-
“Nendeni Mkafanye Wanafunzi”Mnara wa Mlinzi—2004 | Julai 1
-
-
5. (a) Petro alitiije maneno ya Yesu? (b) Petro alibarikiwaje kwa kutii maagizo ya Yesu?
5 Mapema katika huduma yake duniani, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kwa njia yenye kutokeza kwamba kutambua mamlaka yake na kutii amri zake kungewaletea baraka. Pindi moja alimwambia hivi Petro ambaye alikuwa mvuvi: “Vuta mpaka mahali penye kilindi, nanyi mshushe nyavu zenu, mvue.” Petro alikuwa na hakika kwamba hakukuwa na samaki, hivyo akamwambia Yesu: “Mwalimu, tulitaabika usiku wote na hatukupata chochote.” Hata hivyo, Petro aliongeza kusema hivi kwa unyenyekevu: “Lakini nitazishusha nyavu kwa amri yako.” Baada ya kutii amri ya Kristo, Petro alivua “samaki wengi sana.” Akiwa amelemewa na hisia, Petro ‘alianguka magotini pa Yesu, akisema: “Ondoka kwangu, kwa sababu mimi ni mtu mwenye dhambi, Bwana.”’ Lakini Yesu akamjibu: “Acha kuogopa. Tangu sasa na kuendelea utakuwa ukiwavua watu wakiwa hai.” (Luka 5:1-10; Mathayo 4:18) Tunajifunza nini kutokana na masimulizi hayo?
6. (a) Masimulizi kuhusu samaki waliovuliwa kimuujiza yanaonyesha nini kuhusiana na utii ambao Yesu hutaka? (b) Tunaweza kumwigaje Yesu?
6 Yesu aliwapa Petro, Andrea, na mitume wengine mgawo wa “kuwa wavuvi wa watu,” si kabla, bali baada ya kuvua samaki wengi sana isivyo kawaida. (Marko 1:16, 17) Ni wazi kwamba Yesu hakutaka wamtii bila kufikiri. Aliwapa sababu yenye kusadikisha ya kumtii. Kama vile kutii amri ya Yesu ya kutupa nyavu kulivyowawezesha kuvua samaki wengi isivyo kawaida, ndivyo kutii amri ya Yesu ya ‘kuvua watu’ kungetokeza baraka nyingi. Mitume walitii wakiwa na imani kamili. Masimulizi hayo yanamalizia: “Wakazirudisha mashua kwenye nchi kavu, wakaacha kila kitu, wakamfuata.” (Luka 5:11) Leo, tunapowatia wengine moyo washiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi, tunamwiga Yesu. Hatutaki tu watu wafanye yale tunayowaambia, bali sisi huwapa sababu zenye kusadikisha za kutii amri ya Kristo.
-
-
“Nendeni Mkafanye Wanafunzi”Mnara wa Mlinzi—2004 | Julai 1
-
-
9. (a) Masimulizi kuhusu jinsi Petro na mitume wengine walivyovua samaki huonyesha nini kuhusu nia inayofaa ya kumtii Kristo? (b) Ni nini iliyo nia inayofaa ya kumtii Mungu na Kristo leo, na kwa nini?
9 Masimulizi kuhusu kuvuliwa kwa samaki wengi isivyo kawaida yanaonyesha pia umuhimu wa kuwa na nia inayofaa ya kumtii Kristo, yaani, upendo. Petro aliposema, “Ondoka kwangu, kwa sababu mimi ni mtu mwenye dhambi,” Yesu hakuondoka, wala hakumshutumu Petro kwa dhambi yoyote. (Luka 5:8) Yesu hata hakumkemea Petro kwa kumwomba aondoke, bali alimjibu hivi kwa fadhili: “Acha kuogopa.” Ingekuwa nia mbaya kumtii Kristo kwa sababu ya woga usiofaa. Badala yake, Yesu alimwambia Petro kwamba yeye na wenzake wangetumiwa kuwa wavuvi wa watu. Vivyo hivyo, leo hatuogopeshi watu au kuwafanya waone aibu au wahisi wana hatia, ili kuwalazimisha wamtii Kristo. Utii wa nafsi yote unaotegemea upendo kwa Mungu na Kristo ndio tu hufanya moyo wa Yehova ushangilie.—Mathayo 22:37.
-