-
Ni Nini Linalowapata Vijana?Mnara wa Mlinzi—1997 | Desemba 1
-
-
Ni Nini Linalowapata Vijana?
HABARI njema au habari mbaya—wataka kusikia ipi kwanza? Waulizwapo swali hilo, watu wengi huchagua kusikia habari mbaya kwanza wakitarajia kwamba habari njema zitadumu akilini.
Tuchunguzapo linalowapata vijana, fikiria kwanza hali ya sasa. Kwa kawaida watu wenye umri mkubwa zaidi hueleza kwamba vijana leo si kama vijana wa wakati uliopita. Kwa upande ule mwingine, vijana huonea uchungu dokezo lolote la kwamba hawafikii viwango vya mwaka-jana. Hata hivyo, wachunguzaji makini wa jamii ya binadamu hukubali kwamba vijana wa leo wako tofauti.
Tofauti Jinsi Gani?
Ingawa watu kwa ujumla huamini kwamba vijana wapaswa kuwa na adabu nzuri, kuwa na hisi ya kuchukua madaraka, na kuwastahi wengine, mara nyingi uhalisi haufikii hayo. Kulingana na uchunguzi uliochapishwa katika gazeti la habari The Independent la London, vijana “[wana]kuza ‘roho mpya ya uasi’ dhidi ya ulimwengu ambao waona kuwa umewatamausha sana.” “Roho [hiyo] mpya ya uasi” yaonekana katika matokeo ya uchunguzi yaonyeshayo kwamba vijana wengi zaidi wa siku ya kisasa hawataki kujiona kuwa “wenye busara na wenye kuchukua madaraka.” Afadhali waonwe kuwa “wasiotulia na wasiotabirika.”
Kwa kielelezo, katika Uingereza, uhalifu uliorekodiwa—ambao mwingi wake ulifanywa na vijana—uliongezeka mara kumi kati ya mwaka wa 1950 na mwaka wa 1993. Ongezeko la matumizi mabaya ya dawa na alkoholi lafanana na ongezeko la uhalifu. Wakati uleule, lasema gazeti The Times la London, karibu nchi zote ambazo zimesitawi zimeona “maongezeko makubwa katika miparanganyo ya kisaikolojia na ya kijamii miongoni mwa vijana tangu Vita ya Ulimwengu ya Pili.” Kulingana na David J. Smith, profesa wa elimu-jinai, miparanganyo hiyo “[hai]husiani na hali ya uhitaji au ukwasi wenye kuongezeka katika njia yoyote sahili.” Utafiti waonyesha kwamba tofauti kubwa zaidi sasa ni dhahiri kati ya vijana na watu wenye umri mkubwa zaidi.
Leo watoto na matineja wachanga hukabili mkazo unaoongezeka. Visa vya kujaribu au kufanikiwa kujiua, vimekuwa mambo ya kawaida. Majaribio ya kujiua ya watoto wenye umri wa chini ya miaka 12 yaliongezeka maradufu kwa muda unaopungua miaka kumi, laripoti gazeti Herald la Glasgow, Scotland. Watoto wenye umri mkubwa zaidi huruhusu kukata tumaini kuwachochee kujiua. Hilo gazeti laeleza hivi: “Majaribio ya kujiua ni matokeo mabaya zaidi ya kuongezeka kwa matatizo ya kiakili katika vijana yanayoelekea sana kushinda msaada wanaotolewa.”
Ni Nani Mwenye Lawama?
Watu wazima huona likiwa jambo rahisi kuwalaumu vijana kwa sababu ya maoni ya vijana “yaliyopotoka.” Hata hivyo, kusema kweli kabisa, je, watu wazima hawana sehemu kubwa ya lawama kwa sababu ya yale yanayotukia leo miongoni mwa vijana? Kukandamizwa na marika, kupuuzwa na wazazi, kukosekana kwa vigezo vya kuiga ambavyo vijana waweza kutumaini, ni mambo ambayo hutajwa mara nyingi kuwa sababu ya tabia iliyopotoka ya vijana. “Mshuko-moyo wa watu kwa ujumla uko vilevile ulivyokuwa miaka 30 iliyopita,” adai Profesa Sir Michael Rutter, mkuu wa Medical Research Council Child Psychiatry Unit ya Uingereza. “Lakini,” aongeza kusema hivi, “kutukia kwa mshuko-moyo miongoni mwa matineja na vijana kumeongezeka sana. . . . Bila shaka kuvunjika kwa familia huchangia; si talaka tu, lakini viwango vya kawaida vya kutopatana na kupambana miongoni mwa watu wazima.”
Mtafiti mmoja adai kwamba vijana “[wana]kataa desturi.” Kwa nini? “Kwa sababu njia za kidesturi hazitumiki tena kamwe.” Kwa kielelezo chukua maoni yanayobadilika ya madaraka ya kijinsia. Wanawake wengi vijana wakubali vitabia vilivyo vya kiume zaidi vya uchokozi wa kutumia nguvu na vya ujeuri, huku wanaume vijana wakikubali vitabia vya kike. Jinsi ilivyo tofauti na kawaida za wakati uliopita!
Lakini kwa nini twaona mabadiliko haya makubwa sasa? Na kuna habari njema gani kuhusu vijana leo? Vijana waweza kuwaje na wakati ujao salama? Makala yetu inayofuata yachunguza majibu ya maswali hayo.
-
-
Vijana Wenye Wakati Ujao SalamaMnara wa Mlinzi—1997 | Desemba 1
-
-
“KAMA vile [kisa cha ubakaji] chochote kiwezavyo kuwa chenye kuogofya na cha kuchukiza mno”—hivyo ndivyo hakimu aliyekuwa akiongoza kesi ya majuzi alivyofafanua huo uhalifu. Genge la matineja wanane, wenye umri wa kuanzia miaka 14 hadi 18, lilimvizia mtalii wa kike katika eneo fulani ndani ya jiji la London, likamshambulia kingono kwa kurudia-rudia, kisha likamtupa kwenye mfereji uliokuwa karibu ingawa alisema kwamba hangeweza kuogelea. Yaeleweka kwamba, mama ya mmojawapo wa matineja hao alijulisha wazi kwamba alihisi akiwa mgonjwa alipoona ripoti ya habari za televisheni juu ya mambo ambayo mwana wake alikuwa amefanya.
Kwa kusikitisha, tukio hilo ladhihirisha linalotukia katika jamii leo. Unyama umekuwa jambo la kawaida, uwe katika utendaji wa kihalifu, zogo la nyumbani, au mapambano ya kikabila ya Wabalkani, Afrika ya kati na magharibi, na kwingineko. Vijana hukua katikati ya hali hizo, au wao huzisikia mara nyingi. Basi, si ajabu kwamba wengi hupata kuwa wakatili, wasioonyesha “shauku ya kiasili,” na “wasio na hali ya kujidhibiti.”—2 Timotheo 3:3.
“Wakali”
Mtume Mkristo Paulo alipomwandikia mzee mwenzake Timotheo barua yake ya pili, Roma ilikuwa serikali kuu ya ulimwengu. Ujahili na ukatili yalikuwa mambo yaliyoenea katika viwanja vya michezo vya Roma. Na bado, Paulo alionya kwamba wakati ujao, nyakati zingepata kuwa “ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Kwa kupendeza, neno la Kigiriki lifafanualo nyakati hizi kuwa “ngumu kushughulika nazo” latia ndani wazo la kuwa ‘kali.’ Tukio fulani wakati wa huduma ya kidunia ya Yesu zaidi ya miaka 30 mapema laonyesha jambo lililosababisha ukali fulani wa wakati wake.
Yesu alikuwa ametoka tu kuwasili kwa mashua kwenye ukingo wa mashariki wa Bahari ya Galilaya. Alipokuwa akikanyaga kwenye ukingo, wanaume wawili walimkabili. Sura yao isiyostaarabika na kupiga mayowe kwao kulifanya ieleweke kabisa kwamba jambo fulani kuwahusu halikuwa sawa hata kidogo. Walikuwa “wakali isivyo kawaida,” kwa hakika, walikuwa wamepagawa na roho waovu.a Walilopaaza sauti lilitokana na roho waovu walioongoza matendo yao ya jeuri. Wanaume hao walipiga mayowe wakisema hivi: “Tuna nini nawe, Mwana wa Mungu? Je, ulikuja hapa kututesa-tesa kabla ya wakati uliowekwa?” Roho waovu waliowapagaa wanaume hao wawili walijua vizuri kwamba Mungu alikuwa tayari ameweka wakati wa kutekeleza hukumu yake dhidi ya roho waovu. Hilo lingemaanisha uharibifu wao udumuo milele. Lakini hadi wakati huo walikuwa wadhihirishe uwezo wao mbalimbali unaopita ule wa kibinadamu ili kuchochea ujeuri mkali. Utendaji wa Yesu wa kimuujiza wa kuwafukuza roho waovu hao ndio tu ulioletea wanaume hao wawili kitulizo.—Mathayo 8:28-32; Yuda 6.
Watu leo, kutia na vijana, watendapo kwa njia yenye kichaa, yafaa tukumbuke tukio hilo. Kwa nini? Kwa sababu katika karne hii ya 20, twakabili hatari ya namna hiyo, kama vile kitabu cha mwisho cha Biblia, Ufunuo, kielezavyo: “Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameteremka kwenu, akiwa na hasira kubwa, akijua ana kipindi kifupi cha wakati.” (Ufunuo 12:12) Tafadhali, ona kwamba kutwezwa huko kwa Shetani kwaandamana na “hasira kubwa” kwa sababu ajua kwamba wakati wake ni mfupi.
Kushambuliwa
Kama itajwavyo mara nyingi kwenye kurasa za jarida hili, Kristo Yesu alitawazwa awe Mfalme wa Ufalme wa Mungu katika mbingu mwaka wa 1914. Mara moja Yesu alichukua hatua dhidi ya adui mkuu wa Mungu, Shetani. Hivyo, Ibilisi na roho waovu wake wamefukuzwa kutoka mbinguni, nao sasa waelekeza uangalifu wao juu ya dunia hii. (Ufunuo 12:7-9) Kiasi cha uvutano wake kikiwa kimewekewa mipaka sana, Shetani “hutembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta sana kunyafua mtu fulani.” (1 Petro 5:8) Ni nani walio mawindo rahisi kwake? Je, haieleweki kwamba ingekuwa wale ambao hasa hawana uzoefu katika maisha na mahusiano ya kibinadamu? Hivyo vijana leo wamekuwa malengo ya Ibilisi. Kupitia kufuatia kwingi kwao muziki na wasaa, wanatumiwa vibaya kwa urahisi na Ibilisi.—Waefeso 6:11, 12.
Hata vijana wajaribupo kufanikisha maisha yao, wao hujikuta wanazuiwa. Tangu mwisho wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, watu katika nyingi za nchi zilizokuwa vitani awali wamejaribu kulipia kwa kutolea familia zao mtindo-maisha wa ukwasi. Mali za kimwili, wasaa na burudani ya kupita kiasi, ni mambo ambayo yamekuwa miradi mikubwa. Tokeo ni kwamba wengi wameteseka. “Waazimiao kuwa matajiri,” Paulo alimwonya Timotheo, “huanguka ndani ya kishawishi na mtego na tamaa nyingi zisizo za akili na zenye kuumiza . . . Kwa maana kupenda fedha ni mzizi wa mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikilia kupenda huku wengine . . . wamejichoma wenyewe kotekote kwa maumivu mengi.” (1 Timotheo 6:9, 10) Kwa ujumla, twakuta watu wa jamii ya leo ya kufuatia vitu vya kimwili wakiwa wamechomwa kwa maumivu ya kiuchumi, kifedha, na kihisia-moyo. Miongoni mwao mna vijana wengi, wahasiriwa wa hila hiyo ya adui mkuu wa Mungu.
-