Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Vitu vya Kuchukiwa na Mataifa Yote”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Kutendwa Kikatili Katika Kambi za Mateso

      Adolf Hitler alikuwa rafiki mkubwa wa makasisi. Wakati wa 1933, mwaka uleule ambao mwafaka kati ya Vatikani na Nazi ya Ujerumani ulitiwa sahihi, Hitler alianzisha kampeni ya kuwaangamiza Mashahidi wa Yehova katika Ujerumani. Kufikia 1935 waliharimishwa katika taifa lote. Lakini ni nani aliyeanzisha hayo?

      Padri mmoja Mkatoliki, akiandika katika Der Deutsche Weg (gazeti la Kijerumani lililochapwa katika Lodz, Poland), alisema katika toleo lalo la Mei 29, 1938 hivi: “Sasa kuna nchi moja duniani ambako wale waitwao eti . . . Wanafunzi wa Biblia [Mashahidi wa Yehova] wameharimishwa. Hiyo ni Ujerumani! . . . Wakati Adolf Hitler alipochukua mamlaka, na Episkopati (Baraza la Maaskofu) ya Wakatoliki wa Ujerumani ikarudia ombi lao, Hitler alisema: ‘Hawa waitwao eti Wanafunzi wa Biblia Wenye Bidii [Mashahidi wa Yehova] ni wazusha-fujo; . . . Mimi ninawaona kuwa watu bandia; Mimi sivumilii kwamba Wakatoliki Wajerumani watashushiwa heshima kwa njia hiyo na huyu Mwamerika Jaji Rutherford; Ninaharimisha [Mashahidi wa Yehova] katika Ujerumani.’”—Italiki ni zetu.

      Je, ilikuwa tu ni Baraza la Maaskofu Wakatoliki wa Ujerumani waliotaka hatua hizo zichukuliwe? Kama ilivyoripotiwa katika Oschatzer Gemeinnützige, la Aprili 21, 1933, katika hotuba ya redio Aprili 20, mhudumu Mluther Otto alihutubu kuhusu “ushirikiano wa karibu zaidi” kwa upande wa Kanisa la Luther la Ujerumani la Jimbo la Saxony pamoja na viongozi wa kisiasa wa taifa, na kisha yeye akajulisha hivi: “Matokeo ya kwanza ya ushirikiano huo tayari yaweza kuonwa katika kupigwa marufuku leo kwa International Association of Earnest Bible Students [Mashahidi wa Yehova] na madhehebu yalo katika Saxony.”

      Baadaye, Serikali ya Nazi ilianzisha mojawapo minyanyaso ya Wakristo iliyo ya unyama zaidi katika historia iliyorekodiwa. Maelfu ya Mashahidi wa Yehova—kutoka Ujerumani, Austria, Poland, Chekoslovakia, Uholanzi, Ufaransa, na nchi nyinginezo—walitupwa ndani ya kambi za mateso. Humo waliteswa kwa ukatili na unyama mwingi uwezao kuwaziwa. Ilikuwa kawaida kwao kutukanwa na kupigwa mateke, kisha kulazimishwa kuupinda mwili kuanzia kwenye magoti, kuruka, na kutambaa kwa saa nyingi, hadi walipozirai au kuanguka kwa sababu ya uchovu, huku askari-walinzi wakiangua kicheko. Wengine walilazimishwa kusimama wakiwa uchi au wakiwa wamevaa nguo chache sana katika ua wakati wa kipupwe. Wengi walichapwa viboko hadi wakazimia na migongo yao ikajaa damu. Wengine walitumiwa kama violezo katika majaribio ya kitiba. Wengine waliangikwa juu kwa viwiko vyao, huku mikono yao ikiwa imefungwa nyuma yao. Ingawa walikuwa hoi kwa sababu ya njaa na walikuwa na nguo haba katika hali ya hewa yenye baridi sana, walilazimishwa kufanya kazi nzito, wakifanya kazi kwa saa nyingi, mara nyingi wakitumia mikono yao wenyewe wakati koleo na vifaa vingine vilipohitajiwa. Wanaume na wanawake pia walitendwa vivyo hivyo. Umri wao ulianzia utineja hadi miaka ya sabini. Watesi wao walipiga kelele za kumkaidi Yehova.

      Katika jitihada za kuvunja roho ya Mashahidi, kamanda wa kambi katika Sachsenhausen aliagiza August Dickmann, Shahidi mchanga, auawe mbele ya wafungwa wote, Mashahidi wa Yehova wakiwa mbele kabisa ambapo wangeathirika zaidi na matokeo ya jambo hilo. Baada ya hilo, wafungwa wale wengine waliambiwa waondoke, lakini Mashahidi wa Yehova walipaswa wabaki. Kwa mkazo mwingi kamanda aliwauliza, ‘Ni nani sasa aliye tayari kutia sahihi taarifa?’—taarifa ya kukana imani ya mtu na kuonyesha utayari wa kuwa mwanajeshi. Hakuna mmoja wa wale Mashahidi 400 au zaidi aliyeitikia. Kisha wawili wakajitokeza mbele! La, si ili kutia sahihi, lakini ili kuomba kwamba sahihi zao zilizotolewa karibu mwaka mmoja hivi uliokuwa umepita ziweze kufutwa.

      Katika kambi ya Buchenwald, mkazo uo huo ulitumiwa. Ofisa wa Nazi Rödl aliwaambia Mashahidi: “Yeyote kati yenu akikataa kupigana dhidi ya Ufaransa au Uingereza, nyote lazima mtakufa!” Vikosi viwili vyenye silaha vya polisi wa SS vilikuwa vikingoja kwenye lango la kambi. Hakuna Shahidi hata mmoja aliyekubali. Kutendwa kikatili kukafuata, lakini tisho la yule ofisa halikutekelezwa. Ikaja kujulikana waziwazi kwamba, ingawa Mashahidi katika kambi wangefanya karibu kila aina ya kazi waliyopewa, hata ingawa waliadhibiwa kwa kunyimwa chakula na kazi nyingi, bado wangekataa kwa dhati kufanya lolote lenye kuunga mkono vita au lolote lililoelekezwa dhidi ya mfungwa mwingine.

      Ni vigumu sana kueleza mambo mabaya waliyopatwa nayo. Mamia yao walikufa. Baada ya waokokaji kuachiliwa kutoka kwenye kambi mwishoni mwa vita, Shahidi mmoja kutoka Flanders aliandika: “Ni tamaa isiyoyumbayumba ya kutaka kuishi, tumaini na itibari katika Yeye, Yehova, ambaye ni mwenye nguvu zote, na kupenda Ile Theokrasi, kulikofanya iwezekane kuvumilia yote hayo na kupata ushindi.—Warumi 8:37.”

      Wazazi walitenganishwa bila huruma na watoto wao. Wenzi waliooana walitenganishwa, na wengine hawakupata kuonana tena. Muda mfupi baada ya kuoa, Martin Poetzinger alikamatwa na kupelekwa kwenye kambi yenye sifa mbaya ya Dachau, kisha katika Mauthausen. Mke wake, Gertrud, alifungwa katika Ravensbrück. Hawakuonana kwa miaka tisa. Akikumbuka mambo aliyoona katika Mauthausen, aliandika hivi baadaye: “Gestapo walijaribu kila njia ili kutushawishi tuvunje imani yetu katika Yehova. Kunyimwa chakula, urafiki wa hila, ukatili, kusimama siku baada ya siku katika fremu, kuangikwa juu ya nguzo ya meta 3 kwa viwiko vilivyozungushwa nyuma, kuchapwa viboko—yote hayo na mengine ya aibu sana kuweza kutajwa yaliweza kujaribiwa.” Lakini alibaki akiwa mwaminifu-mshikamanifu kwa Yehova. Yeye pia alikuwa miongoni mwa waokokaji, na baadaye alitumikia akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova.

      Wafungwa kwa Sababu ya Imani Yao

      Mashahidi wa Yehova hawakuwa katika kambi za mateso kwa sababu walikuwa wahalifu. Maofisa walipotaka mtu wa kuwanyoa, walimwamini Shahidi akiwa na kijembe, kwa sababu walijua kwamba hakuna Shahidi ambaye angetumia kifaa hicho kuwa silaha ili kumdhuru mwanadamu mwingine. Maofisa wa SS kwenye kambi ya maangamizo ya Auschwitz walipohitaji mtu wa kuwasafishia nyumba zao au kutunza watoto wao, walichagua Mashahidi, kwa sababu walijua hao hawangejaribu kuwapatia sumu au kujaribu kutoroka. Wakati kambi ya Sachsenhausen ilipokuwa ikihamwa mwishoni mwa ile vita, walinzi waliweka miongoni mwa kikundi cha Mashahidi kigari ambacho ndani yacho walikuwa na nyara waliyoteka. Kwa nini? Kwa sababu walijua kwamba Mashahidi hawangeiba mali yao.

      Mashahidi wa Yehova walifungwa kwa sababu ya imani yao. Mara kwa mara waliahidiwa kwamba wangefunguliwa kutoka kambi ikiwa tu wangetia sahihi taarifa ya kukana imani zao. Polisi wa SS walifanya kila jambo waliloweza ili kuwashawishi au kuwalazimisha Mashahidi kutia sahihi taarifa kama hiyo. Hasa hilo ndilo walilotaka.

      Mashahidi wote isipokuwa wachache, walithibitika kuwa wenye uaminifu-maadili usiovunjika. Lakini wao walifanya mengi zaidi ya kuteseka kwa sababu ya uaminifu-mshikamanifu wao kwa Yehova na ujitoaji wao kwa jina la Kristo. Walifanya zaidi ya kuvumilia mateso ya kupata habari kwao ambayo walikumbwa nayo. Walidumisha mahusiano yenye nguvu ya umoja wa kiroho.

      Roho yao haikuwa ile ya wokovu wa kibinafsi kwa vyovyote vile. Walionyeshana upendo wa kujidhabihu. Wakati mmoja wao alipokuwa hoi, wengine wangeshiriki naye chakula chao kidogo. Waliponyimwa utibabu wote, walitunzana kwa upendo.

      Habari ya funzo la Biblia iliwafikia Mashahidi kujapokuwa na jitihada zote za wanyanyasi wao kuizuia—zikiwa zimefichwa katika vifurushi vya zawadi kutoka nje, kwa maelezo ya wafungwa wapya, hata kwa kufichwa katika mguu wa mbao wa mfungwa mpya, au kwa njia nyinginezo walipokuwa katika migawo ya kazi nje ya kambi. Nakala zilipitishwa kutoka kwa mmoja hadi mwingine; nyakati nyingine zilirudufishwa kisiri kwenye mashine mlemle ndani ya ofisi za maofisa wa kambi. Hata mikutano mingine ya Kikristo ilifanywa ndani ya kambi, ingawa hatari kubwa ilihusika.

      Mashahidi waliendelea tu kuhubiri kwamba Ufalme wa Mungu ndio tumaini pekee la wanadamu—na walifanya hivyo katika kambi za mateso! Katika Buchenwald, kwa sababu ya utendaji uliopangwa, maelfu ya wafungwa walisikia habari njema. Katika kambi ya Neuengamme, karibu Hamburg, kampeni ya kutoa ushahidi kwa kadiri kubwa ilipangwa kwa uangalifu na kufanywa mapema katika 1943. Kadi za kutoa ushuhuda zilitayarishwa katika lugha kadhaa zilizosemwa kambini. Jitihada zilifanywa ili kufikia kila mfungwa wa vita. Mipango ilifanywa kwa ajili ya funzo la Biblia la kibinafsi la kawaida pamoja na waliopendezwa. Mashahidi walikuwa na bidii sana katika kuhubiri kwao hivi kwamba baadhi ya wafungwa wa kisiasa walilalamika hivi: “Mahali popote uendapo, yote unayosikia ni habari kuhusu Yehova!” Wakati maagizo yalipokuja kutoka Berlin ya kuwatawanya Mashahidi miongoni mwa wafungwa wengine ili kuwadhoofisha, jambo hilo hasa lilifanya iwezekane kwao kutoa ushahidi kwa watu zaidi.

      Kuhusu Mashahidi wa kike waaminifu 500 au zaidi katika Ravensbrück, mpwa wa kike wa Jenerali wa Ufaransa Charles de Gaulle aliandika hivi kufuatia kuachiliwa kwake: “Mimi ninawastaajabia kikweli. Walikuwa watu wa kutoka mataifa tofauti: Wajerumani, Wapoland, Warusi na Wacheki, na wamevumilia mateso makubwa sana kwa sababu ya imani zao. . . . Wote walionyesha ujasiri mkubwa sana na mtazamo wao ulifanya hatimaye hata S.S wawaheshimu. Wangaliweza kuachiliwa huru mara hiyo ikiwa wangalikana imani yao. Lakini, kinyume cha hayo, hawakuacha ukinzani wao, hata wakafaulu kuleta vitabu na trakti kambini.”

      Kama Yesu Kristo, walijithibitisha wenyewe kuwa washindi wa ulimwengu uliotaka kuwafanya washikamane na mfinyango wao wa kishetani. (Yn. 16:33) Christine King, katika kitabu New Religious Movements: A Perspective for Understanding Society, asema hivi kuwahusu: “Mashahidi wa Yehova walitoa mwito wa ushindani dhidi ya wazo la mamlaka kamili la jamii mpya, na mwito huo wa ushindani, kutia na udumifu wayo, kwa wazi uliwasumbua wabuni wa utaratibu mpya. . . . Njia zilizokuwa zimetumiwa kwa muda mrefu za mnyanyaso, mateso, kufungwa gerezani na kudhihakiwa hazikuwafanya Mashahidi wageuke wawe na msimamo wa Nazi na kwa kweli zilikuwa zikipata matokeo ya kinyume dhidi ya wapinzani wao. . . . Kati ya pande hizo mbili zenye kudai uaminifu-mshikamanifu, pambano lilikuwa kali sana, tena sana, kwa sababu Wanazi hao wenye nguvu zaidi kimwili hawakuwa na uhakika sana katika mambo mengi, hawakuwa na msingi imara sana katika usadikisho wao, hawakuwa na uhakika sana juu ya kudumu kwa Enzi ya miaka 1,000. Mashahidi hawakuwa na shaka juu ya msingi wao, kwa sababu imani yao ilikuwa imekuwa dhahiri tangu wakati wa Abeli. Ingawa Wanazi walilazimika kugandamiza upinzani na kuwasadikisha wategemezaji wao, mara nyingi wakitumia usemi na maneno ya mfano ya Ukristo wa kimafarakano, Mashahidi walikuwa na uhakika juu ya uaminifu-mshikamanifu wa washiriki wao ulio kamili, na usiotikisika, hata kufikia kifo.”—Kilichapwa katika 1982.

      Mwishoni mwa vita, Mashahidi zaidi ya elfu moja waliookoka walitoka kwenye kambi hizo, imani yao ikiwa imara na upendo wao kwa mmoja na mwenzake ukiwa wenye nguvu. Majeshi ya Warusi yalipokaribia, walinzi walihama Sachsenhausen upesi. Waliwakusanya wafungwa kulingana na taifa. Lakini Mashahidi wa Yehova walibaki pamoja wakiwa kikundi kimoja—230 kutoka kambi hiyo. Huku Warusi wakiwafuatia kwa karibu, walinzi wakaanza kuona wasiwasi. Hakukuwa chakula, na wafungwa walikuwa hoi; na bado, yeyote aliyebaki nyuma au akaanguka kwa sababu ya uchovu alipigwa risasi. Maelfu ya wale waliopigwa risasi kwa njia hiyo walitapanyika huku na huku katika njia waliyopitia. Lakini Mashahidi walisaidiana hivi kwamba hata wale walio hoi zaidi hawakubaki barabarani! Hata ingawa baadhi yao walikuwa na umri wa miaka kati ya 65 na 72. Wafungwa wengine walijaribu kuiba chakula njiani, na wengi walipigwa risasi wakijaribu kufanya hivyo. Kinyume cha hayo, Mashahidi wa Yehova walitumia fursa kuwaambia watu kwenye njia ya uhamiaji kuhusu makusudi yenye upendo ya Yehova, na baadhi yao, kwa sababu ya shukrani kwa ujumbe wenye kufariji, waliwaandalia chakula wao wenyewe na cha ndugu zao wa Kikristo.

  • “Vitu vya Kuchukiwa na Mataifa Yote”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 661]

      Tafsiri ya Taarifa Ambayo Polisi wa SS Walijaribu Kuwalazimisha Mashahidi Watie Sahihi

      Kambi ya mateso .......................................

      Idara 2

      TAARIFA

      Mimi, ...................................................

      niliyezaliwa tarehe ..................................................

      katika .......................................................

      ninatoa taarifa ifuatayo:

      1. Mimi nimekuja kujua kwamba International Bible Students Association inapiga mbiu ya mafundisho yasiyo kweli na hiyo hufuatilia makusudi ya uhasama dhidi ya Serikali chini ya kisitiri cha dini.

      2. Mimi kwa sababu hiyo niliacha tengenezo hilo kabisa na nikajiweka huru kabisa na mafundisho ya farakano hilo.

      3. Mimi ninatoa uhakikisho hapa kwamba sitakuwa na sehemu yoyote kamwe katika utendaji wa International Bible Students Association. Watu wowote wanaonijia na mafundisho ya Wanafunzi wa Biblia, au ambao kwa njia yoyote ile wanafunua uhusiano wao nao, nitawashutumu mara hiyo. Fasihi zote kutoka kwa Wanafunzi wa Biblia ambazo zitaletwa nyumbani kwangu nitazipeleka mara hiyo kwa kituo cha polisi kilichoko karibu.

      4. Mimi nitaheshimu sheria za Serikali kuanzia sasa, hasa kukiwa vita, mimi nitachukua silaha mkononi, na kulinda nchi yangu, na kuungana kwa kila njia na jumuiya ya watu.

      5. Mimi nimejulishwa kwamba nitachukuliwa tena mara hiyo ndani ya kifungo cha ulinzi ikiwa nitatenda tofauti na taarifa niliyotoa leo.

      .................................., Tarehe ................ ...........................................................

      Sahihi

      [Sanduku katika ukurasa wa 662]

      Barua Kutoka kwa Baadhi ya Wale Waliohukumiwa Kifo

      Kutoka kwa Franz Reiter (aliyekabili kifo kwa kukatwa kichwa) kwa mama yake, Januari 6, 1940, kutoka kwa gereza la Berlin-Plötzensee:

      “Ninasadiki kwa nguvu katika imani yangu kwamba ninatenda vile inavyofaa. Nikiwa hapa, bado ningeweza kubadili nia yangu, lakini kwa Mungu hiyo ingekuwa ni kutokuwa mwaminifu-mshikamanifu. Sisi sote hapa twataka kuwa waaminifu kwa Mungu, kwa heshima yake. . . . Kwa yale niliyojua, ikiwa ningalikula kiapo [cha kijeshi], ningalitenda dhambi inayostahili kifo. Huo ungekuwa uovu kwangu. Nisingepata ufufuo. Lakini nashikamana na yale aliyosema Kristo: ‘Yeyote atakayeokoa uhai wake ataupoteza; lakini yeyote atakayepoteza uhai wake kwa ajili yangu, huyo ataupokea.’ Na sasa, Mama yangu mpendwa na ndugu na dada zangu wote, leo niliambiwa hukumu yangu, na msiogopeshwe, ni kifo, nami nitauawa kesho asubuhi. Nina nguvu yangu kutoka kwa Mungu, sawa na ilivyokuwa sikuzote kwa Wakristo wote wa kweli huko nyuma. Mitume wanaandika, ‘Yeyote aliyezaliwa kutoka kwa Mungu hawezi kufanya dhambi.’ Ndivyo ilivyo kwangu mimi. Hilo nilikuthibitishia, na ungeweza kulitambua. Mpendwa wangu, usihuzunike. Ingekuwa vizuri kwa nyinyi nyote kuyajua Maandiko Matakatifu vizuri hata zaidi. Ikiwa mtasimama imara hadi kifo, tutaonana tena kwenye ufufuo. . . .

      “Wako Franz

      “Hadi tutakapoonana tena.”

      Kutoka kwa Berthold Szabo, aliyeuawa kwa kupigwa risasi, katika Körmend, Hungaria, mnamo Machi 2, 1945:

      “Dada yangu mpendwa, Marika!

      “Muda huu wa saa moja unusu ambao nimebaki nao, nitajaribu kukuandikia ili uweze kuwajulisha wazazi wetu kuhusu hali yangu, ninapokabili kifo mara hii.

      “Ninawatakia wao amani ya akili ileile ambayo ninayo katika pindi hii ya mwisho katika ulimwengu uliojaa misiba. Sasa ni saa nne, na nitauawa saa tano unusu; lakini mimi ni mtulivu sana. Uhai wangu wa baadaye ninauweka mikononi mwa Yehova na Mwana wake Mpendwa, Yesu Kristo, Mfalme, ambaye hatasahau kamwe wale wanaowapenda kikweli. Ninajua pia kwamba karibuni kutakuwa na ufufuo wa wale waliokufa au, ndiyo kusema waliolala, katika Kristo. Ningependa pia kutaja hasa kwamba ninawatakia nyote baraka za Yehova zenye utajiri zaidi kwa ajili ya upendo mlionionyesha. Tafadhali mbusu baba na mama kwa ajili yangu, na Annus pia. Hawapaswi kunisikitikia; tutaonana tena karibuni. Mkono wangu ni mtulivu sasa, na nitaenda kupumzika hadi Yehova atakaponiita tena. Hata sasa nitatimiza nadhiri niliyofanya kwa ajili yake.

      “Sasa wakati wangu umekwisha. Mungu na awe nanyi na mimi pia.

      “Kwa upendo mwingi, . . .

      “Berthi”

      [Sanduku katika ukurasa wa 663]

      Watambuliwa Kuwa Wajasiri na Wenye Masadikisho

      ◆ “Wajapokabiliwa na matatizo makubwa ajabu, Mashahidi katika kambi walikutana na kusali pamoja, wakatokeza fasihi na kugeuza watu wafuate imani yao. Wakitegemezwa na ushirika wao, na wakiwa tofauti na wafungwa wengine wengi, wakifahamu vema sababu za kuwapo kwa sehemu kama hizo na sababu za wao kuteseka hivyo, Mashahidi walithibitika kuwa kikundi kidogo cha wafungwa wanaokumbukwa, waliopewa alama ya pembe-tatu ya zambarau na kutambuliwa kwa ujasiri na masadikisho yao.” Ndivyo alivyoandika Dakt. Christine King, katika “The Nazi ­State and the New Religions: Five Case Studies in Non-Conformity.”

      ◆ “Values and Violence in Auschwitz,” cha Anna Paweł­czyńska, chasema: “Kikundi hicho cha wafungwa kilikuwa kani imara ya kimafundisho na kilishinda vita dhidi ya Unazi. Kikundi cha Wajerumani cha farakano hilo kilikuwa kimekuwa kisiwa duni cha upinzani usiotikisika miongoni mwa taifa lililotiwa hofu, na katika roho iyo hiyo ya kutoghadhibika walifanya kazi kambini katika Auschwitz. Waliheshimiwa na wafungwa wenzao . . . wafanyakazi wa magereza, na hata maofisa wa SS. Kila mtu alijua kwamba hakuna ‘Bibelforscher’ [Shahidi wa Yehova] ambaye angefuata amri iliyo kinyume cha imani zake za kidini.”

      ◆ Rudolf Hoess, katika masimulizi yake ya maisha yaliyochapwa katika kitabu “Commandant of Auschwitz,” alisema juu ya kuuawa kwa Mashahidi wa Yehova fulani kwa kukataa kuvunja kutokuwamo kwao kwa Kikristo. Yeye alisema: “Hivyo ndivyo ninavyowazia kwamba lazima wafia-imani Wakristo wa kwanza wawe walionekana huku wakingoja katika sarakasi ili hayawani mwitu waje kuwararuararua. Nyuso zao zikiwa zimebadilika kabisa, macho yao yakiwa yameinuliwa mbinguni, na mikono yao ikiwa imefumbwa na kuinuliwa katika sala, wakakabili kifo. Wote waliowaona wakifa waliguswa moyo sana, na hata kikosi cha wauaji chenyewe kiliguswa moyo.” ­(Kitabu hicho kilitangzwa katika Poland chini ya kichwa “Autobiografia Rudolfa Hössa-komendanta obozu ­oświęcimskiego.”)

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki