-
“Endelea Kuangalia Huduma Ambayo Uliikubali Katika Bwana”Mnara wa Mlinzi—2008 | Januari 15
-
-
“Endelea Kuangalia Huduma Ambayo Uliikubali Katika Bwana”
“Endelea kuangalia huduma ambayo uliikubali katika Bwana, ili uitimize.”—KOL. 4:17.
1, 2. Wakristo wana wajibu gani kuelekea wanadamu wote?
TUNA wajibu mzito sana kuelekea majirani wetu. Maamuzi ambayo wanafanya sasa yatamaanisha uzima au kifo wakati wa “ile dhiki kuu.” (Ufu. 7:14) Mwandikaji wa kitabu cha Methali alisema hivi kwa mwongozo wa roho: “Wakomboe wale wanaopelekwa kwenye kifo; na uwazuie wale wanaopepesuka wakielekea kuchinjwa.” Ni maneno mazito kama nini! Tunaweza kuwa na hatia ya damu tukikosa kutimiza wajibu wetu wa kuwaonya watu kuhusu uamuzi ulio mbele yao. Kwa kweli, andiko hilo linaendelea kusema hivi: “Ikiwa utasema: ‘Tazama! Hatukujua hili,’ je, yule anayeipima mioyo hatatambua hilo, na yule anayeichunguza nafsi yako mwenyewe hatajua hilo naye hakika hatamlipa mtu wa udongo kulingana na utendaji wake?” Ni wazi kwamba watumishi wa Yehova hawawezi kusema kwamba ‘hawajui’ hatari ambayo watu wanakabili.—Met. 24:11, 12.
2 Yehova anathamini uhai. Anawahimiza watumishi wake wajitahidi kadiri wanavyoweza ili kusaidia kuokoa uhai wa watu wengi iwezekanavyo. Ni lazima kila mhudumu wa Mungu atangaze ujumbe wenye kuokoa uhai ulio katika Neno la Mungu. Kazi yetu ni kama ya mlinzi ambaye anatoa onyo anapoona hatari. Hatutaki damu ya watu wanaokabili hatari ya kuangamia iwe juu ya vichwa vyetu. (Eze. 33:1-7) Kwa hiyo, ni jambo la maana sana tuendelee kujitahidi ‘kulihubiri neno’!—Soma 2 Timotheo 4:1, 2, 5.
3. Funzo hili na makala mbili zinazofuata zitazungumzia mambo gani?
3 Funzo hili litazungumzia jinsi unavyoweza kushinda vipingamizi katika huduma yako ya kuokoa uhai, na pia jinsi unavyoweza kuwasaidia watu wengi zaidi. Funzo linalofuata litazungumzia jinsi unavyoweza kuboresha ufundi wako wa kufundisha kweli zilizo muhimu sana. Makala ya tatu ya funzo itaonyesha matokeo fulani yenye kutia moyo ambayo watangazaji wa Ufalme wanapata ulimwenguni pote. Hata hivyo, kabla ya kuzungumzia habari hizo, ni vizuri tuchunguze tena kwa nini nyakati zetu ni za hatari sana.
Kwa Nini Watu Wengi Hawana Tumaini?
4, 5. Wanadamu wanakumbwa na nini, na watu wengi wanahisi namna gani?
4 Matukio ya ulimwengu yanaonyesha kwamba tunaishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo,” na mwisho uko karibu sana. Wanadamu wanakumbwa na matukio na hali ambazo Yesu na wanafunzi wake walisema zingekuwapo katika “siku za mwisho.” “Maumivu ya taabu,” kutia ndani vita, upungufu wa chakula, matetemeko ya nchi, na misiba mingine inawakumba wanadamu. Uasi-sheria, uchoyo, na mitazamo ya kutomwogopa Mungu imeenea sana. Hata watu ambao wanajitahidi kuishi kupatana na viwango vya Biblia wanakabili “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.”—Mt. 24:3, 6-8, 12; 2 Tim. 3:1-5.
5 Hata hivyo, wanadamu wengi hawajui matukio ya ulimwengu yanamaanisha nini. Kwa sababu hiyo, wanahangaikia usalama wao na wa familia zao. Wengi wanafadhaika sana wanapofiwa na wapendwa wao au wanapopata misiba mingine. Watu hao hawana tumaini kwa sababu hawana ujuzi sahihi kuhusu kwa nini mambo kama hayo yanatukia na suluhisho ni nini.—Efe. 2:12.
6. Kwa nini “Babiloni Mkubwa” ameshindwa kuwasaidia wafuasi wake?
6 “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo, haijawafariji wanadamu. Badala yake, kupitia “divai ya uasherati wake” imefanya watu wengi wayumbe-yumbe na kuvurugika kiroho. Zaidi ya hayo, kama kahaba, dini ya uwongo imewashawishi na kuwaongoza “wafalme wa dunia.” Inatumia mafundisho ya uwongo na mazoea ya kuwasiliana na pepo kuwafanya wanadamu wengi wajitiishe kabisa kwa viongozi wao wa kisiasa. Kwa hiyo, dini ya uwongo imekuwa na nguvu na uvutano, hata hivyo, imekataa kabisa kweli ya kidini.—Ufu. 17:1, 2, 5; 18:23.
7. Wanadamu wengi watapatwa na nini, lakini baadhi yao wanaweza kusaidiwa jinsi gani?
7 Yesu alifundisha kwamba wanadamu wengi wanatembea katika barabara pana ambayo inaongoza kwenye uharibifu. (Mt. 7:13, 14) Watu fulani wako kwenye barabara hiyo pana kwa sababu wameamua kukataa kimakusudi mafundisho ya Biblia, lakini wengine wengi wako kwenye barabara hiyo kwa sababu wamedanganywa, au wako gizani kwa sababu hawajafundishwa na viongozi wao wa kidini mambo ambayo kwa kweli Yehova anataka wafanye. Labda wengine wangebadili maisha yao ikiwa wangeonyeshwa waziwazi sababu za Kimaandiko za kufanya hivyo. Lakini wale ambao wanabaki ndani ya Babiloni Mkubwa na kuendelea kukataa viwango vya Biblia hawataokolewa wakati wa “ile dhiki kuu.”—Ufu. 7:14.
Endelea Kuhubiri “Bila Kuacha”
8, 9. Wakristo wa karne ya kwanza walifanya nini walipokabili upinzani, na kwa nini?
8 Yesu alisema kwamba wanafunzi wake wangehubiri habari njema ya Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Kwa hiyo, Wakristo wa kweli sikuzote wameona kushiriki katika kazi ya kuhubiri kuwa uthibitisho wa ushikamanifu wao kwa Mungu na takwa la msingi la imani yao. Hivyo, wafuasi wa mapema wa Yesu waliendelea kuhubiri hata walipokabili upinzani. Walimtegemea Yehova ili awape nguvu, huku wakimwomba awawezeshe kuendelea “kusema neno [lake] kwa ujasiri wote.” Kwa hiyo, Yehova aliwajaza roho takatifu, nao wakasema neno la Mungu kwa ujasiri.—Mdo. 4:18, 29, 31.
9 Wafuasi wa Yesu walipopingwa kwa jeuri, je, waliyumbayumba katika azimio lao na kuacha kuhubiri? Hawakuacha kamwe. Kazi ya kuhubiri ya mitume iliwaudhi viongozi wa dini ya Kiyahudi, wakawakamata mitume, wakawatisha, na kuwapiga viboko. Hata hivyo, mitume ‘waliendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.’ Walielewa waziwazi kwamba walipaswa ‘kumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’—Mdo. 5:28, 29, 40-42.
10. Wakristo wanakabili majaribu gani leo, lakini mwenendo wao mzuri unaweza kuwa na matokeo gani?
10 Watumishi wengi wa Mungu leo hawajawahi kupigwa viboko wala kutiwa gerezani kwa sababu ya kuhubiri. Hata hivyo, Wakristo wote wa kweli wanakabili majaribu na matatizo mbalimbali. Kwa mfano, dhamiri yako iliyozoezwa na Biblia inaweza kukuchochea ujiendeshe kwa njia isiyopendwa na watu wengi au inayokufanya uonekane kuwa tofauti. Wafanyakazi na wanashule wenzako, au majirani wanaweza kukuona kuwa mtu wa ajabu kwa sababu maamuzi yako yanategemea kanuni za Biblia. Hata hivyo, maoni yao mabaya hayapaswi kukuvunja moyo. Ulimwengu uko katika giza la kiroho, lakini Wakristo wanapaswa ‘kuangaza kama mianga.’ (Flp. 2:15) Huenda watu fulani wenye mioyo minyoofu wataona na kuvutiwa na matendo yako mazuri na kumpa Yehova utukufu.—Soma Mathayo 5:16.
11. (a) Huenda watu fulani wakaitikia jinsi gani kazi ya kuhubiri? (b) Paulo alikabili upinzani wa aina gani, naye alifanya nini?
11 Tunahitaji ujasiri ili kuendelea kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Huenda watu fulani, hata watu wa ukoo, wakakudhihaki au kujaribu kukuvunja moyo kwa njia nyingine. (Mt. 10:36) Mtume Paulo alipigwa kihalisi mara nyingi kwa sababu alitimiza huduma yake kwa uaminifu. Ona jinsi alivyosema kuhusu upinzani huo: “Baada ya sisi kuwa tumeteseka kwanza na kutendewa kwa dharau,” akaandika, “tulijipa ujasiri kwa njia ya Mungu wetu ili kuwaambia ninyi habari njema ya Mungu kwa kupambana sana.” (1 The. 2:2) Bila shaka, haikuwa rahisi kwa Paulo kuendelea kuhubiri habari njema baada ya kukamatwa, kuvuliwa nguo, kupigwa kwa fimbo, na kutupwa gerezani. (Mdo. 16:19-24) Alipata jinsi gani ujasiri wa kuendelea? Tamaa yake kubwa ilikuwa kutimiza kazi ya kuhubiri aliyopewa na Mungu.—1 Kor. 9:16.
12, 13. Watu wengine wana matatizo gani, nao wanajitahidi kukabiliana nayo jinsi gani?
12 Inaweza pia kuwa vigumu kudumisha bidii yetu katika maeneo ambako watu hawapatikani nyumbani kwa urahisi au ambako wengi hawapendezwi na ujumbe wa Ufalme. Tunaweza kufanya nini katika hali kama hizo? Huenda tukahitaji kujipa ujasiri zaidi na kuwahubiria watu kwa njia isiyo rasmi. Tunaweza pia kubadili wakati wetu wa kuhubiri au kuhubiri hasa katika maeneo ambako tunaweza kupata watu wengi.—Linganisha Yoh. 4:7-15; Mdo. 16:13; 17:17.
13 Watu wengi wanakabili matatizo mengine kama vile uzee na magonjwa, ambayo yanaweza kuwazuia kushiriki kwa ukamili zaidi katika kazi ya kuhubiri. Ikiwa unapatwa na matatizo hayo, usivunjike moyo. Yehova anajua udhaifu wako na anathamini yale unayoweza kufanya. (Soma 2 Wakorintho 8:12.) Hata ikiwa unakabili matatizo ya aina gani, iwe ni upinzani, kutopendezwa kwa watu, au magonjwa, wahubirie wengine habari njema kadiri hali zako zinavyokuruhusu.—Met. 3:27; linganisha Marko 12:41-44.
“Endelea Kuangalia Huduma” Yako
14. Mtume Paulo aliwawekea Wakristo wenzake mfano gani, naye alitoa shauri gani?
14 Mtume Paulo aliitimiza huduma yake kwa bidii sana, naye aliwatia moyo waamini wenzake wafanye hivyo. (Mdo. 20:20, 21; 1 Kor. 11:1) Mtu mmoja ambaye Paulo alimtia moyo sana ni Arkipo, Mkristo aliyeishi katika karne ya kwanza. Paulo aliandika hivi katika barua yake kwa Wakolosai: “Mwambieni Arkipo hivi: ‘Endelea kuangalia huduma ambayo uliikubali katika Bwana, ili uitimize.’” (Kol. 4:17) Hatujui Arkipo alikuwa nani au alikabili hali gani, lakini tunajua kwamba aliikubali huduma. Ikiwa wewe ni Mkristo aliyejiweka wakfu, wewe pia umeikubali huduma. Je, unaendelea kuiangalia huduma hiyo ili uitimize?
15. Wakfu wa Mkristo unahusisha nini, na ni maswali gani yanayotokea?
15 Kabla ya kubatizwa, tulisali kutoka moyoni na kuweka wakfu maisha yetu kwa Yehova. Hivyo, tuliazimia kufanya mapenzi yake. Kwa hiyo basi, tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, kweli kufanya mapenzi ya Mungu ndilo jambo la maana zaidi maishani mwangu?’ Huenda tukawa na wajibu mbalimbali ambao Yehova anatutazamia tutimize, kama vile kuandaa mahitaji ya familia yetu. (1 Tim. 5:8) Lakini tunatumia namna gani nguvu na wakati wetu unaobaki? Tunatanguliza nini maishani?—Soma 2 Wakorintho 5:14, 15.
16, 17. Vijana Wakristo au wale ambao hawana madaraka mengi wanaweza kufikiria mapendeleo gani?
16 Je, wewe ni Mkristo kijana aliyejiweka wakfu ambaye amemaliza au anakaribia kumaliza masomo? Inaelekea kwamba kwa sasa huna madaraka mazito ya familia. Basi, unapanga kutumia maisha yako jinsi gani? Ni maamuzi gani ambayo yatakusaidia zaidi kutimiza ahadi yako ya kufanya mapenzi ya Yehova? Vijana wengi wamepanga mambo yao ili wafanye upainia, na wamepata uradhi na shangwe kubwa sana.—Zab. 110:3; Mhu. 12:1.
17 Labda wewe ni kijana. Umeajiriwa kazi ya wakati wote lakini huna madaraka mengi isipokuwa kutimiza mahitaji yako. Bila shaka, unafurahi kushiriki katika utendaji wa kutaniko kadiri hali zako zinavyokuruhusu. Je, unaweza kupata shangwe zaidi? Je, umefikiria kupanua huduma yako? (Zab. 34:8; Met. 10:22) Katika maeneo fulani, bado kuna kazi nyingi ya kumtangazia kila mtu ujumbe wa kweli unaoleta uzima. Je, unaweza kufanya mabadiliko fulani katika maisha yako ili utumike katika eneo lenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme?—Soma 1 Timotheo 6:6-8.
18. Wenzi fulani wa ndoa ambao ni vijana walifanya mabadiliko gani, na matokeo yalikuwa nini?
18 Kwa mfano, mfikirie Kevin na Elena, kutoka Marekani.a Walitaka sana kununua nyumba kama wenzi wengi wa ndoa wanavyofanya katika eneo lao baada ya kufunga ndoa. Wote wawili walifanya kazi ya wakati wote na waliishi maisha ya starehe. Lakini, hawakuwa na wakati wa kutosha wa kushiriki katika utumishi wa shambani kwa sababu ya kazi zao za kuajiriwa na kazi nyingine za nyumbani. Walitambua kwamba walikuwa wakitumia wakati na nguvu nyingi kutunza mali yao. Hata hivyo, Kevin na Elena walipoona maisha rahisi na yenye furaha ya wenzi fulani wa ndoa mapainia, waliamua kubadili mambo wanayotanguliza maishani. Baada ya kutafuta mwongozo wa Yehova kupitia sala, waliuza nyumba yao na kuhamia kwenye nyumba ya kupanga. Elena aliamua kufanya kazi kwa saa chache na akawa painia. Kevin alichochewa na matokeo mazuri ambayo mke wake alikuwa akipata katika huduma, akaacha kazi yake ya wakati wote na akawa painia. Punde si punde, walihamia nchi moja ya Amerika Kusini ili watumike katika eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Kevin anasema hivi: “Ndoa yetu ilikuwa yenye furaha sikuzote, lakini tulipojitahidi kufikia miradi ya kiroho, furaha yetu iliongezeka zaidi.”—Soma Mathayo 6:19-22.
19, 20. Kwa nini kuhubiri habari njema ndiyo kazi ya maana zaidi leo?
19 Kuhubiri habari njema ndiyo kazi ya maana zaidi inayofanywa duniani leo. (Ufu. 14:6, 7) Inachangia kutakaswa kwa jina la Yehova. (Mt. 6:9) Ujumbe wa Biblia unaboresha maisha ya maelfu ya watu ambao wanaukubali kila mwaka, na hilo linaweza kuwaongoza kwenye wokovu. Hata hivyo, “watasikiaje bila mtu wa kuhubiri?” akauliza mtume Paulo. (Rom. 10:14, 15) Kwa kweli watasikiaje tusipohubiri? Kwa nini usiazimie kufanya yote unayoweza ili utimize huduma yako?
20 Njia nyingine ya kuwasaidia watu waelewe umuhimu wa nyakati hizi zenye hatari na matokeo ya maamuzi yao ni kuboresha uwezo wako wa kufundisha. Habari inayofuata itazungumzia jinsi unavyoweza kufanya hivyo.
[Maelezo ya Chini]
a Majina yamebadilishwa.
-
-
Kazia Uangalifu ‘Ufundi Wako wa Kufundisha’Mnara wa Mlinzi—2008 | Januari 15
-
-
Kazia Uangalifu ‘Ufundi Wako wa Kufundisha’
“Lihubiri neno, . . . karipia, kemea, himiza, kwa ustahimilivu wote na ufundi wa kufundisha.”—2 TIM. 4:2.
1. Yesu aliwapa wanafunzi wake amri gani, naye aliweka mfano gani?
HATA ingawa Yesu alifanya kazi nzuri za kuponya katika huduma yake duniani, alijulikana hasa kuwa mwalimu wala si mponyaji au mfanya-miujiza. (Marko 12:19; 13:1) Yesu alitanguliza kazi ya kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu, na ndivyo wafuasi wake wanavyofanya leo. Wakristo wamepewa mgawo wa kuendeleza kazi ya kufanya wanafunzi kwa kuwafundisha watu kushika mambo yote ambayo Yesu aliamuru.—Mt. 28:19, 20.
2. Tunahitaji kufanya nini ili tutimize mgawo wetu wa kuhubiri?
2 Ili kutimiza mgawo wetu wa kufanya wanafunzi, tunajitahidi daima kuboresha ufundi wetu wa kufundisha. Mtume Paulo alikazia umuhimu wa ufundi huo alipomwandikia Timotheo, mhubiri mwenzake. Alisema hivi: “Jiangalie daima wewe mwenyewe na kufundisha kwako. Kaa katika mambo haya, kwa maana kwa kufanya hivyo utajiokoa wewe mwenyewe na wale wanaokusikiliza pia.” (1 Tim. 4: 16) Kufundisha ambako Paulo alikuwa akizungumzia hakukumaanisha tu kumpa mtu ujuzi. Wahudumu Wakristo wenye matokeo wanafikia mioyo ya watu na kuwachochea wafanye mabadiliko katika maisha yao. Huo ni ufundi. Basi tunaweza kusitawisha jinsi gani “ufundi wa kufundisha” tunapowahubiria wengine habari njema ya Ufalme wa Mungu?—2 Tim. 4:2.
Kusitawisha “Ufundi wa Kufundisha”
3, 4. (a) Tunaweza kusitawisha namna gani “ufundi wa kufundisha”? (b) Shule ya Huduma ya Kitheokrasi inatusaidia jinsi gani kuwa walimu wenye matokeo?
3 Kamusi moja inasema “ufundi” ni “ustadi ambao mtu anapata kwa kujifunza, kutumia yale anayojifunza, au kwa kutazama.” Ili tuwe walimu wa habari njema wenye matokeo tunahitaji kukazia uangalifu mambo hayo matatu. Tunaweza kuelewa kwa usahihi habari tunayofundisha ikiwa tu tutajifunza habari hiyo na kusali. (Soma Zaburi 119:27, 34.) Kuwatazama wahudumu wenye matokeo wakifundisha kunatusaidia kujifunza njia zao na kuwaiga. Na kujitahidi kutumia kwa ukawaida yale tunayojifunza kutatusaidia kuboresha ufundi wetu.—Luka 6:40; 1 Tim. 4:13-15.
4 Yehova ni Mfundishaji wetu Mkuu. Kupitia sehemu inayoonekana ya tengenezo lake, anawapa watumishi wake duniani mwongozo wa jinsi wanavyopaswa kutimiza kazi yao ya kuhubiri. (Isa. 30:20, 21) Kwa kusudi hilo, kila kutaniko linakuwa na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kila juma, ambayo imekusudiwa kuwasaidia wote waliojiandikisha katika shule hiyo kuwa watangazaji wenye matokeo wa Ufalme wa Mungu. Kitabu kikuu cha shule hiyo ni Biblia. Neno la Yehova lililoongozwa na roho linatuambia mambo tunayopaswa kufundisha. Zaidi ya hayo, linaonyesha njia za kufundisha zinazofaa na zenye matokeo. Shule ya Huduma ya Kitheokrasi inatukumbusha kwa ukawaida kwamba tutakuwa walimu wenye ustadi zaidi tukitegemea Neno la Mungu tunapofundisha, tukitumia maswali mazuri, tukifundisha kwa njia rahisi, na kupendezwa kikweli na wengine. Acheni tuchunguze kila moja ya mambo hayo. Kisha, tutazungumzia jinsi tunavyoweza kuufikia moyo wa mwanafunzi.
Tegemea Neno la Mungu Unapofundisha
5. Tunapaswa kutegemea nini tunapofundisha, na kwa nini?
5 Yesu, yule mwalimu mkuu zaidi kati ya walimu wote wa kibinadamu, alitegemea Maandiko alipofundisha. (Mt. 21:13; Yoh. 6:45; 8:17) Hakuzungumza kwa jina lake mwenyewe, bali kwa jina la Yule aliyemtuma. (Yoh. 7:16-18) Tunafuata mfano wake. Kwa hiyo, yale tunayosema iwe tunahubiri nyumba kwa nyumba au tunaongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani, yanapaswa kutegemea mamlaka ya Neno la Mungu. (2 Tim. 3:16, 17) Hata tukitoa hoja za werevu jinsi gani hatuwezi kamwe kuwasaidia watu na kuwachochea kwa nguvu kama Maandiko yaliyoongozwa na roho yanavyoweza kuwachochea. Biblia ina mamlaka. Njia nzuri zaidi ya kumsaidia mwanafunzi aelewe jambo lolote lile ni kumwomba asome yale ambayo Maandiko yanasema kuhusu jambo hilo.—Soma Waebrania 4:12.
6. Mwalimu anaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba mwanafunzi anaelewa habari ambayo anajifunza?
6 Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba mwalimu Mkristo hapaswi kujitayarisha kwa ajili ya funzo la Biblia. Kinyume chake, mwalimu anapaswa kuchagua kimbele na kwa uangalifu maandiko yaliyotajwa ambayo yeye au mwanafunzi atasoma katika Biblia wakati wa funzo. Kwa kawaida, ni vizuri kusoma maandiko ambayo ndiyo msingi wa mafundisho yetu. Ni muhimu pia kumsaidia mwanafunzi aelewe maana ya kila andiko analosoma.—1 Kor. 14:8, 9.
Tumia Maswali kwa Ufundi
7. Kwa nini kutumia maswali ni njia nzuri ya kufundisha?
7 Kutumia maswali kwa ufundi kunachochea fikira na kumsaidia mwalimu kuufikia moyo wa mwanafunzi. Kwa hiyo, badala ya kumfafanulia mwanafunzi wako maandiko, mwombe akufafanulie maandiko hayo. Nyakati nyingine swali la ziada au hata maswali kadhaa yanaweza kumsaidia mwanafunzi aelewe vizuri jambo fulani. Unapotumia maswali kumfundisha mwanafunzi, kwa kweli unamsaidia kuelewa sababu za fundisho hilo na pia unamsaidia yeye mwenyewe asadiki fundisho hilo.—Mt. 17:24-26; Luka 10:36, 37.
8. Tunaweza kutambua jinsi gani mambo yaliyo moyoni mwa mwanafunzi?
8 Njia ya kufundisha inayotumiwa katika vitabu vyetu ni ya maswali na majibu. Hapana shaka kwamba watu wengi unaojifunza nao Biblia wataweza kujibu haraka maswali yaliyo katika kitabu wakitumia habari iliyo katika mafungu. Hata hivyo, mwalimu mwenye utambuzi hatatosheka tu na majibu sahihi. Kwa mfano, mwanafunzi anaweza kueleza kwa usahihi yale ambayo Biblia inasema kuhusu uasherati. (1 Kor. 6:18) Hata hivyo, maswali ya maoni yaliyotungwa kwa ustadi yanaweza kufunua maoni ya mwanafunzi kuhusu yale anayojifunza. Mwalimu anaweza kuuliza hivi: “Kwa nini Biblia inakataza mahusiano ya ngono nje ya ndoa? Una maoni gani kuhusu sheria hiyo ya Mungu? Je, unafikiri kwamba kuna faida yoyote ya kuishi kupatana na viwango vya Mungu vya maadili?” Majibu ya mwanafunzi kwa maswali kama hayo yanaweza kufunua mambo yaliyo moyoni mwake.—Soma Mathayo 16:13-17.
Fundisha kwa Njia Rahisi
9. Tunapaswa kukumbuka nini tunapofundisha habari za Kimaandiko?
9 Kwa kadiri fulani kweli nyingi zilizo katika Neno la Mungu ni rahisi kueleweka. Hata hivyo, huenda watu ambao tunajifunza nao Biblia wamevurugwa na mafundisho ya dini ya uwongo. Daraka letu tukiwa walimu ni kuifanya Biblia ieleweke kwa urahisi. Walimu wazuri wanafundisha kwa njia iliyo rahisi, wazi, na sahihi. Tukifuata mwongozo huo, hatutafanya kweli iwe ngumu kueleweka. Epuka habari zisizo za lazima. Hatuhitaji kuzungumzia kila jambo katika andiko tunalosoma. Kazia tu mambo ya maana yanayofafanua jambo mnalozungumzia. Kadiri mwanafunzi anavyofanya maendeleo, ndivyo atakavyoelewa hatua kwa hatua kweli za ndani za Maandiko.—Ebr. 5:13, 14.
10. Ni mambo gani yanayoamua wingi wa habari ambayo mtajifunza wakati wa funzo la Biblia?
10 Tunapaswa kujifunza habari nyingi kadiri gani katika kikao kimoja? Tunahitaji kutumia utambuzi tunapoamua hilo. Uwezo na hali za mwanafunzi na mwalimu zinatofautiana, lakini tunapaswa sikuzote kukumbuka kwamba kusudi letu tukiwa walimu ni kumsaidia mwanafunzi ajenge imani yenye nguvu. Kwa hiyo, tunampa wakati wa kutosha wa kusoma, kuelewa, na kukubali kweli zilizo katika Neno la Mungu. Hatupaswi kuzungumzia habari nyingi kuliko anavyoweza kuelewa. Tunapaswa pia kuhakikisha kwamba funzo linasonga. Mara tu mwanafunzi anapoelewa jambo fulani, tunasonga kwenye jambo linalofuata.—Kol. 2:6, 7.
11. Mfano wa mtume Paulo unatufunza nini kuhusu kufundisha?
11 Mtume Paulo alipozungumza na wapya, alifanya ujumbe wa habari njema ueleweke kwa urahisi. Hata ingawa alikuwa na elimu ya juu, aliepuka kutumia lugha ya wasomi. (Soma 1 Wakorintho 2:1, 2.) Kweli rahisi za Kimaandiko zinawavutia watu wanyoofu na kuwaridhisha. Watu hawahitaji kuwa na elimu ya juu ili waelewe kweli hizo.—Mt. 11:25; Mdo. 4:13; 1 Kor. 1:26, 27.
Wasaidie Wanafunzi Wathamini Mambo Wanayojifunza
12, 13. Ni nini kinachoweza kumchochea mwanafunzi afuate yale anayojifunza? Toa mfano.
12 Ili tuwe na matokeo mazuri, ni lazima mafundisho yetu yaguse moyo wa mwanafunzi. Mwanafunzi anahitaji kuelewa jinsi habari hiyo inavyomhusu yeye binafsi, inavyomletea faida, na jinsi maisha yake yanavyoweza kuwa mazuri zaidi akifuata mwongozo wa Maandiko.—Isa. 48:17, 18.
13 Kwa mfano, huenda tunazungumzia andiko la Waebrania 10:24, 25, ambalo linawatia moyo Wakristo wakusanyike pamoja na waamini wenzao ili watiwe moyo kupitia Maandiko na kufurahia ushirika wenye upendo. Ikiwa mwanafunzi hajaanza kuhudhuria mikutano ya kutaniko, tunaweza kumweleza kwa ufupi jinsi mikutano hiyo inavyofanywa na mambo ambayo yatazungumziwa. Tunaweza kutaja kwamba mikutano ya kutaniko ni sehemu ya ibada yetu na kumwonyesha kwamba inatuletea faida. Kisha tunaweza kumwalika mwanafunzi ahudhurie. Anapaswa kuchochewa kufuata sheria za Kimaandiko kwa sababu anatamani kumtii Yehova, wala si kumpendeza mwalimu wake.—Gal. 6:4, 5.
14, 15. (a) Mwanafunzi wa Biblia anaweza kujifunza nini kumhusu Yehova? (b) Kujua utu wa Mungu kunaweza kumfaidi jinsi gani mwanafunzi wa Biblia?
14 Faida moja ya msingi ambayo wanafunzi wanapata wanapojifunza Biblia na kufuata kanuni zake ni kwamba wanamjua na kumthamini Yehova kibinafsi. (Isa. 42:8) Mbali na kwamba yeye ni Baba mwenye upendo, Muumba, na Mmiliki wa ulimwengu wote, yeye pia anawafunulia utu na uwezo wake wale ambao wanampenda na wanamtumikia. (Soma Kutoka 34:6, 7.) Musa alipokuwa karibu kuongoza taifa la Israeli kutoka utumwani Misri, Yehova alijitambulisha kwa maneno haya: “Nitakuwa kile nitakachokuwa.” (Kut. 3:13-15) Maneno hayo yalimaanisha kwamba Yehova angekuwa chochote kile ambacho angehitaji kuwa ili atimize makusudi yake kuhusiana na watu wake waliochaguliwa. Hivyo, Waisraeli walipata kumjua Yehova akiwa Mwokozi, Shujaa, Mwandalizi, na Mtimizaji wa ahadi na pia walimjua katika njia nyingine nyingi.—Kut. 15:2, 3; 16:2-5; Yos. 23:14.
15 Huenda Yehova asiwasaidie wanafunzi wetu kimuujiza kama alivyomsaidia Musa. Hata hivyo, kadiri wanafunzi wanavyoendelea kukua katika imani na kuthamini zaidi yale wanayojifunza na kuanza kuyatumia, bila shaka, wataona uhitaji wa kumtegemea Yehova ili awape ujasiri, hekima, na mwongozo. Wanapofanya hivyo, wao pia watapata kumjua Yehova akiwa Mshauri mwenye hekima na mwenye kutegemeka, Mlinzi, na Mwandalizi mkarimu wa vitu vyote wanavyohitaji.—Zab. 55:22; 63:7; Met. 3:5, 6.
Pendezwa Kikweli na Mwanafunzi
16. Kwa nini uwezo wa kiasili wa kufundisha si muhimu zaidi ili kuwa mwalimu mwenye matokeo?
16 Ikiwa unahisi kwamba wewe si mwalimu stadi, jipe moyo. Yehova na Yesu wanasimamia programu ya elimu inayoendeshwa ulimwenguni pote leo. (Mdo. 1:7, 8; Ufu. 14:6) Wanaweza kubariki jitihada zetu hivi kwamba maneno yetu yanaweza kuwachochea watu wenye mioyo minyoofu. (Yoh. 6:44) Hata ikiwa mwalimu hana uwezo wa kiasili wa kufundisha, upendo wake wa kutoka moyoni unaweza kuwa na matokeo mazuri sana kwa mwanafunzi. Mtume Paulo alionyesha kwamba alielewa umuhimu wa kuwapenda wanafunzi.—Soma 1 Wathesalonike 2:7, 8.
17. Tunaweza kuonyesha kwa njia gani kwamba tunapendezwa kikweli na kila mwanafunzi wa Biblia?
17 Vivyo hivyo, tunaweza kupendezwa kikweli na kila mwanafunzi wa Biblia tukitumia wakati ili kumfahamu. Tunapozungumzia kanuni za Maandiko pamoja naye, inaelekea kwamba tutaelewa hali zake. Huenda tukaona kwamba tayari anaishi kupatana na mambo fulani ambayo amejifunza katika Biblia. Lakini labda anahitaji kufanya marekebisho fulani katika mambo mengine. Tukimsaidia mwanafunzi kuona kwamba habari tunayozungumzia katika funzo la Biblia inamhusu yeye binafsi, tunaweza kumsaidia kwa upendo awe mwanafunzi wa kweli wa Kristo.
18. Kwa nini ni jambo la maana kusali pamoja na mwanafunzi wetu na kusali kwa ajili yake?
18 Jambo la maana hata zaidi ni kwamba tunaweza kusali pamoja na mwanafunzi wetu na kusali kwa ajili yake. Anapaswa kuona wazi kwamba kusudi letu ni kumsaidia amjue Muumba wake vizuri zaidi, amkaribie zaidi, na kufaidika kwa kufuata mwongozo wa Mungu. (Soma Zaburi 25:4, 5.) Tunaposali ili Yehova abariki jitihada za mwanafunzi za kutumia yale anayojifunza, mwanafunzi ataona umuhimu wa kuwa ‘mtendaji wa neno.’ (Yak. 1:22) Mwanafunzi anaposikiliza sala zetu za kutoka moyoni, yeye pia atajifunza kusali. Ni shangwe kama nini kuwasaidia wanafunzi wa Biblia wasitawishe uhusiano wao pamoja na Yehova!
19. Habari inayofuata itazungumzia jambo gani?
19 Inatia moyo kujua kwamba Mashahidi zaidi ya milioni sita na nusu ulimwenguni pote wanajitahidi sana kusitawisha “ufundi wa kufundisha,” wakiwa na kusudi la kuwasaidia watu wenye mioyo minyoofu washike mambo yote ambayo Yesu aliamuru. Kazi yetu ya kuhubiri ina matokeo gani? Swali hilo litajibiwa katika habari inayofuata.
-
-
Watu Wenye “Mwelekeo Unaofaa” WanaitikiaMnara wa Mlinzi—2008 | Januari 15
-
-
Watu Wenye “Mwelekeo Unaofaa” Wanaitikia
“Wale wote waliokuwa na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele wakawa waamini.”—MDO. 13:48.
1, 2. Wakristo wa mapema walitii jinsi gani unabii wa Yesu wa kwamba habari njema ingehubiriwa katika dunia yote inayokaliwa?
KITABU cha Biblia cha Matendo kina masimulizi yenye kusisimua kuhusu jinsi Wakristo wa mapema walivyotii unabii wa Yesu wa kuhubiri habari njema ya Ufalme katika dunia yote inayokaliwa. (Mt. 24:14) Wahubiri hao wenye bidii waliwawekea kielelezo wote ambao wangekuja baadaye. Kwa sababu ya bidii ya kuhubiri ya wanafunzi wa Yesu huko Yerusalemu, maelfu ya watu, kutia ndani “umati mkubwa wa makuhani,” walijiunga na kutaniko la karne ya kwanza.—Mdo. 2:41; 4:4; 6:7.
2 Wamishonari wa mapema waliwasaidia wengine wengi kukubali Ukristo. Kwa mfano, Filipo alienda Samaria ambako umati ulimsikiliza. (Mdo. 8:5-8) Paulo alisafiri kotekote akiwa na watu mbalimbali ili kuhubiri ujumbe wa Kikristo huko Kipro, maeneo ya Asia Ndogo, Makedonia, Ugiriki, na Italia. Katika majiji ambako alihubiri, umati mkubwa wa Wayahudi na Wagiriki wakawa waamini. (Mdo. 14:1; 16:5; 17:4) Tito alitimiza huduma fulani huko Krete. (Tito 1:5) Petro alihubiri sana huko Babiloni, na kufikia wakati alipoandika barua yake ya kwanza, kati ya mwaka wa 62 na 64 W.K. hivi, kazi ya Wakristo ilijulikana sana huko Ponto, Galatia, Kapadokia, Asia, na Bithinia. (1 Pet. 1:1; 5:13) Zilikuwa nyakati zenye kusisimua kama nini! Wahubiri hao Wakristo wa karne ya kwanza walihubiri kwa bidii sana hivi kwamba maadui wao walidai kwamba walikuwa “wameipindua dunia inayokaliwa.”—Mdo. 17:6; 28:22.
3. Watangazaji wa Ufalme wanapata matokeo gani leo katika kazi yao ya kuhubiri, na matokeo hayo yanakufanya uhisi namna gani?
3 Leo pia, kutaniko la Kikristo limebarikiwa na ongezeko kubwa ajabu. Je, hutiwi moyo unaposoma ripoti ya kila mwaka ya Mashahidi wa Yehova na kuona matokeo yanayopatikana ulimwenguni pote? Je, huchangamki kujua kwamba watangazaji wa Ufalme waliongoza mafunzo ya Biblia zaidi ya milioni sita katika mwaka wa utumishi wa 2007? Kwa kuongezea, hudhurio la Ukumbusho wa kifo cha Yesu Kristo mwaka uliopita linaonyesha kwamba watu milioni kumi hivi ambao si Mashahidi wa Yehova walipendezwa sana na habari njema hivi kwamba walihudhuria mwadhimisho huo muhimu. Hilo linaonyesha kwamba bado kuna kazi nyingi ya kufanya.
4. Ni nani wanaoitikia ujumbe wa Ufalme?
4 Leo, kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, watu ‘wote wenye mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele’ wanaitikia ujumbe wa kweli. (Mdo. 13:48) Yehova anawavuta watu kama hao waje katika tengenezo lake. (Soma Hagai 2:7.) Tunahitaji kudumisha mtazamo gani kuelekea huduma ya Kikristo ili tushiriki kikamili katika kazi hii ya kuwakusanya watu?
Hubiri Bila Ubaguzi
5. Yehova anawakubali watu wa aina gani?
5 Wakristo wa karne ya kwanza walielewa kwamba “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” (Mdo. 10:34, 35) Mtu hawezi kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova asipokuwa na imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu. (Yoh. 3:16, 36) Na ni mapenzi ya Yehova kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Tim. 2:3, 4.
6. Wahubiri wa Ufalme hawapaswi kufanya nini, na kwa nini?
6 Haingefaa watangazaji wa habari njema wawabague watu kwa sababu ya kabila, cheo, sura, dini, au jambo lingine lolote. Tua kidogo na ufikirie jambo hili: Je, huthamini kwamba mtu ambaye alizungumza nawe kwa mara ya kwanza kuhusu kweli za Kimaandiko hakukubagua? Basi, kwa nini ukatae kumpa mtu yeyote ujumbe ambao unaweza kuokoa uhai wake ikiwa atausikiliza?—Soma Mathayo 7:12.
7. Kwa nini hatupaswi kuwahukumu wale tunaowahubiria?
7 Yehova amemweka rasmi Yesu awe Hakimu; kwa hivyo, hatuna haki ya kumhukumu mtu yeyote. Na hilo linafaa kwa sababu tofauti na Yesu, sisi tunaweza kuhukumu tu ‘kulingana na sura inayoonekana kwa macho yetu tu,’ au ‘kulingana tu na jambo lililosikiwa na masikio yetu,’ lakini Yesu anaweza kujua mawazo ya ndani na fikira za moyo.—Isa. 11:1-5; 2 Tim. 4:1.
8, 9. (a) Sauli alikuwa mtu wa aina gani kabla ya kuwa Mkristo? (b) Mfano wa mtume Paulo unapaswa kutufundisha nini?
8 Watu wa malezi mbalimbali wamekuwa watumishi wa Yehova. Mfano mmoja unaojulikana sana ni Sauli wa Tarso, ambaye baadaye aliitwa mtume Paulo. Sauli, ambaye alikuwa Farisayo, aliwapinga vikali Wakristo. Alilitesa kutaniko la Kikristo kwa sababu aliamini kabisa kwamba hawakuwa waabudu wa kweli. (Gal. 1:13) Hakuna mwanadamu yeyote ambaye angefikiri kwamba Sauli angekuwa Mkristo. Hata hivyo, Yesu aliona sifa fulani nzuri katika moyo wa Sauli naye akamchagua ili atimize kazi ya pekee. Kwa hiyo, Sauli akawa kati ya washiriki watendaji na wenye bidii zaidi wa kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza.
9 Mfano wa mtume Paulo unatufundisha nini? Huenda kuna watu ambao wanaonekana wanapinga vikali ujumbe wetu katika eneo letu. Ingawa huenda tukawa na shaka kwamba hawatakuwa kamwe Wakristo wa kweli, tunapaswa kuendelea kujitahidi kuwahubiria. Nyakati nyingine, hata watu ambao wanaonekana kuwa hawapendezwi hata kidogo wanaitikia. Kazi yetu ni kuendelea kuwahubiria wote “bila kuacha.”—Soma Matendo 5:42.
Baraka Zinawangojea Wale Wanaohubiri “Bila Kuacha”
10. Kwa nini hatupaswi kukataa kuwahubiria watu ambao wanaonekana kuwa wenye kutisha? Simulia mambo ya kwenu.
10 Sura ya nje inaweza kudanganya. Kwa mfano, Ignacio,a alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova alipokuwa gerezani katika nchi moja ya Amerika Kusini. Watu walimwogopa kwa sababu alikuwa mjeuri sana. Basi, wafungwa ambao walitengeneza vitu na kuwauzia wafungwa wengine walimtumia Ignacio kukusanya madeni kutoka kwa wale ambao hawakutaka kulipa haraka. Hata hivyo, kadiri Ignacio alivyofanya maendeleo ya kiroho na kutumia mambo aliyokuwa akijifunza, ndivyo mtu huyo aliyekuwa mkatili na mjeuri alivyozidi kuwa mwenye fadhili. Sasa hakuna yeyote anayemtumia kukusanya madeni, hata hivyo, Ignacio ameridhika kwamba kweli za Biblia na roho ya Mungu imebadili utu wake. Pia, anafurahi kwa kuwa wahubiri wa Ufalme ambao walijitahidi kujifunza naye hawakuwa na ubaguzi.
11. Kwa nini tunaendelea kuwatembelea watu?
11 Moja ya sababu zinazofanya tuendelee kuwatembelea watu ambao tayari tumewahubiria habari njema ni kwamba hali na mitazamo yao inaweza kubadilika na kwa kweli inabadilika. Tangu tulipowatembelea mara ya mwisho, huenda wengine wao wamepatwa na ugonjwa mbaya, wamepoteza kazi, au wamefiwa na mpendwa wao. (Soma Mhubiri 9:11.) Matukio ya ulimwengu yanaweza kuwachochea watu wafikirie kwa uzito kuhusu wakati wao ujao. Matukio hayo yanaweza kumfanya mtu ambaye hakupendezwa au hata aliyepinga akubali ujumbe wetu. Hivyo, hatupaswi kukosa kuwahubiria wengine habari njema katika kila nafasi inayofaa.
12. Tunapaswa kuwa na maoni gani kuelekea watu tunaowahubiria, na kwa nini?
12 Inaonekana wanadamu wana mwelekeo wa kuwahukumu na kuwabagua wengine. Lakini Yehova anamkazia uangalifu mtu mmoja-mmoja. Anaona sifa nzuri za kila mtu. (Soma 1 Samweli 16:7.) Tunapaswa kujitahidi kufanya vivyo hivyo katika huduma yetu. Mambo mengi yaliyoonwa yanaonyesha matokeo mazuri ya kuwa na maoni yanayofaa kuelekea watu wote tunaowahubiria.
13, 14. (a) Kwa nini painia mmoja alikuwa na maoni yasiyofaa kumhusu mwanamke aliyekutana naye katika huduma? (b) Tunajifunza nini kutokana na jambo hilo?
13 Dada mmoja painia anayeitwa Sandra, alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba katika kisiwa kimoja cha Karibea alikutana na Ruth, ambaye alikuwa akijishughulisha sana na mashindano fulani. Ruth alishinda mara mbili tuzo la malkia wa taifa wa mashindano hayo. Alipendezwa sana na yale ambayo Sandra alikuwa akimwambia, basi funzo la Biblia likapangwa. Sandra anakumbuka hivi: “Nilipoingia katika nyumba yake, niliona picha kubwa ya Ruth akiwa amevalia mavazi ya mashindano hayo, vilevile niliona vikombe alivyokuwa ameshinda. Nilifikiri kimakosa kwamba mtu aliyekuwa maarufu na aliyejishughulisha sana na mashindano hangependezwa na kweli. Kwa hiyo, nikaacha kumtembelea.”
14 Baada ya muda, Ruth alikuja kwenye Jumba la Ufalme, na mkutano ulipomalizika, alimuuliza Sandra hivi, “Kwa nini uliacha kuja kujifunza na mimi?” Sandra aliomba msamaha naye akapanga kuanza tena kujifunza naye. Ruth alifanya maendeleo haraka, akaondoa picha zake za mashindano ukutani, akaanza kushiriki katika utendaji wote wa kutaniko, kisha akaweka maisha yake wakfu kwa Yehova. Bila shaka, Sandra alitambua kwamba maoni aliyokuwa nayo kumhusu Ruth yalikuwa mabaya.
15, 16. (a) Mhubiri mmoja alipata matokeo gani alipomhubiria mtu wake wa ukoo? (b) Kwa nini hatupaswi kusitasita kumhubiria mtu wa ukoo anayeshikilia sana imani ya kidini?
15 Wahubiri wengi wamepata matokeo mazuri kwa kuwahubiria washiriki wa familia yao wasio waamini, hata ilipofikiriwa kwamba hawangeikubali kweli. Kwa mfano, mfikirie Joyce, dada mmoja Mkristo huko Marekani. Shemeji yake alikuwa amefungwa na kuachiliwa mara nyingi kutoka gerezani tangu akiwa kijana. Joyce anaeleza hivi: “Watu walisema kwamba maisha yake yalikuwa yameharibika kabisa kwa sababu alijishughulisha na dawa za kulevya, alikuwa mwizi, na alifanya mambo mengine mengi mabaya. Hata hivyo, jambo la kushangaza ni kwamba niliendelea kuzungumza naye kweli za Biblia kwa miaka 37.” Jitihada zake za kumsaidia mtu wake wa ukoo kwa subira zilithawabishwa sana mtu huyo alipoamua mwishowe kuanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova na kufanya mabadiliko makubwa katika maisha yake. Hivi karibuni, Shemeji huyo wa Joyce alibatizwa akiwa na umri wa miaka 50 katika kusanyiko la wilaya huko California, Marekani. Joyce anasema hivi: “Nililia kwa shangwe. Ninafurahi sana kwamba sikuchoka kumsaidia!”
16 Huenda ukasitasita kuongea na watu fulani wa ukoo kuhusu kweli za Biblia kwa sababu ya malezi yao. Hata hivyo, Joyce hakusitasita kuongea na shemeji yake. Kwa kweli, mtu anaweza kujua namna gani yale yaliyo katika moyo wa mtu mwingine? Huenda mtu huyo anatafuta kwa unyoofu kweli ya kidini. Kwa hivyo, usimnyime nafasi ya kuipata kweli hiyo.—Soma Methali 3:27.
Kitabu Chenye Matokeo cha Kujifunzia Biblia
17, 18. (a) Ripoti kutoka ulimwenguni pote zinaonyesha nini kuhusu faida za kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? (b) Umepata matokeo gani mazuri kwa kutumia kitabu hicho?
17 Ripoti kutoka nchi nyingi ulimwenguni pote zinaonyesha kwamba watu wengi wenye mioyo minyoofu wanafurahia sana kitabu cha kujifunzia Biblia kinachoitwa Biblia Inafundisha Nini Hasa? Dada painia anayeitwa Penni, huko Marekani, alianzisha mafunzo kadhaa akitumia kitabu hicho. Wawili walikuwa wazee kwa umri na walikuwa washiriki wenye bidii katika makanisa yao. Penni hakujua jinsi ambavyo wangeitikia kweli za Kimaandiko zilizo katika kitabu Biblia Inafundisha. Hata hivyo, anaandika hivi: “Kwa sababu habari imeelezwa kwa njia iliyo wazi, inayopatana na akili, na inayoeleweka kwa urahisi, walikubali haraka kwamba mambo waliyokuwa wakijifunza ni ya kweli. Hawakubisha wala kukasirika.”
18 Pat, mhubiri aliye nchini Uingereza, alianza kujifunza Biblia pamoja na mwanamke ambaye ni mkimbizi kutoka katika nchi moja ya Asia. Mwanamke huyo alilazimika kukimbia kutoka katika nchi yao baada ya mume wake na wanawe kuchukuliwa na askari-jeshi waasi na kutoweka kabisa. Alitishwa kwamba angeuawa, nyumba yake ilikuwa imeteketezwa, naye alikuwa amelalwa kinguvu na genge la wanaume. Mambo yote hayo yalifanya maisha yake yakose kusudi, na mara nyingi alifikiria kujiua. Hata hivyo, kujifunza Biblia kulimpa tumaini. Pat anaandika hivi: “Maelezo na mifano rahisi ya kitabu Biblia Inafundisha ilimgusa moyo sana.” Mwanafunzi huyo alifanya maendeleo ya haraka, akastahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, naye akaomba kubatizwa katika kusanyiko lililofuata. Ni shangwe kama nini kuwasaidia watu wanyoofu kuelewa na kuthamini tumaini linalotolewa na Maandiko!
“Tusife Moyo Katika Kufanya Yaliyo Mema”
19. Kwa nini kazi ya kuhubiri ni muhimu sana?
19 Kazi yetu ya kuhubiri na kufanya wanafunzi inazidi kuwa muhimu sana kadiri siku zinavyopita. Maelfu ya watu wenye mwelekeo unaofaa wanaitikia ujumbe wetu kila mwaka. Lakini, “ile siku kuu ya Yehova iko karibu,” kwa hivyo, wale ambao wanaendelea kukaa katika giza la kiroho ‘wanapepesuka wakielekea kuchinjwa.’—Sef. 1:14; Met. 24:11.
20. Kila mmoja wetu anapaswa kuazimia kufanya nini?
20 Bado tunaweza kuwasaidia watu kama hao. Lakini ili tuwasaidie, ni muhimu tuwaige Wakristo wa karne ya kwanza ambao ‘waliendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.’ (Mdo. 5:42) Fuata mfano wao kwa kuendelea hata unapokabili matatizo. Kazia uangalifu ‘ufundi wako wa kufundisha,’ na uwahubirie watu wote bila ubaguzi! “Tusife moyo katika kufanya yaliyo mema,” kwa kuwa tukiendelea, tutavuna baraka nyingi sana za kukubaliwa na Mungu.—2 Tim. 4:2; soma Wagalatia 6:9.
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
-