-
Nitapata Pesa Wapi?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
Uwe na Usawaziko
Umewahi kujaribu kuendesha baiskeli ukiwa umebeba vitu kadhaa kama vile mfuko wa shule, mpira, na labda mifuko mingine iliyo na vyakula? Vitu vinapokuwa vingi, inakuwa vigumu zaidi kudumisha usawaziko! Ndivyo inavyoweza kuwa pia na kazi inayodai mengi. Ukitumia akili, muda, na wakati mwingi sana katika kazi hiyo, huenda afya yako na masomo yako yakaathiriwa. Mbali na hayo, kazi ngumu inayochukua muda mwingi inaweza kufanya iwe vigumu kwako kuhudhuria mikutano, kujifunza Biblia, na kushiriki katika huduma ya Kikristo. Kijana anayeitwa Michèle anasema: “Kuna nyakati ambazo nimekosa mikutano kutokana na uchovu wa kufanya kazi baada ya shule.”
Usipoteze usawaziko kwa kuwa na maoni yasiyofaa kuhusu pesa. Yesu alisema kwamba wenye furaha ya kweli ni wale “wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Pia alisema: “Hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.” (Luka 12:15) Kijana Mkristo anayeitwa Maureen, anatii shauri hilo. Anasema: “Sitaki kunaswa na miradi ya kufuatia vitu vya kimwili. Ninajua hali yangu ya kiroho itaathirika nikinaswa na mtego wa kutafuta pesa tu.”
Ni kweli kwamba katika sehemu fulani za ulimwengu, vijana wanalazimika kufanya kazi kwa saa nyingi ili kusaidia familia zao. Hata hivyo, ikiwa hali yako ni tofauti, mbona upoteze usawaziko wako? Kulingana na wataalamu wengi, kufanya kazi kwa zaidi ya saa 20 kwa juma huku ukiendelea na masomo kunaweza kusababisha madhara. Wataalamu wengine wanapendekeza wanafunzi wasifanye kazi kwa zaidi ya saa nane hadi kumi kwa juma. Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema: “Konzi moja ya pumziko ni afadhali kuliko konzi mbili za kazi ngumu na kufuatilia upepo.”—Mhubiri 4:6.
Kumbuka, “nguvu za udanganyifu za utajiri,” zinaweza kusonga upendezi wako wa mambo ya kiroho. (Marko 4:19) Kwa hiyo, ukiamua kufanya kazi baada ya shule ili upate pesa, panga ratiba yako ili utangulize mambo ya kiroho. Mwombe Yehova akusaidie. Anaweza kukupa nguvu za kukabili hali hiyo na kukusaidia kuendelea kuwa na usawaziko wa kiroho.
-
-
Nitapata Pesa Wapi?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
[Sanduku katika ukurasa wa 155]
Heshimu Pesa—Usizipende
Kwa mpishi, kisu chenye makali ni kifaa muhimu. Lakini kisu hichohicho mikononi mwa mtu asiye na ujuzi au asiye makini kinaweza kutokeza madhara makubwa. Pesa ni kama kisu chenye makali. Ukijua jinsi ya kuzitumia, zitakuwa na faida kwako. Lakini usipokuwa mwangalifu, unaweza kuumia! Kwa mfano, mtume Paulo aliwaonya Wakristo wasipende pesa. Watu fulani wameazimia kuwa matajiri, na katika harakati hizo wamepoteza marafiki, wamevunja mahusiano ya kifamilia, na kuharibu uhusiano wao na Mungu. Kwa sababu hiyo, “wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.” (1 Timotheo 6:9, 10) Hilo linatufundisha nini? Jifunze kutumia pesa inavyofaa. Ziheshimu, lakini usizipende!
-