Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Moldova
    2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
    • Kwa sababu viongozi wa serikali waliwachukia watu wa Yehova, afisa mmoja wa jeshi la Moldova alimtumia polisi fulani mkuu agizo la serikali lililoidhinishwa Aprili 25, 1925. Agizo hilo lilisema hivi: “Kupatana na Kifungu cha Polisi wa Usalama Na. 17274/925, tuna pendeleo la kukuarifu kwamba Wizara ya Mambo ya Ndani imeamua kupiga marufuku na kukomesha mahubiri ya ‘Wanafunzi wa Biblia,’ na tunataka uchukue hatua zinazohitajika ili kutimiza lengo hilo.”

      Ripoti ambayo ofisi ya Rumania ilituma kwenye makao makuu Oktoba 17, 1927, inaonyesha jinsi upinzani huo wa serikali ulivyowaathiri akina ndugu. Kwa ufupi, ripoti hiyo ilisema kwamba mikutano ya makutaniko ilikuwa imesimamishwa na kukatazwa kila mahali, na ‘mamia ya ndugu walikuwa wamefikishwa mbele ya mahakama za jeshi na za umma.’ Pia ilisema hivi: ‘Ni mikutano michache tu iliyoweza kufanywa katika majira ya kiangazi, kwa kuwa wapelelezi na polisi wa siri walipeleleza makutaniko, na bado wanayapeleleza, hasa makutaniko ya vijijini ambayo ni mengi. Mikutano mingi hufanywa misituni, mahali palipofichika vizuri.’

      Ripoti hiyo ilisema hivi pia: ‘Kazi ya waangalizi wanaosafiri ilikatizwa mwezi wa Machi. Katika mwezi uo huo, waziri wa mambo ya ndani alitoa amri kali kisiri kwamba wahudumu wa wakati wote wakamatwe na wafungwe. Punde si punde, karibu wahudumu wote wa wakati wote walikuwa wamefungwa. Ijapokuwa hatuogopi wala ndugu hawaogopi, kwa kuwa tumepata upinzani tangu kazi ilipoanzishwa katika nchi hii, wakati huu mbinu zao za kukomesha kazi ya kuhubiri ni zenye mafanikio sana hivi kwamba ni vigumu kuhubiri.’

  • Moldova
    2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
    • [Sanduku katika ukurasa wa 83-85]

      Wakristo Waliodumisha Msimamo wa Kutokuwamo

      George Vacarciuc: Ndugu Vacarciuc alilelewa na wazazi waliokuwa Mashahidi wa Yehova. Mnamo Desemba 1942 aliitwa na Wafashisti ajiandikishe katika jeshi. Kwa sababu alikataa kujiunga na jeshi, alifungwa katika chumba chenye giza tititi kwa siku 16 na kupewa chakula kidogo sana. Wenye mamlaka walimwita tena, na bila kumwambia hukumu yake, walimwahidi kwamba hukumu hiyo ingefutwa kama angejiunga na jeshi. Alikataa tena.

      George alihukumiwa kifungo cha miaka 25. Lakini aliachiliwa na jeshi la Sovieti Septemba 25, 1944. Hata hivyo, miezi miwili haikupita na Wasovieti wakajaribu tena kumwandikisha jeshini. Kwa sababu hakukubali kutenda kinyume cha dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia, alihukumiwa kifungo cha miaka kumi katika kambi mbalimbali za kazi ngumu. Kwa muda wa mwaka mmoja, familia yake haikujua mahali alipokuwa. Baada ya miaka mitano, Ndugu Vacarciuc aliachiliwa Desemba 5, 1949. Alirudi nyumbani huko Corjeuţi na aliendelea kuwa mwaminifu hadi kifo chake Machi 12, 1980.

      Parfin Goreacioc: Ndugu Goreacioc alizaliwa mwaka wa 1900, na alijifunza kweli ya Biblia katika kijiji cha Hlina kati ya mwaka wa 1925 na 1927. Yeye na ndugu zake, Nicolae na Ion, walifundishwa kweli na Damian na Alexandru Roşu, Wanafunzi wa Biblia wa kwanza katika kijiji hicho.

      Parfin na Mashahidi wengine walikamatwa mwaka wa 1933 na kupelekwa hadi mji wa Khotin, ambako walihojiwa na kutozwa faini kwa sababu ya kuhubiri. Katika mwaka wa 1939, kwa sababu ya uchochezi wa kasisi wa kijiji, Parfin alipelekwa kwenye kituo cha polisi katika kijiji jirani cha Ghilavăţ. Polisi walimlaza kifudifudi kwenye kitanda cha mbao, wakamfunga, na kumpiga tena na tena kwenye nyayo.

      Wafashisti walipotwaa mamlaka, Parfin alikamatwa tena na kupelekwa gerezani. Hata hivyo, mwaka uo huo, Wasovieti walimweka huru, lakini muda mfupi baadaye walimkamata tena kwa sababu alikataa kujiunga na jeshi. Alifungwa Chisinau kwa miezi kadhaa kisha akaachiliwa.

      Wasovieti walimkamata Parfin tena mwaka wa 1947, na kumhukumia adhabu ya uhamisho wa miaka minane kwa sababu ya kuhubiri juu ya Ufalme wa Mungu. Watoto wake walihamishwa hadi Siberia mwaka wa 1951. Lakini hawakujiunga na baba yao wala hawakumwona tena kamwe. Parfin akawa mgonjwa sana alipokuwa uhamishoni na alidumisha uaminifu wake hadi kifo chake mwaka wa 1953.

      Vasile Pădureţ: Ndugu Pădureţ alizaliwa mwaka wa 1920 katika kijiji cha Corjeuţi, na alijifunza kweli mwaka wa 1941 chini ya utawala wa Wafashisti. Kwa hiyo, yeye pia aliteswa na Wafashisti na Wasovieti. Aliwaambia Wasovieti hivi kwa ujasiri: “Sikuwapiga risasi Wakomunisti wala sitawaua Wafashisti.”

      Vasile alihukumiwa kifungo cha miaka kumi katika kambi ya kazi ngumu huko Urusi kwa sababu aliongozwa na dhamiri yake kuchukua msimamo huo unaopatana na Biblia. Hata hivyo, kifungo hicho kilipunguzwa na baada ya miaka mitano, Agosti 5, 1949, alirudi nyumbani. Alipokamatwa kwa mara ya tatu mpango wa kuwahamisha Mashahidi hadi Siberia ulikuwa umeanzishwa. Kwa hiyo, Aprili 1, 1951, Vasile na familia yake walipanda gari-moshi kwenda Siberia. Baada ya kukaa huko kwa miaka mitano, waliruhusiwa kurudi Corjeuţi, Moldova. Vasile alikuwa mwaminifu hadi kifo chake, Julai 6, 2002, wakati masimulizi haya yalipokuwa yakiandikwa.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 89, 90]

      ‘Singebadilisha Utumishi Wangu kwa Chochote Kile’

      Ion Sava Ursoi

      Alizaliwa: 1920

      Alibatizwa: 1943

      Maisha yake: Alitumikia kama mwangalizi wa mzunguko wakati wa utawala wa Wakomunisti.

      Nilizaliwa Caracuşeni, Moldova, na nilijifunza kweli kabla ya Vita vya Pili vya Ulimwengu. Mke wangu alikufa mwaka wa 1942. Wakati wa mazishi yake watu wenye ghasia walinifukuza kutoka makaburini. Kwa nini? Kwa sababu nilikuwa nimeacha dini yangu. Baadaye katika mwaka huo, serikali ya Kifashisti ilijaribu kuniandikisha jeshini. Lakini kwa sababu sikutaka kuunga mkono siasa, nilikataa. Nilihukumiwa kifo, lakini hukumu hiyo ilibadilishwa kuwa kifungo cha miaka 25. Nilihamishwa kutoka kambi moja hadi nyingine. Jeshi la Sovieti lilituweka huru nilipokuwa gerezani huko Craiova, Rumania.

      Lakini mara tu baada ya kuachiliwa, Wakomunisti walinifunga gerezani tena. Walinipeleka Kalinin, Urusi. Miaka miwili baadaye, katika mwaka wa 1946, waliniruhusu kurudi nyumbani, ambako nilisaidia kupanga upya kazi ya kuhubiri. Kisha Wasovieti walinikamata tena mwaka wa 1951. Wakati huu walinihamisha hadi Siberia pamoja na Mashahidi wengine wengi. Sikurudi nyumbani hadi mwaka wa 1969.

      Ninapofikiria maisha yangu, ninakumbuka pindi nyingi ambapo Yehova alinipa nguvu ya kudumisha uaminifu wangu. Singebadilisha utumishi wangu kwa Muumba kwa chochote kile ulimwenguni. Sasa ninapambana na matatizo ya afya na uzee. Lakini tumaini langu thabiti la kuishi katika ulimwengu mpya, wakati mwili wangu utakapokuwa na nguvu za ujana tena, huimarisha azimio langu la kuendelea “kufanya yaliyo mema.”—Gal. 6:9.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 100-102]

      Nina Sababu Nyingi za Kuimba

      Alexandra Cordon

      Alizaliwa: 1929

      Alibatizwa: 1957

      Maisha yake: Alikabili magumu chini ya utawala wa Sovieti na kwa sasa yeye ni mhubiri wa habari njema.

      Ninapenda sana kuimba na jambo hilo lilinisaidia kupata kweli, na baadaye, liliniimarisha kiroho imani yangu ilipojaribiwa. Nilipokuwa kijana katika miaka ya 1940, nilipata kuwajua vijana fulani huko Corjeuţi waliofurahia kuimba nyimbo za Ufalme na kuzungumzia Biblia walipokuwa na nafasi. Kweli za kiroho nilizojifunza katika mazungumzo hayo na katika nyimbo tulizoimba zilinivutia sana.

      Muda si muda, nikawa mhubiri wa habari njema. Mwaka wa 1953, mimi na Mashahidi wengine kumi tulikamatwa kwa sababu ya kuhubiri habari njema. Nilifungwa katika gereza moja huko Chisinau nikingoja kufikishwa mahakamani. Nilidumisha nguvu yangu ya kiroho kwa kuimba nyimbo za Ufalme, jambo ambalo lilimkasirisha askari mmoja. Alisema hivi: “Uko gerezani. Haifai kuimba hapa!”

      Nilimjibu hivi: “Nimeimba maisha yangu yote. Kwa nini niache sasa? Unaweza kunifunga gerezani, lakini huwezi kuifunga midomo yangu kwa kufuli. Moyo wangu u huru, nami nampenda Yehova. Kwa hiyo nina sababu nyingi za kuimba.”

      Nilihukumiwa kifungo cha miaka 25 katika kambi ya kazi ngumu huko Inta karibu na Mzingo wa Aktiki. Katika miezi michache ya kiangazi, mimi na Mashahidi wengine tulifanya kazi msituni. Wakati huo pia, nyimbo za Ufalme ambazo tulijua, zilitusaidia kuwa wenye nguvu kiroho na kuhisi moyoni kwamba tulikuwa huru. Zaidi ya hayo, tofauti na yule askari huko Chisinau, askari huko Inta walitutia moyo tuimbe.

      Nilikaa katika kambi ya Inta kwa miaka mitatu, miezi mitatu, na siku tatu. Kisha, msamaha ulitolewa na nikaachiliwa. Nilienda Tomsk, Urusi, kwa sababu sikuruhusiwa kurudi Moldova. Huko niliungana tena na mume wangu ambaye pia alikuwa amefungwa kwa kipindi fulani. Tulikuwa tumetengana kwa miaka minne.

      Kwa sababu ya kukamatwa, sikuweza kubatizwa ili kuonyesha kwamba nimejiweka wakfu kwa Yehova. Hivyo, niliwauliza ndugu huko Tomsk kuhusu jambo hilo. Kwa kuwa wengine pia walitaka kubatizwa, mara moja ndugu walipanga kuwe na ubatizo. Hata hivyo, kwa sababu ya marufuku, waliamua kufanya ubatizo huo usiku katika ziwa lililokuwa katika msitu wa karibu.

      Wakati uliopangwa ulipowadia, tuliondoka katika viunga vya Tomsk na kuingia msituni tukiwa wawili-wawili ili mpango wetu usigunduliwe. Watu walipaswa kufuatana wawili-wawili hadi wafike salama kwenye ziwa. Hivyo ndivyo ilivyopangwa. Lakini, dada wawili wazee waliotutangulia mimi na mwenzangu walipotea njia. Sisi tuliwafuata, na kama ilivyopangwa wale waliokuwa nyuma yetu wakatufuata. Punde, mimi, mwenzangu, na watu wengine wanane hivi tulipotea msituni. Tulilowa kabisa kwa sababu ya unyevu vichakani na tulitetemeka kwa baridi. Tulihofia kwamba tungekutana na dubu au mbwa-mwitu ambao wanapatikana katika eneo hilo. Tulikuwa na wasiwasi sana hivi kwamba tulishtuka kila tuliposikia sauti fulani.

      Nilitambua kwamba ingekuwa hatari kushikwa na hofu au kukata tamaa, kwa hiyo, nilipendekeza tusimame tuli na kupiga mbinja ya wimbo wa Ufalme, huenda wale wengine wangetusikia. Tulisali pia kwa moyo wote. Wazia furaha yetu tuliposikia sauti ya wimbo uleule ikitufikia polepole katika msitu huo wenye giza! Naam, ndugu zetu walikuwa wamesikia wimbo wetu! Mara moja waliwasha tochi ili tujue mahali walipokuwa. Baada ya muda mfupi, tulizamishwa katika maji baridi sana ziwani, lakini tulifurahi sana hivi kwamba hata hatukusikia baridi.

      Sasa nina umri wa miaka 74 na nimerudi Corjeuţi, ambako nilikuwa nimejifunza kweli. Licha ya uzee, bado ninaimba mara nyingi, hasa ili kumsifu Baba yetu wa mbinguni.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 104-106]

      Nilijitahidi Kuwaiga Wazazi Wangu

      Vasile Ursu

      Alizaliwa: 1927

      Alibatizwa: 1941

      Maisha yake: Alikuwa msimamizi wa kutaniko na alifanya kazi ya kuchapa vitabu kisiri.

      Wazazi wangu, Simeon na Maria Ursu, walibatizwa mwaka wa 1929. Kati ya watoto wao watano, mimi ndiye mkubwa. Wakati wa utawala wa Wafashisti, Baba na Mama walikamatwa na kuhukumiwa kifungo cha miaka 25 katika kambi ya kazi ngumu kwa sababu hawakuunga mkono siasa. Ndugu na dada wa kiroho wa kutaniko la Corjeuţi walitutunza sisi watoto na walilima shamba la familia yetu. Kwa hiyo hatukukosa chakula kamwe. Nyanya yetu mzee, ambaye hakuwa Shahidi, alisaidia pia kututunza. Nilikuwa na umri wa miaka 14 wakati huo.

      Kwa sababu ya mfano mzuri wa wazazi wangu, nilijitahidi sana kuwasaidia ndugu na dada zangu kiroho. Hivyo, niliwaamsha mapema kila asubuhi ili tujifunze sehemu fulani katika kitabu kinachozungumzia Biblia. Hawakufurahi nilipowaamsha, lakini sikuwaruhusu kuendelea kulala. Nilitambua umuhimu wa kujifunza kwa ukawaida. Kwa hiyo, wazazi wetu walipoachiliwa na kurudi nyumbani mwaka wa 1944, walifurahi kuona kwamba hali yetu ya kiroho ilikuwa nzuri. Tulifurahi sana wazazi wetu waliporudi! Lakini furaha yetu haikudumu.

      Mwaka uliofuata, Wasovieti walimkamata Baba na kumfunga huko Norilsk, Siberia, kaskazini mwa Mzingo wa Aktiki. Miaka mitatu baadaye, nilimwoa Emilia, dada mchangamfu aliyependa mambo ya kiroho. Nilimjua Emilia vizuri sana tangu utotoni. Mwaka mmoja tu baada ya arusi yetu, mimi na mama yangu tulikamatwa. Tulipelekwa Chisinau, ambako tulihukumiwa kifungo cha miaka 25 katika kambi ya kazi ngumu. Emilia aliwatunza kwa upendo ndugu na dada zangu ambao sasa walikuwa wamenyang’anywa wazazi wao na kaka yao.

      Hatimaye nikapelekwa Vorkuta ili kufanya kazi katika migodi ya makaa. Kambi hiyo ya kazi ngumu iliyokuwa kaskazini mwa Mzingo wa Aktiki ilijulikana kuwa mbaya sana. Miaka miwili baadaye, mwaka wa 1951, Emilia, ndugu zangu watatu, na dada yangu mmoja walihamishwa hadi Tomsk, magharibi mwa Siberia. Mwaka wa 1955, Emilia aliomba ahamishwe hadi Vorkuta ili aungane nami. Alipokuwa huko alijifungua mtoto wa kike ambaye tulimwita Tamara. Baadaye tulipata watoto wengine wawili.

      Msamaha ulitangazwa mnamo Septemba 1957, na tukaachiliwa. Lakini mwezi mmoja baadaye nilikamatwa tena. Nilihukumiwa kifungo cha miaka saba katika kambi ya kazi ngumu huko Mordvinia, karibu na Saransk, Urusi. Ndugu wengine wengi walifungwa huko pia, na wengine walikuja baadaye. Wake wetu walipokuja kututembelea, walituletea kisiri magazeti na vitabu kwa ukawaida. Tulithamini sana jambo hilo. Mnamo Desemba 1957, Emilia alihamia Kurgan, magharibi mwa Siberia, ili amtunze binti yetu, Tamara, aliyekuwa anakaa na wazazi wa Emilia. Kwa sababu hiyo, mimi na Emilia tulitengana kwa miaka saba. Hatukuwa na njia nyingine ya kuzuia Tamara asipelekwe kwenye shule ya serikali.

      Niliachiliwa mwaka wa 1964, lakini sikuruhusiwa kurudi nyumbani Moldova. Ijapokuwa sikuweza kusafiri kwa uhuru, niliweza kujiunga na mke wangu na binti yangu huko Kurgan, ambako nilitumikia kama kiongozi wa funzo la kitabu kutanikoni. Mwaka wa 1969, tulihamia Krasnodar katika Milima ya Kaukasus. Baada ya kutumikia huko kwa miaka minane, tukahamia Chirchik, Uzbekistan. Huko nilifanya kazi ya kuchapa vitabu kisiri. Hatimaye, tuliruhusiwa kurudi Moldova mwaka wa 1984. Tulihamia jiji la Tighina lenye wakazi 160,000 na wahubiri 18 tu. Tangu wakati huo idadi hiyo imeongezeka na sasa kuna makutaniko tisa na karibu wahubiri na mapainia 1,000 katika mji huo.

      Je, ninajuta kwamba nilikaa miaka mingi katika kambi za kazi ngumu na magereza kwa ajili ya Bwana? Hata kidogo! Nilipobatizwa nikiwa kijana mwenye umri wa miaka 14, tayari nilielewa waziwazi masuala yaliyohusika: ama unampenda Mungu ama unaupenda ulimwengu! Kwa sababu nilikuwa nimeamua kumtumikia Yehova, sikufikiria kamwe kuvunja uaminifu wangu.—Yak. 4:4.

      [Picha]

      Kushoto: Vasile Ursu

      Kushoto kabisa: Vasile na mke wake Emilia, na binti yake, Tamara

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki