Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Yesu Kristo—Yule Mmishonari Mkuu Zaidi
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Februari 15
    • Yesu Kristo—Yule Mmishonari Mkuu Zaidi

      “Mimi ni mwakilishi kutoka kwake, na Yeye alinituma.”—YOH. 7:29.

      1, 2. Mmishonari ni nani, na ni nani anayeweza kuitwa Mmishonari mkuu zaidi?

      UNAFIKIRIA nini unaposikia neno “mmishonari”? Watu fulani wanafikiria wamishonari wa dini zinazodai kuwa za Kikristo, ambao wengi wao wanajiingiza katika siasa na shughuli za kiuchumi za nchi ambako wanatumikia. Hata hivyo, ukiwa Shahidi wa Yehova, inaelekea unafikiria wamishonari ambao wanatumwa na Baraza Linaloongoza ili kuhubiri habari njema katika nchi mbalimbali ulimwenguni. (Mt. 24:14) Wamishonari hao wanatumia bila uchoyo wakati na jitihada zao katika kazi nzuri ya kuwasaidia watu wamkaribie Yehova Mungu na hivyo kuwa na uhusiano mzuri pamoja naye.—Yak. 4:8.

      2 Maneno “mmishonari” na “wamishonari” hayapatikani katika maandishi makuu ya Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Hata hivyo, kuhusu Waefeso 4:11, maelezo ya chini katika Biblia ya Marejeo yanaonyesha kwamba neno la Kigiriki linalotafsiriwa “waeneza-injili” linaweza pia kutafsiriwa “wamishonari.” Yehova ndiye Mweneza-injili mkuu, lakini hawezi kuitwa Mmishonari mkuu, kwa sababu hakuwahi kutumwa na mtu yeyote. Lakini Yesu Kristo alisema hivi kuhusu Baba yake wa mbinguni: “Mimi ninamjua, kwa sababu mimi ni mwakilishi kutoka kwake, na Yeye alinituma.” (Yoh. 7:29) Ili kuonyesha kwamba aliupenda sana ulimwengu wa wanadamu, Yehova alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee duniani. (Yoh. 3:16) Yesu anaweza kuitwa Mmishonari mkuu zaidi, Mmishonari bora zaidi, kwa kuwa sababu moja iliyofanya atumwe duniani ilikuwa ‘kutoa ushahidi juu ya ile kweli.’ (Yoh. 18:37) Alifanikiwa kabisa kutangaza habari njema ya Ufalme, na bado tunafaidika na matokeo ya utumishi wake. Kwa mfano, tunaweza kuiga njia zake za kufundisha katika huduma yetu, iwe tunatumwa tukiwa wamishonari au hapana.

      3. Tutachunguza maswali gani?

      3 Daraka la Yesu akiwa mhubiri wa Ufalme linatokeza maswali kama haya: Yesu alipatwa na mambo gani duniani? Kwa nini mafundisho yake yalikuwa na matokeo mazuri? Na kwa nini huduma yake ilifanikiwa?

      Kuwa Tayari Kusaidia Katika Mazingira Mapya

      4-6. Taja mabadiliko fulani ambayo Yesu alikabiliana nayo alipotumwa duniani.

      4 Wamishonari wa siku hizi na Wakristo fulani ambao wanahamia katika maeneo ambako kuna uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme huenda wakahitaji kuishi maisha ya chini sana kuliko yale waliyozoea. Lakini hatuwezi hata kufikiria tofauti kati ya hali za Yesu duniani na zile za mbinguni, ambako aliishi pamoja na Baba yake katikati ya viumbe wa kimalaika ambao walimtumikia Yehova wakiwa na nia nzuri. (Ayu. 38:7) Ilikuwa tofauti kama nini kuwa katikati ya wanadamu wenye dhambi katika ulimwengu mpotovu! (Marko 7:20-23) Yesu hata alivumilia mashindano kati ya wanafunzi wake wa karibu zaidi. (Luka 20:46; 22:24) Bila shaka, alitenda kwa ukamilifu katika kila jambo alilokabili duniani.

      5 Yesu hakuanza kuzungumza kimuujiza lugha ya wanadamu; alianza kujifunza lugha hiyo akiwa mtoto mchanga. Lilikuwa badiliko kubwa kama nini kwa mtu aliyekuwa akiwaongoza malaika mbinguni! Akiwa duniani, Yesu alitumia angalau lugha moja kati ya “lugha za wanadamu.” Lugha hiyo ilikuwa tofauti kabisa na ‘lugha za malaika.’ (1 Kor. 13:1) Hata hivyo, hakuna mwanadamu aliyesema maneno yenye kuvutia kama Yesu.—Luka 4:22.

      6 Fikiria mabadiliko mengine ambayo Mwana wa Mungu alihitaji kukabiliana nayo alipokuja duniani. Ingawa Yesu hakurithi dhambi kutoka kwa Adamu, alikuja kuwa mwanadamu, kama wale ambao baadaye wangekuja kuwa “ndugu” zake au wafuasi wake watiwa-mafuta. (Soma Waebrania 2:17, 18.) Usiku wa mwisho wa maisha yake duniani, Yesu alijizuia kumwomba Baba yake wa mbinguni atume “vikosi zaidi ya kumi na viwili vya malaika.” Lakini fikiria viumbe wa kimalaika ambao alikuwa na mamlaka juu yao akiwa Mikaeli yule Malaika Mkuu! (Mt. 26:53; Yuda 9) Ndiyo, Yesu alifanya miujiza; hata hivyo, yale aliyofanya alipokuwa duniani yalikuwa si kitu yakilinganishwa na yale ambayo angeweza kutimiza huko mbinguni.

      7. Wayahudi walitenda jinsi gani kuhusiana na Sheria?

      7 Kabla ya kuwa mwanadamu, akiwa “Neno,” huenda Yesu alikuwa Msemaji wa Mungu ambaye aliwaongoza Waisraeli nyikani. (Yoh. 1:1; Kut. 23:20-23) Hata hivyo, ‘walipokea Sheria kama ilivyopitishwa na malaika lakini hawakuishika.’ (Mdo. 7:53; Ebr. 2:2, 3) Kwa kweli, viongozi wa dini ya Kiyahudi walishindwa kutambua kusudi la Sheria. Kwa mfano, fikiria sheria kuhusu Sabato. (Soma Marko 3:4-6.) Waandishi na Mafarisayo ‘walipuuza mambo mazito zaidi ya Sheria, yaani, haki na rehema na uaminifu.’ (Mt. 23:23) Hata hivyo, Yesu hakukata tamaa na kuacha kutangaza ile kweli.

      8. Kwa nini Yesu anaweza kutusaidia?

      8 Yesu alikuwa tayari kusaidia. Alichochewa na upendo kuelekea watu na alitaka sana kuwasaidia. Hakupoteza kamwe roho ya kueneza injili. Na kwa sababu ya uaminifu wake kwa Yehova alipokuwa duniani, Yesu alikuja kuwa “mwenye daraka la wokovu wa milele kwa wale wote wanaomtii.” Zaidi ya hayo, “kwa kuwa yeye mwenyewe ameteseka alipokuwa akijaribiwa, anaweza kuwasaidia wale [kama sisi] wanaojaribiwa.”—Ebr. 2:18; 5:8, 9.

      Alizoezwa Vizuri Kuwa Mwalimu

      9, 10. Ni mazoezi ya aina gani ambayo Yesu alipata kabla ya kutumwa duniani?

      9 Leo, kabla ya Wakristo kutumwa wakiwa wamishonari, Baraza Linaloongoza linafanya mipango ili wazoezwe. Je, Yesu Kristo alizoezwa? Ndiyo, lakini hakuhudhuria shule za kirabi kabla ya kutiwa mafuta kwa roho na kuwa Masihi; wala hakufundishwa na mmoja wa viongozi mashuhuri wa kidini. (Yoh. 7:15; linganisha Matendo 22:3.) Basi, kwa nini Yesu alikuwa na sifa za kustahili kufundisha?

      10 Haidhuru Yesu alijifunza nini kutoka kwa mama yake, Maria, na baba yake mlezi, Yosefu, yeye alipata mazoezi yaliyokuwa muhimu zaidi kwa ajili ya huduma kutoka Chanzo cha juu zaidi. Yesu alisema hivi kuhusu mazoezi hayo: “Sijasema kutokana na msukumo wangu mwenyewe, bali Baba mwenyewe aliyenituma amenipa amri kuhusu jambo la kutangaza na la kusema.” (Yoh. 12:49) Ona kwamba Mwana alipewa maagizo hususa kuhusu yale aliyopaswa kufundisha. Kabla ya kuja duniani, bila shaka Yesu alitumia wakati mwingi kusikiliza maagizo ya Baba yake. Je, kuna mazoezi mengine bora kuliko hayo aliyopokea?

      11. Yesu alionyesha kwa kadiri gani mtazamo wa Baba yake kuelekea wanadamu?

      11 Tangu alipoumbwa, Mwana huyo alikuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja na Baba yake. Kabla ya kuwa mwanadamu, Yesu alitambua mtazamo wa Mungu kuelekea wanadamu kwa kuchunguza jinsi Yehova alivyoshughulika nao. Mwana huyo alionyesha upendo kama wa Mungu kuwaelekea wanadamu kwa kadiri kubwa hivi kwamba akiwa hekima inayofananishwa na mtu, angeweza kusema hivi: “Vitu nilivyopenda sana vilihusiana na wana wa binadamu.”—Met. 8:22, 31.

      12, 13. (a) Yesu alijifunza namna gani kwa kuchunguza jinsi Baba yake alivyoshughulika na Waisraeli? (b) Yesu alitumia jinsi gani mazoezi aliyopata?

      12 Pia, mazoezi ambayo Mwana huyo alipata yalitia ndani kuchunguza jinsi Baba yake alivyoshughulikia hali ngumu. Kwa mfano, fikiria jinsi Yehova alivyoshughulika na Waisraeli waasi. Andiko la Nehemia 9:28 linasema hivi: “Mara tu walipopata kupumzika, wakatenda tena mabaya mbele zako [Yehova], nawe ukawaacha mkononi mwa adui zao, ambao waliwakanyagia chini. Kisha wakawa wanarudi na kukulilia wapate msaada, nawe ukasikia kutoka mbinguni kwenyewe na kuwakomboa kulingana na rehema zako nyingi, tena na tena.” Akitumika pamoja na Yehova na akimchunguza, Yesu alisitawisha huruma kama ya Yehova kuwaelekea watu wa eneo lake.—Yoh. 5:19.

      13 Yesu alitumia mazoezi aliyopata kwa kuwashughulikia wanafunzi wake kwa huruma. Usiku kabla ya kifo chake, mitume wote ambao aliwapenda sana ‘walimwacha na kukimbia.’ (Mt. 26:56; Yoh. 13:1) Mtume Petro hata alimkana Kristo mara tatu! Hata hivyo, Yesu alifungua njia ili mitume wamrudie. Alimwambia Petro: “Nimeomba dua kwa ajili yako ili imani yako isififie; na wewe, mara tu utakapokuwa umerudi, watie nguvu ndugu zako.” (Luka 22:32) Israeli la kiroho limejengwa juu ya “mitume na manabii,” na msingi wa mawe wa ukuta wa Yerusalemu Mpya una majina ya mitume waaminifu 12 wa Mwana-Kondoo, Yesu Kristo. Mpaka leo hii, Wakristo watiwa-mafuta pamoja na washiriki wao waliojiweka wakfu, wale “kondoo wengine,” wanasitawi wakiwa tengenezo linalohubiri kuhusu Ufalme chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu na uongozi wa Mwana wake mpendwa.—Efe. 2:20; Yoh. 10:16; Ufu. 21:14.

      Jinsi Yesu Alivyofundisha

      14, 15. Ni katika njia gani mafundisho ya Yesu yalitofautiana na yale ya waandishi na Mafarisayo?

      14 Yesu alitumia jinsi gani mazoezi yake katika kuwafundisha wafuasi wake? Tunaona wazi jinsi njia ya Yesu ya kufundisha ilivyokuwa bora zaidi tunapoilinganisha na ile ya viongozi wa dini ya Kiyahudi. Waandishi na Mafarisayo ‘walilibatilisha neno la Mungu kwa sababu ya mapokeo yao.’ Tofauti na watu hao, mambo ambayo Yesu alisema hayakutokana naye; sikuzote alifundisha neno au ujumbe wa Mungu. (Mt. 15:6; Yoh. 14:10) Tunahitaji pia kufanya hivyo.

      15 Kuna jambo lingine ambalo lilimfanya Yesu awe tofauti kabisa na viongozi wa kidini. Alisema hivi kuhusu waandishi na Mafarisayo: “Mambo yote wanayowaambia ninyi, yafanyeni na kuyashika, lakini msifanye kulingana na matendo yao, kwa maana wao husema lakini hawatendi.” (Mt. 23:3) Yesu aliishi kulingana na mambo aliyofundisha. Acheni tuchunguze mfano mmoja ambao unathibitisha ukweli wa jambo hilo.

      16. Kwa nini ungesema kwamba Yesu aliishi kulingana na maneno yake yaliyo katika Mathayo 6:19-21?

      16 Yesu aliwahimiza wanafunzi wake ‘wajiwekee hazina mbinguni.’ (Soma Mathayo 6:19-21.) Je, Yesu mwenyewe aliishi kulingana na himizo hilo? Ndiyo, kwa kuwa angeweza kusema hivi kwa unyoofu kujihusu: “Mbweha wana mapango na ndege wa mbinguni wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali popote pa kulaza kichwa chake.” (Luka 9:58) Yesu aliishi maisha rahisi. Alijishughulisha hasa na kazi ya kutangaza habari njema ya Ufalme, na alionyesha maana ya kuishi bila mahangaiko yanayotokana na kujiwekea hazina duniani. Yesu alionyesha umuhimu wa kujiwekea hazina mbinguni, “ambako nondo na kutu havili, na ambako wezi hawavunji na kuiba.” Je, unafuata himizo la Yesu la kujiwekea hazina mbinguni?

      Sifa Zilizomfanya Yesu Apendwe na Watu

      17. Ni sifa gani zilizomfanya Yesu awe mweneza-injili asiye na kifani?

      17 Ni sifa gani zilizomfanya Yesu awe mweneza-injili asiye na kifani? Sifa moja ilikuwa mtazamo wake kuelekea watu aliowasaidia. Yesu aliiga sifa nzuri za Yehova kama vile unyenyekevu, upendo, na huruma. Ona jinsi sifa hizo zilivyowavuta watu wengi kwa Yesu.

      18. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Yesu alikuwa mnyenyekevu?

      18 Kwa kukubali mgawo wa kuja duniani, Yesu “alijiondolea mwenyewe hali yake na kuchukua umbo la mtumwa na kuwa kama wanadamu.” (Flp. 2:7) Hilo lilikuwa tendo la unyenyekevu. Zaidi ya hayo, Yesu hakuwadharau watu. Hakuwaambia watu, ‘Nilitoka mbinguni, kwa hiyo mnapaswa kunisikiliza.’ Tofauti na wale waliojitangaza wenyewe kwa uwongo kuwa masihi, Yesu hakujitutumua kwa sababu ya cheo chake cha kuwa Masihi wa kweli. Nyakati nyingine, aliwakataza watu wasiwaambie wengine yeye alikuwa nani au yale aliyokuwa amefanya. (Mt. 12:15-21) Yesu alitaka watu wafanye uamuzi wao wa kumfuata kwa msingi wa yale ambayo walijionea wenyewe. Wanafunzi wake walitiwa moyo kama nini kwa sababu Bwana wao hakuwatazamia wawe kama malaika wakamilifu ambao alishirikiana nao huko mbinguni!

      19, 20. Sifa kama upendo na huruma zilimchochea Yesu jinsi gani kuwasaidia watu?

      19 Pia, Yesu Kristo alionyesha upendo, sifa kuu ya Baba yake wa mbinguni. (1 Yoh. 4:8) Yesu aliwafundisha wasikilizaji wake kwa sababu aliwapenda. Kwa mfano, fikiria hisia zake kumhusu mtawala fulani kijana. (Soma Marko 10:17-22.) Yesu ‘alimpenda’ na alitaka kumsaidia, lakini mtawala huyo kijana hakutaka kuachana na mali zake nyingi ili awe mfuasi wa Kristo.

      20 Sifa nyingine ambayo ilimfanya Yesu apendwe ni huruma. Kama wanadamu wote wasio wakamilifu, wale waliokubali mafundisho yake walikuwa wamelemewa na matatizo. Yesu alijua hilo, hivyo aliwafundisha kwa huruma na pia aliwasikitikia. Kwa mfano: Pindi moja, Yesu na mitume wake walikuwa na shughuli nyingi hivi kwamba hawakupata wakati wa kula chakula. Hata hivyo, Yesu alifanya nini alipoona umati wa watu umekusanyika? “Akawasikitikia, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji. Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi.” (Marko 6:34) Yesu alitambua hali yenye kusikitisha ya watu wa eneo lake naye akajitahidi sana kuwafundisha na kufanya miujiza kwa faida yao. Wengine walivutiwa na sifa zake nzuri, wakachochewa na maneno yake, nao wakawa wanafunzi wake.

      21. Tutachunguza nini katika habari inayofuata?

      21 Tunaweza kujifunza mengi zaidi kuhusu huduma ya Yesu ya kidunia, kama itakavyoonyeshwa na habari inayofuata. Tunaweza kumwiga Yesu Kristo, yule Mmishonari mkuu zaidi, katika njia gani nyingine?

  • Mwige Yule Mmishonari Mkuu Zaidi
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Februari 15
    • Mwige Yule Mmishonari Mkuu Zaidi

      “Iweni waigaji wangu, kama vile mimi nilivyo mwigaji wa Kristo.” —1 KOR. 11:1.

      1. Kwa nini tunapaswa kumwiga Yesu Kristo?

      MTUME PAULO alimwiga yule Mmishonari mkuu zaidi, Yesu Kristo. Pia, Paulo aliwahimiza hivi Wakristo wenzake: “Iweni waigaji wangu, kama vile mimi nilivyo mwigaji wa Kristo.” (1 Kor. 11:1) Baada ya Yesu kuwapa mitume wake somo kuhusu unyenyekevu kwa kuwaosha miguu, aliwaambia hivi: “Niliweka kielelezo kwa ajili yenu, ili, kama vile nilivyowafanyia ninyi, ninyi pia mfanye hivyo.” (Yoh. 13:12-15) Tukiwa Wakristo leo, tuna wajibu wa kumwiga Yesu Kristo kwa maneno na kwa matendo na pia kwa sifa tunazoonyesha.—1 Pet. 2:21.

      2. Hata ingawa hujawekwa rasmi na Baraza Linaloongoza kuwa mmishonari, unaweza kuwa na mtazamo gani?

      2 Katika habari iliyotangulia, tulijifunza kwamba mmishonari ni mtu anayetumwa akiwa mweneza-injili, yaani, mtu anayewapelekea wengine habari njema. Kuhusu jambo hilo, Paulo aliuliza maswali fulani yenye kupendeza. (Soma Waroma 10:11-15.) Ona kwamba mtume huyo aliuliza: “Watasikiaje bila mtu wa kuhubiri?” Kisha, akanukuu maneno haya ya unabii wa Isaya: “Jinsi ilivyo yenye kupendeza miguu ya wale wanaotangaza habari njema ya mambo mema!” (Isa. 52:7) Hata ikiwa hujawekwa rasmi na kutumwa kutumikia ukiwa mmishonari katika nchi ya kigeni, unaweza kuwa na roho ya kueneza-injili, na hivyo kumwiga Yesu ukiwa mtangazaji wa habari njema mwenye bidii. Mwaka jana, wahubiri 6,957,852 wa Ufalme; ‘walifanya kazi ya waeneza-injili’ katika nchi 236.—2 Tim. 4:5.

      “Tumeacha Vitu Vyote na Kukufuata Wewe”

      3, 4. Yesu aliacha nini mbinguni, nasi tunapaswa kufanya nini ili tuwe wafuasi wake?

      3 Ili kutimiza daraka alilopewa duniani, Yesu “alijiondolea mwenyewe hali yake na kuchukua umbo la mtumwa,” na hivyo kuacha maisha na utukufu aliokuwa nao mbinguni. (Flp. 2:7) Hata tukimwiga Kristo kadiri gani, yale tunayofanya hayawezi kulinganishwa na yale ambayo Yesu alifanya alipokuja duniani. Lakini tunaweza kubaki imara tukiwa wafuasi wake, kwa kutotamani mambo tuliyoacha katika ulimwengu wa Shetani.—1 Yoh. 5:19.

      4 Pindi moja, mtume Petro alimwambia Yesu hivi: “Tazama! Tumeacha vitu vyote na kukufuata wewe.” (Mt. 19:27) Petro, Andrea, Yakobo, na Yohana waliacha haraka nyavu zao walipoalikwa wamfuate Yesu. Waliacha kazi yao ya uvuvi na kufanya huduma kuwa kazi yao kuu. Kulingana na simulizi la Injili ya Luka, Petro alisema hivi: “Tazama! Tumeacha vitu vyetu wenyewe na kukufuata wewe.” (Luka 18:28) Wengi wetu hatukuacha “vitu vyetu” vyote ili kumfuata Yesu. Hata hivyo, tulihitaji ‘kujikana wenyewe’ ili kuwa wafuasi wa Kristo na watumishi wa Yehova wenye kujitoa kwa moyo wote. (Mt. 16:24) Hatua hiyo imetuletea baraka nyingi. (Soma Mathayo 19:29.) Kuwa na roho ya kueneza-injili kwa kumwiga Kristo kunaleta shangwe moyoni mwetu, hasa ikiwa tumeshiriki hata kwa kadiri ndogo kumsaidia mtu fulani amkaribie Mungu na Mwana wake mpendwa.

      5. Eleza jambo lililoonwa linaloonyesha uamuzi ambao mhamiaji anaweza kufanya baada ya kujifunza kweli ya Biblia.

      5 Valmir, Mbrazili anayeishi nchini Suriname, alikuwa mchimba-dhahabu. Alikuwa mlevi na aliishi maisha mapotovu kiadili. Pindi moja alipokuwa katika jiji fulani, Mashahidi wa Yehova walianza kujifunza Biblia pamoja naye. Alijifunza kila siku, akafanya mabadiliko makubwa, na muda si muda akabatizwa. Alipoona kwamba kazi yake inamtatiza kuishi kulingana na mafundisho ya Biblia, aliuza biashara yake iliyokuwa yenye faida kubwa naye akarudi Brazili ili kusaidia familia yake kupata hazina za kiroho. Baada ya kujifunza kweli ya Biblia, wahamiaji wengi wanaacha kwa kupenda kazi zao katika nchi zenye utajiri na kurudi katika nchi za kwao ili kuwasaidia kiroho watu wao wa ukoo na wengineo. Kwa kweli, wahubiri hao wa Ufalme wanaonyesha roho ya kueneza-injili.

      6. Tunaweza kufanya nini ikiwa hatuwezi kuhamia katika maeneo ambako kuna uhitaji mkubwa zaidi wa watangazaji wa Ufalme?

      6 Mashahidi wengi wamehamia katika maeneo ambako kuna uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Wengine hata wanatumikia katika nchi za kigeni. Huenda sisi binafsi tusiweze kuhama, lakini tunaweza kumwiga Yesu kwa kufanya sikuzote yote tuwezayo katika huduma.

      Yehova Anatoa Mazoezi Yanayohitajiwa

      7. Ni shule gani zinazowazoeza wale wanaotaka kuboresha uwezo wao wakiwa wahubiri wa Ufalme?

      7 Kama Yesu alivyozoezwa na Baba yake, sisi pia tunaweza kufaidika na elimu ambayo Yehova anatoa sasa. Yesu mwenyewe alisema hivi: “Imeandikwa katika Manabii, ‘Na wote watafundishwa na Yehova.’” (Yoh. 6:45; Isa. 54:13) Leo, kuna shule ambazo zimekusudiwa hasa kututayarisha kuwa wahubiri wa Ufalme. Bila shaka, sote tumefaidika kwa kadiri fulani na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi katika makutaniko yetu. Mapainia wana pendeleo la kuhudhuria Shule ya Utumishi wa Painia. Mapainia wengi wenye uzoefu wamefurahi kuhudhuria shule kwa mara ya pili. Wazee na watumishi wa huduma wamehudhuria Shule ya Huduma ya Ufalme ili kuboresha uwezo wao wa kufundisha na wa kuwatumikia waamini wenzao. Waseja wengi ambao ni wazee na watumishi wa huduma wamehudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma ambayo inawazoeza kuwasaidia wengine katika kazi ya kuhubiri. Na ndugu na dada wengi ambao wamepewa migawo katika nchi za kigeni wamepata mazoezi katika Shule ya Gileadi.

      8. Ndugu fulani wako tayari kudhabihu nini ili wapate mazoezi yanayotolewa na Yehova?

      8 Mashahidi wengi wa Yehova wamefanya mabadiliko ili wahudhurie shule hizo. Ili ahudhurie Shule ya Mazoezi ya Kihuduma huko Kanada, Yugu aliacha kazi yake kwa sababu mkubwa wake alikataa kumpa likizo. “Sijuti kamwe,” Yugu alisema. “Kwa kweli, ikiwa wangenionyesha upendeleo na kunipa likizo, wangenitazamia nibaki daima katika kampuni hiyo ili kuonyesha ushikamanifu wangu. Lakini sasa ninaweza kukubali mgawo wowote kutoka kwa Yehova.” Ili kufaidika na mazoezi yanayotolewa na Mungu, wengi wamekuwa tayari kudhabihu mambo ambayo wakati fulani waliyathamini sana.—Luka 5:28.

      9. Toa mfano unaoonyesha matokeo mazuri ya mafundisho ya Biblia na jitihada za bidii.

      9 Mafundisho ya Biblia na jitihada za bidii zina matokeo mazuri sana. (2 Tim. 3:16, 17) Fikiria kisa cha Saulo huko Guatemala. Alipozaliwa alikuwa na udhaifu fulani wa akili, na mmoja wa walimu wake alimwambia mama yake kwamba hapaswi kumlazimisha mvulana huyo kujifunza kusoma, kwa kuwa kufanya hivyo kutamvunja moyo tu. Saulo aliacha shule bila kujua kusoma. Hata hivyo, Shahidi mmoja alimfundisha Saulo kusoma, akitumia broshua Jitahidi Kusoma na Kuandika. Mwishowe, Saulo akafanya maendeleo hata akaanza kutoa hotuba kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Baadaye, mama ya Saulo alikutana na mwalimu wa Saulo katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba. Aliposikia tu kwamba Saulo alijifunza kusoma, mwalimu huyo alimwomba mama ya Saulo aje naye nyumbani kwake juma lililofuata. Juma lililofuata, mwalimu huyo alimuuliza Saulo, “Leo utanifundisha nini?” Saulo alianza kusoma fungu fulani katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? “Siwezi kuamini kwamba sasa unanifundisha,” akasema mwalimu huyo. Alimkumbatia Saulo huku akibubujikwa na machozi.

      Mafundisho Yanayochochea Moyo

      10. Ni kifaa gani bora tunachotumia kufundishia kweli ya Biblia?

      10 Yesu alitegemeza mafundisho yake juu ya mambo ambayo Yehova alimfundisha moja kwa moja na juu ya maagizo yaliyo katika Neno la Mungu lililoandikwa. (Luka 4:16-21; Yoh. 8:28) Tunamwiga Yesu kwa kufuata mashauri yake na kushikamana na Maandiko. Hivyo, sote tunasema na kufikiri kwa upatano, na hilo linachangia umoja wetu. (1 Kor. 1:10) Tunashukuru kama nini kwamba “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anachapisha vichapo vinavyotegemea Biblia ili kutusaidia kudumisha umoja katika mafundisho yetu na kutimiza kazi yetu tukiwa waeneza-injili! (Mt. 24:45; 28:19, 20) Kimoja cha vichapo hivyo ni kitabu Biblia Inafundisha, ambacho kinapatikana katika lugha 179.

      11. Dada mmoja huko Ethiopia alishinda upinzani jinsi gani akitumia kitabu Biblia Inafundisha?

      11 Kujifunza Maandiko kwa kutumia kitabu Biblia Inafundisha kunaweza hata kubadili mioyo ya wapinzani. Pindi moja, Lula, dada painia huko Ethiopia, alikuwa akiongoza funzo la Biblia wakati mtu wa ukoo wa mwanafunzi wake alipokuja kwa hasira na kusema kwamba hawahitaji kujifunza. Kwa utulivu, Lula alizungumza na mtu huyo akitumia mfano wa pesa bandia ulio katika sura ya 15 ya kitabu Biblia Inafundisha. Mwanamke huyo alitulia na akawaruhusu waendelee kujifunza. Mwanamke huyo alikuja tena wakati wa funzo lililofuata naye akaomba awe na funzo lake binafsi la Biblia, na hata akaomba alipie funzo hilo! Baada ya muda alianza kujifunza mara tatu kwa juma na akafanya maendeleo mazuri ya kiroho.

      12. Toa mfano ili kuonyesha jinsi vijana wanavyoweza kufundisha kweli za Biblia kwa mafanikio.

      12 Vijana wanaweza kuwasaidia wengine kwa kutumia kitabu Biblia Inafundisha. Keanu mwenye umri wa miaka 11 huko Hawaii alipokuwa akisoma kitabu hicho shuleni, mwanafunzi mwenzake alimuuliza, “Kwa nini husherehekei sikukuu?” Keanu alisoma jibu moja kwa moja katika nyongeza yenye kichwa “Je, Tusherehekee Sikukuu?” Kisha, akafungua ukurasa wa yaliyomo wa kitabu hicho na kumuuliza mvulana huyo kichwa ambacho kinampendeza zaidi. Funzo la Biblia likaanzishwa. Mwaka uliopita wa utumishi, Mashahidi wa Yehova waliongoza mafunzo ya Biblia 6,561,426, na wengi wao walikitumia vizuri kitabu Biblia Inafundisha. Je, unatumia kifaa hicho kuongoza mafunzo ya Biblia?

      13. Kujifunza Biblia kunaweza kuwa na uvutano wenye nguvu juu ya watu katika njia gani?

      13 Kujifunza Maandiko kwa kutumia kitabu Biblia Inafundisha kunaweza kuwa na uvutano wenye nguvu juu ya wale wanaotamani kufanya mapenzi ya Mungu. Wenzi wa ndoa ambao ni mapainia wa pekee huko Norway walianzisha funzo la Biblia pamoja na familia moja kutoka Zambia. Wenzi hao wa ndoa kutoka Zambia walikuwa na mabinti watatu na hawakutaka tena kupata mtoto mwingine. Hivyo, wakati mke alipopata mimba, waliamua kuitoa. Siku chache kabla ya kumwona daktari, walijifunza sura yenye kichwa “Maoni ya Mungu Kuhusu Uhai.” Picha ya kitoto ambacho hakijazaliwa iliyo katika sura hiyo iliwagusa moyo sana hivi kwamba wakaamua wasitoe mimba hiyo. Walizidi kufanya maendeleo mazuri ya kiroho na baadaye mtoto wao wa kiume alipozaliwa wakampa jina la ndugu aliyekuwa akijifunza pamoja nao.

      14. Eleza jinsi kuishi kulingana na yale tunayofundisha kunavyoweza kuwa na matokeo mazuri.

      14 Sehemu muhimu ya njia ya Yesu ya kufundisha ni kwamba aliishi kulingana na mambo aliyofundisha. Watu wengi wanavutiwa na mwenendo mzuri wa Mashahidi wa Yehova, ambao wanamwiga Yesu katika jambo hilo. Gari la mfanyabiashara mmoja huko New Zealand lilivunjwa na wezi wakaiba mkoba wake. Aliripoti kisa hicho kwa polisi fulani, naye akamwambia hivi: “Utapata mkoba wako na vitu vilivyomo ikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova ataupata.” Dada mmoja Shahidi aliyekuwa akiwapelekea watu magazeti ya habari aliupata. Alipojulishwa hilo, mwenye mkoba huo alikuja kumwona dada huyo nyumbani kwake. Mfanyabiashara huyo alifurahi alipopata hati yake yenye thamani sana ndani ya mkoba huo. Dada huyo alimwambia, “Ilifaa nirudishe vitu hivi, hasa kwa kuwa mimi ni Shahidi wa Yehova.” Mfanyabiashara huyo alishangaa, huku akikumbuka yale ambayo yule polisi alikuwa amemwambia asubuhi hiyohiyo. Kwa wazi, Wakristo wa kweli wanaishi kulingana na mafundisho ya Biblia na wanamwiga Yesu.—Ebr. 13:18.

      Iga Mtazamo wa Yesu Kuelekea Watu

      15, 16. Tunaweza jinsi gani kuwafanya watu wavutiwe na ujumbe tunaohubiri?

      15 Mtazamo wa Yesu kuelekea watu uliwafanya wavutiwe na ujumbe wake. Kwa mfano, upendo na unyenyekevu wake uliwavutia watu wa hali ya chini. Aliwahurumia wale waliomjia na akawafariji kwa maneno ya fadhili, naye aliwaponya wengi kimwili. (Soma Marko 2:1-5.) Hatuwezi kufanya miujiza, lakini tunaweza kuonyesha upendo, unyenyekevu, na huruma, sifa ambazo zinasaidia kuwavuta watu kwenye kweli.

      16 Painia mmoja wa pekee anayeitwa Tariua alipata matokeo mazuri alipomwonyesha huruma Beere, mwanamume mzee anayeishi kwenye mojawapo ya visiwa vya mbali vya Kiribati huko Pasifiki ya Kusini. Ingawa mwanamume huyo alionyesha kwamba hakutaka kusikiliza, Tariua alitambua kwamba alikuwa amepooza naye akamhurumia. “Je, umewahi kusikia yale ambayo Mungu anaahidi kwa ajili ya watu wagonjwa na wazee?” aliuliza. Kisha, akasoma andiko moja kutoka katika unabii wa Isaya. (Soma Isaya 35:5, 6.) Mwanamume huyo alivutiwa na akasema, “Nimekuwa nikisoma Biblia kwa miaka mingi na nimekuwa nikitembelewa na mmishonari mmoja wa dini yangu kwa miaka mingi, lakini sijawahi kuona hilo katika Biblia.” Beere alianza kujifunza Biblia, na alifanya maendeleo mazuri ya kiroho. Ndiyo, ingawa amepooza sana, yeye sasa amebatizwa, anaongoza kikundi hicho cha mbali, na anaweza kutembea kotekote katika kisiwa hicho ili kuhubiri habari njema.

      Endelea Kumwiga Kristo

      17, 18. (a) Unaweza jinsi gani kuwa mweneza-injili mwenye mafanikio? (b) Wale wanaotimiza huduma yao kwa bidii wataona ukweli wa maneno gani?

      17 Kama inavyoonyeshwa tena na tena na mambo mazuri yaliyoonwa katika mahubiri, tunaweza kuwa waeneza-injili wenye mafanikio ikiwa tutasitawisha na kuonyesha sifa kama za Yesu. Hivyo basi, ni jambo linalofaa kama nini kwamba tumwige Kristo tukiwa waeneza-injili wenye bidii!

      18 Watu fulani walipokuwa wanafunzi wa Yesu katika karne ya kwanza, Petro aliuliza: “Kwa kweli kutakuwa na nini kwa ajili yetu?” Yesu akamjibu: “Kila mtu ambaye ameacha nyumba au ndugu au dada au baba au mama au watoto au mashamba kwa ajili ya jina langu atapokea mara nyingi zaidi naye atarithi uzima wa milele.” (Mt. 19:27-29) Tutaona ukweli wa maneno hayo ikiwa tutaendelea kumwiga Mmishonari mkuu zaidi, Yesu Kristo.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki