Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Miujiza ya Yesu—Je, Kweli Ilitukia?
    Mnara wa Mlinzi—2004 | Julai 15
    • Miujiza ya Yesu—Je, Kweli Ilitukia?

      “WATU walimletea [Yesu Kristo] watu wengi walioingiwa na roho waovu; naye akawafukuza hao roho kwa neno moja, naye akawaponya wote waliokuwa na hali mbaya.” (Mathayo 8:16) Yesu ‘aliamka, akaukemea upepo na kuiambia bahari: “Nyamaza, utulie!” Na upepo ukapunguka, kukawa utulivu mkubwa.’ (Marko 4:39) Unayaonaje maneno hayo? Je, unaamini kwamba yanaeleza matukio halisi ya kihistoria, au unayaona kuwa ni hekaya au ni hadithi tu?

      Watu wengi leo wana shaka sana kuhusu ukweli wa miujiza ya Yesu. Inaonekana kwamba habari kuhusu miujiza na maajabu mengine ya kimungu hupuuzwa katika enzi hii ambapo watu wanatumia darubini, hadubini, wanachunguza anga, na kubadili maumbile.

      Wengine huyaona masimulizi kuhusu miujiza kuwa mambo ya kubuniwa au hekaya tu. Kitabu kimoja kinachodai kuchunguza yule Yesu wa “kweli” kinasema kwamba hadithi kuhusu miujiza ya Kristo ni “matangazo tu” ya kuueneza Ukristo.

      Wengine huona miujiza ya Yesu kuwa udanganyifu mtupu. Wakati mwingine, Yesu mwenyewe ndiye hushutumiwa kuwa mdanganyifu. Justin Martyr wa karne ya pili W.K. anasema kwamba wale waliomchambua Yesu “hata walimwita mchawi na mdanganya-watu.” Wengine hudai kwamba Yesu “hakufanya miujiza yake akiwa nabii wa Wayahudi, bali akiwa mchawi aliyezoezwa katika mahekalu ya wapagani.”

      Ni Nini Maana ya Neno “–siowezekana”?

      Huenda ukahisi kwamba kuna sababu kuu inayofanya watu wawe na shaka na kutoamini miujiza. Wao huliona kuwa jambo gumu, hata lisilowezekana, kukubali kwamba miujiza hufanyika kwa nguvu zinazozidi zile za kibinadamu. “Miujiza haitokei kwa vyovyote,” akasema kijana mmoja mwagnostiki (mtu aaminiye kwamba ya Mungu hayawezi kujulikana). Kisha akanukuu maneno ya David Hume, mwanafalsafa Mskoti wa karne ya 18, aliyeandika: “Muujiza huvunja sheria za asili.”

      Hata hivyo, wengi wangekuwa waangalifu sana kusema kwamba jambo fulani lisilo la kawaida haliwezi kutokea. Kichapo The World Book Encyclopedia husema kwamba muujiza ni “tukio lisiloweza kuelezeka kupitia sheria za asili zinazojulikana.” Kulingana na maelezo hayo, miaka mia moja iliyopita wengi wangeziona safari za angani, mawasiliano ya redio, na mitambo ya setilaiti inayoongoza vyombo vya kusafiria kuwa “miujiza.” Kwa kweli, si jambo la hekima kudai kwamba miujiza haiwezekani eti kwa sababu hatuwezi kuieleza kwa kutegemea ujuzi tulio nao sasa.

      Tukichunguza uthibitisho fulani wa Biblia kuhusu miujiza ambayo Yesu Kristo alifanya, tutapata nini? Je, miujiza ya Yesu ilitukia kwa kweli?

  • Miujiza ya Yesu Unaweza Kujifunza Nini?
    Mnara wa Mlinzi—2004 | Julai 15
    • Miujiza ya Yesu Unaweza Kujifunza Nini?

      HUENDA ukashangaa kujua kwamba masimulizi ya Biblia kuhusu maisha ya Yesu duniani hayatumii neno la awali la Kigiriki linalotafsiriwa kuwa “muujiza.” Maana halisi ya neno la Kigiriki (dyʹna·mis), ambalo nyakati nyingine hutafsiriwa kuwa “muujiza,” ni “nguvu.” (Luka 8:46) Linaweza pia kutafsiriwa kuwa “uwezo” au ‘kazi zenye nguvu.’ (Mathayo 11:20; 25:15) Msomi mmoja anasema kwamba, neno hilo la Kigiriki “hukazia tendo kubwa ambalo limetimizwa, na hasa nguvu zilizotumiwa kulitimiza. Tukio hilo huelezwa kuwa wonyesho wa nguvu za Mungu.”

      Neno lingine la Kigiriki, (teʹras), kwa kawaida hutafsiriwa kuwa “maajabu.” (Yohana 4:48; Matendo 2:19) Neno hilo hukazia jinsi ambavyo watazamaji huathiriwa. Mara nyingi umati na wanafunzi walistaajabishwa sana na kazi zenye nguvu za Yesu.—Marko 2:12; 4:41; 6:51; Luka 9:43.

      Neno la tatu la Kigiriki (se·meiʹon) linalorejelea miujiza ya Yesu linamaanisha “ishara ya nguvu kutoka kwa Mungu.” Msomi Robert Deffinbaugh anasema kwamba neno hilo “hukazia maana yenye kina zaidi ya muujiza.” Anaongeza kusema: “Ishara ni muujiza unaoeleza ukweli kuhusu Bwana wetu Yesu.”

      Udanganyifu au Nguvu Kutoka kwa Mungu?

      Biblia haisemi kwamba miujiza ya Yesu ilikuwa ujanja au udanganyifu uliokusudiwa kuwafurahisha watu. Ilikuwa wonyesho wa “nguvu kuu za Mungu,” kama katika kisa cha mvulana ambaye kutoka kwake Yesu alifukuza roho mwovu. (Luka 9:37-43) Je, kazi hizo zenye nguvu zingemshinda Mungu Mweza-Yote—Yule anayetajwa kuwa “hodari katika nguvu”? (Isaya 40:26) La!

      Masimulizi ya Injili hurejelea miujiza ya Yesu ipatayo 35. Lakini hayataji idadi kamili ya miujiza hiyo. Kwa mfano, andiko la Mathayo 14:14 linasema: ‘Yesu aliona umati mkubwa; naye akawasikitikia, akaponya wagonjwa wao.’ Biblia haituelezi aliponya wagonjwa wangapi pindi hiyo.

      Kazi hizo zenye nguvu zilikuwa muhimu kuhusiana na dai la Yesu kwamba alikuwa Mwana wa Mungu, Masihi aliyeahidiwa. Naam, Biblia ilithibitisha kwamba Yesu alifanya miujiza kwa nguvu kutoka kwa Mungu. Mtume Petro alimtaja Yesu kuwa “mwanamume aliyeonyeshwa hadharani na Mungu kwenu kupitia kazi zenye nguvu na mambo ya ajabu na ishara ambazo Mungu alifanya kupitia kwake katikati yenu, kama vile ninyi wenyewe mnavyojua.” (Matendo 2:22) Pindi nyingine Petro alisema kwamba ‘Mungu alimtia Yesu mafuta kwa roho takatifu na nguvu, naye akaenda akipita katika nchi akitenda mema na kuwaponya wote waliokandamizwa na Ibilisi; kwa sababu Mungu alikuwa pamoja naye.’—Matendo 10:37, 38.

      Miujiza ilikuwa muhimu sana katika mafundisho ya Yesu. Andiko la Marko 1:21-27 linaonyesha jinsi watu walivyoitikia mafundisho ya Yesu na mojawapo ya miujiza yake. Andiko la Marko 1:22 linasema kwamba umati ‘ulistaajabia njia yake ya kufundisha,’ nao mstari wa 27 unaonyesha kwamba watu ‘walishangaa’ alipomfukuza roho mwovu. Ujumbe wa Yesu na kazi zake zenye nguvu zilithibitisha kwamba alikuwa Masihi aliyeahidiwa.

      Yesu hakudai tu kwamba yeye ndiye Masihi; bali miujiza aliyofanya kwa nguvu kutoka kwa Mungu, pamoja na maneno na matendo yake mengine, yalithibitisha kwamba alikuwa Masihi. Alipoulizwa kuhusu mamlaka na daraka lake rasmi, Yesu alijibu hivi kwa ujasiri: “Mimi nina ushahidi ulio mkubwa zaidi kuliko ule wa Yohana [Mbatizaji], kwa maana kazi zilezile ambazo Baba yangu alinigawia kutimiza, kazi hizo zenyewe ambazo ninafanya, hutoa ushahidi juu yangu kwamba Baba alinituma.”—Yohana 5:36.

      Uthibitisho Kwamba Miujiza ya Yesu Ilikuwa ya Kweli

      Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba miujiza ya Yesu ilikuwa halisi na ya kweli? Fikiria baadhi ya mambo yanayothibitisha kwamba miujiza hiyo ilikuwa ya kweli.

      Yesu hakuvuta fikira kwake mwenyewe alipofanya kazi zenye nguvu. Alihakikisha kwamba miujiza yoyote aliyofanya ilimletea Mungu sifa na utukufu. Kwa mfano, kabla ya kumponya mtu mmoja kipofu, Yesu alikazia kwamba uponyaji huo ungetukia “ili kazi za Mungu zipate kufunuliwa katika kisa chake.”—Yohana 9:1-3; 11:1-4.

      Tofauti na watu wadanganyifu, wachawi, na wale wanaodai kuponya kwa imani, Yesu hakutumia njia ya kupumbaza akili, ujanja, maonyesho yenye kutazamisha, uchawi, au zile ibada za kuchochea hisia za watu. Hakutumia ushirikina wala vitu vinavyofikiriwa kuwa vitakatifu. Ona jinsi Yesu alivyowaponya watu wawili vipofu bila kujionyesha. Masimulizi yanasema: ‘Yesu aliwasikitikia, akayagusa macho yao, na mara moja wakapata kuona, nao wakamfuata.’ (Mathayo 20:29-34) Hakukuwa na sherehe wala kujionyesha. Yesu alifanya miujiza yake hadharani, mara nyingi mbele ya watazamaji wengi. Hakutumia jukwaa lenye mwangaza au vifaa vingine vya kipekee. Tofauti na miujiza ya Yesu, mara nyingi miujiza ya siku hizi haiwezi kuthibitishwa.—Marko 5:24-29; Luka 7:11-15.

      Nyakati nyingine, Yesu alikiri kwamba wale walionufaika na miujiza yake walikuwa na imani. Lakini ukosefu wa imani wa mtu haukumzuia Yesu kufanya miujiza. Alipokuwa Kapernaumu huko Galilaya, “watu walimletea watu wengi walioingiwa na roho waovu; naye akawafukuza hao roho kwa neno moja, naye akawaponya wote waliokuwa na hali mbaya”—Mathayo 8:16.

      Yesu alifanya miujiza ili kutosheleza mahitaji halisi ya kimwili ya watu, wala si kutosheleza tamaa ya watu wenye udadisi. (Marko 10:46-52; Luka 23:8) Wala hakufanya miujiza ili ajinufaishe kwa njia yoyote ile.—Mathayo 4:2-4; 10:8.

      Namna gani Masimulizi ya Injili?

      Tumepata ukweli kuhusu miujiza ya Yesu kupitia vile vitabu vinne vya Injili. Je, kuna sababu za kutegemea masimulizi hayo tunapochunguza kama miujiza ya Yesu ilikuwa ya kweli? Ndiyo, ziko.

      Kama ambavyo tumeona, miujiza ya Yesu ilifanywa hadharani, mbele ya watazamaji wengi. Vitabu vya mapema kabisa vya Injili viliandikwa wakati ambapo wengi wa watazamaji hao walikuwa hai. Kuhusu unyoofu wa waandikaji wa Injili, kitabu The Miracles and the Resurrection kinasema: “Lingekuwa jambo lisilofaa kabisa kudai kwamba waeneza-injili walitumia miujiza kuficha ukweli wa kihistoria wakiwa na nia ya kuieneza imani yao. . . . Walitaka tu kuandika mambo kwa unyoofu.”

      Wayahudi walioupinga Ukristo hawakutilia shaka kazi zenye nguvu zinazotajwa katika vitabu vya Injili. Walitilia shaka tu chanzo cha nguvu zilizotumiwa kuifanya. (Marko 3:22-26) Hata wachambuzi wa baadaye hawakuweza kukanusha kwamba Yesu alifanya miujiza. Kinyume chake, katika karne ya kwanza na ya pili W.K., miujiza iliyofanywa na Yesu ilitajwa. Ni wazi kwamba tuna kila sababu ya kuyaona masimulizi ya vitabu vya Injili kuhusu miujiza ya Yesu kuwa ya kweli.

      Mtu Aliyefanya Miujiza Hiyo

      Uchunguzi wa miujiza ya Yesu haungekuwa kamili kama tungetaja tu hoja zinazopatana na akili ambazo zinaonyesha kwamba miujiza hiyo ni ya kweli. Vikieleza kazi za Yesu zenye nguvu, vitabu vya Injili humwonyesha kuwa mtu mwenye hisia nyingi na huruma isiyo na kifani, na mwenye kuwajali sana wanadamu wenzake.

      Fikiria kisa cha mkoma mmoja aliyemkaribia Yesu na kumsihi sana hivi: “Ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.” ‘Kwa kumsikitikia,’ Yesu alinyoosha mkono wake na kumshika mkoma huyo na kusema: “Ninataka. Takasika.” Mtu huyo alipona mara moja. (Marko 1:40-42) Hivyo, Yesu alionyesha hisia-mwenzi zilizomchochea kutumia nguvu alizopewa na Mungu kufanya miujiza.

      Ilikuwaje Yesu alipokutana na msafara wa mazishi ukitoka katika jiji la Naini? Kijana huyo aliyekuwa amekufa alikuwa mwana wa pekee wa mjane. ‘Kwa kumsikitikia’ mwanamke huyo, Yesu alimkaribia na kumwambia: “Acha kulia.” Kisha akamfufua mwanaye.—Luka 7:11-15.

      Jambo lenye kufariji tunaloweza kujifunza kutokana na miujiza ya Yesu ni kwamba ‘alisikitika,’ naye akafanya mambo ili kuwasaidia watu. Lakini miujiza hiyo si historia tu. Andiko la Waebrania 13:8 linasema: “Yesu Kristo ni yuleyule jana na leo, na milele.” Kwa kuwa anatawala akiwa Mfalme wa kimbingu sasa, yeye yu tayari na ana uwezo wa kutumia kwa kadiri kubwa zaidi nguvu alizopewa na Mungu za kufanya miujiza, kuliko wakati alipokuwa duniani akiwa mwanadamu. Hivi karibuni, Yesu atatumia nguvu hizo kuwaponya wanadamu watiifu. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia kujifunza mengi kuhusu tazamio hilo zuri la wakati ujao.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki