Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Epukeni Manung’uniko
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Julai 15
    • Epukeni Manung’uniko

      “Endeleeni kufanya mambo yote bila kunung’unika.”—WAFILIPI 2:14.

      1, 2. Ni shauri gani ambalo mtume Paulo aliwapa Wakristo huko Filipi na Korintho, na kwa nini?

      AKIONGOZWA kwa roho, mtume Paulo aliliandikia barua kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza huko Filipi na kulisifu sana. Aliwasifu waamini wenzake wa jiji hilo kwa sababu ya ukarimu wao na bidii yao, naye akaeleza jinsi alivyofurahia matendo yao mema. Hata hivyo, Paulo aliwakumbusha ‘waendelee kufanya mambo yote bila kunung’unika.’ (Wafilipi 2:14) Kwa nini mtume huyo alitoa shauri hilo?

      2 Paulo alijua matokeo ya kunung’unika. Miaka kadhaa mapema, alilikumbusha kutaniko la Korintho kwamba kunung’unika kunaweza kuwa hatari. Paulo alisema kwamba wakati Waisraeli walipokuwa nyikani walimkasirisha Yehova tena na tena. Jinsi gani? Kwa kutamani mambo mabaya, kwa kuabudu sanamu na kufanya uasherati, kwa kumjaribu Yehova, na kwa kunung’unika. Paulo aliwatia moyo Wakorintho wajifunze kutokana na mifano hiyo. Aliandika hivi: “Wala tusiwe wanung’unikaji, kama baadhi yao walivyonung’unika, na kuangamizwa na mwangamizaji.”—1 Wakorintho 10:6-11.

      3. Kwa nini tunapendezwa na habari ya kunung’unika?

      3 Sisi watumishi wa Yehova leo tunaonyesha roho kama ya kutaniko lililokuwa Filipi. Tuna bidii katika matendo mema, nasi tunapendana. (Yohana 13:34, 35) Hata hivyo, tunapofikiria madhara yaliyowapata watu wa Mungu zamani kwa sababu ya kunung’unika, tuna sababu nzuri ya kutii shauri hili: “Endeleeni kufanya mambo yote bila kunung’unika.” Acheni kwanza tufikirie mifano ya watu walionung’unika ambayo inatajwa katika Maandiko. Kisha, tutazungumzia mambo fulani tunayoweza kufanya ili kuepuka kusababisha madhara kwa kunung’unika.

      Kusanyiko Lenye Uovu Linamnung’unikia Yehova

      4. Waisraeli walinung’unikaje nyikani?

      4 Neno la Kiebrania linalomaanisha ‘kunung’unika au kulalamika’ linatumiwa katika Biblia kuhusiana na mambo yaliyotukia wakati Waisraeli walipokuwa nyikani kwa miaka 40. Mara kwa mara, Waisraeli walionyesha kwamba hawakuridhika na hali yao maishani, nao wakanung’unika kwa sababu hiyo. Kwa mfano, majuma machache tu baada ya kukombolewa kutoka utumwani Misri, ‘kusanyiko zima la wana wa Israeli lilianza kunung’unika juu ya Musa na Haruni.’ Waisraeli walilalamika kuhusu chakula, wakisema: “Laiti tungekufa kwa mkono wa Yehova katika nchi ya Misri tulipokuwa tukiketi kando ya vyungu vya nyama, tulipokuwa tukila mkate na kushiba, kwa sababu ninyi mmetutoa na kutuleta nyikani ili kuliua kutaniko lote kwa njaa.”—Kutoka 16:1-3.

      5. Waisraeli waliponung’unika, walikuwa wakimnung’unikia nani hasa?

      5 Lakini, Yehova alikuwa amewapa Waisraeli vitu walivyohitaji nyikani. Aliwapa chakula na maji kwa upendo. Waisraeli hawakukabili kamwe hatari ya kufa kwa njaa nyikani. Lakini, kwa sababu ya kutoridhika, walijifanya kwamba wanaumia sana, nao wakaanza kunung’unika. Ingawa walimlalamikia Musa na Haruni, machoni pa Yehova walikuwa wananung’unika hasa dhidi ya Mungu mwenyewe. Musa aliwaambia Waisraeli hivi: “Yehova amesikia manung’uniko yenu mnayonung’unika juu yake. Na sisi ni nani? Manung’uniko yenu si juu yetu, bali ni juu ya Yehova.”—Kutoka 16:4-8.

      6, 7. Kama inavyoonyeshwa kwenye Hesabu 14:1-3, mtazamo wa Waisraeli ulibadilikaje?

      6 Muda mfupi baadaye, Waisraeli walilalamika tena. Musa aliwatuma watu 12 kuipeleleza Nchi ya Ahadi. Kumi kati yao walirudi na ripoti mbaya. Ikawaje? “Wana wote wa Israeli wakaanza kunung’unika juu ya Musa na Haruni, na kusanyiko lote likaanza kusema dhidi yao: ‘Laiti tungalikufa katika nchi ya Misri, au laiti tungalikufa katika nyika hii! Na kwa nini Yehova anatuleta kwenye nchi hii [Kanaani] ili tuanguke kwa upanga? Wake zetu na watoto wetu wadogo watakuwa nyara. Je, si afadhali kwetu turudi Misri?’”—Hesabu 14:1-3.

      7 Mtazamo wa Waisraeli ulikuwa umebadilika kama nini! Mwanzoni, walipowekwa huru kutoka Misri na kukombolewa kupitia Bahari Nyekundu, uthamini wao uliwachochea kumwimbia Yehova sifa. (Kutoka 15:1-21) Lakini kwa sababu ya matatizo ya nyikani na kuwaogopa Wakanaani, watu wa Mungu walipoteza uthamini wao na kuonyesha mtazamo wa kutoridhika. Badala ya kumshukuru Mungu kwa uhuru aliowapa, walimlaumu kwa sababu walidhani kwamba wamekosa vitu fulani. Hivyo, kunung’unika kulionyesha kwamba hawakuthamini maandalizi ya Yehova. Haishangazi kwamba Yehova alisema hivi: “Kusanyiko hili lenye uovu litaendelea kuwa na manung’uniko haya ambayo linaendeleza juu yangu mpaka wakati gani?”—Hesabu 14:27; 21:5.

      Manung’uniko Katika Karne ya Kwanza

      8, 9. Toa mifano ya watu walionung’unika ambayo inatajwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

      8 Mifano hiyo kuhusu manung’uniko ilihusisha vikundi vya watu ambao yaonekana walionyesha waziwazi kwamba hawakuridhika. Hata hivyo, wakati Yesu Kristo alipokuwa Yerusalemu kwa ajili ya Sherehe ya Vibanda mwaka wa 32 W.K., “umati ulikuwa ukinong’onezana mambo mengi juu yake.” (Yohana 7:12, 13, 32) Walikuwa wakinong’onezana kumhusu Yesu, wengine wakisema kwamba yeye ni mtu mwema na wengine wakisema yeye si mwema.

      9 Pindi nyingine, Yesu na wanafunzi wake walikaribishwa katika nyumba ya yule mkusanya-kodi aliyeitwa Lawi, au Mathayo. “Mafarisayo na waandishi wao wakaanza kuwanung’unikia wanafunzi wake, wakisema: ‘Kwa nini mnakula na kunywa pamoja na wakusanya-kodi na watenda-dhambi?’” (Luka 5:27-30) Baadaye, huko Galilaya, “Wayahudi wakaanza kumnung’unikia [Yesu] kwa sababu alisema: ‘Mimi ndio mkate ambao ulishuka kutoka mbinguni.’” Hata baadhi ya wafuasi wa Yesu waliudhika kwa sababu ya mambo aliyosema, nao wakaanza kunung’unika.—Yohana 6:41, 60, 61.

      10, 11. Kwa nini Wayahudi wenye kusema Kigiriki walinung’unika, na wazee Wakristo wanaweza kufaidikaje kutokana na jinsi malalamiko hayo yalivyoshughulikiwa?

      10 Muda mfupi baada ya Pentekoste 33 W.K., kulikuwa na kisa fulani cha kunung’unika ambacho kilikuwa na matokeo mazuri. Wanafunzi wengi wapya kutoka nchi za nje ya Israeli walikuwa wakifurahia ukarimu wa waamini wenzao huko Yudea. Lakini matatizo fulani yalizuka kuhusiana na ugawaji wa maandalizi yaliyokuwepo. Simulizi linasema hivi: “Wayahudi wenye kusema Kigiriki walianza kunung’unika juu ya Wayahudi wenye kusema Kiebrania, kwa sababu wajane wao walikuwa hawaangaliwi katika ugawaji wa kila siku.”—Matendo 6:1.

      11 Wanung’unikaji hao walikuwa tofauti na Waisraeli nyikani. Wayahudi wenye kusema Kigiriki hawakulalamika kwa ubinafsi kuhusu matatizo yao wenyewe. Badala yake, walisema kwamba wajane fulani hawakuwa wakitimiziwa mahitaji yao. Isitoshe, wanung’unikaji hao hawakuzusha fujo wala hawakulalamika kwa sauti dhidi ya Yehova. Waliwaeleza mitume malalamiko yao, nao mitume wakapanga hatua ichukuliwe haraka kwa sababu malalamiko hayo yalifaa. Huo ni mfano bora sana ambao mitume waliwawekea wazee Wakristo leo! Wachungaji hao wa kiroho huepuka ‘kuziba masikio yao ili wasikie kilio cha kulalamika cha mtu wa hali ya chini.’—Methali 21:13; Matendo 6:2-6.

      Jihadhari na Madhara ya Kunung’unika

      12, 13. (a) Toa mfano unaoonyesha madhara ya kunung’unika. (b) Ni nini kinachoweza kumfanya mtu anung’unike?

      12 Mifano mingi ya Kimaandiko ambayo tumezungumzia inaonyesha kwamba manung’uniko yaliwaathiri sana watu wa Mungu wa kale. Basi, tunapaswa kufikiria kwa uzito madhara ambayo yanaweza kutokea leo kwa kunung’unika. Hebu fikiria mfano huu. Vyuma vingi vinaweza kushika kutu. Mtu asipochukua hatua mapema wakati anapogundua kwamba chuma kimeshika kutu, chuma hicho kinaweza kuliwa na kutu mpaka kisiwe na faida yoyote. Magari mengi sana yameharibika, si kwa sababu ya matatizo ya injini, bali kwa sababu vyuma vyake vimeliwa na kutu kabisa hivi kwamba ni hatari kutumia magari hayo. Tunaweza kutumiaje mfano huo kuhusiana na kunung’unika?

      13 Kama vile vyuma fulani hushika kutu, wanadamu wasio wakamilifu wana mwelekeo wa kulalamika. Tunapaswa kuwa chonjo kugundua dalili yoyote ya kutaka kulalamika. Kama vile unyevu na hewa yenye chumvi hufanya chuma kishike kutu haraka, taabu zinaweza kutufanya tutake sana kunung’unika. Mkazo unaweza kufanya tuudhike sana tunaposumbuliwa kidogo. Kadiri hali zinavyozidi kuwa mbaya katika siku hizi za mwisho za mfumo huu, mambo yanayoweza kufanya tulalamike huenda yataongezeka. (2 Timotheo 3:1-5) Hivyo, huenda mtumishi mmoja wa Yehova akaanza kunung’unika kuhusu mtumishi mwenzake. Huenda akanung’unika kwa sababu ndogo, kama vile udhaifu wa mwingine, uwezo wake, au mapendeleo yake ya utumishi.

      14, 15. Kwa nini tunapaswa kuchukua hatua dhidi ya mwelekeo wa kulalamika?

      14 Hata tuwe tumekasirishwa na jambo gani, tusipodhibiti mwelekeo wetu wa kutaka kulalamika, tunaweza kusitawisha mtazamo wa kutoridhika na vilevile tabia ya kunung’unika. Naam, kunung’unika kunaweza kutudhoofisha kabisa kiroho. Waisraeli waliponung’unika kuhusu maisha yao nyikani, walimlaumu hata Yehova. (Kutoka 16:8) Acheni tuepuke kufanya hivyo!

      15 Uwezekano wa chuma kuharibiwa na kutu unaweza kupunguzwa kwa kukipaka rangi ya kuzuia kutu na kurekebisha haraka sehemu zilizoliwa. Vivyo hivyo, tukigundua kwamba tuna mwelekeo wa kulalamika, tunaweza kuudhibiti kwa kusali na kuchukua hatua haraka kujirekebisha. Tunaweza kufanyaje hivyo?

      Ona Mambo Kama Yehova

      16. Tunaweza kushindaje mwelekeo wa kulalamika?

      16 Tunaponung’unika tunakazia fikira shida zetu, tunajifikiria wenyewe, na kusahau baraka tunazopata tukiwa Mashahidi wa Yehova. Ili kushinda mwelekeo wa kulalamika, tunahitaji kujikumbusha baraka hizo. Kwa mfano, kila mmoja wetu ana pendeleo zuri la kutambulishwa kwa jina la Yehova. (Isaya 43:10) Tunaweza kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja naye, nasi tunaweza kuzungumza na “Msikiaji wa sala” wakati wowote ule. (Zaburi 65:2; Yakobo 4:8) Maisha yetu yana kusudi kwa sababu tunaelewa suala la enzi kuu ya ulimwengu wote na tunakumbuka kwamba tuna pendeleo la kudumisha utimilifu wetu kwa Mungu. (Methali 27:11) Tunaweza kuhubiri habari njema ya Ufalme kwa ukawaida. (Mathayo 24:14) Imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo hutuwezesha kuwa na dhamiri safi. (Yohana 3:16) Hizo ni baraka tunazopata haidhuru tuna matatizo gani.

      17. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kuona mambo kama Yehova, hata ikiwa tuna sababu nzuri ya kulalamika?

      17 Acheni tujitahidi kuona mambo kama Yehova, bali si kulingana na maoni yetu. Mtunga-zaburi Daudi aliimba hivi: “Nijulishe njia zako, Ee Yehova; nifundishe mapito yako mwenyewe.” (Zaburi 25:4) Ikiwa tuna sababu nzuri ya kulalamika, Yehova anaiona. Anaweza kusuluhisha jambo hilo sasa hivi. Basi, kwa nini nyakati nyingine yeye huruhusu shida ziendelee? Huenda ni kwa sababu anataka kutusaidia tusitawishe sifa nzuri, kama vile subira, uvumilivu, imani, na ustahimilivu.—Yakobo 1:2-4.

      18, 19. Toa mfano kuonyesha faida zinazoweza kutokea tunapovumilia hali ngumu bila kulalamika.

      18 Kuvumilia hali ngumu bila kulalamika hutusaidia kuboresha utu wetu na vilevile kuwavutia wale wanaotazama mwenendo wetu. Katika mwaka wa 2003, kikundi fulani cha Mashahidi wa Yehova kilisafiri kwa basi kutoka Ujerumani ili kuhudhuria kusanyiko Hungaria. Dereva wa basi hilo hakuwa Shahidi, naye hakufurahia wazo la kwamba angekuwa na Mashahidi hao kwa siku kumi. Hata hivyo, baada ya safari, maoni yake yalibadilika kabisa. Kwa nini?

      19 Wakati wa safari hiyo, kulikuwa na matatizo fulani. Lakini Mashahidi hawakulalamika. Dereva huyo alisema kwamba hicho ndicho kikundi bora zaidi cha abiria ambacho amewahi kuhudumia! Hata aliahidi kwamba wakati ambapo Mashahidi watamtembelea nyumbani kwake, atawakaribisha na kuwasikiliza kwa makini. Naam, abiria hao walimvutia mtu huyo sana kwa “kufanya mambo yote bila kunung’unika”!

      Msamaha Huendeleza Umoja

      20. Kwa nini tunapaswa kusameheana?

      20 Namna gani ikiwa tuna sababu ya kulalamika kuhusu mwamini mwenzetu? Ikiwa ni jambo zito, tunapaswa kutumia kanuni zinazotajwa katika maneno ya Yesu kwenye Mathayo 18:15-17. Hata hivyo, nyakati nyingine si lazima tufanye hivyo kwa kuwa mara nyingi watu hutukosea katika mambo madogo. Kwa nini tusione hali hiyo kuwa nafasi ya kusamehe? Paulo aliandika hivi: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia. Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:13, 14) Je, tuko tayari kusamehe? Yehova ana sababu ya kulalamika juu yetu. Lakini, yeye huendelea kutuhurumia na kutusamehe.

      21. Wale wanaosikiliza manung’uniko wanaweza kuathiriwaje?

      21 Hata tuwe tumekosewa kwa njia gani, kunung’unika hakutatatua matatizo. Neno la Kiebrania linalomaanisha “kunung’unika” linaweza pia kumaanisha “kulalamika kwa hasira.” Yaelekea sisi huhisi vibaya tunapokuwa karibu na mtu mwenye tabia ya kunung’unika, nasi hujitahidi juu chini kumwepuka. Tukinung’unika, au kulalamika kwa hasira, wale wanaosikiliza wanaweza kuhisi vibaya pia. Wanaweza kuhisi vibaya sana na hata kutuepuka! Mtu anaweza kutusikiliza tunaponung’unika, lakini hatavutiwa nasi.

      22. Msichana mmoja alisema nini kuhusu Mashahidi wa Yehova?

      22 Kusamehe huendeleza umoja, na watu wa Yehova wanathamini sana umoja. (Zaburi 133:1-3) Katika nchi moja ya Ulaya, msichana mmoja Mkatoliki mwenye umri wa miaka 17 aliiandikia ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ili kueleza jinsi anavyovutiwa nao. Alisema hivi: “Hilo ndilo tengenezo moja tu ninalojua ambalo washiriki wake hawagawanywi na chuki, pupa, ubaguzi, ubinafsi, wala utengano.”

      23. Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

      23 Kuthamini baraka zote za kiroho tunazopata tukiwa waabudu wa Mungu wa kweli, Yehova, kutatusaidia kuendeleza umoja na kuepuka kunung’unika dhidi ya wengine katika mambo ya kibinafsi. Makala inayofuata itaonyesha jinsi sifa za kiroho zinavyoweza kutuzuia tusihusike katika aina fulani hatari ya kunung’unika, yaani, kunung’unika kuhusu sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova.

  • Kazia Fikira Mema ya Tengenezo la Yehova
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Julai 15
    • Kazia Fikira Mema ya Tengenezo la Yehova

      “Hakika tutashiba mema ya nyumba yako.”—ZABURI 65:4.

      1, 2. (a) Mipango iliyohusiana na hekalu ingewafaidi watu wa Mungu jinsi gani? (b) Daudi aliungaje mkono ujenzi wa hekalu?

      DAUDI wa Israeli la kale ni mmoja wa watu wa pekee sana ambao wanazungumziwa katika Maandiko ya Kiebrania. Mchungaji huyo, ambaye pia alikuwa mwanamuziki, nabii, na mfalme alimtegemea kabisa Yehova Mungu. Uhusiano wake wa karibu sana pamoja na Yehova ulimchochea kutamani kumjengea Mungu nyumba. Nyumba hiyo, au hekalu, ingekuwa kituo cha ibada ya kweli huko Israeli. Daudi alijua kwamba mipango iliyohusiana na hekalu ingewaletea watu wa Mungu shangwe na baraka. Hivyo, Daudi aliimba hivi: “Mwenye furaha ni yule unayemchagua [Yehova] na kumfanya akaribie, ili apate kukaa katika nyua zako. Hakika tutashiba mema ya nyumba yako, mahali patakatifu pa hekalu lako.”—Zaburi 65:4.

      2 Daudi hakuruhusiwa asimamie ujenzi wa nyumba ya Yehova. Badala yake, Sulemani mwana wake ndiye aliyepewa pendeleo hilo. Daudi hakunung’unika eti kwa sababu mtu mwingine amepewa pendeleo ambalo yeye mwenyewe alilitamani sana. Jambo la maana kwake lilikuwa ujenzi wa hekalu. Aliunga mkono mradi huo kwa moyo wote kwa kumpa Sulemani ramani za ujenzi ambazo alikuwa amepokea kutoka kwa Yehova. Zaidi ya hayo, Daudi alipanga maelfu ya Walawi katika migawanyo ya utumishi, naye akachanga kiasi kikubwa cha dhahabu na fedha kwa ajili ya ujenzi wa hekalu.—1 Mambo ya Nyakati 17:1, 4, 11, 12; 23:3-6; 28:11, 12; 29:1-5.

      3. Watumishi wa Mungu wana mtazamo gani kuelekea mipango ya ibada ya kweli?

      3 Waisraeli waaminifu waliunga mkono mipango iliyofanywa kwa ajili ya ibada ya kweli kwenye nyumba ya Mungu. Tukiwa watumishi wa Yehova leo, sisi pia huunga mkono mipango ya ibada katika sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova. Hivyo, tunaonyesha kwamba tuna mtazamo kama wa Daudi. Hatulalamiki. Badala yake, tunakazia fikira mema ya tengenezo la Mungu. Je, umewahi kufikiria mambo mengi mema ambayo tunaweza kuyathamini? Hebu tuzungumzie baadhi ya mambo hayo.

      Kuwathamini Wale Wanaoongoza

      4, 5. (a) “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” hutimizaje utume wake? (b) Mashahidi wengine wamehisije kuhusu chakula cha kiroho wanachopokea?

      4 Tuna sababu nzuri za kumthamini “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” aliyewekwa rasmi na Yesu Kristo kusimamia mali zake duniani. Jamii ya mtumwa inayofanyizwa na Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho huongoza kazi ya kuhubiri habari njema, hupanga mikutano ya ibada, na kuchapisha vitabu vinavyozungumzia Biblia katika lugha zaidi ya 400. Mamilioni ya watu ulimwenguni pote huthamini na kutumia ‘chakula hicho cha kiroho kwa wakati unaofaa.’ (Mathayo 24:45-47) Naam, hakuna sababu ya kunung’unika kuhusu chakula hicho.

      5 Kwa miaka mingi, Elfi, Shahidi mmoja wa Yehova ambaye ni mzee kwa umri, amefarijiwa na kupata msaada kwa kutumia mashauri ya Kimaandiko yaliyo katika vichapo vya jamii ya mtumwa. Elfi alishukuru sana na kuandika hivi: “Siwezi kufanikiwa bila tengenezo la Yehova.” Peter na Irmgard pia wamekuwa watumishi wa Mungu kwa miaka mingi. Irmgard anathamini habari zote zinazochapishwa na “tengenezo la Yehova lenye upendo na linalojali.” Habari hizo zinatia ndani zile zinazotayarishwa kwa ajili ya watu wenye mahitaji ya pekee, kama wale wasioweza kuona au kusikia vizuri.

      6, 7. (a) Utendaji wa makutaniko ulimwenguni pote unasimamiwaje? (b) Wengine wamesema nini kuhusu sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova?

      6 “Mtumwa mwaminifu” huwakilishwa na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, ambalo ni kikundi kidogo cha wanaume waliotiwa mafuta kwa roho wanaotumikia kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York. Baraza Linaloongoza huwaweka rasmi watumishi wa Yehova wenye uzoefu watumikie kwenye ofisi za tawi ambazo zinasimamia utendaji wa makutaniko zaidi ya 98,000 ulimwenguni pote. Wanaume wanaofikia matakwa ya Biblia huwekwa rasmi kuwa wazee na watumishi wa huduma katika makutaniko hayo. (1 Timotheo 3:1-9, 12, 13) Wazee huliongoza na kulichunga kwa upendo kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wao. Kuna faida kubwa kama nini kuwa sehemu ya kundi hilo na kufurahia upendo na umoja unaopatikana miongoni mwa “ushirika mzima wa akina ndugu”!—1 Petro 2:17; 5:2, 3.

      7 Badala ya kunung’unika, mara nyingi akina ndugu na dada hueleza jinsi wanavyothamini mwongozo wa kiroho wenye upendo kutoka kwa wazee. Mfano mmoja ni wa Birgit, ambaye ni mke Mkristo mwenye miaka zaidi ya 30. Kabla ya kufikia umri wa miaka 20, alikuwa na mashirika mabaya na alikuwa karibu kutumbukia katika dhambi. Lakini mashauri ya Biblia yaliyo wazi kutoka kwa wazee na msaada wa waamini wenzake ulimsaidia kuepuka hatari. Birgit anahisije sasa? Anasema hivi: “Ninashukuru sana kwamba bado niko katika tengenezo la Yehova ambalo linapendeza sana.” Mvulana mmoja mwenye umri wa miaka 17 anayeitwa Andreas anasema hivi: “Kwa kweli hili ni tengenezo la Yehova, tengenezo bora zaidi ulimwenguni.” Je, hatupaswi kuthamini mambo mema katika sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova?

      Wale Wanaoongoza Si Wakamilifu

      8, 9. Baadhi ya watu walioishi wakati mmoja na Daudi walitendaje, na Daudi alitendaje?

      8 Bila shaka, wale waliowekwa rasmi kuongoza ibada ya kweli si wakamilifu. Wote hukosea, na wengine wana udhaifu ambao wanajitahidi sana kurekebisha. Je, jambo hilo linapaswa kutuhuzunisha? Hapana. Hata watu waliopewa madaraka mengi katika Israeli la kale walifanya makosa mazito. Kwa mfano, Daudi alipokuwa kijana, aliombwa aende kumpigia muziki Mfalme Sauli ili kumtuliza. Baadaye, Sauli alijaribu kumuua Daudi, na ilimbidi Daudi akimbie ili kuokoa uhai wake.—1 Samweli 16:14-23; 18:10-12; 19:18; 20:32, 33; 22:1-5.

      9 Waisraeli wengine walitenda kwa hila. Kwa mfano, Yoabu, mkuu wa jeshi la Daudi, alimuua Abneri ambaye alikuwa mtu wa ukoo wa Sauli. Absalomu alipanga njama dhidi ya baba yake, Daudi, ili anyakue ufalme. Na Daudi alisalitiwa na Ahithofeli, mshauri wake mwenye kutegemeka. (2 Samweli 3:22-30; 15:1-17, 31; 16:15, 21) Lakini Daudi hakulalamika kwa uchungu; wala hakuacha ibada ya kweli. Badala yake, Daudi alitenda kwa njia tofauti kabisa. Taabu zilimchochea Daudi kushikamana na Yehova na kudumisha mtazamo wake mzuri ambao alikuwa ameonyesha wakati alipokimbia kwa sababu ya Sauli. Wakati huo, Daudi aliimba hivi: “Unionyeshe kibali, Ee Mungu, unionyeshe kibali, kwa maana nafsi yangu imekukimbilia wewe; na katika kivuli cha mabawa yako nimekimbilia mpaka shida zipitilie mbali.”—Zaburi 57:1.

      10, 11. Mkristo mmoja anayeitwa Gertrud alikabili hali gani alipokuwa kijana, naye alisema nini kuhusu kutokamilika kwa waamini wenzake?

      10 Hatuna sababu ya kulalamika kwamba kuna hila katika tengenezo la Mungu leo. Yehova wala malaika wake wala wachungaji wa kiroho hawawezi kukubali watu waovu wenye hila waendelee kuwepo katika kutaniko la Kikristo. Hata hivyo, sisi sote hukabili hali ya kutokamilika kwa wanadamu, iwe ni kutokamilika kwetu au kutokamilika kwa watumishi wengine wa Mungu.

      11 Alipokuwa kijana, mwabudu mmoja wa Yehova wa muda mrefu anayeitwa Gertrud alishutumiwa kwa uwongo kwamba yeye si mhubiri wa wakati wote wa Ufalme bali yeye ni mdanganyifu. Alitendaje? Je, Gertrud alinung’unika kwa kutendewa hivyo? Hapana. Muda mfupi kabla ya kifo chake katika mwaka wa 2003 akiwa na umri wa miaka 91, alikumbuka yaliyopita na kusema hivi: “Mambo hayo na mengine yamenifundisha kwamba licha ya makosa ya watu, Yehova huongoza kazi yake muhimu, ambayo ametupa sisi wanadamu wasio wakamilifu.” Gertrud alipokabili kutokamilika kwa watumishi wenzake wa Mungu, alisali kwa Yehova kutoka moyoni.

      12. (a) Wakristo fulani wa karne ya kwanza waliweka mfano gani mbaya? (b) Tunapaswa kukazia fikira nini?

      12 Kwa kuwa hata Wakristo washikamanifu na wenye bidii zaidi si wakamilifu, wakati mtumishi aliyewekwa rasmi anapokosea, acheni tuendelee “kufanya mambo yote bila kunung’unika.” (Wafilipi 2:14) Litakuwa jambo lenye kuhuzunisha kama nini ikiwa tutafuata mfano mbaya wa watu fulani katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza! Kulingana na mwanafunzi Yuda, walimu wa uwongo wa wakati huo walikuwa ‘wakipuuza mamlaka na kuwatukana watukufu.’ Isitoshe, watenda-dhambi hao walikuwa “wanung’unikaji, walalamikaji juu ya fungu lao maishani.” (Yuda 8, 16) Tusiwaige kamwe walalamikaji hao wenye kunung’unika. Badala yake acheni tukazie fikira mambo mazuri ambayo tunapata kutoka kwa “mtumwa mwaminifu.” Acheni tuthamini mema ya tengenezo la Yehova na ‘kuendelea kufanya mambo yote bila kunung’unika.’

      “Maneno Hayo Yanashtua”

      13. Wengine walitendaje waliposikia mafundisho fulani ya Yesu Kristo?

      13 Ingawa wengine katika karne ya kwanza walinung’unika dhidi ya watumishi waliowekwa rasmi, wengine walinung’unika kwa sababu ya mafundisho ya Yesu. Kama ilivyoandikwa katika Yohana 6:48-69, Yesu alisema hivi: “Yule ambaye hula mwili wangu na kunywa damu yangu ana uzima wa milele.” Waliposikia maneno hayo, “wengi kati ya wanafunzi wake . . . wakasema: ‘Maneno hayo yanashtua; ni nani ambaye anaweza kuyasikiliza?’” Yesu alijua kwamba ‘wanafunzi wake walikuwa wakinung’unika juu ya hilo.’ Isitoshe, ‘kwa sababu ya hilo wengi kati yao wakaenda zao kwenye mambo yaliyo nyuma wakawa hawatembei tena pamoja naye.’ Lakini si wanafunzi wote walionung’unika. Ona kilichotukia wakati Yesu alipowauliza wale mitume 12 hivi: “Je, ninyi pia mnataka kwenda?” Mtume Petro alimjibu: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele; na sisi tumeamini na tumejua kwamba wewe ndiye Mtakatifu wa Mungu.”

      14, 15. (a) Kwa nini watu wachache huchukizwa na mafundisho fulani ya Kikristo? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na kisa cha Emanuel?

      14 Katika nyakati zetu, watu wachache sana miongoni mwa watu wa Mungu wamechukizwa na mafundisho fulani ya Kikristo na kunung’unika dhidi ya sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova. Kwa nini hilo hutukia? Mara nyingi kunung’unika huko husababishwa kwa kutoelewa njia ya Mungu ya kufanya mambo. Muumba huwafunulia watu wake ukweli hatua kwa hatua. Hivyo, uelewaji wetu wa Maandiko unahitaji kuboreshwa mara kwa mara. Wengi kati ya watu wa Yehova hufurahia marekebisho hayo. Wachache ‘huwa waadilifu kupita kiasi’ na kuchukizwa na mabadiliko hayo. (Mhubiri 7:16) Huenda wakafanya hivyo kwa sababu ya kiburi, na wengine huangukia mtego wa kutegemea akili zao. Hata sababu iwe nini, kunung’unika kwa aina hiyo ni hatari, kwa sababu kunaweza kuturudisha katika ulimwengu na njia zake.

      15 Kwa mfano, Shahidi mmoja anayeitwa Emanuel alichambua mambo fulani aliyosoma katika vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45) Aliacha kusoma vichapo vyetu vya Kikristo na mwishowe akawaambia wazee wa kutaniko lao kwamba ameacha kuwa Shahidi wa Yehova. Lakini baada ya muda mfupi, Emanuel alitambua kwamba mafundisho ya tengenezo la Yehova ni ya kweli. Aliwafikia Mashahidi, akakubali kosa lake, naye akarudishwa kuwa Shahidi wa Yehova. Hivyo, Emanuel akapata furaha tena.

      16. Ni mambo gani yanayoweza kutusaidia kuondoa mashaka kuhusu mafundisho fulani ya Kikristo?

      16 Namna gani tukihisi kwamba tunataka kunung’unika kwa sababu tuna mashaka kuhusu mafundisho fulani ambayo watu wa Yehova wanaamini? Acheni tuwe na subira. Mwishowe huenda “mtumwa mwaminifu” akachapisha habari fulani ambazo zitajibu maswali yetu na kuondoa mashaka yetu. Ni jambo la hekima kuomba msaada wa wazee Wakristo. (Yuda 22, 23) Sala, funzo la kibinafsi, na kushirikiana pamoja na waamini wenzetu wanaohangaikia mambo ya kiroho kunaweza kutusaidia pia kuondoa mashaka na kuthamini zaidi kweli za Biblia zenye kuimarisha imani ambazo tumejifunza kupitia njia ya Yehova ya mawasiliano.

      Dumisha Mtazamo Unaofaa

      17, 18. Badala ya kunung’unika, tunapaswa kuwa na mtazamo gani, na kwa nini?

      17 Ni kweli kwamba wanadamu wasio wakamilifu wamerithi dhambi, na huenda wengine wakawa na mwelekeo wenye nguvu wa kunung’unika bila sababu. (Mwanzo 8:21; Waroma 5:12) Lakini tukiwa na tabia ya kunung’unika, tunaweza kuhatarisha uhusiano wetu pamoja na Yehova Mungu. Hivyo, tunahitaji kudhibiti mwelekeo wa kunung’unika.

      18 Badala ya kunung’unika kuhusu mambo katika kutaniko, inafaa tudumishe mtazamo unaofaa na kufuata ratiba inayotuwezesha kuwa na shughuli nyingi, shangwe, hofu ya Mungu, usawaziko, na imani yenye nguvu. (1 Wakorintho 15:58; Tito 2:1-5) Yehova anaongoza mambo yote katika tengenezo lake, na Yesu anajua mambo yanayotendeka katika kila kutaniko, kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza. (Ufunuo 1:10, 11) Kwa subira, mngojee Mungu na Kristo, Kichwa cha kutaniko. Wachungaji wenye kutegemeka wanaweza kutumiwa kurekebisha mambo yanayohitaji kunyooshwa.—Zaburi 43:5; Wakolosai 1:18; Tito 1:5.

      19. Hadi wakati ambapo Ufalme utaongoza shughuli zote za wanadamu, tunapaswa kukazia fikira nini?

      19 Hivi karibuni, mfumo huu mbovu wa mambo utakomeshwa, na Ufalme wa Kimasihi utaongoza shughuli zote za wanadamu. Kabla ya wakati huo, ni muhimu sana kila mmoja wetu adumishe mtazamo unaofaa! Hilo litatusaidia kutambua sifa nzuri za waamini wenzetu, badala ya kukazia fikira udhaifu wao. Tutapata furaha tunapofikiria sifa zao nzuri. Badala ya kuumia kihisia kwa sababu ya kunung’unika, tutatiwa moyo na kujengwa kiroho.

      20. Tutapata baraka gani tukiwa na mtazamo unaofaa?

      20 Mtazamo unaofaa utatusaidia pia kukumbuka baraka nyingi tunazopata kwa kushirikiana na sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova. Ulimwenguni pote, hilo tu ndilo tengenezo linaloonyesha ushikamanifu kwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Unahisije kuhusu jambo hilo la kweli na kuhusu pendeleo la kumwabudu Mungu wa pekee wa kweli, Yehova? Acha mtazamo wako uwe kama wa Daudi, aliyeimba hivi: “Ee msikiaji wa sala, kwako wewe watu wote wenye mwili watakuja. Mwenye furaha ni yule unayemchagua na kumfanya akaribie, ili apate kukaa katika nyua zako. Hakika tutashiba mema ya nyumba yako.”—Zaburi 65:2, 4.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki