-
Jihadhari na Desturi Zisizompendeza MunguMnara wa Mlinzi—2005 | Januari 1
-
-
Katika sehemu nyingine ya Afrika, mtoto anazaliwa. Hakuna mtu anayeruhusiwa kumwona mtoto huyo. Kwa kawaida, mtoto huwekwa ndani ya nyumba nao watu wasio washiriki wa familia hawaruhusiwi kumwona mpaka baada ya sherehe ya kumpa jina.
-
-
Jihadhari na Desturi Zisizompendeza MunguMnara wa Mlinzi—2005 | Januari 1
-
-
Sherehe za Kuzaliwa na Kumpa Mtoto Jina
Desturi nyingi zinazohusiana na kuzaliwa kwa mtoto zinafaa. Hata hivyo, katika maeneo ambako kuzaliwa kwa mtoto huonwa kuwa hatua ya kutoka katika makao ya roho ya wazazi waliokufa hadi kwenye ulimwengu wa wanadamu, Wakristo wa kweli wanapaswa kuwa waangalifu. Kwa mfano, katika sehemu fulani za Afrika, mtoto aliyezaliwa huwekwa ndani ya nyumba naye hapewi jina mpaka kipindi fulani cha wakati kipite. Ingawa kipindi hicho cha kungojea huenda kikatofautiana kulingana na mahali, mwishoni mwa kipindi hicho kunakuwa na sherehe ya kumpa mtoto jina, na wakati huo mtoto hutolewa nje na kuonyeshwa rasmi kwa watu wa ukoo na marafiki. Wakati huo, jina la mtoto hutangazwa rasmi.
Kikieleza maana ya desturi hiyo, kitabu Ghana—Understanding the People and Their Culture kinasema: “Wakati wa siku saba za kwanza za maisha yake, mtoto huonwa kuwa katika ‘safari’ ya kutoka ulimwengu wa roho na kuelekea kwenye maisha duniani. . . . Kwa kawaida, mtoto huwekwa ndani ya nyumba nao watu wasio washiriki wa familia hawaruhusiwi kumwona.”
Kwa nini kuna kipindi cha kungoja kabla ya sherehe ya kumpa mtoto jina? Kitabu Ghana in Retrospect kinaeleza: “Kabla ya siku ya nane, mtoto haonwi kuwa binadamu. Anahusianishwa kwa kadiri fulani na ulimwengu wa roho ambako ametoka.” Kitabu hicho kinaendelea kusema: “Kwa kuwa jina ndilo humfanya mtoto awe binadamu, wakati mume na mke wanapohofu kwamba mtoto wao atakufa, kwa kawaida hawatampa jina mpaka wawe na hakika kwamba ataishi. . . . Kwa hiyo, sherehe hiyo ya kutoka hali moja ya maisha hadi nyingine, ambayo nyakati nyingine huitwa kumtoa mtoto nje, huonwa kuwa yenye matokeo makubwa kwa mtoto na wazazi wake. Hiyo ndiyo sherehe ambayo humwingiza mtoto katika ushirika au ulimwengu wa wanadamu.”
Kwa kawaida, mzee wa ukoo ndiye husimamia sherehe hiyo ya kumpa mtoto jina. Mambo yanayofanyika wakati wa sherehe hiyo hutofautiana kulingana na mahali, lakini mara nyingi hutia ndani kumwagwa kwa toleo la kinywaji, kusali kwa roho za wazazi waliokufa ili kuwashukuru kwamba mtoto amefika salama, na mila na desturi nyingine.
Kutangazwa kwa jina la mtoto ndilo tukio muhimu la sherehe hiyo. Ingawa wazazi ndio wenye daraka la kumpa mtoto wao jina, mara nyingi watu wengine wa ukoo huwa na uvutano mkubwa kuhusu jina atakalopewa mtoto. Huenda majina mengine yakawa na maana yenye fumbo katika lugha ya kienyeji, kama vile “alienda na akarudi,” “Mama amerudi mara ya pili,” au “Baba amerudi tena.” Majina mengine yana maana ambayo imekusudiwa kuwazuia wazazi waliokufa wasimrudishe tena mtoto aliyezaliwa katika ulimwengu wa wafu.
Bila shaka, hakuna ubaya wowote katika kufurahia kuzaliwa kwa mtoto. Kumpa mtoto jina la mtu mwingine na kumpa jina ambalo linahusiana na hali za kuzaliwa kwake ni desturi zinazokubalika, na kuamua wakati wa kumpa mtoto jina ni uamuzi wa kibinafsi. Hata hivyo, Wakristo wanaotaka kumpendeza Mungu huwa waangalifu kuepuka desturi au sherehe yoyote ambayo itafanya watu wafikiri kwamba wanakubaliana na maoni ya kwamba mtoto aliyezaliwa ni “mgeni” anayepita kutoka ulimwengu wa roho wa wazazi waliokufa hadi ulimwengu wa walio hai.
Isitoshe, ingawa wengi katika jamii huona sherehe ya kumpa mtoto jina kuwa desturi muhimu ya kutoka hali moja ya maisha hadi ile nyingine, Wakristo wanapaswa kufikiria dhamiri za watu wengine na jinsi watu wasioamini watakavyoliona jambo hilo. Kwa mfano, wengine wangefikia mkataa gani ikiwa familia ya Kikristo ingemficha mtoto wao asionekane na watu hadi sherehe ya kumpa jina ifanywe? Watu wangekuwa na maoni gani ikiwa mtoto angepewa majina yanayopingana na madai yao ya kuwa walimu wa ile kweli ya Biblia?
Hivyo, wanapoamua jinsi na wakati wa kuwapa watoto wao majina, Wakristo wanajitahidi ‘kufanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu’ ili wasiwakwaze wengine. (1 Wakorintho 10:31-33) Wao ‘hawaweki kando amri ya Mungu kusudi wabaki na mapokeo’ ambayo yamekusudiwa hasa kuwaheshimu wafu. Badala yake, wanamheshimu na kumtukuza Yehova, Mungu aliye hai.—Marko 7:9, 13.
-