-
Wahudumu wa Habari NjemaTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
kuonyesha imani yake kwa kuwahubiria wengine habari njema, anaweza kusaidiwaje?
14 Ni vizuri wazazi wazungumze na mmoja wa wazee wa Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko ili kuona ikiwa mtoto huyo anastahili kuwa mhubiri. Mratibu wa baraza la wazee atapanga wazee wawili (mmoja wao akiwa mshiriki wa halmashauri ya utumishi) wakutane na mtoto huyo na mzazi mmoja au wote wawili ambao ni waamini, au mlezi wake. Ikiwa mtoto ana ujuzi wa msingi wa kweli za Biblia na anaonyesha wazi kwamba anataka kushiriki katika utumishi, jambo hilo litathibitisha kwamba amefanya maendeleo. Baada ya kufikiria mambo hayo na mengine yanayowahusu watu wazima, wazee hao wanaweza kuamua ikiwa mtoto huyo anastahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa. (Luka 6:45; Rom. 10:10) Wanapokutana na mtoto, hakuna haja ya kuzungumzia baadhi ya mambo ambayo kwa kawaida yanawahusu watu wazima tu.
15 Wakati wa mazungumzo, wazee wanapaswa kumpongeza mtoto kwa maendeleo yake na kumtia moyo ajitahidi kufikia ubatizo. Kwa kuwa wazazi wamejitahidi kumfundisha mtoto wao kweli, wao pia wanastahili kupongezwa. Ili kuwasaidia wazazi kumsaidia zaidi mtoto wao, wazee wanapaswa kuwaonyesha habari yenye kichwa “Ujumbe kwa Wazazi Wakristo,” kwenye ukurasa wa 179-181.
WAKFU NA UBATIZO
16 Ikiwa umemjua na kumpenda Yehova kwa kupatanisha maisha yako na matakwa yake na kwa kushiriki katika huduma ya shambani, unahitaji kuimarisha uhusiano wako pamoja naye. Jinsi gani? Kwa kujiweka wakfu kwake na kuonyesha wakfu huo kwa kubatizwa katika maji.—Mt. 28:19, 20.
17 Kuweka wakfu humaanisha kutenga kwa ajili ya kusudi takatifu. Kujiweka wakfu kwa Mungu kunamaanisha kusali kwake na kumwahidi kwamba utatumia maisha yako kumtumikia na kutembea katika njia zake. Humaanisha kumwabudu yeye peke yake milele. (Kum. 5:9) Hilo ni jambo la kibinafsi unalofanya faraghani. Hakuna mtu anayeweza kufanya hivyo kwa niaba yako.
18 Hata hivyo, haitoshi tu kumwambia Yehova faraghani kwamba unataka kuwa mali yake. Unahitaji kuwaonyesha wengine kwamba umejiweka wakfu kwa Mungu. Unafanya hivyo kwa kubatizwa katika maji, kama Yesu alivyofanya. (1 Pet. 2:21; 3:21) Ikiwa umeamua kumtumikia Yehova na unataka kubatizwa, unapaswa kufanya nini? Unapaswa kumwambia mratibu wa baraza la wazee. Atapanga wazee kadhaa wazungumze nawe ili kuhakikisha kwamba unatimiza matakwa ya Mungu kwa ajili ya wale wanaotaka kubatizwa. Kwa habari zaidi, tafadhali soma “Ujumbe kwa Mhubiri Ambaye Hajabatizwa,” kwenye ukurasa wa 182-184 wa kitabu hiki na “Maswali kwa Ajili ya Wale Wanaotaka Kubatizwa,” kwenye ukurasa wa 185-207.
RIPOTI YA MAENDELEO YA HUDUMA
19 Kwa miaka mingi, ripoti za maendeleo ya ibada safi ulimwenguni pote zimewatia moyo watu wa Yehova. Tangu Yesu Kristo alipowaambia wanafunzi wake kwamba habari njema ingehubiriwa duniani kote, Wakristo wa kweli wametamani sana kujua jinsi ambavyo kazi hiyo ingetimizwa.—Mt. 28:19, 20; Marko 13:10; Mdo. 1:8.
20 Wafuasi wa Yesu walifurahia kusikiliza ripoti za maendeleo ya kazi ya kuhubiri. (Marko 6:30) Kitabu cha Biblia cha Matendo kinatuambia kwamba kulikuwa na watu 120 hivi roho takatifu ilipomiminwa juu ya wanafunzi siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K. Muda mfupi baadaye idadi ya wanafunzi iliongezeka hadi 3,000 hivi, kisha 5,000 hivi. Iliripotiwa kwamba ‘Yehova aliendelea kuwaongezea kila siku watu waliokuwa wakiokolewa’ na kwamba “umati mkubwa wa makuhani wakawa waamini.” (Mdo. 1:15; 2:5-11, 41, 47; 4:4; 6:7) Habari hizo za ongezeko ziliwatia moyo sana wanafunzi! Ripoti hizo zenye kusisimua ziliwachochea kuendelea kufanya kazi waliyopewa na Mungu, licha ya mateso makali yaliyoanzishwa na viongozi wa dini ya Kiyahudi!
21 Karibu mwaka wa 60 na 61 W.K., Paulo katika barua yake kwa Wakolosai aliandika kwamba habari njema ilikuwa ikizaa “matunda na kuongezeka ulimwenguni kote” na “ilihubiriwa katika uumbaji wote chini ya mbingu.” (Kol. 1:5, 6, 23) Wakristo wa karne ya kwanza walitii Neno, na roho takatifu iliwatia nguvu kutimiza kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote kabla ya mfumo wa mambo wa Kiyahudi kufikia mwisho wake mwaka wa 70 W.K. Wakristo hao waaminifu walitiwa moyo kwelikweli kusikia ripoti za matokeo ya kazi hiyo!
Je, unajitahidi kutimiza kikamili huduma kabla ya mwisho kuja?
22 Vivyo hivyo, tengenezo la Yehova la kisasa hujitahidi kuweka rekodi sahihi za kazi inayofanywa ili kutimiza Mathayo 24:14 inayosema hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” Tukiwa watumishi wa Mungu waliojiweka wakfu, tuna kazi inayopaswa kufanywa haraka. Kila mmoja wetu anapaswa ajitahidi kutimiza kikamili huduma kabla ya mwisho kuja. Yehova atahakikisha kwamba kazi hiyo inakamilika, na tukishiriki kuifanya, tutapata kibali chake.—Eze. 3:18-21.
RIPOTI YAKO YA UTUMISHI WA SHAMBANI
23 Tunapaswa kuripoti nini? Fomu ya Ripoti ya Utumishi wa Shambani inayochapishwa na tengenezo ina mambo yanayopaswa kuripotiwa. Hata hivyo, maelezo na ufafanuzi ufuatao, utakusaidia sana.
24 Katika safu ya “Machapisho (Yaliyochapishwa na ya Kielektroniki),” andika jumla ya machapisho yote iwe ni yaliyochapishwa au ya kielektroniki uliyowapa watu ambao si Mashahidi waliobatizwa. Katika safu ya “Video Ambazo Zilionyeshwa” andika jumla ya video zote ambazo ulionyesha.
25 Unaporipoti “Ziara za Kurudia,” jumlisha ziara zote za kurudia ulizofanya kwa kusudi la kuchochea upendezi ulioonyeshwa na mtu ambaye si Shahidi aliyejiweka wakfu na kubatizwa. Ziara ya kurudia inaweza kufanywa kwa kumtembelea mtu kibinafsi, kwa kuandika barua, kupiga simu, kutuma ujumbe kupitia simu au barua pepe, au kumpelekea chapisho fulani. Kila mara unapoongoza funzo la Biblia la nyumbani, unaweza kuhesabu ziara ya kurudia. Mzazi anaweza kuhesabu ziara moja ya kurudia kila juma anapoongoza ibada ya familia ikiwa kuna mtoto ambaye hajabatizwa.
26 Ingawa funzo la Biblia huongozwa kila juma, huripotiwa kama funzo moja tu kwa mwezi. Wahubiri wanapaswa kuandika idadi ya mafunzo ya Biblia yaliyoongozwa katika mwezi. Mafunzo ya Biblia ambayo yanaweza kuripotiwa yanatia ndani watu wote ambao si Mashahidi waliojiweka wakfu na kubatizwa. Unaweza kuhesabu funzo la Biblia unapojifunza na ndugu au dada asiyetenda unapoombwa na mshiriki wa halmashauri ya utumishi au unapojifunza na mhubiri aliyebatizwa karibuni ambaye hajamaliza kitabu Furahia Maisha Milele!
27 Ni muhimu kutoa ripoti sahihi ya “Saa.” Kwa kawaida huo ni muda unaotumia unapohubiri nyumba kwa nyumba, barabarani, unapofanya ziara za kurudia, unapoongoza mafunzo ya Biblia, au unapowahubiria rasmi au isivyo rasmi watu ambao si Mashahidi waliojiweka wakfu na kubatizwa. Wahubiri wawili wanapohubiri pamoja, wote wanaweza kuhesabu saa, lakini mmoja tu ndiye atakayehesabu ziara ya kurudia au funzo la Biblia litakaloongozwa. Wazazi wawili wanaoshirikiana kuwafundisha watoto wao wakati wa Ibada ya Familia wanaweza kuhesabu saa moja kwa juma. Ndugu wanaweza kuhesabu muda wanaotumia kutoa hotuba za watu wote. Mkalimani wa hotuba ya watu wote anaweza pia kuhesabu muda huo. Muda unaotumiwa kwa shughuli nyingine muhimu kama vile, kujitayarisha kwa ajili ya utumishi wa shambani, kuhudhuria mkutano wa utumishi, shughuli za kibinafsi wakati wa utumishi, na kadhalika hauhesabiwi.
28 Kila mhubiri atatumia dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia kusali na kuamua muda aliotumia kutoa ushahidi. Baadhi ya wahubiri wanahubiri katika maeneo yenye watu wengi, na wengine huhubiri katika maeneo yasiyo na watu wengi hivyo wanatumia muda mwingi kusafiri. Maeneo yanatofautiana; maoni ya wahubiri kuhusu huduma yao hutofautiana. Baraza Linaloongoza haliweki sheria jinsi makutaniko yanavyohesabu muda uliotumika katika utumishi wa shambani, wala hakuna mtu aliyeteuliwa ili kuwahukumu wengine kuhusu jambo hilo.—Mt. 6:1; 7:1; 1 Tim. 1:5.
29 Muda unaotumia katika utumishi wa shambani unapaswa kuripotiwa saa nzima-nzima. Hata hivyo, mhubiri asiyejiweza kwa sababu ya uzee, ulemavu, ugonjwa au udhaifu mwingine wowote, anaweza kuripoti utumishi wa dakika 15, 30, na 45. Hata ikiwa alitoa ushahidi kwa dakika 15 tu kwa mwezi, anaweza kuripoti muda huo. Atahesabiwa kuwa mhubiri wa Ufalme anayetenda. Mhubiri ambaye hajiwezi kwa mwezi mmoja au miezi kadhaa, labda kwa sababu ya ugonjwa au jeraha kubwa, anaweza pia kuhusishwa katika mpango huo. Mpango huo unawahusu wale tu wenye udhaifu mkubwa wa kimwili. Halmashauri ya utumishi itaamua ikiwa mhubiri anastahili kuhusishwa katika mpango huo.
REKODI YA KUTANIKO YA MHUBIRI
30 Ripoti yako ya utumishi wa shambani ya kila mwezi huandikwa kwenye Rekodi ya Kutaniko ya Mhubiri. Rekodi hizo ni za kutaniko unaloshirikiana nalo. Ukitaka kuhamia kutaniko lingine, hakikisha unawajulisha wazee. Mwandishi atahakikisha kwamba rekodi zako zinatumwa kwenye kutaniko unalohamia. Kwa kufanya hivyo, wazee wa kutaniko unalohamia watakukaribisha na wataendelea kukusaidia kiroho. Ikiwa utakuwa mbali na kutaniko lako kwa muda usiozidi miezi mitatu, tafadhali endelea kutuma ripoti yako ya utumishi katika kutaniko lako.
KWA NINI TUNARIPOTI UTUMISHI WETU WA SHAMBANI?
31 Je, nyakati nyingine wewe husahau kutoa ripoti yako ya utumishi wa shambani? Bila shaka sote tunahitaji kukumbushwa mara kwa mara. Lakini tukisitawisha mtazamo unaofaa na tukielewa umuhimu wa kuripoti utumishi wetu wa shambani, inaweza kuwa rahisi kukumbuka kufanya hivyo.
32 Wengine wameuliza: “Kwa kuwa Yehova anajua yale ambayo ninafanya katika utumishi wake, kwa nini nitoe ripoti kutanikoni?” Ni kweli kwamba Yehova anajua yale tunayofanya, naye anajua ikiwa tunamtumikia kwa nafsi yote au tunafanya kidogo kwa kulinganisha na uwezo wetu. Hata hivyo, kumbuka kwamba Yehova alirekodi siku ambazo Noa alikaa ndani ya safina na miaka ambayo Waisraeli walisafiri jangwani. Mungu aliweka rekodi ya wale waliokuwa waaminifu na wale ambao hawakutii. Alirekodi jinsi nchi ya Kanaani ilivyotekwa hatua kwa hatua na mambo yaliyotimizwa na waamuzi waaminifu wa Israeli. Naam, alirekodi habari nyingi sana kuhusu matendo ya watumishi wake. Alitumia roho yake kuongoza kuandikwa kwa matukio hayo, na hivyo kutuonyesha umuhimu wa kuandika rekodi sahihi.
33 Matukio ya kihistoria yaliyoandikwa katika Biblia yanaonyesha usahihi wa ripoti na rekodi za watu wa Yehova. Katika visa vingi, masimulizi ya Biblia hayangekuwa yenye kuchochea ikiwa hesabu kamili haingetajwa. Fikiria mifano ifuatayo: Mwanzo 46:27; Kutoka 12:37; Waamuzi 7:7; 2 Wafalme 19:35; 2 Mambo ya Nyakati 14:9-13; Yohana 6:10; 21:11; Matendo 2:41; 19:19.
34 Ingawa ripoti hizo hazionyeshi kila jambo tunalofanya katika utumishi wetu kwa Yehova, zinatimiza kusudi muhimu katika tengenezo la Yehova. Katika karne ya kwanza, baada ya kuhubiri, mitume wa Yesu waliripoti “mambo yote waliyokuwa wamefanya na kufundisha.” (Marko 6:30) Nyakati nyingine, ripoti zinaweza kuonyesha mambo hususa yanayohitaji kushughulikiwa katika sehemu fulani ya huduma yetu. Takwimu zinaweza kuonyesha kama kuna maendeleo katika utendaji fulani, na vilevile ikiwa hakuna ongezeko kubwa la wahubiri. Huenda wahubiri wanahitaji kutiwa moyo au kuna matatizo yanayopaswa kushughulikiwa. Waangalizi wanaohusika watachunguza ripoti hizo na kujitahidi kurekebisha hali yoyote ambayo huenda inazuia maendeleo ya mtu mmoja-mmoja au ya kutaniko lote.
35 Pia, ripoti hulisaidia tengenezo kujua maeneo yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri. Ni maeneo gani yenye matokeo mazuri? Ni maeneo gani yenye ukuzi mdogo? Ni machapisho gani yanayohitajiwa ili kuwasaidia watu wajifunze kweli? Ripoti husaidia tengenezo kujua machapisho yanayohitajiwa katika maeneo mbalimbali ulimwenguni na kisha huhakikisha kwamba yanapatikana.
36 Wengi wetu hutiwa moyo na ripoti. Je, hatusisimuki tunaposikia kuhusu mambo ambayo ndugu zetu wanatimiza wanapohubiri habari njema ulimwenguni pote? Ripoti za ongezeko hutusaidia kuona jinsi tengenezo la Yehova linavyopanuka. Mambo yaliyoonwa huchangamsha moyo, huzidisha bidii yetu na kutuchochea tushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri. (Mdo. 15:3) Ni muhimu kila mmoja wetu atoe ripoti ya utumishi wa shambani na hilo huonyesha kwamba tunawajali ndugu zetu ulimwenguni pote. Kupitia jambo hilo dogo tunaonyesha kwamba tunatii mipango ya tengenezo la Yehova.—Luka 16:10; Ebr. 13:17.
KUJIWEKEA MALENGO
37 Hatuna sababu yoyote ya kulinganisha utumishi wetu wa shambani na wa mtu mwingine. (Gal. 5:26; 6:4) Hali za watu hutofautiana sana. Kwa upande mwingine, tunaweza kupata faida nyingi sana tukiweka malengo halisi tunayoweza kufikia ili kupima maendeleo yetu katika huduma. Tukifikia malengo hayo tutaridhishwa na mambo tuliyotimiza.
38 Ni wazi kwamba sasa Yehova anaharakisha kazi ya kukusanya watu watakaookoka ile “dhiki kuu.” Tunaishi wakati ambapo unabii huu wa Isaya unatimia: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa lenye nguvu. Mimi mwenyewe, Yehova, nitaharakisha jambo hilo kwa wakati wake.” (Ufu. 7:9, 14; Isa. 60:22) Ni heshima kubwa sana kuwa wahudumu wa habari njema katika siku hizi za mwisho!—Mt. 24:14.
-
-
Njia za Kuhubiri Habari NjemaTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 9
Njia za Kuhubiri Habari Njema
YESU KRISTO alihubiri habari njema kwa bidii, akiwawekea mfano mzuri wafuasi wake. Alichukua hatua ya kuwatafuta watu, akizungumza nao na kuwafundisha nyumbani kwao na hadharani. (Mt. 9:35; 13:36; Luka 8:1) Yesu alizungumza na watu binafsi, aliwafundisha wanafunzi wake faraghani, na hata alihutubia maelfu ya watu. (Marko 4:10-13; 6:35-44; Yoh. 3:2-21) Alitumia kila pindi aliyopata kuwatia watu moyo na kuwapa tumaini. (Luka 4:16-19) Hakuacha nafasi ya kuhubiri impite hata alipohitaji kupumzika au kula. (Marko 6:30-34; Yoh. 4:4-34) Tunaposoma masimulizi ya huduma ya Yesu yaliyoongozwa na roho, je, hatuchochewi kuiga mfano wake? Bila shaka tunachochewa kumwiga, kama mitume walivyochochewa.—Mt. 4:19, 20; Luka 5:27, 28; Yoh. 1:43-45.
2 Fikiria nafasi ambazo Wakristo wanazo za kushiriki katika kazi iliyoanzishwa na Yesu Kristo miaka 2,000 hivi iliyopita.
KUHUBIRI NYUMBA KWA NYUMBA
3 Tukiwa Mashahidi wa Yehova tunatambua umuhimu wa kuhubiri habari njema ya Ufalme kwa utaratibu, yaani, nyumba kwa nyumba. Tumetumia sana njia hiyo hivi kwamba ni alama inayotutambulisha. Faida za kutumia njia hii ili kuwafikia mamilioni ya watu katika muda mfupi zimeonyeshwa pia na ongezeko kubwa tunalopata. (Mt. 11:19; 24:14) Kuhubiri nyumba kwa nyumba hutupatia fursa ya kuonyesha kwamba tunampenda Yehova na jirani zetu.—Mt. 22:34-40.
4 Mahubiri ya nyumba kwa nyumba hayakubuniwa hivi karibuni na Mashahidi wa Yehova. Mtume Paulo alisema kwamba aliwafundisha watu nyumbani kwao. Akiwaeleza waangalizi huko Efeso kuhusu huduma yake, alisema hivi: “Tangu siku ya kwanza niliyokanyaga mkoa wa Asia, . . . sikuepuka kuwaambia ninyi jambo lolote lenye faida na kuwafundisha . . . nyumba kwa nyumba.” Kupitia njia hiyo na nyinginezo, Paulo alitoa “ushahidi kikamili kwa Wayahudi na Wagiriki kuhusu toba kwa Mungu na kuwa na imani katika Bwana wetu Yesu.” (Mdo. 20:18, 20, 21) Wakati huo, watawala Waroma walichochea ibada ya sanamu na watu wengi ‘walionekana kuwa wanaogopa sana miungu.’ Watu walihitaji kumtafuta kwa haraka “Mungu aliyeumba ulimwengu na vitu vyote vilivyomo,” ambaye wakati huo alikuwa “anawatangazia wanadamu wote kila mahali kwamba wanapaswa kutubu.”—Mdo. 17:22-31.
5 Leo kuna uhitaji mkubwa hata zaidi wa kuwapelekea watu habari njema haraka. Mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo unakaribia kwa kasi sana. Tunachochewa kuongeza bidii yetu tunapotambua uhitaji huo. Hakuna njia nyingine bora ya kuwatafuta watu wenye njaa ya kiroho kuliko njia ya kuhubiri nyumba kwa nyumba ambayo imetumiwa kwa muda mrefu. Bado ina matokeo mazuri leo kama ilivyokuwa katika siku za Yesu na mitume.—Marko 13:10.
6 Je, unashiriki kikamili katika huduma ya nyumba kwa nyumba? Ikiwa ndivyo, uwe na hakika kwamba unamfurahisha Yehova. (Eze. 9:11; Mdo. 20:35) Huenda isiwe rahisi kwako kuhubiri nyumba kwa nyumba. Labda una udhaifu wa kimwili au watu wengi katika eneo lenu hawataki kusikiliza. Au kuna vizuizi vya serikali. Huenda wewe ni mwenye haya, na unaogopa kuzungumza na watu usiowafahamu. Kwa sababu hiyo, kila mara unapohubiri nyumba kwa nyumba unakuwa na wasiwasi. Usikate tamaa. (Kut. 4:10-12) Ndugu zako pia wanakabili hali kama hizo katika maeneo mengine.
7 Yesu aliwaahidi wanafunzi wake hivi: “Tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:20) Ahadi hiyo hutuimarisha tunapofanya kazi ya kuhubiri na kufundisha. Tunahisi kama mtume Paulo aliyesema: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yule anayenipa nguvu.” (Flp. 4:13) Unga mkono kikamili mipango ya kutaniko ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Unapohubiri na wengine, watakutia moyo na kukusaidia kuboresha ustadi wako. Sali ili ushinde vizuizi ambavyo huenda ukakabili, na ujitahidi kuwa mhubiri wa habari njema mwenye bidii.—1 Yoh. 5:14.
8 Unapowatangazia wengine habari njema, utapata nafasi za kuwaeleza ‘sababu ya tumaini ulilo nalo.’ (1 Pet. 3:15) Utafahamu vizuri zaidi tofauti kati ya wale walio na tumaini la Ufalme na wale wasio na tumaini. (Isa. 65:13, 14) Utaridhika kwa kujua kwamba umetii amri ya Yesu ya ‘kuacha nuru yako iangaze,’ na huenda hata ukawa na pendeleo la kuwasaidia wengine wamjue Yehova na wapate kweli inayoongoza kwenye uzima wa milele.—Mt. 5:16; Yoh. 17:3; 1 Tim. 4:16.
9 Mipango hufanywa ili kuhubiri nyumba kwa nyumba katikati ya juma na pia mwisho juma. Makutaniko fulani hupanga kuhubiri jioni katika maeneo ambayo ni vigumu kuwapata watu nyumbani mchana. Huenda watu wakawa tayari kuwakaribisha wageni alasiri au jioni badala ya asubuhi.
KUWATAFUTA WALE WANAOSTAHILI
10 Yesu aliwaagiza wanafunzi wake ‘wawatafute’ wale wanaostahili. (Mt. 10:11) Hakuwatafuta watu wenye mwelekeo unaofaa kwa kuhubiri tu nyumba kwa nyumba. Kwa kweli, alitumia kila nafasi aliyopata ili kuhubiri rasmi au isivyo rasmi. (Luka 8:1; Yoh. 4:7-15) Pia, mitume waliwahubiria watu katika maeneo mbalimbali.—Mdo. 17:17; 28:16, 23, 30, 31.
Lengo letu ni kumpelekea kila mtu ujumbe wa Ufalme inapowezekana
11 Vivyo hivyo, lengo letu ni kumpelekea kila mtu ujumbe wa Ufalme inapowezekana. Hiyo inamaanisha kwamba tunapaswa kuiga njia ambazo Yesu na wanafunzi wake walitumia katika kazi ya kuhubiri na kufundisha na vilevile kubadilikana kulingana na nyakati na hali za watu katika eneo letu. (1 Kor. 7:31) Kwa mfano, wahubiri wamefanikiwa kuwapata watu katika sehemu zao za biashara. Katika nchi nyingi, wahubiri wamepata matokeo kwa kuhubiri barabarani, bustani za kupumzikia, maegesho ya magari, au popote pale watu wanapopatikana. Makutaniko fulani yamepanga kuhubiri kwa kutumia meza au vigari vyenye machapisho katika eneo lao. Isitoshe, ofisi ya tawi inaweza kupanga mahubiri ya pekee ya hadharani katika barabara zenye watu wengi sana katika majiji, kwa kutumia wahubiri wa makutaniko mbalimbali. Matokeo ni kwamba watu wasiopatikana nyumbani wanaweza kupata habari njema mahali pengine.
12 Tunapokutana na watu wanaopendezwa na ujumbe wa Biblia katika maeneo ya umma, tunaweza kuwapa chapisho linalowafaa. Ili kusitawisha upendezi, unaweza kumpa anwani au namba yako ya simu na kupanga kumrudia, au umwonyeshe tovuti ya jw.org, au umwelekeze kwenye eneo lililo karibu naye ambapo mikutano ya kutaniko hufanywa. Huenda kuwahubiria watu katika maeneo ya umma ikawa njia nzuri ya kupanua huduma yako na utakayofurahia.
13 Hata hivyo, kazi ya Wakristo leo haihusu tu kutangaza habari njema. Ili ufanikiwe kuwasaidia wengine waikubali kweli inayoongoza kwenye uzima, unahitaji kuwarudia tena na tena watu waliopendezwa ili wafanye maendeleo na kuwa Wakristo wakomavu.
KUFANYA ZIARA ZA KURUDIA
14 Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Lakini pia aliwaambia: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha kushika mambo yote niliyowaamuru.” (Mt. 28:19, 20) Unaweza kupata shangwe katika utumishi wa Yehova ukifanya ziara za kurudia. Huenda watu uliowahubiria habari njema wakafurahi ukiwatembelea tena. Unapozungumza nao habari zaidi kuhusu Biblia, unaweza kuimarisha imani yao katika Mungu na kuwasaidia kutambua uhitaji wao wa kiroho. (Mt. 5:3) Ukipanga kurudi wakati unaofaa na ukijitayarisha vizuri, huenda ukaanzisha funzo la Biblia. Unapaswa kuwa na lengo hilo unapofanya ziara za kurudia. Sisi hupanda mbegu ya kweli na vilevile kuitia maji.—1 Kor. 3:6.
15 Huenda ikawa vigumu kwa wengine kufanya ziara za kurudia. Labda umezoea kuhubiri kifupi habari njema na unafurahia kufanya hivyo. Lakini huenda ukaogopa kumrudia mwenye nyumba ili kuendeleza mazungumzo ya Biblia. Matayarisho mazuri yatakusaidia kuwa na ujasiri. Tumia mapendekezo yanayotolewa katika mkutano wa katikati ya juma. Pia, unaweza kupanga kuhubiri na mhubiri mwenye uzoefu ili akusaidie.
KUONGOZA MAFUNZO YA BIBLIA
16 Alipokuwa akizungumza na mtu aliyegeuzwa imani na kuwa Myahudi ambaye alikuwa akisoma Neno la Mungu, mweneza-injili Filipo alimwuliza hivi: “Je, kweli unajua unayosoma?” Mwanamume huyo alijibu: “Kwa kweli, ninawezaje kuyaelewa mtu fulani asiponiongoza?” Masimulizi ya Biblia kwenye Matendo sura ya 8 yanaeleza kwamba Filipo ‘alimtangazia habari njema kumhusu Yesu,’ akianza na andiko ambalo mtu huyo alikuwa akisoma. (Mdo. 8:26-36) Hatujui Filipo alizungumza naye
-