-
Akili ZilizovurugikaAmkeni!—2004 | Januari 8
-
-
Akili Zilizovurugika
NICOLE amekuwa akishuka moyo tangu alipokuwa na umri wa miaka 14. Hata hivyo, alipokuwa na umri wa miaka 16, alianza kuhisi tofauti—alisisimuka kupita kiasi na kuhisi ana nguvu nyingi mno. Aliwaza sana, alisema mambo yasiyoeleweka, alikosa usingizi na kushuku kwamba marafiki wake wanamtumia ili kujifaidi. Kisha, Nicole alidai kwamba angeweza kubadilisha rangi ya vitu. Hapo ndipo mama yake alipotambua kwamba Nicole anahitaji kumwona daktari, kwa hiyo akampeleka hospitalini. Baada ya kumchunguza, madaktari wakagundua kwamba Nicole ana ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika.a
Kama Nicole, mamilioni ya watu ulimwenguni pote wana ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika au ugonjwa wa kushuka moyo. Magonjwa hayo yanaweza kusababisha madhara makubwa mno. Steven anayeugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika anasema: “Nilifadhaika kwa miaka mingi, nilishuka moyo na wakati mwingine nikasisimuka kupita kiasi. Matibabu yalisaidia, lakini bado nilifadhaika.”
Ni nini kinachosababisha magonjwa ya kihisia? Watu walioshuka moyo au wenye ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika hukabili magumu gani? Wagonjwa na wale wanaowatunza wanaweza kusaidiwaje?
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya dalili zilizotajwa zinaweza pia kuwa dalili za ugonjwa wa akili, matumizi ya dawa za kulevya, au hata mabadiliko yanayotukia wakati wa kubalehe. Ugonjwa unaweza kutambuliwa tu baada ya kuchunguzwa kikamili na mtaalamu.
-
-
Kuishi na Ugonjwa wa KihisiaAmkeni!—2004 | Januari 8
-
-
Kuishi na Ugonjwa wa Kihisia
WATU wengi sana wanaugua magonjwa ya kihisia. Kwa mfano, inakadiriwa kwamba zaidi ya watu milioni 330 ulimwenguni pote wameshuka moyo sana, hali inayowafanya wahuzunike sana na wasipendezwe na shughuli za kila siku. Inakadiriwa kwamba miaka 20 ijayo, idadi ya watu walioshuka moyo itazidi ile ya wagonjwa wengine isipokuwa tu wagonjwa wa moyo. Basi si ajabu kwamba watu wanasema ugonjwa huo umewakumba watu wengi kama mafua.
Katika miaka ya karibuni, watu wengi zaidi wameufahamu ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika. Dalili za ugonjwa huo zinatia ndani kushuka moyo na baadaye kusisimuka kupita kiasi. Kitabu kimoja kilichochapishwa hivi majuzi na Chama cha Kitiba cha Marekani kinasema kwamba “mtu anaposhuka moyo, anaweza kutaka kujiua. Wakati mtu amesisimuka sana, anaweza kushindwa kuamua mambo vizuri na kufanya mambo hatari bila kutambua.”
Inakadiriwa kwamba asilimia 2 ya watu nchini Marekani wanaugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika, hivyo kuna mamilioni ya watu wanaougua ugonjwa huo nchini humo pekee. Hata hivyo, takwimu hazionyeshi msononeko ambao wagonjwa hao hupata.
Mtu Hulemewa na Huzuni Anaposhuka Moyo
Wengi wetu tunajua jinsi mtu huhisi anapohuzunika. Baada ya muda mfupi, labda saa au siku kadhaa, huzuni hiyo huisha. Hata hivyo, ugonjwa wa kushuka moyo ni tofauti. Kwa njia gani? Dakt. Mitch Golant anasema kwamba ‘sisi ambao hatuna ugonjwa wa kushuka moyo tunajua kwamba hatimaye huzuni hutoweka, lakini kwa watu wenye ugonjwa huo huzuni hufuatwa na msisimuko, kisha hisia hizo hubadilika-badilika daima.’
Ugonjwa wa kushuka moyo huathiri watu kwa njia mbalimbali. Kwa mfano, wengine huugua katika majira fulani, hasa majira ya baridi kali. Kitabu kilichochapishwa na Chama cha Kitiba cha Umma kinasema: “Watu wanaoshuka moyo katika majira fulani huathiriwa zaidi wakiwa katika maeneo ya kaskazini ya dunia na kukiwa na mawingu mengi. Ingawa inasemekana kwamba watu hao huathiriwa zaidi wakati wa baridi kali, wakati mwingine wao huathiriwa pia wanapofanya kazi mahali penye giza, wakati wowote ambapo kuna mawingu, na wasipoona vizuri.”
Ni nini kinachosababisha ugonjwa wa kushuka moyo? Haijulikani waziwazi. Ijapokuwa huenda mtu akarithi ugonjwa huo, mara nyingi watu huathiriwa na mambo yanayotukia maishani. Imeonekana kwamba wanawake huathiriwa mara mbili zaidi ya wanaume.a Lakini haimaanishi kwamba wanaume hawawezi kuugua. Inakadiriwa kwamba kati ya asilimia 5 na 12 ya wanaume wataugua ugonjwa wa kushuka moyo wakati fulani maishani mwao.
Mtu anapougua ugonjwa huo, karibu maisha yake yote huathiriwa. Sheila, anayeugua ugonjwa huo, anasema mgonjwa “huvurugika kabisa, hukosa kujiamini na kujiheshimu, hushindwa kufikiri vizuri na kufanya maamuzi vizuri, na huumia sana anapozidiwa.”
Wakati mwingine mgonjwa anaweza kufarijika kwa kumweleza mtu mwingine anayejali hisia zake. (Ayubu 10:1) Hata hivyo, tunapaswa kutambua kwamba kushuka moyo hakuwezi kumalizwa kwa kuwa na maoni yanayofaa tu wakati hali hiyo inaposababishwa na kemikali za mwili. Wakati huo, mgonjwa hawezi kudhibiti huzuni yake. Isitoshe, tayari huwa amefadhaishwa na hali hiyo kama tu watu wa familia na marafiki.
Mfikirie Paula,b Mkristo aliyehuzunika vibaya kabla ugonjwa wake haujatambuliwa. Anasema: “Wakati mwingine nilipokuwa kwenye mikutano ya Kikristo, nilirudi kwenye gari na kulia bila sababu yoyote. Nilijihisi mpweke sana na nilifadhaika sana. Ijapokuwa nilikuwa na marafiki wengi walionijali, bado nilihuzunika.”
Ellen pia alipatwa na jambo kama hilo, na alihitaji kulazwa hospitalini. Anasema: “Nina mume, wana wawili, na mabinti-wakwe wawili, na wote wananipenda sana.” Basi, Ellen anapaswa kuwa na furaha na kuhisi anathaminiwa na familia yake. Lakini mtu anaposhuka moyo, huwa na mawazo mabaya, hata ya kipumbavu, na anaweza kulemewa.
Pia ugonjwa huo unaweza kuathiri sana familia nzima. Dakt. Golant anaandika hivi: “Mtu unayempenda anaposhuka moyo, unaishi na wasiwasi kwa kuwa hujui kama atapata nafuu au atashuka moyo zaidi. Unaweza kuhisi mpweke na hata kuhuzunika na kukasirika kwa kuwa unaona maisha yamebadilika kabisa.”
Mara nyingi, watoto wanaweza kutambua kwamba mzazi ameshuka moyo. Dakt. Golant anaandika hivi: “Mtoto wa mama aliyeshuka moyo hutambua haraka hisia za mama yake, na huona mabadiliko yoyote yanayotokea.” Dakt. Carol Watkins anasema kwamba watoto wa mzazi aliyeshuka moyo “wanaweza kuwa na tabia zisizofaa, kushindwa kujifunza, na kutopatana na marafiki. Wanaweza kushuka moyo pia.”
Hisia Zinazobadilika-Badilika
Ugonjwa wa kushuka moyo hutatiza sana. Lakini iwapo pia mtu aliyeshuka moyo anasisimuka kupita kiasi, huwa anaugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika.c Lucia anayeugua ugonjwa huo anasema: “Hisia za mtu anayeugua ugonjwa huo hubadilika-badilika daima.” Jarida The Harvard Mental Health Letter linasema kwamba katika kipindi cha kusisimuka kupita kiasi, mgonjwa “anaweza kuingilia mambo ya wengine na kuwatawala, na ghafula anaweza kushikwa na hasira.”
Lenore anakumbuka wakati aliposisimuka kupita kiasi. Anasema: “Nilikuwa na nguvu nyingi sana. Wengine waliniona kuwa mwanamke shujaa. Watu wengine waliniambia, ‘Laiti ningekuwa kama wewe.’ Mara nyingi nilijihisi nikiwa na nguvu nyingi sana, kana kwamba ningeweza kufanya jambo lolote. Nilifanya mazoezi kupita kiasi. Nilifanya kazi kila siku ijapokuwa nililala kwa muda mfupi sana—kwa saa mbili au tatu tu. Lakini, bado niliamka nikiwa na nguvu nyingi.”
Hata hivyo, baada ya muda Lenore akaanza kushuka moyo. Anasema: “Kipindi cha msisimuko kilipofikia upeo, nilihisi hasira kutoka ndani kama mashine iliyokuwa ikiendeshwa bila kuzimwa. Kwa ghafula, hisia zangu nzuri zikabadilika, nikawa mkali na mjeuri. Niliwafokea washiriki wa familia bila sababu. Nilikuwa mwenye hasira, mwenye chuki, na singejizuia hata kidogo. Baada ya hisia hizo zenye kutisha, nilichoka ghafula, nikalia, na kushuka moyo sana. Nilihisi kuwa mwovu na asiyefaa kitu. Wakati mwingine, ningebadilika na kuwa mchangamfu kama zamani kana kwamba hakuna kitu kilichokuwa kimetukia.”
Hisia zinazobadilika-badilika za mgonjwa huwavuruga washiriki wa familia. Mary, ambaye mume wake ana ugonjwa huo anasema hivi: “Mimi huvurugika ninapomwona mume wangu akiwa mwenye furaha na akiongea sana halafu ghafula anabadilika na kushuka moyo na kunyamaza. Ni vigumu sana kwetu kuamini kwamba hawezi kujizuia.”
Ni kweli kwamba mgonjwa hutaabishwa zaidi na ugonjwa huo. Mgonjwa mmoja anayeitwa Gloria anasema hivi: “Mimi hutamani niwe kama watu wanaoweza kudhibiti maisha yao. Ni mara chache tu ambapo wagonjwa wenye hisia zinazobadilika-badilika huishi maisha ya kawaida.”
Ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika husababishwa na nini? Ni rahisi zaidi mtu arithi ugonjwa huo kuliko ule wa kushuka moyo. Chama cha Kitiba cha Marekani kinasema: “Kulingana na uchunguzi wa kisayansi, watu wa karibu zaidi wa familia, yaani wazazi, ndugu, dada, au watoto wa watu wenye ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika wako katika hatari ya kupatwa na ugonjwa huo mara 8 mpaka 18 zaidi ya watu wanaotoka katika familia zisizo na ugonjwa huo. Isitoshe, kuna uwezekano mkubwa wa kushuka moyo sana ikiwa mtu wa familia ana ugonjwa huo.”
Tofauti na kushuka moyo, inaonekana ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika huwapata wanaume na wanawake kwa kiwango kilekile. Ijapokuwa mara nyingi ugonjwa huo huanza mtu anapokuwa mtu mzima, vijana na watoto wamepatikana na ugonjwa huo. Hata hivyo, kuchunguza dalili na kuutambua ugonjwa huo ni jambo gumu sana hata kwa wataalamu wa tiba. Dakt. Francis Mark Mondimore wa Chuo cha Tiba katika Chuo Kikuu cha Johns Hopkins, anaandika hivi: “Ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika ni ugonjwa wa akili unaobadilika kama kinyonga kwani dalili za wagonjwa hutofautiana na hata kipindi kimoja cha ugonjwa hutofautiana na kingine kwa mgonjwa yuleyule. Ugonjwa huo ni kama zimwi linalosababisha hofu nyingi na kutoweka, kisha hutokea tena kwa kishindo baada ya miaka mingi na kumfanya mgonjwa asisimuke kupita kiasi.”
Ni wazi kwamba si rahisi kugundua magonjwa ya kihisia na ni vigumu hata zaidi kukabiliana nayo. Lakini wagonjwa wana matumaini.
[Maelezo ya Chini]
a Sababu moja ni kwamba wanawake wanaweza kushuka moyo baada ya kujifungua na kuathiriwa na mabadiliko ya homoni wakati wa kukoma kwa hedhi. Pia, wanawake huenda hospitalini mara nyingi na hivyo wengi huchunguzwa.
b Baadhi ya majina katika makala hizi yamebadilishwa.
c Madaktari wanasema kwamba mara nyingi kila hisia huendelea kwa miezi mingi. Hata hivyo, wanasema kwamba hisia za wagonjwa fulani hubadilika haraka-haraka mara kadhaa kwa mwaka. Hisia za wagonjwa wachache hubadilika-badilika katika kipindi cha saa 24.
[Blabu katika ukurasa wa 6]
“Ni mara chache tu ambapo wagonjwa wenye hisia zinazobadilika-badilika huishi maisha ya kawaida.”—GLORIA
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]
Dalili za Kushuka Moyo Sanad
● Kushuka moyo siku nzima, karibu kila siku kwa angalau majuma mawili
● Kutopendezwa na shughuli zilizopendeza hapo awali
● Kupunguza au kuongeza uzito sana
● Kulala sana au kukosa usingizi kwa ukawaida
● Kufanya mambo haraka-haraka au polepole sana
● Kuchoka sana bila sababu
● Kuhisi hufai au mwenye hatia, au yote mawili
● Kushindwa kukaza fikira
● Kufikiria kujiua mara nyingi
Baadhi ya dalili hizi huenda pia zikawa dalili za dysthymia—ugonjwa wa kushuka moyo kidogo lakini kwa muda mrefu
[Maelezo ya Chini]
d Orodha hii inaonyesha tu baadhi ya dalili za kushuka moyo na haipasi kutumiwa kubainisha ugonjwa wa kushuka moyo. Nyingine huenda zikawa dalili za matatizo mengine mbali na ugonjwa wa kushuka moyo.
-
-
Tumaini kwa WanaouguaAmkeni!—2004 | Januari 8
-
-
Tumaini kwa Wanaougua
ZAMANI, watu waliwaepuka watu wenye magonjwa ya kihisia. Hivyo, wengi waliougua walitengwa na jamii. Baadhi yao walifutwa kazi au hawangeweza kuajiriwa. Wengine walikataliwa na watu wa familia. Mara nyingi, jambo hilo lilizidisha matatizo na kuwazuia wasipate msaada.
Hata hivyo, katika miaka ya majuzi ugonjwa wa kushuka moyo na wa hisia zinazobadilika-badilika umeeleweka zaidi. Sasa inajulikana kwamba magonjwa hayo yanaweza kutibiwa. Lakini si rahisi sikuzote kupata msaada. Kwa nini?
Kutambua Dalili
Ugonjwa wa kihisia hauwezi kutambuliwa kwa kupima damu au kwa picha ya eksirei. Badala yake, tabia ya mtu, jinsi anavyofikiri, na kufanya maamuzi huchunguzwa kwa muda fulani. Dalili fulani lazima zionekane ili ugonjwa huo utambuliwe. Nyakati nyingine watu wa familia na marafiki huwa hawajui kwamba mtu anaugua ugonjwa huo wanapoona dalili. Dakt. David J. Miklowitz anaandika hivi: “Hata watu wanapoona tabia ya mtu imebadilika, wao huwa na maoni tofauti kuhusu kisababishi chake.”
Isitoshe, hata watu wa familia wanapoona kwamba mtu ni mgonjwa sana, huenda wakashindwa kumsadikisha kwamba anahitaji matibabu. Au ikiwa wewe ndiwe mgonjwa, huenda usitake kutafuta msaada. Dakt. Mark S. Gold anaandika hivi: “Labda unaamini yale unayofikiri unaposhuka moyo—kwamba hufai, hivyo hakuna haja ya kuomba msaada ikiwa huna tumaini. Huenda ukataka kutafuta ushauri lakini unafikiri kwamba kushuka moyo ni jambo la aibu, kwamba wewe ndiwe mwenye lawama. . . . Labda hujui kwamba umeshuka moyo.” Hata hivyo, watu walioshuka moyo sana wanahitaji kumwona daktari.
Bila shaka, sote hushuka moyo wakati fulani na hiyo haimaanishi kwamba tuna ugonjwa wa kihisia. Lakini vipi hisia hizo zikiendelea? Ama vipi zikidumu kwa muda mrefu isivyo kawaida, labda majuma mawili au zaidi? Zaidi ya hayo, tuseme huzuni hiyo haikuruhusu kufanya shughuli za kila siku, iwe ni kazini, shuleni, au shughuli za kirafiki. Wakati huo, huenda ikafaa kumwona daktari anayeweza kuchunguza na kutibu magonjwa ya kihisia.
Iwapo ugonjwa huo umesababishwa na kasoro ya kemikali mwilini, huenda ukaandikiwa dawa. Katika visa fulani, huenda mgonjwa akapewa mashauri ya kumsaidia akabiliane na hali hiyo. Nyakati nyingine, njia zote mbili zimetumiwa kwa matokeo.a Jambo la maana ni kutafuta na kupata msaada. Lenore, anayeugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika aliyetajwa katika makala iliyotangulia, anasema: “Mara nyingi wagonjwa huogopa na kuaibika kwa sababu ya hali yao. Hata hivyo, mtu huaibika zaidi anapojua ana tatizo na hatafuti msaada anaohitaji sana.”
Lenore anaelezea hali yake hivi: “Nililala kwa mwaka mmoja hivi. Kisha, siku moja nilipojihisi nina nguvu kidogo, niliamua kumwona daktari.” Lenore alipimwa na kupatikana na ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika, na kupewa matibabu. Hilo lilibadilisha maisha yake. Lenore anasema: “Mimi hujihisi vizuri ninapotumia dawa, ingawa ninahitaji kujikumbusha kwamba nikiacha kuzitumia ugonjwa utarudi.”
Hali yake ni kama ya Brandon ambaye ameshuka moyo. Anasema: “Nilipokuwa kijana, mara nyingi nilitaka kujiua kwa sababu nilijihisi sifai hata kidogo. Nilienda kumwona daktari nikiwa na miaka 30 na kitu.” Kama Lenore, Brandon anatumia dawa kukabiliana na ugonjwa huo, lakini mengi zaidi yanahusika. Anasema: “Ili niwe na afya bora, mimi hutunza akili na mwili wangu. Mimi hupumzika na kula vizuri. Mimi pia hujaza akili na moyo wangu kwa mawazo yajengayo kutoka katika Biblia.”
Hata hivyo, Brandon anasema ugonjwa wa kushuka moyo ni tatizo la kitiba si la kiroho. Kutambua jambo hilo ni muhimu ili kupona. Brandon asimulia: “Wakati mmoja Mkristo mwenzangu mwenye nia nzuri aliniambia kwa kuwa andiko la Wagalatia 5:22, 23 linasema kwamba shangwe ni tunda la roho takatifu ya Mungu, nimeshuka moyo kwa sababu nimeihuzunisha roho hiyo. Jambo hilo lilinifanya nihisi hatia na kushuka moyo hata zaidi. Lakini nilipoanza kupata msaada, huzuni ilianza kwisha. Nilihisi vizuri zaidi! Laiti ningetafuta msaada mapema.”
Kushinda Hisia Mbaya
Hata baada ya ugonjwa kugunduliwa na kuanza kutibiwa, yaelekea mgonjwa ataendelea kuathiriwa. Kelly, ambaye anapambana na ugonjwa mbaya wa kushuka moyo amefaidika sana kutokana na msaada wa daktari. Pia, ametambua kwamba msaada wa wengine ni muhimu sana. Mwanzoni, Kelly hakutaka kuomba msaada kwa sababu hakutaka kuwa mzigo kwa wengine. Anasema: “Nilihitaji kujifunza kuomba msaada na kuukubali. Nilipowaeleza wengine jinsi nilivyohisi ndipo nilipoanza kupata nafuu.”
Akiwa Shahidi wa Yehova, Kelly huhudhuria mikutano pamoja na waamini wenzake kwenye Jumba la Ufalme. Hata hivyo, wakati mwingine hata pindi hizo zenye furaha huleta magumu. Anasema: “Mara nyingi mwangaza, kuchangamana na watu, na kelele hunisumbua sana. Kisha mimi huhisi hatia na kushuka moyo zaidi kwa sababu nahisi kwamba naugua kwa kuwa mimi si mtu wa kiroho.” Kelly hushughulikiaje hali hiyo? Anasema: “Nimejifunza kwamba ugonjwa wa kushuka moyo unahitaji kutibiwa. Ninapougua, haimaanishi kwamba upendo wangu kwa Mungu na kwa Wakristo wenzangu umepungua. Ugonjwa wangu si kipimo cha hali yangu ya kiroho.”
Lucia, aliyetajwa mapema katika mfululizo huu wa makala, anathamini sana matibabu mazuri ambayo amepata. Anasema: “Daktari amenisaidia sana kujua jinsi ya kushughulikia hisia zangu zinazobadilika-badilika.” Lucia pia anakazia umuhimu wa kupumzika. Anasema hivi: “Usingizi ni wa maana sana katika kushughulika na msisimuko wa kupita kiasi. Ninapokosa kulala vizuri, msisimuko unaongezeka. Nimejizoeza kupumzika kitandani hata kama sipati usingizi.”
Sheila, aliyetajwa mapema pia, amefaidika kwa kuandika jinsi anavyohisi kila siku katika kitabu. Mtazamo wake umebadilika sana. Lakini bado anapata magumu fulani. Sheila anasema: “Kwa sababu fulani, uchovu hunifanya niathiriwe na mawazo mabaya. Lakini nimejua kuyakomesha au angalau kuyapunguza.”
Kufarijiwa na Neno la Mungu
Biblia huwaimarisha wengi walio na ‘fikira zinazofadhaisha.’ (Zaburi 94:17-19, 22) Kwa mfano, Cherie alisema kwamba andiko la Zaburi 72:12, 13 lilimsaidia sana. Hapo mtunga-zaburi anasema hivi kuhusu Mfalme aliyewekwa na Mungu, Yesu Kristo: “Atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi. Atamsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini, naye ataziokoa nafsi za maskini.” Cherie pia ametiwa moyo na maneno ya mtume Paulo kwenye Waroma 8:38, 39: “Nimesadiki kwamba wala kifo wala uzima wala malaika wala serikali wala mambo yaliyopo sasa wala mambo yatakayokuja wala nguvu wala kimo wala kina wala uumbaji mwingine wowote havitaweza kututenga na upendo wa Mungu.”
Elaine, anayeugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika, ameimarishwa kwa sababu ana uhusiano mzuri pamoja na Mungu. Yeye hufarijiwa sana na maneno haya ya mtunga-zaburi: “Moyo uliovunjika na kupondwa, Ee Mungu, hutaudharau.” (Zaburi 51:17) Anasema: “Nimefarijiwa kujua kwamba Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo, Yehova, ananielewa. Nimeimarishwa kwa kumkaribia katika sala, hasa ninapofadhaika na kusononeka sana.”
Kama tulivyoona, ni vigumu kuishi na ugonjwa wa kihisia. Hata hivyo, Cherie na Elaine wamegundua kwamba kumtegemea Mungu katika sala na kupata matibabu yanayofaa kumewawezesha waboreshe maisha yao. Watu wa familia na marafiki wanaweza kuwasaidiaje watu wanaougua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika au wa kushuka moyo?
[Maelezo ya Chini]
a Amkeni! halipendekezi tiba yoyote hususa. Wakristo wanapaswa kuhakikisha kwamba matibabu wanayotumia hayapingani na kanuni za Biblia.
[Blabu katika ukurasa wa 10]
“Nilipoanza kupata msaada, huzuni ilianza kwisha. Nilihisi vizuri zaidi!”—BRANDON
[Sanduku katika ukurasa wa 9]
Maoni ya Mwenzi wa Ndoa
“Kabla Lucia hajawa mgonjwa, wengine walivutiwa na hekima yake. Hata sasa watu wanapomtembelea mke wangu wakati ambapo ametulia, wao huvutiwa na uchangamfu wake. Lakini wengi hawajui kwamba nyakati nyingine Lucia hushuka moyo halafu anasisimuka kupita kiasi. Hiyo ni dalili ya ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika ambao ameugua kwa miaka minne iliyopita.
“Anaposisimuka, mara nyingi yeye hukaa macho hadi saa saba, saa nane, au hata saa tisa usiku akiwaza na kuwazua. Yeye huwa na nguvu nyingi sana. Yeye huhangaishwa na mambo madogo sana na kutumia pesa vibaya. Yeye hujiingiza kwenye hatari kubwa sana, akifikiri kwamba hawezi kuathiriwa kiadili, kimwili, au vinginevyo. Hali hiyo ya kusisimuka kupita kiasi inaweza kumfanya atake kujiua. Baadaye msisimuko huo hufuatwa na kushuka moyo kwa kiwango kilekile cha msisimuko.
“Maisha yangu yamebadilika sana. Hata ingawa Lucia anapata matibabu, yale tunayoweza kutimiza leo ni tofauti na yale tuliyotimiza zamani au tutakayotimiza wakati ujao. Mambo hayo hubadilika kulingana na hali zetu. Imenibidi nibadilike sana.”—Mario.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]
Mgonjwa Anapopewa Dawa
Wengine hufikiri kwamba kutumia dawa ni udhaifu. Lakini wazia jambo hili: Mtu mwenye ugonjwa wa kisukari anahitaji kutumia dawa, kutia ndani kujichoma sindano za insulini. Je, inamaanisha kwamba mtu huyo ni dhaifu? La, hasha! Hiyo ni njia ya kusawazisha kemikali mwilini mwa mgonjwa ili aendelee kuwa na afya.
Ndivyo ilivyo pia na matibabu ya ugonjwa wa kushuka moyo au wa hisia zinazobadilika-badilika. Ingawa watu wengi wamefaidika kutokana na ushauri ambao umewasaidia kuelewa ugonjwa wao, inafaa kutahadhari. Ikiwa kemikali za mwili zinahusika, ugonjwa huo hauwezi kumalizwa kwa mashauri. Steven, anayeugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika anasimulia: “Daktari aliyenitibu alitumia mfano huu: Unaweza kumfundisha sana mtu fulani kuendesha gari, lakini ukimpa gari ambalo halina usukani au breki, basi mafunzo hayo hayatamsaidia. Vivyo hivyo, huenda mashauri pekee yasimsaidie mtu aliyeshuka moyo. Hatua ya kwanza ni kusawazisha kemikali za ubongo.”
[Picha katika ukurasa wa 10]
Biblia huwaimarisha wengi walio na mawazo yasiyofaa
-
-
Wengine Wanaweza Kusaidiaje?Amkeni!—2004 | Januari 8
-
-
Wengine Wanaweza Kusaidiaje?
LABDA unamjua mtu anayeugua ugonjwa wa kushuka moyo au wa hisia zinazobadilika-badilika. Ikiwa ndivyo, unawezaje kumtegemeza? D. J. Jaffe wa Shirika la Kitaifa la Wagonjwa wa Akili anashauri hivi: “Tofautisha ugonjwa na mgonjwa; chukia ugonjwa lakini umpende mgonjwa.”
Kwa sababu ya kuwa na subira na upendo, mwanamke anayeitwa Susanna alifaulu kufanya hivyo. Rafiki yake aliugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika. Susanna anasema: “Nyakati nyingine hata hakutaka kuniona.” Badala ya kukata tamaa, Susanna alifanya utafiti ili aufahamu ugonjwa huo. Anasema: “Sasa natambua jinsi rafiki yangu alivyoathiriwa na ugonjwa wake.” Susanna anasema kwamba kuna faida kubwa kumwelewa mgonjwa. Anasema: “Jambo hilo linaweza kukusaidia kupenda na kuthamini zaidi sifa nzuri za mgonjwa.”
Ikiwa anayeugua ni mshiriki wa familia, anahitaji kutiwa moyo sana. Mario, aliyetajwa katika makala zilizotangulia, alijifunza jambo hilo mapema. Mke wake, Lucia, ambaye pia alitajwa mapema, anaugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika. Mario anasema: “Mwanzoni, nilifaidika kwa kuandamana na mke wangu alipoenda kumwona daktari na kujifunza kuhusu ugonjwa huo wa ajabu ili nifahamu jambo ambalo tunakabili. Mimi na Lucia tulizungumza sana na tukashughulikia hali yoyote iliyotokea.”
Utegemezo wa Kutaniko la Kikristo
Biblia huwashauri Wakristo wote ‘waseme kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika’ na ‘kuwa wenye ustahimilivu kuelekea wote.’ (1 Wathesalonike 5:14) Unawezaje kufanya hivyo? Kwanza, ni muhimu kuelewa tofauti kati ya ugonjwa wa akili na wa kiroho. Kwa mfano, mwandikaji wa Biblia Yakobo alisema kwamba sala inaweza kumsaidia mtu mwenye ugonjwa wa kiroho apone. (Yakobo 5:14, 15) Hata hivyo, Yesu alisema kwamba wale wenye matatizo ya kimwili wanahitaji daktari. (Mathayo 9:12) Bila shaka, inafaa sikuzote kusali kwa Yehova kuhusu matatizo yoyote, kutia ndani ya afya. (Zaburi 55:22; Wafilipi 4:6, 7) Lakini, Biblia haisemi kwamba matatizo ya kiafya yanaweza kusuluhishwa tu kwa kuongeza utendaji wa kiroho.
Hivyo, Wakristo wenye utambuzi huepuka kudokeza kwamba watu walioshuka moyo wamejiletea matatizo. Matamshi kama hayo ni kama yale ya watu waliodai kumfariji Ayubu lakini hawakumsaidia. (Ayubu 8:1-6) Ukweli ni kwamba mara nyingi ugonjwa wa kushuka moyo hauwezi kupona bila matibabu, hasa ikiwa mgonjwa ameshuka moyo sana na hata anataka kujiua. Katika hali kama hizo, daktari anahitajika.
Isitoshe, kuna mambo ambayo Wakristo wenzetu wanaweza kufanya ili kusaidia. Bila shaka, subira inahitajiwa. Kwa mfano, shughuli fulani za Kikristo zinaweza kuwashinda watu wenye magonjwa ya kihisia. Diane, mwenye hisia zinazobadilika-badilika, anasema: “Ni vigumu kwangu kuhubiri. Ni vigumu kuwapelekea wengine habari njema zenye furaha kutoka kwa Biblia nikiwa sijisikii vizuri na sina furaha.”
Ili uwasaidie wagonjwa hao, jitahidi kuwa mwenye huruma. (1 Wakorintho 10:24; Wafilipi 2:4) Jaribu kuona mambo kama mgonjwa anavyoyaona. Usimlemee mgonjwa kwa kumtarajia afanye mengi. Carl, ambaye ameshuka moyo, anasema: “Watu wasipotarajia mengi kutoka kwangu, pole kwa pole mimi huanza kujiheshimu. Kwa msaada wa marafiki wenye umri mkubwa nimeweza kujenga uhusiano wa karibu na Mungu na nimepata furaha nyingi sana kwa kuwasaidia wengine wafanye hivyo.”
Wagonjwa wanaweza kupata kitulizo kikubwa wakisaidiwa. Fikiria mfano wa mwanamke Mkristo anayeitwa Brenda ambaye pia ana ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika. Anasema: “Marafiki wangu kutanikoni wamenisaidia na kunijali ninaposhuka moyo badala ya kunishutumu kuwa dhaifu kiroho. Mara nyingi wameniruhusu tuandamane kwenye utumishi na kuacha nisikilize tu au kunihifadhia kiti kwenye Jumba la Ufalme ili niingie wakati ambapo watu wote wameketi.”
Cherie, ambaye ameshuka moyo na alitajwa katika makala iliyotangulia, pia amesaidiwa sana na wazee wa kutaniko wenye upendo na wanaojali. Anasema: “Wazee hunihakikishia kwamba Yehova ananipenda na hunisomea Neno la Mungu, Biblia, na kunieleza juu ya kusudi la Yehova la kuleta paradiso yenye amani na afya bora. Wanaposali nami hata kwenye simu, mimi hujihisi vizuri. Ninajua kwamba Yehova na ndugu zangu hawajanitupa na hilo huniimarisha.”
Hakuna shaka kwamba watu wa familia na marafiki wanaweza kumsaidia sana mgonjwa ajihisi vizuri. Lucia anasema: “Sasa naona ninaweza kudhibiti maisha yangu. Mimi na mume wangu tumejitahidi kukabiliana na hali hiyo, na sasa hali ni afadhali sana.”
Wengi ambao wamepambana na magonjwa ya akili wametambua kwamba hilo ni pambano la muda mrefu. Hata hivyo, Biblia inaahidi kwamba katika ulimwengu mpya wa Mungu, “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24) Hakutakuwa na magonjwa yenye kutaabisha ambayo yanawakumba watu wengi leo. Inachangamsha moyo sana kufikiria ahadi ya Mungu ya ulimwengu mpya ambapo magonjwa yote, kutia ndani ya kihisia, yatatokomea kabisa. Biblia inasema kwamba wakati huo hakutakuwa maombolezo wala kilio wala maumivu.—Ufunuo 21:4.
[Blabu katika ukurasa wa 12]
Yesu alisema kwamba wagonjwa wanahitaji daktari.—MATHAYO 9:12
[Blabu katika ukurasa wa 13]
Biblia inaahidi kwamba katika ulimwengu mpya wa Mungu, “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”—ISAYA 33:24
-