Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Wamishonari Wasukuma Mpanuko wa Ulimwenguni Pote
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Shule ya Gileadi

      Katikati ya vita ya ulimwengu, huenda lilionekana kuwa jambo lisiloweza kufanya kazi kwa maoni ya kibinadamu kupanga kwa ajili ya mpanuko wa utendaji wa kuhubiri Ufalme katika mashamba ya kigeni. Na bado, katika Septemba 1942, kwa kumtegemea Yehova, waelekezi wa mashirika mawili kati ya mashirika makuu halali yaliyotumiwa na Mashahidi wa Yehova yalikubali pendekezo la N. H. Knorr la kuanzisha shule iliyokusudiwa kuwazoeza wamishonari na wengine kwa ajili ya utumishi maalumu. Ingeitwa Watchtower Bible College of Gilead. Baadaye jina hilo lilibadilishwa likawa Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower. Hakuna pesa za mafunzo zingelipwa, na wanafunzi wangepewa malazi na chakula kwa gharama ya Sosaiti katika kipindi cha mazoezi yao.

      Miongoni mwa wale walioalikwa kusaidia kupanga mtaala wa mafunzo alikuwa Albert D. Schroeder, aliyekuwa tayari amepata ujuzi mwingi katika Idara ya Utumishi kwenye makao makuu ya Sosaiti katika Brooklyn na akiwa mwangalizi wa tawi la Sosaiti katika Uingereza. Mtazamo wake unaofaa, vile alivyojitoa mwenyewe kusaidia wengine, na kupendezwa kwa uchangamfu na wanafunzi kuliwafanya wale aliowafunza wampende wakati wa miaka 17 aliyotumikia akiwa msajili na mfunzi katika shule hiyo. Katika 1974 akawa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, na mwaka uliofuata alipewa mgawo wa kutumikia katika Halmashauri ya Kufundisha yayo.

      Ndugu Schroeder na wafunzi wenzake (Maxwell Friend, Eduardo Keller, na Victor Blackwell) walipanga mtaala wa mafunzo wa miezi mitano uliokazia funzo la Biblia yenyewe na tengenezo la kitheokrasi, pia mafundisho ya Biblia, kusema mbele ya watu, huduma ya shambani, utumishi wa mishonari, historia ya kidini, sheria ya kimungu, jinsi ya kushughulika na maofisa wa serikali, sheria ya kimataifa, kuweka maandishi, na lugha moja ya kigeni. Mtaala umerekebishwa kwa muda wa miaka iliyopita, lakini funzo la Biblia yenyewe na umaana wa kazi ya kueneza evanjeli nyakati zote ni mambo ambayo yamechukua mahali pa kwanza. Kusudi la mtaala huo ni kutia nguvu imani ya wanafunzi, kuwasaidia wasitawishe sifa za kiroho zinazohitajika ili kuweza kushinda magumu ya utumishi wa mishonari. Mkazo umewekwa juu ya umaana wa kumtegemea Yehova kabisa na kuwa na uaminifu-mshikamanifu kwake. (Zab. 146:1-6; Mit. 3:5, 6; Efe. 4:24) Wanafunzi hawapewi majibu yaliyokaririwa kwa kila kitu lakini huzoezwa kufanya utafiti na husaidiwa kuthamini kwa nini Mashahidi wa Yehova huamini yale wanayoamini na kwa nini wao hushikamana na njia fulani za kufanya mambo. Wanajifunza kutambua kanuni wanazoweza kufanya kazi nazo. Hivyo msingi huwekwa kwa ajili ya ukuzi zaidi.

      Mialiko kwa waliotazamiwa kuwa wanafunzi kwa ajili ya darasa la kwanza ilipelekwa Desemba 14, 1942. Ilikuwa ni katikati ya kipupwe wakati wanafunzi 100 waliofanyiza darasa hilo walipojiandikisha kwenye majengo ya shule yaliyoko katika upande wa juu wa jimbo la New York, katika South Lansing. Walikuwa wenye nia, wenye hamu, na kidogo wenye wasiwasi. Ingawa mafunzo ya darasa ndiyo yaliyokuwa hangaiko la mara hiyo, hawangeweza kujizuia kujiuliza ni wapi katika shamba la ulimwengu wangeweza kutumwa baada ya kuhitimu.

      Katika hotuba moja kwa darasa hilo la kwanza katika Februari 1, 1943, siku ya kufungua shule, Ndugu Knorr alisema: “Mnapewa matayarisho zaidi kwa ajili ya kazi inayofanana na ile ya mtume Paulo, Marko, Timotheo, na wengine waliosafiri kwenda sehemu zote za Milki ya Roma wakipiga mbiu ya ujumbe wa Ufalme. Iliwabidi waimarishwe kwa Neno la Mungu. Iliwabidi wawe na ujuzi wa wazi kuhusu makusudi Yake. Katika sehemu nyingi iliwabidi wasimame imara wakiwa peke yao dhidi ya wenye vyeo na wakuu wa ulimwengu huu. Huenda mkapatwa na mambo ayo hayo; na Mungu atakuwa nguvu yenu wakati huo.

      “Kuna sehemu nyingi ambako ushahidi kuhusu Ufalme haujatolewa kwa kadiri kubwa. Watu wanaoishi katika sehemu hizo wamo gizani, wamezuiwa humo na dini. Katika baadhi ya nchi hizo ambako kuna Mashahidi wachache imeonwa kuwa watu wa nia njema huwa tayari kusikiliza na wangejishirikisha na tengenezo la Bwana, ikiwa wangefunzwa ifaavyo. Lazima kuwe na mamia na maelfu zaidi ambao wangeweza kufikiwa ikiwa kungekuwa na wafanyakazi wengi zaidi shambani. Kwa neema ya Bwana, kutakuwa na wengi zaidi.

      “SI kusudi la koleji hii kuwatayarisha kuwa wahudumu walioagizwa rasmi. Nyinyi tayari ni wahudumu na mmekuwa watendaji katika huduma kwa miaka mingi. . . . Mtaala wa mafunzo katika koleji ni kwa kusudi hususa la kuwatayarisha kuwa wahudumu wenye uwezo zaidi katika maeneo ambako mtaenda. . . .

      “Kazi yenu kuu ni ile ya kuhubiri gospeli ya Ufalme nyumba hadi nyumba kama vile Yesu na mitume wake walivyofanya. Mtakapokwisha kupata sikio lenye kusikia, pangeni kufanya ziara ya kurudia, anzeni funzo la nyumbani, na kupanga kampuni [kutaniko] ya watu wote kama hao katika jiji au mji. Si kwamba tu itawapendeza kupanga kampuni, bali ni lazima mwasaidie waelewe Neno, mwaimarishe, mwasemeze pindi kwa pindi, mwasaidie katika mikutano yao ya utumishi na katika mipango yao ya kitengenezo. Watakapokuwa wenye nguvu na waweza kujiendeleza na kuhubiri eneo, mnaweza kuondoka kwenda kwenye jiji jingine ili kupiga mbiu ya Ufalme. Pindi kwa pindi huenda mkahitaji kurudi ili kuwajenga katika imani takatifu zaidi na kuwaimarisha katika mafundisho; kwa hiyo kazi yenu itakuwa ile ya kuchunga ‘kondoo wengine’ wa Bwana, na si kuwaacha. (Yn. 10:16) Kazi yenu halisi ni kuwasaidia watu wa nia njema. Ni lazima mchukue hatua ya kwanza kutimiza mambo, lakini mkitegemea uongozi wa Mungu.”a

      Miezi mitano baadaye washiriki wa darasa hilo la kwanza walikamilisha mazoezi yao maalumu. Wao walipata viza, mipango ya usafiri ikafanywa, na wakaanza kwenda kwenye nchi tisa za Amerika ya Latin. Miezi mitatu baada ya kuhitimu kwao, wamishonari waliozoezwa Gileadi wa kwanza kuondoka Marekani walikuwa njiani kuelekea Kuba. Kufikia 1992, wanafunzi zaidi ya 6,500 kutoka nchi zaidi ya 110 walikuwa wamezoezwa na baadaye wakatumikia katika nchi na vikundi vya visiwa zaidi ya 200.

      Hadi kufikia wakati wa kifo chake miaka 34 baada ya kuanzishwa kwa Shule ya Gileadi, Ndugu Knorr alionyesha kupendezwa sana binafsi na kazi ya wamishonari. Kila muhula wa shule, alikuwa akizuru darasa la wakati huo mara kadhaa kadiri ilivyowezekana, akitoa mihadhara na kuandamana na washiriki wengine wa wafanyakazi wa makao makuu ili kusema na wanafunzi. Baada ya wahitimu wa Gileadi kuanza utumishi wao katika nchi za kigeni, alizuru kibinafsi vikundi vya wamishonari, akawasaidia kutatua matatizo, na kuwapa kitia-moyo kilichohitajiwa. Hesabu ya vikundi vya wamishonari ilipoongezeka, alipanga kuwe na ndugu wengine wanaostahili vizuri wafanye ziara hizo pia, ili kwamba wamishonari wote, hata wawe walitumikia wapi, wangepokea uangalifu wa kibinafsi wa kawaida.

  • Wamishonari Wasukuma Mpanuko wa Ulimwenguni Pote
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • [Picha katika ukurasa wa 526]

      Sherehe za kuhitimu za Gileadi zilikuwa jambo kuu la kiroho

      . . . nyingine kwenye mikusanyiko mikubwa (New York, 1950)

      . . . nyingine kwenye chuo cha shule (ambapo N. H. Knorr anaonyeshwa akisema mbele ya maktaba ya shule, katika 1956)

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki