Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Moldova
    2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
    • Majaribu Makali Chini ya Utawala wa Wafashisti

      Punde si punde, serikali ya Kifashisti ya Antonescu, iliyoshirikiana na Hitler na muungano wa Ujerumani, Italia, na Japani, ilijaribu kuvunja uaminifu wa Mashahidi wa Yehova kwa kutumia nguvu. Fikiria kisa cha Anton Pântea aliyezaliwa mwaka wa 1919. Anton alijifunza kweli alipokuwa kijana na alikuwa na bidii katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Alikuwa karibu kupigwa mara kadhaa, lakini aliepuka jambo hilo kwa muda kwa kutetea kijasiri haki ya kusema juu ya imani yake akiwa raia wa Rumania. Hata hivyo, hatimaye polisi walimkamata. Maafisa Wafashisti walimburuta hadi kwenye kituo cha polisi, wakampiga usiku kucha, kisha, wakamwachilia. Ndugu Pântea ana umri wa miaka 84 sasa na bado ameazimia kumtumikia Yehova kwa uaminifu.

      Mtu mwingine mwaminifu ni Parfin Palamarciuc aliyejifunza kweli ya Biblia huko Moldova katika miaka ya 1920. Yeye pia alikuwa mtangazaji mwenye bidii wa habari njema. Mara nyingi, alihubiri katika miji na vijiji kuanzia Chernovtsy hadi Lvov huko Ukrainia bila kurudi nyumbani kwa majuma kadhaa. Kwa sababu Parfin alikataa kujiunga na jeshi, Wafashisti walimkamata mwaka wa 1942 na kumfikisha mbele ya mahakama ya jeshi huko Chernovtsy.

      Nicolae, mwana wa Parfin, alisema hivi juu ya matukio hayo: “Ndugu 100 walihukumiwa kifo katika mahakama hiyo. Walikuwa wauawe mara moja baada ya kuhukumiwa. Maafisa waliwakusanya ndugu hao na kuwachagua ndugu kumi ambao wangepigwa risasi kwanza. Lakini hao kumi walilazimishwa kuchimba kwanza makaburi yao, huku wale wengine 90 wakitazama. Lakini kabla ya kuwapiga risasi, maafisa waliwapa nafasi nyingine kukana imani yao na kujiunga na jeshi. Wawili walikana imani; wanane wakapigwa risasi. Kisha wengine kumi wakapangwa katika mstari. Lakini kabla ya kupigwa risasi walilazimishwa kuwazika waliouawa.

      “Ndugu walipokuwa wakifukia makaburi, afisa mmoja wa cheo cha juu aliwasili. Aliuliza ni Mashahidi wangapi waliokana imani. Alipoambiwa ni wawili tu, alisema kwamba kama watu 80 wangehitaji kufa ili 20 wajiunge na jeshi, basi ni afadhali wale 92 waliobaki wapelekwe kufanya kazi katika kambi. Kwa hiyo, hukumu ya kifo ilibadilishwa kuwa kifungo cha miaka 25 katika kambi ya kazi ngumu. Hata hivyo, yapata miaka mitatu baadaye, jeshi la Sovieti liliwaweka Mashahidi huru kutoka katika kambi za Rumania. Baba yangu aliokoka magumu hayo na mengine mengi. Alikuwa mwaminifu kwa Yehova hadi kifo chake mwaka wa 1984.”

      Je, Ni Kosa Kukataa Desturi za Kanisa la Othodoksi?

      Vasile Gherman alikuwa kijana, na mke wake alikuwa amejifungua mtoto wa kike wakati Wafashisti walipomkamata Vasile mnamo Desemba 1942. Vasile alishtakiwa kwa “makosa” mawili, kukataa kujiunga na jeshi na pia kukataa binti yake abatizwe katika Kanisa la Othodoksi. Anasema hivi kuhusu kesi hiyo: “Kesi yangu na kesi za ndugu wengine waaminifu 69 zilisikilizwa katika mahakama ya jeshi huko Chernovtsy Februari 1943. Kabla ya kuhukumiwa, wenye mamlaka walitulazimisha kutazama wahalifu sita wakiuawa. Kwa hiyo, tulikuwa na hakika kwamba tungehukumiwa kifo.

      “Tulizungumzia jambo hilo na kuazimia kusimama imara katika imani na kujitahidi sana kudumisha shangwe hadi kesi imalizike. Kwa msaada wa Yehova tulifaulu. Kama tulivyotarajia, sisi sote 70 tulihukumiwa kifo, tulihisi kwamba tulikuwa tukiteswa kwa ajili ya uadilifu. Hakuna hata mmoja kati yetu aliyevunjika moyo, na jambo hilo liliwaudhi sana adui zetu. Lakini jambo la kushangaza ni kwamba badala ya kutupiga risasi, wenye mamlaka walibadili hukumu yetu kuwa kifungo cha miaka 25 katika kambi ya kazi ngumu huko Aiud, Rumania. Lakini baada ya miezi 18 tu, mnamo Agosti 1944, jeshi la Wasovieti liliwaweka huru wafungwa waliokuwa katika kambi hiyo.”

      Mwaka wa 1942, Wafashisti waliwaandikisha watu 800 hivi kutoka kijiji cha Şirăuţi, Moldova, katika jeshi la Jenerali Antonescu. Kati yao kulikuwa na Mashahidi kadhaa kutia ndani Nicolae Anischevici. Nicolae anasema hivi: “Walipokuwa wakituandikisha, polisi walituamuru tushiriki katika sherehe fulani ya kidini. Sisi Mashahidi tulikataa. Tulikataa pia kubeba silaha. Kwa hiyo, polisi walitushutumu kuwa Wakomunisti na wakatukamata. Hata hivyo kabla ya kutufunga, walituruhusu kueleza sababu ya kutojiunga na jeshi.

      “Kesho yake tulihamishwa hadi Briceni, kitovu cha mahakama ya wilaya hiyo. Tulivuliwa mavazi yote na miili yetu ikachunguzwa kabisa. Kisha kasisi mwenye cheo cha juu jeshini akatuhoji. Alikuwa mwenye fadhili, alielewa kwamba uamuzi wetu ulitegemea dhamiri, na alipanga tupewe chakula. Na zaidi ya hayo, aliandika kwamba tulikataa kujiunga na jeshi kwa sababu tunamwamini Yesu.

      “Kutoka Briceni tulipelekwa hadi kwenye kituo cha polisi huko Lipcani. Huko, polisi walitupiga kikatili hadi usiku. Kisha wakatufunga katika chumba fulani pamoja na ndugu wengine wawili na mwanamke mmoja. Baadaye tuligundua kwamba mwanamke huyo alikuwa mpelelezi. Tulipigwa kila siku, kwa siku kadhaa. Hatimaye, mimi nilipelekwa Chernovtsy ili nihukumiwe katika mahakama ya jeshi. Nilipewa wakili ambaye alinisaidia sana nikiwa huko. Hata hivyo, afya yangu ilikuwa imezorota sana kwa sababu ya mateso hivi kwamba wakuu wa jeshi walifikiri ningekufa. Mwishowe waliamua kunipeleka nyumbani bila kunihukumu.”

      Dada Jasiri Wadumisha Uaminifu

      Dada pia walikabili mateso kwa sababu ya hasira ya Wafashisti. Mmojawapo ni Maria Gherman (yeye si mtu wa ukoo wa Vasile Gherman lakini walikuwa katika kutaniko moja). Maria alipokamatwa mwaka wa 1943, alipelekwa kwenye kituo cha polisi huko Balasineşti. Anasema hivi: “Polisi walinikamata kwa sababu nilikataa kwenda katika kanisa la Othodoksi. Kwanza walinihamisha hadi Lipcani, Moldova, kisha nikapelekwa Chernovtsy, Ukrainia, ambako nilihukumiwa.

      “Hakimu aliniuliza kwa nini nilikataa kwenda kanisani. Nilimwambia kwamba ninamwabudu Yehova tu. Mimi na dada wengine 20 tulihukumiwa kifungo cha miaka 20 kwa sababu ya ‘kosa’ hilo. Baadhi yetu tuliingizwa kwenye chumba kidogo sana pamoja na wafungwa wengine 30. Hata hivyo, mchana nilifanya kazi katika nyumba za matajiri. Watu hao walinitendea vizuri kuliko maafisa wa gereza, angalau walinipa chakula cha kutosha!

      “Baada ya muda, tulifaulu kuwasiliana na ndugu waliokuwa katika sehemu nyingine ya gereza. Jambo hilo lilileta faida nyingi kwa kuwa tuliweza kuwasaidia ndugu kupata chakula cha kiroho na cha kimwili pia.”

      Mara tu baada ya mateso ya Wafashisti kukoma, ndugu hao waaminifu pamoja na Mashahidi wengine wengi huko Moldova, walikabili shambulizi lingine la imani yao chini ya serikali ya Kikomunisti ya Urusi iliyotawala eneo hilo baada ya Wafashisti.

      Mbinu ya Wasovieti ya Kuwahamisha Watu

      Ujerumani ilipoelekea kushindwa vitani, baadhi ya maafisa wa serikali ya Rumania iliyoongozwa na Mfalme Michael, walipindua serikali ya Antonescu mwaka wa 1944. Kisha Rumania ilivunja uhusiano wake na muungano wa Ujerumani, Italia, na Japani na ikajiunga na Urusi. Mwaka uo huo, jeshi la Sovieti lilitwaa tena eneo hilo, kwa hiyo, Moldova ikawa tena sehemu ya Muungano wa Sovieti, na kuitwa SSR ya Moldavia.

      Mwanzoni, watawala Wakomunisti wa Moldova hawakuwanyanyasa Mashahidi wa Yehova. Lakini amani hiyo haikudumu kwa muda mrefu. Punde msimamo wa Kikristo wa kutounga mkono mambo ya siasa ulipingwa vikali tena, kutia ndani msimamo wa Mashahidi wa kukataa kupiga kura katika uchaguzi wa chama. Chini ya utawala wa Sovieti, kutounga mkono siasa hakukubaliwa hata kidogo. Kwa hiyo, serikali ilinuia kutatua tatizo hilo kwa kuwahamisha Mashahidi wa Yehova na watu wengine “wasiotakiwa” kuanzia mwaka wa 1949.

      “Uamuzi uliofanywa na Baraza Kuu la Chama cha Wakomunisti” kuwahusu watu kutoka SSR ya Moldavia ambao wangehamishwa ulionyeshwa katika hati fulani rasmi. Baadhi ya watu hao walikuwa “wamiliki wa mashamba, wenye biashara kubwa, watu walioshirikiana na wavamizi Wajerumani, wale waliowasaidia polisi wa Ujerumani na Rumania, wanachama wa vyama na mashirika ya Wafashisti, shirika fulani la Wafinland lisilokuwa la Kisoshalisti, waumini wa madhehebu yasiyo halali, na pia familia za watu hao wote.” Wote hao walipaswa kupelekwa magharibi mwa Siberia hadi “wakati usiojulikana.”

      Uhamisho mwingine ulianza mwaka wa 1951, lakini wakati huo ni Mashahidi wa Yehova pekee waliohamishwa. Stalin mwenyewe aliagiza uhamisho huo ulioitwa Operation North. Zaidi ya familia 720 za Mashahidi, yaani, watu 2,600 hivi, walihamishwa kutoka Moldova hadi Tomsk, magharibi mwa Siberia, umbali wa kilometa 4,500 kutoka Moldova.

      Maagizo ya serikali yalisema kwamba watu walipaswa kupewa nafasi ya kutosha kufunga virago vyao kabla ya kupelekwa kwenye magari-moshi. Na zaidi ya hayo, mabehewa yalikuwa “yatengenezwe vizuri ili yafae kuwasafirisha wanadamu.” Lakini maagizo hayo hayakutiwa maanani.

      Kwa kawaida, wanajeshi na maafisa wanane hivi walifika nyumbani kwa Mashahidi usiku wa manane. Waliwaamsha na kuwaonyesha barua ya uhamisho. Waliwapa saa chache tu kufunga virago vyao kabla ya kuwapeleka kwenye magari-moshi.

      Walisafirishwa kwa mabehewa ya mizigo. Watu 40 hivi walisongamana katika kila behewa kwa majuma mawili ya safari. Hakukuwa na viti na baridi iliingia kwenye mabehewa. Katika pembe moja ya behewa kulikuwa na shimo sakafuni ambalo lilitumiwa kama choo. Kabla ya kuwahamisha ndugu, maafisa walipaswa kuandika orodha ya mali za kila mtu. Hata hivyo, mara nyingi waliorodhesha tu vitu duni; vitu vyenye thamani “vilipotea” tu.

      Hata hivyo, licha ya magumu yaliyowapata, ndugu hawakupoteza furaha yao ya Kikristo. Magari-moshi yaliyowasafirisha Mashahidi yalipofika kwenye vituo vya gari-moshi, sauti za nyimbo za Ufalme zilisikika kutoka ndani ya mabehewa. Hivyo, ndugu katika kila gari-moshi walijua kwamba hawakuwa peke yao, bali walikuwa wakihamishwa pamoja na mamia ya Mashahidi wenzao. Kuwaona wengine wakidumisha furaha katika hali hizo ngumu kuliwatia moyo na kuwaimarisha wote wadumishe uaminifu wao kwa Yehova katika hali yoyote ile.—Yak. 1:2.

      Imani Inayostahili Kuigwa

      Ivan Mikitkov ni mmojawapo wa watu wa Moldova waliopelekwa uhamishoni Siberia. Ivan alikamatwa kwa mara ya kwanza huko Moldova pamoja na Mashahidi wengine mwaka wa 1951, na kupelekwa uhamishoni Tomsk. Alipewa kazi ya kukata miti katika msitu mkubwa wa Siberia unaoitwa taiga. Ingawa hakuishi katika kambi ya kazi ngumu, bado alikuwa chini ya vizuizi, na polisi wa siri walipeleleza utendaji wake wote. Hata hivyo, yeye na ndugu zake wa kiroho waliwahubiria wengine kila walipopata nafasi.

      Ivan anasema hivi: “Tulipanga kuwe na makutaniko katika mazingira hayo magumu. Hata tulianza kunakili vitabu. Muda si muda, watu kadhaa ambao tuliwahubiria walikubali kweli na kubatizwa. Lakini, hatimaye wenye mamlaka walitambua utendaji wetu na wakapeleka baadhi yetu kwenye kambi za kazi ngumu.

      “Mimi na Mashahidi wenzangu Pavel Dandara, Mina Goraş, na Vasile Şarban, tulihukumiwa kifungo cha miaka 12 katika kambi ya kazi ngumu chini ya usimamizi mkali. Wenye mamlaka walifikiri kwamba vifungo hivyo vikali vingewatisha wengine wasihubiri, lakini mbinu hiyo haikufua dafu. Ndugu zetu waliendelea kuhubiri kotekote walikopelekwa. Niliachiliwa mwaka wa 1966, baada ya kukamilisha kifungo changu. Nilirudi Tomsk na kukaa huko kwa miaka mitatu.

      “Mwaka wa 1969, nilihamia Bonde la Donets ambako nilikutana na Maria, dada mwaminifu na mwenye bidii ambaye nilimwoa. Nilikamatwa tena mwaka wa 1983. Wakati huo nilihukumiwa adhabu maradufu, kifungo cha gereza cha miaka mitano, na uhamisho wa miaka mitano. Bila shaka nilihisi kwamba hukumu hiyo ilikuwa ngumu zaidi kuliko ile ya kwanza kwa sababu wakati huu ningetengana na mke na mtoto wangu ambao pia wangepatwa na magumu. Ninashukuru kwamba niliachiliwa mwaka wa 1987, baada ya Mikhail Gorbachev kuwekwa kuwa katibu mkuu wa Chama cha Kikomunisti cha Sovieti. Niliruhusiwa kurudi Ukrainia na hatimaye Moldova.

      “Niliporudi Bălţi, jiji la pili kwa ukubwa nchini Moldova, jiji hilo lilikuwa na wahubiri 370 na makutaniko matatu. Leo jiji hilo lina zaidi ya wahubiri 1,700 na makutaniko 16!”

      “Je, Unataka Kufa Kama Vasile?”

      Wasimamizi wa kambi na wapelelezi wa KGB (Halmashauri ya Usalama wa Kitaifa ya Sovieti) walitunga mbinu za kinyama ili kuvunja uaminifu wa ndugu. Constantin Ivanovici Şobe anasimulia kile kilichompata babu yake Constantin Şobe: “Mwaka wa 1952, Babu alikuwa amefungwa katika kambi moja ya kazi ngumu katika wilaya ya Chita, mashariki ya Ziwa Baikal huko Siberia. Maafisa wa kambi walitisha kumpiga risasi yeye na Mashahidi wengine wasipokana imani yao.

      “Kwa sababu ndugu hao walikataa kukana imani yao, maafisa waliwakusanya nje ya kambi karibu na msitu. Giza lilikuwa likiingia walipompeleka Vasile, rafiki wa karibu zaidi wa Babu, msituni na kutangaza kwamba watampiga risasi. Ndugu walingoja wakiwa na wasiwasi. Punde walisikia bunduki zikifyatuliwa.

      “Askari walirudi na kumpeleka Shahidi wa pili, babu yangu, msituni. Baada tu ya kuingia msituni, walifika kwenye uwanja fulani wenye makaburi kadhaa yaliyokuwa yamechimbwa, na moja lilikuwa limefukiwa. Afisa mkuu alisema hivi akimwangalia Babu na kuelekeza kidole kwenye kaburi lililofukiwa: ‘Je, unataka kufa kama Vasile, au unataka kurudi nyumbani kwa familia yako ukiwa mtu huru? Una dakika mbili kufanya uamuzi.’ Babu hakuhitaji dakika mbili. Mara moja alijibu: ‘Vasile, mliyempiga risasi, alikuwa rafiki yangu kwa miaka mingi. Sasa ninatarajia kumwona tena atakapofufuliwa katika ulimwengu mpya. Nina hakika kwamba nitakuwa katika ulimwengu mpya pamoja na Vasile. Lakini, vipi wewe?’

      “Afisa huyo hakutarajia jibu hilo. Alimrudisha babu na wale wengine kambini. Hata hivyo, babu hakuhitaji kungoja hadi ufufuo ili kumwona Vasile tena. Hiyo ilikuwa mbinu mbovu iliyokusudiwa kuvunja uaminifu wa ndugu.”

      Mbinu ya Wakomunisti ya Kueneza Uwongo Haikufaulu

      Wakomunisti walichapisha vitabu na vijitabu, na kutengeneza sinema zilizoeneza uwongo juu ya watu wa Mungu ili kuwachochea watu wawachukie na kuwashuku Mashahidi wa Yehova. Kijitabu kimoja kilikuwa na kichwa Double Bottom. Kijitabu hicho kilipewa jina hilo kwa sababu ndugu walikuwa wakitengeneza sehemu ya siri ya kufichia vitabu katika masanduku ya nguo na mikoba yao. Nicolai Voloşanovschi anakumbuka jinsi kamanda wa kambi alivyojaribu kutumia kijitabu hicho kumfedhehesha mbele ya wafungwa wengine.

      Nicolai anasema hivi: “Kamanda huyo alikusanya wafungwa wote katika jengo moja kambini. Kisha akasoma sehemu mbalimbali katika kijitabu hicho, kutia ndani sehemu zilizokuwa na maelezo ya uwongo kunihusu. Alipomaliza, nilimwomba ruhusa kuuliza maswali machache. Bila shaka kamanda huyo alikubali ombi langu akidhani kwamba angepata nafasi ya kunifanyia mzaha.

      “Nilimwuliza kamanda huyo ikiwa anakumbuka aliponihoji mara ya kwanza nilipokuja kambini. Alisema anakumbuka mahojiano hayo. Kisha nikamwuliza kama anakumbuka maswali ambayo aliniuliza kuhusu nchi niliyozaliwa, uraia wangu, na kadhalika alipokuwa akijaza fomu za kuniandikisha kambini. Tena alijibu ndiyo. Hata aliwaambia wale waliokuwa wakisikiliza majibu niliyotoa wakati huo. Kisha nikamwomba aeleze yale aliyoandika katika fomu hizo. Alikiri kwamba yale aliyoandika hayakupatana na majibu yangu. Niliwatazama wasikilizaji na kusema: ‘Mwaona, kijitabu hiki kiliandikwa kwa njia iyo hiyo.’ Wafungwa walipiga makofi, na kamanda akatoka kwa hasira.”

      Njama ya Kusababisha Migawanyiko ili Kushinda

      Katika miaka ya 1960, viongozi wa Sovieti walioudhika walitunga mbinu mpya za kuharibu umoja wa Mashahidi wa Yehova. Kitabu Upanga na Ngao (The Sword and the Shield), kilichochapishwa mwaka wa 1999, kinazungumzia baadhi ya ripoti za KGB, ambazo zilikuwa za siri wakati huo, zilizopatikana katika hifadhi za nyaraka za serikali. Ripoti hiyo inasema: “Maafisa wakuu wa KGB ambao waliongoza ‘pambano dhidi ya Mashahidi wa Yehova’ walifanya mkutano mnamo Machi 1959, na kuamua kwamba mbinu bora ingekuwa ‘kuendelea kuwakandamiza [Mashahidi wa Yehova] kwa kusababisha migawanyiko.’ Maafisa wa KGB waliazimia kusababisha migawanyiko miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, kuwavunja moyo, kuwavunjia heshima, na vilevile kuwafunga viongozi wao wakuu kwa mashtaka ya uwongo.”

      Mbinu za “kusababisha migawanyiko” zilihusisha jitihada za pamoja za kuwafanya ndugu wawashuku ndugu wenzao kotekote katika Muungano wa Sovieti. Ili kutimiza lengo hilo, KGB ilieneza uvumi kwamba ndugu kadhaa walioongoza walikuwa wameanza kushirikiana na KGB. Wapelelezi wa KGB walieneza uvumi huo kwa ujanja sana hivi kwamba Mashahidi wengi walianza kuwashuku ndugu wenzao.

      Mbinu nyingine ya KGB ilikuwa kuwazoeza wapelelezi kujifanya kuwa Mashahidi wa Yehova “wanaohubiri kwa ukawaida,” kisha wangejaribu kustahili kupata madaraka katika tengenezo. Bila shaka, wapelelezi hao walikuwa wakiwasiliana na KGB. Wapelelezi wa KGB pia waliwaendea kisiri Mashahidi wa kweli na kujaribu kuwahonga kwa kiasi kikubwa cha pesa ili waunge KGB mkono.

      Jambo la kusikitisha ni kwamba mbinu hizo zilifaulu kwa kadiri fulani kuharibu umoja wa ndugu, kutia ndani ndugu wa Moldova. Hivyo, polepole ndugu walianza kuwashuku ndugu wenzao. Baadhi ya ndugu walijitenga na tengenezo na kuanzisha kikundi ambacho kilijulikana kama upinzani.

      Kabla ya matukio hayo, ndugu katika Muungano wa Sovieti walitumia neno “njia,” walipokuwa wakirejezea tengenezo la Yehova, chakula cha kiroho, na ndugu walioongoza. Sasa ndugu walichanganyikiwa na kutilia shaka njia hiyo. Walitatuaje vurugu hiyo? Kwa kushangaza, Serikali ya Sovieti iliwasaidia. Ndiyo, wale waliotunga njama hiyo walisaidia kutatua matatizo waliyosababisha. Vipi?

      Walipuuza Roho ya Mungu

      Mapema katika miaka ya 1960, wenye mamlaka wa Sovieti waliwafunga “viongozi” wengi wa Mashahidi kutoka sehemu zote za Muungano wa Sovieti katika kambi moja iliyokuwa umbali wa kilometa 150 kutoka jiji la Saransk katika jamhuri ya Mordvinia, magharibi mwa Urusi. Kabla ya hapo, ndugu hawakuweza kuwasiliana vizuri kwa sababu walikaa mbali sana na wenzao, hivyo kutoelewana kulitokea kwa urahisi. Lakini sasa wale wafuasi wa kikundi cha upinzani, na wale wasiojiunga na kikundi hicho, walikuwa pamoja. Kwa hiyo, waliweza kuongea ana kwa ana na kutofautisha kweli na uwongo. Kwa nini wenye mamlaka waliwaweka ndugu hao wote pamoja? Inaonekana walifikiri kwamba ndugu wangezozana, na hivyo kuzidisha migawanyiko iliyokuwapo. Hata hivyo, mbinu hiyo iliyopangwa kwa werevu, haikufua dafu kwa sababu walioitunga walipuuza roho ya Yehova inayoleta umoja.—1 Kor. 14:33.

      Ndugu mmoja aliyepelekwa Mordvinia ni Gheorghe Gorobeţ. Anasema hivi: “Muda mfupi baada ya kukamatwa na kupelekwa gerezani, ndugu mmoja aliyekuwa mfuasi wa kikundi cha upinzani alifungwa pamoja nami. Alipoona kwamba ndugu walioongoza bado walikuwa wamefungwa, alishangaa, kwa kuwa alikuwa ameambiwa kwamba sisi sote tuliachiliwa huru na tulikuwa tukiishi raha mustarehe na kupewa pesa na KGB!”

      Ndugu Gorobeţ anaongeza hivi: “Katika mwaka wangu wa kwanza gerezani, zaidi ya watu 700 walifungwa kwa sababu za kidini. Wengi wao walikuwa Mashahidi wa Yehova. Sote tulifanya kazi katika kiwanda kimoja na tulikuwa na nafasi ya kuongea na wale waliokuwa wamejiunga na kikundi cha upinzani. Hivyo, mambo mengi yaliyosababisha migawanyiko yalitambuliwa katika mwaka wa 1960 na 1961. Hatimaye, mwaka wa 1962, ndugu wa halmashauri ya nchi waliosimamia kazi katika Muungano wa Sovieti waliandika barua wakiwa katika kambi ya kazi ngumu. Barua hiyo ilitumiwa makutaniko yote katika Muungano wa Sovieti na matatizo mengi yaliyosababishwa na mbinu za KGB yalitatuliwa.”

      Kutambua Njia ya Kweli

      Ndugu Gorobeţ alirudi Moldova mara alipoachiliwa kutoka katika kambi ya kazi ngumu mnamo Juni 1964. Alipowasili Tabani, aligundua kwamba Mashahidi wengi huko bado walikuwa wamechanganyikiwa kuhusu njia ambayo Yehova anatumia kuwalisha na kuwaongoza watu Wake. Ndugu kadhaa walisoma Biblia peke yake.

      Halmashauri ya ndugu watatu waliokomaa kiroho iliwekwa ili kurekebisha hali hiyo. Kwanza walitembelea makutaniko yaliyokuwa kaskazini mwa Moldova, ambako Mashahidi wengi waliishi. Ndugu walipoona kwamba ndugu hao na waangalizi wengine Wakristo bado walikuwa waaminifu licha ya kuteswa sana, walisadikishwa kwamba bado Yehova anatumia tengenezo lilelile lililowafundisha kweli.

      Mwishoni mwa miaka ya 1960, KGB ilitambua kwamba kazi ya kuhubiri ilikuwa ikiendelea licha ya mateso na mbinu nyingine. Kitabu Upanga na Ngao kinaeleza hatua ambayo KGB ilichukua: “Maafisa wa [KGB] walishikwa na wasiwasi waliposikia kwamba hata ndani ya kambi za kazi ngumu, ‘viongozi wa Mashahidi wa Yehova walidumisha imani yao inayopinga Ukomunisti na waliendelea kufanya kazi ya Yehova.’ Maafisa wa KGB ambao walikuwa wakitunga njama dhidi ya Mashahidi wa Yehova walifanya mkutano [huko Chisinau] mnamo Novemba 1967 ili kuzungumzia mbinu mpya za ‘kuzuia kazi ya Mashahidi’ na ‘mafundisho yao yanayopinga Ukomunisti.’”

      Kunyanyaswa na Ndugu Waasi

      Ni jambo la kuhuzunisha kwamba baadhi ya Mashahidi walidanganywa na “mbinu [hizo] mpya” na hivyo kutimiza kabisa lengo la KGB. Baadhi yao walivunja uaminifu wao kwa sababu ya pupa au woga; wengine walikuwa ndugu waliotengwa ambao waliwachukia Mashahidi. Wenye mamlaka walianza kuwatumia ili kuvunja uaminifu wa Mashahidi waaminifu. Mashahidi waliokuwa wamevumilia vifungo vya gereza na kazi ngumu katika kambi walisema kwamba kunyanyaswa na ndugu waliotengwa, ambao baadhi yao walikuwa waasi-imani, lilikuwa jaribu gumu kuliko majaribu mengine yoyote ambayo walipata.

      Waasi-imani wengi walikuwa wafuasi wa kikundi cha upinzani. Mwanzoni, kikundi hicho kilikuwa na Mashahidi kadhaa waliokuwa wamechanganyikiwa kwa sababu ya uwongo ulioenezwa na KGB. Lakini baadhi ya wale ambao bado walishirikiana na kikundi hicho mwishoni mwa miaka 1960 walionyesha roho ya jamii ya mtumwa mwovu. Kwa sababu walipuuza onyo la Yesu, walianza “kuwapiga watumwa [wenzao].”—Mt. 24:48, 49.

      Hata hivyo, ijapokuwa maafisa wa KGB na wafuasi wao walijitahidi kwa muda mrefu kusababisha migawanyiko ili kuwashinda watu wa Mungu, mbinu yao haikufua dafu. Mapema katika miaka ya 1960, ndugu waaminifu walipoanza kurudisha umoja katika tengenezo nchini Moldova, ndugu wengi nchini humo walikuwa wamejiunga na kikundi cha upinzani. Lakini kufikia mwaka wa 1972, karibu wote walikuwa wakifanya kazi kwa uaminifu pamoja na tengenezo la Yehova.

      Mtesaji Aliyefurahia Kusoma Gazeti Letu

      Ndugu waaminifu waliobaki Moldova wakati wa utawala wa Kikomunisti waliendelea kufanya kazi ya kuhubiri kwa kadiri walivyoweza. Waliwahubiria watu wa familia zao, marafiki, wanashule na wafanyakazi wenzao. Lakini walihubiri kwa tahadhari sana kwa sababu maafisa wengi wa chama nchini Moldova walikuwa Wakomunisti washupavu. Hata hivyo, si Wakomunisti wote waliowadharau Mashahidi wa Yehova.

      Simeon Voloşanovschi anasema hivi: “Polisi walipekua nyumba yetu na kutunyang’anya magazeti na vitabu vingi, ambavyo afisa mkuu aliorodhesha. Baadaye afisa huyo alirudi na orodha hiyo na kuniomba nihakikishe kwamba magazeti na vitabu vyote viliorodheshwa kwa usahihi. Nilipochunguza orodha hiyo, niliona kwamba gazeti moja la Mnara wa Mlinzi, ambalo linazungumzia jinsi ya kufanya maisha ya familia yawe yenye furaha zaidi, halikuwa limeorodheshwa. Nilimwuliza afisa huyo juu ya gazeti hilo. Alijibu hivi kwa aibu: ‘Nililipeleka nyumbani, na tulilisoma pamoja na familia yangu.’ Kisha nikamwuliza, ‘Lakini mlilipenda?’ ‘Bila shaka, tulilipenda sana!’ akajibu.”

      Upinzani Wapungua, Ongezeko Laendelea

      Wakomunisti waliacha kuwakamata na kuwahamisha watu wa Yehova katika miaka ya 1970. Hata hivyo, mara kwa mara ndugu walikamatwa na kufikishwa mahakamani kwa sababu ya kuhubiri au kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Lakini hawakuhukumiwa vifungo vikali sana.

  • Moldova
    2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
    • Ibada ya Kweli Inasitawi

      Ijapokuwa serikali ya Kikomunisti ya Sovieti ilikuwa na nguvu nyingi za kisiasa na kijeshi wakati huo, haikufaulu kukomesha ibada ya kweli, bali kupitia mbinu zao za kuwahamisha watu, Wasovieti walisaidia kueneza habari njema hadi ‘sehemu za mbali zaidi za dunia.’ (Mdo. 1:8) Yehova aliahidi hivi kupitia Isaya: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa . . . Hilo ndilo fungu la urithi la watumishi wa Yehova, na uadilifu wao ni kutoka kwangu.” (Isa. 54:17) Maneno hayo yamethibitika kuwa ya kweli kabisa!

  • Moldova
    2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 113-115]

      Nilizaliwa Uhamishoni

      Lidia Sevastian

      Alizaliwa: 1954

      Alibatizwa: 1995

      Maisha yake: Alilelewa na mama Shahidi na baba asiyeamini, lakini hakushirikiana na Mashahidi wa Yehova kwa miaka mingi.

      Mama na nyanya yangu walijifunza kweli na kuwa Mashahidi wa Yehova mapema katika miaka ya 1940. Baba alikuwa mtu mwema lakini hakukubali kweli ya Biblia wakati huo. Mwaka wa 1951, Mama alikuwa na watoto wawili na alikuwa na mimba ya mapacha. Yapata mwezi wa Aprili mwaka huo, wenye mamlaka walijaribu kuvunja familia yetu. Baba alipokuwa kazini, Mama, aliyekuwa karibu kujifungua, ndugu na dada zangu walipelekwa kwenye gari-moshi la kwenda Siberia. Hata hivyo, Mama alifaulu kumtumia Baba ujumbe, naye alienda nyumbani haraka. Ijapokuwa hakuwa Shahidi, alipanda gari-moshi na kwenda uhamishoni pamoja na familia yake.

      Wakati wa safari ya kwenda Siberia, Mama aliruhusiwa kukatiza safari na kubaki mjini Asino kwa muda mfupi ili ajifungue mapacha. Wengine walilazimika kuendelea na safari hadi wilaya ya Tomsk, ambako Baba alipanga nyumba. Alifanya kazi pamoja na akina ndugu. Majuma machache baadaye, Mama na wale mapacha wachanga walijiunga na familia. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba mapacha hao walikufa kwa sababu ya maisha magumu sana ya familia yetu.

      Hata hivyo, watoto wengine wanne walizaliwa uhamishoni, kutia ndani mimi na ndugu yangu pacha. Baba alitutunza sote kwa uaminifu. Hatimaye tuliruhusiwa kurudi nyumbani mwaka wa 1957. Mama aliendelea kutufundisha kupenda kanuni za Biblia, ijapokuwa alipelelezwa sana na polisi wa siri.

      Kwa upande mwingine, Baba alihangaikia hasa kuwapa watoto wake elimu bora. Kwa hiyo, nilipokuwa na umri wa miaka 16, nilijiunga na chuo kikuu huko Chisinau. Baadaye niliolewa na kuhamia Kazakhstan, mbali sana na wazazi wangu na tengenezo la Yehova. Nilirudi Chisinau mwaka wa 1982, na mara moja nilianza kuwatafuta watu wa Yehova, lakini sikufaulu. Kwa miaka minane nilidhani kwamba hakukuwa na mtu mwingine yeyote katika jiji hilo aliyetaka kumwabudu Yehova.

      Kisha, siku moja nilipokuwa nikingoja basi, niliwasikia wanawake wawili wakiongea kumhusu Yehova. Nilisonga karibu ili nisikie vizuri zaidi. Wanawake hao walifikiri kwamba mimi ni mpelelezi wa KGB, kwa hiyo walianza kuzungumzia habari nyingine. Walipoondoka niliwafuata, na hilo liliwatia wasiwasi. Kwa hiyo niliwakaribia haraka, na baada ya kuongea nao kwa muda, walisadikishwa kwamba mimi si mpelelezi. Tamaa yangu ya kushirikiana na tengenezo la Yehova ilitimia hatimaye! Hata hivyo, jambo la kusikitisha ni kwamba mume wangu alipinga msimamo wangu.

      Tulikuwa na watoto wawili wakati huo. Mwaka wa 1992, nilifanyiwa upasuaji wa uti wa mgongo, kwa hiyo nililazwa hospitalini na sikuweza kutoka kitandani kwa miezi sita. Katika pindi hiyo yenye kushusha moyo, jambo zuri ajabu lilitukia: Mwana wangu Pavel, alichukua msimamo wake upande wa Yehova, akabatizwa mwaka wa 1993 katika kusanyiko la kimataifa huko Kiev. Baada ya muda nilipona kiasi cha kuweza kutembea tena. Kwa hiyo, mwaka wa 1995, mimi pia nilibatizwa ili kuonyesha kwamba nimejiweka wakfu kwa Yehova.

      Leo, watu wengi wa familia yetu ni Mashahidi na ninamshukuru Yehova na mama yangu kwa jambo hilo. Nilikumbuka sikuzote uaminifu wa Mama, na ninafurahi kwamba baba yangu, aliyetutunza kwa uaminifu sana, alikuja kuwa mtumishi wa Yehova kabla ya kifo chake.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 117, 118]

      Dhabihu Zetu Si Kitu Zikilinganishwa na za Yehova

      Mihai Ursoi

      Alizaliwa: 1927

      Alibatizwa: 1945

      Maisha yake: Aliteswa chini ya utawala wa Wafashisti na Wakomunisti.

      Nilianza kuhubiri habari njema mwaka wa 1941. Mwaka wa 1942, nilipokuwa na umri wa miaka 15, nilikuwa nipate mazoezi ya kijeshi katika shule yetu. Picha za Mfalme Michael wa Rumania, Jenerali Antonescu, na Bikira Mariamu zilikuwa zimetundikwa darasani. Tulipoingia darasani, tulipaswa kupiga magoti mbele ya picha hizo na kufanya ishara ya msalaba. Mimi na vijana wengine wawili tulikataa kupiga magoti.

      Polisi walitupiga kikatili kwa sababu ya kukataa. Tulilala shuleni usiku huo. Asubuhi tulipelekwa Corjeuţi ambako tulipigwa tena. Kutoka Corjeuţi, tulipelekwa sehemu mbalimbali, kisha tukatembea kwa miguu umbali wa kilometa 100 hadi mahali ambapo tungehukumiwa katika mahakama ya jeshi. Miguu yangu ilitoka damu kwa sababu ya kutembea sana. Hatimaye niliruhusiwa kurudi nyumbani bila kuhukumiwa, yaelekea kwa sababu ya umri wangu mdogo.

      Nilipokuwa na umri wa miaka 18, niliitwa na serikali ya Sovieti nijiandikishe jeshini. Tena nilikataa kuvunja uaminifu wangu na nikapigwa vibaya. Rafiki yangu Gheorghe Nimenco alipigwa pia, naye alikufa majuma sita baadaye kutokana na majeraha aliyopata. Tena niliruhusiwa kurudi nyumbani, nadhani kwa sababu ya umri wangu. Wasovieti walinikamata tena mwaka wa 1947, na wakati huo walitisha kunipiga risasi nisipojiunga na jeshi. Hata hivyo, badala ya kuuawa nilihukumiwa kifungo cha upweke kwa miezi miwili, na baada ya hapo nilipelekwa kufanya kazi kwenye mradi wa kujenga Mfereji wa Volga-Don. Kazi hiyo ilikuwa hatari sana na watu wengi walikufa. Niliponea chupuchupu katika msiba mmoja ambamo watu wengi walikufa na nikarudi nyumbani Moldova.

      Nilipokuwa huko nilioa. Mimi na mke wangu Vera, aliyekuwa na mimba, tulihamishwa mwaka wa 1951. Tulisafiri kwanza kwa gari-moshi na baadaye kwa mashua hadi msitu mkubwa sana wa Siberia unaoitwa taiga, ambako nilifanya kazi ya kukata miti. Mimi na Vera tuliishi katika kibanda kimoja pamoja na familia nyingine 16. Tulifurahi tuliporuhusiwa kurudi Moldova mwaka wa 1959.

      Mambo kadhaa yameniimarisha katika miaka hiyo migumu na hata sasa. Jambo moja ni imani ya ndugu yangu Ion. (Ona ukurasa wa 89.) Alihukumiwa kifo, lakini alikataa kuvunja uaminifu wake, ijapokuwa hakujua kwamba hukumu yake ingebadilishwa. Ninaimarishwa pia ninapotafakari jinsi ambavyo Yehova amenitunza mimi na mke wangu, tulipovumilia majaribu kwa ajili ya jina lake. Hata hivyo, dhabihu zetu si kitu zikilinganishwa na jinsi ambavyo Yehova alijidhabihu alipomtuma Mwana wake afe kwa ajili yetu. Ninapotafakari dhabihu hiyo ya pekee, ninatiwa nguvu ya kukabili majaribu ya kila siku kwa shangwe.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 121-123]

      Yehova Alinitunza kwa Upendo

      Mihailina Gheorghiţa

      Alizaliwa: 1930

      Alibatizwa: 1947

      Maisha yake: Alikuwa mjumbe na mtafsiri wakati wa marufuku.

      Nilijifunza kweli mwaka wa 1945 na nilifurahia kuhubiri habari njema katika kijiji chetu cha Glodeni, na katika kijiji jirani cha Petrunea. Wakuu wa shule walikataa kunipa cheti cha kuhitimu kwa sababu nilihubiri shuleni. Hata hivyo, nilifurahia kutumia elimu yangu kusaidia kutafsiri magazeti na vitabu vya Biblia kutoka Kirumania na Kiukrainia hadi Kirusi.

      Muda mfupi baada ya kubatizwa, nilikamatwa nilipokuwa nikitafsiri na nikahukumiwa kifungo cha miaka 25 katika kambi ya kazi ngumu huko Vorkuta, kaskazini ya Mzingo wa Aktiki, ambako niliwapata dada wengine wengi. Licha ya hali ngumu sana, sisi sote tuliendelea kuhubiri. Tulifaulu pia kupata vitabu na magazeti. Na hata tulinakili magazeti na vitabu vingine humo kambini.

      Siku moja nilikutana na mwanamke fulani ambaye alikuwa amekamatwa kwa sababu wenye mamlaka walifikiri kimakosa kwamba yeye ni Shahidi. Nilimtia moyo achunguze Neno la Mungu kwa sababu Yehova ana uwezo wa kuweka watu wake huru ikiwa ni mapenzi yake. Hatimaye, alikubali kujifunza Biblia na akawa dada yetu. Muda mfupi baadaye aliachiliwa kabla hajamaliza kifungo chake.

      Baadaye nilihamishwa hadi Karaganda, Kazakhstan. Mwishowe, Julai 5, 1956, mimi pia niliachiliwa. Nilihamia Tomsk, ambako nilikutana na kuolewa na Alexandru Gheorghiţa, ambaye alikuwa amefungwa kwa miaka sita kwa sababu ya imani yake. Tuliendelea kuhubiri katika eneo kubwa la Siberia, tukijua kwamba polisi wa siri bado walikuwa wakitupeleleza. Baadaye tulihamia Irkutsk, magharibi mwa Ziwa Baikal. Tuliendelea kunakili vitabu kisiri tukiwa huko. Baadaye tulitumikia Bishkek, Kyrgyzstan. Ijapokuwa tulijihadhari tulipohubiri, Alexandru alikamatwa na kuhukumiwa kifungo cha miaka kumi.

      Mwendesha-mashtaka aliniambia kwamba ningeweza kumtembelea Alexandru aliyekuwa gerezani akisubiri kuhukumiwa. Kwa kawaida jambo hilo halikuruhusiwa, kwa hiyo nilimwuliza ni kwa nini alitutendea kwa fadhili hivyo. Aliniambia: “Ninyi ni wenzi wa ndoa wachanga na mna mtoto. Huenda mkafikiria upya uamuzi wenu.” Nilimwambia mwendesha-mashtaka huyo kwamba zamani mimi na Alexandru tuliazimia kumtumikia Yehova kwa uaminifu na bado tunashikilia azimio hilo. Alijibu hivi: “Hata Biblia yenu inasema kwamba mbwa aliye hai ni afadhali kuliko simba aliyekufa.” (Mhu. 9:4) “Ni kweli,” nikamjibu, “lakini mbwa aliye hai ambaye wewe unazungumzia hataurithi ulimwengu mpya wa Mungu.”

      Alexandru alifungwa kwa miaka kumi, na kwa mwaka mwingine mmoja alifungwa nyumbani mwake. Baada ya Alexandru kuachiliwa, tulihamia Kazakhstan na kisha Uzbekistan, ili kusaidia katika kazi ya kuhubiri. Hatimaye tulirudi Moldova mwaka wa 1983, tukiwa tumeridhika kwa sababu tulikuwa na pendeleo lisilo na kifani la kuwasaidia watu wenye mioyo minyofu katika sehemu nyingi kumjua Yehova.

      Ninapofikiria mambo yaliyopita, ninakubali kwamba maisha yangu hayakuwa rahisi. Lakini hivyo ndivyo ilivyo na watu wasio Mashahidi. Wao pia wamekabili matatizo mengi maishani. Lakini sisi tumeteswa kwa ajili ya habari njema. Kwa hiyo, Yehova ametulinda na kututunza kwa upendo. Zaidi ya hayo, tunajua kwamba baada ya magumu kukoma tutaishi maisha mazuri yenye kuvutia kwa umilele wote.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki