Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Shule ya Gileadi Miaka 60 ya Mazoezi ya Kimishonari
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Juni 15
    • Wanafunzi Wapokea Maagizo ya Mwisho

      Msemaji wa kwanza katika mfululizo wa hotuba fupifupi, John Larson, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Marekani, alitoa hotuba yenye kuimarisha imani yenye kichwa “Ikiwa Mungu Yuko Upande Wetu, Nani Atakayekuwa Dhidi Yetu?” (Waroma 8:31) Msemaji huyo alieleza msingi wa Biblia utakaowasaidia wanafunzi kuwa na uhakika kamili katika nguvu za Yehova za kuwasaidia kushinda vizuizi vyovyote vinavyoweza kuwakabili katika migawo yao. Akitumia Waroma 8:38, 39, Ndugu Larson aliwahimiza wanafunzi hivi: “Tua ufikirie nguvu ambayo Mungu anatumia kwa niaba yako, na ukumbuke kwamba hakuna chochote kinachoweza kuuzuia upendo wa Yehova kwako.”

      Aliyefuata kwenye programu alikuwa Guy Pierce, mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Alichagua hotuba yenye kichwa “Dumisheni Macho Yenu Yakiwa Yenye Furaha!” (Luka 10:23) Alieleza kwamba furaha ya kweli inatia ndani kumjua Yehova na kuelewa kusudi lake la milele na pia kuona utimizo wa unabii mbalimbali wa Biblia. Popote wanapoenda, wanafunzi wanaweza kuendelea kuwa na furaha ya kweli kwa kudumisha macho yao yakiwa yenye furaha. Ndugu Pierce aliwatia moyo wanafunzi watafakari kwa uzito kuhusu wema wa Yehova na kukaza akili zao na moyo wao katika kufanya mapenzi Yake. (Zaburi 77:12) Kwa kudumisha mtazamo unaofaa, wanafunzi wanaweza kushinda matatizo yoyote yanayoweza kuwapata.

      Kisha wanafunzi wakapokea maneno ya mwisho ya kuwatia moyo kutoka kwa walimu wao wawili waliokuwa wakiwafundisha kila siku. “Je, Unatafuta Utukufu?” akauliza Lawrence Bowen katika kichwa cha hotuba yake. Watu wengi huhusianisha utukufu na sifa, heshima, na umashuhuri wao wenyewe. Hata hivyo, mtunga-zaburi Asafu, alipata kuelewa maana ya utukufu wa kweli, yaani hazina isiyo na kifani ya kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova. (Zaburi 73:24, 25) Wanafunzi waliohitimu walitiwa moyo kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova kwa kuendelea kujifunza zaidi Biblia. Malaika “wanatamani kuchungulia” ndani ya mambo yanayohusu kutimizwa kwa kusudi la Yehova kupitia Kristo. (1 Petro 1:12) Wanataka kujifunza mambo mengi iwezekanavyo kumhusu Baba yao ili waweze kuuonyesha utukufu wake. Kisha msemaji akawahimiza wanafunzi wamtukuze Yehova katika migawo yao ya mishonari kwa kuwasaidia wengine kuipata hazina hiyo yenye thamani isiyo na kifani.

      Mwandikishaji wa shule hiyo, Wallace Liverance, akamalizia mfululizo huo wa kwanza wa hotuba kwa kichwa “Sema Hekima ya Mungu Katika Siri Takatifu.” (1 Wakorintho 2:7) Hekima hiyo ya Mungu ambayo mtume Paulo alizungumza juu yake katika utumishi wake wa mishonari ni nini? Ni njia ya Yehova yenye hekima na nguvu ya kuleta amani na umoja ulimwenguni. Hekima hiyo inamhusu Yesu. Badala ya kuhubiri Injili ya kijamii, mtume Paulo aliwasaidia watu kujua jinsi Mungu atakavyoondoa madhara ya dhambi ya Adamu. (Waefeso 3:8, 9) Msemaji akawatia moyo wasikilizaji wake hivi: “Tumieni pendeleo lenu la utumishi kama alivyofanya Paulo ambaye aliuona mgawo wake wa mishonari kuwa nafasi ya kuwasaidia watu kuona jinsi ambavyo Yehova angetimiza kusudi lake.”

  • Shule ya Gileadi Miaka 60 ya Mazoezi ya Kimishonari
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Juni 15
    • Ndugu Wakomavu Watoa Mashauri

      Shule ilipokuwa ikiendelea, wanafunzi walifaidika kwa kushirikiana na washiriki wa familia ya Betheli ya Marekani. Washiriki wa ofisi ya tawi Robert Ciranko na Robert P. Johnson waliwahoji watumishi kadhaa ambao wamemtumikia Yehova kwa muda mrefu kutia ndani waangalizi wasafirio waliokuwa wakipokea mazoezi ya pekee kwenye Kituo cha Elimu cha Watchtower. Wote waliohojiwa walikuwa wahitimu wa Gileadi ambao wakati fulani walikuwa mishonari. Lilikuwa jambo lenye kutia moyo kwa wanafunzi hao, pamoja na familia na rafiki zao kusikia maneno yenye hekima kutoka kwa wanaume hao wa kiroho wenye ujuzi.

      Waliwashauri hivi: “Endeleeni kuwa na shughuli nyingi iwezekanavyo katika huduma na kutanikoni.” “Msijione kuwa watu bora sana. Kazieni fikira kusudi lenu la kuwa mishonari na kuufanya mgawo wenu kuwa nyumbani kwenu.” Maelezo mengine yalionyesha jinsi ambavyo mazoezi ya Gileadi humwezesha mhudumu kufanya kazi nzuri hata mgawo wake uwe wapi. Baadhi yake ni: “Tulijifunza kushirikiana na kufanya kazi pamoja.” “Shule ilitusaidia kukubali tamaduni mpya.” “Tulifundishwa kutumia Maandiko kwa njia mpya.”

      John E. Barr, mshiriki wa muda mrefu wa Baraza Linaloongoza, alitoa hotuba ya msingi ya programu. Kichwa chake cha kimaandiko kilikuwa “Mvumo Wao Ulitoka Ukaenda Kuingia Katika Dunia Yote.” (Waroma 10:18) Akauliza, Je, watu wa Mungu wameweza kutimiza hilo leo? Bila shaka, ndiyo! Tangu mwaka wa 1881, wasomaji wa gazeti Mnara wa Mlinzi waliulizwa hivi: “Je, unahubiri?” Kisha msemaji akawakumbusha wasikilizaji wote ule mwito wa kihistoria kwenye kusanyiko la mwaka wa 1922 huko Cedar Point, Ohio, Marekani: “Tangazeni Mfalme na Ufalme wake!” Kadiri ambavyo wakati umepita, bidii ya watumishi waaminifu wa Mungu imewachochea kutangaza kweli nzuri za Ufalme kwa mataifa yote. Kwa vichapo na kwa mahubiri, habari njema imewafikia watu duniani pote—ikimletea Yehova utukufu na sifa. Katika hotuba ya mwisho yenye kusisimua, Ndugu Barr aliwahimiza wanafunzi wanaohitimu wafikirie baraka walizo nazo, akisema: “Siku baada ya siku, unaposali kwa Yehova ukiwa katika mgawo wako, mshukuru kutoka moyoni kwa sehemu ambayo umeshiriki katika kutimiza maneno haya, ‘Mvumo wao ulitoka ukaenda kuingia katika dunia yote.’”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki