-
Watumishi wa Yehova Wana Tumaini la KweliMnara wa Mlinzi—2003 | Agosti 15
-
-
Watumishi wa Yehova Wana Tumaini la Kweli
“Hayo mabaki ya Yakobo yatakuwa kati ya kabila nyingi mfano wa umande utokao kwa BWANA, . . . . yasiyomngojea mtu.”—MIKA 5:7.
1. Ni katika njia gani Israeli wa kiroho ni chanzo cha burudisho?
YEHOVA ndiye Mfanyizaji mkubwa wa mvua na umande. Ni kazi bure kuwatumaini wanadamu walete umande au mvua. Nabii Mika aliandika: “Na hayo mabaki ya Yakobo yatakuwa kati ya kabila nyingi mfano wa umande utokao kwa BWANA, mfano wa manyunyu katika manyasi; yasiyomngojea mtu, wala kuwakawilia wanadamu.” (Mika 5:7) Ni nani “mabaki ya Yakobo” leo? Hao ni Waisraeli wa kiroho, mabaki ya “Israeli wa Mungu.” (Wagalatia 6:16) Kwa “kabila nyingi” duniani, mabaki hao ni kama ‘umande wenye kuburudisha utokao kwa BWANA’ na “manyunyu katika manyasi.” Naam, leo Wakristo watiwa-mafuta ni zawadi ambayo Mungu amewapa watu. Wakiwa watangazaji wa Ufalme, wanatumiwa na Yehova kuwapa watu ujumbe wake wa tumaini la kweli.
2. Kwa nini tuna tumaini la kweli ingawa tunaishi katika ulimwengu huu wenye misukosuko?
2 Haishangazi kwamba ulimwengu huu hauna tumaini la kweli. Katika ulimwengu unaotawaliwa na Shetani Ibilisi, tunatazamia kuwepo na misukosuko ya kisiasa, kuzorota kwa maadili, uhalifu, matatizo ya kiuchumi, ugaidi, na vita. (1 Yohana 5:19) Watu wengi wana wasiwasi kuhusu wakati ujao. Hata hivyo, tukiwa waabudu wa Yehova hatuogopi kwa kuwa tuna tumaini hakika la wakati ujao. Tumaini hilo ni la kweli kwa kuwa linategemea Neno la Mungu. Tunamwamini Yehova na Neno lake kwa sababu mambo anayosema hutimia sikuzote.
3. (a) Kwa nini Yehova angeyachukulia hatua mataifa ya Israeli na Yuda? (b) Kwa nini maneno ya Mika yanaweza kutumika katika siku zetu pia?
3 Unabii wa Mika ulioongozwa na roho ya Mungu hututia nguvu kutembea katika jina la Yehova na hutupatia msingi wa kuwa na tumaini la kweli. Katika karne ya nane K.W.K., wakati Mika alipotabiri, watu waliokuwa wamefanya agano pamoja na Mungu walikuwa wamegawanyika na kuwa mataifa mawili, Israeli na Yuda. Mataifa hayo yalipuuza agano la Mungu na kwa sababu hiyo, maadili yakazorota, kukawa na uasi-imani, na kufuatia sana vitu vya kimwili. Kwa hiyo, Yehova akaonya kwamba angeyachukulia hatua. Bila shaka, maonyo ya Mungu yalielekezwa kwa watu wa siku za Mika. Lakini hali leo zinafanana sana na za siku za Mika hivi kwamba maneno yake yanaweza kutumika pia katika siku zetu. Tutaona jinsi maneno ya Mika yanavyotumika katika siku zetu tunapochunguza baadhi ya mambo makuu ya sura saba za kitabu chake.
Muhtasari Unaonyesha Nini?
4. Kitabu cha Mika sura ya 1 mpaka ya 3 kina habari gani?
4 Na tuchunguze kwa ufupi yaliyomo katika kitabu cha Mika. Katika sura ya 1, Yehova anafunua uasi wa Israeli na Yuda. Kwa sababu ya makosa yao, Israeli litaharibiwa nayo adhabu ya Yuda itafika kwenye malango ya Yerusalemu. Sura ya 2 inafunua kwamba matajiri na watu wenye mamlaka wanawaonea wanyonge na walio dhaifu. Lakini kuna ahadi pia kutoka kwa Mungu. Watu wa Mungu watakusanywa na kuwekwa pamoja. Sura ya 3 inatoa matamko ya Yehova dhidi ya viongozi wa taifa na manabii wakosaji. Viongozi wanapotosha haki, nao manabii wanasema uwongo. Licha ya hayo, Mika anatiwa nguvu na roho takatifu ili atangaze hukumu ya Yehova inayokuja.
5. Kuna jambo gani kuu katika Mika sura ya 4 na ya 5?
5 Sura ya 4 inatabiri kwamba katika siku za mwisho, mataifa yote yatauendea mlima ulioinuliwa wa nyumba ya Yehova ili yafundishwe naye. Kabla ya hayo, Yuda litapelekwa uhamishoni Babiloni, lakini Yehova atalikomboa. Sura ya 5 inafunua kwamba Mesiya atazaliwa Bethlehemu ya Yuda. Atawachunga watu wake na kuwakomboa kutoka kwa mataifa yenye uonevu.
6, 7. Ni mambo gani yanayozungumziwa katika sura ya 6 na ya 7 ya unabii wa Mika?
6 Sura ya 6 ya Mika inasimulia mashtaka ya Yehova dhidi ya watu wake sawa na vile kesi inavyoendeshwa mahakamani. Ametenda nini ili kuwafanya waasi? Hakuna. Ukweli ni kwamba, matakwa yake hayapiti kiasi hata kidogo. Anataka waabudu wake watende haki na wawe na rehema na kiasi wanapotembea naye. Badala ya kufanya hivyo, Israeli na Yuda wameasi na lazima wapatwe na matokeo mabaya ya uasi wao.
7 Katika sura ya mwisho ya unabii wake, Mika anashutumu uovu wa watu wa siku zake. Hata hivyo, havunjiki moyo kwa kuwa ameazimia ‘kuonyesha mtazamo wa kumngojea’ Yehova. (Mika 7:7, NW) Kitabu hicho kinamalizia kwa maneno ya uhakika kwamba Yehova atawahurumia watu wake. Historia inathibitisha kwamba tumaini hilo lilitimizwa. Kwa rehema, baada ya kuwapa watu wake nidhamu, Yehova aliwarudisha mabaki fulani katika nchi yao mwaka wa 537 K.W.K.
8. Unaweza kuelezaje kwa ufupi yaliyomo katika kitabu cha Mika?
8 Yehova anafunua habari nzuri kama nini kupitia Mika! Kitabu hiki kilichoongozwa na roho ya Mungu kina mifano yenye kuonya kuhusu jinsi Mungu anavyoshughulika na watu wasio waaminifu wanaodai kumtumikia. Kinatabiri mambo yanayotukia leo. Pia kinatoa shauri la Mungu kuhusu jinsi tunavyopaswa kujiendesha wakati huu wa magumu ili kuliimarisha tumaini letu.
Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova Asema
9. Kulingana na Mika 1:2, Yehova angefanya nini?
9 Sasa na tuchunguze kitabu cha Mika kwa undani zaidi. Katika Mika 1:2 tunasoma: “Sikilizeni, enyi watu wa kabila zote; sikiliza, Ee dunia, na vyote vilivyomo; Bwana MUNGU [“Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova,” NW] na ashuhudie juu yenu, yeye Bwana kutoka hekalu lake takatifu.” Bila shaka maneno hayo yangalivuta fikira zako kama ungaliishi siku za Mika. Naam, yanavuta fikira zako kwa sababu Yehova anazungumza kutoka hekalu lake takatifu naye hazungumzi tu na Israeli na Yuda bali na watu kila mahali. Katika siku za Mika, watu walikuwa wamempuuza Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova, kwa muda mrefu sana. Muda si muda, mambo yangebadilika. Yehova alikuwa ameamua kuchukua hatua ya kukata maneno.
10. Kwa nini maneno ya Mika 1:2 ni muhimu kwetu?
10 Ndivyo ilivyo leo. Andiko la Ufunuo 14:18-20 linaonyesha kwamba Yehova anazungumza tena kutoka katika hekalu lake takatifu. Hivi karibuni, atachukua hatua ya kukata maneno, nao wanadamu watatikiswa tena na matukio muhimu. Wakati huu, ‘mzabibu mwovu wa dunia’ utatupwa ndani ya sindikio kubwa la divai la hasira ya Yehova, na hivyo kuharibu kabisa mfumo wa mambo wa Shetani.
11. Maneno ya Mika 1:3, 4 yanamaanisha nini?
11 Sikiliza mambo ambayo Yehova atafanya. Andiko la Mika 1:3, 4 linasema: “Angalieni, BWANA anakuja akitoka mahali pake, naye atashuka, na kupakanyaga mahali pa dunia palipoinuka. Na hiyo milima itayeyuka chini yake, nayo mabonde yatapasuliwa, kama vile nta iliyo mbele ya moto, kama maji yaliyomwagika tena kutelemka gengeni.” Je, Yehova ataacha makao yake ya mbinguni na kukanyaga kihalisi milima na mabonde ya Nchi ya Ahadi? La, si lazima. Atahitaji tu kuelekeza fikira zake duniani ili mapenzi yake yatimizwe. Isitoshe, si dunia halisi itakayopatwa na mambo yanayotajwa, bali ni wakaaji wake. Yehova atakapochukua hatua, watu wasio waaminifu watapatwa na matokeo mabaya—kana kwamba milima imeyeyuka kama nta nayo mabonde yamepasuliwa na tetemeko la ardhi.
12, 13. Kulingana na 2 Petro 3:10-12, ni nini hufanya tumaini letu liwe hakika?
12 Huenda maneno ya unabii wa Mika 1:3, 4 yakakukumbusha unabii mwingine ulioongozwa na roho ya Mungu unaotabiri matukio mabaya duniani. Mtume Petro aliandika hivi katika 2 Petro 3:10: “Siku ya Yehova itakuja kama mwizi, ambayo katika hiyo mbingu zitapitilia mbali kwa kelele ya kuchatachata, lakini elementi zikiwa moto sana zitafumuliwa, na dunia na kazi zilizo ndani yayo zitagunduliwa.” Sawa na unabii wa Mika, maneno ya Petro hayahusu mbingu na dunia halisi. Yanahusu dhiki kubwa itakayoupata ulimwengu huu usiomhofu Mungu.
13 Ingawa msiba huo unakuja, Wakristo wanaweza kutazamia wakati ujao wakiwa na uhakika kama Mika. Jinsi gani? Kwa kutii shauri linalopatikana katika mistari inayofuata ya barua ya Petro. Mtume huyo anasema: “Mwapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu, mkingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova!” (2 Petro 3:11, 12) Tutakuwa na tumaini hakika la wakati ujao ikiwa tutasitawisha moyo mtiifu na kuhakikisha kwamba mwenendo wetu ni mtakatifu na maisha yetu yamejawa na vitendo vya ujitoaji-kimungu. Ili kufanya tumaini letu liwe hakika, tunapaswa pia kukumbuka kwamba siku ya Yehova itakuja hakika.
14. Kwa nini Israeli na Yuda walistahili adhabu?
14 Yehova anaeleza kwa nini watu wake wa kale wanastahili kuadhibiwa. Andiko la Mika 1:5 linasema: “Kwa sababu ya kosa la Yakobo yametokea haya yote, na kwa sababu ya makosa ya nyumba ya Israeli. Nini kosa la Yakobo? Je, silo Samaria? Na nini mahali pa Yuda palipoinuka? Sipo Yerusalemu?” Israeli na Yuda yapo kwa sababu ya Yehova. Hata hivyo, mataifa hayo yamemwasi Yehova, na uasi wao umefika hata kwenye miji yao mikuu, Samaria na Yerusalemu.
Maovu Yaongezeka
15, 16. Watu wa siku za Mika walikuwa na hatia ya vitendo gani viovu?
15 Mfano wa uovu uliotendwa na watu wa siku za Mika unaelezwa waziwazi katika Mika 2:1, 2: “Ole wao wakusudiao mambo maovu, na kutenda mabaya vitandani mwao! Kunapopambazuka asubuhi huyafanya, kwa sababu ya katika uwezo wa mikono yao. Nao hutamani mashamba, na kuyashika; na nyumba pia, nao huzichukua; nao humwonea mtu na nyumba yake, naam; mtu na urithi wake.”
16 Watu wenye pupa hukesha usiku wakifanya njama za kuwanyang’anya majirani wao mashamba na nyumba. Asubuhi wanaharakisha kutekeleza njama zao. Hawangetenda maovu hayo kama wangekumbuka agano la Yehova. Sheria ya Musa ina maandalizi ya kuwalinda maskini. Chini ya Sheria hiyo, hakuna familia inayopaswa kupoteza kabisa urithi wake. Hata hivyo, watu hao wenye pupa hawajali. Wanapuuza andiko la Mambo ya Walawi 19:18, linalosema: “Umpende jirani yako kama nafsi yako.”
17. Ni nini kinachoweza kutukia wakati wale wanaodai kumtumikia Mungu wanapotanguliza vitu vya kimwili maishani?
17 Hilo linaonyesha jambo linaloweza kutokea wakati watu wanaodai kumtumikia Mungu wanapopuuza miradi ya kiroho na kutanguliza vitu vya kimwili. Paulo aliwaonya Wakristo wa siku zake hivi: “Wale waazimiao kuwa matajiri huanguka ndani ya kishawishi na mtego na tamaa nyingi zisizo za akili na zenye kuumiza, ambazo hutumbukiza watu ndani ya uharibifu na uangamizo.” (1 Timotheo 6:9) Mtu anapofanya utafutaji wa pesa kuwa mradi mkuu maishani, kwa kweli anakuwa mwabudu wa mungu wa uwongo—Utajiri. Mungu huyo hatoi tumaini lolote hakika la wakati ujao.—Mathayo 6:24.
18. Watu waliofuatia vitu vya kimwili katika siku za Mika wangepatwa na nini?
18 Wengi katika siku za Mika wanajifunza kupitia magumu kwamba ni ubatili kutegemea vitu vya kimwili. Kulingana na Mika 2:4, Yehova anasema: “Siku hiyo watatunga mithali juu yenu, na kuomboleza kwa maombolezo ya huzuni nyingi, na kusema, Sisi tumeangamizwa kabisa; yeye analibadili fungu la watu wangu; jinsi anavyoniondolea hilo! Awagawia waasi mashamba yetu.” Naam, wezi hao wa nyumba na mashamba watapoteza urithi wao wa familia. Watahamishwa mpaka nchi ya kigeni, nayo mali yao itaporwa na “waasi,” yaani, watu wa mataifa. Hawatakuwa na tumaini lolote la wakati ujao wenye ufanisi.
19, 20. Nini kilichotukia kwa Wayahudi waliomtumaini Yehova?
19 Hata hivyo, wale wanaomtumaini Yehova hawatakatishwa tamaa. Yehova ni mwaminifu kwa maagano yake pamoja na Abrahamu na Daudi, naye huwahurumia watu ambao, kama Mika, wanampenda na kuhuzunikia raia wenzao waliotengwa na Mungu. Kwa ajili ya wanyoofu, kutakuwa na urudisho katika wakati wa Mungu unaofaa.
20 Jambo hilo linatukia mwaka wa 537 K.W.K, wakati mabaki ya Wayahudi wanaporudishwa katika nchi yao baada ya Babiloni kuanguka. Wakati huo maneno ya Mika 2:12 yanapata utimizo wa kwanza. Yehova anasema: “Hakika nitakukusanya, Ee Yakobo, nyote pia; bila shaka nitawakusanya waliobaki wa Israeli; nitawaweka pamoja kama kondoo wa Bozra; kama kundi la kondoo kati ya malisho yao; watafanya mvumo kwa wingi wa watu.” Yehova ana upendo ulioje! Baada ya kuwaadhibu watu wake, anaruhusu mabaki warudi na kumtumikia katika nchi aliyowapa babu zao.
Hali Leo Zinafanana Sana na za Siku za Mika
21. Hali leo zinafananaje na za siku za Mika?
21 Baada ya kuchunguza sura mbili za kwanza za Mika, je, umevutiwa kuona jinsi hali zinavyofanana na za leo? Kama ilivyokuwa katika siku za Mika, wengi leo wanadai kwamba wanamtumikia Mungu. Hata hivyo, kama vile Yuda na Israeli, watu hao wamegawanyika na hata wamepigana. Wengi walio matajiri kati ya wale wanaojidai kuwa Wakristo wamewaonea maskini. Viongozi wa kidini wanazidi kuachilia mazoea yanayoshutumiwa waziwazi katika Biblia. Haishangazi kwamba hivi karibuni dini zinazodai kuwa za Kikristo zitaharibiwa, pamoja na dini nyingine ambazo ni sehemu ya “Babiloni Mkubwa,” yaani, milki ya ulimwengu ya dini za uwongo! (Ufunuo 18:1-5) Lakini, kulingana na ilivyokuwa katika siku za Mika, Yehova atakuwa na watumishi waaminifu ambao watabaki duniani.
22. Ni vikundi gani viwili ambavyo vimeweka tumaini lao katika Ufalme wa Mungu?
22 Katika mwaka wa 1919, Wakristo watiwa-mafuta walio waaminifu walijitenga kabisa na dini zinazodai kuwa za Kikristo nao wakaanza kutangaza habari njema ya Ufalme kwa mataifa yote. (Mathayo 24:14) Kwanza walitafuta waliobaki kati ya Israeli wa kiroho. Kisha wakaanza kukusanya “kondoo wengine,” na vikundi hivyo viwili vikawa “kundi moja, mchungaji mmoja.” (Yohana 10:16) Ingawa sasa wanamtumikia Mungu katika nchi 234, kwa kweli waabudu hao wote waaminifu ‘wamewekwa pamoja.’ Kufikia sasa, kundi la kondoo ‘linavuma kwa wingi wa watu,’ kutia ndani wanawake na watoto. Hawaweki tumaini lao katika mfumo huu wa mambo, bali katika Ufalme wa Mungu, ambao hivi karibuni utaleta paradiso duniani.
23. Kwa nini unaamini kwamba tumaini lako ni hakika?
23 Kuhusu waabudu waaminifu wa Yehova, mstari wa mwisho wa Mika sura ya 2 unasema: “Mfalme wao naye amepita akiwatangulia, naye BWANA ametangulia mbele yao.” Je, utakuwa katika msafara huo wa ushindi, ukimfuata Mfalme wako, Yesu Kristo, Yehova mwenyewe akiwa kiongozi? Ikiwa ndivyo, ujue kwa hakika kwamba utapata ushindi na kwamba tumaini lako ni hakika. Jambo hilo litakuwa wazi hata zaidi tunapochunguza mambo mengine makuu ya unabii wa Mika.
-
-
Tutatembea Katika Jina la Yehova Milele!Mnara wa Mlinzi—2003 | Agosti 15
-
-
Tutatembea Katika Jina la Yehova Milele!
“Sisi . . . tutakwenda kwa jina la BWANA [“tutatembea katika jina la Yehova,” “NW”] Mungu wetu, milele na milele.”—MIKA 4:5.
1. Ni ujumbe gani unaopatikana katika Mika sura ya 3 mpaka ya 5?
YEHOVA ana habari fulani anayotaka kuwaambia watu wake, naye anamtumia Mika kama nabii wake. Mungu anakusudia kuwachukulia hatua wakosaji. Ataadhibu Israeli kwa sababu ya kuasi imani. Hata hivyo, inafurahisha kwamba Yehova atawabariki wale wanaotembea katika jina lake. Ujumbe huo unaelezwa waziwazi katika sura ya 3 mpaka ya 5 ya unabii wa Mika.
2, 3. (a) Viongozi wa Israeli wanapaswa kuonyesha sifa gani, lakini wanafanya nini hasa? (b) Unaweza kuelezaje usemi wa mfano unaotumiwa katika Mika 3:2, 3?
2 Nabii wa Mungu anatangaza hivi: “Tafadhali sikieni, enyi vichwa vya Yakobo, mnaoitawala nyumba ya Israeli. Je! haiwapasi ninyi kujua hukumu [“haki,” NW]?” Naam, wanapaswa kufanya hivyo, lakini wanafanya nini hasa? Mika anasema: “Ninyi mnaoyachukia mema, na kuyapenda mabaya; ninyi mnaowachuna watu ngozi yao, na nyama mifupani mwao. Naam, mnakula nyama ya watu wangu, na kuwachuna ngozi zao, na kuivunja mifupa yao; naam, kuwakata vipande vipande kama kwa kutiwa chunguni, na kama nyama sufuriani.”—Mika 3:1-3.
3 Viongozi hao wanawaonea maskini na walio dhaifu! Watu wanaomsikia Mika wanauelewa kwa urahisi usemi wa mfano unaotumiwa hapa. Ikiwa kondoo aliyechinjwa atachemshwa, kwanza huchunwa ngozi kisha hukatwakatwa. Nyakati nyingine mifupa huvunjwa ili uboho utoke. Kisha nyama na mifupa huchemshwa katika chombo kikubwa, kama kile kinachotajwa na Mika. (Ezekieli 24:3-5, 10) Huo ni mfano unaowafaa kama nini viongozi waovu wanaowatendea kikatili watu wa siku za Mika!
Yehova Anataka Tuwe Wenye Haki
4. Ni tofauti gani iliyopo kati ya Yehova na viongozi wa Israeli?
4 Kuna tofauti kubwa sana kati ya Yehova, Mchungaji mwenye upendo, na viongozi wa Israeli. Wanashindwa kutimiza wajibu wao wa kulinda kundi kwa sababu hawatendi haki. Badala yake, wanawatumia kondoo hao wa mfano kwa faida yao, wakiwanyima haki na kuwatesa kwa “matendo ya umwagaji damu,” kama inavyotajwa katika Mika 3:10, NW. Tunaweza kujifunza nini kutokana na hali hiyo?
5. Yehova anataka wale wanaoongoza kati ya watu wake wafanye nini?
5 Mungu anataka wale wanaoongoza kati ya watu wake watende haki. Tunaona jambo hilo kati ya watumishi wa Yehova leo. Isitoshe, hilo linapatana na Isaya 32:1, Biblia Habari Njema, ambapo tunasoma hivi: “Kutatokea mfalme atakayetawala kwa uadilifu, nao viongozi wataongoza kwa kufuata haki.” Lakini tunaona nini katika siku za Mika? ‘Wanaochukia mema na kuyapenda mabaya’ wanaendelea kupotosha haki.
Ni Sala za Nani Zinazojibiwa?
6, 7. Ni jambo gani muhimu linalokaziwa katika Mika 3:4?
6 Je, watu wa siku za Mika wanaweza kutazamia kupata kibali cha Yehova? La, hasha! Andiko la Mika 3:4 linasema: ‘Watamwomba BWANA, asiwaitikie. Naam, atawaficha uso wake wakati huo, kwa kadiri walivyotenda mabaya kwa matendo yao.’ Andiko hilo linakazia jambo muhimu sana.
7 Yehova hatajibu sala zetu ikiwa tunazoea kutenda dhambi. Itakuwa hivyo ikiwa tunaishi maisha maradufu, huku tukificha makosa yetu na kujifanya kwamba tunamtumikia Mungu kwa uaminifu. Kulingana na Zaburi 26:4, Daudi aliimba: “Sikuketi pamoja na watu wa ubatili, wala sitaingia mnamo wanafiki.” Bila shaka, Yehova hatajibu sala za wale wanaotenda kinyume cha Neno lake kimakusudi!
Kutiwa Nguvu kwa Roho ya Mungu
8. Manabii wa uwongo wa siku za Mika walionywa kuhusu nini?
8 Mazoea mabaya yamekuwa jambo la kawaida miongoni mwa viongozi wa kiroho wa Israeli. Manabii wa uwongo wanawapotosha kiroho watu wa Mungu. Viongozi wenye pupa wanapaaza sauti, “Amani” lakini huandaa vita dhidi ya mtu awaye yote asiyetia kitu vinywani mwao. “Kwa hiyo,” Yehova anasema, “itakuwa usiku kwenu, msipate kuona maono; tena itakuwa giza kwenu, msiweze kubashiri; nalo jua litawachwea manabii, nao mchana utakuwa mweusi juu yao. Na hao waonaji watatahayarika, na wenye kubashiri watafadhaika; naam, hao wote watajifunika midomo yao.”—Mika 3:5-7a.
9, 10. ‘Kujifunika midomo’ kunamaanisha nini, na kwa nini Mika hana sababu ya kufanya hivyo?
9 Kwa nini ‘wajifunike midomo’? Watu wanaoishi siku za Mika wanafanya hivyo kwa sababu ya aibu. Watu hao waovu wanapaswa kuona aibu ‘kwa kuwa Mungu hatawajibu.’ (Mika 3:7b, NW) Yehova hasikilizi sala za waovu wenye kiburi.
10 Mika hahitaji ‘kujifunika midomo.’ Haoni aibu. Yehova anajibu sala zake. Ona Mika 3:8, ambapo nabii huyo mwaminifu anasema: “Bali mimi, hakika nimejaa nguvu kwa roho ya BWANA; nimejaa hukumu [“haki,” NW] na uwezo.” Mika anashukuru kama nini kwamba katika muda mrefu ambao amefanya huduma yake kwa uaminifu, sikuzote ‘amejaa nguvu, kwa roho ya Yehova’! Jambo hilo limempa nguvu ya ‘kumhubiri Yakobo kosa lake, na Israeli dhambi yake.’
11. Wanadamu wanatiwaje nguvu kutangaza ujumbe wa Mungu?
11 Mika anahitaji nguvu zinazozidi zile za kibinadamu ili kutangaza ujumbe wa hukumu kali ya Mungu. Roho ya Yehova, au nguvu yake ya utendaji, ni muhimu. Namna gani sisi? Tunaweza kutimiza kazi yetu ya kuhubiri ikiwa tu Yehova anatutia nguvu kwa roho yake takatifu. Ikiwa tunazoea kutenda dhambi kimakusudi hatutafanikiwa katika jitihada zetu za kuhubiri. Kwa hiyo Mungu hawezi kujibu sala zetu za kumwomba atutie nguvu ya kufanya kazi yake. Bila shaka hatuwezi kutangaza ujumbe wa hukumu wa Baba yetu wa mbinguni tusipokuwa na ‘roho ya Yehova.’ Kupitia sala zinazosikiwa na kwa msaada wa roho takatifu, tunaweza kusema neno la Mungu kwa ujasiri kama Mika.
12. Kwa nini wanafunzi wa mapema wa Yesu waliweza ‘kufuliza kusema neno la Mungu kwa ujasiri wote’?
12 Labda unakumbuka masimulizi katika Matendo 4:23-31. Wazia kwamba wewe ni mmoja wa wanafunzi wa Yesu wa karne ya kwanza. Wanyanyasi wenye msimamo mkali wamekuwa wakijaribu kuwanyamazisha wafuasi wa Kristo. Lakini waaminifu hao wanamsihi hivi Bwana Mwenye Enzi Kuu: “Yehova, yaangalie matisho yao, na kuwaruhusu watumwa wako kufuliza kusema neno lako kwa ujasiri wote.” Inakuwaje? Wanapoomba dua, mahali ambapo wamekusanyika pamoja panatikiswa, nao wote wanajazwa roho takatifu na kusema neno la Mungu kwa ujasiri. Na tumwendee Yehova katika sala na kutegemea msaada wake kupitia roho takatifu tunapotimiza huduma yetu.
13. Ni nini kitakachopata Yerusalemu na Samaria, na kwa nini?
13 Fikiria tena siku za Mika. Kulingana na Mika 3:9-12, viongozi wenye hatia ya damu wanahukumu ili wapate rushwa, makuhani wanafundisha ili wapate ijara, nao manabii wa uwongo wanabashiri ili wapate pesa. Basi haishangazi kwamba Mungu ameagiza mji mkuu wa Yuda, Yerusalemu, ‘uwe magofu’! Kwa kuwa ibada isiyo ya kweli na upotovu wa maadili umeenea sana Israeli, Mika anaongozwa na roho ya Mungu kutoa onyo kwamba Mungu atafanya Samaria kuwa “magofu.” (Mika 1:6, BHN) Kwa hakika, Mika anauona uharibifu wa Samaria uliotabiriwa ambao unatekelezwa na majeshi ya Ashuru katika mwaka wa 740 K.W.K. (2 Wafalme 17:5, 6; 25:1-21) Ni wazi kwamba ujumbe huo mzito juu ya Yerusalemu na Samaria ungeweza kutolewa kwa nguvu za Yehova tu.
14. Unabii wa Mika 3:12 ulitimizwaje, nao unapaswa kutufanya tuwe na maoni gani?
14 Bila shaka, Yuda haliwezi kuepuka hukumu kali ya Yehova. Ili kutimiza unabii wa Mika 3:12, Sayuni “utalimwa kama shamba lilimwavyo.” Kulingana na maoni yetu ya sasa, tunajua kwamba mambo hayo yalitukia Wababiloni walipoharibu Yuda na Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. Uharibifu huo ulitukia miaka mingi baada ya unabii wa Mika, lakini alikuwa na uhakika kwamba ungetukia. Tunapaswa kuwa na uhakika uo huo kwamba mfumo huu mwovu wa mambo utakoma katika “siku ya Yehova” iliyotabiriwa.—2 Petro 3:11, 12.
Yehova Anyoosha Mambo
15. Unaweza kuelezaje kwa maneno yako mwenyewe unabii wa Mika 4:1-4?
15 Tunapofikiria unabii huo, tunaona kwamba sasa Mika anatoa ujumbe wa tumaini wenye kusisimua. Tunapata maneno yenye kutia moyo kama nini katika Mika 4:1-4! Mika anasema: “Itakuwa katika siku za mwisho ya kwamba mlima wa nyumba ya BWANA utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na watu wa mataifa watauendea makundi makundi. . . . Naye atafanya hukumu kati ya watu wa kabila nyingi, naye atawakemea [‘atayanyoosha mambo kuhusu,’ NW] mataifa wenye nguvu walio mbali; nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe. Bali wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu; kwa kuwa kinywa cha BWANA wa majeshi kimesema hivi.”
16, 17. Andiko la Mika 4:1-4 linatimizwaje leo?
16 Ni nani hao “watu wa mataifa” na “mataifa wenye nguvu” wanaotajwa hapo? Hao si mataifa na serikali za ulimwengu huu. Badala yake, unabii huo unahusu watu mmoja-mmoja kutoka katika mataifa yote ambao wamejiunga na utumishi mtakatifu kwenye mlima wa Yehova wa ibada ya kweli.
17 Kupatana na unabii wa Mika, hivi karibuni watu wote duniani watafuata kikamili ibada safi ya Yehova. Leo, watu ‘walio na mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele’ wanafundishwa njia za Yehova. (Matendo 13:48) Yehova anafanya hukumu na kunyoosha mambo kiroho kwa waamini wanaounga mkono Ufalme. Wataokoka “dhiki kubwa” wakiwa sehemu ya “umati mkubwa.” (Ufunuo 7:9, 14) Kwa kuwa wamefua panga zao kuwa majembe, hata leo watu hao wanaishi kwa amani pamoja na Mashahidi wenzao na watu wengine. Inafurahisha kama nini kuwa kati yao!
Kuazimia Kutembea Katika Jina la Yehova
18. ‘Kuketi chini ya mzabibu na mtini wako’ humaanisha nini?
18 Tunasisimuka kuona wengi wakijifunza njia za Yehova wakati huu ambapo watu duniani pote wanaogopa sana. Tunatamani sana wakati ambapo hivi karibuni watu wote wanaompenda Mungu hawatajifunza vita tena bali wataketi chini ya mzabibu na mtini wao. Mara nyingi mitini hupandwa katika mashamba ya mizabibu. (Luka 13:6) Kuketi chini ya mzabibu na mtini wako humaanisha kuwa na amani, ufanisi, na usalama. Hata sasa, uhusiano wetu pamoja na Yehova hutupatia amani ya akili na usalama wa kiroho. Hali hizo zitakapokuwako chini ya utawala wa Ufalme, hatutaogopa chochote, tutakuwa salama salimini.
19. Inamaanisha nini kutembea katika jina la Yehova?
19 Ni lazima tutembee katika jina la Yehova ili kupata kibali na baraka zake. Jambo hilo linaonyeshwa kwa uzito katika Mika 4:5, ambapo nabii huyo anasema: “Maana mataifa yote watakwenda, kila moja kwa jina la mungu wake, na sisi tutakwenda kwa jina la BWANA [“tutatembea katika jina la Yehova,” NW] Mungu wetu, milele na milele.” Kutembea katika jina la Yehova hakumaanishi kusema tu kwamba yeye ni Mungu wetu. Tunapaswa kufanya zaidi ya kushiriki kwenye mikutano ya Kikristo na kazi ya kuhubiri Ufalme, ingawa mambo hayo ni muhimu pia. Ikiwa tunatembea katika jina la Yehova, tunajiweka wakfu kwake na tunajitahidi kumtumikia kwa uaminifu kwa sababu tunampenda kwa moyo wote. (Mathayo 22:37) Na tukiwa waabudu wake, sisi kwa hakika tumeazimia kutembea katika jina la Yehova Mungu wetu milele na milele.
20. Ni nini kilichotabiriwa katika Mika 4:6-13?
20 Sasa tafadhali chunguza maneno ya unabii wa Mika 4:6-13. “Binti Sayuni” lazima aende uhamishoni ‘na kufika hata Babeli.’ Ndivyo ilivyotukia kwa wakaaji wa Yerusalemu katika karne ya saba K.W.K. Hata hivyo, unabii wa Mika unaonyesha kwamba kuna mabaki watakaorudi Yuda, na baada ya Sayuni kurudishwa Yehova atahakikisha kwamba maadui wake wamepondwa-pondwa.
21, 22. Andiko la Mika 5:2 lilitimizwaje?
21 Matukio mengine yenye kutokeza yanatabiriwa katika Mika sura ya 5. Kwa mfano, ona yanayosemwa katika Mika 5:2-4. Mika anatabiri kwamba Mtawala aliyewekwa na Mungu—ambaye “matokeo [“asili,” NW] yake yamekuwa tangu zamani za kale” —atatoka Bethlehemu. Atatawala akiwa mchungaji ‘kwa nguvu za Yehova.’ Isitoshe, Mtawala huyo atakuwa mkuu, si katika Israeli tu, bali “hata miisho ya dunia.” Huenda ulimwengu kwa ujumla ukatatanika kujua mtawala huyo ni nani, lakini sisi tunamfahamu.
22 Ni nani aliye mtu mkuu zaidi aliyepata kuzaliwa Bethlehemu? Na ni nani ‘atakayekuwa mkuu hata miisho ya dunia’? Si mwingine ila Mesiya, Yesu Kristo! Herode Mkuu alipowauliza makuhani wakuu na waandishi mahali ambapo Mesiya angezaliwa, walimjibu hivi: “Bethlehemu ya Yudea.” Hata walinukuu maneno ya Mika 5:2. (Mathayo 2:3-6) Baadhi ya watu wa kawaida walifahamu jambo hilo pia, kwa kuwa andiko la Yohana 7:42 linawanukuu wakisema: “Je, Andiko halijasema kwamba Kristo anakuja kutokana na uzao wa Daudi, na kutoka Bethlehemu kijiji ambako Daudi alikuwa kwa kawaida?”
Burudisho la Kweli kwa Watu
23. Ni mambo gani yanayotukia ambayo yanatimiza Mika 5:7?
23 Andiko la Mika 5:5-15 linataja uvamizi wa Ashuru ambao ungefanikiwa kwa muda mfupi tu, nalo linaonyesha kwamba Mungu atalipiza kisasi dhidi ya mataifa yasiyotii. Andiko la Mika 5:7 linaahidi kwamba mabaki ya Wayahudi waliotubu watarudishwa katika nchi yao, lakini maneno hayo yanaweza kutumika katika siku zetu pia. Mika anasema: “Mabaki ya Yakobo yatakuwa kati ya kabila nyingi mfano wa umande utokao kwa BWANA, mfano wa manyunyu katika manyasi.” Mfano huo wenye kuvutia unatumiwa kutabiri kwamba mabaki ya kiroho ya Yakobo, au Israeli, yatakuwa zawadi ambayo Mungu atawapa watu. “Kondoo wengine” wa Yesu, ambao wana tumaini la kuishi duniani, wanafurahia kutumikia bega kwa bega na mabaki ya leo ya “Israeli wa Mungu,” wakisaidia kuwaburudisha wengine kiroho. (Yohana 10:16; Wagalatia 6:16; Sefania 3:9) Kuhusu habari hiyo, kuna jambo muhimu tunalopaswa kulifikiria. Tukiwa watangazaji wa Ufalme, sote tunapaswa kuthamini pendeleo letu la kuwapa wengine burudisho la kweli.
24. Ni mambo gani yaliyokuvutia katika Mika sura ya 3 mpaka ya 5?
24 Umejifunza nini katika sura ya 3 mpaka ya 5 ya unabii wa Mika? Labda umejifunza mambo kama haya: (1) Mungu anataka wale wanaoongoza kati ya watu wake watende haki. (2) Yehova hatajibu sala zetu ikiwa tunazoea kutenda dhambi kimakusudi. (3) Tunaweza tu kutimiza kazi yetu ya kuhubiri ikiwa Mungu atatutia nguvu kwa roho yake takatifu. (4) Ili kupata kibali cha Yehova, lazima tutembee katika jina lake. (5) Tukiwa watangazaji wa Ufalme, tunapaswa kuthamini pendeleo letu la kuwapa watu burudisho la kweli. Huenda kuna mambo mengine yaliyokuvutia. Ni mambo gani mengine tunayoweza kujifunza katika kitabu hiki cha Biblia cha unabii? Makala inayofuata itatusaidia kujifunza mambo yanayofaa katika sura mbili za mwisho za unabii wa Mika wenye kutia imani nguvu.
-
-
Yehova Anataka Nini Kwetu?Mnara wa Mlinzi—2003 | Agosti 15
-
-
Yehova Anataka Nini Kwetu?
“BWANA anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda [“kutembea,” “NW”] kwa unyenyekevu na Mungu wako?”—MIKA 6:8.
1, 2. Kwa nini huenda watumishi fulani wa Yehova wakavunjika moyo, lakini ni nini kinachoweza kuwasaidia?
VERA ni Mkristo mwaminifu mwenye umri wa miaka 75 hivi na mwenye afya mbaya. Yeye anasema, “wakati mwingine mimi huangalia nje dirishani na kuona ndugu na dada zangu Wakristo wakihubiri nyumba kwa nyumba. Ninatokwa na machozi kwa sababu ninataka kuwa pamoja nao, lakini ugonjwa hupunguza utumishi wangu kwa Yehova.”
2 Je, umewahi kuhisi hivyo? Bila shaka wote wanaompenda Yehova wanataka kutembea katika jina lake na kutimiza viwango vyake. Lakini namna gani ikiwa afya yetu inazidi kuwa mbaya, tumezeeka, au tuna madaraka ya familia? Huenda tukavunjika moyo kwa kadiri fulani kwa kuwa hali hizo zinaweza kutuzuia kufanya yote ambayo tungetaka kufanya katika utumishi wa Mungu. Ikiwa tunakabili hali kama hiyo, yaelekea tutatiwa moyo sana kwa kuchunguza Mika sura ya 6 na ya 7. Sura hizo zinaonyesha kwamba matakwa ya Yehova hayapiti kiasi hata kidogo na kwamba yanaweza kutimizwa.
Jinsi Mungu Anavyowatendea Watu Wake
3. Yehova anawatendeaje Waisraeli waasi?
3 Kwanza, na tuchunguze Mika 6:3-5 na tuone jinsi Yehova anavyotendea watu wake. Kumbuka kwamba katika siku za Mika Waisraeli ni waasi. Hata hivyo, kwa huruma Yehova anazungumza nao kwa maneno, “Enyi watu wangu.” Naye anawasihi: “Enyi watu wangu, kumbukeni, tafadhali,” NW. Badala ya kuwashtumu vikali, yeye anajaribu kufikia mioyo yao kwa kuwauliza, “Nimewatenda nini?” Hata anawatia moyo ‘washuhudie juu’ yake.
4. Kielelezo cha huruma cha Yehova kinapaswa kutufanya tutendeje?
4 Mungu anatuwekea sote kielelezo kilichoje! Kwa huruma aliwaita watu wa Israeli na Yuda walioasi katika siku za Mika, “watu wangu,” na kuzungumza nao kwa maneno kama vile “tafadhali.” Basi, bila shaka, tunapaswa kuonyesha huruma na rehema tunaposhughulika na washiriki wa kutaniko. Ni kweli kwamba, huenda isiwe rahisi kupatana na watu fulani, au huenda wakawa dhaifu kiroho. Hata hivyo, ikiwa wanampenda Yehova, tungependa kuwasaidia na kuwaonyesha huruma.
5. Ni jambo gani la msingi linalotajwa katika Mika 6:6, 7?
5 Sasa na tuangalie Mika 6:6, 7. Mika anauliza mfululizo wa maswali, akisema: “Nimkaribie BWANA na kitu gani, na kuinama mbele za Mungu aliye juu? Je! nimkaribie na sadaka za kuteketezwa, na ndama za umri wa mwaka mmoja? Je! BWANA atapendezwa na elfu za kondoo waume, au na elfu kumi za mito ya mafuta? Je! nimtoe mzaliwa wangu wa kwanza kwa kosa langu, mzao wa mwili wangu kwa dhambi ya roho yangu?” La, haiwezekani kumpendeza Yehova kwa “elfu za kondoo waume, au na elfu kumi za mito ya mafuta.” Lakini kuna jambo litakalompendeza. Ni jambo gani hilo?
Ni Lazima Tutende Haki
6. Ni matakwa gani matatu ya Mungu yanayotajwa katika Mika 6:8?
6 Katika Mika 6:8 tunajifunza mambo ambayo Yehova anataka kwetu. Mika anauliza: “BWANA anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda [“kutembea,” NW] kwa unyenyekevu na Mungu wako?” Matakwa hayo matatu yanahusu jinsi tunavyohisi, tunavyofikiri, na tunavyotenda. Ni lazima tutake kuonyesha sifa hizo, tufikirie jinsi ya kuzionyesha, na kuchukua hatua ya kufanya hivyo. Na tuchunguze matakwa hayo matatu moja baada ya lingine.
7, 8. (a) Inamaanisha nini “kutenda haki”? (b) Ni matendo gani yasiyo ya haki yanayoenea katika siku za Mika?
7 “Kutenda haki” humaanisha kutenda yaliyo sawa. Njia ya Mungu ya kufanya mambo ndiyo kiwango cha haki. Hata hivyo, watu wa siku za Mika wanatenda isivyo haki. Katika njia gani? Ona Mika 6:10. Mwishoni mwa mstari huo, inaelezwa kwamba wafanyabiashara wanatumia “kipimo kilichopunguka,” yaani, kipimo kidogo sana. Mstari wa 11 unaongezea kwamba wanatumia “mawe ya kupimia ya udanganyifu.” Na kulingana na mstari wa 12, “ulimi wao una udanganyifu.” Kwa hiyo, katika siku za Mika kipimo kilichopunguka, mawe ya kupimia ya udanganyifu, na ulimi wa udanganyifu ni mambo yaliyoenea katika biashara.
8 Ukosefu huo wa haki haupatikani tu katika sehemu za biashara. Unapatikana mahakamani pia. Andiko la Mika 7:3 linaonyesha kwamba “mkuu aomba rushwa, kadhi yu tayari kuipokea.” Mahakimu wanapewa rushwa ili wawahukumu isivyo haki watu wasio na hatia. “Mtu mkubwa,” au raia mashuhuri, anajiunga na uhalifu huo. Kwa kweli, Mika anasema kwamba mtu mkuu, hakimu, na kadhi ‘hufuma,’ au hupanga pamoja matendo yao maovu.
9. Yuda na Israeli wameathiriwaje na mambo yasiyo ya haki yanayotendwa na waovu?
9 Mambo yasiyo ya haki yaliyotendwa na viongozi waovu yanaathiri Yuda na Israeli yote. Andiko la Mika 7:5 linasema kwamba ukosefu wa haki umefanya marafiki wa karibu na hata wenzi wa ndoa wasiaminiane. Mstari wa 6 unaonyesha kwamba ukosefu wa haki umefanya watu wa jamaa wa karibu kama vile wana na baba, mabinti na mama wadharauliane.
10. Wakristo hujiendeshaje katika hali za sasa zenye ukosefu wa haki?
10 Namna gani leo? Je, hatuoni hali kama hizo? Kama vile Mika, sisi pia tunazungukwa na ukosefu wa haki, hali ya kutoaminiana, na kuvunjika kwa maisha ya jamii na ya familia. Hata hivyo, tukiwa watumishi wa Mungu katika ulimwengu huu usio na uadilifu, haturuhusu roho ya ulimwengu huu ya ukosefu wa haki iingie katika kutaniko la Kikristo. Badala yake tunajitahidi kufuata kanuni za haki na uaminifu-maadili, na kuonyesha sifa hizo katika shughuli zetu za kila siku. Kwa kweli ‘tunajiendesha wenyewe kwa kufuata haki katika mambo yote.’ (Waebrania 13:18) Je, huamini kwamba kwa kutenda haki tunapata baraka nyingi zinazotoka kwa akina ndugu wanaotumainiana kikweli?
Watu Husikiaje “Sauti ya BWANA”?
11. Andiko la Mika 7:12 linatimizwaje?
11 Mika anatabiri kwamba ingawa kuna ukosefu wa haki, watu wa aina zote watapata haki. Nabii huyo anatabiri kwamba watu watakusanywa ‘kutoka bahari mpaka bahari, na kutoka mlima mpaka mlima’ ili wawe waabudu wa Yehova. (Mika 7:12) Leo, katika utimizo wa mwisho wa unabii huo, watu kutoka mataifa yote, wala si taifa moja hususa, wananufaika na haki ya Mungu isiyo na ubaguzi. (Isaya 42:1, BHN) Jambo hilo linathibitikaje?
12. Ni kwa njia gani “sauti ya BWANA” inasikiwa leo?
12 Ili kupata jibu, fikiria maneno ya awali ya Mika. Andiko la Mika 6:9, ZSB linasema: “Sauti ya BWANA inalia katika muji, na mwenye akili ataogopa jina lako.” Watu wa mataifa yote wanaisikiaje “sauti ya BWANA,” na jambo hilo linahusianaje na jinsi tunavyotenda haki? Bila shaka, watu leo hawasikii sauti ya Mungu kihalisi. Hata hivyo, kupitia kazi yetu ya kuhubiri inayofanywa ulimwenguni pote, sauti ya Yehova inasikiwa na watu wa jamii zote na wa aina zote. Kwa sababu hiyo, wale wanaosikiliza ‘wanaogopa jina la Mungu,’ na kuliheshimu sana. Kwa kweli, tunatenda kwa haki na upendo tunapotumikia tukiwa watangazaji wa Ufalme wenye bidii. Kwa kuwajulisha wote jina la Mungu bila kubagua, ‘tunatenda haki.’
Ni Lazima Tupende Rehema
13. Kuna tofauti gani kati ya sifa ya fadhili-upendo na upendo?
13 Sasa, na tuzungumzie takwa la pili linalotajwa katika Mika 6:8. Yehova anataka ‘tupende rehema.’ Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “rehema” pia limetafsiriwa “fadhili-upendo” au “upendo mwaminifu-mshikamanifu.” Fadhili-upendo humaanisha kuwajali au kuwahurumia wengine. Sifa ya fadhili-upendo inatofautiana na upendo. Jinsi gani? Upendo ni sifa inayohusisha mambo mengi zaidi. Upendo unaweza hata kuelekezwa kwa vitu na sifa. Kwa mfano, Maandiko hutaja mtu “apendaye mvinyo na mafuta” na pia mtu “apendaye hekima.” (Mithali 21:17; 29:3) Kwa upande mwingine, sikuzote sifa ya “fadhili-upendo” huhusisha watu, hasa wale wanaomtumikia Mungu. Kwa hiyo andiko la Mika 7:20, NW linataja ‘fadhili-upendo alizoonyeshwa Abrahamu’—mtu aliyemtumikia Yehova Mungu.
14, 15. Fadhili-upendo huonyeshwaje, na ni uthibitisho gani wa sifa hiyo uliotajwa?
14 Katika Mika 7:18, nabii huyo anasema kwamba Mungu ‘hufurahia fadhili-upendo.’ Katika Mika 6:8 hatuambiwi tu tuonyeshe fadhili-upendo, bali tuipende sifa hiyo. Tunajifunza nini kutokana na maandiko hayo? Sifa ya fadhili-upendo huonyeshwa kwa hiari na kwa kupenda kwa sababu tunataka kuionyesha. Kama Yehova, sisi hufurahia kuwaonyesha fadhili-upendo wale walio na uhitaji.
15 Leo, fadhili-upendo ni sifa inayowatambulisha watu wa Mungu. Kwa mfano, mnamo Juni 2001, dhoruba kali ilisababisha mafuriko makubwa sana huko Texas, Marekani, na kuharibu maelfu ya nyumba, kutia ndani mamia ya nyumba za Mashahidi wa Yehova. Ili kuwasaidia ndugu zao Wakristo waliokuwa na uhitaji, Mashahidi wapatao 10,000 walitumia wakati wao na nguvu zao kwa hiari, bila malipo. Kwa zaidi ya nusu mwaka, wafanyakazi hao wa kujitolea walifanya kazi mfululizo, wakitumia wakati wao—mchana na usiku na miisho-juma—kujenga upya Majumba ya Ufalme 8 na zaidi ya nyumba 700 kwa ajili ya ndugu zao Wakristo. Wale ambao hawakuweza kufanya kazi hiyo, walitoa chakula, vifaa, na pesa. Kwa nini maelfu ya Mashahidi hao waliwasaidia ndugu zao? Kwa sababu ‘wanapenda fadhili-upendo.’ Ni jambo linalosisimua kama nini kujua kwamba ndugu zetu ulimwenguni pote wanaonyesha matendo hayo ya fadhili-upendo! Naam, kutimiza takwa la ‘kupenda fadhili-upendo’ si mzigo, bali huleta shangwe!
Kutembea kwa Unyenyekevu na Mungu
16. Ni mfano gani unaosaidia kukazia uhitaji wa kutembea kwa unyenyekevu na Mungu?
16 Takwa la tatu linalopatikana katika Mika 6:8 ni ‘kutembea kwa unyenyekevu na Mungu wako.’ Hii inamaanisha kutambua kupungukiwa kwetu na kumtegemea Mungu. Kwa mfano: Ebu wazia msichana mdogo ambaye amemshika baba yake mkono kwa nguvu wanapotembea mahali penye dhoruba. Msichana huyo anajua kwamba hana nguvu sana, lakini anamtumaini baba yake. Lazima sisi pia tutambue kupungukiwa kwetu na tumtumaini Baba yetu wa mbinguni. Tunaweza kudumishaje tumaini hilo? Njia moja ni kukumbuka kwa nini ni jambo la hekima kukaa karibu na Mungu. Mika anatukumbusha sababu tatu: Yehova ni Mkombozi, Kiongozi, na Mlinzi wetu.
17. Ni jinsi gani Yehova aliwakomboa, akawaongoza, na kuwalinda watu wake wa kale?
17 Kulingana na Mika 6:4, 5 Mungu anasema: “Nalikupandisha kutoka nchi ya Misri.” Naam, Yehova alikuwa Mkombozi wa Israeli. Yehova anaendelea kusema: “Naliwapeleka Musa, na Haruni, na Miriamu, watangulie mbele yako.” Musa na Aroni walitumiwa kuongoza taifa hilo, naye Miriamu akawaongoza wanawake wa Israeli katika dansi ya ushindi. (Kutoka 7:1, 2; 15:1, 19-21; Kumbukumbu la Torati 34:10) Yehova aliongoza taifa hilo kupitia watumishi wake. Katika mstari wa 5, Yehova anakumbusha taifa la Israeli kwamba aliwalinda dhidi ya Balaki na Balaamu na aliwalinda pia katika mkondo wa mwisho wa safari yao kutoka Shitimu huko Moabu mpaka Gilgali katika Nchi ya Ahadi.
18. Leo Mungu anatendaje akiwa Mkombozi, Kiongozi, na Mlinzi wetu?
18 Tunapotembea na Mungu, anatukomboa kutoka katika ulimwengu wa Shetani, anatuongoza kupitia Neno lake na tengenezo lake, na kutulinda tukiwa kikundi tunaposhambuliwa na wapinzani. Kwa hiyo, tuna kila sababu ya kushika kwa nguvu mkono wa Baba yetu wa mbinguni tunapotembea naye katika mkondo wa mwisho wenye dhoruba wa safari yetu ya kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu, ambao ni bora zaidi ya Nchi ya Ahadi ya kale.
19. Unyenyekevu unahusianaje na kupungukiwa kwetu?
19 Kutembea na Mungu kwa unyenyekevu hutusaidia pia kuona hali zetu kwa njia inayofaa. Hiyo ni kwa sababu kuonyesha unyenyekevu hutia ndani kufahamu kupungukiwa kwetu. Huenda uzee au afya mbaya ikapunguza yale tunayoweza kufanya katika utumishi wa Yehova. Hata hivyo, badala ya kuacha hali hiyo ituvunje moyo, tunapaswa kukumbuka kwamba Mungu hukubali jitihada na dhabihu zetu ‘kulingana na tulicho nacho, si kulingana na kile ambacho hatuna.’ (2 Wakorintho 8:12) Kwa kweli, Yehova anataka tumtumikie kwa nafsi yote, na kufanya tuwezayo kulingana na hali zetu. (Wakolosai 3:23) Tunapojitahidi kufanya yote tuwezayo katika utumishi wa Mungu, yeye hutubariki sana.—Mithali 10:22.
Mtazamo wa Kungojea Huleta Baraka
20. Ni kwa kujua nini tunasaidiwa kuwa na mtazamo kama ule Mika?
20 Tunapopata baraka za Yehova tunachochewa kuiga mtazamo wa Mika. Yeye anasema: “Nitamngojea Mungu wa wokovu wangu.” (Mika 7:7) Maneno hayo yanahusianaje na kutembea kwetu na Mungu kwa unyenyekevu? Kuwa na mtazamo wa kungojea, au subira, hutusaidia tusikate tamaa kwa sababu siku ya Yehova haijafika bado. (Mithali 13:12) Kwa kweli, sote tunatamani kuona mwisho wa ulimwengu huu mwovu. Hata hivyo, kila juma kuna maelfu ya watu wanaoanza kutembea na Mungu. Kujua hivyo hutupa sababu ya kuwa na mtazamo wa kungojea. Shahidi mmoja ambaye ametumikia kwa muda mrefu alisema hivi kuhusiana na hilo: “Ninapokumbuka miaka 55 ambayo nimekuwa nikihubiri, ninasadiki kwamba sijapoteza chochote kwa kumngojea Yehova. Kinyume cha hilo, nimeepuka mambo mengi yenye kuumiza.” Je, umepata kuona jambo kama hilo?
21, 22. Andiko la Mika 7:14 linatimizwaje leo?
21 Bila shaka, kutembea na Yehova hutunufaisha. Kama tunavyosoma katika Mika 7:14, Mika anawalinganisha watu wa Mungu na kondoo wanaoishi salama pamoja na mchungaji wao. Leo, katika utimizo mkubwa zaidi wa unabii huo, mabaki ya Israeli wa kiroho na vilevile “kondoo wengine” wanapata ulinzi wanapokuwa na Mchungaji wao wanayemtumaini, Yehova. Wanakaa “peke yao, mwituni katikati ya Karmeli,” wakiwa wametengwa kwa njia ya kiroho na ulimwengu huu unaozidi kuwa na misukosuko na hatari nyingi.—Yohana 10:16; Kumbukumbu la Torati 33:28; Yeremia 49:31; Wagalatia 6:16.
22 Watu wa Yehova wanapata ufanisi kama ilivyotabiriwa pia katika Mika 7:14. Akizungumza kuhusu kondoo au watu wa Mungu, Mika anasema: “Na walishe katika Bashani na Gileadi.” Kama vile kondoo huko Bashani na Gileadi walivyokula kwenye malisho yenye rutuba, wakanawiri, ndivyo watu wa Mungu leo wanavyopata ufanisi wa kiroho—ambao ni baraka nyingine kwa wale wanaotembea kwa unyenyekevu na Mungu.—Hesabu 32:1; Kumbukumbu la Torati 32:14.
23. Tunaweza kujifunza nini kwa kuchunguza Mika 7:18, 19?
23 Katika Mika 7:18, 19, nabii huyo anakazia tamaa ya Yehova ya kuwasamehe wale wanaotubu. Mstari wa 18 unasema kwamba Yehova ‘anasamehe uovu, na kuliachilia kosa.’ Kulingana na mstari wa 19, ‘atatupa dhambi zao zote katika vilindi vya bahari.’ Tunajifunza nini kutokana na hilo? Tunaweza kujiuliza kama tunamwiga Yehova kwa njia hiyo. Je, sisi huwasamehe wengine makosa ambayo huenda wakatutendea? Watu hao wanapotubu na kuomba msamaha, bila shaka tungependa kumwiga Yehova kwa kuwa tayari kuwasamehe kabisa kabisa.
24. Umenufaikaje na unabii wa Mika?
24 Tumenufaikaje kwa kuchunguza unabii wa Mika? Tumekumbushwa kwamba Yehova hutoa tumaini la kweli kwa wale wanaovutwa kwake. (Mika 2:1-13) Tumetiwa moyo kufanya yote tuwezayo kuendeleza ibada ya kweli ili tuweze kutembea katika jina la Mungu milele. (Mika 4:1-4) Nasi tumehakikishiwa kwamba hata hali zetu ziweje, tunaweza kutimiza matakwa ya Yehova. Ndiyo, unabii wa Mika unatutia nguvu kwelikweli tutembee katika jina la Yehova.
-