-
Kuzorota kwa Maadili Ulimwenguni PoteAmkeni!—2007 | Aprili
-
-
Kuzorota kwa Maadili Ulimwenguni Pote
“KILA mahali watu hudanganya,” anasema David Callahan, ambaye aliandika kitabu kuhusu mazoea ya watu kudanganya (The Cheating Culture) kilichotolewa hivi majuzi. Baadhi ya mambo anayotaja ambayo yanafanyika nchini Marekani ni, “wanafunzi wa sekondari na vyuo vikuu kuiba mitihani,” kutoa nakala za muziki na filamu bila idhini, “wizi kazini,” “ulaghai wa hali ya juu katika huduma za afya,” na kutumia dawa za kuongeza nguvu katika michezo. Anakata kauli hivi: “Mambo hayo yote pamoja na ukiukaji wa haki na sheria yanaonyesha kwamba maadili yamezorota sana.”
Gazeti The New York Times lilisema kwamba Tufani Katrina, ambayo ilikumba Marekani mwishoni mwa mwaka wa 2005, “ilitokeza mojawapo ya mbinu za ulaghai na mipango ya hila ya hali ya juu na maamuzi ya kipumbavu sana yaliyosababisha matumizi mabaya sana ya pesa za serikali katika nyakati za kisasa.” Seneta mmoja nchini Marekani alisema: “Ilishangaza sana kuona ulaghai huo wa wazi, ujasiri uliohusika kufanya mipango hiyo ya hila, na matumizi mabaya sana ya pesa za serikali.”
Bila shaka, bado kuna watu wasio na ubinafsi wanaoonyesha fadhili za kibinadamu. (Matendo 27:3; 28:2) Lakini mara nyingi tunawasikia watu wakisema: “Nitafaidikaje?” Inaonekana kwamba mtazamo wa ubinafsi na kujitanguliza ndio unaotawala.
Inasemekana kwamba wakati uliopita, ubinafsi na ukosefu mbaya sana wa maadili ulichangia kuporomoka kwa milki mbalimbali, kama vile Milki ya Roma. Je, mambo yanayotendeka sasa yanaweza kuwa dalili ya tukio kubwa zaidi? Je, si wazi kwamba ulimwengu mzima unaathiriwa na “kuongezeka kwa uasi-sheria,” ambao Biblia ilitabiri kuwa ungeonyesha mwisho wa mfumo huu wa mambo unakaribia?—Mathayo 24:3-8, 12-14; 2 Timotheo 3:1-5.
Hali Inazidi Kuzorota Ulimwenguni Pote
Likiripoti kuhusu “warsha juu ya kutendewa vibaya kingono na ponografia (picha au habari za ngono)” katika maeneo ya mabanda ya sehemu moja nchini Uganda, gazeti Africa News la Juni 22, 2006 (22/6/2006) lilisema kwamba “uzembe wa wazazi umefanya ukahaba na matumizi ya dawa za kulevya kuongezeka katika eneo hilo.” Gazeti hilo lilisema: “Ofisa anayesimamia Kitengo cha Ulinzi wa Watoto na Familia katika Kituo cha Polisi cha Kawempe, Bw. Dhabangi Salongo, alisema kwamba visa vya watoto kutendewa vibaya na jeuri nyumbani vimeongezeka sana.”
Daktari mmoja nchini India alisema kwamba “jamii inapoteza misingi yake ya kitamaduni.” Mwelekezaji mmoja wa filamu nchini humo alisema kwamba “kuongezeka kwa matumizi ya dawa za kulevya na ukosefu wa maadili katika ngono ni ishara nyingine inayoonyesha kwamba India inazama katika ‘upotovu wa maadili kama ule wa nchi za Magharibi.’”
Hu Peicheng, katibu-mkuu wa Shirika la Mambo ya Jinsia na Kujamiiana la China huko Beijing, alisema hivi: “Zamani katika jamii, tulijua kutofautisha lililo sawa na lililo kosa. Sasa tunaweza kufanya chochote tutakacho.” Makala moja katika gazeti China Today ilieleza hivi: “Siku hizi jamii inazidi kukubali ngono nje ya ndoa.”
Hivi karibuni, Gazeti Yorkshire Post lilisema: “Inaonekana kwamba watu wanapenda kuonyesha uchi wao katika programu za televisheni na makampuni ya biashara hutumia programu hizo ili kuuza bidhaa zao. Miaka fulani iliyopita, programu kama hizo zingezua kasheshe. Leo, tunazungukwa na picha nyingi chafu kutoka kila mahali na ponografia . . . imekubaliwa na jamii.” Gazeti hilo liliongeza kusema: “Habari ambazo wakati mmoja zilionekana kuwa zinafaa tu watu walio na umri wa zaidi ya miaka 18, leo huonwa kuwa zinafaa watu wote, na kulingana na maoni ya wanaopinga ponografia, habari hizo zinawalenga hasa watoto.”
Gazeti The New York Times Magazine lilisema hivi: ‘Baadhi ya vijana huzungumza kuhusu jinsi walivyofanya ngono kama tu wanavyozungumza kuhusu chakula watakachokula.’ Gazeti Tweens News, ambalo hutoa mwongozo kwa ajili ya wazazi walio na watoto wenye umri wa miaka 8 hadi 12, lilisema hivi: “Kwa mwandiko wa kitoto, msichana mmoja alikuwa ameandika ujumbe huu wenye kuhuzunisha sana: ‘Mama yangu ananilazimisha niwe na marafiki wa kiume na nifanye ngono. Nina umri wa miaka 12 tu . . . jamani nisaidieni!’”
Mambo yamebadilika sana. Gazeti Toronto Star la Kanada lilisema kwamba miaka michache iliyopita “wazo tu la watu wa jinsia moja kuishi pamoja waziwazi lingezua kasheshe.” Hata hivyo, Barbara Freemen, mwalimu wa historia ya jamii katika Chuo Kikuu cha Carleton, Ottawa, anasema: “Leo watu wanasema, ‘Maisha yangu ya faragha ni yangu tu. Mtu hapaswi kuyaingilia.’”
Kwa wazi, katika miongo michache iliyopita, maadili yamezorota haraka katika sehemu nyingi ulimwenguni. Ni nini kimesababisha mabadiliko hayo makubwa? Wewe binafsi unahisije kuhusu mabadiliko hayo? Na mabadiliko hayo yanaonyesha nini kuhusu wakati ujao?
-
-
Maadili Yalipoporomoka GhafulaAmkeni!—2007 | Aprili
-
-
Maadili Yalipoporomoka Ghafula
UNGESEMA maadili yalianza kuporomoka ghafula wakati gani? Je, uliona yalipoanza kuporomoka au labda una watu wa ukoo na marafiki wenye umri mkubwa ambao waliona mambo hayo yalipoanza kutendeka? Wengine wanasema kwamba Vita vya Kwanza vya Ulimwengu ambavyo vilianza 1914, vilitokeza kipindi hiki cha maadili yaliyopotoka kupita kiasi. Profesa wa historia Robert Wohl aliandika hivi katika kitabu chake (The Generation of 1914) kinachozungumzia kizazi cha 1914: “Wale walioishi wakati wa vita wanaamini kabisa kwamba ulimwengu mmoja uliisha na mwingine ukaanza Agosti 1914.”
“Kila mahali, viwango vya tabia katika jamii ambavyo tayari vilikuwa vikiporomoka viliharibika kabisa,” anasema mwanahistoria Norman Cantor. “Ikiwa wanasiasa na majenerali waliwatendea mamilioni waliokuwa chini yao kama wanyama wanaopelekwa machinjioni, basi ni kanuni gani za kidini au za kiadili ambazo zingeweza kuwazuia watu wasitendeane kwa ukatili kama wanyama wa mwituni? . . . Uchinjaji uliofanyika wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu [1914-1918] ulishusha kabisa thamani ya uhai wa mwanadamu.”
Katika kitabu chake cha kihistoria (The Outline of History), mwanahistoria Mwingereza H. G. Wells alisema kwamba baada ya ulimwengu kukubali nadharia ya mageuzi, “maadili yalianza kupotoka kwa kiwango kikubwa.” Kwa nini? Wengine walidai kwamba mwanadamu ni mnyama wa hali ya juu tu. Wells, ambaye alikuwa mwanamageuzi, aliandika hivi mnamo 1920: “Waliamua kwamba mwanadamu ni mnyama wa kijumuiya kama mbwa-mwitu wakali wa India . . . , ilionekana sawa kwao kwamba wenye nguvu kati ya binadamu walipaswa kukandamiza na kutiisha walio dhaifu.”
Kwa kweli, kama Cantor alivyosema, vita vya kwanza vya ulimwengu viliathiri sana maoni ya watu kuhusu maadili. Alieleza hivi: “Kila kitu ambacho kizazi cha zamani kilifanya kilionwa kuwa makosa, iwe ni siasa zake, mavazi, au maoni yake kuhusu ngono.” Makanisa ambayo yalipotosha mafundisho ya Kikristo kwa kukubali nadharia ya mageuzi na kuwatia moyo watu wajihusishe katika vita, yalichangia sana kuporomoka kwa maadili. Brigedia Jenerali Frank Crozier wa Uingereza aliandika: “Makanisa ya Kikristo ndiyo wachochezi wakuu wa umwagikaji wa damu ulioko, nasi tumeyatumia sana.”
Sheria za Maadili Zatupiliwa Mbali
Mwongo mmoja baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, wakati wa ile inayoitwa Miaka ya Kujitumbukiza Kwenye Anasa (1920-1929), kanuni za zamani na vizuizi vya maadili viliwekwa kando na mwelekeo wa kukubali mwenendo wowote ukachukua mahali pake. Mwanahistoria Frederick Lewis Allen anasema hivi: “Miaka kumi iliyofuatia vita hivyo inaweza kuitwa kwa kufaa kuwa Mwongo wa Tabia Mbaya. . . . Utaratibu wa mambo wa zamani pamoja na fungu la kanuni ambazo zilikuwa zimefanya uhai uwe bora na wenye thamani, zilikuwa zimetoweka, na haikuwa rahisi kupata kanuni nyingine.”
Mshuko Mkubwa wa Kiuchumi ulimwenguni ambao ulitukia katika miaka ya 1930 uliwatumbukiza watu kwenye umaskini uliowafanya wafikirie mambo kwa uzito. Hata hivyo, kufikia mwisho wa mwongo huo, ulimwengu ulikuwa umeingia tena katika vita vingine vilivyosababisha vifo na uharibifu mkubwa sana, yaani, Vita vya Pili vya Ulimwengu. Punde si punde, mataifa yakaanza kutengeneza silaha za maangamizi, na hivyo kuukomboa ulimwengu kutokana na Mshuko huo. Wakati huohuo kufanya hivyo kuliutumbukiza ulimwengu katika kuteseka na kutokeza hali zenye kuogofya sana. Kufikia mwisho wa vita hivyo, mamia ya majiji yalikuwa magofu; majiji mawili nchini Japani yalikuwa yameangamizwa kabisa, kila moja kwa bomu la atomi! Mamilioni ya watu walikufa katika kambi za mateso zenye ukatili. Kwa ujumla, vita hivyo vilisababisha vifo vya wanaume, wanawake, na watoto wapatao milioni 50.
Wakati wa hali hizo zenye kutisha sana za Vita vya Pili vya Ulimwengu, badala ya kushikamana na viwango vya maadili vilivyokuwepo kwa muda mrefu, watu walianzisha viwango vyao wenyewe vya maadili. Kitabu (Love, Sex and War—Changing Values, 1939-1945) kinachozungumzia kubadilika kwa kanuni za maadili kilisema hivi: “Ilionekana kwamba viwango vyote vya maadili kuhusu ngono vilikuwa vimeondolewa wakati wa vita, kwani ukosefu wa maadili ambao uliruhusiwa kwa watu waliokuwa vitani uliwaathiri pia raia. . . . Hekaheka na msisimko wa vita ulimomonyoa maadili, na uhai wa raia ulionekana kuwa usio na thamani kubwa kama tu ule wa askari waliokuwa vitani.”
Hofu ya kwamba mtu anaweza kufa wakati wowote iliwafanya watu watamani sana kuwa na mahusiano ya kimahaba, hata kwa muda mfupi tu. Akitetea utovu huo wa maadili katika ngono wakati wa miaka hiyo ya vita, mwanamke mmoja Mwingereza alisema hivi: “Si eti tulikuwa na maadili mapotovu, ni kwamba tu vita vilikuwa vikiendelea.” Askari mmoja Mmarekani alikiri hivi, “Kwa maoni ya watu wengi, tulikuwa na maadili mapotovu, lakini tulikuwa vijana na tungeweza kufa wakati wowote.”
Watu wengi walionusurika vita hivyo waliathiriwa sana na mambo yenye kutisha waliyoyaona. Hadi leo, watu wengine kutia ndani wale ambao wakati huo walikuwa watoto, hukumbuka matukio hayo vizuri sana na kuhisi ni kana kwamba yanatukia tena. Wengi walipoteza imani yao na viwango vya maadili. Bila kuheshimu mamlaka yoyote ambayo inaweza kuweka viwango vya lililo sawa na lililo kosa, watu walianza kuona mambo yote yanaweza kubadilika ikitegemea hali.
Viwango Vipya
Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, uchunguzi mbalimbali ulichapishwa kuhusu tabia ya watu kuelekea ngono. Uchunguzi mmoja kama huo nchini Marekani katika miaka ya 1940 uliitwa Ripoti ya Kinsey iliyokuwa na zaidi ya kurasa 800. Kwa sababu hiyo, watu wengi walianza kuzungumza waziwazi kuhusu mambo ya ngono ambayo kabla ya hapo hayangeweza kuzungumziwa waziwazi. Ingawa baadaye ilionekana kwamba takwimu zilizotolewa katika ripoti hiyo kuhusu watu wanaofanya ngono na watu wa jinsi yao na matendo mengine mapotovu ya ngono zilikuwa zimetiliwa chumvi, uchunguzi huo ulifunua jinsi maadili yalivyoporomoka baada ya vita hivyo.
Kwa kipindi fulani, kulikuwa na jitihada ya kudumisha maadili yanayofaa. Kwa mfano, kwenye redio, sinema, na televisheni, habari chafu zilichujwa. Lakini jambo hilo halikudumu. William Bennett, ambaye awali alikuwa waziri wa elimu wa Marekani, alieleza hivi: “Hata hivyo, kufikia miaka ya 1960, ustaarabu ulianza kuporomoka kwa kasi nchini Marekani.” Jambo hilo lilionekana pia katika nchi nyingine nyingi. Kwa nini maadili yaliporomoka kwa kasi sana katika miaka ya 1960?
Kana kwamba mambo hayo yalitendeka kwa mfululizo, harakati ya kuwakomboa wanawake na kubadilika kwa mitazamo kuhusu ngono pamoja na yale yaliyoitwa maadili mapya, yalianza mwongo huohuo. Pia, dawa za kupanga uzazi zilibuniwa. Kwa kuwa sasa watu wangeweza kufurahia ngono bila hofu ya kupata mimba, walianza kufanya ngono ovyoovyo bila kuwajibika.
Wakati huohuo, vyombo vya habari, sinema, na televisheni vililegeza viwango vyake vya maadili. Baadaye, Zbigniew Brzezinski, ambaye hapo awali alikuwa mkuu wa Baraza la Usalama wa Kitaifa la Marekani alisema hivi kuhusu maadili yanayoonyeshwa katika televisheni: “Wanatukuza kujitosheleza, wao huonyesha jeuri na ukatili kuwa mambo ya kawaida, [na] wanaunga mkono kufanya ngono na watu wengi.”
Kufikia miaka ya 1970, mashine za kuchezea kanda za video zilikuwa zimeanza kutumiwa sana. Sasa watu wangeweza kuona picha chafu sana wakiwa faraghani, habari ambazo hawangeweza kutazama katika majumba ya sinema ya umma. Katika nyakati za karibuni, mtu yeyote aliye na kompyuta, popote alipo ulimwenguni anaweza kupata ponografia chafu zaidi kwenye Intaneti.
Matokeo yake yanatisha. Hivi majuzi, msimamizi mmoja wa gereza huko Marekani alisema: “Miaka kumi iliyopita vijana walipoletwa hapa, ningeweza kuwapa mashauri kuhusu lililo sawa na lililo kosa. Lakini vijana wanaoletwa siku hizi hawaelewi ninasema nini.”
Tunaweza Kupata Wapi Mwongozo?
Hatuwezi kutafuta mwongozo kuhusu maadili kutoka kwa makanisa ya ulimwengu. Badala ya kushikilia kanuni za uadilifu kama Yesu na wafuasi wake wa karne ya kwanza, makanisa yamejifanya kuwa sehemu ya ulimwengu huu na matendo yake maovu. Mwandishi mmoja aliuliza hivi: “Ni vita gani ambavyo vimewahi kupiganwa ambavyo haikudaiwa kwamba Mungu alikuwa akiunga mkono pande zote?” Kasisi mmoja huko New York City alisema hivi miaka fulani iliyopita kuhusu kushikilia viwango vya Mungu vya maadili: “Kanisa ndilo shirika pekee ulimwenguni ambalo wafuasi wake wanahitajiwa kutimiza matakwa machache sana ya kiadili kuliko hata yale ambayo mtu anahitaji kutimiza ili aingie kwenye basi.”
Ni wazi kwamba kuporomoka haraka kwa maadili katika ulimwengu huu kunaonyesha kwamba hatua fulani zinapaswa kuchukuliwa. Hatua gani? Ni mabadiliko gani yanayohitajiwa? Ni nani atakayefanya mabadiliko hayo, nayo yatafanywaje?
[Blabu katika ukurasa wa 5]
“Uchinjaji uliofanyika wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu [1914-1918] ulishusha kabisa thamani ya uhai wa mwanadamu”
[Picha katika ukurasa wa 6, 7]
Vitumbuizo vilivyopotoka vinapatikana kwa urahisi zaidi
-
-
Ulimwengu Huu Unaelekea Wapi?Amkeni!—2007 | Aprili
-
-
Ulimwengu Huu Unaelekea Wapi?
BIBLIA ilitabiri zamani sana kuhusu kuzorota kwa maadili tunakoona leo na ikafafanua hali hiyo hivi: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, . . . wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili . . . wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakizikana nguvu zake.”—2 Timotheo 3:1-5.
Huenda ukakubali kwamba unabii huo wa Biblia unafafanua vizuri hali ya ulimwengu leo. Hata hivyo, ulirekodiwa karibu miaka 2,000 iliyopita! Unabii huo unaanza kwa maneno haya: “Katika siku za mwisho.” Maneno hayo, “siku za mwisho,” yanamaanisha nini?
“Siku za Mwisho” za Nini?
Maneno “siku za mwisho” yanatumika sana siku hizi. Katika Kiingereza peke yake, maneno hayo yanatumiwa katika vichwa vya vitabu vingi sana. Kwa mfano, fikiria kitabu cha karibuni, The Last Days of Innocence—America at War, 1917-1918 (Siku za Mwisho za Kutokuwa na Hatia—Marekani Vitani, 1917-1918). Dibaji ya kitabu hicho inaeleza wazi kwamba maneno “siku za mwisho,” yanapotumiwa katika kitabu hicho, yanarejelea kipindi fulani hususa ambacho kimekuwa na upotovu mkubwa wa maadili.
Dibaji hiyo inaendelea kusema hivi: “Mnamo 1914, nchi hiyo ilikuwa ikibadilika haraka zaidi kuliko wakati mwingine wowote katika historia yake.” Kwa kweli, mnamo 1914 ulimwengu ulitumbukia katika vita ambavyo havikuwa vimewahi kutokea. Kitabu hicho kinasema: “Hivyo vilikuwa vita kamili, si vita kati ya jeshi moja na jeshi lingine, bali vita kati ya taifa moja na lingine.” Vita hivyo, kama tutakavyoona, vilitukia mwanzoni mwa kile kipindi ambacho Biblia inakiita “siku za mwisho.”
Biblia inafundisha kwamba ulimwengu utapitia kipindi hususa kinachoitwa “siku za mwisho.” Kwa kweli, Biblia inasema kwamba kulikuwa na ulimwengu ambao ulipitilia mbali au ulikwisha. Inaeleza hivi: “Ulimwengu wa wakati huo uliangamia kwa gharika ya maji.” Jambo hilo lilitukia lini, na ni ulimwengu upi huo uliokwisha? Ulikuwa ‘ulimwengu wa kale wa watu wasiomwogopa Mungu’ katika siku za mtu aliyeitwa Noa. Vivyo hivyo ulimwengu wa leo utakwisha. Hata hivyo, wale wanaomtumikia Mungu wataokoka mwisho wa ulimwengu huu, kama vile Noa na familia yake walivyookoka.—2 Petro 2:5; 3:6; Mwanzo 7:21-24; 1 Yohana 2:17.
Yale Ambayo Yesu Alisema Kuhusu Mwisho
Yesu Kristo pia alizungumza kuhusu “siku za Noa” wakati ‘gharika ilikuja na kuwafagilia mbali wote.’ Alilinganisha hali zilizokuwepo kabla ya Gharika, yaani, kabla tu ya ulimwengu huo kwisha, na hali ambazo zingekuwepo katika kipindi ambacho alitaja kuwa “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3, 37-39) Tafsiri nyingine za Biblia hutumia usemi “mwisho wa dunia” au “mwisho wa nyakati.”—Union Version, Zaire Swahili Bible, na Biblia Habari Njema.
Yesu alitabiri jinsi ambavyo maisha yangekuwa duniani kabla tu ya ulimwengu kwisha. Alisema hivi kuhusu vita: “Taifa litasimama kupigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme.” Wanahistoria wamesema kwamba hilo lilitukia kuanzia mwaka wa 1914. Hiyo ndiyo sababu dibaji ya kitabu kilichotajwa ilisema kwamba 1914 ulikuwa mwanzo wa “vita kamili, si vita kati ya jeshi moja na jeshi lingine, bali vita kati ya taifa moja na lingine.”
Katika unabii wake, Yesu aliongezea hivi: “Kutakuwa na upungufu wa chakula na matetemeko ya nchi mahali pamoja baada ya pengine. Mambo yote hayo ni mwanzo wa maumivu ya taabu.” Aliendelea kusema kwamba kungekuwa na mambo mengine mengi kutia ndani “kuongezeka kwa uasi-sheria.” (Mathayo 24:7-14) Kwa kweli tumeona mambo hayo yakitukia. Leo maadili yamezorota sana hivi kwamba yanatimiza unabii wa Biblia!
Tunapaswa kuishije katika siku hizi zenye maadili yaliyopotoka? Ona yale ambayo mtume Paulo aliwaandikia Wakristo huko Roma kuhusu kuzorota kwa maadili. Alitaja kuhusu “hamu za ngono yenye kufedhehesha” ambazo watu walikuwa nazo, akisema hivi: “Wanawake wao walibadili matumizi yao wenyewe ya asili kuwa yale yaliyo kinyume cha asili; na vivyo hivyo pia hata wanaume waliacha matumizi ya asili ya mwanamke na kuwakiana tamaa kali katika uchu wao kuelekeana wao wenyewe, wanaume kwa wanaume, wakitenda mambo machafu.”—Waroma 1:26, 27.
Wanahistoria wanasema kwamba wakati huo jamii ya wanadamu ilipokuwa ikizama katika upotovu wa maadili, “Wakristo wachache waliokuwapo walisumbua dhamiri za ulimwengu huo wa kipagani uliopenda anasa kwa sababu walimcha Mungu na walikuwa na mwenendo safi kiadili.” Hilo linapaswa kutufanya tutue kidogo na kujiuliza: ‘Namna gani mimi na marafiki ninaochagua? Je, tunaonekana kuwa tofauti, wenye maadili mazuri, tofauti na wengine walio na maadili mabaya?’—1 Petro 4:3, 4.
Jambo Tunalokabiliana Nalo
Biblia inatufundisha kwamba licha ya ukosefu wa maadili unaotuzunguka, tunahitaji kuwa “wasio na hatia, watoto wa Mungu wasio na dosari katikati ya kizazi kilicho kombo na kilichopotoka.” Ili kufanya hivyo, tunahitaji “kulishika sana neno la uzima.” (Wafilipi 2:15, 16) Maneno hayo ya Biblia yanaonyesha jinsi ambavyo Wakristo wanaweza kubaki bila doa kiadili. Wanahitaji kushika sana mafundisho ya Neno la Mungu na kutambua kwamba kufuata viwango vyake vya maadili ndiyo njia bora zaidi ya maisha.
“Mungu wa mfumo huu wa mambo,” Shetani Ibilisi, anajaribu kuvuta watu upande wake. (2 Wakorintho 4:4) Biblia inatuambia kwamba ‘anaendelea kujigeuza mwenyewe kuwa malaika wa nuru.’ Wahudumu wake, yaani, wale wanaomtumikia kwa kutenda kama yeye, hufanya vivyo hivyo. (2 Wakorintho 11:14, 15) Wanawaahidi watu uhuru na furaha, lakini Biblia inasema kwamba “wao wenyewe ni watumwa wa uharibifu.”—2 Petro 2:19.
Usijidanganye. Wale wanaopuuza viwango vya maadili vya Mungu wataona cha mtema-kuni. Mtunga-zaburi alisema: ‘Wokovu uko mbali sana na waovu, kwa maana hawajayatafuta masharti ya Mungu.’ (Zaburi 119:155; Methali 5:22, 23) Je, tunakubaliana na maneno hayo? Ikiwa ndivyo, acheni tulinde akili na mioyo yetu dhidi ya propaganda zinazoendeleza maadili mapotovu.
Hata hivyo, wengi huwaza hivi kwa njia isiyo ya hekima, ‘Ikiwa jambo ninalofanya halivunji sheria basi ni sawa.’ Lakini hilo si kweli. Kwa upendo Baba yetu wa mbinguni hatoi mwongozo kuhusu maadili ili afanye maisha yako yawe yenye kuchosha na yenye vizuizi vingi bali ili akulinde. ‘Anakufundisha ili ujifaidi mwenyewe.’ Anataka uepuke matatizo na ufurahie maisha. Naam, kama vile Biblia inavyofundisha, kumtumikia Mungu ‘kuna ahadi ya uzima wa sasa na ule utakaokuja.’ Huo ni “uzima ulio wa kweli,” uzima wa milele katika mfumo mpya alioahidi!—Isaya 48:17, 18; 1 Timotheo 4:8; 6:19.
Kwa hiyo, linganisha manufaa ya kufuata mafundisho ya Biblia na maumivu ambayo huwapata wale ambao hawayafuati. Kupata kibali cha Mungu kwa kumsikiliza ndiyo njia bora zaidi ya maisha! Mungu anaahidi hivi: “Kwa habari yake mtu anayenisikiliza, yeye atakaa salama wala hatasumbuliwa na hofu ya msiba.”—Methali 1:33.
Jamii Inayofuata Maadili
Biblia inasema kwamba ulimwengu huu utakapopitilia mbali, “mtu mwovu hatakuwako tena.” Pia inasema: “Kwa maana wanyoofu ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake.” (Zaburi 37:10, 11; Methali 2:20-22) Hivyo, mabaki yote ya ukosefu wa maadili yataondolewa duniani, kutia ndani wote wanaokataa kufuata mafundisho yanayofaa ya Muumba wetu. Paradiso ya kidunia, kama ile ambayo Mungu aliwapa wanadamu wa kwanza, hatimaye itaenezwa duniani pote na wale wanaompenda Mungu.—Mwanzo 2:7-9.
Wazia shangwe ya kuishi katika dunia kama hiyo iliyo paradiso! Kati ya wale watakaopata pendeleo la kuiona watakuwa mabilioni ya wale watakaofufuliwa. Shangilia katika ahadi za Mungu: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3, 4.
[Blabu katika ukurasa wa 9]
Ulimwengu wa wakati uliopita ulipokwisha, watu fulani wanaomwogopa Mungu waliokoka
[Picha katika ukurasa wa 10]
Ulimwengu huu utakapokwisha, dunia itakuwa paradiso
-