunami. (Mathayo 24:45) Kujitolea kutumia wakati, nguvu, na mali zetu kuhusiana na mpango huo ni njia moja nzuri ya kuonyesha rehema.
“Mkiendelea Kuonyesha Upendeleo”
8. Upendeleo unatuzuia jinsi gani tusionyeshe rehema?
8 Akionya kuhusu tabia inayotuzuia kuonyesha rehema na kufuata “sheria ya kifalme” ya upendo, Yakobo aliandika hivi: “Mkiendelea kuonyesha upendeleo, mnafanya dhambi, kwa maana sheria inawakaripia ninyi kuwa ni wakosaji.” (Yakobo 2:8, 9) Kumwonyesha upendeleo mtu aliye tajiri kimwili au wale walio mashuhuri kunaweza kutufanya tusisikie “kilio cha kulalamika cha mtu wa hali ya chini.” (Methali 21:13) Upendeleo unazuia roho ya rehema. Tunaonyesha rehema kwa kuwatendea wengine bila ubaguzi.
9. Kwa nini si vibaya kuwaonyesha ufikirio wa pekee wale wanaostahili?
9 Je, kutokuwa na ubaguzi kunamaanisha kwamba hatuwezi kumwonyesha mtu fulani ufikirio wa pekee? Bila shaka hapana. Kuhusu mfanyakazi mwenzake Epafrodito, mtume Paulo aliwaandikia Wakristo wa Filipi hivi: “Mwendelee kuwaheshimu sana watu wa namna hiyo.” Kwa nini? “Kwa sababu alikaribia sana kufa kwa ajili ya kazi ya Bwana, akiihatarisha nafsi yake, ili ajazie kikamilifu kutokuwapo kwenu hapa ili kunitolea mimi utumishi wa kibinafsi.” (Wafilipi 2:25, 29, 30) Utumishi wa uaminifu uliofanywa na Epafrodito ulistahili kuthaminiwa. Zaidi ya hayo, kwenye andiko la 1 Timotheo 5:17, tunasoma hivi: “Wanaume wazee wanaosimamia kwa njia nzuri wahesabiwe kustahili heshima mara mbili, hasa wale wanaofanya kazi kwa bidii katika kusema na kufundisha.” Sifa nzuri za kiroho zinastahili pia kuthaminiwa. Kuonyesha ufikirio kama huo si kuonyesha upendeleo.
‘Hekima Inayotoka Juu Ni Yenye Kujaa Rehema’
10. Kwa nini tunapaswa kuuzuia ulimi wetu?
10 Kuhusu ulimi, Yakobo alisema hivi: “Huo ni kitu kitundu chenye kudhuru, umejaa sumu yenye kuua. Kwa huo sisi humbariki Yehova, naam, Baba, na bado kwa huo sisi huwalaani wanadamu ambao wamekuja kuwako ‘kwa mfano wa Mungu.’ Kubariki na kulaani hutoka katika kinywa kilekile.” Kuhusiana na hilo, Yakobo aliongeza hivi: “Ikiwa mna wivu mkali na ugomvi katika mioyo yenu, msiwe mkijigamba na kusema uwongo juu ya ile kweli. Hii siyo hekima inayoshuka kutoka juu, bali ni ya kidunia, ya kinyama, ya roho waovu. Kwa maana mahali ambapo pana wivu na ugomvi, hapo pana machafuko na kila jambo baya. Lakini hekima inayotoka juu kwanza kabisa ni safi kiadili, kisha yenye kufanya amani, yenye usawaziko, tayari kutii, yenye kujaa rehema na matunda mema, haifanyi tofauti zenye ubaguzi, si ya kinafiki.”—Yakobo 3:8-10a, 14-17.
11. Tunaweza kuwa wenye rehema jinsi gani katika kutumia ulimi wetu?
11 Hivyo, jinsi tunavyotumia ulimi wetu inaweza kuonyesha ikiwa tuna hekima yenye “kujaa rehema.” Namna gani ikiwa kwa sababu ya wivu au ugomvi tunajigamba, kusema uwongo, au kueneza porojo zenye kuumiza? Andiko la Zaburi 94:4 linasema: “Wote wanaofanya mambo yenye kuumiza wanaendelea kujivuna wenyewe.” Porojo zenye kuumiza zinaweza kuharibu haraka sifa nzuri ya mtu asiye na hatia! (Zaburi 64:2-4) Zaidi ya hayo, fikiria madhara ambayo “shahidi wa uwongo [ambaye] husema uwongo mtupu” anaweza kusababisha. (Methali 14:5; 1 Wafalme 21:7-13) Baada ya kuzungumza kuhusu kutumia vibaya ulimi, Yakobo anasema hivi: “Haifai, ndugu zangu, mambo haya kuendelea kutendeka kwa njia hiyo.” (Yakobo 3:10b) Tukiwa na rehema ya kweli tutatumia ulimi wetu kwa njia iliyo safi, yenye amani, na usawaziko. Yesu alisema: “Ninawaambia ninyi kwamba kila neno lisilofaa ambalo watu husema, watatoa hesabu juu yake katika Siku ya Hukumu.” (Mathayo 12:36) Ni jambo la maana kama nini kwamba tuwe wenye rehema katika kutumia ulimi wetu!
‘Mwasamehe Watu Makosa Yao’
12, 13. (a) Tunajifunza nini kuhusu rehema kutokana na mfano wa mtumwa aliyekuwa na deni kubwa la pesa la bwana wake? (b) Inamaanisha nini kumsamehe ndugu yetu “mpaka mara 77”?
12 Mfano wa Yesu wa mtumwa aliyedaiwa deni la dinari 60,000,000 na bwana wake, mfalme, unaonyesha njia nyingine ya kuwa wenye rehema. Kwa kuwa hakuwa na mali ya kulipa deni hilo, mtumwa huyo alisihi aonyeshwe rehema. “Akisikitishwa na hayo,” bwana wa mtumwa huyo alimsamehe deni lake. Lakini mtumwa huyo alitoka na kumkuta mtumwa mwenzake aliyekuwa na deni lake la dinari mia moja tu na bila rehema akamtupa gerezani. Mfalme aliposikia yale yaliyotukia, alimwita yule mtumwa aliyesamehewa na kumwambia: “Mtumwa mwovu, nilifuta lile deni lote kwa ajili yako, uliponisihi. Haikukupasa wewe, nawe, kuwa na rehema juu ya mtumwa mwenzako, kama mimi pia nilivyokuwa na rehema juu yako?” Kwa hiyo, bwana akaamuru mtumwa huyo apelekwe kwa walinzi wa jela. Yesu alimalizia mfano huo hivi: “Vivyo hivyo Baba yangu wa mbinguni atashughulika nanyi pia ikiwa kila mmoja wenu hatamsamehe ndugu yake kutoka moyoni mwake.”—Mathayo 18:23-35.
13 Mfano huo unaonyesha waziwazi kama nini kwamba rehema inatia ndani kuwa tayari kusamehe! Yehova ametusamehe deni kubwa la dhambi. Je, sisi pia hatupaswi ‘kuwasamehe watu makosa yao’? (Mathayo 6:14, 15) Kabla ya Yesu kusimulia mfano huo kuhusu mtumwa asiye na rehema, Petro alimuuliza hivi: “Bwana, ndugu yangu atanitendea dhambi mara ngapi nami nimsamehe? Mpaka mara 7?” Yesu akamjibu: “Ninakuambia, si, Mpaka mara 7, bali, Mpaka mara 77.” (Mathayo 18:21, 22) Ndiyo, mtu mwenye rehema yuko tayari kusamehe “mpaka mara 77,” yaani, kuendelea kusamehe.
14. Kulingana na Mathayo 7:1-4, tunaweza kutenda kwa rehema kila siku jinsi gani?
14 Akitaja njia nyingine ya kuonyesha rehema, Yesu alisema hivi katika Mahubiri yake ya Mlimani: “Acheni kuhukumu ili msihukumiwe; kwa maana kwa hukumu mnayohukumu, mtahukumiwa . . . Basi, kwa nini unautazama unyasi ulio katika jicho la ndugu yako, lakini hulifikirii boriti lililo katika jicho lako mwenyewe? Au unawezaje kumwambia ndugu yako, ‘Niruhusu niutoe unyasi ulio katika jicho lako’; wakati, tazama! boriti limo katika jicho lako mwenyewe?” (Mathayo 7:1-4) Kwa hiyo, kila siku tunaweza kutenda kwa rehema kwa kuvumilia kasoro za wengine bila kuwahukumu au kuwachambua-chambua sana.
“Tuwatendee Wote Mema”
15. Kwa nini hatupaswi kuwatendea kwa rehema waamini wenzetu tu?
15 Ingawa kitabu cha Biblia cha Yakobo kinakazia kuwatendea waamini wenzetu kwa rehema, hilo halimaanishi kwamba tunapaswa kuwatendea kwa rehema wale walio tu katika kutaniko la Kikristo. Andiko la Zaburi 145:9 linasema hivi: “Yehova ni mwema kwa wote, na rehema zake ziko juu ya kazi zake zote.” Tunahimizwa tuwe “waigaji wa Mungu” na “tuwatendee wote mema.” (Waefeso 5:1; Wagalatia 6:10) Ijapokuwa hatuupendi “ulimwengu au vitu vilivyo katika ulimwengu,” hatuyapuuzi mahitaji ya wale walio katika ulimwengu.—1 Yohana 2:15.
16. Ni mambo gani yanayopaswa kuamua jinsi tunavyoweza kuwaonyesha wengine rehema?
16 Tukiwa Wakristo, tuko tayari sikuzote kuwasaidia kwa njia yoyote tunayoweza wale wanaopatwa na “tukio lisilotazamiwa” au wale walio katika hali mbaya sana. (Mhubiri 9:11) Bila shaka, hali zetu zitaamua yale tunayoweza kufanya na kadiri tunavyoweza kufanya. (Methali 3:27) Tunapowasaidia wengine kimwili, tunapaswa kuwa waangalifu ili matendo yetu mazuri yasifanye wengine wawe wavivu. (Methali 20:1, 4; 2 Wathesalonike 3:10-12) Hivyo, mtu anayeonyesha rehema ya kweli anatenda kwa hisia nyororo za huruma na pia kupatana na akili.
17. Ni njia gani bora ya kuwaonyesha rehema wale walio nje ya kutaniko la Kikristo?
17 Njia bora ya kuwaonyesha rehema wale walio nje ya kutaniko la Kikristo ni kuwahubiria kweli za Biblia. Kwa nini? Kwa sababu wanadamu wengi leo wanapapasa-papasa katika giza la kiroho. Kwa kuwa hawajui jinsi ya kukabiliana na matatizo yao wala hawana tumaini lolote la wakati ujao, watu wengi “wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:36) Ujumbe wa Neno la Mungu unaweza kuwa ‘taa kwa mguu wao,’ na hivyo kuwasaidia kukabiliana na matatizo ya maisha. Pia, unaweza kuwa ‘nuru kwa barabara yao’ katika maana ya kwamba Biblia inatabiri kusudi la Mungu la wakati ujao, na hivyo kuwapa msingi wa kuwa na tumaini zuri. (Zaburi 119:105) Ni pendeleo kama nini kuwapelekea ujumbe mzuri ajabu wa kweli wale ambao wanauhitaji sana! Kwa kuwa “dhiki kuu” inakaribia sana, huu ndio wakati wa kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mathayo 24:3-8, 21, 22, 36-41; 28:19, 20) Hakuna tendo lingine la rehema lililo la maana kuliko hilo.
Toeni “Vitu Vilivyo Ndani”
18, 19. Kwa nini tunapaswa kuonyesha rehema zaidi katika maisha yetu?
18 Yesu alisema hivi: “Vitoeni viwe kama zawadi za rehema vitu vilivyo ndani.” (Luka 11:41) Ili tendo zuri la wema liwe tendo la rehema ya kweli, linapaswa kutoka ndani, yaani, katika moyo wenye upendo na ulio tayari kusaidia. (2 Wakorintho 9:7) Rehema kama hiyo inaburudisha kama nini katika ulimwengu huu wenye ukatili, uchoyo, ambamo watu wengi hawajali mateso na matatizo ya wengine!
19 Basi, acheni tujitahidi kuonyesha rehema zaidi katika maisha yetu. Kadiri tunavyokuwa wenye rehema, ndivyo tunavyomwiga Mungu. Hilo linatusaidia kuishi maisha yenye kusudi na yenye kuridhisha.—Mathayo 5:7.
-